Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 1/15 kur. 10-16
  • Wakisema “Amani” Wakati Haipo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakisema “Amani” Wakati Haipo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JERAHA HALIJAPONYWA
  • Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Hukumu ya Yehova Dhidi ya Wafundishaji Bandia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • “Mchungaji” wa Kifalme wa Unabii wa Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Sababu Gani Jumuiya ya Wakristo Haitaokoka?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 1/15 kur. 10-16

Wakisema “Amani” Wakati Haipo

1. Jamii ya Yeremia ya leo inajipaa wapi kwa habari ya watangazaji wa “amani,” wakati haipo?

NABII Yeremia hakuwamo kati ya watu wa siku zake waliokuwa wakisema “Amani,” wakati haikuwako. Vivyo hivyo jamii ya Yeremia ya kisasa haimo kati ya wanenaji wa Jumuiya ya Wakristo wanaowaiga wanaume wale waliodumu katika kusema “Amani,” katika siku za Yeremia. Mwishowe ni nani watakaojionyesha kuwa wasema kweli, hao watangazaji wa “amani,” au ‘wale wenye kusema kuna msiba!’ kama wanavyoitwa.

2, 3. (a) Watu wanaona wanapaswa kutumainia nini kama chanzo cha amani iliyo imara, yenye kuendelea? (b) Ili kuonyesha kutojiweza kwa chanzo hicho cha amani, baadaye Yeremia aliambiwa aseme nini?

2 Ili mambo ya kilimwengu yawe na matokeo yenye amani wanadamu wanajiona wana lazima ya kuangalia juu kwa msaada kutoka kwa nguvu zipitazo za kibinadamu. Walakini si Mungu wa nabii wa zamani Yeremia wanayeangalia kuwa Chanzo cha amani ya kudumu, iliyo imara. Nguvu zisizo za kawaida wanazozitumainia zilete amani zitajionyesha kuwa miungu wa uongo, wasiojiweza kabisa! Akituonya sote juu ya kulipuliwa kwa ndoto zisizo na msingi za wafalme, wana wa wafalme, makuhani, manabii na watu wenye kuhangaika wakati miungu wao wa amani watakapowakatisha tamaa, nabii Yeremia aliyeongozwa kwa roho aliambiwa aseme hivi juu ya wakati huo:

3 “Wakati ule [kama ilivyotabiriwa katika Yeremia 7:32-34], asema [Yehova], [watu, yaani, Wababeli washindi] watatoa mifupa ya wafalme wa Yuda, na mifupa ya wakuu wake, na mifupa ya makuhani, na mifupa ya manabii, na mifupa ya wenyeji wa Yerusalemu, itoke makaburini mwao; nao wataitawanya mbele ya jua, na mwezi, na jeshi lote [la nyota] la mbinguni, walivyovipenda [kama vitu vya kuabudu], na kuvitumikia, na kuandamana navyo, na kuvitafuta, na kuviabudu; [mifupa hiyo] haitakusanywa pamoja tena, wala kuzikwa; itakuwa ni samadi juu ya uso wa nchi.”​—Yer. 8:1, 2.a

4. Kwa hiyo kunajisiwa kwa makaburi kunaonyesha nini wazi kwa waabudu wa miungu wa uongo, nacho ni nini wasichostahili kukipata?

4 Aha, ndivyo, viumbe vya kimbinguni vilivyokuwa vimeng’aa kuelekea chini kwa matazamio mazuri juu ya wenyeji wa Yerusalemu na nchi ya Yuda wakati huo vingetazama chini kwa kutojiweza wakati wa msiba huo wakati ambapo ulizo hili lingejibiwa, Ni nani Mungu wa ile kweli? Kunajisiwa kwa makaburi ya watu wenye sifa katika dini na siasa kungeonyesha namna wale wanaoabudu miungu wa uongo huku wakivunja Amri Kumi za Mungu wanavyochukiwa. Hata amani ile waliyolala nayo katika kifo ingeharibiwa. (Ayubu 3:13-19) Machoni pa Yehova, wenye kuabudu miungu wa uongo kwa bidii hawajipatii utakaso au utakatifu wenye kulinda, sana sana hivyo wanapodai kuwa katika uhusiano wa Kikristo na Mungu wa Biblia na bado wanavunja amri zake zilizosemwa waziwazi. (Kut. 20:1-6; 1 Yohana 5:21; 2 Kor. 6:16) Hawastahili kupata heshima inayopewa wafu!

5. Watesi wa Mashahidi wa Yehova watagunduaje kwamba dhihaka zao juu ya Yehova zinahusu miungu wao wenyewe?

5 Kwa hiyo siku ya mapambano itakuja kwa wale ambao wamewatesa mashahidi Wakristo wa Yehova, na kuwadhihaki kwa maneno haya yenye dharau, ‘Mungu wenu Yehova yu wapi? Na aje awaokoe sasa!’ (Zab. 22:7, 8) Katika “dhiki kuu” inayokaribia ambayo katika hiyo Jumuiya ya Wakristo itaangamia, watesi ambao waliipendeza kwa matendo yao wataona kama miungu wao wanaweza kuwasaidia. Ndipo watakapojifunza kwamba miungu wao hawataweza kuwaokoa kutokana na hukumu ya Mungu ambaye walimdhihaki.

6, 7. (a) Waliohamishwa Babeli wangependelea nini, na sababu gani? (b) Kujapokuwa kusihi kwa Yehova wapate kumrudia, itikio limekuwaje kama lile katika siku za Yeremia?

6 Katika siku za Yeremia kungekuwa na waokokaji wa uharibifu wa Yerusalemu. Namna gani juu yao? Wangehamishwa kwenye nchi ya Babeli. Huko, kwa habari yao, “kufa kutachaguliwa kuliko kuishi.” (Yer. 8:3) Ingawa Yehova aliwasihi Waisraeli wenye kuvunja agano warudi kwenye uhusiano wenye amani pamoja naye, walichukua ‘mwendo wenye kupendwa na wengi’ wa ulimwengu huu mpaka kufikia mwaka 607 K.W.K. Kwa hiyo hawakuweka msingi salama wa wakati ujao wenye amani chini ya baraka za Yehova. Vilevile katika nyakati za kisasa, Jumuiya ya Wakristo imechukua mwendo wenye kupendwa na wengi. Kwa makumi ya miaka sasa tangu mwaka 1919 W.K., jamii ya Yeremia ambayo washiriki wake ni mashahidi watiwa mafuta wa Yehova imejulisha njia ya kurudi kwenye uhusiano wenye amani na Mungu wa Biblia. Walakini washiriki walio wengi wa Jumuiya ya Wakristo wamekataa kusikiliza. Ni kama vile tu alivyosema Yeremia:

7 “Mbona, basi, watu hawa wa Yerusalemu wamegeuka waende nyuma, wasikome kugeuka hivyo? hushika udanganyifu sana, hukataa kurudi. . . . hapana mtu aliyetubia maovu yake, akisema, Nimefanya nini? Kila mtu hurudia mwendo Wake mwenyewe [wenye kupendwa na wengi].”​—Yer. 8:4-6.

8. Shida huko nyuma ilihusu kukosa gani kwa akili, kama vile ilivyo leo?

8 Shida ilikuwa nini huko nyuma katika siku za Yeremia wakati Yehova alipowajilia watu wake wa agano? Vilevile, shida ni nini leo na watu wa Jumuiya ya Wakristo? Ilikuwa ni na ingali ni kukosa kutumia nguvu zao za akili kama zile za ndege wenye kuhama zinazowafahamisha wakati wa masika. Ndege wa kutoka kaskazini waliokuwa wamekimbilia katika sehemu za kusini zenye joto wakati wa majira ya baridi ya sehemu za kaskazini kama yale ya Palestina hurudi mara moja kwenye sehemu zao zenye viota na za kuzalia kule kaskazini zaidi. “Bali,” asema Yehova kwa njia ya kutofautisha, “watu wangu hawazijui [hukumu] za [Yehova].” (Yer. 8:7) Ilikuwa vivyo hivyo katika siku za Yesu na mitume wake, kabla ya Warumi kuuharibu Yerusalemu katika mwaka 70 W.K. (Mt. 16:2-4; Luka 19:44) Imekuwa vivyo hivyo kwa Jumuiya ya Wakristo katika siku hizi za jamii ya Yeremia.

JERAHA HALIJAPONYWA

9, 10. (a) Ni nini msingi wa viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wa kudai kwamba ni wenye hekima na wenye kufahamiana na sheria? (b) Katika kukataa dai lao, ni maono gani ya kimbele anayotupa Yehova ya matokeo ya shughuli (matendo) yao?

9 Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanadai kuwa ni wenye hekima, msingi wake si kwa ajili ya kuwa na Biblia bali kwa sababu ya kuwa na mazoezi ya seminari. Wanasisitiza kwamba wanaifahamu sheria ya Mungu wa Biblia na wanafahamu namna ya kuifasiri na kuitumia. Walakini Mungu wa Biblia anafahamu vingine. Anatazamia wakati ujao ulio karibu, wakati matokeo yao ya kuyaongoza mambo ya Jumuiya ya Wakristo yatakapowaelekea kweli kweli. Akiwa na maono hayo ya kimbele Yehova anasema hivi:

10 “Mwasemaje, Sisi tuna akili, na torati ya [Yehova] tunayo pamoja nasi? Lakini, tazama [wakati wa kutokea kwa taabu ya mwisho], kalamu yenye uongo ya waandishi imeifanya kuwa uongo. Wenye hekima wametahayari, wamefadhaika na kushikwa; tazama, wamelikataa neno la [Yehova]; wana akili gani ndani yao? Basi, kwa hiyo [wakati wa kuzungukwa na majeshi ya adui] nitawapa watu wengine wake zao, na mashamba yao nitawapa wale watakaowamiliki; maana kila mmoja wao, tangu aliye mdogo hata aliye mkubwa, ni mtamanifu; tangu nabii hata kuhani, kila mmoja hutenda mambo ya udanganyifu.”​—Yer. 8:8-10.

11, 12. (a) ‘Kalamu ya waandishi’ wa Jumuiya ya Wakristo ‘imefanyaje kazi katika uongo mtupu’? (b) Kulingana na Yeremia 8:9, sababu ya kalamu ya waandishi wa Jumuiya ya Wakristo kuandika mambo ya uongo ni nini?

11 Kwa kuandika mambo yanayotofautiana na yale ambayo Yehova ametabiri, ‘kalamu ya waandishi’ wa Jumuiya ya Wakristo ya kisasa karibuni itaonekana ilikuwa kalamu ya “uongo.” Haijaandika kweli. Kama matokeo, katika huu “wakati wa mwisho,” wakati ambapo mengi sana yameandikwa juu ya Jumuiya ya Wakristo, “kalamu” hiyo ya kidini pasipo shaka ‘imefanya kazi katika uongo mtupu.’ (Dan. 12:9) Sababu gani hilo limekuwa hivyo?

12 “Tazama,” alisema Yehova katika Yeremia 8:9, “wamelikataa [watu wenye sifa ya kuwa na hekima] neno la [Yehova]; wana akili gani ndani yao?” Ee ndiyo, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo huenda wakataja kichwa cha andiko kutoka katika Biblia, walakini katika mahubiri yao yanayofuata wataachana na yale yanayosemwa na Biblia. Watafundisha mapokeo yaliyofanywa na wanadamu yanayolifanya Neno la Mungu lililoandikwa kutokuwa na thamani. Watazungumza juu ya siasa au badiliko la kijamii. Wanajionyesha kuwa ni “wenye hekima” ya kimungu, walakini wanaweka filosofia za Kigiriki na “hekima ya dunia hii” mbele ya yanayosemwa na Biblia juu ya nafsi ya kibinadamu, juu ya hali ya wafu, juu ya utu wa Mungu, na kadhalika. (1 Kor. 3:19) Hata hivyo, wanauendea mtego. Mwishowe ‘watashikwa’ na maongozi yao wenyewe yenye hekima ya kiulimwengu. Wanaaibishwa na kutiishwa chini ya matokeo yenye kuogopesha sana.

13. Ni nani wenye kuchukua daraka kubwa zaidi kwa sababu washiriki wa kanisa wamejipatia “mapato ya udhalimu,” tangu aliye wa chini kabisa mpaka aliye mkubwa zaidi? Na namna gani hivyo?

13 Viongozi wa kidini wamewatia moyo “kondoo” zao katika kufuatia mambo ya ulimwengu yenye ahadi ya kuleta sifa na thawabu za mambo ya kimwili. Wamewapendelea walio matajiri huku wakiwaumiza walio maskini. Wameamrisha kupewa malipo ya fedha kwa ajili ya utumishi wao wa kidini. Kwa kuweka mfano huo, wanalo daraka kubwa kwa uhakika wa kwamba washiriki wao wa kanisa, wa chini kabisa pamoja na wakubwa kabisa, huweka faida za kiroho mwisho na “mapato ya udhalimu” au “fedha ya aibu” kwanza. (1 Pe. 5:1, 2) Basi, namna inavyofaa, kwamba Yehova hazuii Wakristo hao wa kujidai wasipoteze ‘mapato yao ya udhalimu’ katika “dhiki kuu” inayokaribia juu ya Jumuiya ya Wakristo! Hivyo Neno la unabii la Yehova litatimizwa juu yao.

14. Viongozi wa kidini wameliponya jeraha la kiroho la Jumuiya ya Wakristo kwa kadiri gani?

14 Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wangali wanatumainiwa kama madaktari (waganga) wa kiroho. Walakini tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka 1918, je! wamefaulu katika kuponya jeraha la kiroho, “jeraha [Kiebrania: Sheber],” ambalo Jumuiya ya Wakristo imepata? Maandishi ya miaka 60 sasa tangu wakati huo yanatoa mambo ya hakika juu ya viongozi wa kidini. Yanaonyesha kwamba wameshindwa kuifikia sababu yenyewe hasa ya ‘kuugua kwake na sababu gani haitaokoka “dhiki kuu” bali itapata uharibifu chini ya hukumu kali ya Mungu. Wao huendelea kuziponya dalili zenyewe tu walakini hawaponyi sababu yenyewe hasa ya hali iliyohukumiwa maangamizi na Mungu ya Jumuiya ya Wakristo. Wameponya jeraha lake ki-nje-nje, katika ngozi, “kwa juu-juu tu,” kana kwamba ni jambo dogo kwa Yehova Mungu.

15. Viongozi wa kidini wanaonaje juu ya masuluhisho ya kidini ambayo wametumia, na wanawahakikisha kondoo zao kwa maneno gani?

15 Tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza Jumuiya ya Wakristo imepata washiriki wengi sana wa kanisa, walakini namna gani juu ya hali ya kiroho ya washiriki hawa na uhusiano wao na Yehova Mungu? Masuluhisho ya kidini ambayo viongozi wa kidini wametumia hayajafanya mambo kuwa afadhali, hayakuzuia uulimwengu mbaya sana usivamie (usiingilie) makanisa. Hatuhitaji kuwaeleza wasomaji wetu jambo hili kwa urefu. Viongozi wanatumainia masuluhisho waliyotumia. Kwa maneno yanayowafanya kondoo wao wanaougua wasijihadhari, “makuhani” [“mapadre”] na “manabii” hao wa kisasa wanaendelea kuhakikishia Jumuiya ya Wakristo kwa maneno haya: “Kuna amani! Kuna amani!” au, “Yote yako sawa, yote yako sawa.”​—Yer. 8:11; NW, An American Translation; tazama pia The New English Bible.

16. Viongozi wa kidini wanasemaje mambo yaliyo tofauti na yale yanayosemwa na jamii ya Yeremia?

16 Kwa njia hiyo viongozi hawa wa kidini wanatenda kwa udanganyifu. Wanawafanya kondoo wao wafikiri kwamba hamna jambo baya na Jumuiya ya Wakristo. Wanadai kwamba uhusiano wayo na Mungu ni mzuri, na hivyo hakuna dhiki inayotazamiwa kutoka kwake. Kwa hiyo, hawasikilizi matabiri yanayotolewa na jamii ya Yeremia juu ya uharibifu wa mapema wa Jumuiya ya Wakristo katika “dhiki kuu.”​—Yer. 6:14.

17. Sababu gani hakika hakuna amani kati ya Yehova na Jumuiya ya Wakristo?

17 Kwa njia hiyo hali hiyo yenye kuogopesha inafanywa kuwa jambo la uongo na wanenaji wa Jumuiya ya Wakristo katika kutoa kwao mahakikisho hayo ya amani, “wala hapana amani.” Hakuna uhusiano wenye amani kati ya Yehova na Jumuiya ya Wakristo. Dhambi zake hazifunikwi na damu ya Kristo yenye kupatanisha. Dhambi zake nyingi nyingi hazisameheki. Hivyo Mungu hana amani nayo. Uharibifu, si “amani” au fanaka ya kiroho, unaingojea, kwa sababu viongozi wake wa kidini na washiriki wake wa kanisa bila aibu ‘wametenda yanayomchukiza’ Yehova.​—Yer. 8:12.

18. Uharibifu utaipata Jumuiya ya Wakristo namna gani, nao uharibifu huo utaenea kadiri gani?

18 Viongozi hao wa kidini na kondoo zao wakiwa na maono hayo ya kutokujihadhari uharibifu utawangukia “ghafula,” ndiyo, kama kwamba ‘kwa dakika moja.’ (Yer. 4:20; 6:25, 26; NW) Tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka 1918 kukaguliwa kamili kwa Jumuiya ya Wakristo kumefanywa na Yehova, na upesi, katika wakati wake uliowekwa, lazima ataigeuzia fikira zake ipasavyo, kama vile tu alivyoufanyia Yerusalemu wa kale. Ndipo wanadini wake wenye kujitumaini watakapoanguka kwenye uharibifu. Yehova atafagilia mbali kila kitu; hakutakuwako cho chote cha kuokota kama masalio. Mali zo zote walizoruhusiwa kupata na Yehova ‘zitawapotea’ na kuangukia mikononi mwa adui.​—Yer. 8:12, 13.

19. (a) Yesu aliwaambia wanafunzi wake wafanye nini wakati uharibifu wa mapema wa Yerusalemu ungeonyeshwa kwa ishara? (b) Wale waliokuwa katika nchi isiyo na kinga katika siku za Yeremia walifanya nini, kwa kukatisha tamaa matumaini yao?

19 Huko nyuma katika mwaka 33 W.K., Kristo alipotabiri uharibifu ambao ungekuja juu ya Yerusalemu katika mwaka 70 W.K., aliwaambia Wayahudi hao wafanye nini? Watoke Yerusalemu na jimbo lote la Uyahudi wakati uharibifu uliokuwa unakaribia ungeonyeshwa kwa ishara. Mtu aliyekuwa kondeni au katika sehemu za mashambani hakupaswa kwenda Yerusalemu walakini mara moja alipaswa kuondoka katika Uyahudi wote, ili apate usalama na kuokoka. (Mt. 24:15-18; Luka 21:20, 21) Walakini katika siku za Yeremia, wakati wa kukaribia kwa waharabu wa Kibabeli, watu hao waliona ni afadhali kutoka katika nchi isiyo na kinga na kukimbilia Yerusalemu na miji ‘ mingine yenye ngome. Humo, katika hizo ambazo zingeweza kuwa ngome wakati wa mazingiwa, walipendelea kunyamaa katika kifo, iwapo ingekuwa lazima. Walakini msaada kutoka kwa Yehova, Mungu wa hekalu lao, haukupatikana. Mahali pake, aliwaacha wanywe kinywaji kichungu, “maji yenye uchungu” yenye kuleta kifo. Kwa sababu ya mahakikisho ya “manabii” wao wa uongo, kulikuwako ‘kutazamia amani,’ walakini ikawaje? “Lakini hayakuja mema yo yote; tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!” Sauti au habari za majeshi yenye kushambulia ya uharibifu zilikuwako katika masikio yao.​—Yer. 8:14-16.

20. Kulingana na Yeremia 8:17, ni nani aliyetuma majeshi hayo yenye kuleta kifo, nao unabii huu ulitimizwaje?

20 Katika siku za Yeremia Yehova Ndiye aliyetuma mawakili wake wa kuleta uharibifu juu ya Waisraeli wenye kuvunja agano. Walikuwa wamefanya mbele zake mambo yenye kumchukiza, wakilichafua hekalu lake na nchi yake. “Maana, tazama, nitatuma nyoka, naam, fira, kati yenu, wasioweza kutumbuizwa kwa uganga; nao watawauma, asema [Yehova].” (Yer. 8:17) Wakati huo hakukuwa Musa katika Israeli wa kuinua nyoka wa shaba juu ya mti kusudi Waisraeli waponywe kutokana na kuumwa na nyoka kwa kuitazama tu nyoka wa shaba katika imani. (Hes. 21:4-9; Yohana 3:14, 15) Waharabu Wababeli wenye kuleta ukiwa hawakuwa wakicheza; kule nyuma katika mwaka 609 K.W.K. hakuna kitu chenye kufanywa na Waisraeli hao wenye kuzingirwa kingeweza kutenda kama hirizi kuwaachisha hawa wajibu wao waliopewa na Mungu. “Miji yenye maboma,” ambayo katika hiyo Waisraeli walikuwa wamekimbilia, isingeweza kuwakinga kutokana na hukumu ya Yehova.

21. Katika Yeremia 8:18, 19, Yehova alionyeshaje kwamba hakupendezwa moyoni mwake kuleta msiba wa taifa zima?

21 Yehova hakufurahia moyoni mwake kuleta msiba huu wa taifa zima. Kwa hiyo alitoa onyo la wakati wake, akitabiri kuachwa bila wakaaji kwa nchi ya Yuda na kuhamishwa kwa wengi wa waokokaji kwenye Babeli iliyo mbali. Huko wahamishwa hao wenye taabu, wakistaajabia ‘kazi ya ajabu ya Yehova,’ wangemlilia awasaidie. Kwa hiyo alisema hivi: “Sauti ya kilio cha binti ya watu wangu, itokayo katika nchi [Babeli] iliyo mbali sana; Je! [Yehova] hayumo Sayuni? mfalme wake hayumo ndani yake?”​—Yer. 8:18, 19.

22. Sababu gani kazi ya Mungu ilionekana kuwa ya ajabu naye Yehova alisema sababu yake ilikuwa nini?

22 Wahamishwa hao Wayahudi wasingeweza kujifanya wafikiri kwamba Yehova angeacha Yerusalemu (Sayuni) ukiwa umeshushwa sana hivyo pasipo hekalu lililo nyumba ya Mungu wao na pasipo kiti cha enzi cha kifalme ambacho mzao wa Mfalme Daudi aliketi akiwa mfalme mtiwa mafuta wa Yehova. Lo! namna lilivyokuwa suto kwa jina Lake, kwa wakati huo! Kama vile hilo lilivyokuwa jambo la ajabu huko nyuma, uharibifu wa Jumuiya ya Wakristo unaokaribia utakuwa jambo la ajabu hata zaidi. Sababu ya kuja kwake inaonyeshwa na jibu la Yehova kwa kilio cha wahamishwa Wayahudi cha msaada: “Mbona wamenikasirisha kwa sanamu zao walizochonga, na kwa ubatili wa [miungu wao wa] kigeni?”​—Yer. 8:19b; Isa. 28:21.

23. Kulingana na Yeremia 8:20, ni jambo gani litatokea kwa matumaini ya wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo ya wokovu kupitia kwa kazi zao?

23 Matumaini ya wokovu ya Jumuiya ya Wakristo si ya kimaandiko; ni lazima waangamie! Wakati u karibu kuja wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo watakaposema; “Mavuno yamepita, wakati wa hari [wa kutokeza njia ya wokovu] umekwisha, wala sisi hatukuokoka.” (Yer. 8:20) Na tusiwe kati ya wale wanaosema jambo hili!

24. Huzuni juu ya ujumbe huu wetu wa msiba ilionyeshwa kwa usemi gani wa mshangao katika Yeremia 8:21, 22?

24 Watu ambao leo wanafuata Jumuiya ya Wakristo huenda wakajisikia kuhuzunishwa na ujumbe huo wetu. Zamani sana Yeremia alijisikia kuhuzunishwa na taraja la kuharibiwa kwa hekalu ambalo alitumikia kama kuhani na kwa sababu taifa ambalo yeye alikuwa mshiriki lingechinjwa na kutawanywa. Akiwa amekata tamaa juu ya kupata nafuu kiroho kwa watu wake na katika unyofu wote wa moyoni na pasipo maono ya kindani yenye uchungu, yeye angeweza kusema hivi kwa mshangao: “Kwa sababu ya maumivu [shéber, au kuvunjwa-vunjwa] ya binti ya watu wangu nimeumia [shabár] mimi; [nimehuzunika]; ushangao umenishika. Je! hapana zeri katika Gileadi? huko hakuna tabibu? mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?​—Yer. 8:21, 22.

25. Je! Jumuiya ya Wakristo ina suluhisho lo lote la kuponya leo, nao wapenda amani ya kuendelea wanapaswa kufanya nini sasa?

25 Hali ya kiroho iliyovunjwa-vunjwa ya Yerusalemu wa kale na nchi ya Yuda ilikuwa isiyoweza kuponyeka. Kwa hiyo kweli kweli walivunjwa-vunjwa na Wababeli katika mwaka 607 K.W.K. Leo, katika tarehe hii iliyoendelea sana, hamna ‘zeri ya Gileadi,’ inayoweza kuponya Jumuiya ya Wakristo. Kwa hiyo sasa, kabla ya uharibifu kuipata “ghafula,” ebu na wapenda kweli na amani ya kudumu pamoja na Yehova Mungu waikimbie.

​—Kutoka The Watchtower Ago. 1, 1979.

(Mfululizo huu juu ya unabii wa Yeremia utaendelezwa).

[Maelezo ya Chini]

a Angalia Baruki 2:24, 25, Douay Version

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki