Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 9/1 kur. 397-403
  • Ni kwa Njia Gani Tunavyoweza Kuwa “Waigaji wa Mungu”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni kwa Njia Gani Tunavyoweza Kuwa “Waigaji wa Mungu”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUWA WANYOFU NA WENYE HAKI
  • WAAMINIFU NA WENYE KUTEGEMEKA
  • YACHUKIE ANAYOYACHUKIA MUNGU
  • KUMWIGA MUNGU KWA HABARI YA UPENDO
  • SABABU GANI UJITAHIDI KUWA MKAMILIFU KAMA MUNGU ALIVYO MKAMILIFU?
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Jaribuni Kuwa Kama Yeye”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Iweni Waigaji wa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 9/1 kur. 397-403

Ni kwa Njia Gani Tunavyoweza Kuwa “Waigaji wa Mungu”?

“Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”​—Mt. 5:48.

1. Imetupasa tujisikieje juu ya Baba yetu wa kimbinguni, na kwa sababu gani?

WAKATI unapopendezwa na mtu kweli kweli, je! hutaki uwe kama yeye alivyo? Huenda hata ukajitahidi sana umwige yeye. Ndivyo watoto walivyo. Vivulana vingi vinasikika vikisema, “Nitakapokuwa mtu mzima mimi nitakuwa kama baba’angu hasa.” Je! sivyo inavyotupasa kujisikia juu ya Baba yetu wa kimbinguni, Yehova Mungu? Lo! yeye anapendeza namna gani katika kila njia! Yeye anaturuzuku kwa wingi namna gani, hata kufikia hatua ya kufanya mipango tukombolewe kutoka kwa dhambi na mauti tupate kufurahia uzima wa milele! (Yohana 3:16; Zab. 145:16) Je! tusivutwe tutake kuwa kama yeye alivyo? Lakini ni kwa njia gani tunavyoweza kumwiga yeye? Ni kwa kadiri gani ambavyo twaweza kuwa kama Mungu?

2. (a) Kwa sababu gani yawezekana kwetu kuwa wakamilifu kama vile Mungu alivyo mkamilifu? (b) Neno la Kiingereza perfect linatumiwaje mara kwa mara, na hii inalinganaje na maana ya maneno ya Kiebrania na Kigiriki yaliyotafsiriwa “mkamilifu”?

2 Huenda ukashangazwa na kadiri ambavyo Yesu Kristo alitia mkazo tuwe kama Mungu. Katika Mahubiri yake juu ya Mlima alisema hivi: “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Lakini je! sisi viumbe visivyokamilika twaweza tukawa wakamilifu? Ndiyo, kwa maana katika Maandiko neno ‘kamili’ linatumiwa kwa njia mbalimbali hata katika mazungumzo yetu ya kila siku. Hivyo yaweza kusemwa kwamba kitu ni kikamilifu ikiwa kinafaa sana katika matumizi yaliyokusudiwa. Kwa kuwa ndivyo ilivyo, twaona kwamba watumishi wa Mungu kama vile Nuhu na Ayubu walisemekana kuwa ‘wakamilifu.’ (Mwa. 6:9; Ayubu 2:3) Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yaliyotafsiriwa hapa kama “mkamilifu” yana maana ya kuwa ‘kitu kizima, kilichositawi kabisa, kisichopungua,’ kama vile neno la Kiingereza perfect linavyofafanuliwa kama “kitu kizima, kamili, kisicho na hitilafu.”

3, 4. (a) Ni katika maana gani ambavyo Nuhu na Ayubu walikuwa wakamilifu? (b) Ni katika maana gani tunavyoweza kuwa wakamilifu kama vile Baba yetu wa kimbinguni alivyo mkamilifu?

3 Ni kweli, watu kama vile Nuhu na Ayubu hawakuwa ‘wakamilifu’ katika maana ya kutokuwa na dhambi, lakini kwa ujumla wao walifanya yale ambayo Mungu alitaka wafanye, tukiufikiria wakati walimoishi na hali zao. Wao walimpendeza Mungu; walifanya yale aliyowatazamia kwa kufaa. Kwa hiyo hawakuwa na kosa, walikuwa wasiolaumika, wakamilifu katika maana hiyo.

