Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 5/15 kur. 237-239
  • Unakwenda Arusini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unakwenda Arusini?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SABABU ZA KWENDA
  • KWA WAUME NA WAKE
  • WAZAZI NA WATOTO
  • KUFAIDIKA KUTOKANA NA KARAMU
  • Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Arusi za Kikristo Zapaswa Kuonyesha Kiasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Ni Arusi ya Namna Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 5/15 kur. 237-239

Unakwenda Arusini?

WATU wengine hawahudhurii arusi kamwe, hata arusi ya rafiki mkubwa, wakidai kwamba wana shughuli mno. Lakini ni vema kukumbuka kwamba Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alipokuwa duniani hakuwa mwenye shughuli mno asiweze kuihudhuria karamu ya ndoa katika Kana. Kwa kweli, ishara ya kwanza aliyoifanya kama uhakikisho wa Umasihi wake ilikuwa katika arusi hii. Divai ilipokwisha, alifanyiza zaidi kwa mwujiza, divai iliyo bora na kwa wingi. Pale, matokeo ya mwujiza huu yalikuwa kwamba “wanafunzi wake wakamwamini.”​—Yohana 2:1-11.

Arusi ya kwanza ilikuwa ile ya Adamu na Hawa nayo ilifanywa na Yehova Mungu, Muumba. Mungu kwanza alimfanya Adamu auone ubora wa kuwa na mwenzi, kwa maana twasoma kwamba alipokwisha kuwapa majina wanyama wote Adamu aliona kwamba yeye mwenyewe ‘hakuwa na msaidizi wa kufanana naye.’ Kisha Mungu akamwumba Hawa na “akamleta kwa Adamu.” Si ajabu kwamba, alipofahamishwa kwake, Adamu alisema: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.”​—Mwa. 2:18-23.

Kati ya watumishi wa Mungu nyakati za kale hakuna maandishi ya kuonyesha kulikuwako sherehe ya kawaida ya kidini ikishirikishwa na arusi. Wala hakukuwako kitu cho chote kama leseni, ijapokuwa hatua za wazi zilichukuliwa zilizokifanya kifungo cha ndoa kuwa cha lazima kulingana na sheria. Lakini, jambo moja ni hakika, kwamba, hata kama ilivyo leo, arusi ilikuwa wakati wa furaha. Kinachotilia mkazo furaha inayoshirikishwa na karamu za ndoa ni mtajo wa ndoa ya Mwana-Kondoo, hivyo kuutumia mpango huu unaofahamiwa sana na wanadamu kuuonyesha ujamaa unaokuja kuwamo kati ya Yesu Kristo na wafuasi wake mbinguni. Juu ya ndoa hii, twasoma: “Msifuni Yah, enyi watu . . . Na tufurahi na kufanya shangwe, na tumpe yeye utukufu, kwa maana ndoa ya Mwana-Kondoo imefika naye mkewe amejipamba.”​—Ufu. 19:6, 7, NW.

Kwa kawaida arusi zinakuwa za furaha sana nazo zina mambo mengi ya kupendeza, hasa kwa wanawake, ambao kwa kawaida wanaelekea kuwa wenye mahaba zaidi na wenye kupendezwa zaidi na arusi kuliko wanaume. Kwa kawaida bibi-arusi anapambwa vizuri. Na mara nyingi kuna maua na muziki wa kuiongezea furaha ya wakati huo.

Imeonekana kwamba mabibi-arusi wanafanya mambo mengi katika arusi yao; wanataka kuifanya iwe tamasha nzuri kama wawezavyo. Nao wanafanya hivi kwa hekima ya mwanamke iliyo ya ajabu. Yaelekea sana kuwa mabwana-arusi wengi wanapendelea iwe vingine, lakini kwa kuikamilisha mipango yote huenda hata hawa wamekwisha kazia mioyoni mwao na akilini umuhimu wa hatua wanayoichukua. Kama ilivyoonwa na wataalamu wa moyo wa kilimwengu, sherehe yenye kutazamisha inavuta fikira sana kwenye mwanamume au bwana-arusi hata anafahamishwa zaidi kwamba tangu sasa yeye ni mwanamume aliyeoa. Halafu, tena, mabibi-arusi ni wenye hekima katika kufanya matayarisho mengi kwa arusi yao, kwa maana kuoa au kuolewa ni mojawapo ya hatua zilizo nzito sana anazoweza kuzichukua mtu nayo inachukuliwa kwa taraja la kudumu maisha yote.

SABABU ZA KWENDA

Kuna sababu nyingi mbalimbali za watu kwenda arusini. Mtu mwenye mahaba sana kwa kawaida ataona udhuru mwingi wa kwenda arusini. Sababu nzuri sana ya kwenda, bila shaka ni kwa sababu rafiki mwema au jamaa wa karibu anaoa au kuolewa. Watu wawili wanaooana wanauona kama wonyesho wa upendo au heshima kwa wengine kuhudhuria arusi yao. Watu wengine wanakwenda kwa sababu ni wa jamaa ya bibi-arusi au ya bwana-arusi na kwa hiyo wanajisikia wana wajibu wa kuonekana huko. Wengine wanakwenda kwa sababu ya mambo ya kisiasa yanayoelekea kukupendekeza kuwapo kwao. Upekuzi vile vile waweza kufanya wengine waende, hata kama vile nafasi ya kuvalia mavazi mazuri inavyoweza kufanya wanawake fulani wahudhurie.

Ijapokuwa arusi ni wakati wa furaha, isisahauliwe kwamba, kulingana na Biblia, ni wakati mzito vile vile. Mwanamume na mwanamke wanapooana wanatazamiwa kupatana daima. Yajulikana sana kwamba watu wawili wanaoana “kwa yaliyo bora au mabaya zaidi” na “mpaka kifo” kitakapowatenganisha. Kwa kufaa, kwenye arusi zinazoongozwa na mashahidi wa Yehova mhudumu mwenye kusimamia anarudia kuonyesha msingi wa Maandiko kwa ndoa na wajibu wa Maandiko kwa mwanamume na mwanamke. Ijapokuwa yote haya yanatajwa hasa kwa wale wawili wanaooana, je! si mashauri mema kwa wote vile vile wanaosikiliza? Kabisa!

KWA WAUME NA WAKE

Leo, kati ya watu kwa jumla, ndoa inavunjiwa heshima kwa kadiri ambavyo watu zaidi na zaidi wanavyoendelea kuishi pamoja kama mume na mke bila ya kuoana kwanza. Kati ya wale wanaooana wakati wote uaminifu unakuwa mchache kwa nadhiri za ndoa na kwa mtu na mwenzake na wakati wote kunakuwa na talaka zaidi. Maelekeo yote ya siku hizi, kama vile utafutaji wa mambo ya kimwili, ufisadi, na upotovu, yote pamoja yanafanya iwe vigumu kufaulu katika ndoa. Hivyo hata kati ya watumishi wa Mungu wa Kikristo walio wakf huenda wengine wakashawishiwa watengane na kufuata kila mmoja njia yake wasipoweza kupata talaka inayofaa kulingana na Maandiko.

Je! hao wote, na vile vile wengineo walio na ‘dhiki zaidi katika mwili wao’ kuliko walivyotazamia, wasingefaidika kwa kuhudhuria sherehe ya arusi​—ya namna ya inayoongozwa katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova? (1 Kor. 7:28) Ingekuwa vema kama nini kwao kuyalinganisha matendo wanayotendeana na mashauri ya Biblia yanayotolewa! Bwana-arusi anapopewa mashauri, kila mume aweza vile vile kujiuliza mwenyewe ni kwa kadiri gani ambavyo anavyoifikia kanuni iliyowekwa na Mwanzilishi wa ndoa katika Neno lake Biblia. Ndivyo ilivyo na kwa kila mke bibi-arusi anapopewa mashauri juu ya wajibu wake kulingana na Maandiko kwa mumewe. Ikiwa ndoa ya watu wawili imekuwa ya vivi hivi na isiyo na mageuzi yo yote, kuhudhuria arusi na kuona na kuwasikia vijana wanaopendana na wenye tumaini kamili wakiweka nadhiri zao za ndoa vile vile kwaweza kusaidia kukumbusha wakati walipojisikia hivyo juu ya mtu na mwenzake. Huenda hata kukawavuta wafanye jambo fulani juu ya kuuchochea ‘upendo wao wa kwanza.’

WAZAZI NA WATOTO

Wazazi, wanaotumainia sikuzote watoto wao wawe na ndoa yenye furaha, nao vile vile wanaweza kufaidika kutokana na kuhudhuria sherehe hiyo ya arusi. Hivyo, mhudumu mmoja wa Kikristo, alipokuwa akitoa hotuba yake ya arusi, aliwasifu wazazi wa vijana wale wawili kwa kuwalea watoto wao “katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova” hata watoto wao wakaweza kuwa na ndoa ya kuheshimika katika nyumba yao ya ibada. Bila shaka, wazazi wote wenye vijana wa kiasi cha kuoa au kuolewa, wanaposikia maneno hayo, wanafanywa wathamini zaidi kadiri ya mambo yanayotiwa ndani katika kulea watoto wao.​—Efe. 6:4, NW.

Alipoendelea, mhudumu uyu huyu aliwasifu vile vile vijana wenyewe kwa kuwa waliepuka mitego ya ufisadi kusudi kwamba waweze kuwa na sherehe hiyo ya arusi iliyo ya kuheshimika. Lo! maneno hayo yalikuwa kichocheo cha namna gani kwa wasikilizaji vijana wafuate kanuni za Biblia na kutumia kujiweza! Vile vile walisaidiwa kufahamu namna ambavyo maneno ya mtume yalivyo kweli kwamba “utauwa hufaa kwa mambo yote,” kutia na furaha katika ndoa.​—1 Tim. 4:8.

Wale wanaofikiria ndoa kwa uzito nao kadhalika wanakubali kufaidika kutokana na kuhudhuria arusi kama hiyo. Wanapomsikia msemaji akiutaja wajibu na vile vile mapendeleo ya watu waliooana, yawapasa iwasaidie wawe na maoni ya kukomaa ya ndoa kuliko maoni ya mahaba tu, kana kwamba ndoa ilikuwa ni kitanda cha waridi. Watasaidiwa kuona ni kadiri gani ya furaha katika ndoa inayotegemea mambo yafaayo, kama vile kuwa mwenye busara, asiye na choyo na kufikiriana mtu na mwenzake. Vile vile, watakuwa wamekwisha sisitiza juu yao kwamba katika ndoa watu wanakuwa na ‘dhiki katika mwili wao’ na kwa hiyo lazima wajitayarishe “kuyatwaa machungu pamoja na matamu.”

KUFAIDIKA KUTOKANA NA KARAMU

Kunao wengine wanaofahamiana na wale wanaooana wanaotwaa nia ya kwamba wao hawana wakati wa kuihudhuria sherehe ya arusi penye Jumba la Ufalme, lakini wanao wakati wa kufika kwenye shangwe zinazofuata, wakati ambapo kutakuwako kunywa divai, kula na kucheza dansi. Hii yaweza kusemwa ni kulitanguliza gari mbele ya farasi. Kwa kweli, inakaribiana na kosa lililofanywa na mwindaji wa kale Esau, aliyependelea bakuli ya chakula cha dengu kuliko baraka za kiroho za ahadi iliyofanywa kwanza kwa babu yake Ibrahimu. Kuwako kwa mtu katika arusi ni wonyesho wa heshima kwa wale wanaooana, lakini kuwako kwa mtu katika karamu peke yake huenda kukamaanisha kwamba mapendezi ya mtu hasa katika maisha ni kuwa na wakati mzuri.​—Ebr. 12:16.

Karamu za arusi kati ya mashahidi wa Yehova mara nyingi zimefanywa kuwa nyakati za faida ya kiroho na za kujenga. Majuzi, penye mojawapo ya karamu hizi kulikuwako hotuba fupi, zikiunganisha uchangamfu na mashauri yafaayo yakitolewa na rafiki kadha wakubwa wa wenye kuoana. Vile vile nyimbo za Kikristo zilizofaa hasa kwa wakati huo ziliimbwa vizuri, na, bila shaka, shangwe zilianza kwa kuomba baraka za Mungu juu ya kipindi hicho.

Hapa vile vile kwapaswa kuwepo na uangalifu kwamba karamu inaendelea kuwa yenye kuheshimika na kwamba haigeuki kuwa ghasia au karamu ya ulevi, kama inavyotukia mara nyingi kati ya walimwengu. Kwa ufupi, penye karamu za arusi hali kadhalika shauri la mtume na litiiwe: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” Kufanya hivyo kutaifanya sherehe ya arusi, pamoja na shangwe zitakazofuata, si nyakati zenye furaha tu lakini vile vile nyakati za kujengana mtu na mwenzake na za kumbukumbu zipendezazo.​—1 Kor. 10:31.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki