Uaminifu Katika Wakati wa Mwisho
“Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.”—1Pet. 4:3.
1. Kwa sababu gani ubaya wa wanadamu unaelekea kuzidi kuwa mbaya wakati huu?
TANGU Vita ya Kwanza ya Ulimwengu tumekuwa katika kipindi cha ajabu sana katika historia ya mwanadamu, kipindi kilichotiwa alama na jeuri isiyolinganika, umwagaji mwingi wa damu na kuenea sana kwa uharibifu wa tabia. Juu ya kipindi kama hiki maelfu ya miaka iliyopita, maandishi ya historia ya Biblia yasema: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.” (Mwa. 6:5) “Wao hawakufahamu” mapenzi ya Mungu kwa wanadamu. Hiyo ilieleza hali ya mambo ilivyokuwa katika siku zilizotangulia gharika kuu ya wakati wa Nuhu. Yesu Kristo alisema hali kama izo hizo zingekuwapo katika siku za mwisho za taratibu iliyopo ya utawala wa kibinadamu. (Mt. 24:37-39, NW) Tangu mwaka wa 1914 C.E. tumekuwa tukiishi katika hizo “siku za mwisho.”
2, 3. Wakristo wanaona uvutano gani mbaya, na kwa sababu gani inawapasa wauzuie?
2 Kwa kuwa wanadamu wanashuka kidogo kidogo kwenye upotovu wa adili zaidi na zaidi, mkazo juu ya Wakristo wa kweli wa kuyaona matendo ya ufisadi kama yanayokubalika unaongezeka. Kuwaza kwa inayoitwa “adili mpya” kunaenea kati ya watu wa kilimwengu wanaowazunguka nako kumejaa katika vitabu na kujifurahisha kunakotayarishwa na watu hao. Hii inatoa uvutano mbaya juu ya Wakristo wote. Inahitaji uzuizi imara kwa upande wao. Huenda wengine hata walishiriki katika maisha ya ufisadi mbele ya kuwa Wakristo wa kweli. Lakini kwa kuwa sasa wamevaa utu mpya uliofuatishwa kulingana na kanuni za juu za adili za Neno la Mungu, wakati wa kuishi kama vile mataifa umepita. Kuurudia kungekuwa kama vile mbwa anayeyarudia matapiko yake.—2 Pet. 2:22.
3 Lakini, kuwa kwao Wakristo wa kweli hakumaanishi wanaacha kupatwa na tamaa za mwili usiokamilika. Wanapatwa nazo, nazo tamaa hizo ni sehemu iliyo dhaifu kwao. Wasipojikinga sikuzote kwa adili kwa kujiweza wanaweza kudhuriwa vyepesi na shambulio katika mahali hapa palipo dhaifu. Shetani, mungu wa huu ulimwengu mpotovu wa wanadamu, anajitahidi kupapata mahali hapa palipo dhaifu kwa njia ya uvutano wenye kupotosha wa ulimwengu wake. Leo anatumia maarifa yale yale aliyowafanya Wamoabu na Wamidiani wayatumie walipojaribu kuwapotosha Waisraeli katika karne ya kumi na tano mbele ya Wakati wetu wa Kawaida na kwa njia hiyo kumfanya Yehova Mungu adui yao. Kwa hiyo leo Shetani anajaribu kuwashawishi Wakristo kwa tamaa za mwili wazivunje sheria za Mungu na kwa njia hiyo kuwaletea hukumu mbaya ya Mungu.—1 Pet. 5:8.
4. Nini kiwezacho kutokea wakati Mkristo anapoiruhusu akili yake ikae juu ya tamaa mbaya?
4 Wakati Mkristo anapovifurahia vitabu vyenye upotovu wa adili na namna nyingine za kujifurahisha zinazotayarishwa na taratibu ya mambo ya Ibilisi, je! yeye hajifanyi kupatikana na kuwa asiyelindwa? Je! kuwaza tamaa mbaya hakutaelekeza kwenye kushindwa nazo nyumaye na hivyo kufanya dhambi machoni pa Mungu? (Yak. 1:14, 15) Kuendelea katika mwendo huo kutaleta uharibifu ulio hakika kutoka kwa Mungu, kama kulivyowafanyia Waisraeli 24,000 waliouawa katika nyanda za Moabu. Shetani atakuwa amejipatia ushindi juu yao kwa kuwafanya wawe wasioaminika kwa Mungu wao na Mfalme.—Hes. 25:1-9.
UAMINIFU KATIKA YOTE
5, 6. (a) Uaminifu kwa Mungu unatia nini ndani? (b) Yesu alisema inampasa Mkristo atafute nini zaidi ya Ufalme? Namna gani?
5 Huenda Mkristo afikiri kwamba yeye ni mwaminifu kwa Yehova Mungu kwa kuwa anazihubiri habari njema za Ufalme kwa bidii, lakini uaminifu unatia ndani mengi zaidi ya hilo. Askari wa Kiisraeli waliopigana kishujaa juu ya Waamori walifikiri walikuwa waaminifu kwa Mungu vile vile, lakini wengi walishindwa kuona kwamba wapaswa uaminifu uonyeshwe na mwenendo wote wa mtu vile vile. Mkristo akishindwa na tamaa mbaya kuhubiri kwake juu ya ufalme wa Mungu ni kwa bure. Kwa kweli anajionyesha kuwa asiyeaminika kwa ufalme wa Mungu akizivunja sheria zake za adili. Mwenendo wake usio wa Kikristo unaleta shutumu juu ya jina la Mungu wake na Mfalme.—2 Pet. 2:2.
6 Lazima Mkristo auonyeshe uaminifu wake waziwazi kwa Mungu na Ufalme kwa njia yake yote ya maisha, hata katika ambayo huenda yaonwe kama mambo madogo. Lazima iwe tofauti sana na njia ya maisha iliyopotoka ya ulimwengu, hata ingawa hili laweza kuwafanya wamjuao na jamaa zake wazungumze juu yake kwa njia ya matusi. (1 Pet. 4:3, 4) Angalia namna Yesu alivyoonyesha waziwazi kinachopaswa kuambatana na kupendezwa kwa mtu na ufalme wa Mungu. “Bali utafuteni kwanza ufalme wake,” yeye alisema. Lakini akaongezea “na haki yake.” (Mt. 6:33) Hivyo, ili Mkristo autegemeze ufalme wa Mungu kwa uaminifu, lazima aishi kulingana na haki ya Mungu inayosemwa katika sheria zilizoandikwa kwa njia ya kimungu na maonyo ya Biblia. Kwa njia yake ya maisha lazima auonyeshe Ukristo wa kweli wazi.
7. (a) Kwa kuwa Wakristo wa kweli wanao ujamaa wa kipekee na Yehova, zaidi inawapasa wapende nini? Kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani Mkristo ana hatia ya kutokuaminika anapoyaacha yaliyo haki?
7 Kama vile Waisraeli katika siku za Musa, Wakristo wa kweli wanao ujamaa wa kipekee na Yehova Mungu. Hii inahitaji wayapende yaliyo safi na haki, kama vile Mungu afanyavyo. Adui yake mkuu, Shetani Ibilisi, anayapenda yaliyo machafu na yasiyo haki, na kwa hiyo ulimwengu huu wa wanadamu wasiotii unatokeza matunda machafu yasiyo ya haki ya mungu wake mwovu na mtawala. (Yohana 8:44; 2 Kor. 4:4) Kuacha kwa Mkristo yale yaliyo haki kwa kushindwa na tamaa mbaya kungemaanisha kwamba yeye kwa kutokuaminika anamfuata mungu mwingine, mungu mwovu wa ulimwengu huu. Yeye anayatokeza matunda mabaya ya huyo. Angekuwa kama Waisraeli wasio waaminifu walioshawishiwa na tamaa mbaya walipokuwa katika karamu ya Wamoabu na Wamidiani nao wakajitia katika ibada ya Baali. Tunapoitafuta haki ya Yehova, tunajitahidi kwa ajili ya usafi mwingi zaidi wa kuwaza na wa mwenendo. Tunalitii onyo la Maandiko: “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Rum. 12:2.
8. Je! kuna sehemu yo yote ya maisha zetu inayoweza kuitwa ya faragha machoni pa Yehova? Eleza kwa mifano.
8 Jina la Yehova li juu ya Wakristo wa kweli wanaoushuhudia ufalme wake. Jina hilo linayasimamia yaliyo manyofu na safi katika ulimwengu wote. Fimbo ya ufalme wake, inayopungwa na Mwanawe, “ni fimbo ya adili.” (Ebr. 1:8) Je! haiwapasi raia walio waaminifu kwa ufalme huo na Mfalme wake aliye mkuu zaidi, Yehova Mungu, waionyeshe haki hiyo katika kila upande wa maisha zao? Je! uaminifu hauhitaji hili? Wao wanalichukua jina la Yehova wakati wote, na ikiwa mtu anadhani anaweza kuzoea jambo fulani baya au hata lisilo la uaminifu kwa faragha, yeye analishutumu jina hilo. Kwa kweli hakuna sehemu ya maisha zetu inayoweza kuitwa “ya faragha” kwa kadiri ambavyo Yehova anapaswa. Tukifanya yaliyo mabaya kwa siri, ni siri kwa wanadamu wengine peke yao. Yehova ameyaona. Je! yeye hakuyaona yale ambayo Waisraeli wasioaminika walifanya katika hema za Wamoabu na Wamidiani? Je! yeye hakuyaona yale ambayo wazee wa Israeli wasioaminika walifanya karne nyingi nyumaye katika vyumba vya faragha katika ua wa ndani wa hekalu la Yehova Yerusalemu? Je! yeye hakuwaona wakijitia katika ibada ya sanamu humo? Kutokuaminika huko juu ya Mungu hakufichiki. Walikuwa wakijidanganya wenyewe waliposema: “[Yehova] hatuoni; [Yehova] ameiacha nchi hii.” (Eze. 8:9-12) Hakuna Mkristo wa kweli ambaye angependa kufanya kosa lile lile la kutumia kuwaza huku kwa uongo kama vile Wakristo wa uongo leo wanaodai Mungu amekufa walivyofanya.
9, 10. (a) Eleza namna ambavyo tamaa za kimwili zinavyoweza kumtia Mkristo taabani. (b) Uaminifu watiwa ndani hapa namna gani?
9 Mkristo anaanza kuingia taabani anapoacha kuwa na ulinzi wenye nguvu. Mahali pa kujiepusha na hali zinazochochea tamaa mbaya za kimwili, huenda akajaribu kutembea karibu zaidi na ukingo kama awezavyo. Ijapokuwa dhamiri yake yaweza kumwambia kwamba tamaa hiyo haifai, huenda akaiwaza, na kadiri anavyoendelea kucheza nayo ndivyo tamaa hiyo inavyozidi kuwa yenye nguvu. Kama vile Waisraeli wasioaminika, yeye haizuii tamaa mbaya ya “mambo yenye kudhuru.” (1 Kor. 10:6, NW) Hali kama hiyo yaweza kusitawi wakati watu wawili wasiooana wa kiume na kike wanapoanza kuchocheana nyege kwa faragha kwa kuweka mikono yao katika sehemu za siri za mtu na mwenzake. Hiyo ni namna ya ufisadi nayo haimfai Mkristo, ambaye njia yake ya maisha yapaswa iionyeshe haki ya Yehova.
10 Je! twaweza kuongozwa katika mambo hayo na yanayokubalika katika ulimwengu kwa jumla? Sivyo, kwa maana ulimwengu hautupi kanuni zifaazo. Unaonyesha, si haki ya Yehova Mungu, bali uovu wa “mungu wa dunia hii,” adui ya Yehova. (2 Kor. 4:4) Mahali pa kujiachilia tutiwe katika usingizi wa kutokufikiri, au hata kujidanganya wenyewe, yatupasa kujua kwa uaminifu kwamba nyege zinapochochewa hii yaweza kuongoza kwenye tamaa yenye nguvu mno ya kutosheleza nyege hizo kwa ngono. Huu ni uhakika wa maisha. Kutosheleza huko ni kwa kawaida nako kwafaa kwa watu waliomo katika mpango wa ndoa. Lakini kwa watu wasiooana kuzitosheleza nyege hizo katika mwungano huo ni kuvunja kwa uzito sheria ya kimungu; kwa kweli, ni kutokuaminika juu ya Mungu kwa upande wa Mkristo. Basi, je! haupaswi uaminifu utulinde na kujihatirisha na uvunjaji huo, ukitufanya tuepuke matendo ambayo kwa hatari yanachochea nyege?
11. (a) Ni sababu gani watu wengine wanayoitoa kutetea “kukumbatiana” kwenye tamaa, na kwa nini sababu hii ni mbaya? (b) Ingawa mwenendo mchafu hautii ndani ngono, hata hivyo wawezaje kufikia hatua ya kuwa “uasherati” (por·neiʹa)?
11 Katika mazoea ya kisasa ya “kufanyiana miadi,” vijana wengi wanajitia katika “kukumbatiana” kunakochochea nyege nyingi. Lakini huenda wengine wakabisha kwamba hili si kosa maadam hakuna kuungana kwenyewe kwa viungo vya uzazi, kwa kuwa, kama wanavyoyafahamu mambo, hiki ndicho Biblia inachokataza waziwazi kwa watu wasiooana. Kuwaza huko ni kwenye makosa na kwa hatari vile vile. Wakristo wanasihiwa wavitoe viungo vyao si tena “vitumiwe na uchafu na uasi” bali “vitumiwe na haki mpate kutakaswa.” (Rum. 6:19) Hata “kukumbatiana” kwao kwenye nyege kusipofikia hatua ya “uasherati” (Kigiriki, por·neiʹa) katika maana ya Biblia ya neno hili, hata hivyo kwaweza kuanzisha “uchafu” (Kigiriki, a·ka·thar·siʹa), namna ya mwenendo wa adabu mbaya, ulio mchafu. “Uchafu” umepangwa kufuata “uasherati” katika orodha ya mtume ya matendo ya mwili usiokamilika, naye anaonya kwamba wale ambao kwa kutokutubu “wanazoea mambo hayo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Gal. 5:19, 21, NW) Si hivyo tu, lakini matendo hayo machafu huenda kidogo kidogo yakawa mazito katika namna au yakaendelea kufikia hatua ambapo kwa kufaa yanapangwa kama “uasherati” (por·neiʹa). Hii ni kwa maana neno hili kulingana na Maandiko linamaanisha namna zote za ufisadi mzito au mwenendo mchafu kama ule uwezao kupatikana katika mahali pa umalaya, si kwa ngono ya watu wasiooana peke yake.
12. (a) Je! kuchumbiana kunawapa watu wawili haki ya kujitia katika kufanyiana upendo wenye tamaa? (b) Imewapasa watu wasiooa au kuolewa waepuke hali gani, na kwa sababu gani?
12 Ni kawaida kwa watu wawili waliopatana kuoana kuonyeshana upendano. Lakini hii haimaanishi wanaweza kwa haki kujitia katika ngono iliyowekwa kwa ajili ya watu waliooana. Wakiwa hawako huru kuwa na ngono yenyewe mpaka wameoana, haiwapasi wajitie katika namna ya ‘mchezo wa upendo’ wa ndani ambao, katika ndoa, unaitangulia ngono. Kufanya hivyo kungekuwa uchafu kwa upande wao, wakionyesha kutokuuheshimu mpango wa Mungu, ukosefu wa uaminifu kwa kanuni zake safi za utakatifu. Kwa hiyo, katika wonyesho wo wote wa upendano, uaminifu wao wapaswa uwavute kutumia uangalifu na kujizuia kupaswao. Haiwapasi kukosea si desturi ya mahali tu waziwazi na kufanya hatari ya kukwaza watu, lakini vile vile wanapokuwa peke yao haiwapasi wajitie katika matendo ambayo yangewaletea aibu ikiwa mtu mwingine angetokea mahali pale kwa ghafula. Je! si kweli kwamba kuwako kwa wengine mara nyingi ni ulinzi mzuri kwetu juu ya udhaifu wetu na tamaa za kimwili? Giza na faragha, kwa upande mwingine, vinapunguza ulinzi wetu navyo vyaweza kuzidhoofisha nia zetu. (Linganisha Mithali 9:16-18; Yohana 3:20, 21; Waefeso 5:7-13.) Hata wajapokuwa wamechumbiana, je! Wakristo wasingekuwa wenye hekima kuepuka kuihatirisha heshima juu yao wenyewe na heshima yao kwa mmoja na mwenzake kwa kuepuka hali zinazowatia kwenye mwenendo mchafu? Wanaweza kuziepuka hizi kwa kutokujitenga na wengine kwa kadiri ambavyo hawajioni kujizuia vyema kwa kujua kwamba mtu fulani angeweza kuingia chumbani kwa vyepesi au mahali hapo walipo. Bila shaka wale ambao hawajachumbiana wanayo sababu ya kujizuia hata zaidi, wakipendelea kufurahia ushirika wa mmoja na mwenzake wakiwa nje waziwazi pamoja na watu wengine, siyo wakiwa faraghani peke yao.
TENDO LA KUNDI
13, 14. Ni tendo gani la kundi la Kikristo linalolingana na lile lililochukuliwa na wazee waaminifu wa Israeli kwa habari ya wale waliokuwa wasioaminika kwa Mungu, na kwa sababu gani tendo hili ni la lazima kwa wale wanaozoea mwenendo wa ufisadi?
13 Waisraeli waliposhindwa na tamaa za kimwili penye karamu ya Wamoabu na Wamidiani na kujitia katika ibada ya utukuzo wa nguvu za uzazi, tendo lilichukuliwa juu yao na Mungu na wajumbe wa kundi la Israeli. Yawezekana wajumbe hao wenye kuwakilisha wenyewe waliwaua Waisraeli wasio waaminifu kama 1,000. (Hes. 25:3-5) Kifani cha hili chaweza kupatikana katika kundi la Kikristo leo. Ingawa halikupewa mamlaka ya kuwaua washiriki wasio waaminifu na Mungu ambao wanazoea dhambi nzito, mamlaka imetolewa kwalo kuwachukulia tendo kwa kuwatenga na ushirika wa kundi ikiwa hawatubu. (1 Kor. 5:11-13) Hii ni lazima ili kuliweka kundi kuwa safi. Kama lingeshindwa kufanya hivyo, lingewezaje kwa haki kujidai kuwa mali ya Yehova na Yesu Kristo, ambao ni wenye haki? Lina wajibu wa kuzitegemeza sheria za Mungu za haki.
14 Kwa kuwa ufisadi wote ulio mzito unaomaanishwa na neno por·neiʹa ni mwenendo mchafu uwezao kumzuia mtu asiurithi ufalme wa Mungu, kundi la Kikristo kwa haki linawatenga na ushirika watu wauzoeao na wasioonyesha toba lo lote la unyofu wa moyo. Ndivyo ilivyo na kwa wale wanaoendelea kuwamo katika namna yo yote ya “uchafu.” Lakini, uchafu ni neno lenye maana nyingi lililo na uzito wa kadiri mbalimbali—hata kama vile mtu kwa kimwili awezavyo kuwa na uchafu kidogo au awezavyo kuwa mchafu kabisa, ndivyo ilivyo na kwa uchafu wa adili. Kwa hiyo, katika kuamua kadiri ya uchafu, kichocheo, hali na mambo yaliyoelekeza kwenye uchafu huo lazima yote yafikiriwe ili kuamua uzito wa mwenendo. Kwa hiyo, kupendezwa kwa kundi la Kikristo kuuhifadhi usafi wake si kusiko na busara bali kunalingana na mambo ya hakika, wala si kwenye haraka mno kuchukua tendo la kutenga na ushirika wala si kwenye kukawia ambapo mazoea mazito, yasiyofanyiwa toba yanalihitaji. Hii ni kupatana na yaliyoandikwa katika 2 Timotheo 2:19, ambayo, kati ya mambo mengine, yanasema: “Kila alitajaye jina la [Yehova] na auache uovu.” Tendo la hukumu linalochukuliwa na wazee wa kundi linalilinda kundi na sifa yake lisije likapakwa madoa ama kuchafuliwa. Vile vile linatoa onyo zuri kwa wote katika kundi juu ya linaloweza kumpata mtu anayewaza tamaa mbaya kwa adili.
15. Mtu awezaje kupata msamaha wa matendo mabaya?
15 Bila shaka, ikiwa mtu anaonyesha wazi majuto ya moyoni juu ya dhambi aliyotenda na kutafuta msamaha, aweza kusamehewa. Mungu anaonyesha wazi nia ya kumsamehe mtu huyo, nalo kundi la Kikristo linatenda kupatana na msamaha wa Mungu. (1 Yohana 1:9) Huenda mtu huyo akakaripiwa waziwazi kwa mwenendo wake mbaya, au aweza kukaripiwa kwa faragha juu yake na halmashauri ya hukumu. (1 Tim. 5:20) Hata mtu ambaye ilikuwa lazima atengwe na ushirika aweza kupata msamaha ikiwa nyumaye anahakikisha kwamba ametubu kweli kweli na kugeuka kutoka mwenendo wake mbaya. Kwa hiyo hali hii si isiyo na tumaini kwa lazima kwa mtu anayetenda dhambi.—Eze. 33:11.
EPUKA MATENDO YASIYO YA UAMINIFU
16, 17. Imetupasa kushika ulinzi wenye nguvu juu ya nini? Eleza namna ambavyo twaweza kufanya hivyo.
16 Ni muhimu kwetu kujua kwamba sisi wanadamu tunazo tamaa za kimwili zinazotufanya tuwe wepesi kudhuriwa. Kwa hiyo, yatupasa tushike ulinzi wenye nguvu na kujua hali zinazoweza kuuhatirisha ulinzi wetu. Akijua kwamba mwili ni dhaifu, mtume Paulo alisema: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” (1 Kor. 9:27) Hii yamaanisha inatupasa tujitahidi sikuzote kuzizuia nyege zetu. Hatuwezi kuikomesha jitihada ya kutumia kujiweza. Tukisoma vitabu vyenye kuchochea nyege vinavyoonyesha kuwaza kwenye upotovu kwa watu wa kilimwengu, je! tutasaidiwa katika kushika ulinzi wenye nguvu au havitatudhoofisha? Bila shaka hatutiwi nguvu tukiziacha akili zetu zikae juu ya tamaa mbaya, sivyo? Kuliko hivyo, tutajifanya wepesi kudhuriwa hata zaidi. Ingekuwa bora kulifuata shauri katika Wafilipi 4:8, linalosema: “Hatimaye, ndugu zangu, mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo.” Halisemi kuyafikiri mambo yaliyo maovu wala mambo yanayochochea tamaa chafu. Tunapoyafikiri mambo yaliyo haki, je! tutaelekea kujitia katika matendo yaliyo maovu?
17 Yatupasa tujue kwamba Ibilisi anajaribu kutushawishi kufanya yaliyo mabaya machoni pa Mungu na, tukimruhusu, atatuelekeza moja kwa moja kwenye hatua ya kuingia kwa kasi katika matendo ya ufisadi. Tukijiruhusu tuvutwe na kujaribu kukadiri tunayoyafanya, je! hatutafuti taabu itakayokuja bila shaka? Je! isingekuwa bora kukishinda kishawishi mwanzoni? Je! Waisraeli waliojitia katika ibada ya Baali wasingekuwa bora zaidi kama wangevipinga vishawishi vile vile vya kwanza vilivyowekwa mbele yao na Wamoabu na Wamidiani?
18. (a) Biblia inashikamanisha maana gani na ‘kumgusa mwanamke,’ na kwa sababu gani? (b) Uhakika huu umepaswa kuwa na matokeo gani juu ya maoni ya watu wasiooa ama kuolewa?
18 Kifikirie kisa cha Hawa. Alijua kwamba haikumpasa hata kuligusa tunda lililokatazwa katika bustani ya Edeni, kwa maana kugusa ndiyo iliyokuwa hatua ya kwanza kuelekea kulila. (Mwa. 3:3) Kutokuruhusiwa kulila tunda katika mti huu mmoja hakukumwekea ugumu wo wote, kwa vile yalikuwako matunda mengine mengi aliyoruhusiwa kuyala. Kuligusa kwake kulionyesha wazi tamaa mbaya kwa ajili ya ambacho Mungu alikuwa amekataza. Tukilikumbuka hili, huenda tukalifikiria kwa uzito onyo lililomo katika 1 Wakorintho 7:1: “Ni heri mwanamume asimguse mwanamke.” Katika Maandiko ya Kiebrania, ‘kugusa’ nyakati nyingine kunatumiwa kuonyesha ngono. (Linganisha Mithali 6:29; Mwanzo 20:6, 7.) Hii yawezekana kwa maana mstari wa matukio yanayoelekeza kwenye ngono unaanza na kumgusa mwanamke au mwanamume kwa njia ya tamaa. Yesu alionya juu ya hata ‘kumtazama mwanamke kwa kumtamani,’ akisema kwamba mtu afanyaye hivyo “amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mt. 5:28) Basi, yaonekana kwamba ‘kumgusa mwanamke’ kwaweza kutia ndani na kugusana ko kote kwa kimwili na mwanamke au mwanamume kwa njia inayotokana na nyege hizo zisizofaa. Ikiwa mtu hawezi kuzizuia nyege zake naye anaelekea ‘kuwagusa’ wanawake au wanaume kwa tamaa au kwa njia ya uchafu, basi, kama vile mtume Paulo anavyoendelea kusema, ingekuwa afadhali aoe au aolewe. (1 Kor. 7:2, 9) Kwa sasa, mwendo uwafaao Wakristo ambao wangali hawajaoa ama kuolewa ni kuepuka ‘kutazama’ au ‘kugusa’ kunakoweza kuelekeza kwenye kosa zito kwa wepesi sana. Ndipo watakapokuwa na furaha yenye kuridhisha ya dhamiri safi mbele za Mungu na mwanadamu.
19. Kwa sababu gani imetupasa tujitahidi kuionyesha haki ya Yehova maishani mwetu?
19 Tumejifunza kumpenda Yehova Mungu kwa sababu ya haki yake, sheria njema na fadhili za upendo au upendo mwaminifu. Twalifurahia tumaini la kuja kwa dunia yote chini ya utawala wa ufalme wake bila ya kukatizwa na serikali mbovu. Hii twajua itamaanisha utawala wa haki kwa wanadamu, pamoja na amani ya milele na usalama. Je! haimpasi kila mtu mwenye furaha kuwa karibu na Mtawala huyu wa haki wa ulimwengu wote kama sehemu ya tengenezo lake la kidunia ajitahidi kwa nguvu zake zote kuionyesha haki ya Mungu maishani mwake kwa kuishi kulingana na sheria Zake? Bila shaka huku kungekuwa ni kuonyesha uaminifu kwake, sivyo?
20. Ni kwa njia gani kuonyesha uaminifu ni sehemu ya kuuiga mfano wa Yesu Kristo?
20 Ukristo wa mtu unaonyeshwa, si kwa wonyesho wa waziwazi tu wa uhakika wa kwamba yeye amejiweka wakf kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa katika maji, lakini vile vile kwa kuonyesha wazi utu kama wa Kristo. Hiyo inatia ndani utu mpya “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki ya kweli na uaminifu.” (Efe. 4:24, NW) Nyakati zote Yesu Kristo alijiongoza mwenyewe kupatana na sheria za haki za Mungu. Sheria hizo zilikuwamo moyoni mwake, nazo zilizivuta tamaa za moyo wake zipatane na mapenzi ya Mungu. (Yohana 5:30) Sheria izi hizi za haki zapaswa ziwemo mioyoni mwetu na kuzivuta tamaa zake.
FAIDA ZA KUWA WAAMINIFU
21, 22. Ni nini nyingine za faida zinazotokana na kuwa mwaminifu kwa Yehova, nazo hizi zalinganaje na raha za kimwili?
21 Raha ambayo huenda mtu awe nayo sasa kutokana na kufuata tamaa mbaya za kimwili ni ya muda tu. Lakini faida zinazotokana na kuwa mwaminifu kwa Yehova zaweza kuwa za milele. Kwa sababu gani uziache faida hizo za milele kwa ajili ya kukimbilia vitambo vidogo vya raha? Musa alichagua “kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo,” kwa maana faida zinazotokana na kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova ni bora zaidi. (Ebr. 11:25) Faida yenye kutokeza sana tuwezayo kuifikiria leo ni kuwa sehemu ya “mkutano mkubwa” wa waabudu waaminifu wa Yehova watakaohifadhiwa kupita “dhiki kubwa” inayokuja itakayoleta mwisho wenye msiba kwa taratibu iliyopo ya mambo.—Dan. 2:44; Ufu. 7:9, 14.
22 Faida nyingine kubwa ni kuishi milele katika wakati mpya ambao ufalme wa Mungu utauleta. Je! kuishi katika amani na usalama chini ya watawala wenye haki si kwenye faida kubwa zaidi kwake kuliko vitambo vichache vyenye kupita kasi vya raha isiyofaa? Je! uzima wenyewe si bora zaidi kuliko raha hizo? Kutokuaminika juu ya Yehova kwaweza kumaanisha kifo cha milele, lakini uaminifu kwake waweza kumaanisha tofauti yake yenyewe, uzima wa milele. “Na hii ndiyo ahadi aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele.” (1 Yohana 2:25) Faida hizi na nyingine nyingi za ajabu zawajia walio waaminifu.
23. Kwa hiyo ni nini ulio mwendo wa hekima kufuata leo?
23 Kwa kuwa tumekwisha kufika pale pale mlangoni pa wakati mpya, ungekuwa msiba kwa Mkristo kushindwa kwa sababu ya kuwaza tamaa mbaya za kimwili na kuwa asiyeaminika kwa Mungu wa kweli. Ingekuwa hekima zaidi kama nini kushika dhamiri safi kwa kufuata njia nyofu ya uaminifu kwa Mungu katika huu wakati wa mwisho!—Zab. 37:28, 29.
—Kutoka The Watchtower, Oct. 1, 1973.
[Picha katika ukurasa wa 156]
Wakristo wasiooana wanaojitayarisha kwa ajili ya ndoa wanaweza kujilinda juu ya mwenendo mchafu kwa kuepuka kutumia wakati pamoja wakiwa faraghani peke yao