Kupata Furaha Katika Kulea Watoto
1, 2. (a) Mfalme Sulemani aliona nini alipokuwa akihukumu kati ya akina mama wawili, na n’nini kilichomsaidia ahukumu kwa haki? (b) Ujamaa unapasaje mambo ambayo mtu anafanya?
MNAMO utawala wa Mfalme Sulemani mwenye hekima yeye aliagizwa afanye hukumu kati ya wanawake wawili, waliokuwa wakiishi katika nyumba moja, ambao walikuwa wamezaa wana. Usiku mtoto mmoja alikufa naye mama yake kwa utulivu akamchukua aliye hai mahali pa huyu wake aliyekufa. Asubuhi aliye mama wa kweli alimshtaki mama mdanganyifu juu ya wivi alipogundua kwamba mtoto aliyekufa hakuwa wake, nayo kesi hii ikamfikia Sulemani. Kwa kuwa Sulemani hakuweza kuamua ukweli wa kisa hiki, aliagiza kwamba mtoto aliye hai akatwe vipande viwili vinavyolingana ili kila mdai apate sehemu yake. Habari inasema hivi: “Ndipo mwanamke yule, ambaye mtoto aliye hai ni wake, akamwambia mfalme, kwa maana moyoni mwake alimwonea mtoto wake huruma, akasema, Ee bwana wangu, mpe huyu mtoto aliye hai, wala usimwue kamwe. . . . Ndipo mfalme akajibu, akasema, Mpe huyu wa kwanza mtoto aliye hai, maana yeye ndiye mama yake.” (1 Fal. 3:26, 27) Sulemani aliufahamu upendo wa wazazi kwa watoto. Si kwamba tu yeye alikuwa amejifunza hivyo kutokana na maono, yeye mwenyewe akiwa baba, bali vile vile yeye aliyafahamu maoni ya Mungu juu ya mpango wa jamaa kama yalivyosemwa katika Maandiko.
2 Ukamatano wa karibu karibu wa jamaa ni baraka. Wakati Andrea wa Bethsaida alipomgundua Masihi, alimwendea nani kwanza na habari njema hizi? “Huyo akamwona kwanza Simoni, ndugu yake mwenyewe, akamwambia, Tumemwona Masihi (maana yake, Kristo).” (Yohana 1:41) Ujamaa unaleta kifungo kisichokanwa. Itikio la Andrea lilikuwa la asili.
3. Kwa sababu gani udugu wa Kikristo ni kifungo cha kuunganisha chenye nguvu hata zaidi?
3 Kunacho kifungo chenye kuunganisha hata zaidi, nacho hicho ndio udugu wa Kikristo. Katika Warumi 12:10 Biblia inasema hivi: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.” Katika 1 Petro 5:9 (NW) unatajwa “ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.” Katika Marko 10:29, 30 ujamaa wa kimwili unalinganishwa na ule ambao kweli inaleta, Yesu akisema hivi: “Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.” Ndiyo, Wakristo wamejifunza kwamba akina ndugu katika kweli wanacho kitu fulani ambacho hata ndugu za kimwili hawanacho.—Yohana 13:34, 35.
4. Kwa sababu gani jamaa za Kikristo zaweza kutazamia kuwa na umoja ambao jamaa nyingine hazina?
4 Lakini wakati ambapo jamaa yako inakuwa na ndugu za kimwili ambao vile vile wamo katika kweli ninyi mumo katika hali yenye pendeleo. Wazazi ambao ni watumishi wa Mungu walio wakf na waliobatizwa wanao upendo wa asili kwa watoto wao ambao Mungu aliutia katika wanadamu. Vile vile wanayo nafasi ya kufanyiza umoja katika jamaa ambao unaweza kuleta furaha na uradhi usiopatikana kwa njia nyingine. Wanaweza kuwasaidia watoto wao wawe watumishi waaminifu wa Mungu; si kwamba tu hii itaileta jamaa karibu karibu zaidi lakini vile vile ndio urithi bora wanaoweza kuupitisha kwa watoto wao. Na hali leo hilo si jambo jepesi kama ambavyo huenda likasikika kuwa.
KUZUIA MAGUMU
5, 6. (a) N’nini kitakachowasaidia wazazi wazuie magumu ambayo huenda yakahitaji kuangaliwa? (b) Njia za kupashana habari zawezaje kuwekwa wazi kati ya wazazi na watoto wao?
5 Katika kukuza jamaa, magumu yatatokea. Hakuna faida ya kuwazia kwamba hayatatokea, kwa maana yatatokea. Kwa hiyo weka macho yako na masikio wazi kwa dalili zo zote zake. Mtoto wako anapokujia akiwa na magumu madogo madogo, si hekima kumfukuza kwa majibu ya haraka haraka. Huo ndio wakati wa kuonyesha kupendezwa kwingi na yaliyomo katika akili ya mtoto na kumvuta aseme anayowaza kwa maulizo. Wazazi wengi wanasema kwamba wanapata ugumu katika kuwafanya watoto wao waseme, wawaambie yaliyomo akilini mwao. Je! huenda ikawa ni kwa sababu wazazi wenyewe walikatiza mazungumzo wakati uliopita ambapo watoto walitaka kuzungumza nao wakahitaji msaada? Ni upumbavu kama nini kukomesha mazungumzo na mtoto wako ati kwa sababu hujisikii katika hali ya kuzungumza wakati huo.
6 Mzazi anayetafuta mambo ya kuzungumza na watoto wake na kuonyesha nia ya kweli ya kuzungumza habari yo yote ile hataona njia za kupashana habari zikiharibika bali ataziona wazi sikuzote zikivuma na habari zinazowambia mambo anayohitaji kuyajua, na zinazoleta uchangamfu na ufahamu katika ukamatano wa jamaa. Mzazi aliye na nia ya kusikiliza kwa kawaida atakuwa nao watoto wenye nia ya kuzungumza. Lakini je! watoto watawaendea wazazi wakiwa na magumu makubwa ikiwa wazazi hawasikilizi magumu madogo madogo, wakisaidia kuyatatua kwa njia inayoonyesha fadhili na ufahamu? Je! sasa hivi wewe unaye rafiki unayetumaini na ambaye una imani katika yeye, ambaye waweza kumwendea ukiwa na ugumu mzito, ukijua kwamba yeye atatumia wakati akiyasikiliza yote uliyo nayo asikudharau kwa sababu tu unao ugumu? Ndivyo imempasa kila mtoto ajisikie juu ya wazazi wake. Je! watoto wako wanajisikia hivyo juu yako? Mithali 17:17 inasema hivi: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Inasikitisha wakati inapokuwa lazima mtoto atafute namna hiyo ya ukamatano nje ya jamaa.
7. Kusimamia nyumba kwa njia nzuri kwatia mambo gani ndani?
7 Mtume Paulo aliandika kwamba imempasa mwangalizi awe “mwenye kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu; (yaani, mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?).” (1 Tim. 3:4, 5) Hii haisemi kwamba, bila ya kujali ni kadiri gani ya watu ambao baba anaweka kwa mapendezi mengine, ni sawa tu maadamu anajitia ndani na kushughulika na mambo wakati watoto wake waingiapo taabani. Sivyo, imempasa aisimamie nyumba yake kwa njia nzuri, akichunguza kwa uangalifu, akizuia magumu, akitangulia kutazama mbele mambo yanayoweza kusitawi kati ya wale waliomo katika usimamizi wake. Onyo la kuzuia ni afadhali zaidi kuliko onyo la kuadhibisha. Baba anayechunguza katika kuzuia magumu ni mwenye hekima zaidi kuliko yeye anayeridhishwa na kuyatatua yanapositawi. Ni kweli kwamba mawakili wanajifanyia jina kwa kuteta mahakamani. Lakini baba za Kikristo wanajifanyia majina mema kwa kusimamia kwa njia inayoepuka magumu.
UONGOZI KWA ‘MJINGA’
8. Wazazi wanawezaje kusaidia watoto wao wawe na maoni yafaayo?
8 Watoto wamekuwa na maono machache tu maishani, lakini hakuna faida kwa wazazi kuzidi kuwakumbusha uhakika huo. Kwa upande mwingine, ikiwa mtoto anasaidiwa kweli aufahamu ubora mwingi ambao Maandiko yanauweka juu ya maono na namna ambavyo yeye mwenyewe amepaswa awe macho ajifunze kutokana na kila maono, basi mtoto ataelekea kuwa na nia ifaayo juu ya msaada ambao mzazi anatoa naye atafaidika sana kutokana na matukio mbalimbali yanayopasa maisha yake kwa kadiri miaka inavyozidi kupita. Kwa kweli, inatupasa sote tuwe tukijifunza kutokana na kila maono tuliyo nayo. Na ikiwa mtoto anafahamu kwamba wazazi wake wanajua kwamba kuna masomo ambayo wao wenyewe wanaweza kujifunza kutokana na hali mbalimbali, basi yeye hataelekea sana kuchukizwa na maono yake mwenyewe naye atauitikia zaidi utaratibu wa kujifunza.
9. Maandiko yanasemaje juu ya wale wanaokataa kujifunza kutokana na maono?
9 Maandiko yanasema nini juu ya maono? Yanawalaumu vikali wale wanaokataa kwa ushupavu kusikiliza na kujifunza kutokana na maono, yakisema hivi: “Enyi wajinga, hata lini mtapenda ujinga? na wenye dharau kupenda dharau yao, na wapumbavu kuchukia maarifa? Geukeni kwa ajili ya maonyo yangu.” (Mit. 1:22, 23) “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mit. 22:3.
10. Wajapokuwa vijana ni wajinga, ni nini njia nyingine za kuondoa hili?
10 Zipo njia ambazo kwazo wazazi wanaweza kusaidia kuondoa ujinga wa watoto. Wazazi wenye busara wanaweza kuwasaidia kwa fadhili walio wajinga juu ya mambo yasiyopendeza waliyo nayo bila ya kuwaaibisha watoto mbele ya wengine. Vile vile, wanapowafundisha Biblia wanawapa ujuzi uwezao kuwahekimisha zaidi kupita maono yote ya maisha. Zaburi 19:7 yatuambia hivi: “Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima.” Nayo Zaburi 119:130 yaongezea: “Kufafanusha maneno yako kwatia nuru, na kumfahamisha mjinga.”
11. Je! kuwa kijana na mjinga ni jambo la kuaibikia?
11 Kuwa kijana na mjinga silo jambo la kuaibikia. Ni hatua tu ya ukuzi, na lazima mtu avumilie. Lakini wakati mtu anapokataa kukubali kwamba ni mjinga naye anaendelea na kutenda matendo ya upumbavu na kuasi, akileta suto juu ya jamaa yake na kundi la Kikristo, hili ni jambo la kuaibikia. Mzazi anayejua hivyo na kumsaidia mtoto wake kwa busara afahamu hivyo atathawabishwa sana mtoto wake anapofanya maendeleo kuelekea kukomaa.
12. Wazazi wanawezaje kusaidia watoto wao wajifunze ubora wa kuonyesha heshima?
12 Mtu anapokuwa mwenye ujuzi katika njia za Yehova atakua katika ufahamu wa ubora wa kuonyesha heshima vile vile. Imewapasa wazazi waweke mfano mwema kwa watoto wao katika jambo hili. Imempasa baba aonyeshe heshima kwa mama, akijua kwamba mama ni mrithi mwenzake wa “neema ya uzima.” (1 Pet. 3:7) Yeye, vile vile, yampasa “kumstahi mumewe.” (Efe. 5:33) Imewapasa wote wawili wawaheshimu wazee katika kundi, wakiishi kupatana na shauri la Maandiko: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu.” (Ebr. 13:17) Kwa kushikamana hivyo na njia za Yehova wanaonyesha heshima kwa Yehova na mpango wake wa kitheokrasi.—1 Kor. 11:3.
13. (a) Maoni ya urafiki yamepaswa yawe na matokeo gani juu ya ukamatano wa mzazi na mtoto? (b) Ni kwa njia gani vipindi vya biashara vya televisheni vinavyoonyesha maoni yaliyopotoshwa ya ukamatano huu nyakati nyingine?
13 Wakati mfano huo mwema unapowekwa na wazazi, si vigumu kwa watoto kuishika kanuni ya heshima. Yaelekea watakuwa na heshima nyingi kwa wazazi wao na kuwaonyesha staha kwa njia nyingi. Kama ilivyosemwa, ni kweli kwamba wazazi na watoto wao wamepaswa wawe kama marafiki. Lakini hii ina maana ya mambo kama vile ukamatano wa uchangamfu na urafiki tu unaopaswa kuwa kati yao wala siyo usawa kwa njia nyingine katika jamaa. Matumizi ya kanuni za Biblia yanataka kwamba kuwe na ufahamu wa wazi juu ya aliye baba na aliye mtoto. Tofauti na hili, je! wewe umepata kuona katika vipindi vya biashara katika televisheni kwamba mara nyingi watoto wanaonyeshwa wakifundisha wazazi, wakiwaonyesha wao kama wenye kufuata mitindo ya kikale au wenye kuhitaji kurekebishwa au kupatanishwa na hali za kisasa? Matangazo kama hayo yanamtia mwana moyo amkaze baba yake anunue namna ya motokaa ambayo mwana anataka. Au yanamtia binti moyo amkaze mama ili aruhusiwe kununua mavazi “mapya” na “yaliyo tofauti,” marashi, sabuni za kuoshea nywele na vitu vingine ambavyo kwa kweli si vipya hata kidogo. Hii ni hila tu ya ulimwengu wa biashara ya kujifaidi kwa njia ya fedha bila ya kujali mabaya yatakayotokea nyumbani. Lakini Biblia yaonyesha wazi kwamba watoto ndio wajinga zaidi, na yawapasa watiwe moyo waonyeshe heshima kwa wale walioishi muda mrefu zaidi na walioona mengi zaidi maishani.
14, 15. (a) Kwa sababu gani watoto wafundishwe kuwaza wao wenyewe? (b) Toa mashauri ambayo yanaweza kusaidia wazazi katika jitihada zao za kusaidia watoto wao wakuze uwezo wa kufikiri.
14 Bila shaka, lazima watoto wafundishwe kuwaza wao wenyewe. Siku moja itawapasa kujifanyia maamuzi yao wenyewe, nayo malezi ya mapema yaweza kusaidia katika hili. Biblia inatia moyo sana kusitawisha uwezo wa kufikiri, nalo hili ni mojawapo la mambo yaliyo ya muhimu ambalo katika hilo wazazi wanaweza kusaidia watoto wao. Watakuza namna fulani ya kufikiri; kwa hiyo sababu gani usihakikishe kwamba wanajifunza kufikiria mambo kwa msingi wa mambo ambayo Biblia inayasema juu ya Yehova na njia zake. Mithali 5:1, 2 inasema hivi: “Mwanangu, sikiliza hekima yangu; tega sikio lako, mzisikie akili zangu; upate kuilinda busara, na midomo yako iyahifadhi maarifa.” Ikiwa wataka kumsaidia mtu akuze uwezo wa kufikiri ni jambo la maana kutomfanyia mwanafunzi mambo ambayo yeye mwenyewe aweza kujifanyia. Wanapotoa kweli kwa wengine, Wakristo wamejifunza ubora wa kumvuta msikilizaji kwenye mazungumzo, kumtia ndani, kujua yaliyomo akilini mwake, kisha kumfanya afikiri na kufikia mikataa ifaayo. Haya ni mashauri ambayo imewapasa wazazi wayakumbuke katika kusaidia watoto wao wakuze uwezo wa kufikiri.
15 Uwezo huu waweza kukuzwa kidogo kidogo mtoto anapozidi kukua. Kuna maamuzi mengi anayoweza kuruhusiwa ajifanyie, madogo madogo. Mwulize hivi, “Wadhani ingekuwa bora kufanya nini hapa?” Pengine jibu lake litaonyesha yeye anahitaji msaada zaidi kidogo. Jadiliana naye nawe umwelekeze upande unaofaa. Usichukizwe wala usikose kusubiri. Mtume Paulo alielekeza nyuma kwenye utoto wake mwenyewe kama mfano naye akasema: “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.” (1 Kor. 13:11) Alikuza uwezo wa kufikiri alipozidi kukua.
16. Hata watu wa kilimwengu wanajaribuje kutayarisha watoto wao kwa wakati ujao?
16 Hata wazazi wengine wasio sehemu ya kundi la Kikristo wanauona ubora wa kuwatayarisha watoto wao kwa wakati ujao. Wao hawaachi wakati ujao wa mtoto uongozwe na bahati wala hawamruhusu yeye achague anavyotaka kufanya, isipokuwa nyumaye anapoweza kufanya hivyo. Kwa mfano, huenda wakaanza mapema katika maisha ya mtoto kumtayarisha asimamie biashara ya jamaa, kuangalia mali ya jamaa au kuanza kazi mpya. Lakini inapokuwa juu ya dini, siyo hali ya fedha ya wakati wake ujao, mara nyingi wanasema watamruhusu mtoto ajiamulie nyumaye kwa kuwa wanaiona kama kitu kisicho na maana sana. Kwa hiyo, usifikiri kwamba ulimwengu hauikubali kanuni ya utayarishaji na malezi. Unafanya hivyo sana, lakini kwa kufuatia mambo ya kimwili, siyo mambo ya kiroho.
KUTOA SHAURI LINALOJENGA
17. Je! inatosha kutoa tu shauri la usawa, au jambo jingine zaidi lahitajiwa?
17 Nyakati nyingine, wanapokwisha kupokea shauri, watu wamesikika wakisema: “Mimi sikuyajali aliyoyasema; kwa kweli yalikuwa haki nayo yalistahili. Sikupendezwa kamwe na namna alivyoyasema.” Bila shaka, katika nyumba ya Kikristo shauri limepaswa likubaliwe hata ikiwa halikutolewa kwa njia ya kupendeza sana. Lakini je! kuna mambo ambayo mzazi aweza kukumbuka ili afanye shauri liwe jepesi kukubaliwa na watoto? Bila shaka yapo. Siyo shauri la kujua tu yaliyo mabaya na yanayohitajiwa kwa maendeleo, bali vile vile kujua namna ya kulishughulikia jambo lenyewe na namna ya kulisema.
18, 19. (a) Wakati na mahali vinakujaje katika hili jambo la kutoa shauri? (b) N’nini kingine kitakachosaidia kufanya shauri liwe jepesi zaidi kukubaliwa?
18 Jambo moja la kufikiria ni wakati wa kutoa shauri. Mara nyingi huenda wakati ufaao ukawa mara tu kosa linapofanywa, lakini sivyo ilivyo sikuzote. Kungoja mpaka mzazi na mtoto vile vile wawe katika hali ya utulivu wa akili zaidi huenda kukawa afadhali. Vile vile, mahali pamepaswa pafikiriwe. Ikiwa kosa lilifanywa katika mahali pa kukutanikia pa kundi, nyumbani kwa mtu mwingine au mlipokuwa dukani, pengine shauri lingeahirishwa mpaka mmefika nyumbani.
19 Namna ya kulisema inatia ndani fadhili, uangalifu, utulivu na busara. Huenda ukamruhusu mtoto aeleze mambo fulani mwenyewe, ukifahamu kwamba pengine wewe huyajui yote yanayopaswa. Na ungeweza kuuliza maulizo kuona kama anaelewa. Tabasamu laweza kufaa ikiwa jambo lenyewe si zito sana na ikiwa shauri linapokewa kwa hiari. Lakini katika wakati mzito zaidi ambapo shauri imara lahitajiwa tabasamu laweza kutoa maoni mabaya. Nyakati zote imempasa mtu ahakikishe kwamba shauri linafahamika waziwazi.
20, 21. (a) Kwa sababu gani kwa kawaida vitisho haviwi na matokeo bora katika kulea watoto? (b) Njia bora ni gani?
20 Vitisho na maonyo kwa kawaida haviwi na matokeo bora. Kwa sababu gani? Kwa maana huenda vikatokeza woga tu wa adhabu iliyokusudiwa, siyo chuki ya ubaya wenyewe. (Zab. 97:10) Katika Waefeso 6:9, mabwana wanashauriwa ‘waache kuogofya, huku mkijua ya kuwa yeye aliye Bwana wao na wenu yuko mbinguni, wala kwake hakuna upendeleo.’
21 Njia iliyo bora ni kuonyesha faida ya kufanya mambo namna Yehova anavyoyafanya na, iwezekanapo, sababu kwa nini mambo fulani ni mabaya. Kwa kutumainia mema tia moyo mwendo ufaao, lakini wakati ule ule onyesha wazi kwa upendo matokeo ya kutokutii yatakavyokuwa. Pana tofauti kati ya kutisha na kuonyesha yatakavyokuwa matokeo ya mwendo fulani bila shaka. Angalia namna ya ukaribishaji ambayo kwayo Yehova anatia moyo mwendo ufaao: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; . . . ndipo utakapofahamu kumcha [Yehova], na kupata kumjua Mungu.” (Mit. 2:1-5) Lakini nyumaye katika sura hii, matokeo yanajulishwa kwa njia ya fadhili lakini iliyo imara: “Ili upate kwenda katika njia ya watu wema, na kuyashika mapito ya wenye haki. Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mit. 2:20-22.
MASHIRIKA
22, 23. Washirika wanakuwa na matokeo gani juu ya mtoto, na kwa hiyo nia ya wazazi imepaswa kuwaje juu ya jambo hili?
22 Wazazi wa Kikristo wanaona mara nyingi kwamba magumu yanatokea wakati watoto wao wanapoanza kushirikiana na watoto wengine katika ujirani au na wanashule wenzao. Bila shaka, lazima wawe na ushirika fulani na watu wa nje. Kujitenga kabisa leo kunaelekea kutowezekana nako hakufai. Washirika wa kilimwengu wanatofautiana kwa kadiri ya maongozi yasiyo ya Kikristo wanayoyatoa. Lakini imewapasa wazazi wajue watoto wao wanazungumza na kucheza na nani. Wajapokuwa watu fulani wa kilimwengu leo wanazo tabia fulani za kutamanika, lazima ikumbukwe kwamba mtu asiye mwabudu wa Yehova hawezi kusemekana kuwa rafiki mwema.—1 Kor. 15:33.
23 Kwa njia ya ujumla mtu aweza kusema kwamba kunazo namna mbili tu za washirika. Mithali 13:20 inasema hivi: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” Bila shaka, hapa wenye hekima hawajulishwi hasa ni akina nani. Lakini Biblia inaonyesha wazi katika sehemu nyingine namna ya hekima inayomaanishwa. Zaburi 111:10 inasema hivi: “Kumcha [Yehova] ndio mwanzo wa hekima.” Kwa hiyo waabudu wa Yehova ndio wenye hekima ambao imewapasa watoto wako washirikiane nao. Hii itawasaidia wawe wenye hekima kweli kweli. Hali bora kabisa ni kuwa kwa wazazi na orodha nzuri sana kwa watoto wao hata pasibaki wakati wa mashirika ya nje. Kuwa pamoja na jamaa au Wakristo wengine kunakuwa kwenye kupendeza sana na kwenye kuvuta moyo hata mashirika mengine hayawi kishawishi. Lakini yakipata kuwa hivyo, basi imewapasa wazazi watumie wakati kumwonyesha mtoto wazi maoni ya Biblia juu ya jambo hili; wakati ule ule imewapasa watumie kujiweza kunakohitajiwa.
24. Kwa sababu gani watoto wenyewe wamepaswa wafahamu inavyosema Biblia juu ya mashirika mabaya?
24 Je! imewapasa wazazi wa Kikristo wawe wanyofu hivyo katika kufundisha watoto wao juu ya mashirika ya kilimwengu? Sababu gani isiwe hivyo? Kwa ujumla, watoto wanafurahia kuelezwa ukweli wa jambo ili lisifahamike vibaya. Wengine kati yao leo wanadai wanataka wazee “wasimulie mambo kama yalivyo.” Bila shaka, wamepaswa watoto wafundishwe fadhili na busara vile vile ili waweze kushughulika na wengine kwa njia ya upendo. Lakini haitoshi kwa wazazi peke yao kuzijua hatari za mashirika mabaya. Ikiwa watoto watalindwa, basi wao vile vile lazima wazijue hatari, na ni daraka la wazazi kulionyesha wazi jambo hili.
25. Imewapasa wazazi wamtegemee nani kwa uongozi katika kulea watoto wao, na kwa sababu gani?
25 Wanapojaribu kusitawisha ndani ya watoto wao sifa zisizoharibika upesi wanazozihitaji ili wayaokoke majaribu ambayo yangali mbele ya Wakristo wote wa kweli, imewapasa wazazi wamtegemee Yehova kwa nguvu na uongozi. (1 Kor. 3:10-15) Kulea watoto ili kwamba waweze kukua wakawe chanzo cha furaha kwa wazazi wao na heshima kwa Mungu si jambo jepesi. Inahitaji kuwa macho sikuzote. Lakini, lijapokuwa daraka linaloleta vitambo vidogo vya wasiwasi nyakati nyingine, ni pendeleo vile vile tulilopewa na Mungu mwenye upendo linaloleta furaha hasa. Kwa kweli uradhi na furaha vyaweza kuwako katika kulea watoto.
[Picha katika ukurasa wa 346]
Nia ya kweli ya kusikiliza magumu madogo madogo ya watoto wako ni ya maana katika kuziweka njia za kupashana habari wazi