Miaka Elfu ya Faraja kwa Wanadamu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1-3. Watu wengi wenye ujuzi wanakubaliana juu ya nini kwa habari ya uhitaji wa wanadamu, lakini wanatofautianaje katika jambo hili?
LEO watu wenye ujuzi wanakubaliana katika jambo moja—kwamba wanadamu wanahitaji faraja. Katika hili wameungana mkono, ajapokuwa kila mmoja kwa kawaida ana ufumbuzi tofauti wa kutoa. Ross Smyth, aliyekuwa rais wa World Federalists of Canada wakati uliopita, majuzi alitoa hotuba ambamo alisema hivi:
2 “Leo ufundi wa hali ya usafirishaji na mawasiliano umeifanya dunia kuwa kijiji. Lakini ni kijiji pasipo jumbe wa mji (“mayor”), pasipo baraza yenye kuongoza ifaavyo, jeshi la polisi na utaratibu wa hukumu. Kama vile ndege kubwa yenye abiria 365 ipitavyo kasi hewani, ndivyo na dunia yetu ya sayari inavyopita mbio mbio angani ikiwa na abiria bilioni 3-1/2 lakini hakuna mtu anayeiongoza.”
3 Bw. Smyth anaonyesha uhitaji wa msingi, yaani, serikali fulani iliyo na mamlaka, uwezo na hekima ya kuongoza ifaavyo kwa faida ya watu. Yeye anaamini kwamba serikali ya ulimwengu iliyoungana katika utawala ndilo jibu.
4. Ni serikali gani iliyo jibu kwa uhitaji wa wanadamu?
4 Kwa karibu miaka elfu sita wanadamu wamehitaji faraja, lakini hakuna wakati mwingine walipopata kuihitaji kwa haraka sana kama sasa. Ni serikali gani ambayo ndiyo jibu hasa? Mungu, aliyeiumba dunia na kumweka mwanadamu juu yake, anatuambia kwamba yeye atatoa serikali ambayo itauondoa uharibifu wote wa miaka elfu sita iliyopita ikifanya hivyo kwa muda wa miaka elfu moja tu na kuwaletea wanadamu mahitaji yao yote na tamaa za kupata furaha. Hii ndiyo ufalme wa Mungu wa Kimasihi.
5-7. Ni kazi gani ya kutangulia ambayo lazima ifanywe mbele ya kuja kwa kipindi cha miaka elfu cha faraja?
5 Utailetaje faraja hii? Biblia yaonyesha kwamba kazi fulani ya kutangulia lazima ifanywe mbele tu ya hiyo miaka elfu ili serikali ya Mungu iwe na miaka elfu kamili ya amani ya kurudisha wanadamu kwenye hali njema.
6 Kama ilivyozungumzwa katika matoleo yaliyopita ya gazeti hili, dini ya uongo na taratibu ya kisiasa na ya kibiashara ya ulimwengu huu lazima iharibiwe. Utaliona hili likisimuliwa katika Biblia katika Ufunuo sura za 17-19. Kufutiliwa mbali kwa wapotovu na waharabu wa dunia kutaleta faraja kuu, lakini kungali kutakiacha chanzo chenyewe hasa cha ole za dunia bila kuondolewa. N’nani au n’nini chanzo hiki?
CHANZO HASA CHA OLE ZA MWANADAMU
7 Chanzo hasa cha ole za wanadamu ni Shetani Ibilisi, mtu asiyeonekana wa kiroho. Mtu huyu anao uwezo mkuu. Yeye si ‘kanuni ya uovu’ tu, wala yeye haridhishwi na kushawishi watu, hapa na pale, ili watende dhambi. Yeye anaitwa “mungu wa dunia hii,” “mtawala wa ulimwengu,” “audanganyaye ulimwengu wote.”—2 Kor. 4:4; Yohana 14:30, NW; Ufu. 12:9.
8, 9. Kwa sababu gani dunia imepatwa na ole zilizo kubwa kupita zote katika kizazi chetu?
8 Mnamo kipindi cha wakati tangu mwaka wa 1914 C.E., ulimwengu umepatwa na ole zilizo kubwa kupita zote. Biblia yaeleza sababu yake. Yaonyesha kwamba wakati huo hatua ya msingi ilichukuliwa juu ya adui huyu wa Mungu na mwanadamu na Yesu Kristo, aliyefanya vita na Shetani na mashetani wenzake naye akawatupa watoke katika mbingu mbele za Mungu na kuja chini katika ujirani wa dunia. Juu ya matokeo ya pigano hili, Biblia yasema hivi: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufu. 12:7-12.
9 Kwa kweli, tangu wakati huo dunia yote imekuwa mahali pa kufanyiwa kazi na mashetani waovu, watu waovu wa kiroho, kwa zaidi ya miaka 50 sasa. Hii yaonyesha kwa nini taabu zinaongezeka katika kizazi chetu. Kwa hiyo, dunia itakaposafishwa kwa kuharibiwa kwa vyama vibovu vya kibinadamu na wafuasi wavyo, lazima Ibilisi na mashetani wake waondolewe ili faraja kamili ipate kuja.
10, 11. Biblia inaonyesha nini kitakachotukia taratibu za kidunia zitakapokwisha kuharibiwa?
10 Biblia haituachi tukisie kama hilo ndilo litakalotukia hasa. Mara imalizapo kusimulia kuharibiwa kwa hii taratibu ya mambo duniani na majeshi ya kimbinguni ya Kristo, Biblia inasema:
11 “Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache.”—Ufu. 20:1-3.
AMANI NA KUFUNGULIWA KUTOKA MAUTINI
12. Kufungiwa kwa Shetani shimoni kutakuwa na matokeo gani kwa dunia?
12 Tendo hili ambalo kwalo Yesu Kristo anamtia Ibilisi (pamoja na mashetani wake) kifungoni katika “shimo kubwa” (NW) kwa amri ya Yehova, linawafanya kana kwamba ‘hawakuwako’ kwa miaka elfu. (Luka 8:30, 31; linganisha Ufunuo 17:8.) Hivyo hakutakuwako mgogoro kutoka makao yasiyoonekana ya kiroho wa kupotosha wanadamu duniani. Hii itamaanisha mengi zaidi kwa wanadamu kuliko tuwezavyo kufahamu hasa. Shetani amekuwa ndiye “mfalme wa uwezo wa anga,” yaani, mtawala asiyeonekana. Ebu wazia itakavyomaanisha kwa ujamaa wenye amani kati ya wanadamu Shetani mwenyewe atakapokuwa si “roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi” tena.—Efe. 2:2.
13. N’nini kitakachotukia Shetani atakapokwisha kufungiwa shimoni?
13 Shetani atakapofungiwa shimoni miaka elfu ya utawala wa Kimasihi itaanza. Idadi ndogo ya ndugu za kiroho wa Yesu Kristo waliobaki duniani watafanya kazi pamoja na wenzi wao wairembeshe dunia kwanza kama bustani ya paradiso. Kisha ufufuo wa wafu utaanza. Mtume Yohana anatoa habari za njozi hii: “Nayo bahari ikawatoa wafu waliomo ndani yake, na mauti na Hades vikawatoa wafu waliomo ndani yavyo, nao wakahukumiwa mmoja mmoja kulingana na matendo yao.”—Ufu. 20:13, NW.
14. Ni nafasi gani itakayotolewa kwa waliofufuliwa?
14 Kati ya wale watakaotoka katika kaburi la kawaida la wanadamu atakuwako yule mtenda mabaya aliyeangikwa juu ya mti wa kufishia kando ya Yesu, ambaye Yesu alimwambia: “Kweli mimi nakuambia wewe leo hii: Pamoja nami wewe utakuwa katika Paradiso.” (Luka 23:43, tafsiri ya Rotherham; New World Translation) Mtenda mabaya huyu atatoka Hades aingie katika Paradiso ya kidunia waliyorudishiwa wanadamu na ufalme wa Yesu Kristo. Katika Paradiso hiyo mtenda mabaya ataishiriki nafasi ya kuusahihisha mwendo wake wa maisha na kuondolewa kutokamilika kwa kibinadamu na hali ya dhambi pamoja na wafu wengine wote wa kibinadamu waliofufuliwa. Kwa njia hii, mwishoni mwa utawala wa Kristo wa miaka elfu, yeye ataweza kuufikia mradi wa ukamilifu wa kibinadamu katika mfano wa Mungu. Lakini, wale wote watakaofikia ukamilifu wa kibinadamu na hali ya kutofanya dhambi duniani mwishoni mwa miaka elfu lazima wapite katika jaribu la mwisho la uaminifu wao kwa utawala wa Mungu wa enzi yote ya ulimwengu wote, ili wapate kuudumisha uzima wao mkamilifu.—Ufu. 20:7-9.
15, 16. (a) Ni kwa njia gani “hao wafu waliosalia hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu”? (b) Namna gani juu ya wanadamu waliokamilishwa wasioendelea kuwa waaminifu mnamo jaribu la mwisho?
15 Wale wanadamu wakamilifu duniani watakaodumisha ukamilifu wao na kuendelea kuwa waaminifu kwa utawala wa Mungu ufaao watatangazwa kuwa wenye haki na Mwamuzi Mkuu Zaidi Sana, Yehova Mungu. Yeye atawatangaza watu hawa walio safi kuwa wenye kustahili uzima wa milele, na Yeye atawapa haki ya kupata uzima usiokoma katika furaha katika Paradiso ya kidunia. Wakiwa huru na laana yote, watiifu hawa ndipo watakapoishi kweli kweli kulingana na maoni kamili ya Mungu. Kwa hiyo, kwa njia hii ni kwamba “hao wafu waliosalia [mbali na wale wenye kuufurahia ufufuo wa kimbinguni] hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu.” (Ufu. 20:5) Maneno haya yanatumika kwa “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa Har–Magedoni na vile vile waliofufuliwa.
16 Lakini wanadamu hao waliokamilishwa ambao hawatalipita jaribu la uaminifu wa kimungu mnamo “muda mchache” ambapo Shetani atafunguliwa ikiisha kumalizika miaka elfu moja wataharibiwa milele, sawa na Yohana anavyolionyesha jambo hili katika njozi yake, akisema: “Nayo mauti na Hades vikatupwa katika ziwa la moto. Hii maana yake mauti ya pili, ziwa la moto. Zaidi ya hayo, mtu awaye yote asiyepatikana ameandikwa katika kitabu cha uzima alitupwa katika ziwa la moto.” (Ufu. 20:14, 15, NW) Kwa hiyo hawa wasioaminika hawaufikii uzima wa milele.
MIAKA ELFU ILIYO HALISI
17, 18. New Catholic Encyclopedia kinatoa maelezo gani juu ya miaka elfu ya utawala wa Kristo?
17 Je! utawala wa miaka elfu wa ufalme wa Kimasihi ni wa miaka elfu kamili, iliyo halisi? Wengine wanasema Hapana. New Catholic Encyclopedia kinaendelea kusema hivi kinapokwisha kutaja kwamba “utawala wa miaka 1,000 wa Yesu [ni.] mfano wa muda wote wa maisha ya Kanisa”:
18 “ . . . Kufungwa mnyororo kwa Shetani mnamo kipindi kiki hiki kwaonyesha kwamba maongozi ya Shetani yamepunguzwa sana, hayakuondolewa kabisa. Kupunguzwa kwa maongozi ya Shetani ndiyo matokeo ya kufaa kwa Ukombozi wa Kristo. Kutakapokwisha kuwako jaribu la mwisho karibu na mwisho wa wakati . . . Shetani atashindwa kabisa na Kristo.”
19, 20. Je! maongozi ya Shetani yamepunguzwa mnamo ‘muda wa maisha ya Kanisa’?
19 Lakini kutokana na tuliyoyaangalia, ni wazi kwamba utawala wa miaka elfu wa Kristo siyo ‘muda wa maisha ya Kanisa,’ ulioanza siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 C.E., na ukaendelea hata sasa—zaidi ya miaka 1,900. Kwa nini sivyo? Basi, je! maongozi ya Shetani yamepunguzwa hasa, kwa sababu ya “kufaa kwa Ukombozi wa Kristo”? Kama ndivyo, mtume Petro asingaliona lazima ya kuwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”—1 Pet. 5:8.
20 Wala mtume Paulo asingalisukumwa kuwaonya ndugu zake hivi: “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu . . . [ni] juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”—Efe. 6:11, 12.
21, 22. N’nini kinachoonyesha Ibilisi hakuacha kuchukua hatua juu ya kundi la Kikristo mnamo utawala ‘wa mfano,’ kama vile Encyclopedia cha Kikatoliki kinavyoeleza?
21 Zaidi ya hayo, ukiisha kuitabiri vita mbinguni, Ufunuo unasema hivi: “Joka [Ibilisi] akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” (Ufu. 12:17) Je! hii yasikika kama kutiwa mnyororo kwa Shetani?
22 Lo! ingekatisha tamaa kama nini kwa wanadamu ikiwa miaka elfu ingekuwa imekwisha kupita tayari, kama maoni haya ya Kikatoliki yanavyotaka kuonyesha! Hakujapata kuwa na faraja yo yote kwa wanadamu miaka yote hiyo. Hata Wakristo wa kweli wamepatwa na mateso makali. Wanadamu kwa jumla wameugua wakiwa katika mambo mengi yenye kulemea na taabu, na katika miaka michache iliyopita ole zao zimeongezeka.—Rum. 8:19-22.
23, 24. Lazima wale wanaotamaini faraja ya milele kutokana na magumu ya ulimwengu huu na ole wafanye nini sasa?
23 Kulingana na orodha ya wakati ya Biblia, tu karibu na mwisho wa miaka elfu sita ya historia ya mwanadamu, nao utawala wa kifalme wa Kristo kwa ajili ya faraja na kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu unakaribia sana. Lo! ni tumaini zuri ajabu! Je! wewe watamani kuishi chini ya utawala huo ujao? Ndilo jambo la pekee lifaalo na la kawaida kutamani.
24 Ikiwa wewe ungependa uuone wakati huo wa faraja, huwezi kuupata katika serikali zilizoundwa na wanadamu, kwa maana shauri lote la serikali njema lategemea kanuni za haki. Huzipati hizi katika serikali za wanadamu wasiokamilika. Kwa hiyo ikiwa wewe unapenda kanuni za haki, utapendezwa kujifunza mengi zaidi juu ya serikali ya Mungu na watawala wake. Hii itaangaliwa katika matoleo yajayo ya gazeti hili.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.