“Mchungaji” wa Kifalme wa Unabii wa Biblia
1. “Wachungaji” wa kisiasa wa ulimwengu wamewawekaje watu, nalo jambo hili litatengenezwaje?
WACHUNGAJI” wa kisiasa wa taratibu hii ya mambo wanawatenganisha watu wenye mfano wa kondoo. Kila kikundi cha watu kimo katika zizi tofauti ya kitaifa. Hakuna zizi moja yenye kutia ndani wanadamu wote. Tengenezo la amani na usalama wa ulimwengu, Umoja wa Mataifa, limeshindwa kutoa zizi ya namna hiyo ya ulimwengu wote ingawa sasa linayo mataifa washiriki 151.a Halitimizi uhitaji wa watu wa zizi moja chini ya Mchungaji mmoja. Ni Muumba peke yake, ambaye “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote,” anayeweza kutokeza Mchungaji wa Kiserikali mwenye kuhitajiwa kwa ajili ya kukusanya watu wote kwenye zizi moja.—Matendo 17:26.
2, 3. (a) Sababu gani Yehova aliona ni vema kuwapindua wachungaji waliokuwa wazao wa Mfalme Daudi? (b) Sababu gani Yeremia 23:1, 2 linatamka ole juu ya wachungaji wa namna hiyo?
2 “Kupitia kwa watu wake mwenyewe wateule Israeli, Muumba aliuonyesha ulimwengu wote kwamba, chini ya taratibu iliyopo ya mambo, hakuna mwanadamu asiyekamilika awezaye kuleta wanadamu wote pamoja kuwa kundi moja na kuwatawala kama mchungaji wao mmoja. Ndivyo ilivyokuwa hata kwa habari ya nasaba (mfuatano) ya wafalme waliokuwa wazao wa Mfalme Daudi, ambaye aliuteka Yerusalemu na kuufanya mji mkuu katika mwaka 1070 K.W.K. Kama mawakili wa kidunia Wa Mungu wa Israeli waliketi juu ya kilichoitwa ‘kiti cha enzi cha Yehova.’ (1 Nya. 29:23; 2 Nya. 13:8) Kwa sababu ya kuharibika kwenye kuendelea kwa wachungaji hao wa kiserikali (isipokuwa wachache) Mungu aliona vema kuipindua nasaba hii baada ya miaka 463 ya kutawala.
3 “0le wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! asema [Yehova]. Kwa sababu hiyo [Yehova], Mungu wa Israeli, asema hivi, juu ya uwachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema [Yehova].”—Yer. 23:1, 2.
4. Mwendo wa Shalumi (Yehoahazi) na Yehoyakimu kama “wachungaji” ulikuwaje?
4 Baada ya kifo cha mfalme mwema Yosia katika mwaka 628 K.W.K., wana wake watatu na mjukuu wake mmoja walijionyesha kuwa wabaya katika matendo yao. Matokeo yake yalikuwa kutawanyika kwa raia zao. Kwa mfano, kulikuwa na Shalumi, au Yehoahazi, ambaye alikuwa wa kwanza kumrithi Yosia katika ‘kiti cha enzi cha Yehova.’ Baada ya kutawala robo moja ya mwaka, alihamishwa mpaka Misri. Akafia huko. (Yer. 22:10-12) Kwa habari ya ndugu yake mkubwa, Yehoyakimu, utawala wake wa miaka 11 ulikuwa wenye uonezi sana na umwagaji mwingi wa damu hata kwamba hakustahili jambo bora zaidi kuliko maiti yake kutupwa nje ya malango ya Yerusalemu na kuzikwa pamoja na “maziko ya punda.”—Yer. 22:13-19.
5. Mwendo wa Konia (Yehoyakimu) na Sedekia kama “wachungaji” ulikuwaje?
5 Yehoyakimu alirithiwa na mwanawe mchanga, Yehoyakini, vilevile mwenye kuitwa Yekonia au Konia. (Mt. 1:11, 12) Kwa sababu alikuwa mzao wa Mfalme Daudi naye aliketi juu ya ‘kiti cha enzi cha Yehova,’ huenda yeye angeheshimiwa kama pete ya muhuri yenye thamani kwenye mkono wa kuume wa Yehova. Hata hivyo kwa ajili ya uovu wake alistahili kung’olewa na kutupwa utumwani katika nchi ya Babeli. Baada ya kutawala miezi mitatu na siku 10 tu alilazimika kukubali kushindwa na mfalme wa Babeli ambaye wakati huo alikuwa akiuzingira Yerusalemu. Yehoyakini na zaidi ya Waisraeli 10,000 walipelekwa utumwani Babeli, ili wafie huko. Yeye hakumwacha mwana kusudi akalie kiti hicho cha enzi, walakini amu (ndugu ya baba) wake, Sedekia mwana wa Yosia, alifanywa kuwa mfalme kama kibaraka wa Mfalme Nebukadreza. (2 Fal. 24:5-17; Yer. 22:24-30) Sedekia alivunja kiapo chake alichokifanya katika jina la Yehova. Hivyo, wakati alipoelekeana na matokeo ya mwendo wake wa kuasi naye akatafuta habari kwa nabii Yeremia, ilimletea Sedekia ujumbe wa kuhukumiwa maangamizi peke yake.
6. “Ole” hiyo juu ya “wachungaji” hao ilipataje kuwa ole kwa raia zao, naye Yehova alisababisha kutawanywa kwao namna gani?
6 Yale yaliyowapata wale “wachungaji” wanne wa kifalme wa ufalme wa Yuda na wachungaji wadogo walio wana wa wafalme yalikuwa ni “ole,” hakika. Vilevile hii ilimaanisha kutawanywa kwa raia zao wenye mfano wa kondoo waliokwenda uhamishoni Misri na Babeli. Hii iliacha nchi ya Yuda ikiwa ukiwa. Kwa sababu ya uovu wao “wachungaji” hao ndio waliosababisha kutawanywa kwa “kondoo” hao. Mungu wa Israeli, Yehova, aweza kusemwa kwamba ndiye aliyewatawanya kwa maana ya kwamba alitokeza majeshi yenye kuangamiza tena yenye kuadibisha kwa kusudi la kuleta adhabu juu ya watu wake wasiotii.—Yer. 23:1, 2; 2 Nya. 36:9-21.
YULE AMBAYE JINA LAKE LITAITWA ‘YEHOVA NI HAKI YETU’
7, 8. (a) Ni nani awezaye kutokeza “mchungaji” mkuu zaidi kuliko wafalme hao wa mwisho wanne wa Yerusalemu, na sababu gani? (b) Katika kumwahidi “mchungaji” mkuu zaidi namna hiyo, Yehova alisema nini katika Yeremia 23:3-6?
7 Mchungaji aliye bora twampata katika Mungu wa Biblia, Yehova. Yeye aweza kutokeza mchungaji wa kiserikali aliye bora zaidi ya wale wafalme wanne wa mwisho wa Yerusalemu, ambao uovu wao ulitokeza kutawanywa kwa raia wenye mfano wa kondoo. Kwa sababu ya kukatisha tamaa ambako watawala wa kibinadamu wasiokamilika huwachia raia zao, Mchungaji wa kimbinguni Yehova ameahidi kutoa mchungaji wa kiserikali aliye mkuu namna hiyo. Kwa hiyo baada ya kutamka “ole” juu ya “wachungaji” wenye kukatisha tamaa wa ufalme wa Yuda, alimwongoza nabii wake Yeremia akasema hivi:
8 “Nami nitakusanya mabaki ya kundi langu, katika nchi zile zote nilizowafukuza, nami nitawaleta tena mazizini mwao; nao watazaa na kuongezeka. Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea mmoja wao, asema [Yehova]. Tazama siku zinakuja, asema [Yehova], nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki [tofauti na machipukizi ya kifalme ya Daudi yasiyo ya haki]. Naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu ya haki katika nchi. Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama; na jina lake atakaloitwa ni hili, [Yehova] ni haki yetu.”—Yer. 23:3-6.
9. Sababu gani uhakika wa kwamba jina la “mchungaji” huyo lingekuwa ‘Yehova Ni Haki Yetu’ usingemaanisha kwamba yeye ndiye Yehova mwenyewe?
9 “Naye ataitwa: ‘Bwana ni Mtukuzaji wetu,’ ” Hivyo ndivyo chapa ya mwaka 1978 ya tafsiri ya Chama cha Kiyahudi cha Wachapaji cha Amerika ilivyotafsiri Yeremia 23:6, hali tafsiri ya Moffatt yasema hivi, “bingwa wetu.” Hakuna mwanamume ye yote duniani aliyepata kuwa na jina hilo kwa halisi. Hata hivyo unabii huo unatimizwa katika Yesu Kristo. Kupewa kwake cheo cha jina hilo hakumaanishi kwamba Yesu ndiye Yehova Mungu mwenyewe. Mwisraeli yule aliyeitwa Yehozadaki, ambaye jina lake maana yake ni “Yehova Atangazwa kuwa Haki” au “Yehova Ni Mwenye Haki,” hakuwa Yehova mwenyewe. (1 Nya. 6:14, 15) Yeremia 33:16 latuambia kwamba hata Yerusalemu ungeitwa “Yehova ni Haki Yetu,” walakini je! hilo lamaanisha kwamba Yerusalemu ulikuwa Yehova mwenyewe? Sivyo! Jina la mfalme wa mwisho mwenye kutawala wa Yerusalemu lilikuwa Sedekia, nalo jina hilo maana yake ni “Haki ya Yah.” Yule mfalme ambaye jina lake angeitwa ‘Yehova Ni Haki Yetu,’ yaani, Yesu Kristo, anatofautiana sana na Mfalme Sedekia.
10, 11. (a) Ahadi ya Yeremia 23:5, 6 ilitimizwa juu ya watu gani? (b) Jina ‘Yehova Ni Haki Yetu’ lilishikamanishwa kwa kufaa na nani, na namna gani hivyo?
10 Unabii wa Yeremia 23:5, 6 haukutimizwa katika siku za Yesu juu ya Yuda na Israeli na Yerusalemu wa halisi. Sehemu hizo za Kiyahudi zilimkataa Yesu kuwa Masihi. Walipatwa na uharibifu na kutawanywa na Warumi katika mwaka 70 W.K. Kwa kweli unabii huu unatimizwa juu ya Waisraeli wa kiroho, wanafunzi watiwa mafuta wa Kristo.
11 Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ya mwaka 1914-1918 mabaki ya Israeli wa kiroho yalitawanywa na viongozi wa kidini na mataifa ya Jumuiya ya Wakristo ambayo wakati huo yalikuwa yakipigana katika vita ya ulimwengu. Walakini kuanzia mwaka 1919 na kuendelea Yehova alimtumia Yesu Kristo aliyetukuzwa kuyakusanya mabaki yaliyotawanywa pamoja kwenye umoja wa kiroho, ulimwenguni pote. Washiriki wa mabaki hawa waliorudishwa wenye kutubu wa Waisraeli wa kiroho walisafishwa na hivyo wakafanywa kuwa wenye kufaa kutangaza “habari njema hizi za ufalme” katika mataifa yote, katika “dunia yote inayokaliwa na watu.” (Mt. 24:9-14, NW) Katika njia hii, kupitia kwa fadhili za Yehova zisizostahilika kupitia kwa Kristo, walitangazwa kuwa wenye haki au walitukuzwa. Yehova alijionyesha kuwa Mtegemezaji wao, “bingwa” wao, nao wakawa mashahidi wake Wakristo. (Isa. 43:10) Maadamu kibali hii ingekuja kupitia kwa Mchungaji wa Kifalme ambaye wakati huo alikuwa ametawazwa, Yesu Kristo, jina ‘Yehova Ni Haki Yetu’ lilistahili kushikamanishwa naye.
12. Kuwafungua mabaki kutoka Babeli na kuwakalisha tena katika nchi ya Yuda kulifungulia njia kuzaliwa gani kwa maana?
12 Ili kuonyesha jambo hili kimbele, Yehova aliwatoa mabaki ya Kiisraeli “kutoka nchi ya kaskazini” na kuwarudisha katika nchi ya kwao katika mwaka 537 K.W.K. (Yer. 23:7, 8) Kuwaleta huku kutoka Babeli na kuwakalisha tena katika nchi ya Yuda iliyokaa ukiwa kwa muda mrefu kulitokeza njia kwa kuzaliwa kukubwa zaidi duniani kulikopata kutukia, katika Bethlehemu-Yuda. Kulikuwa kuzaliwa kwa Yesu Kristo kama mzao wa Mfalme Daudi.—Luka 2:1-38; 3:23-31.
13. (a) Yehova alimtokezea Daudi “Chipukizi la haki” ijapokuwa nini juu ya nasaba ya Daudi? (b) Yehova alitendeaje mabaki kwa kupatana na jina la chipukizi, ‘Yehova Ni Haki Yetu’?
13 Kwa njia hiyo Yehova alimtokezea Daudi “Chipukizi la haki,” ujapokuwa unabii wake wenye ole juu ya Mfalme Konia (au, Yekonia; au, Yehoyakini).b (Yer. 22:24 hadi 23:2; Mt. 1:11-16; 2 Fal. 25:27-30) Hili “Chipukizi la haki,” Yesu Kristo, alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kama dhabihu kwa ajili ya raia zake za kibinadamu za wakati ujao. Kwa kufanya hivi aliweka msingi kwa wafuasi wake waliojiweka wakf 144,000 ‘kutangazwa kuwa wenye haki’ wakiwa na tazamio la kuwa warithi washirika pamoja naye katika ufalme wake wa kimbinguni. (Rum. 8:14-17; 1 Kor. 1:30, 31) Tangu mwaka 1919 W.K., yajapokuwa mashtaka yanayofanywa na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo juu ya mabaki ya hawa warithi wa Ufalme 144,000, Yehova amerudisha mabaki hawa kwenye kibali na utumishi wake. Kwa njia hiyo Yehova amewafanya kuwa mabingwa, amewatukuza, au ‘kuwatangaza kuwa wenye haki,’ kupitia kwa Kristo. —Rum. 8:31-33; Yer. 23:6, Moffatt; JPS; NW.
14. Kati ya mabaki waliotiwa mafuta, Yehova ametokeza watumishi gani tangu kuzaliwa kwa Ufalme katika mwaka 1914?
14 Kati ya mabaki yaliyorudishwa ya Waisraeli wa kiroho Yehova ametokeza wazee au waangalizi waaminifu. Kwa kuwa ufalme wa Kimasihi ulizaliwa mbinguni mwishoni mwa Nyakati za Mataifa katika mwaka 1914, waangalizi hawa wanatumikia kama wachungaji wa kifalme duniani mpaka mabaki yote yamalize mwendo wao wa kidunia na kujiunga na “Mchungaji” wa Kifalme katika ufalme wake wa kimbinguni.—Yer. 23:3, 4; Isa. 32:1, 2.
NAMNA VIONGOZI WA KINDINI WA JUMUIYA YA WAKRISTO WALIVYOSHINDWA
15. Tofauti na hali ya mabaki watiwa mafuta, Jumuiya ya Wakristo inajipata katika hali gani sasa?
15 Chini ya Mfalme wa kimbinguni, anayeitwa jina lake ‘Yehova Ni Haki Yetu,’ mabaki yaliyorudishwa ya Waisraeli wa kiroho yanaishi katika paradiso ya kiroho. (Yer. 23:3-6) Paradiso ya kiroho ya namna hiyo yenye amani na usalama haipatikani leo katika Jumuiya ya Wakristo. Inajipata katika hali iliyochafuliwa na uzinzi na yenye njaa ya kiroho. Hali yake ni yenye kuvunja moyo nayo ni utangulizi wa matokeo yenye kuvunja moyo hata zaidi. Yatamfanya mtu asesetuke kama mlevi aliyezoea vileo.—Yer. 23:9, 10; Mt. 24:21, 22.
16, 17. Kwa kupatana na Yeremia 23:11-14, ni nani waliosababisha hali ya Jumuiya ya Wakristo ya leo?
16 Wanaosababisha hili ni viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo. Wamewakosea washiriki wao wa kanisa. Ni kama vile tu Yehova alivyosema juu ya manabii wa uongo na makuhani wa hekalu wa siku za Yeremia:
17 “Maana nabii, na kuhani, wote wawili wanakufuru; naam, katika nyumba [hekalu] yangu nimeuona uovu wao, asema [Yehova]. Kwa ajili ya hayo njia yao itakuwa kwao kama mahali pa kuteleza gizani; watatelemshwa na kuanguka hapo. . . . Katika manabii wa Yerusalemu nimeona neno linalochukiza sana; hufanya zinaa (uzinzi); huenenda katika maneno ya uongo, hutia nguvu mikono ya watendao maovu, hata ikawa hakuna mtu arejeaye na kuuacha uovu wake; wote pia wamekuwa kama Sodoma kwangu, na wenyeji wake [Yerusalemu] kama Gomora.”—Yer. 23:11-14.
18. Ni tangu wakati gani na ni katika njia gani viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakrlsto wamekuwa na hatua ya uzinzi wa kiroho?
18 Tangu Jumuiya ya Wakristo ilipoanzishwa katika siku za Konstantino Mkuu, Papa wa Milki ya Rumi, viongozi wa kidini wa Kikatoliki na, baadaye viongozi wa kidini Waprotestanti wamekuwa na hatia ya uzinzi wa kiroho. Namna gani hivyo? Kwa kuwa rafiki wa ulimwengu huu na kushiriki katika siasa zake na matendo yake ya kijeshi.—Yak. 4:4.
19. Viongozl wa kidini na washiriki wao wa kanisa wamechafuliwaje na uasherati wa halisi?
19 Viongozi wa kidini waliruhusu wazinzi na watu wa namna moja wenye kulalana kwa halisi waendelee kuwa katika vyeo vyao na kutumikia katika makanisa yao. Lisilo la kustaajabisha basi, ni viongozi wa kidini kuruhusu watu hao waasherati waendelee kuwa kati ya washiriki wao wenyewe wa kanisa walioandikishwa. Leo hali ya ufisadi ya Jumuiya ya Wakristo ni yenye sifa mbaya, ‘inachukiza,’ kwa kadiri kubwa kuliko katika Sodoma na Gomora. Kwa kufaa sana Jumuiya ya Wakristo itapatwa na msiba wa hiyo miji yenye ufisadi ya kale.
20. Sababu gani viongozi wa kidini watakunywa kinywaji cha mauti?
20 Wakiwa ndio wenye hatia zaidi kati ya watu wa Jumuiya ya Wakristo, viongozi wa kidini watakunywa kinywaji cha mauti: “Kwa kuwa kutoka kwa manabii hao wa Yerusalemu [wakifananisha Jumuiya ya Wakristo] kukufuru [kuasi imani] kumeingia katika nchi yote.”—Yer. 23:15.
21. Katika mwaka 1925 W.K., jamii ya Yeremia ilivutaje fikira za ulimwengu juu ya kukengeuka kwa viongozi wa kidini?
21 Mara moja na bila hofu jamii ya kisasa ya Yeremia ilivuta fikira za ulimwengu juu ya kukengeuka kwa viongozi wa kidini. Mwaka 1925 ulikuwa wa kutokeza kwa habari hii. Kwenye kusanyiko kuu la International Bible Students Association katika Indianapolis, Indiana, U.S.A katika Agosti 24-31, jambo kubwa lilikuwa kutolewa kwa azimio lenye kichwa “Ujumbe wa Tumaini.” Msimamizi wa Sosaiti alijulisha azimio hilo baada ya kutoa hotuba yenye kichwa “Mwito kwenye Utendaji” naye akaanza kulisoma. Kati ya mambo mengine, lilisema hivi:
. . . wanadini, Wakatoliki na Waprotestanti, wote wawili, ni wenye kutokeza sana kwa ajili ya majivuno yao, kwa kuwa wenye kiburi, wasiomheshimu Mungu na wasio na utawa. Kwa hiyo, ni wazi kwamba masuluhisho yanayotolewa na ye yote au wote wa sehemu hizi zilizotangulia kutajwa ni ya bure, yasiyofaa na yasiyo na uweza wa kutosheleza tamaa ya mwanadamu.
Ukatoliki unadai na kujitwalia yaliyo haki ya Mungu kabisa. Wenye kufuata dini ya Kisasa wanamkana Mungu, wanalikana Neno Lake na mpango Wake wa ukombozi, na kutaja nguvu isiyoonac kuwa suluhisho la hali iliyoharibika ya mwanadamu. Wenye Kuhifadhi mazoea ya dini, huku wakidai kuwa wanaiamini Biblia, kwa mwendo wa matendo yao wanaikana Biblia hiyo. Wanafundisha uongo na mafundisho yenye kumvunjia Mungu heshima, na pamoja na Wakatoliki na Wenye kufuata dini Kisasa wanashirikiana na mamlaka za kisiasa na za kibiashara za ulimwengu wakikufuru Mungu kwa kudai waweza kuusimamisha ufalme wa Mungu duniani. Hawa wote wameungana pamoja chini ya Shetani aliye bwana wao mwenye nguvu zipitazo za kibinadamu katika kumsukuma Mungu pembeni na kulivunjia heshima jina lake. . . .
. . . Akifahamu hili, na ya kwamba wakati wake ni mchache, Ibilisi anajaribu kuwashinda watu kwa gharika kubwa ya mafundisho ya uongo na yenye kudanganya na kugeuza akili zao kabisa kutoka kwa Yehova. Wakati umekwisha kufika kwa Mungu kujifanyia mwenyewe jina duniani na kwa watu kuifahamu kweli kuhusu mpango wa kimungu, ambao ndio njia pekee ya kuokoa ulimwengu.—Mafungu 5, 6, 9. Tazama The Watch Tower la Oktoba 15, 1925, kurasa 310, 311. Tazama pia Ufunuo 8:12; 16:8, 9.
22. (a) Ni nani wanaotumikia kwa ajili ya kusudi la Mungu la kujifanyia jina? (b) Viongozi wa kidini wameonyeshaje kutoheshimu jina la Mungu katika njia ile wanayotabiri?
22 Hiyo hotuba “Mwito kwenye Utendaji,” ambayo pamoja nayo azimio lililopo juu lilitolewa, ilisema hivi, katika fungu la 28: “Wakati umekwisha kufika kwa Yehova kujifanyia jina duniani. Kanisa lina sehemu ya kutimiza katika hili kwa kadiri ya kuwa mashahidi wa Bwana.” (Ukurasa 326 wa The Watch Tower la Novemba 1, 1925) Kwa hiyo, tangu mwanzo wa mwaka (1926) kufuatia azimio hilo na kuenenzwa kwalo ulimwenguni pote katika trakiti, jamii ya Yeremia ilifanya jitihada yenye kustahili kuangaliwa ya kuweka jina la Yehova mbele ya wanadamu wote. Walakini viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walijionyesha kuwa wasioheshimu jina la Mungu. Wakilihamisha jina la Mungu kutoka kwa kusudi lake liliosemwa la kuleta tufani ya msiba juu ya Jumuiya ya Wakristo, viongozi wa kidini waliendelea kuwaambia “wao wanaonidharau [yaani, Mungu], [Yehova] amesema, Mtakuwa na amani; nao humwambia kila mtu aendaye kwa ukaidi wa moyo wake, Hamtapatwa na ubaya wo wote.”—Yer. 23:17-20.d
23. (a) Je! Yehova ndiye aliyewatuma viongozi hao wa kidini, au ni nani aliyewatuma? (b) Kulingana na Yeremia 23:21, 22, ni jambo gani lingetukia ikiwa viongozi wa kidini wangesimama katika kundi la urafiki la Yehova?
23 Hata hivyo, ni nani aliyetuma viongozi hao wa kidini pamoja na ahadi zao za amani? Hawakusimama ‘katika kundi la urafiki la Yehova’ ili wajifunze ujumbe wake kwa usahihi. Yehova hakuwa amewatuma katika jina lake. Hakuzungumza nao ili kwamba watabiri yale yaliyokuwa ‘yametoka kinywani mwa Yehova.’ Madhehebu ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo yaliwatuma kutoka katika seminari zake za elimu ya dini. Ni jambo gani lingetukia iwapo viongozi wa kidini wangesimama katika ‘kundi la urafiki la Yehova’ au katika baraza yake na kushikamana na mafunuo yake? Yehova asema hivi: “Lakini kama wangalisimama katika baraza [kundi la urafiki] yangu, ndipo wangaliwasikizisha watu wangu maneno yangu, na kuwageuza waziache njia zao mbaya, na uovu wa matendo yao.”—Yer. 23:21, 22.
24. Ikiwa viongozi wa kidini wangesimama katika baraza ya Yehova, haingekuwaje kwa washiriki wa kanisa wa Jumuiya ya Wakristo na matendo yao?
24 Kama ingekuwa hivyo kusingekuwa na ukosefu wenye kutisha sana wa elimu ya Biblia uliopo leo kati ya waenda kanisani. Kama viongozi wa kidini wenyewe wangechukua uongozi na kushikamana na Neno la Mungu lililofunuliwa na kufundisha mamilioni ya washiriki wao wa kanisa wafanye vivyo hivyo, vita viwili vya Ulimwengu visingetukia, vita ambavyo vilianza ndani ya Jumuiya ya Wakristo! Yehova hakosi kuwaona viongozi wa kidini wenye kusababisha jambo hili. Si kwamba tu yeye amekuwa “Mungu aliye karibu” kusudi kwamba asione mambo yaliyo mbali sana.—Yer. 23:23, 24.
25. Kwa watu wote wanaosikiza, ni nini, kulingana na Yeremia 23:25-28, anachopaswa kufanya sasa mtu ye yote mwenye kitu cha kutoa?
25 Wakati umekwisha kufika kwa watu kuamua kama wataendelea kusikiliza zaidi “ndoto” za viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo au watasikiliza Neno la Yehova kama linavyotangazwa na jamii ya Yeremia. Vilevile wakati umekwisha kufika kwa wale wanaodai kuwa wahudumu wa Mungu kutenda kuhusiana na hoja inayotolewa katika Yeremia 23:25-28: “Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu.”
26. Kwa sababu ni lazima pawepo mtengano kati ya ndoto na Neno la Mungu, jamii ya Yeremia na “mkutano mkubwa” wameamua kufanya nini?
26 “Ndoto” zisizo na msingi, njozi za mioyo ya wanadamu tu zina sehemu gani na Neno la Yehova? Hakuna! Lazima pawepo mtengano kati ya mambo hayo mawili, kama vile kulivyo na mtengano kati ya nafaka na majani yake. Jamii ya Yeremia iliyo na Neno la Mungu ndani yake imeamua kulisema kwa uaminifu kwa wakati wote. Kwa ajili ya kumheshimu Yehova “mkutano mkubwa” wa wasikilizaji umeamua kufanya vivyo hivyo.
27. Ni wakati gani, na namna gani wakati huo, Neno la Mungu linakuwa kama nyundo?
27 Kwa miaka kama 60 sasa jamii ya Yeremia imelisema Neno la Yehova kwa uaminifu. Likiwa lenyewe Neno hilo halijayateketeza matengenezo ya Jumuiya ya Wakristo yawezayo kuteketea; wala halijaponda-ponda taratibu ya mambo iliyo kama mlima. Hata hivyo Neno la ki-mungu kama linavyotangazwa na jamii ya Yeremia halikushindwa. Wakati ambapo, katika wakati uliowekwa wa Yehova, katika “dhiki kubwa,” Neno hilo lililonenwa litakapotekelezwa naye, ndipo ulizo lake mwenyewe litakapojibiwa ndiyo: “Je! neno langu si kama moto? asema [Yehova]; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?” (Yer. 23:29) Kwa hiyo ebu na tudumishe imani katika Neno hilo.
28. Viongozi wa kidini ‘wanaibaje maneno ya Mungu, kila mmoja kutoka kwa mwenzake,’ na kwa hiyo ni nani anayewapinga?
28 Tofauti na jamii ya viongozi wa kidini, wale walio wa jamii ya Yeremia wametumwa na Yehova waseme katika jina lake. Hata hivyo, manabii wa viongozi wa kidini vilevile wanadai wanazungumza katika jina lake na, hivyo, wanasema kweli ya Biblia. Kwa njia hiyo viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo kwa hakika ‘wanaiba’ nguvu na matokeo ya ujumbe wenye msiba unaotangazwa na jamii ya Yeremia. Ni kweli, jamii ya Yeremia inaunga mkono ujumbe wake kwa kutaja maneno haya, ‘Hivi ndivyo anavyosema Yehova.’ Walakini viongozi wa kidini wanajaribu kuongeza uzito na sauti ya kweli kwa yale wanayohubiri kwa kutia maneno haya, ‘Ni Usemi! ’ Kwa kuonekana wanazungumza kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo huenda wakatumia andiko la Biblia kama sababu ya kuhubiri juu ya siasa au hata propaganda (maenezi) ya vita. Hata hivyo Yehova anawapinga manabii hao walio viongozi wa kidini ambao yeye hakuwatuma kutoka katika kundi lake la urafiki na ambao ‘wanaiba’ maneno kutoka katika Biblia yake kusudi wayatumie vibaya.—Yer. 23:30, 31, NW.
29. Yehova ataonyeshaje kwamba manabii hao walio viongozi wa kidini ni wa bandia?
29 Yehova ataonyeshaje kwamba manabii hao walio viongozi wa kidini ni wa bandia (wa kuigiza)? Kwa kutotimiza yale wanayotangaza kuwa ‘ni usemi! ’ au yale wanayodhania kuwa wanazungumza katika jina lake. Yeye hauungi mkono uongo wao. “Tazama, mimi [nawapinga] hao wanaotabiri ndoto za uongo, asema [Yehova], na kuzisema, na kuwakosesha watu wangu kwa uongo wao, na kwa majivuno yao ya upuzi; lakini mimi sikuwatuma, wala sikuwapa amri; wala hawatafaidia watu hawa hata kidogo, asema [Yehova].” (Yer. 23:32) Ni vibaya sana kwa watu hao!
30. Ni jambo gani tutakalolipa uzito unaopasa—mahakikisho ya viongozi wa kidini au Neno la Yehova?
30 Katika wakati huu ambapo Jumuiya ya Wakristo haimo katika amani na Mungu, na tusibembelezwe kwenye kusinzia au kulala kiroho na mahakikisho ya uongo ya viongozi wa kidini ya amani. Na tuchukue kwa uzito “mzigo,” au ujumbe wenye uzito, kutoka kwa Neno la Mungu.—Yer. 23:33.
’MZIGO WA YEHOVA’
31. Wakati wale wa Jumuiya ya Wakristo wanapotuomba tuwaeleze kwa unyofu ni nini ujumbe wenye uzito wa leo, tuna lazima ya kuwaambia nini?
31 Leo ujumbe wa Yehova kwa taratibu ya kisiasa, kidini, na ya kibiashara ni wenye uzito nao unawahukumia maangamizi ukionyesha msiba wenye kuleta uharibifu. Kwa sababu hiyo ni daraka kubwa kwetu kutangaza ujumbe wa Yehova wa huu “wakati wa mwisho.” Kwa hiyo tunapoyajibu maulizo ya watu juu ya kitakachoipata taratibu hii ya mambo, na tuhakikishe kusema kilicho “mzigo” wa Yehova kweli kweli. Wakati jamii ya watu wa kawaida au manabii au makasisi wa Jumuiya ya Wakristo watuulizapo tuwaambie ni jambo gani linaloonyeshwa na Neno la Yehova kuwa mzigo, tuna lazima ya kuwaambia kwamba watu wenyewe wa Jumuiya ya Wakristo ni “mzigo” kwake, ndiyo, ‘Loo! namna ulivyo mzigo! ’ Kwa hiyo atajiondolea “mzigo” huu kwa kuiacha Jumuiya ya Wakristo ipatwe na msiba.
32. Watu wa Jumuiya ya Wakristo wanapingaje yale ambayo jamii ya Yeremia inatangaza kuwa ‘mzigo wa Yehova,’ na kwa hiyo wanabadili nini?
32 Watu wasiomheshimu Yehova hawapendi kukubali jambo ambalo jamii ya Yeremia inatangaza kuwa ‘mzigo wa Yehova.’ Kwa hiyo hawapendi kulikumbuka kuwa jambo zito kweli kweli. Kwa njia ya maneno yenye upinzani, wanawafuata manabii na makasisi wao kwa kutoa yale wanayosisitiza kuwa ndio “mzigo” wenyewe wa Neno la Mungu. Walakini maneno yao yenye upinzani msingi wake si Maandiko Matakatifu. Ni kwa tafsiri yao wenyewe, na kwa hiyo ‘kwa kila mmoja linakuwa neno lake.’ Kwa wanadini hao wenye kuwa na maoni yao, jamii ya Yeremia inasema hivi: “Mmeyapotosha maneno ya Mungu aliye hai, ya [Yehova] wa majeshi, Mungu wetu.” (Yer. 23:33-36) Walakini je! wanaweza kubadili msiba ambao ‘mzigo wa Yehova’ unatuonya juu yake? Aha, Hasha!
33, 34. Jamii ya Yeremia inapaswa kuvuta fikira za wanadini wanaouita ujumbe wao kuwa ‘mzigo wa Yehova’ juu ya kuwapo kwa nani?
33 Tofauti na yale ambayo walio wa jamii ya Yeremia wametangaza tangu mwaka wa baada ya vita wa 1919, wanenaji wa Jumuiya ya Wakristo wanatoa ujumbe wao wa uongo, tena wenye kupotosha. Ili waufanye usikike na wengine kuwa wenye uzito, wanayataja yale wanayosema kuwa ‘Mzigo wa Yehova.’ Kwa wanadini hawa Yehova ameendelea kutuma jamii ya Yeremia iwaambie wasitaje mahubiri na matabiri yao kuwa ni ‘Mzigo wa Yehova.’ Kwa hiyo jamii ya Yeremia inapaswa kuwajibu nini wanadini hawa? Hivi:
34 “[Yehova] asema hivi, Kwa sababu mwasema neno hili, ‘Mzigo wa [Yehova]’ nami nimemtuma mtu [jamii ya Yeremia] kwenu kusema, Msiseme, ‘Mzigo wa [Yehova kwa hiyo nipo hapa!]’ ”—Yer. 23:38, 39.
35, 36. Kulingana na Yeremia 23:39, 40, jamii ya Yeremia inapaswa kutangaza uamuzi gani kama ilivyopewa na Yehova kwa wale wanaosema au kusikiza “mzigo” wa uongo?
35 Sawa! Yehova yupo hapa kama Hakimu wa manabii wa Jumuiya ya Wakristo. Yeye anatoa uamuzi gani kuhusiana na “manabii” wanaoutaja ujumbe wao kuwa ‘mzigo wa Yehova’ na kuhusiana na watu wale wanaosikiza “mzigo” wa uongo? Hakimu huyo anatuambia hivi:
36 “Nitawasahau ninyi kabisa, nami nitawatupilia mbali, pamoja na mji huu niliowapa ninyi na babu zenu, mtoke mbele za uso wangu; nami nitaleta juu yenu aibu ya milele, na fedheha ya daima, ambayo haitasahaulika.”—Yer. 23:39, 40.
37. (a) Yehova alitekelezaje uamuzi wake wa kisheria katika siku za Yeremia, na kwa matokeo gani? (b) Na wakati huo mwendo wa Yeremia ulikuwaje, nalo hili litakuwaje hivyo kuhusiana na jamii ya Yeremia?
37 Uamuzi huo uliotajwa wa Hakimu Yehova ulifikilizwa katika siku za Yeremia, wakati Wababeli walipouharibu Yerusalemu na hekalu lake najisi katika mwaka 607 K.W.K. Jambo hili lenye kuwasuta, na kuwavunjia heshima Waisraeli hao washupavu, tena wasioaminika lilithibitisha kwamba Yehova, ambaye walikuwa wamekosa kumheshimu, sasa mwishowe alikuwa amewadharau. Alikuwa amewaacha kwenye matokeo ya uovu wao. Jambo hili lilinyamazisha vinywa vya manabii wa uongo wenye kujitanguliza. Walakini kinywa cha Yeremia kiliendelea kutabiri. Yehova hakumwacha yeye. Kwa kuambatana na hili, Yehova hataiacha jamii ya Yeremia wakati karibuni atakapotekeleza uamuzi wake mzito juu ya viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo na makundi yake.—Yer. 39:11-40:4; Omb. 1:1-22.
’KUPUMBAZWA’—KWA FAIDA
38. Yehova alikuwa amempumbaza Yeremia kwa njia gani, na kwa matokeo gani?
38 Hivyo Yeremia alimaliza miaka 40 ya kusema yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru. Alitambua kwamba Yehova alikuwa amemshinda kwa nguvu. Yehova alikuwa amejionyesha kuwa mwenye nguvu zaidi kumliko. Neno lake lilikuwa na matokeo yenye nguvu yenye kumshawishi Yeremia; (Rotherham) Kwa ajili ya ukweli huu, Yeremia alikuwa amevumilia katika utumishi wa kimungu mpaka ulipomalizika. Kwa habari hii Yehova alikuwa ‘amempumbaza.’ Alikuwa amejionyesha kuwa mwenye nguvu zaidi ya udhaifu wa Yeremia. Kwa hiyo, Yeremia hakupata madhara kwa kupumbazwa.
39, 40. Hii inatukumbusha maneno gani ya Yeremia baada ya Pashuri kumfungua kutoka katika mikatale?
39 Hapa twakumbuka maneno ya Yeremia baada ya Pashuri, mkuu wa hekalu, kumfungua kutoka katika mikatale:
40 “Ee [Yehova], [umenipumbaza], nami [nimepumbazika.]; wewe una nguvu kuliko mimi [juu ya maelekeo yangu], ukanishinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha; mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki. Maana kila ninenapo napiga kelele; nalia, Dhuluma na uharibifu! kwa kuwa neno la [Yehova] limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake; basi, ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia. Maana nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. . . . Lakini [Yehova] yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahaulika kamwe.”—Yer. 20:7-11.
41. Kwa hiyo tutawezeshwaje kuendelea kusema juu ya Mchungaji wa Kifalme anayeitwa ‘Yehova Ni Haki Yetu’?
41 Kama vile “shujaa mwenye kutisha” Yehova atatutia nguvu katika udhaifu wetu. Kwa nguvu zake, tutaendelea kusema juu ya Mchungaji wake wa Kifalme, yeye aitwaye ‘Yehova Ni Haki Yetu.’—
Kutoka The Watchtower Sept. 1, 1979.
[Maelezo ya Chini]
a Kitabu kiitwacho Americana cha Kila Mwaka, uku. 117.
b Tazama kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, kilichochapwa katika mwaka 1973, ukurasa 62, fungu 40 na maneno ya pambizoni, Pia, kitabu Paradise Restored to Mankind—By Theocracy!, kilichochapwa katika mwaka 1972, ukurasa 119, fungu 31.
c “Nguvu isiyoona,” yaani, mageuzi kulingana na wazo la Darwin.
d Barua ya United Press ya Septemba 26, 1977, kutoka Vatican City ilisema hivi: “Papa alisema kwamba yale maono yake mengine ya moyoni anapokaribia miaka 80 yanahusu kudumu kwa Kanisa la Rumi Katoliki. ‘Kanisa hilo litadumu,’ akasema, ‘litadamu katikati ya tufani ya historia. Kanisa hili linadumu likiwa imara na lenye nguvu katika matukio ya ulimwengu ili kutoa injili yote na wokovu wa milele.’ ”
Tazama ukurasa 3-A wa gazeti The Galveston Daily News la Septemba 26, 1977, chini ya kichwa “Papa Paulo Atazamia Kifo Kinachokaribia. ‘