4 Tukiyakumbuka hayo twaweza kuyaelewa maneno ya Yesu. Aliposema, “Mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” hakumaanisha kwamba alitutazamia tuwe wasio na dhambi, bali tuwe wakamilifu kwa njia nyingine. Hii yaweza kuonekana kutokana na habari zinazozunguka maneno ya Yesu. Alikuwa amesema kwamba Mungu anaangaza jua na kunyesha mvua kwa wasio haki na waovu pia, siyo kwa wema na wenye haki peke yao. Kwa hiyo, ikiwa twataka tuwe waigaji wa Mungu, tuwe wakamilifu kama yeye alivyo mkamilifu, tutataka tuwe wenye nia ya kutenda mema nafasi yo yote au uhitaji utokeapo, zaidi ya kuonyesha fadhili, rehema na ukarimu kwa jamaa zetu, rafiki zetu, au wale walio wa kabila letu wenyewe au taifa. Ndipo inapoweza kusemwa kwamba upendo wetu ni kamili.

5, 6. (a) Yaelekea ni kwa sababu gani Yesu alimwambia kijana fulani tajiri kwamba hakuwa mkamilifu? (b) Leo twaweza kujifunza nini kutokana na mambo haya ya karne ya kwanza?

5 Ili tuwe waigaji wa Mungu kwa kuwa wakamilifu kama vile Yeye alivyo mkamilifu, lazima pia tuwe tukifanya yote tuwezayo kwa faida ya ibada safi. Yesu Kristo alionyesha hivi wakati kijana mmoja tajiri alipofikia na kumwuliza analopaswa kufanya arithi uzima wa milele. Yesu alieleza hivi: “Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate.” (Mt. 19:16-23) Yaelekea kijana huyu alizuiwa asimtumikie Mungu kwa nafsi yote na mali zake nyingi za kimwili. Moyo wake ulielekea utajiri. Yesu alijua kwamba angefaidika kama angejiondolea mwenyewe vizuizi hivi. Vilikuwa vikimzuia asiwe mkamilifu au mzima katika utumishi wake kwa Mungu.

6 Maneno ya Yesu juu ya kuwa ‘wakamilifu’ yana maana gani kwetu leo? Hii: Hatuwezi hata kidogo kuridhishwa na kumtolea Mungu utumishi wa kuonyesha tu. Lazima tumpende Yehova Mungu kwa akili yetu yote, moyo, nafsi na nguvu, tusiruhusu tamaa za kipekee zituzuie tusimtolee Yeye ibada kamili. Hivyo iwapo hatuna wajibu wa Maandiko au vizuizi vya afya vya kutufanya tusishiriki wakati wote katika kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu kwa wengine, tutakuwa tukishiriki katika kazi ya wakati wote ya kuhubiri. Hatuwezi tukawa ‘wakamilifu’ tukisita-sita kumtumikia Mungu.

KUWA WANYOFU NA WENYE HAKI

7, 8. (a) Maandiko yanasemaje juu ya kuwa kwa Yehova Mungu mwenye haki? (b) Ili tumwige Mungu kwa habari ya haki, tunahitajiwa tufanye nini ikiwa tumeajiriwa kazi?

7 Kuwa ‘wakamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu’ kunatia ndani kuyapenda yale anayoyapenda. Hii inatia ndani kufuata yaliyo manyofu na haki. Biblia inatuambia kwamba Mungu “hupenda haki,” na kwamba yeye ni “asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Zab. 37:28; Kum. 32:4) Kwa hiyo ili tuwe “waigaji wa Mungu” lazima tuwe waaminifu katika matendo yetu yote, na, ikiwa tumeajiriwa, hiyo inatia na shughuli zetu na tajiri wetu. (Efe. 5:1, NW) Kwa kuwa leo udanganyifu umeenea pote, watu wengi wanaendesha mazoea yaliyo mabaya kweli kweli na kwa njia hiyo ‘wanaandamana na mkutano kutenda uovu.’​—Kut. 23:2.

8 Kwa mfano, wafanya kazi wengi kwa kawaida wanafanya kazi chache sana kama wawezavyo na hali hawapotezi kazi zao, au wakati mtu asipowatazama wanachukua vitu visivyo vyao. Hatuwezi tukafanya hivyo hata kidogo tukawa waigaji wa Mungu. Mazoea ya kutumia vibaya mipango ya afya na ya kusaidia wasio na kazi kwa fedha na ya kukopa na kutolipa yanafanywa na watu wengi pia. Walakini, ili ‘tuwe wakamilifu’ katika haki lazima ‘tufikiri yaliyo mema . . . mbele ya wanadamu,’ tukiufanya ‘mwenendo wetu kuwa mzuri kati ya Mataifa.’​—Zab. 37:21; 2 Kor. 8:21; 1 Pet. 2:12.

9. Tunatakiwa tufanyeje na haki ya Kimungu katika uhusiano wetu na “Kaisari”?

9 Ili tumwige Mungu katika haki yake twahitajiwa pia tuwe waaminifu katika kulipa kodi. Neno la Mungu linatuambia ‘tumpe Kaisari yaliyo ya Kaisari,’ na ‘kuwapa wote haki zao; mtu wa kodi, kodi.’ (Marko 12:17; Rum. 13:7) Majuzi ilikuwa lazima Mkristo tajiri atengwe na ushirika wa kundi la Kikristo la mashahidi wa Yehova kwa kukataa kuzitii amri hizi za Maandiko. Kwa kweli, yeye alikuwa tofauti sana, kama Akani katika Israeli wa kale, kwa maana kwa jumla mashahidi wa Yehova wanayo sifa njema kama walipa kodi wenye kushika sheria. (Yos. 7:1-26) Hivyo, gazeti la Kijeremani Sindelfinger Zeitung lilikuwa na makala yenye kichwa “Watu Walio Waaminifu Zaidi . . . Ni Mashahidi wa Yehova.” Lilizungumza juu ya shauri la kulipa kodi, nalo likamalizia kwa maneno haya: “Mashahidi wa Yehova wanajulikana kama watu walio waaminifu zaidi katika Jamhuri ya Mwungano, ndivyo inavyosema Idara ya Mwungano ya Fedha.” Ndivyo inavyopaswa kuwa, kwa kuwa kusudi hasa la mashahidi wa Yehova ni kuwa waigaji wa Mungu.

WAAMINIFU NA WENYE KUTEGEMEKA

10. Maandiko yanasema nini juu ya kuwa kwa Yehova Mungu mwaminifu na mwenye kutegemeka?

10 Yehova Mungu mwenyewe anatuwekea mfano bora tuuige katika kuwa waaminifu na wenye kutegemeka. Kama vile nabii wa Mungu Musa alivyowaambia watu wake Israeli: “Basi jueni ya kuwa [Yehova], Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake.” (Kum. 7:9) Mrithi wa Musa Yoshua aliushuhudia pia uhakika uu huu, akisema hivi: “Mnajua mioyoni mwenu, na [nafsini] mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” Yehova ndiye “Muumba mwaminifu” wetu ambaye kwake twaweza “kuendelea kupendekeza” nafsi zetu kwa matumaini yote.​—Yos. 23:14; 1 Pet. 4:19, NW; 1 Kor. 10:13.

11. (a) Sisi tuna madaraka gani kwa Mungu kama watoto wake walio wakf? (b) Twawezaje kuonyesha kutegemeka kwetu kwa uaminifu kwa kuiendesha kazi kubwa ya watumishi wa Mungu leo?

11 Kwa hiyo, basi, kama waigaji wa Yehova Mungu, sisi pia yatupasa tuwe waaminifu na wenye kutegemeka. Tunakabidhiwa mambo ya kipekee kama vile wakati, fedha, nguvu na maongozi ya kipekee. Imetupasa tuwe waaminifu katika haya. (1 Kor. 4:1, 2) Je! tumemwambia Yehova kwamba twataka kuwa mmojawapo wa watoto wake, na kwamba tutamtumikia yeye maadamu tuko hai? Je! tunatimiza ahadi yetu juu ya hili kwa uaminifu? Kazi kubwa ambayo Yehova anawataka watumishi wake waifanye sasa ni kuuhubiri ufalme wake, serikali itakayoharibu uovu na kuleta amani duniani. Katika unabii unaotimia katika siku zetu, Yesu alisema hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote . . . ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Je! tunaendesha kuhubiri huku kwa uaminifu? Je! tunafanya hivyo kwa kawaida, tukitembelea watu wote katika eneo ambamo tumegawiwa tuhubiri? Je! tunafanya ziara za kurudia kwa watu wote wanaoonyesha kupendezwa wajue mengi zaidi juu ya Mungu? Je! tu wenye kutegemeka kwa habari ya kuongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia na watu wa namna hiyo?

12, 13. (a) Twawezaje kuonyesha kutegemeka kwa Kimungu katika uhusiano wa ndoa? (b) Wakristo vijana wanawezaje kuonyesha ni wenye kutegemeka?

12 Kuna upande mwingine ambamo ni muhimu tuwe waaminifu na wenye kutegemeka, nao huo ndio uhusiano wetu wa jamaa. Je! sisi kama Wakristo waliooana tunatimiza nadhiri zetu za kupendana na kuangaliana? Au tunaacha mapendezi mengine au mambo, kama vile tamaa za namna fulani, yatufanye tusitoe haki zote kwa mwenzi wetu wa ndoa? Je! nyege zetu zinakuwa juu ya mwenzi wetu kwa uaminifu, au nyakati nyingine tamaa yetu inakuwa ya hapa na pale? Upendo na huruma vitatusaidia tuwe waaminifu na wenye kutegemeka. Tukifanya hivyo, tutakuwa tukimwiga Yehova, tukijionyesha kuwa wakamilifu kama yeye alivyo mkamilifu. Kwa maana Yehova ni Mwenyeji wa kiume aliye mwaminifu na wa kutegemeka wa tengenezo lake lenye mfano wa mke.​—Isa. 54:1, 5.

13 Namna gani juu yenu nyie vijana? Je! mnamwiga Mungu kwa kuwa wenye kutegemeka na waaminifu? Kwa mfano, je! mnapendezwa na migawo yenu ya shule na kuiangalia kwa bidii? Je! mnajionyesha kuwa wenye kutegemeka kwa habari ya kazi nyumbani? Baba arudipo nyumbani usiku, je! anakuta kwamba mmefanya kazi ambazo huenda aliwapa mzifanye? Katika ujana wenu mnayo nafasi ya kumkumbuka Muumba wenu Mkuu kwa kufanya mambo yatakayowafanya mwe wenye thamani machoni pake.​—Mhu. 12:1.

YACHUKIE ANAYOYACHUKIA MUNGU

14. Kwa kumwiga Yehova, ni mambo gani tunayopaswa kuyachukia?

14 Tena njia nyingine ambayo katika hiyo twaweza ‘kuwa waigaji wa Mungu,’ na kwa njia hiyo tujionyeshe kuwa wakamilifu kama Yeye alivyo mkamilifu, ni kwa kuyachukia anayoyachukia Mungu. Je! yeye anachukia nini? Anatuambia hivi: “Mimi, [Yehova], . . . nauchukia wivi na uovu.” “Kuna vitu sita anavyovichukia [Yehova]; naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.” Pia, Biblia yatia moyo hivi: “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu.” “Lichukieni lililo ovu.”​—Isa. 61:8; Mit. 6:16-19; Zab. 97:10; Rum. 12:9.

15. (a) Maana yake nini ‘kuchukia uovu’? (b) Kwa sababu gani ni muhimu tuyachukie mabaya?

15 Maana yake nini ‘kuchukia uovu’? Ina maana ya ‘kujisikia hupendi kabisa’ maovu, ‘kuyachukia zaidi sana sana.’ Ndiyo, haitoshi kwetu kuwa baridi au wasiokuwamo kwa habari ya yaliyo maovu au mabaya. Nyakati nyingine mabaya yanaweza yakawa yenye kuvutia mielekeo yetu yenye dhambi; yanaweza yakaelekea kuchochea, kusisimua au hata kuleta utajiri na raha. Kwa hiyo, ni muhimu sana sana kwamba tuyachukie kabisa yaliyo mabaya. Twawezaje kufanya hivi?

16. Twawezaje kuepuka ubaya usije ukatia mizizi ndani yetu na kusitawi?

16 Kwanza, twaweza tukajaribu kuzuia namna zote za ubaya zisitie mizizi ndani yetu kwa kuilinda mioyo yetu, mapendezi yetu, tamaa na maono ya moyoni. (Mit. 4:23; 1 Pet. 3:10, 11) Njia ya muhimu ya kufanya hivi ni kwa kujiangalia juu ya vitabu, magazeti na makala tunazosoma. Je! tunataka sana tujue uovu ulivyo hata kufikia hatua ya kupenda kusoma juu ya mabaya? Basi haiwezi ikasemwa kuwa tunayachukia. Na ikiwa twayachukia mabaya, hatutakuwa tukitazama vipindi vya televisheni au sinema zinazoonyesha jeuri, ukatili, ufisadi na namna nyingine za ubaya. Hatuwezi kuendelea kuona mambo hayo bila ya kushupazwa nayo na kushindwa kuyachukia tena; kwa kweli, tutakuja hata kuyatamani mambo hayo.

17. (a) Kwa sababu gani lazima tujihadhari juu ya mashirika yetu? (b) Imetupasa tuioneje hatua yo yote ya halmashauri ya hukumu ya kutenga mtu na ushirika, na kwa sababu gani?

17 Pia, ikiwa tunataka kuwa waigaji wa Yehova kwa kuchukia mabaya tutajihadhari sana juu ya watu tunaowachagua kama wenzi, tukikumbuka kwamba “mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Kor. 15:33, NW) Hii inatia ndani na kuunga mkono kwa uaminifu hatua ya halmashauri ya hukumu ya kundi inapotenga mtu na ushirika kwa sababu ya mwenendo usiompasa Mkristo. (1 Kor. 5:1-13) Mtu kama huyo hafai kwa ushirika. Imetupasa tuchukizwe kwa haki na ubaya ambao katika huo alijitia, na suto ambalo mwenendo wake umemletea Yehova Mungu na kundi la Kikristo. Imetupasa tufikirie namna ambavyo mwendo wake mbaya waweza kukwaza Wakristo wapya au wasiokomaa. Imetupasa tuitikie kama mtume Paulo alivyoitikia aliposema hivi: “Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe?”​—2 Kor. 11:29.

KUMWIGA MUNGU KWA HABARI YA UPENDO

18. (a) Ni njia gani iliyo bora tunavyoweza ‘kujionyesha kuwa wakamilifu’ kama vile Mungu alivyo mkamilifu? (b) Tunazo sababu gani za kumwiga yeye kwa njia hii?

18 Lakini, zaidi ya yote, namna ambavyo twaweza kujionyesha kuwa ‘wakamilifu kama Baba yetu alivyo mkamilifu’ ni kwa kuionyesha sifa njema ya upendo. Lo! Neno lake linaisifu sana hii sifa yake! Biblia yasema, “Mungu NI upendo.” Hasa Mungu ameupendekeza “upendo wake mwenyewe kwetu kwa maana, tulipokuwa tungali wenye dhambi, Kristo alitufia sisi.” Kwa kweli mpango huu wa upendo wa Mwana wake mzaliwa wa pekee, Yesu Kristo, umepaswa utufanye tuitikie kwa shukrani! Mtume Yohana alionyesha hivi, akisema: “Ikiwa hivi ndivyo Mungu alivyotupenda sisi, basi sisi wenyewe tu chini ya wajibu kupendana.”​—1 Yohana 4:9-11, 16, NW; Rum. 5:8.

19. Ni kwa njia gani tunavyoweza kuonyesha ukarimu wa Kimungu?

19 Kati ya njia ambazo katika hizo twaweza kuwa kama Mungu kwa habari ya upendo ni kwa kuwa wakarimu. Yehova ndiye Mpaji wa “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili,” naye ‘huwapa wote kwa ukarimu, wala hakemei.’ (Yak. 1:17, 5) Twaweza kuwa wakarimu na nini ili tuwe waigaji wa Mungu? Kwanza, tunayo kweli juu ya makusudi ya Mungu. Na kwa kuwa tumeipokea bure, imetupasa tuitoe bure kwa kuzishiriki habari njema za Ufalme na wengine wakati wo wote ufaao. Twaweza pia kuonyesha ukarimu wa Kimungu kwa kutoa vitu vyetu vya kimwili kwa ukarimu tuiendeleze kazi ya kuuhubiri Ufalme katika eneo letu na ulimwenguni pote. Tena njia nyingine ya kuonyesha ukarimu ni kwa kuwasaidia Wakristo wenzetu wo wote ambao wanaweza kuwa na shida. Ni jambo la muhimu kabisa tuonyeshe ukarimu huo, kwa maana ni njia ya muhimu ambavyo tunaitii amri ya Yesu ‘kuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.’​—Mt. 5:46-48; 1 Yohana 3:17, 18.

20, 21. (a) Ni juu ya nini hasa tunasihiwa ‘tuwe waigaji wa Mungu’? (b) Twawezaje kumwiga Mungu kwa kuwa wenye kusamehe?

20 Njia nyingine ambavyo twaweza kumwiga Mungu kwa habari ya upendo ni kwa kuwa wenye kusamehe. Kwa kweli, habari hii tunayoshauriwa kuwa waigaji wa Mungu ni juu ya kusamehe kwa Mungu. Angalia habari zinazozunguka za shauri la mtume ambalo tumeliangalia: “Iweni wafadhili kwa mtu na mwenzake, wenye huruma, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia kwa Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari. Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.”​—⁠Efe. 4:32-5:2, NW.

21 Kwa kuwa sote tu wasiokamilika nasi hatuna hekima nyingi, ufahamu na busara, je! haitupasi kuwasamehe ndugu zetu wa Kikristo dhambi zao? Ndiyo, upendo “husitiri wingi wa dhambi.” (1 Pet. 4:8) Ikiwa Yehova ‘anakumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi’ na kwa hiyo ‘anaweka dhambi zetu mbali nasi kama mashariki ilivyo mbali na magharibi,’ je! sisi viumbe visivyokamilika haitupasi kuwa wenye nia zaidi ya kuwasamehe wale ambao huenda wakatukosa na wanaoomba msamaha? Kwa kuwa Mungu ‘anasamehe kabisa,’ je! haitupasi tumwige yeye katika hili pia? Hiyo yamaanisha kwamba imetupasa tuwe wenye nia ya kusamehe “mara sabini na saba,” kama vile Yesu alivyomwambia Petro afanye, kutia na hata makosa mazito tuliyotendewa iwapo mkosaji anaonyesha toba la kweli.​—Zab. 103:8-14; Isa. 55:7; Mt. 18:21-35, NW.

22-24. (a) Biblia inasema nini juu ya kuwa kwa Yehova mwenye uvumilivu? (b) Twawezaje sote kumwiga Yehova na kujionyesha pia kuwa wenye uvumilivu?

22 Tena njia nyingine ambavyo Mungu anatuwekea mfano huo wenye upendo ni kwa kutokuwa mwepesi wa hasira na mvumilivu. Akiitaji hali hii yenye kupendeza ya utu wa Mungu, mtume Petro aliandika hivi: “[Yehova] . . . huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Pet. 3:9) Ni ajabu namna gani Mungu alivyojionyesha kutokuwa mwepesi wa hasira alipokuwa akishughulika na taifa lake la Israeli mnamo utawala wa wafalme! Biblia inasema hivi: “[Yehova], Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake.”​—2 Nya. (Sik.) 36:15.

23 Twaweza kuiiga hali hii ya upendo wa Mungu kwa kutosumbuliwa na makosa ya wengine. Nyakati nyingine huenda wale ambao mtu anasimamia wakaonyesha ubaridi au uzembe, na kwa hiyo ni vyepesi kwa mwangalizi kupandwa na hasira. Lakini ili wawe waigaji wa Mungu imewapasa waangalizi pia wawe wavumilivu na wasio wepesi wa hasira.

24 Hasa katika jamaa imetupasa tutumie sifa hii ya uvumilivu. Ni jambo la kawaida kwa waume wa ulimwengu kuwa wenye harara na wake zao. Kwa hiyo, shauri la mtume Paulo kwa Wakristo linafaa sana: “Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao.” (Kol. 3:19) Maneno ya mtume Petro pia juu ya namna ya kutendea wake yanafaa sana. “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” Kulitii shauri hili ni kwa muhimu kama vile kutimiza mapenzi ya Mungu kwa kuuhubiri ujumbe wake wa Ufalme duniani pote kulivyo kwa muhimu.​—1 Pet. 3:7.

25, 26. (a) Mungu ameonyeshaje uvumilivu? (b) Twawezaje kuonyesha uvumilivu wa Kimungu?

25 Njia nyingine tena ambavyo imetupasa tumwige Mungu iwapo twataka kuwa wakamilifu kama vile yeye alivyo mkamilifu ni kwa kuuiga uvumilivu wake wenye upendo. “Upendo . . . huvumilia yote,” ndivyo inavyosema Biblia. (1 Kor. 13:4, 7) Je! Mungu anaonyesha uvumilivu? Ndiyo, kwa maana yeye anaendelea kufanya yaliyo haki, ajapokuwa anahuzunika na kuona vibaya viumbe vyake vikosapo. (Zab. 78:40, 41) Kama vile mtume aliyeongozwa na roho ya Mungu anavyotukumbusha: “Mungu . . . kwa uvumilivu mwingi, alichukuliana na vile vyombo vya ghadhabu.” Kwa sababu gani? Kwa sababu ya upendo wake, ili “audhihirishe wingi wa utukufu wake katika vile vyombo vya rehema.”​—Rum. 9:22, 23.

26 Ikiwa twataka kuwa waigaji wa Mungu kwa habari ya upendo wako lazima sisi pia tuonyeshe uvumilivu. “Tusichoke katika kutenda mema.” (Gal. 6:9) Upendo utatusaidia tuendelee kuwa waaminifu katika kazi yetu ya kuuhubiri Ufalme hata watu tunaosema nao wawe baridi, hata wapinge. Huenda tunatumikia katika makao ya Betheli ambapo vitabu vya Biblia vinachapwa ili kuendesha kuhubiri kwa Ufalme duniani pote. Huenda kazi tunazozifanya zikawa zile zile kila siku, lakini upendo kwa Yehova Mungu utatusaidia tuvumilie, tukijua kwamba zinasaidia kushuhudia jina la Mungu na kuelekeza wengine kwenye wokovu, nao huo ni uhakika wa kwamba tunashukuru kwa yote aliyotufanyia sisi.

SABABU GANI UJITAHIDI KUWA MKAMILIFU KAMA MUNGU ALIVYO MKAMILIFU?

27, 28. (a) Je! shauri la kuwa wakamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu linaachiwa hiari ya mtu? (b) Kwa sababu gani kuwa wakamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu kunatuletea furaha?

27 Kwa kweli mengi yanatiwa ndani katika kuwa waigaji wa Mungu na hivyo kujionyesha kuwa wakamilifu kama yeye alivyo mkamilifu! Lakini angalia kwamba shauri hili la kuwa ‘wakamilifu’ haliachiwi hiari ya mtu. Yesu alisema hivi: “Mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Ndiyo, ikiwa twataka kuwa Wakristo wa kweli, “waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa,” ni muhimu kabisa tuwe wenye haki na wanyofu, waaminifu na wenye kutegemeka, tukiyachukia anayoyachukia Mungu, na kuonyesha upendo kwa kuwa wakarimu, wenye kusamehe na wenye uvumilivu. (Efe. 5:1, NW) Lakini, kwa kweli si vigumu sana kwetu kuwa wakamilifu kama vile Mungu alivyo mkamilifu. Bali, tunafaidika. Kwa maana je! Yehova siye “Mungu mwenye furaha”? (1 Tim. 1:11, NW) Kumwiga Yeye kutatuongezea furaha yetu pia. Namna gani hivyo?

28 Kwanza, kwa kumwiga Yehova tunamfurahisha moyo wake, kama vile anavyotuambia: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mit. 27:11) Bila shaka twaweza kuwa wenye furaha ikiwa mwendo wetu wa maisha unamfurahisha Baba yetu wa kimbinguni. Na kwa kumwiga Mungu si kwamba tu tutakuwa na furaha, amani ya akili na uradhi sasa, lakini pia tutakuwa nalo tumaini lililo hakika la uzima wa milele katika taratibu yake mpya ya mambo. Kwa kweli yatupasa tujitahidi kwa vyo vyote ‘tuwe wakamilifu kama Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu, alivyo mkamilifu’!

​—Kutoka The Watchtower, March 1, 1974.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki