Kumbuka Kukaribia kwa Kuwapo kwa Siku ya Yehova’
“Inawapasa ninyi mwe watu wa namna gani . . . kukumbuka kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova.”—2 Pet. 3:11, 12, NW.
1. “Siku ya Yehova” ni nini, na kwa sababu gani imetupasa sasa tuifikirie kwa uzito?
WAKATI wa kufanya hesabu unakaribia kwa wanadamu wote. Ndio wakati hukumu ya kimungu itakapofikilizwa juu ya waovu, vile vile ni wakati wa ukombozi wa wenye haki. Watu wote watakaokuwa wakiishi wakati huo watatakiwa watoe hesabu ya namna walivyozitumia maisha zao, kwamba ni kwa kutojali kwa kichoyo mapenzi ya Mungu na hali njema ya wanadamu wenzao au kwa kumtii Mungu kwa upendo na bila choyo kuwahurumia wanadamu wenzao. Kwa sababu utakuwa wakati wa kufanya hesabu upande wa Mungu wa kweli, kipindi kinachokuja kinatajwa katika Biblia kama “siku ya Yehova.” Kinastahili tukifikirie kwa uzito.—Sef. 2:2, 3.
2, 3. Mtume Petro aliwasihi Wakristo wote wawe na maoni gani juu ya “siku ya Yehova”?
2 Je! wewe unakumbuka kukaribia kwa siku ya Yehova? Je! waiona kuwa kweli? Mtume Petro aliona hivyo. Aliwatia moyo Wakristo wote waone hivyo, kwa maana katika 2 Petro 3:11-13, NW aliandika hivi: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitakomeshwa katika njia hiyo, inawapasa ninyi mwe watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya kumwabudu Mungu, mkingojea na kukumbuka kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo katika hiyo mbingu kwa kuteketea zitakoma na vitu vya asili kwa kupata moto sana vitayeyuka! Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya tunazongojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.”
3 Je! wewe unakumbuka kukaribia kwa siku hii yenye moto? Je! wewe unaiona kuwa kweli hata unaweza kuiona waziwazi, mara hii mbele yako? Kulingana na The Kingdom Interlinear Translation, usemi huo “kukumbuka kukaribia” ni “kuhimiza.” Hivyo haitupasi tuwe tunaikawiza, yaani, tusiitazame siku ya Yehova kama iko mbali sana, na kuiahirisha.
4. Ni kwa sababu gani ingetokeza hasara kubwa kwetu ikiwa tungeshindwa kuikumbuka siku ya Yehova?
4 Maoni haya ni ya lazima kwa Wakristo wote, katika nyakati zote, bila kujali wakati “siku” ya Yehova itakapofika. Kwa sababu gani? Mtume Paulo anajibu hivi, “kwa maana tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” (l Kor. 7:31, NW) Ni kama tamasha inayogeuka jukwaani ambayo, ijapokuwa iwe nzuri sana, upesi inafuatana na tamasha nyingine, yenye mambo tofauti na wachezaji tofauti, hata hakuna kitu kinachoendelea kwa muda mrefu. (Mhu. 1:4) Basi, kwa sababu gani Mkristo, aliye na tumaini la uzima wa milele katika ulimwengu wa milele wenye mambo bora kweli kweli, apoteze wakati wake na nguvu zake kwa ajili ya jambo la muda, linalopita? Kama inavyosemwa katika 1 Yohana 2:17, ‘ulimwengu huu unapita.’ Karibuni utatoweka kabisa, milele. Je! wewe wasadiki hilo?
MAONI YA MITUME
5, 6. Mitume kwa maoni yao juu ya Kristo na ufalme wake walituwekeaje sisi mfano mzuri?
5 Tukiwa macho na katika upatano wa mambo ambayo Yehova anafanya, tutakuwa washiriki wa baraka kuu sikuzote. Kwa upande mwingine, ikiwa tunaanza kuchelewa, au ikiwa tunasitawisha maoni ya kuwa wenye mashaka kwa mambo tunayoelezwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” tumo hatarini. Tunaweza tukajikuta tumo katika hali kama ya wale wanaochelewa kujipanga katika safu ya askari jeshi, wenye kuchukuliwa kwa vyepesi na adui.—Mt. 24:45.
6 Tamaa hiyo ya kutokosa cho chote ambacho Mungu angetoa yalikuwa ndiyo maoni ambayo mitume wa Kristo walikuwa nayo. Walipomwuliza Yesu hivi, “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako?” wao hawakujua kwamba kuwapo kwa wakati ujao kungekuwa kwa kutoonekana. (Mt. 24:3, NW) Hata alipokwisha kufufuka waliuliza hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” (Matendo 1:6) Wao waliutazamia urudishwe katika njia yenye kuonekana. Kuuliza kwao kulionyesha kwamba walikuwa wakikumbuka kukaribia kwa ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo. Walitazamia waje washiriki katika ufalme huo. Wao hawakuwa kama Wayahudi wasioamini waliomwona Yesu waziwazi akiwa katikati yao katika mwili lakini wasifahamu kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa, hata ikasemekana kwamba “ufalme wa Mungu umo miongoni mwenu.” (Luka 17:21, NW) Yesu alikuwa na ushahidi wote wa kuonyesha yeye alikuwa Masihi. Yeye alikuja katika njia iliyotabiriwa na Maandiko. Lakini Wayahudi hao hawakumkubali. Walijikwaza juu yake. Kwa sababu gani?
7, 8. Ni kwa sababu gani waandishi na Mafarisayo walishindwa kumkubali Yesu kama Masihi aliyeahidiwa?
7 Walikuwa wenye kiburi na wenye kupenda mambo ya kimwili. Walipenda zaidi sifa na kukubaliwa na wanadamu kuliko na Mungu. Yesu aliwaambia waziwazi hivi: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote. . . . [Ninyi] mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.” (Mt. 23:27, 28) Aliwaambia wanafunzi wake kwamba viongozi hao wa kidini walizifanya kazi zao zote ili watazamwe na wanadamu, wakipenda mahali pa heshima sana na kutaka kusifiwa na watu. Walikuwa wenye kupenda fedha, lakini hawakumpenda Mungu.—Luka 16:14.
8 Wakiwa na maoni haya haikuwezekana viongozi wa kidini wa Kiyahudi wamkubali Yesu kama Masihi. Ijapokuwa Kristo alikuwa mbele yao, katika mwili, akifanya matibabu ya ajabu kuliko yote, macho yao yalikuwa yamepofuka. Wakiwa na akili na moyo huu, hawakuona uhakika katika Yesu kwa sababu choyo chao kiliwafanya watafute mambo yasiyo ya kweli, kulingana na kanuni za ulimwengu.—Yohana 5:39-44; Isa. 8:14, 15; Mt. 13:57.
9. Ikiwa tungeahirisha kuwapo kwa siku ya Yehova katika akili na mioyo yetu hali yetu ya kiroho ingepaswaje?
9 Haitupasi sisi leo tuwe wenye kupenda mambo ya kimwili kama wao. Ni jambo la hatari sana kujiachilia wenyewe kuingia katika hali yenye usingizi na yenye utepetevu, tukiahirisha kuwapo kwa siku yenye moto ya Yehova katika akili na mioyo yetu. Tukifanya hivyo, hatutayafahamu maongozi ya Mungu, maagizo anayotupa sisi. Tutashindwa kumjua yeye, kuzifahamu sifa zake bora. Moyo wenye kusinzia hautatufanya tuzifahamu huduma zinazotakiwa kufanywa. Hatutakuwa ‘tayari’ wakati wo wote au kutaka siku hiyo ije. Tutakuwa na maoni yasiyo sawa hata “siku” hiyo itufikie kwa ghafula.—1 The. 5:2-5.
KINACHOONYESHWA NA HALI ZA ULIMWENGU
10. (a) Ni katika njia gani wakati wetu unaonyeshwa na orodha ya tarehe ya Biblia? (b) Viongozi wa ulimwengu wanaionaje hali yenye hatari inayowaelekea wanadamu?
10 Orodha ya tarehe inaonyesha waziwazi wakati huu tunamoishi kuwa wenye maana sana. “Nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilizoanza mwaka wa 607 B.C.E. zikaendelea mpaka mwaka wa 1914 C.E., zimekwisha. (Luka 21:24, NW) Karibuni miaka elfu sita ya historia ya kibinadamu itamalizika. Kulingana na mambo haya ya hakika, tunayoona yakiupata ulimwenguni yenye maana sana. Yanaelekeza kwenye mkataa gani? Hali za ulimwengu zinatoa ushahidi wenye nguvu wa kukaribia kwa mwisho. Sasa, kwa mara ya kwanza, hata viongozi wa ulimwengu wamekubali kwamba uharibifu wa ulimwengu unaelekea kutukia bila shaka. Wanakubali kwamba vita ya atomiki yenye kutumia vifaa vyote ingekuwa yenye hatari sana hata wasingeweza kuwako wenye kushinda, ila wenye kushindwa. Wengi, zaidi wanasayansi,wanasema kwamba kuna hatari iliyo kubwa hata zaidi kutokana na uchafu wa ulimwenguni pote, na vile vile kutokana na ongezeko la haraka la watu duniani, pamoja na njaa kuu mahali pote, maradhi na wasiwasi ambao linaelekea kuleta. Taarifa katika gazeti Washington Post ilisema hivi: “Kwa ghafula katika zo zote za nchi zilizo tofauti—United States, Uingereza, Ufaransa, Ujeremani, Italia, Sweden, Czechoslovakia, Urusi, India, Japan—watu wenye vyeo wameona kukaribia sana kwa hatari isiyo na mfano wake katika zote ambazo zimewapata wanadamu.” Watu hawa wanakubali kwamba, ingawa huenda wanadamu wakasalimika hatari hizi moja moja, wasingeweza kusalimika ikiwa zote, au hata nyingi kati ya hizo, zingetukia mara hiyo. Katika kila sehemu—vita, kuongezeka kwa watu, elimu ya tabia za vitu vyenye uhai na mazingira yao, uvunjaji wa sheria, njaa, maradhi, wasiwasi, uharibifu unaelekea kutokea, na yote hayo yangeweza kutokea mara kwa wakati mmoja.
11. (a) Ni kwa sababu gani si jambo la akili kuitazamia elimu ya ufundi kuondoa magumu? (b) Sababu gani uharibifu wa ulimwengu hautatokana na vyanzo ambavyo wanadamu wanaogopa? (c) Kama inavyoonyeshwa katika Biblia, “dhiki kubwa” itaanza wakati gani?
11 Ijapokuwa wengine wanasema kwamba elimu ya kisasa ya ufundi inaweza na itaondoa magumu, je! elimu ya ufundi inafanya nini sasa? Je! haikushiriki daraka la kufanya hali iwe mbaya zaidi, hasa katika upande wa vita na uchafu? Na hata ikiwa elimu ya ufundi ingeweza kuondoa magumu haya, je! itafanya hivyo? Hapana, kuna choyo kingi mno kati ya watu, kuna mambo mengi mno yenye choyo yanayozuia jitihada za kuondolea hali mbaya. Hata hivyo uharibifu unaotabiriwa hautatokana na vyanzo ambavyo wanadamu wanaogopa. Taratibu ya sasa ya ulimwengu haitajiangukia yenyewe. Kwa kuwa sasa imeonekana kana kwamba imeshindwa, umekaribia wakati wa Yehova mwenyewe aiharibu. Naye aliuonyesha wakati huu waziwazi katika Neno lake hapo zamani. Bila kukosea, Biblia inakazia mwaka wa 1914 C.E. kama ndio wakati ambapo “ufalme wa ulimwengu” ulipopewa kwa Kristo. “Dhiki kubwa” itatokea wakati kizazi kilichokuwa hai wakati huo hakijatoweka.—Ufu. 11:15; Dan. 4:10-17; Mt. 24:21, 34.
12. Ni matukio gani yanayoonyesha kupungua kwa uvutano wa dini ya ulimwengu katika mahali pengi?
12 Mambo yanayotukia katika upande wa dini ni yenye kupendeza sana vile vile kwa wanafunzi wa Neno la Mungu. Wengi wanaacha ukasisi na upadre, makanisa yanafungwa. Lakini kinachoonyesha ishara ya uharibifu wa dini ya ulimwengu si kufungwa kwa makanisa, kupungukiwa kwa washiriki wa kanisa mahali pengi, na kujiuzulu kwa makasisi tu. Kuna zaidi.
13. Ni nini kilichoongoza kwenye kuharibiwa kwa Yerusalemu na taratibu yake ya kidini katika mwaka wa 70 C.E.?
13 Angalia hili: Ni jambo gani zaidi lililoleta hasira ya Mungu ikitokeza uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 C.E.? Kulikuwa kulikataa kwao Neno la Mungu, ndiko kulikoongoza kwenye kufanya namna zote za uchafu. Vile vile, walimpiga teke Mwana wa Mungu wakamkataa kumkubali kama Masihi na pahali pake wakachagua kumtumaini Kaisari. (Mt. 15:1-9; Yohana 19:14-16) Yerusalemu ulistahili sana kupata mwisho. Je! mapadre leo ni afadhali? Wapi, wao, vile vile, wanafanana na viongozi hao wachafu wa kidini wa Yerusalemu wa kale.
14. Kukataa kwa makasisi Biblia kama Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake kumevutaje maoni yao juu ya adili?
14 Wao vile vile wamelikataa Neno la Mungu. Mara nyingine wamezitaja sehemu za Neno la Mungu kama “hadithi za uongo.” Lakini si hayo tu. Ebu zisikilize chache kati ya makala ambazo zimetokea katika magazeti. Kutoka Australia: “Kasisi Asihi Kanisa Liwabariki Wafiraji.” Kutoka mji wa New York: “Je! Ufiraji ni Mbaya Sana? Makasisi wa Episcopal Wasema Sivyo.” Kutoka Sweden: “Fanyeni Sheria Juu ya Wanaume na Wanawake iwe Nyepesi, Makasisi Wanasema.” Kutoka London: “Askofu Ataka Mambo ya Wanaume na Wanawake Yafanywe Halali kwa Umri wa 14.” Hivi ndivyo inavyotukia wakati watu wanapoliacha Neno la Mungu.
15. Ni katika njia gani maskasisi wa Kristendomu wameonyesha kuukataa kwao ufalme wa Mungu wa Kimasihi?
15 Kuukataa kwao ufalme wa Kimasihi wa Mungu mikononi mwa Mwanawe vile vile ni jambo lenye kujulikana sana. Kama Mafarisayo, mapadre wa Kristendomu wamezitumaini serikali za wanadamu. Wanakuwa tayari kuomba wakati marais na wafalme wanapotawazwa. Makasisi wa vitani wanayabariki majeshi yanapokwenda vitani. Na wana nia na moyo wa kuelekeza kwenye tengenezo la Umoja wa Mataifa kama ndiyo njia ambayo kwa hiyo wanadamu watapatia amani na usalama ambao ufalme wa Kimasihi wa Mungu peke yake unaweza kuleta.
16. Basi, pahali pa kupungua kwa hudhurio la kanisani, ni mambo gani yanayohakikisha kwamba uharibifu wa Kristendomu ni karibu?
16 Huu ni mfano mdogo tu wa dhambi ambazo dini za Kristendomu zimefanya. Zimeleta kufuru kubwa zaidi juu ya majina ya Mungu na Kristo, nazo zimejaribu kuiondoa ibada ya kweli ya Yehova katika dunia. Ni mambo haya ndiyo yanayohakikisha kwamba uharibifu wa Kristendomu ni karibu sana.
USHAHIDI ZAIDI WA KUKARIBIA KWA ILE “SIKU”
17-19. (a) Ni wapi pengine tunapopata ushahidi wa kukaribia kwa “siku ya Yehova”? (b) Ni matukio gani fulani kati ya watu wa Mungu yanayoonyesha kwamba kuja kwa taratibu mpya ya Mungu ni karibu sana?
17 Hakuna shaka kwamba hali za ulimwengu zinaonyesha kukaribia kwa “kuwapo kwa siku ya Yehova.” Lakini huo sio ushahidi peke yake. Tunaweza kupata ushahidi wa waziwazi sana wa kukaribia kwayo katika mambo yanayotukia katika kundi la kweli la Kikristo la Mungu—katika mambo ambayo Yehova anafanya kwa habari ya watu wake. Kutokana na matendo ya Mungu katika miaka ya karibuni taratibu mpya yenye haki inaonwa kuwa karibu sana hata tunaweza kuiona ikitukia mbele yetu.
18 Ebu angalia mambo haya ambayo yametukia: Kulingana na tengenezo, sasa makundi ya watu wa Yehova yamepatana zaidi sana na Maandiko, kwa kuwa na mpango wa wazee na watumishi wa huduma. Vile vile yamesaidiwa yaifahamu njozi ya Ezekieli juu ya makao yaliyo kama mji ya usimamizi wa ulimwenguni pote duniani, yaitwayo “[Yehova] yupo hapa.” Yanafahamu kwamba itakuwako baraza ya usimamizi itakayokuwa ikitumikia chini ya ufalme wa Mungu, baraza inayoitwa “mkuu” katika unabii wa Ezekieli. (Eze. 45:7; 48:35) Tena, yanafahamu sasa kwamba “mkutano mkubwa” wa wenye kuokoka “dhiki kubwa” utakuwa ndio msingi wa “dunia mpya,” jamii mpya ya watu wa kidunia itakayofanyizwa na utawala wa Kristo wa miaka elfu. Kufahamu unabii wa Zekaria kumeyaelimisha wapate kufahamu kwamba kila jambo linalofanywa na watu wa Mungu litakuwa katika utakatifu na kutukuzwa kwa enzi kuu ya Yehova, bila kitu kichafu au chenye kudhuru hata kidogo, ili Mungu asiwe na sababu tena ya kuwalaumu watu wake. (Zek. 14:20, 21) Pamoja na hayo, yamefundishwa kwa uangalifu juu ya namna inavyowapasa watu waishi sasa ikiwa wanataka kuokoka “dhiki kubwa.” Yote haya yanasaidia kuwatayarisha wenye mioyo minyofu kuishi katika taratibu mpya ya Mungu. Kuliko zamani tunaona vile vile watu wengi ajabu watakaokuwamo katika “mkutano mkubwa” wakija. Kweli kweli, kutengwa kwa “kondoo” na “mbuzi” kunaendelea kwa haraka sana. Leo watu wanaozitamani sana hali zenye haki wanaziitikia habari njema kwa upesi sana.—Marko 13:10; Mt. 25:31-46; Ufu. 7:9.
19 Kulingana na ushahidi wote huu, kwa kweli angekuwa mtu asiye na masikio na asiyeona ndiye asingefahamu kwamba sisi tunaishi katika kizazi ambacho Yesu alitabiri kwamba ndicho kingetangulia mara hiyo kuja kwa taratibu mpya yenye haki ya Mungu. Na kulingana na ushahidi wote tunaouona, tumeendelea sana katika kizazi hicho.—Mt. 24:34.
MWISHO WA DINI YA UONGO KUJA KWA GHAFULA
20, 21. (a) Ni hali gani juu ya dini ya ulimwengu ambayo huenda ikawafanya wengine waelekee ‘kuahirisha’ siku ya moto ya Yehova? (b) Lakini Ufunuo 17:16, 17 unasema uharibifu wa ‘Babeli Mkuu’ utatokeaje?
20 Walakini, wakati wa kutazama hali ya kidini, kuna wengine wanaoelekea kuiahirisha “siku” ya Yehova yenye moto. Huenda wakawaza katika njia hii: ‘Ni kweli kwamba tunaona dini ya kilimwengu ikikosa nguvu katika maeneo fulani, makanisa yanafungwa, makanisa hayaheshimiwi sana, na ishara nyingine za kushindwa. Ingawaje, hata katika maeneo haya, je! hatuoni mara nyingi kwamba makanisa yanaungana kwa nguvu na siasa? Tena mara nyingi yana sehemu nyingi za viwanda, hata nyumba kubwa ambazo yanatumia kwa mapato ya kibiashara. Tena, katika sehemu nyingine watu wengi wangali wakihudhuria makanisani. Ijapokuwa matendo machafu yaliyoko, watu wengi wangali wakiendelea kuwa washiriki wa kanisa. Basi, je! hatuwezi kusema kwamba nguvu hizi zinazoonyeshwa na makanisa ni ishara za kwamba kuwapo kwa siku ya Yehova yenye moto bado kuko mbali miaka mingi?’
21 Usidanganywe. Mwisho wa dini ya uongo hautakuja kwa kuiona inakwisha ivi hivi kwa sababu ya kukosa msaada. Pahali pake, utakuja katika njia ambayo Mungu, katika njozi yake aliyompa mtume Yohana katika Ufunuo 17:16, 17, alisema ungekuja. Hapo panasomwa hivi: “Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto. Maana Mungu ametia mioyoni mwao kufanya shauri lake, na kufanya shauri moja, na kumpa yule mnyama ufalme wao hata maneno ya Mungu yatimizwe.” Yehova Mungu mwenyewe atatoa amri juu ya uharibifu wa Babeli mwanzoni mwa “siku” yake, na uharibifu huo utakuja kwa ghafula sana.
22-24. (a) Wafuasi wa dini ya ulimwengu wanaitazamaje dini yao na mapadre wao? (b) Yeremia 25:34, 35 linafananishaje uharibifu wa ghafula utakaowapata mapadre na dini yao ya uongo?
22 Tusisahau kwamba dini ya ulimwengu ya Kibabeli inatazamwa na wanaoifuata kama kitu kitakatifu, kitu kizuri sana. Viongozi wake, zaidi mapadre wa Kristendomu, wameheshimiwa kama watu wa Mungu, watakatifu. Hata watu wasio na dini kati ya wanasiasa na wafanya biashara wanawataja kwa majina yenye heshima, kama Reverend, Right Reverend, Father, Holy Father na kwa maneno mengine ya majisifu mno. Ndiyo, dini ya kilimwengu imewaletea watu wengine mambo wanayotamani. Wengine inawapa vyeo; wengine, uwezo wa kisiasa; wengine inawaletea mapato ya fedha. Watu wengine kati ya wale wanaokwenda kanisani wanaona kwamba, ili wamwabudu Mungu, inawapasa wahudhurie au wawe upande wa kanisa, kwa sababu Kristendomu inajidai kumwabudu Mungu, kwa sababu inajidai kuwakilisha Biblia na kuwa ndiyo makao ya kweli.
23 Lakini andiko la Yeremia 25:34, 35 linasema nini juu ya hili? Juu ya jambo litakalowapata viongozi wa Kristendomu sawa kama lilivyosema juu ya jambo lililotazamiwa kuwapata viongozi wa Kiyahudi upesi Yerusalemu ulipokwisha kuharibiwa katika mwaka wa 607 B.C.E., linasema: “Pigeni yowe, enyi wachungaji, na kulia; na kugaagaa katika majivu, enyi mlio hodari katika kundi; maana siku za kuuawa kwenu zimetimia kabisa, nami nitawavunja vipande vipande, nanyi mtaanguka kama chombo cha anasa.”
24 Hivyo mwisho wa dini za uongo za Kristendomu na mapadre wao hautokei kwa kupunguka polepole kwa washiriki wa kanisa. Pahali pake, kama vile chombo kizuri sana, “chombo cha anasa,” kinavyoanguka kwa ghafula kutoka mahali kinapowekwa, kwa mshangao wa wanaokitazama, vivyo ndivyo na mapadre na dini yao ya uongo watakavyopata uharibifu wa ghafula sana.
25. (a) Vivyo hivyo, upesi wa kuanguka kwa Babeli Mkuu unaonyeshwaje katika Ufunuo 18:10, 21? (b) Ufahamu wa uhakika huu wa Maandiko waweza kutulinda juu ya nini?
25 Tena, kwa habari ya upesi wa kuanguka kwa Babeli Mkuu, Ufunuo sura ya 18, mstari wa 10 unasema nini? “[Waombolezaji, kutia na watu wengi wa biashara] wakisimama mbali kwa hofu ya maumivu yake, wakisema, Ole, ole, mji ule ulio mkuu, Babeli, mji ule ulio na nguvu! kwa kuwa katika saa moja hukumu yako imekuja.” Halafu katika mstari wa 21, unaendelea hivi: “Na malaika mmoja mwenye nguvu akainua jiwe, kama jiwe kubwa la kusagia, akalitupa katika bahari, akisema, Kama hivi, kwa nguvu nyingi, utatupwa Babeli, mji ule mkuu, wala hautaonekana tena kabisa.” Kufahamu uhakika huu kwaweza kutulinda na maelekeo yo yote ya ‘kuiahirisha’ siku ya Yehova ati kwa sababu dini ya Kibabeli ingali ikitumia uvutano mkubwa katika maeneo fulani.
[Picha katika ukurasa wa 319]
Dini za uongo za Kristendomu na makasisi wao wataanguka kwa ghafula waharibiwe, kama vile chombo kizuri kinavyoanguka kwa ghafula kutoka mahali kinapowekwa