Watoto Wanahitaji malezi ya Namna Gani?
“Mlee mtoto katika njia impasayo.”—Mit. 22:6.
1, 2. (a) Nini maoni ya wazazi wengi juu ya kulea watoto? (b) Ijapokuwa shauri la Biblia, nini kinachotukia kwa vijana leo?
WAZAZI, je! mmeona kuwa kulea watoto leo ni kazi ngumu? Je wakati wo wote mnajiona kushindwa juu ya namna ya kuzoeza watoto wenu kusudi mwalinde katika nyakati hizi za hatari? Wazazi wengi wanajiona kushindwa. Kweli, Biblia yasema: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Na hali leo wavulana na wasichana vile vile kwa mamilioni wanageukia uasi.
2 Katika mwaka wa 1966 uchunguzi wa Halmashauri ya Wazee ya United States ulifunua wazi kwamba kati ya watoto milioni 29 wa taifa hilo walio na umri wa kati ya miaka kumi na kumi na saba, milioni mbili na nusu, au karibu mmoja kati ya kila kumi na mmoja, walikuwa katika maandishi ya polisi! Tangu wakati huo hali zimezidi kuwa mbaya. Herald-Examiner la Los Angeles la Februari 2, 1970, lilisema: “Uhalifu wa vijana katika California ya Kusini unapanda kwa kadiri ambavyo huenda karibuni kukamatwa kwa vijana kukazidi kule kwa watu wazima—na hali vijana wanafanyiza sehemu ndogo tu ya idadi ya watu wote. Vifungo vimekwisha kujaa tayari na hakuna ukomo wa kuona.” Katika New Zealand, kulingana na habari za wakili wa polisi, uhalifu wa watoto ulipata kuwa maradufu tangu mwaka wa 1966 hata mwaka wa 1970!
3. Ni maelekeo gani yameonekana juu ya uhalifu wa vijana?
3 Uhalifu wa vijana hauongezeki kwa kasi tu, lakini vile vile unakuwa mbaya zaidi; na watoto zaidi wanaufanya wakiwa wenye umri mdogo zaidi. Katika mwaka wa majuzi, katika Baltimore, Maryland, kukamatwa kwa watoto wa miaka kumi na wa chini ya umri huo kulifanywa mara 526. Kukamatwa kwa ajili ya kuiba nyumba za watu usiku nako kulifanywa mara 169, mara 22 kwa ajili ya unyang’anyi, na kukamatwa kwa ajili ya uuaji, wizi wa motokaa na matumizi ya dawa zenye kutia usingizi! Katika Perth, Australia, kadiri ya 80 kwa mia ya wizi wa motokaa inafanywa na vijana wasiofika umri wa 20! Afisa wa polisi huko alisema: “Si jambo lisilo la kawaida tena kumwona mtoto wa miaka 13 akiendesha gari lililoibwa.”
4, 5. (a) Ni matokeo gani yenye msiba ya ufisadi yaliyoshuhudiwa sana leo? (b) Hali hizi ni ushuhuda wa kuishi kwetu katika kipindi gani cha wakati?
4 Ufisadi kati ya vijana vile vile umeenea pote. Alisema hivi msichana wa miaka 16 wa New York City: “Karibu nusu ya darasa langu wanatumia dawa [kuzuia mimba] nayo ile nusu nyingine wanakusudia kuinunua watakapokuwa katika chuo kikuu.” (Times la New York, Septemba 24, 1971) Matokeo yenye msiba ya ufisadi yanatia ndani na maambukizo ya magonjwa ya kisonono na kaswende na kuzaliwa kwa watoto wa haramu. Katika California karibu mara kumi ya kadiri ya vijana waliopatwa na kisonono katika mwaka wa 1960 walipatwa nacho katika mwaka wa 1970. Sasa yakadiriwa kwamba mmoja kati ya wanafunzi watano wa shule za masomo ya juu atapatwa na kisonono au kaswende mbele ya kuhitimu. Katika shule nyingine inakadiriwa kwamba nusu ya jumla ya wanafunzi watapatwa na kisonono au kaswende. Yasemekana kwamba jumla ya wasichana 43,100 wasiofika umri wa 20 katika California walipata mimba katika mwaka wa 1970, bila ya kutia ndani wale walioolewa kwa sababu ya mimba yao.—Examiner la San Francisco, Juni 20, 1971.
5 Msimamizi wa hospitali katika Richmond, Virginia, aliona kwamba mimba za vijana wasiofika umri wa 20 zinaongezeka “kwa njia yenye huzuni,” naye akasema: “Inayoogofya ni hesabu ya mimba kati ya wasichana wa chini ya umri wa miaka 15.” (Newport News Daily Press, Desemba 13, 1970) Evening Bulletin la Philadelphia lilisema: “Zaidi hesabu kubwa ya akina mama wasioolewa ni wasichana wa shule wenye umri wa miaka 11 na 12.” Kutokana na yanayotukia, je! si wazi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” zilizo na hatari zilizotabiriwa na Biblia? Kwa kweli hizi ni siku zilizotiwa alama na uasi mwingi mno, pamoja na ‘kutokutii wazazi.’—2 Tim. 3:1-5.
6. (a) Uasi ulioenea pote unaonyesha nini juu ya malezi wanayoyapata watoto? (b) Ni kitu gani cha kulaumiwa sana kwa ajili ya kuvurugika kwa wazazi wengi juu ya kulea watoto?
6 Kwa maana vijana wengi hivyo wanakuwa waasi, je! haionyeshi kwamba kuna kosa fulani katika malezi wanayoyapata watoto? Kwa wazi wao hawalelewi ‘katika njia iwapasayo.’ (Mit. 22:6) Lakini watoto wanahitaji malezi ya namna gani? Wazazi wengi wamevurugika kwa habari ya jambo hilo. “Kwa maneno yao na matendo, baba wengi na akina mama wanaonyesha wazi kwamba ni kama wamekwisha kupumbazwa na mashaka,” alisema mshiriki wa Baraza ya Uandishi ya Times la New York. “Kanuni za zamani za adabu hazielekei tena kutumika,” akasema. (Times Magazine la New York, Januari 16, 1972) Maoni yenye kupingana ya washauri wa kilimwengu juu ya malezi ya watoto ndiyo ya kulaumiwa sana kwa sababu ya kuvurugika kwa wazazi.
7. (a) Maandishi ya washauri wa kilimwengu juu ya kulea watoto yanakuwaje kwa kawaida? (b) Kama inavyoonyeshwa na Yeremia 8:9, kuna kosa gani katika namna ya malezi ambayo watoto walio wengi leo wamekuwa wakipata?
7 Yajapokuwa maoni ya washauri hawa yanatofautiana sana, uchunguzi wa maandishi yao unafunua wazi jambo fulani la kawaida katika hayo. Na hilo ni kwamba, kwa kawaida wanaipuza Biblia kama chombo cha kufundishia. Je! huu ndio ungeweza kuwa ugumu? Mambo yaliyoendelea kutukia majuzi yanaelekea kuonyesha jibu. Kwa maana ebu fikiria: Je! uasi haukuongezeka sana katika nyakati za majuzi ambapo “kanuni za zamani za adabu” (zile ambazo mara kwa mara msingi wake ni Biblia) zimetupwa kando? Je! hii haionyeshi kwamba vijana wanayahitaji malezi na uongozi ambavyo msingi wake ni mafundisho ya Biblia?—Yer. 8:9.
KWA SABABU GANI KUFUNDISHA WATOTO JUU YA MUNGU
8. (a) Nini kawaida yenye kutokeza ya watoto? (b) Kwa sababu gani majibu ambayo wazazi wanatoa kwa maulizo ya watoto wao ni ya muhimu?
8 Ni jambo la kawaida kwa watoto kuwatazamia wazazi wao kwa uongozi. Vijana wana maulizo mengi sana. Ni kawaida yao kuuliza: “Nani aliyeyafanya maua yanayopendeza?” “Nyota zilipata kuwako angani namna gani?” Au huenda wakauliza: “Mimi nilitoka wapi? Nani aliyenifanyiza mimi?” Haimpasi mtu kudharau umuhimu wa namna watoto wanavyojibiwa juu ya mambo haya. Wanayofundishwa watoto yanakaa ndani yao sikuzote, yakigeuza nia zao na maoni na kwa njia hiyo yakiigeuza njia yao ya wakati ujao ya maisha.
9. (a) Watoto wanafundishwa nini leo kwa kawaida juu ya mwanzo wao? (b) Kuna wonyesho gani kwamba maoni ya mageuzi wanayofundishwa watoto si sawa?
9 Huenda mzazi akajibu: “Hapana aliyetufanyiza sisi wala vitu hivi vingine. Vitu vyote vilijitokeza vyenyewe tu; ilikuwa ni kwa bahati—ajali—kwamba vitu vyote vikatokea.” Haya ndiyo maoni ya mageuzi wanayofundishwa watoto kwa kawaida katika shule leo. Mara nyingi yasemekana kwamba maoni haya ni “ya kijuzi,” na kwamba watu waaminio kwamba kuna Mungu aliyevifanyiza vitu hivi vyote “si wajuzi.” Lakini je! ndivyo ilivyo? Je! Maoni ya leo ya mageuzi ni ya kweli? Basi, fikiria: Je! si jambo la hakika kwamba kweli inapofundishwa, kunakuwa na matokeo mema? Na hali yatazame mamilioni ya watoto waasi leo waliokua wakiwa chini ya taratibu ya elimu iliyoendeleza maoni ya mageuzi!—Zab. 14:1.
10. (a) Kwa sababu gani inavuruga akili kwa mtoto kufundishwa kwamba hakuna Muumba? (b) Wamepaswa watoto wafundishwe nini juu yao wenyewe, majani, mwezi na nyota, na vinginevyo, na kwa sababu gani?
10 Kwa kweli, inavuruga akili za watoto kufundishwa kwamba hakuna Muumba wa kimbinguni. Kwa mfano, watoto wanaweza kuona kwamba wanaume wanajenga nyumba na wanawake kuoka keki. Vitu hivi vinaowafanyizaji. Kwani basi, huenda watoto wakafikiri kwa ufahamu, maua mazuri au nyota zenye kung’aa hazina mfanyizaji? Wamepaswa watoto wafundishwe maelezo yenye busara yaliyomo katika Biblia: “Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu.” (Ebr. 3:4) Wamepaswa waonyeshwe kwamba Biblia haifundishi kwa njia ya ujinga kwamba hakuna aliyetufanyiza, bali yasema: “Jueni kwamba [Yehova] ndiye Mungu; ndiye aliyetuumba [wala sio sisi wenyewe].” (Zab. 100:3) Wamepaswa watoto wafundishwe kwamba Mungu “huyameesha majani kwa makundi, na maboga kwa matumizi ya mwanadamu.” (Zab. 104:14) Vile vile linayoyasema Neno la Mungu juu ya “mwezi na nyota ulizoziratibisha [wewe Mungu]” yamepaswa yaelezwe kwa vijana. (Zab. 8:3) Kweli hizi za Maandiko zitatosheleza tamaa ya mtoto ya kutaka kujua, nazo zitamsaidia kukuza heshima kwa Muumba wetu Mkuu. Namna hii ya kufundisha ni ya lazima ili ‘kumlea mtoto katika njia impasayo.’—Mit. 22:6.
11. Ni nafasi gani anazoweza mzazi kuzipata amfundishe mtoto wake juu ya Mungu?
11 Yampasa mzazi apate nafasi za kujenga upendo na shukrani kwa Yehova Mungu katika watoto wake. Mtoto na mzazi wanapokuwa pamoja chini ya anga lenye nyota tupu, baba aweza kukazia juu ya mwanawe hekima na uwezo wa Yehova katika kufanyiza na kuziratibisha nyota hizi za kimbinguni katika mizunguko yazo. (Zab. 19:1, 2) Nyakati nyingine, pengine mnapoutazama uzuri wa maua, kushuka kwa jua kunakotazamisha, au namna mbalimbali za maisha ya mimea na wanyama, mzazi aweza kuwafundisha watoto kwamba vitu hivi vya ajabu na vizuri ni ushuhuda mbalimbali wa upendo wa Baba yetu wa kimbinguni kwa wanadamu. (Matendo 14:17; Mt. 5:45) Lakini je! fundisho hili juu ya Mungu kwa kweli ‘halivunji sheria za sayansi’?
12. (a) Kwa sababu gani hakuvunji sheria za sayansi kufundisha kwamba mambo ya ajabu tunayoyaona kutuzunguka yaliumbwa na Mungu? (b) Itamfaidije mtoto kujua kwamba kuna Muumba mwenye uwezo wote anayemwangalia yeye?
12 Sivyo, hata kidogo! Linafaa leo sawa na lilivyofaa wakati mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na roho ya Mungu kale aliposema kwamba “mambo yake [Mungu] yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru.” (Rum. 1:20) Ukweli ni, sayansi ya kweli katika miaka ya majuzi imeonyesha wazi ghala kubwa ya maarifa inayoshuhudia namna ulimwengu wote na vyote vilivyo hai vilivyoumbwa kwa ustadi sana, ikitoa ushuhuda kwamba yupo kweli kweli Muumba mwenye nguvu na mwenye akili nyingi. Lo! namna inavyotia nguvu kwa watoto kujua kwamba Mungu huyo mkuu yupo, na kwamba anawaangalia! (1 Pet. 5:7) Hii itawasaidia kuepuka kusumbuliwa kupita kadiri na woga, mashaka na hatari ya ulimwengu wa leo. Itawalinda na masumbufu ya akili au ya moyo, na kuwapa shauri la usalama na tumaini. Kwa njia hiyo hawataitikia kwa jeuri na chuki, lakini wataelekea kutendea wote kwa upendo kama ule wa Mungu.—Zab. 23:1-6; 55:22; Isa. 41:10.
KWA SABABU GANI KUFUNDISHA WATOTO NENO LA MUNGU
13. Kwa sababu gani ni wazi kwamba kumwambia tu mtoto asifanye mabaya hakutoshi?
13 Lakini, kufundisha watoto kwamba kuna Mungu tu hakutoshi. Watoto wamepaswa wafundishwe Neno la Mungu vile vile, pamoja na anayoyataka Mungu kwa wanadamu. Kwa sababu gani? Basi, fikiria: Wazazi wengi wa kisasa wanawaambia watoto wao kwamba kuna Mungu. Na karibu kila mzazi anamwambia mtoto wake ni vibaya kusema uongo, kuiba na kufanya uhalifu mwingineo. Vile vile, mara nyingi akina mama wanawaambia binti zao kwamba ni vibaya kujitia katika ngono mbele ya ndoa. Na hali watoto kwa mamilioni wanayageukia mambo haya ya uasi, wakijua hata wanapoyafanya kwamba wamekwisha kuambiwa kuwa mambo haya ni mabaya. Kwa wazi, kumwambia mtoto hakutoshi. Lakini kwa sababu gani sivyo?
14. Kwa sababu gani mara nyingi watoto hawaitikii mafundisho wanayopewa na watu wazee?
14 Sababu kubwa ni kwamba karibuni watoto wanajifunza kwamba hawawezi kutegemea neno au mfano wa wanadamu. Wanagundua kwamba mara nyingi watu wazee wanakosea, na kwamba kanuni zao za adabu zitageuka. Vile vile, watoto wanaona kwamba mara nyingi watu wazee wanasema jambo moja na kufanya jingine. Kwa hiyo watoto wanapoanza kufahamu kwamba watu wengine wanasema uongo, kuiba na kufanya uasherati, kwa ufahamu wanafikia azimio la kwamba ni sawa kufanya mambo haya mradi hawapatikani, au mradi hawapatwi na madhara. Hivyo watoto leo wanafanya sana mambo yo yote wanayofikiri wanaweza kuyafanya bila ya kupatikana.
15. (a) Ni sababu gani yenye umuhimu zaidi wanayoihitaji watoto ili waepuke mabaya? (b) Kwa sababu gani kujua kwamba amri hizi ni za Mungu Mwenye Nguvu Zote kutakuwa kizuizi cha kutenda mabaya?
15 Kwa wazi, basi, yampasa mtoto awe na sababu yenye umuhimu zaidi ya kutii kuliko kwamba wazazi wake tu au wanadamu wengine wanamtaka atii. Yampasa afundishwe katika jina la Mungu, ambaye hizi ni amri zake kwa kweli, kutokusema uongo, kutokuiba, kutokufanya uasherati ama kujitia katika mazoea mengine mabaya. (Mit. 6:16-19; Marko 10:17-19; Ebr. 13:4) Mafundisho haya kutoka kwa Neno la Mungu yatakazia juu ya mtoto uzito wa kufanya mabaya. Ndipo atakapojua kwamba si neno la mwanadamu tu linalotiwa ndani, lakini ni neno la Muumba mwenyewe, Yeye anayetoa uzima na aliye na uwezo wa kuuondoa milele kwa wavunja sheria wa kukusudia. (Ufu. 21:8) Vile vile, mtoto anakuja kujua kwamba, kama vile Biblia isemavyo, “macho ya [Yehova] yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.” (Mit. 15:3) Hivyo mtoto atajua kwamba hawezi kujitia katika mabaya bila ya kuonwa na Mungu.—Zab. 11:4; Ebr. 4:13.
16. Kufundisha watoto Neno la Mungu kutatoaje kizuizi chenye nguvu zaidi cha kutenda mabaya?
16 Lakini, kadiri ambavyo mtoto anavyofundishwa Neno la Mungu ndivyo kizuizi chenye nguvu hata zaidi, cha maana zaidi cha kutenda mabaya kitakavyokua ndani yake. Funzo la Biblia litaeleza wazi namna Yehova Mungu alivyo kwa mtoto, si kama Muumba Mkuu tu, lakini kama Mtu wa kweli anayewapenda wanadamu kweli kweli. Yeye atajifunza namna Mungu alivyoonyesha upendo wake kwa kumtuma Mwanawe duniani akatoe msingi wa kuwaondoa wanadamu katika dhambi na mauti, kwa njia hiyo akifungua njia kusudi wanadamu wafurahie uzima wa milele katika paradiso chini ya taratibu mpya ya mambo. (Yohana 3:16; 2 Pet. 3:13) Vile vile, mtoto atajifunza kutokana na funzo la Biblia kwamba katika taratibu yake mpya Mungu ataondoa kati ya wanadamu ugonjwa na hata kifo, na vile vile maumivu, taabu na machozi yanayoonekana sana leo. (Ufu. 21:3, 4) Wakati huo watu wote watakuwa wenye urafiki na wenye kupenda amani. Kwa kweli, hata wanyama watakuwa katika amani, na mtoto mchanga ataweza kucheza nao bila ya kuumia. (Isa. 11:6-9; 37:9-11, 29) Kwa kadiri ambavyo mtoto anakuja kuijua mipango hii ya ajabu ya Yehova, ndivyo upendo wake kwa Mungu utakavyokuwa wenye nguvu sana. Kama matokeo, hatataka kufanya lo lote amchukize Baba yake wa kimbinguni aliye mzuri sana. Upendo wa mtoto na shukrani kwa Yehova kwa njia hiyo vitakuwa kama kizuizi chenye nguvu kupita vyote cha kutofanya jambo lo lote ambalo Mungu anasema ni baya.
17. (a) Kwa sababu gani mtu aweza kuwa na hakika kwamba kufundisha watoto Neno la Mungu kutawafaidi katika maisha ya nyumaye? (b) Ni mfano gani wa Biblia unaoonyesha faida ya malezi ya mapema?
17 Lakini je! mtu aweza kuwa na hakika kabisa kwamba mafundisho katika Neno la Mungu yatamfaidi mtoto katika maisha ya nyumaye? Ndiyo, mtu aweza kuwa na hakika, kwa maana ukumbuke kwamba mithali ya Biblia yasema kwamba mtoto akilelewa “katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Mfikirie Yusufu Mwebrania mchanga kama mfano, Baba yake Yakobo kwa wazi alimfundisha juu ya Yehova na sheria zake alipokuwa mchanga. Nyumaye katika maisha Yusufu alikuja kuwa katika nchi ya ugenini ya Misri, mbali na jamaa yake na rafiki. Huko, alipokuwa akimfanyia kazi mwanamume tajiri aliyeitwa Potifa, mke wa mwanamume huyu alianza kufanya majaribio ya kumtongoza Yusufu mwenye uso mzuri. Alikuwa akimwambia: “Lala nami.” Lakini Yusufu alikuwa akikataa, akieleza: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” Hata wakati mkewe Potifa alipomshika Yusufu kwa ghafula na kujaribu kumlazimisha alale naye, yeye alipinga na kutoroka. Ni heshima ya Yusufu na upendo kwa Mungu, vilivyokuwa vimetiwa ndani yake kama mtoto, vilivyomzuia asitende ubaya.—Mwa. 39:1-12.
18. (a) Kufundisha watoto Neno la Mungu kutakuwa na faida gani? (b) Kwa sababu gani watoto wanapatwa na taabu nyingi sana leo?
18 Je! wewe hukubali kwamba leo watoto wanahitaji namna hii ya mafundisho kutoka kwa Neno la Mungu? Kukazia juu ya watoto matakwa ya Mungu ya adili bila shaka kutawasaidia waishi maisha manyofu, yenye furaha. Lakini leo uongozi wa Maandiko unatupwa kando kwa kawaida kama wenye vizuizi vingi kupita kadiri na wenye kuvunja moyo. Kwa mfano, kwa habari ya katazo la ngono kwa watu wasiooana, mtu mmoja aliandika hivi majuzi katika Times Magazine la New York: “Kwa kweli kuna sehemu nyingi zaidi za kuvunjika moyo katika maisha hivi kwamba kutia moyo mvunjo kwa makusudi hakuhitajiwi. . . . Tupaswayo kufanya tuwape watoto wetu uongozi (wao wenyewe, twatumaini), ni kuwaonyesha kwamba twajithamini wenyewe na wengine vile vile, na kwamba kuna njia nyingi mbalimbali za kufanya yatupasayo.” Lakini lo! ni taabu nyingi kama nini iliyoletwa na kukataa huko kwa uongozi wa Mungu, pamoja na mfululizo wa magonjwa ya kisonono na kaswende, watoto wa haramu na utoaji wa mimba, pamoja na maumivu yanayofuatana nayo, kuvunjika moyo na huzuni! Ni wazi kama nini kwamba watoto wanayahitaji mafundisho yanayotolewa katika Neno la Mungu!—Yer. 10:23.
UHITAJI WA ADHABU
19. (a) Je! kwa asili watoto wanaelekea kufanya yaliyo haki, na twajuaje? (b) Nini yanayotiwa ndani katika shauri la kuadhibu?
19 Lakini, ili mpango wa mafundisho katika Neno la Mungu uwe na matokeo mazuri, lazima utie ndani na adhabu yenye upendo vile vile. Hii ni kwa sababu watoto kwa asili hawaelekei kufanya jambo linalofaa. Ni kama vile mithali ya Biblia iliyoongozwa na roho ya Mungu inavyosema: “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.” (Mit. 22:15) Neno “adhabu” lina maana ya kutoa malezi yanayogeuza na kuonyesha makosa. Kwa hiyo inatia na kurudia-rudia mafundisho kusudi kwamba mtoto avutwe kujipatanisha nayo. Lakini adhabu inatia ndani mengi zaidi. Kama wajuavyo wazazi walio wengi, mara nyingi mtoto haonyeshwi makosa kwa maneno tu. (Mit. 29:17, 19) Kwa hiyo malezi ya adhabu huenda yakatia ndani na kurudi au kuadhibu kunakotolewa kwa kusudi la kumwonyesha mtoto makosa. Lakini je! namna hii ya adhabu imepaswa itie ndani na kupiga kofi wakati wo wote? Je! mna ukweli katika mithali ya zamani: “Mtoto alewavyo ndivyo akuavyo”?
20. Nini maoni ya kawaida ya watu wenye mamlaka wa kilimwengu kwa habari ya kutoa adhabu ya kimwili, kama namna ya malezi ya adabu?
20 Watu wenye mamlaka wa kilimwengu wanasema hivi mara nyingi juu ya kulea watoto: ‘Hapana, mtoto hapaswi kupigwa kofi wakati wo wote. Epuka kumvunja mtoto moyo kwa kutumia mashauri hayo makali sana ili kuyageuza maelekeo yake ya asili.’ Habari fulani za Times la New York, Aprili 5, 1972, zilisema: “‘Mtoto alewavyo ndivyo akuavyo’ ni mithali mbaya ya zamani inayozidi kupata ukubali wa wategemezaji wa ‘maadili ya zamani’ waliojiweka wenyewe. Ni vigumu kufahamu kwa sababu gani adhabu iliyokusudiwa, yenye maumivu ikitolewa na mtu mkubwa zaidi na mwenye nguvu zaidi yaweza kufundisha kitu kinginecho kuliko imani ya kwamba nguvu ndizo zinazoshinda.” Lakini je! maoni haya ni sawa? Je! ni kosa kutumia adhabu ya kimwili kwa kusudi la kuonyesha ubaya wa mwenendo wa mtoto?
21. (a) Neno la Mungu linasema nini juu ya matumizi ya adhabu ya kimwili ili kuonyesha ubaya wa mwendo wa mtoto? (b) Twajuaje ni njia ya Mungu kutoa adhabu ya namna hiyo?
21 Mungu ndiye Muumba wa mwanadamu. Hakuna mwingine aliye na mamlaka ya juu zaidi. Neno lake Yeye linasema wazi sana juu ya jambo hilo. Linasema: “Usimnyime mtoto wako mapigo; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na [kaburi].” (Mit. 23:13, 14) Uzima wa mtoto umo hatarini. Kama akiruhusiwa kufuata mwendo mbaya, utaongoza kwenye huzuni yake mwenyewe na kifo cha nyumaye bila ya kibali cha Mungu. Hivyo Biblia yasema: “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi mapema.” (Mit. 13:24) Inaonyesha upendo wa kweli kwa upande wa mzazi kufanya lo lote awezalo kumwonyesha mtoto wake makosa, pamoja na kumpiga kofi. Hii ndiyo njia ya Mungu. “Maana yeye ambaye [Yehova] ampenda,” andiko lasema, “humrudi, naye humpiga [kwa kiboko au mjeledi] kila mwana amkubaliye.”—Ebr. 12:5, 6.
22. (a) Limepaswa kusudi la mzazi liwe nini kwa kutoa adhabu, kama inavyoonyeshwa na mfano wa Mungu? (b) Nini cha kulaumiwa sana kwa sababu ya ongezeko la ajabu la uasi wa vijana leo?
22 Kwa sababu gani Mungu anawafanyia watoto wake hili? “Kwa faida yetu,” mtume Paulo akasema, “ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Ebr. 12:7-11) Watoto, kwa faida yao wenyewe, wanahitaji adhabu hiyo. Ni sehemu ya malezi yaliyo ‘katika njia iwapasayo.’ (Mit. 22:6) Kukataliwa kwa malezi hayo ya adhabu na ulimwengu ndiko kwa kulaumiwa sana kwa sababu ya ongezeko la ajabu la uasi wa vijana na taabu inayotokea na aibu iliyoletwa nao kwa wazazi.—Mit. 29:15.
23. Watoto wanaitikiaje wanapopokea au wanapokosa kupokea adhabu?
23 Tofauti na maoni yapendwayo na watu wengi, watoto wanashukuru wakati wazazi wanapoonyesha kupendezwa kwa kweli nao kwa kutoa viongozi vya busara na vizuizi juu ya matendo yao. Watoto wengine huenda wakanung’unika nyakati nyingine kwa sababu ya adhabu, lakini wanajifunza kupenda na kuheshimu wazazi wanaoonyesha kupendezwa kwa kweli na hali yao njema. Kwa upande mwingine, kukosa kutoa adhabu wanayoihitaji watoto sana kwa upande wa wazazi kutaelekea kumfanya mtoto awaonee wazazi wake uchungu. Si zamani sana gazeti lijulikanalo sana lilizungumza juu ya msichana wa umri wa miaka kumi na mitano aliyetelezea mwenendo mbaya na kuleta aibu juu yake mwenyewe na jamaa yake. Akihuzunishwa na mwenendo wake, yeye alimwambia baba yake: “Baba, ingalikupasa kuagiza niwe na adabu miaka mingi iliyopita, na nisipofanya hivyo, kuliko kusema nami, ingalikupasa kunichapa matako sana. Nisipochukua hatua nzuri, mbona hukunilazimisha? Ulifikiri nilikuwa mpumbavu sana kwamba nisingeweza kuchukua hatua bora?”—McCall’s, Julai 1969, ukurasa wa 114.
24. (a) Wazazi wanawezaje kuonyesha kwamba wanawapenda watoto wao kweli kweli? (b) Nini yatakayokuwa matokeo ya kuuonyesha upendo huu?
24 Wazazi, onyesheni kwamba mnawapenda watoto wenu kweli kweli kwa kuwapa adhabu wanayoihitaji sana. Litiini shauri lenye hekima la Neno la Mungu. Wafundisheni watoto wenu hekima yake. Sitawisheni ndani yao upendo na heshima kwa Muumba, Yehova Mungu. Kwa kufanya hivi mwaweza kuwa na matumaini kwamba ‘mnawalea watoto wenu katika njia iwapasayo, na kwamba hawataiacha.’ (Mit. 22:6) Mwishowe hii itamaanisha kwao uzima usio na kikomo katika taratibu mpya ya mambo iliyo tukufu ya Yehova Mungu. Lo! ni namna gani watoto wako watakavyokuwa wenye shukrani kwako kwa ajili ya kuwatayarisha kusudi wafurahie hili!
[Picha katika ukurasa wa 125]
Wanapotazama kuumba kwa kimungu, yampasa mzazi apate nafasi ya kujenga upendo na shukrani katika watoto wake kwa Yehova Mungu