Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 6/1 kur. 7-12
  • Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JUMUIYA YA WAKRISTO ITAANGAMIA
  • ‘KUJENGA NA KUPANDA’
  • KUHUKUMIWA KWA MATAIFA
  • “Watapigana Nawe”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • “Mchungaji” wa Kifalme wa Unabii wa Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Wakisema “Amani” Wakati Haipo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kitabu Cha Biblia Namba 26—Yeremia
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 6/1 kur. 7-12

Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova

“[Yehova] asema hivi, . . . sema . . . maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja.”​—⁠Yer. 26:2.

1. Yeremia alikuwa nabii wa namna gani, naye Yehova alimtiaje nguvu?

YEREMIA alikuwa nabii mwaminifu. Kwa sababu alikuwa mwenye bidii akiyatangaza “maneno” ya Yehova, taifa zima lilimtakia mabaya. Lakini alipomlilia Yehova amsaidie, Mungu wake alimfariji, akisema: “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya.” Usemi huo wa Yehova ulimpa nguvu za kuvumilia.​—⁠Yer. 15:10, 15, 20.

2. Yeremia alionyesha sifa gani za kupendeza? (Ebr. 13:6)

2 Yeremia alitii kwa kuyatangaza “maneno yote” ya ujumbe mkali wa hukumu ambao Yehova alimpa aunene. ‘Hakuzuia hata neno moja.’ (Yer. 26:2) Hakupunguza maneno yo yote alipokuwa akiufunua wazi uovu wa taifa la Kiyahudi, wa watawala wake na watu wake. Yeremia alihitaji uhodari ili aweze kufanya hivyo, tena alihitaji kuamini kabisa kwamba Yehova angeweza kumsaidia maana alikuwa nabii Wake.

3. Ni nani wanaotumikia kama “Yeremia” wa kisasa,nao wameingizwa katika agano gani?

3 Vivyo hivyo, katika nyakati za kisasa, Yehova ameyainua mabaki machache ya mashahidi wake waliotiwa mafuta watumikie wakiwa jamii ya Yeremia, hasa katika makao ya Jumuiya ya Wakristo yenye unafiki (udanganyifu). Wao pia ‘wanapaswa kusema maneno yote ambayo Yehova anaamuru.’ Maneno hayo ni yenye ujumbe wa kulipa moyo na tumaini kundi la kweli la Kikristo, wala si wa kuonyesha maangamizi tu ya Jumuiya ya Wakristo na mataifa mengine yote. Waisraeli hao wa kiroho wameingizwa katika “agano jipya” lililoelezwa na nabii kwa maneno yenye shauku (bidii) yaliyo katika Yeremia 31:33, 34:

“Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema [Yehova]; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema [Yehova]; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.”

4. Watu wa Mungu wanatazamia tumaini gani kama Ibrahimu? (Ebr. 13:12-15)

4 Yehova anajengea hao “wazao wa Israeli” mji wa mbinguni ambao hautang’olewa, wala hautabomolewa tena mpaka umilele. (Linganisha Waebrania 9:13-15.) Tumaini hilo linatukumbusha jinsi Yehova alivyomtia nguvu Ibrahimu mwaminifu kwa kumpa tumaini la kupata “mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Ebr. 11:10) Na sasa tunaishi katika siku ambazo bibi-arusi wa Kristo, yaani, “mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya,” unakaribia kukamilika mbinguni, wakati, ambao ‘utashuka’ kwa njia ya mfano uletee wanadamu baraka za milele.​—⁠Ufu. 21:2-5, 9.

5. Inatupasa tujulishe wengine “maneno” gani kwa shauku? (b) Ni ujumbe gani wenye sehemu mbili ambao lazima jamii ya Yeremia iuhubiri? (Linganisha Isaya 61:1, 2.)

5 Mji huo ndio ufalme wa mbinguni ambako Yehova anayaelekeza mabaki ya kondoo zake akiyachunga kwa kumtumia Yesu Kristo. Kwa sasa wazee walio kati ya kondoo hao wanatumikia kama wachungaji wadogo wenye kuchunga makundi ya watu wake waliopo duniani kwa uaminifu. (Yer. 23:3, 4) Wao ni mabalozi wa ufalme wa “Chipukizi la haki,” yaani, Daudi Mkubwa, Yesu Kristo, ambaye unabii unasema hivi juu yake:

“Naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi. . . . Na jina lake atakaloitwa ni hili, [Yehova] ni haki yetu.” (Yer. 23:5, 6; linganisha Isaya 32:1, 2; 2 Wakorintho 5:20.)

Inatupasa tuwe wenye shauku (bidii) nyingi ya kutaka kujulisha wengine “maneno” ya Yehova juu ya ufalme huo wenye haki. Lakini Yehova anaiagiza jamii ya kisasa ya Yeremia itangaze pia ujumbe wa maangamizi!

JUMUIYA YA WAKRISTO ITAANGAMIA

6. “Maneno” ya Yeremia yanawafaaje viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo?

6 Viongozi wa dini wa Jumuiya (jamii) ya Wakristo wanadai kwamba wao ni Wakristo. Lakini je! mafundisho na matendo yao yanahakikisha dai lao? Au, wanaonekana kuwa sawa na viongozi wa kidini wa siku za Yeremia? Kwa habari yao, Yeremia alisema hivi:

“Hutega mtego, na kunasa watu. Kama tundu lijaavyo ndege, kadhalika nyumba zao zimejaa hila; kwa hiyo wamekuwa wakuu, wamepata mali.” (Yer. 5:26, 27)

Wamewatamani watu, wakawavuta kwa kujionyesha kijuujuu kwamba wao ni watawa au wakatumia upanga kuwalazimisha wageuke wafuate dini yao, kama ilivyokuwa katika siku zile ambazo mataifa yalikuwa yakihamia nchi mpya na kuanza kuitawala. Lakini msingi wa dini yao ni mafumbo ya kale ya Babeli, wala si Neno la Mungu. (Ufu. 17:5) Mungu wao ni “utatu” wenye kuvuruga akili za watu. Wameingiza katika watu wengi woga wa kuchomwa na “moto wa milele” kwa kuwafundisha uongo kwamba nafsi haifi, kisha wakajipatia pesa nyingi kwa kuombea wale wanaosemekana wanateseka katika ile purgatori ya hadithi tu. Wanauabudu msalaba, kama walivyofanya Wamisri muda mrefu kabla ya Kristo kutokea. Wanazipamba sanamu za watakatifu wao kwa kuzungusha duara ya mwanga wa jua katika vichwa vyazo na kuziwekea tasbihi (ushanga), kama zinavyofanya dini za Mashariki (upande wa Bara Hindi).

“Wamewanda [wamenenepa] sana, wang’aa; naam, wamepita kiasi kwa matendo maovu.”​—⁠Yer. 5:28.

7. Ni kwa njia gani watu wengi katika Jumuiya Wakristo wanafanana na waliokuwa katika Yerusalemu wa siku za Yeremia?

7 Wakati wa Yeremia, wingi wa watu walichagua kuendelea kuiunga mkono taratibu iliyokuwa imehukumiwa maangamizi. Waliupenda udanganyifu, upotovu na uasherati wake. Je! hivyo sivyo walivyo watu wengi leo katika Jumuiya ya Wakristo? Yehova anaonyesha hukumu yake:

“Je! nisiwapatilize kwa mambo hayo? asema [Yehova]; na nafsi yangu, je! nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii? Jambo la ajabu, la kuchukiza, limetokea katika nchi hii! Manabii wanatabiri uongo, na makuhani wanatawala kwa msaada wa hao; na watu wangu wanapenda mambo yawe hivyo.” (Yer. 5:29-31)

Waache viongozi wa dini waendelee kuyahubiri mambo ya uongo ya Kibabeli. Waache wawaunge sana mkono wanasiasa wapotovu. Waache wawaachilie watu wafanye uasherati ovyo ovyo tu, wawaachilie wanaume na wanawake walalane na wenzao, wacheze kamari na kufanya mazoea mengine yanayokatazwa na Neno la Mungu. Huenda wingi wa watu wakapendezwa sana na mambo hayo. Huenda watu wengi ‘wakapenda mambo yawe hivyo.’ Lakini Mungu anasema kwamba karibuni sana atawahukumu kwa sababu ya unafiki wote huo wa kidini.

8. Maangamizi ya Shilo ni unabii wa kitu gani? (ye 7:12)

8 Wakati wa waamuzi wa kwanza wa Israeli, hema na sanduku la Yehova lilikuwako Shilo. Lakini makuhani waliachilia sana mambo mabaya na uasherati mpaka Yehova ‘akawapatiliza’ kwa mambo hayo. Israeli walishindwa kabisa na Wafilisti, sanduku likachukuliwa halafu Eli kuhani mkuu akafa pamoja na wana wake waasherati. (1 Sam. 2:12-29; 4:2-18; 3:10-14) Kulingana na maneno ya Yehova, Yerusalemu wa wakati wa Yeremia ungeangamia kama vile Shilo ulivyoangamia:

“Na sasa, kwa sababu mmezifanya kazi hizi zote, asema [Yehova], nami nikasema nanyi, nikiamka mapema na kunena, lakini hamkusikia; nami nikawaita wala hamkuniitikia; basi, nitaitenda nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, mnayoitumainia, na mahali hapa nilipowapa ninyi na baba zenu, kama nilivyopatenda Shilo.” (Yer. 7:13, 14)

Inazifaa dini za Jumuiya ya Wakristo, zinazodai kwamba zina ushirika na Mungu kupitia kwa Kristo Yesu, ziyasikie maneno hayo.

9, 10. (a) “Kazi” za Jumuiya ya Wakristo zinatofautianaje na za Wakristo wa kweli? (b) Kama ilivyotabiriwa, viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo wanauonaje uharibifu wa tabia njema na jitihada za kuleta amani? (c) Amani ya kweli itapatikanaje?

9 “Kazi” za Jumuiya ya Wakristo zimekuwa ni pamoja na kuunga mkono mipango ya kibinadamu ya kuleta amani, ijapokuwa Yesu aliwafundisha Wakristo wa kweli wauombe ufalme wa Mungu maana ndio utakaotumiwa kuleta amani katika dunia hii. (Mt. 6:10) Viongozi wa Kikatoliki na Kiprotestanti wameushangilia Umoja wa Mataifa kuwa ndilo ‘tumaini la pekee la amani ya wanadamu.’ Wakati uo huo wanatafuta mapendeleo kutoka kwa wanasiasa kwa kuyabariki na kuyaunga mkono mataifa yaliyo wanachama wa Umoja wa Mataifa, yenye kutafuta silaha mbaya kwa kutumia dola bilioni 350 kila mwaka (shilingi milioni elfu 2,800 au Zaire milioni elfu 304). Maneno ya Yeremia yanawafaa sana viongozi wa kidini wa “Yerusalemu” wa kisasa, yaani, makao ya Jumuiya ya Wakristo:

“Tangu aliye mdogo hata aliye mkubwa miongoni mwao, kila mmoja ni mtamanifu; na, tangu nabii hata kuhani, kila mmoja hutenda mambo ya udanganyifu. Wameiponya jeraha ya watu wangu kwa juu juu tu, wakisema, Amani, Amani, wala hapana amani.”​—⁠Yer. 6:13, 14; angalia pia 8:11; 14:13-16; 23:17-20.

10 Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanaachilia tabia mbaya wakisema kwamba mambo ni sawasawa tu, na kumbe yanachukiza sana na kustahili kuadhibiwa na Mungu. Nao watapatwa na nini kwa sababu ya kusema-sema ‘Amani! Amani!? Mtume Paulo anajibu hivi: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 The. 5:3) Hiyo ni kwa sababu amani haitaletwa na mipango ya mataifa yanayojikaza yakijitafutia silaha za vita ya kutumia makombora ya atomu, bali italetwa na ufalme wa Mungu ukiisha haribu mataifa yenye kutokeza vita.​—⁠Dan. 2:44.

11. Linganisha hatia ya damu ya Jumuiya ya Wakristo na hatia ya Yerusalemu wenye kuasi imani.

11 Tangu “majira ya Mataifa” yalipomalizika mwaka 1914, mataifa hayo yamechinja watu milioni 69 kwa hasira katika vita viwili vya ulimwengu, na wengine wengi katika mapigano madogo. (Luka 21:24) Viongozi wa kidini wamekuwa wakienda mara nyingi kubariki majeshi yenye kupigana. Kwa kukubali wanadamu wachinjwe wamekuwa kama Yerusalemu wenye kuasi imani, uliolaumiwa na Yehova, akisema:

“Katika pindo za nguo zako imeonekana damu ya [nafsi] zao maskini wasio na hatia.”

“[Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Angalieni, nitaleta mabaya juu ya mahali hapa, ambayo mtu ye yote akisikia habari yake, masikio yake yatawaka. Kwa sababu wameniacha mimi . . . nao wamepajaza mahali hapa damu ya wasio na hatia.”

Yehova aliwaadhibu vikali wakaaji wa Yuda kwa sababu ya “kuwachoma moto wana wao” wawe dhabihu. Watu wa Jumuiya ya Wakristo watapata adhabu kali pia. ​—⁠Yer. 2:34; 19:3-5; angalia pia 7:31.

12. Ni sikukuu za namna gani zilizomo katika Jumuiya ya Wakristo zinazokatazwa na Neno la Mungu, nazo zinalinganaje na zilizokuwamo katika Yerusalemu wa kale?

12 Lakini, si hatia ya damu tu ambayo dini za uongo za Jumuiya ya Wakristo zimekuwa nayo. Bali, zimeyakubali mafundisho na desturi za Babeli ya kale, ambayo ndiyo iliyokuwa mwanzo wa ile milki kubwa ya ulimwengu ya dini ya uongo. Krismasi (Noel) yao, Easter (Pasaka) yao na sikukuu nyingine nyingi zilianzwa na dini zilizokuwako kabla ya Ukristo. Ndiyo, sikukuu hiyo ya Easter imepata jina lake kutokana na Astarte, mungu-mke wa Wafoenike wa uzazi na mahaba! Kwa habari ya sikukuu nyingine hizo zilizokuwako siku za Yeremia, Yehova alisema hivi:

“Watoto huokota kuni, na baba zao huwasha moto, na wanawake hukanda unga, ili kumfanyizia mikate malkia wa mbinguni, na kuwamiminia miungu mingine sadaka za kinywaji, wapate kunikasirisha mimi. . . . Kwa hiyo, Bwana [Yehova] asema hivi, Tazama, hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa juu ya mahali hapa.”​—⁠Yer. 7:18-20.

‘KUJENGA NA KUPANDA’

13. Sasa jamii ya Yeremia inafanya kazi gani yenye sehemu mbili?

13 Kwa miaka karibu 60 jamii ya kisasa ya Yeremia imekuwa ikiitangazia Jumuiya ya Wakristo hukumu zitakazoletwa na Mungu juu yake. Wakati wa kuletwa kwa hukumu hizo unakaribia. Basi hiyo inaonyesha kutakuwa na kazi ya ‘kung’oa, kubomoa, kuharibu na kuangamiza’ makosa ya dini ya uongo. Inaonyesha pia kwamba kutakuwa na kazi ya ‘kujenga na kupanda,’ kwa kujulisha watu wenye mioyo minyofu “habari njema” za kwamba ufalme wa Mungu ndio utakaotawala badala ya utawala mpotovu uliopo duniani leo. Kazi hiyo ni ya kusitawisha mioyoni mwao hali ya kumthamini Yehova, kuuthamini wema wake na nafasi ya kupata uzima wa milele katika hali za kiparadiso, ambazo zitaweza kuwako kwa sababu ya dhabihu ya Yesu Kristo.​—⁠ Ufu. 7:9-17.

14. Mfano ulio katika Yeremia sura ya 24 unatimizwaje?

14 Kulingana na Yeremia sura ya 24, Yehova alimwonyesha nabii huyo vikapu viwili vya tini, vikiwa vimewekwa mbele ya hekalu la Yehova. Kikapu kimoja kilikuwa na tini mbaya, kikifananisha wale wasiochukua hatua kisha wanapata hasara kwa sababu hawaziamini ahadi za Yehova. Tini nzuri zilikuwa “nzuri sana,” nazo ziliwafananisha mara ya kwanza Wayahudi ambao wangeonyesha imani kwa kutoka uhamishoni Babeli baada ya kukaa huko miaka 70, wakarudishe ibada ya Yehova Yerusalemu. Katika utimizo wa kisasa, wanawafananisha mabaki waaminifu ambao wamerudi kutoka utumwa wa Babeli Mkuu, hasa wa dini za Jumuiya ya Wakristo, tangu mwaka 1919. Kwa habari ya hao waliorudishwa, na wengine ambao wangejiunga nao baadaye, Yehova anasema yafuatayo kupitia kwa nabii wake:

“Kwa maana nitawatulizia macho yangu, wapate mema, nami nitawaingiza katika nchi hii tena; nami nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawapanda, wala sitawang’oa. Nami nitawapa moyo, wanijue ya kuwa mimi ni [Yehova]; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; kwa maana watanirudia moyo wao wote.” (Yer. 24:6, 7)

Hizo “tini nzuri” zinasitawisha urafiki mwingi sana na Mungu wazo, Yehova. Kwa kuwa zina hali ifaayo ya moyoni, zinamtumaini Yehova kabisa aongoze hatua zake.​—⁠Yer. 10:23, 24; 20:12, 13.

KUHUKUMIWA KWA MATAIFA

15. Ni nani kwa ujumla wanaotiwa ndani ya utimizo wa maneno ya Yeremia ya maangamizi?

15 Yeremia alikuwa nabii wa kweli. Alinena kwa jina la Yehova, akaelekeza watu kwenye ibada ya Yehova, kisha kila neno alilotamka kuhusu Yerusalemu, Yuda na mataifa yale mengine lilitimia. Vivyo hivyo, ni hakika kwamba utimizo mkubwa wa unabii wake utatukia leo. Tena kumbuka kwamba, katika utimizo wa kisasa maneno haya ya maangamizi ni juu ya mataifa yote ya dunia nzima, si mataifa ya Jumuiya ya Wakristo tu. Yehova alimpa Yeremia agizo hili:

“Pokea kikombe cha divai ya ghadhabu hii mkononi mwangu, ukawanyweshe mataifa yote, ambao nitakupeleka kwao; nao watakunywa, na kulewa-lewa, na kufanya wazimu, kwa sababu ya upanga nitakaoupeleka kati yao.”

Baada ya mataifa yote yanayopinga mapenzi ya Mungu yenye haki kuharibiwa, “mkuu wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi, atafungwa katika shimo kubwa. (Yohana 12:31; Ufu. 19:11-16, 19, 21; 20:1-3) Jambo hilo litawezesha kuwe na amani na furaha ya milele hapa duniani.​—⁠Ufu. 21:3-5.

16. (a) Kwa sababu gani haitupasi kuogopa? (h) Manabii wa Yehova wametuwekea mfano gani mwema?

16 Je! tuogope kwa sababu sasa hukumu hiyo ya mwisho ipo papa hapa mbele yetu? Je! tuogope mambo tunayoweza kutendwa na adui wakati tunapouhubiri ujumbe huo wa maangamizi? Yeremia hakuogopa. Alimwogopa Yehova peke yake. (Yer. 10:2-7) Alimtii Yehova na kusimama mahali ambapo angeweza kuonekana waziwazi katika malango ya nyumba ya Yehova, kisha akawaeleza watu machukizo yaliyokuwa yakitendwa kwa jina la Mungu. Kama vile Yehova alivyoendelea ‘kuamka mapema na kunena’ na watu kwa kuwatumia manabii wake hapo kwanza, ndivyo Yeremia nabii wake alivyoamkia kazi yake mapema. Alituwekea mfano mwema sana, unaoonyesha kwamba haitupasi kamwe kulegeza mikono yetu leo wala kulala na huku kazi ya Yehova inapaswa kufanywa. ​—⁠Yer. 7:1, 2, 13, 14; 25:3, 4.

17. Uharibifu utakaotoka kwa Yehova utakuwa mkubwa namna gani?

17 Wakati tunapotangaza ‘kubomolewa’ kwa mataifa na falme na kuchukuliwa kwa mahali pao na ufalme wa Mungu, tunatazamia kwa uhakika Yehova amalize ubishi wake na mataifa. Atachukua hatua kwa wakati wake! Hakuna mwovu ye yote atakayeponyoka. Waovu watamalizwa kabisa:

“Na waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”

Wakati uharibifu utakapokuwa ukivuma duniani pote, “wachungaji” wa mataifa na “walio hodari” katika makundi yao watapiga yowe na kugaa-gaa, ‘waanguke kama chombo cha anasa.’ Kutakuwa na mshangao mkuu kama ule unaokuwa katika jamaa wakati chombo cha bei nyingi sana kiangukapo na kuvunjika-vunjika. ‘Watanyamazishwa wasiwe hai kwa sababu ya hasira kali ya Yehova.’​—⁠Yer. 25:31-37.

18. (a) Watu wenye mioyo minyofu wanawezaje kupata ukombozi? (b) Tutaendelea kupata nguvu kwa sababu ya uhakikisho gani tuliopewa?

18 Linalofurahisha ni kwamba, watu wenye mioyo minyofu kutoka mataifa yote wanajiunga na jamii ya Yeremia wajifunzapo wema wa Yehova. Watakombolewa wakati hasira kali ya Mungu itakapopasuka, ili ‘kuyanywesha mataifa yote’ uharibifu mkali. (Yer. 25:17) Hukumu hiyo inakuja mbio-mbio! Baada ya muda mfupi huenda adui za Mungu wakapigana na jamii ya Yeremia na wenzi wao. Lakini sisi tutakuwa kama “ukuta wa boma la shaba” na kuendelea kuupinga mkazo ambao adui watatuletea wakitaka tuache kunena “maneno yote” tuliyoamriwa na Yehova. Sikuzote tunapata nguvu kutokana na ahadi yake hii: “Hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema [Yehova].”​—⁠Yer. 15:20.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki