Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 8/15 kur. 20-24
  • Kuendelea Kuwa na Maoni ya Mungu Juu ya Ngono

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuendelea Kuwa na Maoni ya Mungu Juu ya Ngono
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujiingiza kwa Malaika
  • Ngono Zilizopotoshwa—Wakati Uliopita na Wakati Huu
  • Maoni ya Biblia Juu ya Ngono Zilizopotoshwa
  • Kulalana kwa Watu wa Jinsia Moja ni Nini?
  • Kuepuka Mwenendo Mbaya wa Ngono
  • Maoni ya Biblia Juu ya Kupiga Punyeto
  • Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Maoni Yako Juu ya Ngono—Yanafanyiza Tofauti Gani?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Kuacha Kupiga Punyeto—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Ugoni-Jinsia-Moja—Je, Kweli Ni Mbaya Hivyo?
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 8/15 kur. 20-24

Kuendelea Kuwa na Maoni ya Mungu Juu ya Ngono

BABA yetu wa kimbingu mwenye upendo aliwaumba wazazi wetu wa kwanza wakiwa na zawadi nzuri ajabu ya ngono. Yeye alitia ndani yao tamaa yenye nguvu sana ya kutaka kufunga ndoa na mambo yanayohusiana nayo ili kuwe uhakikisho kwamba jamaa ya kibinadamu ingeendelea kuwapo. Bila shaka, tunapofikiria juu ya mpango huo na uwezekano mkubwa wake wa kuleta raha na furaha kwa wanadamu, tunachochewa tumsifu Mungu Mkuu wetu kwa ajili ya kufikiria njia hiyo nzuri ajabu ya kuijaza dunia.​—Mwanzo 1:27, 28.

Basi haishangazi kwamba wakati Shetani Ibilisi alipomwasi Mungu, yeye alianza kuharibu mpango huo mzuri wa kutokeza jamii nzima ya kibinadamu. Sasa akishughulika na akili za wanadamu waliozaliwa katika hali ya kutokamilika, aliweza kupotosha nia zao kuelekea matumizi yanayofaa ya uwezo wao wa ngono waliopewa na Mungu. Biblia inaonyesha kwamba kufikia wakati wa Gharika, ‘mawazo ya moyo wa mwanadamu yalikuwa yamekuwa mabaya tangu ujana wake.’ (Mwanzo 6:5, 6; 8:21) Jamaa ya kibinadamu ilipozama ndani ya mwendo wa ukosefu wa adili, malaika mbinguni walikuwa wakitazama.

Kujiingiza kwa Malaika

Mungu hakuwaumba malaika wakiwa na tamaa ya kufanya ngono pamoja na wanadamu. Lakini kwa wazi Shetani aliweza kuwafanya wengine wao wafikirie isivyofaa juu ya mambo hayo. Kwa hiyo ndani ya malaika fulani fulani tamaa ilisitawishwa ya jambo ambalo Mungu alikusudia wanadamu peke yao ndio walifurahie ndani ya vifungo vinavyofaa vya ndoa. “Wana wa Mungu” hao wa kimalaika walifanya jambo ovu, wakaacha vyeo vyao mbinguni ili waje duniani kuoa wanawake. (Mwanzo 6:2) Tendo hilo lilichochewa na tamaa iliyositawishwa vibaya, wala si tamaa ya asili iliyotiwa ndani yao na Mungu. Kwa kuwa malaika wanaweza kusitawisha tamaa hizo za ngono zisizo za asili, basi tusishangae kwamba wanadamu pia wanaweza. Akiandika chini ya uongozi wa Mungu, mwanafunzi Yuda alilinganisha malaika waliotamani binti za watu na wanadamu fulani wanaofanya mapenzi na watu wa jinsia yao. Yeye aliandika:

“Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu. Kama vile Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa kando-kando, waliofuata uasherati kwa jinsi moja na hawa, wakaenda kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili, imewekwa kuwa [mfano wa kuonya], wakiadhibiwa katika moto wa milele.”​—Yuda 6, 7.

Ngono Zilizopotoshwa—Wakati Uliopita na Wakati Huu

Tukiwa wanafunzi wa Biblia, tunajua yaliyoupata Sodoma wa kale​—jinsi wanaume na wavulana wachanga wenye wazimu wa kufanya ngono wa mji huo walivyoamuru wanataka kufanya ngono na wale ambao waliwadhania kuwa wageni wa kiume tu katika nyumba ya Lutu. (Mwanzo 19:4-11) Tukio hilo lilitokea miaka karibu 450 tu baada ya Gharika. Katika nyakati hizo za mapema pia likawa jambo la kawaida kwa wanadamu kufanya ngono pamoja na wanyama. Kwa hiyo, miaka 400 hivi baadaye, katika mahali panne tofauti-tofauti, Sheria ya Mungu aliyolipa taifa la Israeli ililaani zoea hilo, na adhabu ya wenye kuivunja ilikuwa kifo. (Kutoka 22:19; Mambo ya Walawi 18:23; 20:15, 16; Kumbukumbu la T0rati 27:21) Pamoja na hilo, Sheria ya Mungu kwa Israeli ilisema kufanya ngono kwa watu wa jinsia moja kulikuwa ni kosa lenye kustahili kifo​—wakosaji walihukumiwa kifo.​—Mambo ya Walawi 18:22; 20:13.

Hata hivyo, katika karne zilizofuata, watu waliokuwa wakiishi kuwazunguka Waisraeli walikuwa wenye kuzoea sana kufanya ngono za watu wa jinsia moja hata kwamba Waisraeli wenyewe pindi baada ya pindi wakahusika katika ngono za watu wa jinsia moja. (1 Wafalme 14:24; 15:12; 22:46) Katika pindi moja Mlawi mmoja alikuwa mgeni katika nyumba moja ya mji wa Gibea wa Kibenyamini, na wanaume wa mji huo wakaizunguka nyumba hiyo wakipaza sauti hivi: “Mlete nje mtu yule aliyefika nyumbani kwako, ili tupate [kufanya ngono naye].” (Waamuzi 19:22) Karibu kabila lote la Benyamini lilifagiliwa mbali kwa kufuata mwelekezo wa Yehova kwa sababu ya jambo hilo.

‘Lakini kwa nini kutokeza historia hiyo ya Biblia isiyopendeza,’ huenda wengine wakawa wanafikiri. Ni kwa sababu leo tunaishi katika jumuiya ambayo imezama katika ukosefu mkubwa sana wa adili, na pia watu wa Mungu wa kisasa wanaelekewa na hatari hiyo. Fikiria kifupi kadiri yakulalana kwa watu wa jinsia moja na matokeo yake:

“Kama 30% ya watu wa [San Francisco] ni watu wa jinsia moja wenye kulalana,” ndivyo linavyosema Medical Tribune la Septemba 23, 1981.

“Suala la [miaka ya kuanza na wa] 1980 ni uvutano wenye kuongezeka wa watu wa jinsia moja wenye kulalana juu ya watu wengine na​—la maana zaidi​—juu ya viwango vya watu wenye kufanya ngono za kawaida. . . . Kukubali kwa ujumla zoea la watu wa jinsia moja wenye kulalana ni ishara kwamba imani zetu za maana zimekuwa zikibadilika,” ndivyo linavyoripoti gazeti Maclean’s la Februari 18, 1980.

“Wingi mkubwa wa watu wa jinsia moja wenye kulalana katika tafrija na matangazo ya habari unawaweka watu wa jinsia moja wenye kulalana katika hali ya kuweza kupotoa viwango na maoni,” ndivyo anavyosema profesa mmoja kwenye Chuo Kikuu cha Sydney katika Australia.

Hakika nia za watu zinapotoshwa zikubali kulalana kwa watu wa jinsia moja kuwa jambo la kawaida, hata kuwa linalofaa. Kulingana na gazeti The Toronto Star la Agosti 24, 1980, “Washiriki wachanga wa United Church . . . wanakubali wazo la kuwa na wahudumu wa jinsia moja wenye kulalana.” Gazeti Daily Mail la London la Juni 5, 1980, linasema: “Kulalana kwa watu wa jinsia moja hakupaswi kuzuia mtu asiwe na cheo katika Kanisa la Methodisti, ndivyo ripoti iliyoandikwa upya inavyopendekeza.” Na wakati mwanamke mmoja alipoandika kusema kwamba alishtuka kwamba mjukuu wake wa kiume mwenye miaka 23 alikuwa akilalana na watu wa jinsia yake, mwandikaji mmoja wa safu ya gazetini alijibu: “Mungu hakuandika Biblia. Kulalana kwa watu wa jinsia moja kumekuwako muda mrefu kama wanadamu . . . Unalopaswa kufanya sasa ni kujifunza kumkubali jinsi alivyo. Yeye yungali mwanamume kijana mzuri.”

Maoni ya Biblia Juu ya Ngono Zilizopotoshwa

Kwa sababu ya porojo za kilimwengu hata wengine kati ya watu wa Mungu wamevutwa hata waone kulalana kwa watu wa jinsia moja na ngono nyingine kama hizo zilizopotoka kuwa ‘si mbaya sana.’ Lakini, Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilisema watu wa jinsia moja wenye kulalana walipaswa kuuawa! Na katika Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki, andiko la 1 Wakorintho 6:9, 10 linasema, kulingana na New International Version: “Msidanganywe: Wala wakosefu wa adili za ngono . . . wala wazinzi wala malaya wa kiume wala wakosaji wa jinsia moja wenye kulalana . . . hawataurithi ufalme wa Mungu.” Na, kulingana na tafsiri iyo hiyo ya Biblia, Warumi 1:26, 27 husema: “Hata wanawake wao walibadili ngono za kawaida kuwa zisizo za kawaida. Vivyo hivyo wanaume pia waliacha ngono za asili pamoja na wanawake wakawakiana tamaa wao kwa wao. Wanaume walifanya vitendo visivyo vya heshima pamoja na wanaume wengine.” Mstari wa 32 unaendelea kusema: “Wale wanaofanya mambo hayo wanastahili kifo.”

Kwa kushangaza, wengine ambao wamehusika katika mwenendo wenye ukosefu wa adili, kama vile kulala wanyama, hawakuona kwamba walilofanya lilikuwa baya sana. Lakini kufanya ngono na mnyama ni kosa. Ni sababu ya kutengwa na ushirika na kundi la Kikristo. Vivyo hivyo, wengine kwa maneno yao wameonyesha kutokuelewa kwao juu ya ni nini mazoea ya watu wa jinsia moja kulalana. Basi, kulalana kwa watu wa jinsia moja ni nini?

Kulalana kwa Watu wa Jinsia Moja ni Nini?

Ili kuelewa hilo, angalia mafafanuzi ya kamusi juu ya kulalana kwa watu wa jinsia moja:

Kamusi ya Webster’s Third New International Dictionary of the English Language: “Tendo la mapenzi pamoja na mtu wa jinsia moja.”

Kamusi The American Heritage Dictionary: “1. Tamaa ya ngono na wengine wa jinsia moja. 2. Ngono pamoja na mwingine wa jinsia moja.”

Kamusi The Random House Dictionary of the English Language: “Tamaa ya ngono au tabia inayoelekezwa kwa mtu au watu wa jinsia moja.”

Ni jambo linalovuta fikira kwamba kulingana na mafafanuzi ya kamusi, kulalana kwa watu wa jinsia moja kunatia TAMAA ya kufanya ngono pamoja na wengine wa jinsia moja. Lakini Biblia inatofautisha zoea la yaliyo mabaya na tamaa au maelekeo ya dhambi. Huenda tamaa hizo zikawapo zijapokuwa jitihada za bidii za kuziondoa akilini na mwilini. Kwa sababu ya mazingira yao ya maisha hapo kwanza, na pengine mambo mengine, huenda tukawa na ndugu na dada Wakristo ambao pindi kwa pindi wanatamani kufanya ngono pamoja na watu wa jinsia yao wenyewe. Lakini wanapigana na tamaa hiyo isiyo ya asili yenye kuongozwa na Shetani​—na hawakubali kushindwa na tamaa hiyo. Kwa hiyo wao si wenye zoea la watu wa jinsia moja wenye kulalana. Wanaongoza mawazo yao, wakijua kwamba tamaa mbaya inayoruhusiwa ikue ni lazima itajionyesha yenyewe katika matendo mabaya.​—Yakobo 1:14, 15; Wakolosai 3:5-10.

Kinacholaaniwa na Mungu katika Biblia, na ambacho ni kosa la kutengwa na ushirika, ni “tendo la mapenzi,” au ‘tabia ya ngono,’ inayoelekezwa kwa mtu mwingine wa jinsia moja. Tendo hilo, au tabia, si lazima iwe ni kutia uume ndani ya mkundu ndipo kuwe ni kulalana kwa watu wa jinsia moja. Tendo lo lote linalohusu viungo vya uzazi vya angalau mmoja wa watu hao, kama vile kupiga busu, kupapasana, kusugua viungo vya uzazi vya mmoja juu ya mwingine, au tabia nyingine kama hiyo yenye kusudi la kuleta raha ya ngono pamoja na mshiriki mwingine wa jinsia moja, ni kulalana kwa watu wa jinsia moja. Na ingawa watu wengi huwafikiria watu wa jinsia moja wanaolalana kuwa wanaume tu, maneno hayo pia yanawahusu wanawake wanaofanya mazoea kama hayo.

Kuepuka Mwenendo Mbaya wa Ngono

Watu ambao huenda wakawa na tamaa ya kufanya ngono na watu wa jinsia yao wanahitaji kupigana sana na tamaa hizo. Wakati huo huo, twapaswa kuwa waangalifu tusiangukie mikononi mwa mtu ambaye huenda akashindwa na tamaa mbaya. Nyakati nyingine vitendo vya watu wa jinsia moja kulalana vimetokezwa na mambo ambayo yenyewe si kosa, kama vile kusugua mtu mgongo au kusuguliwa mgongo na mtu mwingine au kusafishwa mgongo wakati wa kuoga. Au nyakati nyingine watu wanamenyana mweleka kimchezo-mchezo na kuamshwa nyege. Kuna uhitaji wa kujihadhari. Ujue kwamba matendo hayo yanaweza kuongoza, na pindi fulani yameongoza kwenye vitendo vya watu wa jinsia moja kulalana, hata kati ya Wakristo.

Ni kwa sababu gani watu wengine wanahusika katika makosa ya ngono​—katika kulalana kwa watu wa jinsia moja, kulalana na wanyama, kuchungulia sehemu za siri za mwili wa mtu mwingine, na kadhalika? Imeonekana kwamba akili za wakosaji zilikuwa zinafikiria ngono kwa kadiri kubwa. Nyakati nyingine walikuwa wasomaji wenye hamu sana wa vitabu vya ngono chafu. Inaelekea wote walikuwa wenye tabia ya kupiga punyeto. Kwa kuwa habari hii ya kupiga punyeto imetokea kuhusiana na mazoea machafu ya ngono, na tuchunguze zoea hilo kwa msaada wa Neno la Mungu. Biblia inasema nini juu ya kupiga punyeto?

Maoni ya Biblia Juu ya Kupiga Punyeto

Kuna wale ambao wamesema kwamba Biblia inasimulia kupiga punyeto katika Mwanzo sura ya 38, na kwamba Onani aliuawa kwa ajili ya kosa hilo. Lakini hiyo si kweli. Biblia inasema kwamba wakati Onani “alipofanya ngono pamoja na mke wa nduguye alimwaga shahawa zake juu ya ardhi.” (Mwanzo 38:9, NW) Kwa hiyo inaelekea Onani alikatiza kufanya ngono pamoja na Tamari, akamwaga shahawa zake juu ya ardhi badala ya kumpa Tamari. Alifanya hivyo kwa sababu yeye hakutaka kulea watoto kwa jina la nduguye aliyekufa. Na ilikuwa kwa sababu ya kukosa kufanya “ndoa ya ndugu-mkwe” Onani aliuawa.

Vifungu vingine vya maneno viwili katika Maandiko ya Kiebrania vimezungumzwa katika vitabu kuhusu maoni ya Biblia juu ya mtu kupiga punyeto. Cha kwanza, Kumbukumbu la Torati 23:10 na 11, kinaeleza juu ya hali moja wakati Waisraeli walipokuwa katika kambi ya kijeshi. Kulingana na Biblia Today’s English Version, panasema: “Mtu akiwa mchafu kwa sababu aliota ndoto ya kumwaga shahawa wakati wa usiku, ataenda nje ya kambi na kukaa huko. Kuelekea jioni atajisafisha, na wakati wa jua kushuka aweza kurudi kambini.” Lakini jambo linalotajwa hapa si mtu kupiga punyeto. Kupiga punyeto kunasimuliwa hivi: “Kuamsha kimapenzi viungo vya uzazi ambako kwa kawaida kunatokeza msisimuko mkubwa wa nyege na kunafanywa kwa mtu kujisugua au mwili kugusishwa na mwingine.” (Webster’s New Collegiate Dictionary, 1981) Yehova Mungu aliwaumba watu wa kiume kwa njia ya kwamba, wasipofanya ngono, pindi kwa pindi bila kujua watamwaga shahawa wakati wa kulala. Mtoko huo mara nyingi unafuatana na ndoto ya mapenzi, kwa hiyo usemi huu “ndoto ya kumwaga shahawa.” Kwa kuwa kwa kawaida mtoko huo unatukia usiku, unaweza pia kuitwa “mtoko wa usiku.”

Kifungu kile kingine cha maneno kinachozungumza jambo hilo ni Mambo ya Walawi 15:16, 17, ambapo panasema: “Na mtu ye yote akitokwa na shahawa yake, ndipo ataoga mwili wake wote majini, naye atakuwa najisi hata jioni. Na kila nguo, na kila ngozi, ambayo ina shahawa, itafuliwa kwa maji, nayo itakuwa najisi hata jioni.” Kwa wazi kifungu hicho cha maneno hakihusu kupiga punyeto. Kwa wazi kinahusu “ndoto ya kumwaga shahawa” iliyotangulia kutajwa. Ingawa Biblia hutaja ‘kuwa najisi’kuhusiana na mtoko wa shahawa, huko ni kuwa najisi kulingana na desturi ya kidini wala si unajisi wa adili. Jambo hilo linakuwa wazi tunapoangalia katika mstari unaofuata kwamba mwanamume Mwisraeli na mkeye walikuwa najisi vivyo hivyo wakati wa kufanya ngono iliyokubaliwa na Mungu katika ndoa.

Basi, je, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanasema lo lote juu ya kupiga punyeto? Hapana, hayazungumzi habari hiyo. Wala hata ndoto za kumwaga shahawa hazitajwi. Lakini je, hiyo maana yake ni kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hayatoi mwelekezo wo wote wa kuwa na maoni mazuri kuelekea kupiga punyeto? Hapana, yanatoa. Angalia Wakolosai 3:5, ambapo panasema: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya [ya ngono], mawazo mabaya, na kutamani.” Na 1 Wathesalonike 4:4, 5 panasema: “Kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima; si katika hali ya tamaa mbaya [ya ngono], kama Mataifa wasiomjua Mungu.” Shauri hilo linahusu Wakristo waliofunga ndoa na pia wale ambao ni waseja, lakini kujizuia zaidi kwapasa kuonyeshwa na waseja kwa kuwa kutosheleza nyege kwa kufanya ngono ni kwa wale waliooana peke yao.

Je! unaona kwamba kupiga punyeto ni zoea ambalo linavunja amri ya kufisha ‘tamaa mbaya ya ngono’? Ni kweli Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya ngono, sawa na alivyotuumba tukiwa na tamaa ya chakula na vinywaji. Kwa hiyo Biblia haisemi kwamba kuwa na tamaa ya ngono ni kosa, sawa na isivyolaani kuwa na tamaa iliyo ya kawaida, inayofaa ya chakula na vinywaji. Lakini tunajua kwamba katika hali yetu ya kutokamilika, tamaa zaweza kupita kiasi. Mtu anaweza kuwa na tamaa mbaya ya chakula au vileo na kuwa mlafi au mlevi. Vivyo hivyo, ngono yaweza kuwa yenye sehemu kubwa au maana kubwa maishani mwa mtu, na kwa njia hiyo akawa kama watu wa mataifa ambao wana ‘tamaa mbaya ya ngono.’

Mtu anayepiga punyeto anakazia isivyofaa ngono. Yeye analisha na kuamsha tamaa yake ya ngono katika njia mbaya. Lakini si wanaume peke yao wanaofanya hivyo; kumekuwako ongezeko la kupiga punyeto kati ya wanawake. Lakini Mungu aliwapa wanadamu zawadi ya ngono waitumie ndani ya mpango wa ndoa. Lakini mtu anayepiga punyeto anaitumia ngono nje ya mpango wa ndoa kujipatia raha kibinafsi. Mtu wa namna hiyo anahitaji kufisha tamaa yake ya ngono ili ampendeze Mungu. Anahitaji kusitawisha kujiweza ambako ni kwa lazima ili kuacha kukazia ngono maishani mwake na kuruhusu viungo vyake vya uzazi wakati wa mikazo yo yote vijirekebishe kwa njia ya kawaida.

Yesu alifundisha hivi: “Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani [akiwa na nyege], amekwisha kuzini naye moyoni.” (Mathayo 5:28) Mara nyingi mwenye kupiga punyeto ana mawazo ya aina hiyo. Mtu wa namna hiyo bila shaka haishi kulingana na fundisho la Kristo. Hakuna shaka kwamba wanaochochea tamaa yao ya ngono kwa kupiga punyeto wanavunja maagizo ya Mungu ya KUFISHA tamaa yao ya ngono.

Lakini mtu anawezaje kufisha tamaa yake ya ngono na kuepuka kupiga punyeto? Ni kweli kwamba kwa watu ambao wamezoea kupiga punyeto, yaweza kuwa vita kweli kweli kuacha. Lakini mtu hapaswi kukubali kushindwa na vita hiyo! Kwa msaada wa Yehova mtu anaweza kufaulu. Kwanza anapaswa kusitawisha chuki ya zoea hilo. (Zaburi 97:10) Kisha ni jambo la maana kwamba aazimie kwa uthabiti akilini na moyoni mwake kuacha kupiga punyeto. Anapaswa kufanya hiyo iwe habari ya kutajwa katika sala wakati wote; kisha anahitaji kujitahidi kufanya yale anayoomba. Basi hawezi kuchochea moto wa nyege kwa kusoma au kutazama mambo yanayoongeza tamaa yake ya ngono. Wala hawezi kuwa akizungumza juu ya mambo yanayochochea maelekeo yake ya kupiga punyeto. Badala yake, yeye anapaswa kujishughulisha na mambo ya kitheokrasi, kuhudhuria mikutano, utumishi wa shambani, kufanya ziara za kurudia, kuongoza mafunzo ya Biblia, kuwasaidia wengine kiroho, naye atapokea nguvu za kuweza tamaa yake ya ngono. Tatizo hilo likiendelea, hapaswi kusita kutafuta msaada wa mzee katika kundi lao. Dada mwenye tatizo hilo aweza kutafuta msaada na tegemezo la dada mzee kundini.

Hakuna shaka​—kushika ukamilifu kwa Yehova kunahitaji vita ngumu. Lakini kunastahili! Tukipigana sasa dhidi ya mwili wetu wenye maelekeo ya dhambi, basi Yehova atatupa sisi ushindi kamili katika Utaratibu Mpya wake ulio safi na wenye uadilifu. Ebu fikiria hilo! Kisha tutaona kusudi la Yehova tukufu likitimizwa​—dunia yenye kujawa na watu wenye kuishi katika Paradiso​—wote wakiwapo kwa sababu ya zawadi nzuri ajabu ya ngono ambayo Mungu alituumba tukiwa nayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki