Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 6/15 kur. 267-271
  • N’nini “Ufufuo wa Kwanza”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • N’nini “Ufufuo wa Kwanza”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “NAFSI” YAFUFULIWA
  • MAONI YAFAAYO NA YENYE MAKOSA YA “UFUFUO WA KWANZA”
  • HAWAPATWI NA “MAUTI YA PILI”
  • Ule Ufalme na lile Tumaini la Ufufuo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Zishikeni Sana “Habari Njema”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Tumaini la Ufufuo Lina Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Nguvu za Tumaini la Ufufuo
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 6/15 kur. 267-271

N’nini “Ufufuo wa Kwanza”?

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1, 2. Kwa sababu gani maoni ya ufufuo hayapaswi kuwa magumu kuaminika?

JE! wewe unaamini ufufuo? Yaani, kwamba wafu watarudishwa kwenye uzima? Biblia yasema: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Je! wazo hilo linaelekea kuwa lenye mashaka kwako?

2 Kwa kweli, halipaswi kushangaza. Ni kweli, sote twajua kwamba tumefanyizwa kwa vitu vingi sana mwilini na akilini. Lakini kwa hakika umbo letu la msingi laonyeshwa lote katika chembe zetu za mwili, zaidi katika chromosome zile 46 zilizomo katika kiini cha kila chembe. Zaidi ya yote, mazingira yetu na maono vinaungana na urithi wetu wa uzazi kutufanya namna tulivyo. Kwa hiyo, kwa nini lionekane kuwa jambo gumu mno Muumba asiweze kuufanyiza mfano huu kwa mara nyingine​—mpango unaolingana na wa kwanza wa chembe, pamoja na kumbukumbu? Ingekuwa vyepesi zaidi kuliko ilivyokuwa kuzipanga chembe wakati wa kuumbwa kwa mwanadamu, kutia ndani “mwundo” wa kwanza na uwezo wa kutokeza tabia za mtu na wa kupitisha tabia hizo kwa watoto. Muumba alifanya hivi mwanzoni.​—Zab. 139:13-15; Mwa. 5:3.

3. “Nafsi” ndiyo nini? Je! kwaweza kukawako nafsi kusipokuwa na mwili?

3 Lakini namna gani juu ya “nafsi”? Basi, kwanza lazima tuufahamu uhakika wa Maandiko kwamba kila kiumbe chenye uhai kina mwili, kiwe ni cha kimbinguni au cha kidunia. (1 Kor. 15:40) Kwa hiyo hakuna kitu kama ‘kivuli,’ kama kile kinachozungumzwa na wachawi. “Nafsi” ndiye mtu, kutia na utu na mwili vile vile. Katika Maandiko yote, sifa zote za kibinadamu, za akili, za kimwili na za kiroho, zaonyeshwa kama zikitokezwa na nafsi yenye uhai, mtu mwenye uhai. (Law. 7:18, 20, 21; 23:30; Zab. 105:18, NW) Kutenda kwa mwili ndiko kunakouonyesha utu. Maiti, bila ya “roho” au nguvu ya uhai, au bila ya pumzi inayoisaidia nguvu ya uhai, haina utu, wala utendaji. (Mwa. 7:22; Yak. 2:26; Mhu. 9:5, 10) Kwa hiyo si nafsi yenye uhai tena. Nafsi imekufa, ikakoma.​—Eze. 18:4, NW.

“NAFSI” YAFUFULIWA

4. Ni jambo gani lingepaswa kufanywa ili kufufua mtu?

4 Kwa hiyo, ili Mungu afufue mtu, ingempasa kufanya nini? Ingempasa kufanyiza mwili wenye tabia zile zile, akirudisha kumbukumbu vile vile, linalompa mtu tabia alizokuwa nazo wakati wa maisha yake. Hivyo ingepaswa nafsi yote irudishwe. Ndipo mtu angeweza kujijua mwenyewe. Kama sivyo, angekuwa kama mateka aliyepoteza fahamu, asiweze kusema yeye ni nani au alikuwa amefanya nini wakati uliopita.

5. Twajuaje kwamba Yehova aweza kufanya ufufuo?

5 Mtunga zaburi aliandika hivi, akisema kwa Yehova: “Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; chuoni mwako ziliandikwa zote pia, siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado.” (Zab. 139:16) Ikiwa Yehova anao uwezo wa kuona na kuwa na kumbukumbu la tabia za mtoto mara tu mimba inapochukuliwa, kwa nini asiwe na kumbukumbu la kweli la kutumia kuumba tena mtu aliyekufa?​—Linganisha Mwanzo 25:23; Warumi 9:11-13.

6. Kwa sababu gani mwili ule ule usingeweza kurudishwa?

6 Namna gani juu ya mwili wa mtu? Twajua kwamba chembe zinazofanyiza miili ya kibinadamu ni vifaa tu vinavyoifanyiza. Hazina utu. Kwa hiyo je!, kuna haja ya mwili uliofufuliwa kuwa ule ule, yaani, kuwa mwili ule ule uliohifadhiwa, au uliofanyizwa na chembe zile zile zilizokusanywa pamoja kwa mara nyingine? Kwa wazi sivyo. Kwa mfano, huenda mtu akawa alikufa, nazo chembe zilizotoka katika mwili wake uliooza huenda zililisha mti wa matunda wenye kumea karibu na kaburi lake. Huenda ikawa watu wengine waliyala matunda. Kwa hiyo miili ya watu wengi sasa inazo chembe hizo. Kwa wazi, wakati wa ufufuo miili yote isingeweza kurudishiwa chembe zile zile.

7, 8. Kwa sababu gani tusingeweza kusema kwamba mtu aliyefufuliwa angekuwa “mfano” tu?

7 Huenda wengine wakakataa hili, wakisema kwamba, kama ni hivyo, mtu yule angekuwa “mfano” tu, si mtu mwenyewe hasa. Angekuwa kama picha inayonaswa katika televisheni, “nakala iliyohifadhiwa” katika kumbukumbu la Mungu, ndivyo wanavyosema. Lakini wao wanasahau kwamba, hata sasa, sehemu iliyo kubwa ya miili yetu sikuzote inalika na mahali pake panachukuliwa na nyingine. Hii ndiyo sababu lazima tule. Inapokwisha miaka saba hivi mwili wa mtu unaelekea kuwa mwili tofauti. Hata anakuwa na sura tofauti. Lakini je! bado hatumhesabu kuwa mtu yule yule? Bila shaka. Wakati mama amwonapo mwana aliyepotea kwa muda mrefu, hata ikiwa sura yake imegeuka na ikiwa anazo tabia mpya, hali zake za msingi ni zile zile, na haupiti muda mrefu bila ya mama kuweza kumtambua. Naye anamkubali kama mwana wake.

8 Twaweza kutoa mfano hata zaidi: Mtu anakufa. Huenda akawa alipasuliwa vibaya sana katika ajali, au kwamba mapafu yake, ini au viungo vingine viliharibiwa kidogo na ugonjwa fulani. Kwa wazi, lazima arudi akiwa na mwili mpya au ulioponywa ikiwa ataendelea kuwa hai anapokwisha kufufuliwa. Yeye si “mfano” tu, bali ndiye mtu yule yule aliyerudishwa kusudi kwamba aweze kutenda kama “nafsi” Kwa mfano, mwili wa Lazaro ulioza kwa kadiri fulani, kwa maana, kama vile dada yake Lazaro Martha alivyomwambia Yesu penye kaburi: “Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne.” (Yohana 11:39) Na hali, alipofufuliwa na Yesu, yeye alikuwa, si mfano, bali Lazaro, naye alitambuliwa na Yesu Kristo kama Lazaro, vile vile na yeye mwenyewe na jamaa yake.

MAONI YAFAAYO NA YENYE MAKOSA YA “UFUFUO WA KWANZA”

9, 10. Kwa ufupi, ni akina nani wanaoupokea “ufufuo wa kwanza”?

9 Hata hivyo, n’nini maana ya maneno “ufufuo wa kwanza”? “Wa kwanza” waweza kumaanisha wa kwanza katika wakati na/au wa kwanza katika ubora. Kwa hiyo, lazima ufufuo huu uwe tofauti kama kitu cha pekee. Ni akina nani wanaoupokea ufufuo huo?

10 Kwa ufupi, “ufufuo wa kwanza” watumika kwa walio wa kwanza kuurudia ukamili wa uzima. Ukamili huo wa uzima haukupokewa na watu waliofufuliwa na manabii wa zamani, na nyumaye na Yesu Kristo na mitume. Walikufa tena. Hii ni kwa sababu Yesu Kristo hakuwa amekuja katika mamlaka ya Ufalme kuwahukumu watu na kuwathawabisha watumishi wake waaminifu.

11, 12. Toa muhtasari ya sehemu ya njozi ya Yohana ambapo anazungumza juu ya “ufufuo wa kwanza.”

11 Yaangalie sasa masimulizi ya Biblia ya “ufufuo wa kwanza” kama yanavyoonyeshwa katika njozi kwa mtume Yohana. Yohana anasema:

12 “Nami niliviona viti vya enzi, na walikuwako wale walioketi juu yake, nao walipewa nguvu ya kuhukumu. Naam, niliziona nafsi za wale waliokatwa kwa shoka kwa ushuhuda walioutoa kwa Yesu na kwa kusema juu ya Mungu, na wale ambao hawakuwa wameabudu wala mnyama wa mwitu wala mfano wake na ambao hawakuwa wameipokea alama juu ya, kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao. Nao wakawa hai na wakatawala kama wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu. (Mabaki ya wafu hayakuwa hai mpaka miaka elfu ilipomalizika.) Huu ndio ufufuo wa kwanza. Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa mauti ya pili haina mamlaka, lakini watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala kama wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.”​—Ufu. 20:4-6, NW.

13. Je! Yohana aliona “nafsi” zisizo na vichwa, na ni namna gani ya miili waliyokuwa nayo?

13 Zijapokuwa ‘ziliuawa kwa shoka,’ angalia kwamba hizi hazikuonekana kama “nafsi” zisizo na vichwa na Yohana. Bali, walikuwa watu wenye uwezo wa akili wa kuhukumu. Lakini, ili waketi juu ya viti vya enzi mbinguni, iliwapasa kuwa na miili ya kiroho, siyo ya kibinadamu. Juu ya ufufuo wao, mtume Paulo anaandika hivi: “Hupandwa mwili wa asili [katika mauti]; hufufuliwa mwili wa roho.”​—1 Kor. 15:44.

14. Kwa sababu ya maneno ya mtume Paulo katika Wakolosai 2:11-13, ni ulizo gani limetokea juu ya “ufufuo wa kwanza”?

14 Lakini huenda mtu aulize, Je! huu “ufufuo wa kwanza” si ‘kuzaliwa kwa kiroho kwa mara ya pili’ kunakotukia kama mojawapo la mambo ya kwanza katika mwendo wa Mkristo? Je! si kile ambacho mtume Paulo alikizungumza alipolionyesha kundi la Kolosai kwamba tohara ya Kikristo haikuwa ya halisi, katika mwili? Yeye aliandika: “Hii ni tohara kulingana na Kristo. Mmezikwa pamoja naye, mlipobatizwa; na kwa ubatizo, pia, mmefufuliwa pamoja naye kupitia kwa imani yenu katika uwezo wa Mungu aliyemfufua kwa wafu. Mlikuwa wafu, kwa maana mlikuwa watenda dhambi nanyi hamkuwa mmetahiriwa; yeye amewaleta ninyi kwenye uzima pamoja naye, ametusamehe dhambi zetu zote.”​—Kol. 2:11-13, The Jerusalem Bible; linganisha Waefeso 2:1-6.

15, 16. New Catholic Encyclopedia chasema “ufufuo wa kwanza” ni nini?

15 New Catholic Encyclopedia (kilichopewa haki ya ubuni mwaka wa 1967) kinaonyesha maoni haya, kikisema hivi, chini ya kichwa “Imani katika Miaka Elfu”:

16 “. . . ‘Ufufuo wa kwanza’ wafananisha Ubatizo, . . . ambao kwao mtu anashiriki katika Ufufuo wa Kristo. . . . Waaminifu wote, wale waliomo duniani na walioko mbinguni vile vile, wanashiriki katika utawala wa miaka 1,000 wa Yesu, mfano wa muda wa maisha yote ya Kanisa yakiangaliwa katika hali yake tukufu kutoka Ufufuo wa Kristo mpaka Hukumu ya Mwisho.”

17. ‘Muda wa maisha ya Kanisa’ wahakikishaje kwamba New Catholic Encyclopedia, inakosea katika ufafanuzi wake wa “ufufuo wa kwanza”?

17 Je! maelezo haya yanapatana na “ufufuo wa kwanza” ambao Yohana anataja katika Ufunuo 20:4-6, NW​—mahali pa pekee katika Biblia ambapo maneno haya yanatumiwa? Hapana, kwa maana Yohana anasema, “wakatawala kama wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu.” ‘Muda wa maisha ya Kanisa’ umekuwa, si miaka 1,000 tu, bali karibu miaka 2,000.

18. (a) Je! Wakristo wa kweli wametawala kama wafalme tangu wakati wa ubatizo wao na kuendelea? (b) Ni wakati gani Wakristo wanapotawala kama wafalme?

18 Zaidi ya hayo, je! amepata mshiriki ye yote wa kundi la kweli la Kikristo duniani ‘kutawala’ kama mfalme mpaka wakati huu? Hata Paulo, mtume, aliandikia washiriki fulani wa kundi katika Korintho wenye kujitakia makuu: “Mmemiliki PASIPO sisi. Naam, laiti mngemiliki, ili sisi nasi tumiliki pamoja nanyi! Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu.” (1 Kor. 4:8, 9) Alilionyesha shauri la kutawala kwa mmisionari mwenzake Timotheo kama linalokuja kufuata kifo cha kimwili cha Mkristo, akisema hivi: “Ni neno la kuaminiwa. Kwa maana, kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi.”​—2 Tim. 2:11, 12.

19. Yesu alisema nini juu ya wakati ambapo ndugu zake za kiroho wangeanza kutawala kama wafalme?

19 Miaka mingi nyumaye, wakati mtume Yohana alipokuwa uhamishoni katika kisiwa cha Patmo, alimtaja Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa kama akiliambia hivi kundi katika Laodikia: “Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.” (Ufu. 3:21) Kwa hiyo, utawala wote ungekuwa wa wakati ujao, kufuata kifo cha wanafunzi waaminifu wa Kristo, siyo tangu siku ya ubatizo wao.

20. Paulo alisema nini juu ya Wakristo wawili wa kujidai waliofundisha kwamba ufufuo ulikuwa umekwisha kuwako tayari?

20 Paulo vile vile alizungumza juu ya Wakristo wawili wa kujidai, Himenayo na Fileto, kwamba walikuwa ‘wametoka katika kweli, wakisema kwamba ufufuo umekwisha kuwako.’ (2 Tim. 2:17, 18, NW) Kwa hiyo yeye hakuuhesabu ubatizo wa Mkristo kama wakati wa kufufuliwa kwake.

21. Onyesha kwamba “ufufuo wa kwanza” ni kufufuka kwa halisi kutoka kwa wafu.

21 Kwa hiyo, “ufufuo wa kwanza” wa Ufunuo 20:4-6 ni ufufuo hasa, wa halisi kutoka kifo cha kimwili, kutoka Sheol, kaburi la kawaida la wanadamu. Mtume Petro alizungumza juu ya urithi wa kimbinguni, si kama uliokwisha kupatikana tayari, bali kama “uliotunzwa mbinguni” na kama “wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.” Vile vile alizungumza juu ya “ahadi tukufu” za Mungu, kwamba Wakristo ‘wangekuwa washiriki katika hali ya kimungu.’ (1 Pet. 1:4, 5; 2 Pet. 1:4, NW) Ili wapate “hali ya kimungu” ingewapasa kuvua hali ya kibinadamu na ya kimwili, ‘uharibifu wakivaa kutokuharibika.’ Bila shaka miili yao ya nyama haikuwa isiyoweza kuharibika wala isiyokufa.​—1 Kor. 15:50, 52-54.

HAWAPATWI NA “MAUTI YA PILI”

22. Ufunuo 20:6 waonyeshaje kwamba wale waliozaliwa kwa kiroho duniani hawajapata “ufufuo wa kwanza”?

22 Jambo jingine la kuhakikisha laonekana katika Ufunuo 20:6, NW: “Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa mauti ya pili haina mamlaka.” Mauti hiyo ya pili yafananishwa na “ziwa la moto liwakalo kwa kiberiti.” (Ufu: 19:20; 20:14) Je! ndivyo ilivyo kwa wale waliobatizwa tu katika maji na waliofanywa hai kwa kiroho kutoka kifo katika makosa na dhambi na waliofufuliwa pamoja kwa kiroho na ‘kuketishwa . . . katika sehemu za kimbinguni pamoja na Kristo Yesu’? (Efe. 2:1, 5, 6, NW) Hapana, bado yawezekana kwao kuwa wasio waaminifu chini ya jaribu na kuja chini ya adhabu ya “mauti ya pili,” kuharibiwa kabisa. Ndiyo sababu mtume Paulo alionya Wakristo waliobatizwa na wakatiwa mafuta: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” Vile vile, Yesu alishauri hivi: “Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima.”​—1 Kor. 10:12; Ufu. 2:10.

23. Maneno ya mtume Paulo katika Waebrania 6:4-8 na 10:26-31 yanahakikishaje kwamba waliozaliwa kwa roho, wanapokuwapo duniani, si wasioweza kupatwa na mamlaka ya “mauti ya pili”?

23 Ikiwa Wakristo waliobatizwa na wakatiwa mafuta wenye tumaini la kimbinguni wangekuwa wamekwisha furahia “ufufuo wa kwanza” tayari na kuwa wasioweza kupatwa na mamlaka ya “mauti ya pili,” ingalikuwa kazi bure kwa Paulo kuandika kama alivyoandika katika Waebrania 6:4-8 na 10:26-31. Hapa Paulo alionya kwamba mtu aliyepata kuwa mpokeaji wa roho takatifu na ambaye kufuata hapo akawa kafiri asingeweza kurudishwa kwenye toba, kwa maana alimtundika Mwana wa Mungu kwa mara nyingine kwa ajili yake mwenyewe na kumweka Yeye kwenye aibu ya waziwazi. Watu wa namna hiyo, alisema, walimkanyaga Mwana wa Mungu, wakaidharau damu ya agano na kuikasirisha roho ya fadhili zisizostahili. Mungu angefikiliza kisasi juu yao.

24. (a) Yesu Kristo alikuwaje “mzaliwa wa kwanza wa waliokufa”? (b) N’nini “ufufuo wa kwanza”?

24 Kwa kuwa “juu ya hawa [wanaopata ufufuo wa kwanza] mauti ya pili haina mamlaka,” twaweza kufahamu kwa nini unaitwa “ufufuo wa kwanza.” Ni namna ile ile ya ufufuo ambao Yesu Kristo aliupata siku ya tatu ya kifo chake, ufufuo kwenye ukamili wa mara hiyo wa uzima. Ndipo Yesu Kristo alipokuwa “mzaliwa wa kwanza wa waliokufa.” (Ufu. 1:5; Kol. 1:18) “Ufufuo wa kwanza” si wa kwanza katika wakati tu bali vile vile “wa kwanza” kwa kuwa ndio ufufuo ulio bora ambao wafu wangeweza kuupata. Ni ufufuo kwenye uzima usioharibika na usiokoma kama mwana wa Mungu katika mbingu zake mwenyewe.

25. Mtume Yohana anaonyeshaje kwamba Wakristo waliotiwa mafuta duniani hawajaupata “ufufuo wa kwanza”?

25 Hili ni tumaini zuri ajabu. Mtume Yohana aliwaandikia watiwa mafuta wenzake: “Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo.”​—1 Yohana 3:2.

26. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya wale wanaoupokea “ufufuo wa kwanza”?

26 Mungu awezaje kuwa na matumaini hayo kwa hawa hata kuwapa kutokufa na kutokuharibika​—ndiyo, hata kuwafanya wafalme washirika pamoja na Yesu Kristo, wakitawala wanadamu duniani, kutia na wale watakaokuja kutoka mautini katika ufufuo wa kidunia?a Ni wangapi wanaoupokea “ufufuo wa kwanza” kama warithi wa kimbinguni? Wao wanastahilije? Watatawala kwa muda gani na kwa kusudi gani? Maulizo haya yataangaliwa katika matoleo yafuatayo ya Mnara wa Mlinzi.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

[Maelezo ya Chini]

a Maneno “ufufuo wa kwanza” yamaanisha ufufuo wa wengine, kama inavyohakikishwa kabisa katika Biblia.​—⁠Matendo 17:31; 24:15.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki