Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 3/15 kur. 135-141
  • Kuacha Kupiga Punyeto—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuacha Kupiga Punyeto—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAZOEA YA KAWAIDA SANA
  • NI NINI MATOKEO YA MAZOEA HAYA?
  • NAMNA TULIVYOFANYIZWA
  • MAONI YA MKRISTO YA KUPIGA PUNYETO
  • ULINZI NA KUPONYA
  • Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Shinda Zoea la Kupiga Punyeto
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Kuendelea Kuwa na Maoni ya Mungu Juu ya Ngono
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 3/15 kur. 135-141

Kuacha Kupiga Punyeto​—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?

WAKATI fulani kupiga punyeto kulizungumzwa kwa unyamavu faraghani, kama “dhambi ya siri” au “uovu wa mtu peke yake.” Leo kunakuwa kwa haraka neno la kuzungumzwa nyumbani kwa kawaida. Kamusi zinakufafanua kama ‘tendo la kusugua viungo vya mtu vya uzazi mpaka kichocheo kinaletwa kwenye upeo na mshindo, lakini bila ya ngono.’ “Mageuzi makuu ya ngono” ya kisasa pamoja na “adili mpya” yake ni ya kulaumiwa sana kwa kuyafanya mazoea haya yaenee sana, kama vile mfano ufuatao wa maoni ya siku hizi unavyoonyesha.

Kichwa katika Daily News la Chicago kinasema: “Kupiga Punyeto Hakudhuru kwa Kimwili.” Chini ya herufi kubwa za urefu wa nusu-inchi kwenda juu linaeleza namna mtaalamu wa chuo kikuu wa afya anavyowasihi waalimu na vijana washauri wasaidie “kuondosha woga na masumbufu” juu ya mazoea haya. Vile vile inasemekana kwamba “mstadi ajulikanaye sana wa mambo ya wanaume na wanawake” aliwaambia wanafunzi ‘wasonge mbele wakapige punyeto’ wakati wa somo la mambo ya wanaume na wanawake shuleni. Kikaratasi kinachoenezwa sana katika madarasa ya Ufaransa kinapendekeza kupiga punyeto, kikisema “kwaweza kuujaza utupu wa somo la saa moja au wa jioni yenye kuchosha.”

Viongozi wengi wa kidini vile vile wanatia moyo mazoea haya. Kwa mfano, habari iliyotumiwa sana na Kusanyiko Kuu la washiriki milioni 3.1 wa United Presbyterian Church yasema hivi, kwa sehemu: “Hatuoni ushuhuda wo wote wa mashutumu ya kidini, ya moyo wa kibinadamu wala ya utabibu unaopinga kupiga punyeto kwenyewe. . . . Hata kuna sababu fulani ya ubora hakika wa kupiga punyeto.” Katika sinema iliyotayarishwa na wanadini wa Kimethodist wao vile vile wanadai kwamba kupiga punyeto ‘ni shauri bora linaloweza kuchukua mahali pa ngono.’ Sinema hii inaonyesha waziwazi namna wanaume na wanawake vile vile wanavyoweza kupiga punyeto.

Watu wenye mamlaka wa utabibu kwa kawaida wanachukua hali ile ile. Kama vile anavyosema daktari mmoja: “Mimi nakazia ukawaida wa kupiga punyeto, kuzoewa kwake na watu kwa jumla, na kutokudhuru kwake.”

MAZOEA YA KAWAIDA SANA

Katika kizazi hiki cha fujo lazima mtu akubaliane na madaktari juu ya “mazoea ya watu kwa jumla” ya kupiga punyeto. Zitazame habari: “Kila uchunguzi wa makini tufanyao waonyesha wazi kwamba . . . walau 95 kwa mia ya wavulana na vijana wenye umri wa kuanzia miaka kumi na mitatu mpaka 25 wanapitia katika vipindi vya kupiga punyeto kwa kawaida vyenye urefu unaotofautiana,” asema mtu mmoja mwenye mamlaka juu ya habari hii. Kwa habari ya wasichana, chanzo hiki kinasema kwamba “40 mpaka 50 kwa mia wanapatikana wenye kupiga punyeto kabisa.”

Watu wengine wanasema kwamba tarakimu hizi zahakikisha “ukawaida,” na kwamba “kutokuwamo kwa kupiga punyeto katika kijana mwenye afya ni jambo la kuhangaikia.”

Sasa waonaje? Je! unakubali kwamba kwa kuwa ni jambo la kawaida sana, karibu kuwa mazoea ‘ya watu kwa jumla,’ kwamba hii inafanya kupiga punyeto kuwe kazi ya asili na ya kawaida ya mwili? Kusema uongo na kuiba vinaonekana sana leo, na ndivyo na matumizi ya tumbako. Lakini usingesema hii inavifanya viwe vitu vya asili na vifaavyo, sivyo? Mafua “yaliyo ya kawaida” yanawapata watu kwa jumla lakini hii bila shaka haiyafanyi kuwa ya kawaida au ya asili, sivyo?

Basi namna gani juu ya dai la kwamba kupiga punyeto hakudhuru? Je! maneno yaliyotumiwa wakati uliopita yanayofanana​—kama vile “kujichua” na “kujipura”​—si yenye nguvu tena? Mambo ya hakika ni nini?

NI NINI MATOKEO YA MAZOEA HAYA?

Katika karne ya kumi na tisa, na mpaka karibuni sana, ilidhaniwa kwamba kupiga punyeto kungeweza kuiharibu afya ya kimwili ya mtu, kukitokeza mambo kama sura nyeupe isiyo ya afya, ulegevu, hali ya kutoweza kupata usingizi, kifua kikuu, kutoweza kuzaa, udhaifu wa akili, kuumbuka kwa viungo vya uzazi na madhara mengineyo ya kimwili. Lakini, siku hizi imehakikishwa kwamba kupiga punyeto hakusababishi mambo haya. Ni katika visa vinavyopita kadiri tu ambapo wanaume wanapiga punyeto kupita kadiri wanapokuwa wasioweza kuzaa au wanakuwa na shahawa isiyo na ubora mwingi. Mtu mmoja mwenye mamlaka anayesema maoni ya madaktari kwa uchache, akitaja: “Hakuna ushuhuda wo wote wa kisayansi kwamba kupiga punyeto kunadhuru kwa kimwili.”

Ikiwa hakudhuru kwa kimwili, namna gani afya ya akilini, ya moyoni na ya adili ya mpiga punyeto?

Jambo lililo la maana sana, madaktari wanaotuhakikishia kwamba hakuna madhara ya kimwili hata hivyo inawalazimu kuyazungumza madhara ya akilini na moyoni yanayosababishwa na mazoea haya. Chasema hivi Encyclopedia Americana: “Hali iliyo ya kisasa zaidi kuelekea kupiga punyeto ni kwamba matokeo yenye kudhuru yanayoonekana sana . . . hayatokani na madhara yo yote kwa kimwili bali kutokana na mawazo ya ndani ya wale wanaojivunjia heshima na kutokana na maelekeo kuliko nayo ya kuwaondosha katika ujamaa wa kweli na wenzao.”

Bila shaka, dai linafanywa kwamba mawazo hayo ya ndani ya hatia yanatokea kwa sababu tu watu mmoja mmoja wamefundishwa tangu utotoni kuona kupiga punyeto kama jambo lisilo la adabu. Wengi wanasema mawazo haya ya ndani ya hatia si ya akili. Lakini je! ndivyo ilivyo?

Watu walio wengi watakubali kwamba, kwa kweli, ni wazazi wachache wanaouchukua wakati ama kupendezwa na kuzungumza kupiga punyeto na watoto wao. Kwa hiyo, basi, kwa sababu gani mvulana mchanga (au msichana) anayejitia katika kupiga punyeto kwa mara ya kwanza hata hivyo anajiona mwenye hatia? Kwa sababu gani wingi wa wanaojitia katika mazoea haya wanafanya hivyo kwa siri, kwa kujificha?

Kwa sababu kupiga punyeto ni jambo lisilo la asili. Hata hivyo, watoto wadogo wana mawazo machache juu ya ngono ya mwanamume na mwanamke. Lakini kubalehe kunaleta ujuzi wa ndani unaomwambia mwanamume uradhi wake wa tamaa ya ngono utapatikana katika mwanamke, naye mwanamke vivyo hivyo. Kupiga punyeto (kama kulalana kwa mwanamume na mwenzake na mwanamke na mwenzake) kunaupuza mpango huo wa asili. Ni namna moja ya kuacha “matumizi ya mke, ya asili” kwa ajili ya “matumizi yasiyo ya asili.” Kwa hiyo, alama ya dhamiri aliyoitoa Mungu iliyomo katika wanadamu wote kwa njia ya asili, inajifanya isikike katika kuyakataza mazoea hayo, ikitokeza maoni ya ndani ya hatia.​—Linganisha Warumi 1:26, 27; 2:14, 15.

Kwa hiyo, ingawa madaktari wengi pamoja na wale wa akili na moyo wanafanya ionekane kwamba mawazo ya ndani ya hatia juu ya kupiga punyeto yanasababishwa kwa jumla na ‘mafundisho ya kijamii na malezi’ ya mtu, yaweza kuwa ni tofauti yake. Yaani, inaelekea zaidi kwamba, ambapo hapana mawazo hayo ya ndani ya hatia, hii ni kwa sababu mtu mwenyewe aliongozwa na wengine kuamini kwamba mazoea ya kupiga punyeto kwa kweli “ni sawa,” “ya kawaida,” hata “yenye kufaidi.” Kwa hakika maenezi ya maarifa ya kisasa yanajaribu kuikomesha au kuiharibu dhamiri iliyotolewa na Mungu.

Kwa kuwa mazoea ni yale “yasiyo ya asili,” mpiga punyeto anapata adhabu ya akilini. Mazoea ya kawaida yanaharibu maendeleo yake ya kijamii na ya akilini na moyoni, yanamzuia asiwe na maoni yenye afya na nia kuelekea watu wa kike akiwa ni mwanamume na watu wa kiume akiwa ni mwanamke na kwa jumla watu wote. Yaweza kumfanya mtu awe na mazoea ya kufikiri mawazo na maono ya nafsi yake mwenyewe. Au yanaweza, na mara kwa mara yanafanya hivi, kuelekeza kwenye kumlala mwanamume mwenzake au mwanamke mwenzake, ambamo mtu huyo asiyetosheka na utendaji wake wa kipekee wa kiungo cha uzazi, anatafuta mwenzi wa kutumia pamoja naye viungo vya uzazi. Ingawa wanazungumza juu ya ‘ukawaida’ wa kupiga punyeto, watu wenye mamlaka wa utabibu na washughulikiao ugonjwa wa akili lazima wakubali kadiri ambavyo kupiga punyeto kwa mazoea kunavyokuwa kizuizi kabisa cha ndoa yenye furaha na uradhi nyumaye katika maisha. Mambo ya hakika yaonyesha kwamba si jambo lisilo la kawaida kwa mazoea haya kuendelea nyuma ya ndoa hata mahali ambapo mpiga punyeto anaona lazima ya kutafuta msaada wa daktari wa ugonjwa wa akili. Kwa sababu gani iwe hivyo, yakiwa mazoea haya ni “ya kawaida,” “ya asili” na “yenye kufaidi”?

Lakini, ili kuliona jambo hili kwa busara nyingi, inasaidia kufahamu mambo fulani juu ya namna sisi wanadamu tulivyoumbwa​—⁠kwa kimwili, kwa akili na kwa moyo.

NAMNA TULIVYOFANYIZWA

Wakati wa kubalehe, kijana wa kiume au wa kike anapokua kwa habari ya viungo vya uzazi akawe mtu mzima, mageuzi mengi yanatokea mwilini. Vitu vilivyomo damuni, vinavyofanyizwa na kifuko kisicho na kifereji kilichoko chini ya ubongo, mapumbu na vifuko vingine vimo kazini vikifanyiza mageuzi haya. Kwa mvulana, hii inafanya mapumbu yake yaanze kufanyiza chembe za shahawa.

Kwa hiyo basi ni jambo la asili kwa mwanaume mwenye afya na wa kawaida kuwa na nyege za kadiri fulani. Mpango wa ndoa unatoa njia ya kutoshelezea nyege hizo. Lakini namna gani juu ya wale wasiooa au kuolewa? Je! kupiga punyeto ndiyo njia ya pekee​—karibu kufanya uasherati​—ya kuondolea mkazo wa nyege hizo? Na je! ikiwa kupiga punyeto hakuingiliwi, shahawa inayoongezeka itakuwa na matokeo fulani yenye kudhuru?

Jibu kwa maulizo haya ni, Hapana. Zipo njia nyingine za kupunguzia au kuondolea nyege. Moja ni “kusahihisha”​—yaani, kuuelekeza mkazo kwenye utendaji mbalimbali wa kimwili na wa akili. Hivyo mvulana anayekua na kijana wanaweza kuendelea kuwa wenye shughuli na wenye furaha wakijitahidi katika kazi mbalimbali na mambo fulani ayapendayo mtu mwenyewe.

Namna gani juu ya kuongezeka kwa shahawa mwilini? Hakuna hatari ya kufikia kwake kwenye mahali pa kuleta madhara yo yote ya kimwili. Na, kwa hakika, nyege zinaongozwa zaidi na mambo ambayo mtu mwenyewe anayaweka akilini. Halafu, tena, mwili wa mwanamume kwa kawaida unapunguza kadiri ya shahawa kwa njia ya kuitoa vipindi kwa vipindi usiku wakati wa usingizi. Kadiri ndogo kuliko vijana 5 kwa mia wenye umri wa miaka 19, kwa mfano, wanasemekana kutokupatwa na haya. (Ajapokuwa mtu hatoi shahawa hiyo, haimaanishi kwa lazima kuna jambo lililo kombo kwa viungo vya uzazi.) Kinachotukia kwa mwanamume wa kawaida ni kwamba, wakati wa usiku kibofu kinapojawa na mkojo, mkazo unaongezeka juu ya sehemu za akiba ya shahawa zilizo karibu nacho. Huenda hii ikaanzisha kutoka kwa shahawa vipindi kwa vipindi bila ya mtu kujua anapokuwa amelala.

Akieleza kwa sababu gani kutoka huko kwa shahawa kunaitwa “ndoto za majimaji,” na mara nyingi zinafuatana na kuota kwa upumbavu na kwa upuzi, mtaalamu wa elimu ya maendeleo ya kijamii Herbert J. Miles anaandika:

“Haja inayoongezeka ya kuondoa yaliyomo katika kibofu inamfanya mtu kuondoka usingizini kidogo kidogo ambapo akili yenye fahamu inapumzika kuelekea ufahamu wenye bidii wa akili, inayoamuka. Wakati wa kutoka huku kwa polepole usingizini kuelekea kuamka akili imo katika namna ya ‘eneo la mapambazuko’ ambamo akili yenye fahamu kidogo inatenda. Maoni na mawazo yamechanganyika, yamevurugika, na huenda yakatoka kwa maoni mamoja, maono, au tendo mpaka kwa tendo jingine. Maoni haya yaliyochanganyika, yaliyovurugika huenda yakatia ndani mawazo ya mambo ya wanaume na wanawake au utendaji ambayo yasingevumiliwa kama akili yenye fahamu ingalikuwa inaelekeza mawazo.”​—Sexual Understanding Before Marriage, kur. 160, 161.

Basi, hakuna haja ya mtu kujiona mwenye hatia kwa sababu ya kutoka huko kwa shahawa au ndoto zinazofanya hili litukie​—isipokuwa anajua kwamba amekuwa akiyaacha mawazo yake yakae juu ya ufisadi au katika njia isiyo nzuri ya mambo ya wanaume na wanawake.

Lakini, je! kupiga punyeto hakuna matokeo mema zaidi na si kwenye kuridhisha zaidi katika kuondoa wasiwasi wa mambo yanayowapasa wanaume na wanawake kuliko kutoka huku kwa shahawa wakati wa usiku?

Hapana; kwa sababu mahali pa kuondoa wasiwasi kwa wepesi na kwa mara hiyo, mpiga punyeto anaona kwamba utaratibu wake wote wa mishipa ya vena unasisimuliwa sana wasiwasi unapoongezeka kwa sababu ya msisimko wa mtu mwenyewe. Nyuma yake huenda hii ikaacha mtu na maoni ya mvunjo wenye wasiwasi na wenye kuchukiza. Lakini karibuni yeye anakuwa na tamaa yenye kulazimisha alirudie tendo hilo. Ni kipindi kibaya ambacho ni vigumu kukikatiza na kisichotoa uradhi wo wote wa kweli.

Kwamba kupiga punyeto si jambo la kawaida na kwamba si la asili vile vile yaonyeshwa na uhakika wa kwamba watu wasio wa kawaida walioharibika akili ni wapiga punyeto wabaya. Linalofanana kidogo, The Bremerton Sun (Washington) lasema kwamba mapadre wengi walio na masumbufu ya akili na watawa wa kike ni wapiga punyeto wa kuzoea.

MAONI YA MKRISTO YA KUPIGA PUNYETO

Yajulikana sana kwamba leo watu wa ulimwengu, pamoja na kadiri kubwa kwa mia ya waendao kanisani, “wakiisha kufa ganzi,” wanatia moyo na kupendekeza mazoea yasiyo ya asili ya kupiga punyeto. (Efe. 4:19) Tofauti sana na hilo, Wakristo wa kweli wanajaribu kujifunza na kufuata ambavyo Neno la Mungu Biblia linasema juu ya mambo yawapasayo wanaume na wanawake na ya adili. Kweli, maneno “kupiga punyeto” na “kujipura” hayamo katika Biblia. Sheria ya Musa inazungumza juu ya ‘kutoka kwa shahawa,’ lakini kama waelezavyo wafafanusi wa Biblia, mtajo ni juu ya kutoka kwa shahawa bila ya kujua wakati wa usiku, siyo kutoka kwake kulikolazimishwa na mtu mwenyewe. (Law. 15:16) Lakini, kuna kanuni za Biblia zinazozungumza vya kutosha shauri la kupiga punyeto.

Kwa mfano, Wakolosai 3:5, 6 inasema: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu: kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu.” Kama tulivyoona, kupiga punyeto ni “mawazo mabaya” kabisa. Vile vile ni “uchafu,” kwa maana ni mazoea ya ufisadi, na hii yaeleza sababu gani mpiga punyeto kwa kawaida anaona aibu juu ya anachokifanya na kulificha tendo lake la kuchukiza lisionekane na wengine.

Shauri la mtume wa Kikristo Paulo li katika maana yenyewe: “Mungu hakutuitia uchafu, bali tuwe katika utakaso.” Na tena anaandika: “Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.”​—1 The. 4:7; 2 Kor. 7:1.

Namna gani juu ya “tamaa mbaya” ya mpiga punyeto? Je! ‘inafishwa’? Au yeye anailisha tamaa yake sikuzote na kuitia nguvu mpya, ndiyo, hata kufikia mahali pa “kutangulia kupanga kwa ajili ya tamaa za mwili,” tofauti na shauri la Biblia?​—Rum. 13:14, NW.

Andiko linataja kwamba “kutamani, ndiyo ibada ya sanamu,” kwapaswa ‘kufishwe’ vile vile. Hili lingetumika hapa, kwa maana upendano wa mpiga punyeto unaondoshwa kwa Muumba na kuwekwa juu ya kitu kinachotamaniwa, kwa habari hii viungo vyake vya uzazi, vinavyochukua umuhimu usiofaa. Kwa hiyo basi mazoea haya yanaweza kuelekea kwenye ibada ya sanamu, kama vile katika mazoea ya kale ya ibada ya nguvu ya uzazi iliyochukiwa sana na Mungu. Mahali pa kujitoa ‘kwa nafsi yote kwa Yehova’ (Kol. 3:23), mtu aweza kuwa mtumwa wa tamaa zake za kimwili na hamu na kuvifanya hivi chombo cha ibada yake. “Watu kama hao,” mtume asema, “hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali tamaa zao wenyewe zilizo mbaya,” “hamu zao ndizo mungu wao.”​—Rum. 16:18; Flp. 3:19, An American Translation.

Neno autoerotism la Kiingereza linamaanisha kwa halisi upendo wa mtu mwenyewe au ukware wa mtu mwenyewe. Ni neno jingine linalotumika kwa kufaa kwa kupiga punyeto, kwa maana mazoea yanayoendelea yanayafanya mawazo ya mtu kugeukia ndani hivi kwamba anakuwa mwenye kufikiri yake mwenyewe na mchoyo, pamoja na magumu katika kujifungamanisha na wengine. Kwa sababu hii wataalamu wengine wa akili na moyo wa mwanadamu wamekutaja kupiga punyeto kwenye kumfurahisha mtu mwenyewe kama narcissism, kwa kulingana na mungu wa uongo wa Kigiriki Narcissus, aliyependana na mfano wake mwenyewe, kwa uharibifu wake. Je! Biblia haikuonya kwamba ‘watu watakuwa wajipendao wenyewe’ katika hizi “siku za mwisho”?​—2 Tim. 3:1, 2.

Kuendeleza hali ya kutokuoa au kutokuolewa kama “matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni” kuna faida nyingi katika huu wakati wa mwisho. (Mt. 19:12; 1 Kor. 7:32-38) Lakini ye yote asifikiri kwamba kukimbilia kupiga punyeto ndiyo njia ya kufanya hivi. Bali, kujiweza ndio ufunguo wa kuwa na matokeo mazuri katika hali ya kutokuoa au kutokuolewa. ‘Bila kujiweza, na waoe au kuolewa,’ lingali ndilo shauri bora.​—1 Kor. 7:9.

‘Lakini je! kukomesha nyege hakutauharibu utu wangu na kuuvunja utaratibu wangu wa mishipa ya neva?’ huenda mtu aulize. Chajibu kitabu Why Wait Till Marriage?: “Hakuna ushuhuda wa kwamba kujiweza kunadhuru maisha yako kama mwanamume au mwanamke. . . . Mtu au msichana azungukaye nyege zake zikiwa wazi ndiye aliyemo katika hatari iliyo kubwa zaidi. Mtu anayejiweza anaweza kustahimili kungoja.” Nao huu si ugumu mkubwa sana ikiwa mtu anayo roho ya Mungu, kwa maana tunda la roho ni pamoja na “kujiweza.” Akiwa na kujiweza Mkristo aweza kuepuka namna zote za kupiga punyeto, kisha apate faida nyingi​—⁠za akilini, za moyoni na za kiroho zilizo zenye kuridhisha hata zaidi kuliko “matendo ya mwili” yenye kufisha.​—Gal. 5:19-23.

Lakini je! mazoea haya yanayoisumbua dhamiri ya watu wengi sana wanakuja kuyapataje kwa mara ya kwanza?

ULINZI NA KUPONYA

Mtu akifahamu sababu, ni vyepesi kufanyiza ulinzi na kuponya mazoea mabaya. Kwa mfano, je! ulijua kwamba akina mama na akina baba wanaopapasa viungo vya vitoto vyao vitukutu ili wavitulize bila ya kujua wanavitia moyo viwe wapiga punyeto nyumaye? Wavulana na wasichana huenda wakaanza kuchezea sehemu zao za siri wakati wa kubalehe na, wasipopokea onyo lo lote juu ya hili, bila ya kutazamia wamekwisha “kutegwa” katika mazoea haya. Na ikiwa wengine hawajui lo lote juu ya kupiga punyeto huko mbele ya kuingia katika shule ya masomo ya juu, yaelekea watajifunza kutokana na wanafunzi wenzao ama waalimu wenyewe.

Uchunguzi waonyesha kwamba kadiri kubwa kwa mia ya kupiga punyeto haisababishwi sana na kuongezeka kwa mkazo wa tamaa kutoka kwa namna zile zile za wasiwasi na masumbufu yanayoleta hali ya kutoweza kupata usingizi. Vijana wengi na watu wazee walio na wasiwasi wa magumu ya maoni wanakimbilia kupiga punyeto kama njia ya kutorokea masumbufu yao ya kimwili na ya moyoni​—⁠namna ya kisuluhishi au kitulizo, ndivyo wanavyofikiri, cha kuyasahau masumbufu yao. Kwa hiyo, tena, watu wanaosumbuliwa na uchovu, watu wasioajiriwa na wafungwa, zaidi ikiwa wamekuwa wakitumia dawa za kulevya, mara nyingi wanapiga punyeto.

Kwa kuyaepuka mambo haya yanayosababisha na kutia moyo kufanya mazoea haya, mtu anajitahidi sana kuyazuia mazoea haya magumu yasianze. Lakini je! maelfu ya watu walio na mazoea haya sasa wanaweza kufanya nini wayavunje?

Mambo mengi yanashauriwa. Epuka kushirikiana ama na vitabu vya kimalaya ama na wale walio wapotovu. Uzidi kuwa mwenye shughuli ukifanya kazi kwa bidii, kwa kimwili na kwa akili. Usiruhusu magumu yafanyize wasiwasi, unaosababisha masumbufu yanayoihuzunisha akili. Kufanya hivi si vigumu mno mtu akifuata shauri la Biblia katika Mathayo 6:25, 33 na katika Wafilipi 4:8. Usiwe “mpweke” wakati wo wote, ukijaribu kujitenga. Kwa hiyo, wakati wa usiku panga kulala katika chumba kimoja na washiriki wengine wa jamaa. Lala kwa upande, siyo kichalichali wala kifudifudi. Haya ni mawaidha machache ya kupangia kawaida ya kila siku.

Lakini, mtu hawezi kutumaini kuyavunja mazoea haya bila ya kuwa na tamaa ya moyoni ya kuacha. Maadam “tamaa ya mwili, na tamaa ya macho” ni zenye nguvu zaidi kuliko tamaa ya mtu ya kumpendeza Yehova, ni vigumu kuacha. (1 Yohana 2:16; linganisha Yakobo 1:14, 15.) Mara unapokuwa na tamaa ya kweli ya kuyaacha mazoea haya yasiyopendeza, endelea kujitwalia silaha hizi zenye muhimu sana​—uthabiti wa moyo, nia na kujiweza​—ikiwa watumaini kulishinda pigano. Halafu tena, sala haiwezi kusahauliwa, kwa maana Yehova anaahidi kuwabariki wale wanaoomba msaada katika kushughulika na magumu yetu yote.​—Flp. 4:13; Kol. 4:2; 1 Pet. 4:7.

Watu wengine wanaona ni vigumu sana kuyakatiza mazoea haya kwa ghafula. Kwa hiyo, wanapourudia mwendo mbaya nyakati nyingine​—⁠kwa kawaida wakiwa katika hali ya usingizi kidogo​—⁠wanakuza mawazo ya ndani sana ya hatia na ya kutokustahili rehema ya Yehova. Kwa sababu hizi haisaidii tu lakini mara nyingi ni jambo bora kuutafuta msaada na faraja ya mzee wa Kikristo. Wakati ambapo msichana ana ugumu huu huenda akataka kumfikia ama mzee ama dada wa Kikristo aliyekomaa, anayeheshimiwa kwa msaada.​—Tito 2:2-4.

Nguvu nyingine yenye kuvuta ya kumsaidia mtu ayaache mazoea haya huenda ikawa ni tamaa ya kutumikia zaidi katika kundi la Kikristo. Ikiwa mwanamume “anafikia” pendeleo kama hilo amepaswa aangalie kwamba mojawapo la matakwa ya uzee wa Kikristo ni ‘kujiweza.’ (1 Tim. 3:1; Tito 1:8, NW) Ikiwa mwanamume anapiga punyeto kwa kawaida, je! angeweza kuzitimiza kanuni hizo? Kweli, huenda mtu aliye na cheo hicho tayari akawa na jaribu la muda la ugumu huu na, akipigana nao na kuushinda, haimpasi ajisikie asiyestahili. Lakini mpiga punyeto wa kuzoea, akiwa hana kujiweza, yumo katika hatari ya kushindwa na makosa mazito hata zaidi. Hayumo katika hali ya kutumikia kama ‘kielelezo kwa lile kundi’ hata kidogo. (1 Pet. 5:2, 3) Basi, tamaa ya kuwa mwenye utumishi wa upendo kwa Mungu na ndugu ya mtu, yaweza kumsaidia mtu vile vile ajiachishe na mazoea ya kupiga punyeto.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki