“Iweni Waigaji wa Mungu”
“Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.”—Efe. 5:1, 2, NW.
1, 2. (a) Ni nini kinachoweza kusemwa juu ya tabia ya kuiga? (b) Kwa sababu ya tabia ya kuiga iliyomo katika wanadamu, ni mfano gani unaohitajiwa?
IMEONEKANA sana kwamba “mwanadamu ni kiumbe chenye kuiga,” na kwamba “ni kwa kuiga hasa tunavyojifunza kila kitu kuliko kwa kufundishwa.” Mwanafilosofia wa Kigiriki Aristotle alisema hivi: “Kuiga inakuwa tabia ya kurithi katika mwanadamu tangu utoto wake mchanga.”
2 Ni kweli. Sote tunaanza maisha yetu kwa kuiga. Mtoto hajifunzi kutembea, kujilisha, kusema na kufanya mambo mengineyo kwa kusoma vitabu wala kwa kufundishwa. Bali, ni kwa kuwaiga wazazi wake au ndugu zake na dada wakubwa. Nasi twaendelea kuishi tukiiga watu wengine, mara nyingi bila ya kujua. Kwa sababu kuna umuhimu wa tabia ya silika ya kuiga katika wanadamu, ni jambo la maana kama nini kutazama mfano unaofaa! Katika habari hii, hakuna mfano bora kuliko Mungu mwenyewe. “Iweni waigaji wa Mungu,” ndivyo anavyosihi mtume wa Kikristo aliyeongozwa na roho ya Mungu.—Efe. 5:1, NW.
3. Mambo yanaelekea kuwa vingine kuliko ambavyo watu wanadai kwa njia gani, hii ikitokeza maulizo gani?
3 Lakini kwa wazi wingi wa wanadamu wanaiga mifano mibaya, kwa maana ebu utazame uvunjaji wa sheria wote, ufisadi na vita ambamo inaelekea watu kila mahali wanajitia. Na hali wakati uo huo, watu wengi wanasema wanamwabudu Mungu nao wanatoa ushuhuda wa hili kwa kutenda matendo mbalimbali ya kidini. Kwa sababu gani mambo yanaelekea kuwa vingine kuliko ambavyo watu wanadai? Kwa sababu gani watu wanafanya mambo mengi sana mabaya, na hali wanajidai kumwabudu Mungu? Je! aweza mtu kumwabudu Mungu kweli, na huku ashindwe kumwiga yeye?
MIUNGU INAYOIGWA
4. (a) Ni nini kinachoweza kusemwa juu ya tabia ya kibinadamu ya kuabudu? (b) Kuabudu mungu kuna matokeo gani juu ya waabudu?
4 Si kwamba tu mwanadamu aliumbwa akiwa na tabia ya kuiga lakini pia aliumbwa akiwa na tabia ya kuabudu. Je! mwanadamu ameyaonyesha sana maelekeo haya? The World Book Encyclopediaa kinatuambia hivi: “Hakujapata kuwako watu ambao hawakuwa na namna fulani ya dini.” Walakini, jambo la muhimu kukumbuka ni kwamba watu wameabudu miungu mingi mbalimbali zaidi ya Mungu wa kweli, kama vile Biblia inavyosema: “Kuna ‘miungu’ mingi na ‘mabwana’ wengi.” (1 Kor. 8:5, NW) Hata hivyo bila kujali dini yao, watu wameiga katika maisha zao sifa za mungu wanayemwabudu. Mtu hawezi akaabudu mungu bila ya kumwiga sana mungu huyo.
5. Kuabudu miungu ya Wakanaani kulitokeza nini, na kwa sababu gani?
5 Kwa mfano, wataalamu wenye kuchunguza mambo ya kale wanatueleza juu ya miungu mikatili na ya ufisadi ambayo Wakanaani wa kale waliabudu. Na kwa hiyo, kama ambavyo tungetazamia, historia yaonyesha wazi kwamba Wakanaani walikuwa wakatili sana sana na wafisadi, walikuwa wakiendesha desturi za kuogofya sana za kidini zilizotia na kutoa hata wanadamu kama dhabihu. Biblia pia yaonyesha kwamba wafalme wa Kiyahudi Ahazi na Manase walianza kuiabudu miungu ya Wakanaani, hata wakafikia hatua ya kuwatoa watoto wao wenyewe kwayo wawe kama dhabihu ya kuteketezwa! (2 Fal. 16:1-3; 21:1-6) Kwa wazi, onyo lililoongozwa na roho ya Mungu la ‘kuwa waigaji wa Mungu’ halikumaanisha kwamba tuiige miungu ya watu hawa!
6-8. (a) Kwa sababu gani kuwa tu na Biblia hakumaanishi kwamba Mungu wa Biblia ndiye anayeabudiwa? (b) Ni mungu wa namna gani anayeabudiwa katika Kristendomu, nazo sifa za mungu huyu zaonyeshwaje katika waabudu?
6 Lakini, ni hali gani iliyomo katika nchi za Kristendomu? Ni mungu gani anayeabudiwa na watu humo? Je! ndiye Mungu wa Biblia, kama watu wengi wanavyodhani? Zijapokuwa dini za Kristendomu zinayo Biblia, hii haina maana ya kwamba zinaiamini, kuifuata, au hata kwamba zinamwabudu Mungu ambaye Biblia ndilo neno lake. Waisraeli wa kale pia walikuwa na sheria ya Mungu ambayo inasema hivi kwa ufupi: “Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto.” (Kum. 18:9-12) Na hali, kama tulivyoona, hata wengine wa wafalme wao hawakuitii sheria hii. Vivyo hivyo, Kristendomu amemdharau Mungu na Neno lake.
7 The Encyclopedia Americana kinasema hivi juu ya imani ya Kristendomu katika mungu anayepeleka mamilioni ya wanadamu kwenye hell yenye moto: “Hell kama ijulikanavyo na watu wengi ndiyo makao ya roho wabaya; sehemu zenye moto mwingi, . . . ambako nafsi zilizopotea au zilizolaaniwa zinakwenda baada ya kufa zikapatwe na mateso yasiyoelezeka na adhabu ya milele.”b Kwa kuwa watu wa Kristendomu wameabudu mungu anayeyakubali mateso haya, hii yasaidia kueleza sababu gani Kristendomu amepigana vita vya kidini na akatesa watu kwa ukatili sana. Watu wameonyesha sana sifa za mungu wanayemwabudu.
8 Hivyo, wakati mwanafunzi wa Kispania Michael Servetus alipopelekwa mahakamani kama “mzushi,” alihukumiwa kuteketezwa kwa moto akiwa hai jambo hili likichochewa na viongozi wa kidini. Namna hii ya ukatili ya uuaji “ilikubaliwa na kufanywa wakati huo karibu katika ulimwengu wote” na Wakatoliki na Waprotestanti pia, kulingana na Institutes of Ecclesiastical History.c Hata katika nyakati za kisasa ndani ya Kristendomu ndimo vita vya ulimwengu vya kuogofya vilimoanzia, nao viongozi wa kidini wa pande zote mbili za vita walisali kwa mungu wao waupate ushindi na baraka juu ya majeshi ya taifa lao.d Kwa kweli hatutaki tuwe waigaji wa mungu huyu wa Kristendomu wala wa waabudu wake!
9. Mingine ya “miungu” inayopendwa na watu wengi inayoabudiwa na kuigwa leo ni ipi?
9 Isishangaze kwamba mamilioni ya watu wenye kupambanua mambo, hasa vijana, wameacha kuabudu katika makanisa ya Kristendomu. Lakini watu hawa wangali wana tamaa ya kuabudu moyoni. Mara nyingi wanaitosheleza tamaa hii kwa kuona fahari mno juu ya mabingwa wa kucheza dansi, wa kuigiza sinema na wanamichezo hodari hata wanafikia hatua ya kuwaheshimu mno kama miungu. Likisimulia “mungu” wa michezo apendwaye na watu wengi, New York Times la Julai 26, 1973 lilisema kwamba anaelekea kuwa na hakika ya “kuheshimiwa zaidi sana kupita wengine wote wanaoonewa fahari mno hata kufanywa miungu katika michezo ya mshahara, inayofuatwa sana na Waamerika kama dini.” Mara nyingi vijana wanajaribu kuiiga “miungu” hii ya michezo yenye kufurahisha, wakiiga mitindo yao ya nywele, mavazi, usemi na tabia. Lakini wanapofanya hivyo, wao wanaabudu nani hasa?
10, 11. (a) Ibada inayotolewa kwa miungu ya kisasa inamwendea nani, kama inavyoonyeshwa na 1 Wakorintho 10:19, 20? (b) Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba Ibilisi na mashetani wake ndio wanaopokea ibada inayotolewa kwa miungu ipendwayo na watu wengi?
10 Biblia inasema waziwazi sana juu ya dhabihu au ibada inayotolewa kwa miungu ya sanamu. Kwa kweli, huenda ukashtuliwa na inavyosema. Akiandika kwa kuongozwa na roho ya Mungu, mtume wa Kikristo Paulo alieleza hivi: “Basi niseme nini? ya kwamba kile kilichotolewa sadaka kwa sanamu ni kitu? au ya kwamba sanamu ni kitu? Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.” (1 Kor. 10:19, 20) Ndiyo, heshima inayozidi hata inakuwa ibada kwa kweli inamwendea “mungu wa dunia hii,” Shetani Ibilisi, na mashetani wake bila ya kujali kama inatolewa kwa mungu wa sanamu ya mti na jiwe au kwa mungu wa michezoni au wa kujifurahisha! (2 Kor. 4:4) Lakini ni ushuhuda gani unaoonyesha kwamba mashetani hasa wanapewa heshima inayozidi hata inakuwa ibada?
11 Basi, ni nini maelekeo kati ya wapendao michezo fulani sana hata kuheshimu mabingwa wake kupita kiasi? Je! maelekeo leo ni kuzionyesha sifa zenye kupendeza za kweli, usafi na kuifikiria hali njema ya wengine? Sivyo; bali, watu wanaelekea kuwa wadanganyifu, wafisadi, wachafu na wenye kuudhi wengine. Hivi ndivyo wafuasi wanavyoona miungu yao ikifanya. Majuzi msimamizi ajulikanaye sana wa mchezo mmoja wa mpira wa kutumia kibao alisema hivi: “Waona wao [wachezaji] wanavyocheza, wanacheza vyo vyote tu. Ikiwa wachezaji wanaweza kufanya hivyo, sababu gani watazamaji wasiweze?” (New York Times, Oktoba 13, 1973) Kwa hiyo, je! si wazi kwamba kuiga wanadamu wasiokamilika kama “miungu” kunaondoa watu katika ibada ya Mungu wa kweli? Kwa njia hiyo ibada wanayopewa wao inakwenda kwa Ibilisi na mashetani wake hasa, sawa na Biblia inavyoonyesha. (Yohana 8:44) Bila shaka hatutaki tuige “miungu” ya kibinadamu wala mashetani wasioonekana.
MWIGE MUNGU WA KWELI
12. Mungu wa kweli tunayesihiwa tumwige ndiye nani, na kwa sababu gani wazo la kumwiga yeye laweza kutuduwaza sisi?
12 Kwa hiyo ni jambo la maana sana tulitii onyo la upole la mtume: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Efe. 5:1, NW) Kufanya hivyo ni ulinzi juu ya kuwa waigaji wa miungu yo yote ya uongo. Lakini ni nani Mungu wa kweli tunayesihiwa tumwige? Mtunga zaburi wa Biblia anajibu, akisema na Yeye huyo: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zab. 83:18) Ni kwa sababu ya Uumbaji wake wa vitu vyote kwamba Yehova ni MUNGU kweli kweli, kama vile alivyoeleza nabii Yeremia: “[Yehova] ndiye Mungu wa kweli; . . . Ameiumba dunia kwa uweza wake, ameuthibitisha ulimwengu kwa hekima yake, na kwa ufahamu wake amezitandika mbingu.” (Yer. 10:10-12) Tunapouangalia ukubwa wa ulimwengu wote, pamoja na mabilioni yake ya makundi ya nyota, lo! namna tulivyo wadogo na hafifu tukilinganishwa na Muumba Mkuu, Yehova! Hata wazo la kumwiga Yeye linaelekea kutuduwaza sisi. Hiyo yawezekanaje?
13. Kwa sababu gani inawezekana na ni jambo la akili pia wanadamu wamwige Yehova?
13 Yawezekana kwa sababu ya namna ambavyo Yehova Mungu alituumba. Biblia inaeleza hivi: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwa. 1:27) Kuumbwa kwa mfano wa Mungu hakuna maana ya kwamba wanadamu waliumbwa wafanane na Mungu, bali, kwamba Mungu aliweka uwezo wa kutumia sifa zake mwenyewe katika wanadamu wa kwanza. Wakawa watoto wake. Na je! mwana haelekei kutenda kama baba yake, au binti kama mama yake? Kwa kweli, nyakati nyingine mwana anafanana na baba yake sana hata anasemekana kumlanda baba yake. Ndivyo inavyotupasa kuwa. Kwa maana kumbuka kwamba tunasihiwa ‘tuwe waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.’ (Efe. 5:1, NW) Lakini twawezaje kuonyesha kwamba tunamwiga Mungu wa kweli Yehova na siyo miungu ya uongo, kama watoto wapendwa?
14, 15. (a) Ni njia gani kubwa ambavyo wanadamu wanaonyesha wanamwiga Yehova Mungu? (b) Tunasihiwaje tuziige sifa za Mungu?
14 Tukilitazama tena onyo la mtume, twaiona njia kubwa ambavyo twaweza kuonyesha tunamwiga Mungu. Linasema hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.” (Efe. 5:1, 2, NW) Ndiyo, Yehova Mungu ndiye wa kuigwa hasa katika kuonyesha upendo. (1 Yohana 4:8) Mtunga zaburi wa Biblia aliyeongozwa na roho ya Mungu anaandika hivi: “[Yehova] ana fadhili, ni mwingi wa huruma, si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, [Yehova] ni mwema kwa watu wote, na rehema zake zi juu ya kazi zake zote.”—Zab. 145:8, 9.
15 Tunahakikisha kwamba tu waabudu wa Yehova kwa kuziiga sifa zake za upendo na rehema. Tunasihiwa tufanye hivi, kama vile Mwana wa Mungu Yesu Kristo alivyosema: “Endeleeni kuwa wenye rehema, sawa na Baba yenu alivyo mwenye rehema.” Pia, mtume Petro aliandika hivi: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”—Luka 6:36, NW; 1 Pet. 1:15, 16; Mt. 5:44, 45.
16. Ingekuwaje kama kila mtu duniani angemwiga Mungu, nasi tuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba karibuni kila mtu atamwiga?
16 Ebu wazia namna ambavyo ingekuwa kama kila mtu duniani angemwiga Yehova Mungu, ‘na kuendelea kutembea katika upendo’! Kusingekuwa na mwenendo mchafu na mpotovu—kusingekuwa na wizi, kupigana, wala ufisadi; kwa kweli, hakuna mtu ambaye angedhuru wengine. Badala yake, wote wangetendeana kwa fadhili, upendo na rehema, kwa maana huo ndio mfano uliowekwa na Mungu. Je! wewe ungependa uishi katika wakati ambao kila mtu atafanya mapenzi ya Mungu na kutembea katika upendo? Waweza, kwa maana ni kusudi la Yehova Mungu watu wa namna hiyo peke yao ndio waendelee kuishi duniani. Ahadi za Mungu zilizoandikwa zitatimia karibuni. Hii itamaanisha kukoma kwa ulimwengu huu wa wanadamu waovu, kukifuatwa na taratibu mpya ya mambo yenye haki kwa wale wanaofanya mapenzi yake.—1 Yohana 2:17; 2 Pet. 3:5-7, 13.
17, 18. (a) Kwa sababu gani ni muhimu kuwa mwigaji wa Mungu sasa, na kwa sababu gani inahitaji jitihada kumwiga Mungu sasa? (b) Kuwa kwetu mabalozi au wajumbe wa Mungu kunatuwekea wajibu gani?
17 Walakini, ili ustahili kuishi milele katika taratibu mpya ya Yehova ni lazima uwe mwigaji wa Mungu sasa. Hii inahitaji jitihada ya kipekee kwa upande wako upate kumjua Yehova, kwa maana wingi wa wanadamu wanamwiga “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi, wawe wanajua au sivyo. “Ulimwengu mzima uko katika nguvu ya yule mwovu,” ndivyo Biblia inavyoeleza. Je! tabia za mataifa hazionyeshi kwamba mungu wao na mtawala kweli ni Shetani Ibilisi?—Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19; 2 Kor. 4:4, NW.
18 Lakini Wakristo wa kweli ni tofauti. Yesu alisema, “wao si wa ulimwengu.” (Yohana 17:16) Wao wanajitenga na siasa za ulimwengu huu na njia zake mbovu, kwa maana lazima watumikie kama mabalozi au wajumbe wa serikali ya Mungu, wakimwakilisha Yehova Mungu sawasawa, kama vile tusomavyo: “Kwa hiyo sisi tu mabalozi badala ya Kristo, kana kwamba Mungu alikuwa akisihi kupitia kwa sisi.” Je! si kweli kwamba ni wakati tu tutakapoonyesha utu wa Mungu itakapoweza kusemekana kwamba Mungu mwenyewe anasihi kupitia kwetu sisi?—2 Kor. 5:20, NW.
MISAADA YA KUMWIGA MUNGU
19. Kwa sababu gani uhakika wa kwamba Mungu haonekani si kizuizi kisichoshindika cha kutufanya tusimjue yeye hasa na kumwiga?
19 Bila shaka, ili tumwige mtu ye yote lazima tupate kumjua. Ndivyo ilivyo na kumwiga Mungu. Tofauti na vile ambavyo wengine wanaweza wakafikiri, uhakika wa kwamba Mungu haonekani si kizuizi kisichoshindika cha kutufanya tusimjue hasa na kumwiga yeye. Kwa mfano, huenda mchora ramani za majengo aliye mashuhuri akawa amekufa. Lakini kwa kujifahamisha na kazi zake—majengo, madaraja na majumba mengine aliyoyajenga—mtu aweza kusaidiwa kwa kadiri fulani kuziiga njia alizozitumia katika kazi yake. Vivyo hivyo, uumbaji wote wa Yehova unaotuzunguka waweza kutusaidia sana tupate kumjua yeye na kumwiga, kama vile mtume Paulo alivyoonyesha aliposema hivi: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake.”—Rum. 1:20.
20. “Kitabu cha Uumbaji” chawezaje kutusaidia tumwige Mungu?
20 Ndiyo, kinachoitwa “Kitabu cha Uumbaji” chaweza kutuambia mambo yanayoweza kutusaidia tumwige Mungu. Kwa mfano, angalia namna Mungu alivyoipamba dunia na uzuri mwingi na mambo ya kupendeza. Machweo ya jua yanapendeza sana, maua yenye rangi nyingi sana, mashamba yenye kusitawi sana ya kijani, nyimbo za ndege, hewa yenye harufu za kupendeza za miti ya mwitu, na matunda mengi ya kupendeza, njugu, karanga, lozi na vyakula vingine. Kwa wazi, mtu aweza kujifunza kutokana na uumbaji kwamba Mungu ni Mpaji wa ajabu anayependezwa kweli kweli na furaha ya watoto wake wa kidunia. Je! mtu mwenye shukrani asivutwe auige mfano huo? Kwa mfano, je! haimpasi mzazi avutwe na mfano wa Mungu atoe vitu vizuri, vya kupendeza na vya kujenga kwa faida na furaha ya jamaa yake, kwa njia hiyo akimwiga Baba yake wa kimbinguni?—Isa. 64:8; Luka 6:35.
21. (a) Ni nini ulio msaada bora wa kumwiga Mungu, na je! kuwa nao tu kunatosha? (b) Twawezaje tukamsikiliza Mungu?
21 Walakini, “Kitabu cha Uumbaji” kina mipaka ya kutusaidia tumwige Mungu, kama vile majengo yalivyo na ubora wenye mipaka katika kusaidia mwanafunzi amwige aliyechora ramani ya majengo hayo. Kwa mfano, kujifunza vitabu vilivyoandikwa na mchoraji na habari zake mwenyewe kungesaidia sana kufahamiana naye na kumwiga. Vivyo hivyo, msaada ulio bora wa kufahamiana na Mungu na kumwiga ndiyo Kitabu ambacho Mungu ameandikisha kisimulie juu yake. Kitabu hicho ndicho Biblia Takatifu. Walakini, kuwa tu na Biblia, au hata kuisoma tu, hakutakusaidia umwige Yehova Mungu. Imekupasa ujifunze Biblia. Kwa hiyo, imekupasa ‘umsikilize Mungu kwa bidii.’ (Isa. 55:2, 3) Wawezaje kufanya hivi? Kwa kufanya kama vile Yoshua wa kale alivyoamriwa afanye: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo.”—Yos. 1:8.
22. Ni nini kinachohitajiwa ili tumwige Mungu, tubadili maisha yetu na kujipatanisha na mfano wake?
22 Kwa hiyo, ili tumwige Mungu lazima tufanye mengi zaidi kuliko kusoma tu na kujifunza Biblia. Lazima tuifahamu na kuithamini, ili tupate kuvutwa kufanya yote ambayo Mungu anatutaka tuyafanye. Imetupasa tupate “maarifa yaliyo sahihi” juu ya mapenzi ya Mungu na makusudi yake. Haya ndiyo ambayo mtume Paulo alionyesha yaweza kuyabadili maisha yetu tupatane na mfano wa Mungu. Aliandika hivi: “Vueni utu wa kale na mazoea yake, mjivike utu mpya, ambao kupitia kwa maarifa yaliyo sahihi unafanywa mpya kulingana na mfano wake Yeye aliyeuumba.” (Kol. 3:9, 10, NW) Ni kwa kutwaa haya “maarifa yaliyo sahihi” tunapoweza tu kujipatanisha kweli na mfano wa Mungu tukiziiga sifa zake za ajabu, fadhili na rehema. Kupendeza kwa sifa hizi za Kimungu kumepaswa kuivute mioyo yetu.
23. Ni sababu gani ya muhimu tuliyo nayo ya kumwiga Mungu kwa kuwa wenye kusamehe wengine?
23 Sababu zinazotolewa katika Neno lake Yehova za kumwiga yeye zinatusaidia pia tufanye hivyo. Je! sisi twataka Mungu atusamehe? Basi lazima tumwige yeye kwa kuwa wenye kusamehe. Kama vile Yesu alivyosema alipokuwa akimalizia mfano wake juu ya mtumwa asiyesamehe: “Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.” Naye mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.” Bila shaka, kwa kuliangalia Neno la Mungu kwa makini tutajifunza namna ya kumwiga Yehova Mungu na pia namna ya kuvutwa tufanye hivyo.—Mt. 18:35; Efe. 4:32.
24. Ni kwa njia gani sala ilivyo msaada kwetu katika kumwiga Mungu?
24 Msaada mwingine wa kumwiga Mungu ni sala. Katika sala tunasema na Yehova. Tunamfungulia mioyo yetu, tukimwita nyakati za taabu, tunapokuwa na maamuzi makubwa ya kufanya, na vile vile kuzungumza naye mambo ya kila siku. Nasi twajisikia kutegemezwa naye, kuongozwa naye na kufarijiwa, kama vile mtunga zaburi wa Biblia alivyoahidi: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zab. 55:22) Kwa hiyo sala inatufanya tumjue Yehova zaidi na kutusaidia tumwige yeye.
MIFANO YA WAIGAJI WA MUNGU
25, 26. (a) Mfano ulio bora wa kumwiga Mungu ni upi, naye alifanya hivi kwa kadiri gani? (b) Ni mifano gani mingine myema ambayo Maandiko yanatusihi tuiige?
25 Tunasaidiwa pia tumwige Mungu na mfano wa wale ambao wenyewe ni waigaji wa Mungu. Bila shaka, mfano ulio bora ni Yesu Kristo. Kwa kweli, mojawapo ya sababu kubwa za kuja kwake duniani ilikuwa kumjulisha Baba yake wa kimbinguni kwetu sisi. Naye alimwiga Baba yake kwa ukamili hata Yehova Mungu angaliweza kutenda sawasawa na Yesu alivyofanya kama angalikuwa duniani. Ndiyo sababu Yesu angeweza kusema hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.”—Yohana 14:9.
26 Lakini wako wengine wanaosimuliwa katika Biblia waliomwiga Yesu Kristo kwa uaminifu kwa maana yeye alimwiga Mungu, nasi pia twaweza kusaidiwa tumwige Mungu kwa kuitazama mifano yao. (Ebr. sura ya 11) Mtume Paulo alikuwa mmoja, na ndiyo sababu angeweza kutia moyo kwa hekima hivi: “Iweni waigaji wangu mimi, kama vile mimi nilivyo wa Kristo.” (1 Kor. 11:1, NW) Kuuiga mfano wa watu hao wenye imani bila shaka kutatusaidia tumwige Yehova Mungu.
27, 28. (a) Ni kwa njia gani leo tunavyoweza kuwapata watu wanaomwiga Mungu? (b) Ushuhuda unaonyesha ni akina nani wanaomwiga Mungu kweli kweli leo?
27 Walakini, hatuwezi tukaazimia kwamba ni watu wa kale peke yao walioweka mfano mwema wa kumwiga Mungu. Wakristo wanazidi kushauriwa ‘wawakumbuke wale wanaowaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.’ (Ebr. 13:7) Wako watu wengi walio hai leo wanaopatanisha maisha zao na njia za Mungu. Kwa kushirikiana nao kwa kawaida waweza ukasaidiwa sana kuwa mwigaji wa Mungu. Hawa ni akina nani?
28 Kwa kuwa wanadamu ni viumbe vyenye kuiga vinavyoonyesha sifa za mungu vinavyomwabudu kwa njia mbalimbali katika maisha, njia ya kujua si kuwatafuta watu wanaojidai tu kuifuata Biblia, Neno la Mungu wa kweli, bali pia wanaofanya hasa inavyosema. Katika habari hii angalia ripoti iliyotolewa katika gazeti la Journal de Montreal la Julai 27, 1973, juu ya kusanyiko la kidini la zaidi ya watu 28,000 katika Montreal:
“Mashahidi wa Yehova ni watu wastaarabu sana sana. Adabu ndiyo njia yao ya maisha. Umalidadi, usafi, na heshima pia. Nalo hili lilionekana kwa vyepesi penye kusanyiko lao. . . . Hakuna mtu anayekukanyaga miguu, wala hukanyagi karatasi hata moja. Ni safi kweli kweli.
“Unajisikia kana kwamba ulikuwa katika paradiso, kwa maana hali ni ya kuburudisha, ya amani, na ya utulivu. Na kila mtu anavalia kwa adabu, hakuna anayejaribu kujionyesha wala kutaka atazamwe na watu namna alivyo bora kama inavyotukia katika michezo ya mpira wa vijiti.
“Na hasa, hakuna ubaguzi wa rangi. Watu wa mataifa yote wanafurahia kuwa pamoja. Hakuna aliye na makusudi yake mwenyewe yasiyofaa.
“Kwa kweli, kuna mengi ya kujifunza kutokana na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova. Mtu akiwatazama, atafikiri Amerika imebadilishwa!”
29. Kwa sababu gani ni muhimu tushirikiane sana na watu wanaomwiga Mungu?
29 Ndiyo, mashahidi wa Yehova ndio watu wanaomwiga Mungu leo. Kwa hiyo, ukishirikiana nao kwa kawaida, utasaidiwa sana ulitii onyo la mtume: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.” (Efe. 5:1, 2, NW) Katika nyakati zinazohitaji jitihada zilizoko mbele, huwezi ukatazamia kumwiga Mungu kwa uaminifu bila ya kujifaidi na misaada ambayo yeye ameitoa. Nako kushirikiana sana na wale wanaofanya mapenzi ya Mungu ni msaada wa lazima kuweza kupata uzima ukitazamia ukamilifu katika taratibu mpya ya Yehova yenye haki.—2 Pet. 3:13; Ebr. 10:24, 25.
[Maelezo ya Chini]
a Volume 16, ukurasa wa 207 (chapa ya 1970).
b Volume 14, ukurasa wa 81 (chapa ya 1959).
c Cha John Lawrence Von Mosheim, Volume 3, ukurasa wa 258 (chapa ya 1832).
d Tazama Awake! la Aprili 22, 1972, uone maandiko ya kuunga mkono kwa makanisa mataifa yenye kufanya vita mnamo vita vya ulimwengu.
[Picha katika ukurasa wa 395]
ILI ‘TUWE WAIGAJI WA MUNGU,’ TUNAHITAJI MENGI ZAIDI KULIKO KUWA NA “KITABU CHA UUMBAJI” TU; LAZIMA TUSOME BIBLIA TAKATIFU NA KUIELEWA