Lo Lote Ufanyalo—Hubiri!
“Katika kuenenda kwenu, hubirini.”—Mt. 10:7.
1. Kwa sababu gani ni lazima sana habari njema zihubiriwe wakati huu, na ni ulizo gani linalotokea juu ya kuhubiri huku?
TUNAPOTAZAMA hali zenye msukosuko karibu yetu katika ulimwengu, kuongezeka kwa uvunjaji wa sheria, wasiwasi kati ya vijana, huzuni kati ya jamaa, inaonekana wazi kwa njia yenye kusikitisha kwamba wingi wa wanadamu wanahitaji kuyajua mambo mema aliyoyaandika Yehova katika Neno lake, Biblia. Walakini, ulizo lililoulizwa zaidi ya miaka elfu moja na mia tisa iliyopita lingali larudiwa leo: “Tena wamsikieje pasipo mhubiri?” (Rum. 10:14) Wewe unapoyasoma maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu katika Maandiko Matakatifu, unadhani mhubiri anayetajwa ni nani? Je! unadhani inawamaanisha viongozi wa kidini au wengine wenye elimu au uwezo wa pekee?
2. Ni mfano gani mwema walioweka Wakristo wa kwanza, na je! kuhubiri ni kwa jamii fulani ya watu peke yao?
2 Kila mmojawapo wa Wakristo wa kwanza alijiona kuhusika katika jibu la ulizo hili, na ndiyo sababu kila mmoja wao akawa mhubiri. Bila ya kujali uhakika wa kwamba wengine ‘walikuwa watu wasio na elimu, wasio na maarifa,’ wote walijua kadiri fulani ya “habari njema” nao walikuwa na hamu nyingi kuzishiriki na mtu fulani, ye yote waliyeonana naye. (Matendo 4:13) The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries (New York; 1848, cha Dr. Augustus Neander, kilichotafsiriwa kutoka Kijeremani na Henry John Rose, ukurasa wa 41) kilisema hivi: “Kelso, mwandikaji wa kwanza mwenye kupinga Ukristo, anafanya mzaha, kwamba vibarua, washona viatu, wakulima, watu wasiokuwa na maarifa wa kimashamba, walikuwa wahubiri wenye bidii wa Injili.” Kwa hiyo, kuhubiri katika Ukristo wa kwanza hakukuwa kwa jamii fulani ya pekee tu, bali Wakristo wote walijiona wana wajibu wa kuwa wahubiri. Itapendeza kuchanganua namna ambavyo zaidi ya watu milioni moja na mia nane elfu wa namna zote za maisha, kutoka hali zote za elimu, wenye uwezo mbalimbali wamepata kuwa wahubiri wa habari njema leo.—1 Kor. 1:26-29.
KUPATA KUWA MHUBIRI
3. Ni mabadiliko gani yaliyotukia katika maisha za watu kwa sababu ya kazi ya kuhubiri?
3 Hapa twazungumza juu ya wale wahubiri wa Kikristo wanaojulikana ulimwenguni mwote leo kama mashahidi wa Yehova. Kabla ya kujifunza ‘habari njema za ufalme wa Mungu,’ wengi wa hawa walikuwa wamejitia katika matumizi mabaya ya dawa za kulevya, ulevi na njia nyingine za maisha za ufisadi. Wengine walikuwa wamenaswa katika mambo yenye hatari ya kibiashara nao walikuwa wenye wasiwasi mwingi na hangaiko kwa sababu ya kutikisika kwa uchumi na usalama wa fedha. Tena wengine walikuwa wakiishi maisha za vivi hivi tu, wasijue waelekeako na kila mara wakijiuliza hivi: “Kuna kusudi gani katika kuishi? Uzima ndio uu huu tu?” Haya yote yalibadilika kwa maana mtu fulani alikuwa na upendo wa kutosha kwa jirani yake kuweza kumhubiri kweli ya Neno la Mungu. Maisha yasiyo na lengo yenye wasiwasi yakawa na kusudi. Mvunjo na hangaiko ukawa tumaini. Wakiwa na uongozi huu mpya katika maisha, sasa wana furaha ya kuishi.—1 Kor. 6:9-11.
4, 5. (a) Ni hali gani ya wanadamu inayovuta Wakristo washiriki habari njema na wengine? (b) Upendo kwa Mungu unauhusuje wajibu wetu wa kuhubiri?
4 Je! wewe u mmoja wa wale waliofaidika hivyo? Hii yakufanya ujisikieje? Kwanza, bila shaka unajiona mwenye wajibu, wajibu wa kusaidia mtu mwingine katika njia ile ile uliyosaidiwa nayo. Lakini badala ya kujiona mwenye wajibu mgumu usiopendeza, je! moyo wako wenyewe haukuvutwa? Ndiyo, unawaona watu wengi sana waliomo katika hali ile ile uliyokuwa, nawe unawaonea huruma kama vile Yesu alivyofanya kwa watu wa siku zake: “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanavutwa na huruma hiyo kutaka kuwasaidia wanadamu leo.—1 Yohana 3:16; 4:11.
5 Zaidi ya upendo kwa jirani, upendo kwa Mungu ndio unaovuta Wakristo wa kweli wazihubiri ‘habari njema za ufalme wa Mungu.’ Kwa kweli, kupitia kwa Mwanawe yeye amewaamuru wafanye hivyo. (Mt. 24:14; Matendo 10:42) Wote wanaompenda Mungu kweli wanahubiri. Kama vile tusivyoweza kumlipa mtu mshahara ili aishi maisha mema, safi na manyofu kwa ajili yetu huku tukikosa kutii sheria za Mungu za adili, ndivyo tusivyoweza kumlipa “mhubiri” mshahara ili atuhubirie. Inampasa kila mtu achukue furushi lake mwenyewe la madaraka. Hakuna mtu anayeweza kuhubiri badala yetu. Ni wonyesho wa lazima wa upendo wetu kwa Mungu.—1 Yohana 5:3; Gal. 6:5.
6. Imetupasa tulioneje pendeleo letu la kuhubiri, na kwa kujifaidije wenyewe?
6 Kushika amri za Mungu juu ya kuhubiri, au jambo jingine lo lote, hakulemezi. Kula, kunywa, kulala na kupumua hakulemezi, na hali utii kwa sheria hizi za asili za Mungu ni wa lazima, kwa maana uzima wetu wategemea utii huo. Kwa Mkristo, kuhubiri nako ndivyo kulivyo kwa lazima. Ni jambo tunalotaka tulifanye, nayo ni furaha ya namna gani inayoletwa nako! Kujua kwamba mtu aweza kufanya alivyofanya Kristo Yesu na vile Mungu alivyoamuru kwa siku zetu kunaleta maoni ya ndani ya amani na uradhi usiolinganika. Ni furaha namna gani inayoletwa na kufikiri kwamba, hata bila ya wewe kujua, huenda mbegu ilipandwa ambayo pengine itafungulia mtu mwingine njia ajifunze kweli! Kuhubiri kwa uaminifu pia kunasaidia kuleta dhamiri safi, ambayo ni yenye thamani kubwa katika kuwa kwetu wenye furaha na amani ya akili sasa.
7. Huenda mambo gani yakamzuia mtu asihubiri lakini ni maoni gani yafaayo yanayohitajiwa?
7 Kati ya wale wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri leo wamo watu wasioelimika sana, wenye vipingamizi vya kimwili na matatizo mengine ambayo huenda wengine wakaona kama vizuizi, lakini wao hawakuyaacha mambo haya yawazuie wasimtii Mungu na kuonyesha upendo kwa jirani yao. Mmojawapo wa mashahidi wa Yehova aliyeishi katika mtaa wa mashambani maisha yake yote alikuwa mwoga na mwenye haya sana hata asingeweza kwenda dukani kujinunulia vyakula kwa maana aliogopa kukutana na watu. Mwanamke huyu alikuwa mwenye umri wa zaidi ya miaka 50 alipokuwa akijifunza kweli ya Biblia. Sasa anakwenda nyumba kwa nyumba akieleza watu asiopata kuwaona wakati mwingine wo wote habari njema alizojifunza. Sasa hilo ni jambo la kawaida tu analolifanya. Ikiwa twampenda Mungu na jirani yetu, ikiwa tutausahau uwezo wetu kutokana na maoni ya kibinadamu tumtumaini Mungu tu, twaweza kuwa wahubiri wa habari njema na kufurahia huduma yenye matokeo mazuri.—2 Kor. 3:5; Flp. 4:13.
8. Ni sifa gani inayohitajiwa ili kuhubiri, na kwa sababu gani?
8 Bila shaka, inahitaji imani kuu kuweza kusema kwa ujasiri juu ya kweli kutoka kwa Neno la Mungu, kwa maana, zijapokuwa habari njema, hazipendwi na wengi. Ujumbe huu mara nyingi unahitaji mabadiliko makubwa katika njia ya mtu ya maisha, na wengi hawapendi kubadili njia yao ya maisha. Huenda wakaudhihaki ujumbe au wakawa baridi. Tusipokuwa na imani twaweza kuacha kusema. Lakini, Wakristo wa kweli wanavutwa na imani ile ile iliyomvuta mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Lakini kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, Naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena.” (2 Kor. 4:13) Imewapasa Wakristo wa kweli wajiangalie wasizisahau kamwe njia nyingi walizo nazo za kudumisha imani yao kuwa yenye nguvu, wakijua kwamba imani inayodhoofika itawafanya wauache utendaji wao wa kuhubiri.
9. Moyo wahusikaje katika utumishi wetu unaofaa kwa Yehova?
9 Kwa hiyo basi, tumeona kwamba elimu ya kilimwengu na uwezo wa asili siyo matakwa ya kuwa mhubiri; bali, inampasa mtu awe na upendo kwa Mungu, upendo kwa jirani yake, na imani ya kweli yenye msingi wa maarifa ya kweli ya Neno la Mungu. Lakini sasa maulizo yanatokea: “Tutahubiria nani, wakati gani, wapi, na namna gani?” Jawabu kwa maulizo haya laonyeshwa na mtume Paulo, aliyeandika barua kwa wahubiri fulani wa Kikristo katika Rumi. Aliwaambia: “Mlitii kwa mioyo yenu.” (Rum. 6:17) Ndiyo, moyo ndilo jawabu la shauri hili. Kwa hiyo haikuwa lazima Paulo awape maagizo mengi ya waziwazi juu ya ni wakati gani, wapi na namna gani wanavyopaswa kuhubiri. Vivyo hivyo leo, ikiwa tutafanya yale tu moyo wetu unatuvuta tuyafanye, tutaanza kuzungumza na mtu fulani mambo tunayojifunza katika Biblia, na kwa hiyo tutakuwa tumekuwa wahubiri wa habari njema.
KUFIKIA WOTE
10. Ni njia gani yenye matokeo iliyo kuu ya kufikia watu waliyoitumia Wakristo wa kwanza?
10 Kama wahubiri wa habari njema, tamaa yetu imepaswa iwe kuwafikia wote watakaosikia. Siku za mitume Wakristo wote, vijana na wazee, matajiri na maskini, wakulima na wakaa mjini, walizihubiri habari njema. Lo lote walilolijua hao wafuasi wa nyayo za Kristo, juu ya huduma ya Yesu, kifo chake na ufufuo wake, waliwaeleza wengine. Kwa kweli, walitumia kila njia iliyokuwa wazi kwao kuwapelekea watu waliokuwa karibu yao ujumbe huu wa uzima wa milele. Walihubiri mashambani, mijini, masokoni, katika nyumba na po pote walipopata mtu mwenye kutaka kusikiliza. Hawakujificha katika nyumba ya watawa, wala wao hawakungoja wakati uliopangwa ufike ndio wahubiri siku fulani, kama vile viongozi wa kidini wanavyofanya nyakati za kisasa. Wakristo wa kwanza walivutwa moyoni wazitangaze habari njema chini ya hali zote. Yasemekana hivi juu ya mtume Paulo: “Basi katika sinagogi akahojiana na Wayahudi na waliomcha Mungu, na wale waliokutana naye sokoni kila siku.” (Matendo 17:17) Vivyo hivyo leo, kupenda watu kutatusaidia tuwe macho kutumia njia zote zilizo wazi za kufikia watu.—Marko 1:39; 6:56; Luka 8:1; 13:26; Yohana 18:20.
11. Ni njia gani ya kuhubiri watu inayofanya mashahidi wa Yehova wajulikane ulimwenguni pote?
11 Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wanaitumia kwa kufaa njia yao ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Mashahidi wa Yehova wanashiriki katika sehemu hii ya huduma yao katika vikundi au kama mtu mmoja mmoja, siku yo yote ya juma na karibu wakati wo wote wa siku. Mahali ambapo watu hawapo nyumbani wanakuwa waangalifu kupaandika kusudi jitihada zaidi zifanywe kumwona kila mwenye nyumba. Ambapo kupendezwa na Biblia kunaonyeshwa, ziara za kurudia zinafanywa na, iwezekanapo, mpango wa funzo la nyumbani la Biblia unaanzishwa.
12. Kuwa macho katika mafunzo ya Biblia mara nyingi kwaweza kutimiza faida gani zaidi?
12 Wakati wa kuongoza mafunzo ya Biblia katika nyumba za wanaopendezwa, nafasi zinatumiwa kwa faida kuwakaribisha watu wengine wa jamaa washiriki. Pengine pana mgeni nyumbani, kwa hiyo badala ya kuliahirisha funzo mpaka mgeni aondoke, sisi tunamkaribisha ashiriki katika funzo. Nyakati nyingi wageni wanatazamia wakaribishwe au wanapendezwa na kinachoendelea, kwa hiyo wanakubali ukaribishaji.
13. (a) Tuna nafasi gani katika kutoa ushuhuda kwa watu tunaofahamiana nao na jamaa? (b) Kwa sababu gani busara ni ya maana ili tuweze kuzitoa habari njema kwao kwa matokeo mazuri?
13 Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba wakiwa na vitabu fulani vya masomo ya Biblia nyakati zote, na ikiwa wako macho na wataitumia nafasi kwa ujasiri na busara, nyakati nyingine nyingi zapatikana ambazo wanaweza kushiriki habari njema. Kwa mfano, tunao watu tunaofahamiana nao na jamaa ambao twaweza kuonana mara kwa mara, na mara nyingi watataka kutusikiliza sisi kwa hiari zaidi kuliko mgeni. Kwa kweli, katika hali hizo kila wakati kuna hatari ya kukazia mambo mno na kujaribu kuwaambia mengi mno wakati ule ule. Tujapokuwa twawajua vema, si jambo la hekima kusema mengi mno yanayoweza kuwazuia wasiusikie ujumbe. Imetupasa tuwe wenye busara na huruma kwao kama tulivyo kwa wageni tunaokutana nao tunapokwenda nyumba kwa nyumba. Huenda tukaanza kwa mambo machache yaliyo wazi ya habari njema. Ikiwa hawaitikii kwa uchangamfu mara ya kwanza, hakuna haja ya kujitenga nao, bali twajaribu kuziweka wazi njia za kuonana kusudi ushuhuda zaidi uweze kutolewa wakati ujao. Kwa kupendezwa na marafiki na watu wa jamaa wengi wamepata kujifunza habari njema.
14. Je! twaweza kuhubiri kazini petu kwa uaminifu? Eleza.
14 Kazini petu nafasi zinajitokeza mara nyingi ambapo ujumbe waweza kutolewa. Kwa mfano, wakati wa chakula cha mchana shahidi wa Kikristo anaweza kuutumia wakati kusoma Biblia. Anaweza kuwa wa kwanza kuanzisha mazungumzo na mfanya kazi mwenzake na kutaja andiko linalopendeza, kama vile Zaburi 37:10, 11, linalosema kwamba bado kitambo kidogo waovu waharibiwe na wapole waishi duniani kwa amani. Maulizo kama vile, “Unafikiri utaiona siku hiyo?” au, “Wewe na jamaa yako mngependa kuishi wakati huo?” yanaweza kuelekeza mazungumzo kwenye tumaini la Ufalme kwa vyepesi. Bila shaka, haitupasi kuhubiri wakati ambapo tunapaswa kuwa tukifanya kazi, bali imetupasa tujue kwamba mfano wetu kama mfanya kazi mwema ni wa maana sana.
15, 16. (a) Twawezaje kuhubiri tunaposafiri? (b) Tuna nafasi gani za kuhubiri katika nyumba zetu?
15 Nyakati nyingine za kushiriki habari njema zinapatikana safarini. Wasimamizi wa mahoteli, wafanya kazi wa vibanda vya petroli, na wa mikahawa wote wanakihitaji ulicho nacho—habari njema. Anaposafiri kwenye kusanyiko la Kikristo mtu anaweza kueleza kwa urahisi kusudi la safari na pengine atoe nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Awake!, au, ikiwezekana, kitabu kama vile Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele. Anaposafiri katika gari la watu wote mtu anaweza kusoma vitabu vya Kikristo. Mara nyingi aliyekaa karibu yako atapendezwa. Au huenda ukamtolea aliyekaa karibu yako kitu cha kusoma safarini. Watu wengi wamejulishwa habari njema kwa njia hii. Bila shaka, inahitaji bidii kadiri fulani na kujitayarisha mapema kuweza kutumia nyakati hizi kuhubiri na kueneza vitabu vya Kikristo.—Yohana 4:6, 7, 13, 14.
16 Huenda wauza bidhaa wakafika nyumbani pako mara kwa mara. Waweza kuuliza kama hili, “Kuna wakati ambapo watu wanadhani wewe ni mmoja wa mashahidi wa Yehova?” Hii yaweza kuvuta mazungumzo yanayoweza kutumiwa kuzihubiri habari njema. Wengine wanaotembelea wanaweza kupewa nafasi ya kujifunza kweli kwa njia iyo hiyo. Twaweza kuuliza, “Je! wadhani tutakuwa na amani wakati wo wote?” au, “Unafikiri ni nini sababu ya kuwako uvunjaji mwingi sana wa sheria?”
17. Watoto wa shule, kwa sababu gani nafasi zenu za kuhubiri shuleni ni za ajabu sana?
17 Vijana wana nafasi nzuri ajabu ya kueneza habari njema kwa wasikilizaji wanaoelekea kuwapo nyakati zote. Wana shamba linaloelekea kutoguswa, mnamopatikana uelekevu wa akili mara nyingi. Kama unajifunza juu ya wakati ujao, wakati uliopita, au uliopo, Biblia ina mambo yawezayo kutiwa katika mazungumzo ya darasani na faraghani mara kwa mara. Vitabu vya Watch Tower Society vinazungumza habari za namna nyingi, na ukiwa macho, waalimu na wanadarasa pia wanaweza kujulishwa habari njema kupitia kwavyo.
18. Yawezekanaje kwa walio na vizuizi vya kimwili kushiriki katika kazi ya kuhubiri, na ni nani anayefanya tufanikiwe katika jitihada zetu?
18 Huenda likawa tatizo kubwa kwa walio wagonjwa au wenye vizuizi vya kimwili kuzitoa habari njema; hata hivyo, wanalishiriki pendeleo moja na Wakristo wenzao kama wahubiri. Wengi wao wanaandika barua, wanatumia simu, na hawaachi nafasi ipite bila kuzungumza na mgeni juu ya ahadi za Mungu. Unapokuwa hospitalini, wagonjwa wenzako, wauguzi, na madaktari wote wanaweza kujulishwa habari njema kwa busara. Huenda mashahidi hao wasioweza kutoka nje wasione matokeo ya mara hiyo sikuzote, hata hivyo ‘kupanda kwao na kutia maji’ kunaisaidia kazi ya kuhubiri sawa na kule kwa ndugu zao za Kikristo. Inawapasa wote wamtegemee Mungu akuze. Na sikuzote fahamu kwamba, bila ya kujali ni akina nani wanaosikiliza, tunafanya vile Mungu anavyotuambia tufanye. Tunakuwa waaminifu.—1 Kor. 3:6, 7.
KUHUBIRI KWA MFANO
19, 20. (a) Je! yawezekana Yehova asifiwe bila ya kusema neno lo lote? Kwa sababu gani wajibu hivyo? (b) Twawezaje kumsifu Yehova katika ujirani wetu wenyewe kwa mwenendo wetu?
19 Huenda watu wakajifunza mengi juu ya habari njema kwetu pasipo sisi kusema hata neno moja. Zaburi 19:1-3 yaonyesha namna hili linavyowezekana. Mstari wa kwanza na wa pili wasema hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.” Hii yasikika kana kwamba mbingu zinasema kweli juu ya Mungu, lakini kama vile mstari wa tatu unavyosema: “Hakuna lugha wala maneno, sauti yao haisikilikani.”
20 Ushuhuda usio wa maneno wa mbingu unasema mengi juu ya fahari ya Muumba wetu, na, vivyo hivyo, mfano wetu mwema mtaani ndivyo uwezavyo kusaidia sana kuieneza kazi ya kuhubiri. Njia hii ya kuenezea habari njema haipaswi kusahaulika. Huenda jirani zetu wasiwe waamini wenzetu, lakini ni wanadamu wenzetu nao wanastahili kufikiriwa ipasavyo. Neno jema au tabasamu zuri linasaidia sana. Wakati wa shida twaweza hata kuwasaidia kwa njia fulani, kama vile Yesu alivyowahurumia waliokuwa katika shida siku zake. Kuwafikiria kwa unyofu wanapokuwa katika shida kwaweza kuwafanya waone kwamba wako watu duniani wanaolifuata shauri la Yesu: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Zaidi ya huruma yetu ya kibinadamu, huenda wakaona kwamba tu malidadi na safi sana nyumbani. Huenda wakaona kwamba jamaa nzima twafanya kazi pamoja, na tu wenye furaha sikuzote. Kazini petu matumizi ya kanuni za Biblia yatufanya tutokeze kama wafanya kazi waaminifu, wenye bidii. Katika maisha yetu ya kila siku tunawahubiri waliomo mtaani kwa unyamavu. Sasa, wakati sisi au mmoja wa ndugu zetu za Kikristo atakapotembelea nyumba zilizomo katika eneo hilo akiwa na ujumbe wa tumaini la Kikristo, itikio tutakalolipata litaonyesha kwa kadiri fulani mfano uliowekwa. Je! wewe umemfanyia jirani yako nini karibuni hivi kitakachomfanya amsikilize shahidi wa Yehova atakayefuata mlangoni pake?—Gal. 6:10; Marko 10:13-16.
MATOKEO YA KUHUBIRI KWAKO
21. Ni uhakikisho gani tuwezao kuonyesha kwamba Yehova anakubariki kuhubiri kwa watu wake?
21 Huenda tunasoma Yearbook of Jehovah’s Witnesses na twaona kwamba makumi ya maelfu ya watu wanaiitikia kazi ya kuhubiri kila mwaka, na huenda tukashangaa, “Sababu gani hatuoni ukuzi wa haraka zaidi katika kundi letu?” Lakini unapoyachunguza mambo ya hakika waona nini? Angalia miaka mitano, kumi au ishirini iliyopita. Je! hakuna makundi zaidi, wahubiri zaidi wa habari njema katika eneo lako sasa kuliko waliokuwako wakati huo? Je! huwatembelei watu katika huduma mara nyingi zaidi sasa? Inatupasa tuwe wenye subira kama mkulima. Huenda tusione ukuzi kila siku, lakini upo. Tunabarikiwa kama tengenezo, na imetukia kama alivyotabiri Isaya kwa watu wa Yehova: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.”—Isa. 60:22; Yak. 5:7, 8.
22. Eleza sababu kwa nini haitupasi kuvunjika moyo ikiwa baada ya kuhubiri kwetu hatuwezi kuelekeza kidole moja kwa moja kwenye ‘barua yenye sifa.’
22 Lakini namna gani sisi kama watu mmoja mmoja? Je! uhakika wa kwamba hatuwezi tukaelekeza kidole kwa mtu katika kundi na kusema sisi wenyewe tulikuwa tukimsaidia mtu huyo afuate njia ya kweli unamaanisha kwamba Mungu haibariki huduma yetu? Sivyo! Kwa kweli, ni wangapi kati yetu wawezao kuelekeza kidole kwa mtu na kusema tulimleta katika njia ya kweli? Hasa inahitaji jitihada za ndugu wote kusitawisha shamba kwa kuhubiri kwao kwa uaminifu na kwa kuweka mifano myema mtaani, na, mwishowe, Yehova ndiye aletaye ongezeko. Nani ajuaye ni watu wangapi ambao huenda wewe ulisaidia wazijue habari njema? Pengine mfano wako mwema, kufika kwako mlangoni pao au barua uliyoiandika ndiyo kwanza iliyoamsha kupendezwa kwao. Huenda ikawa mtu mwingine ndiye aliyeongoza funzo la Biblia hasa kuongezea kupendezwa kwao na maarifa, lakini wewe washiriki katika hiyo ‘barua yenye sifa.’ Kwa kweli, watu wote wa Mungu wanaweza kuelekeza kidole kwenye mamia ya maelfu waliopata kuwa Wakristo waliobatizwa miaka ya karibuni kama uhakikisho wa kwamba mashahidi wa Yehova wametoshelea sana kuwa wahudumu.—1 Kor. 3:7; 2 Kor. 3:1-6.
23. Kwa sababu gani mashahidi wa Yehova wanaitanguliza kazi ya kuhubiri maishani mwao, nayo siri ya kufanikiwa kwao katika kuhubiri ni nini?
23 Tumeona kwamba ni amri kutoka kwa Mungu kwamba Wakristo wote wahubiri, bila ya kujali umri, ni wanaume au wanawake au elimu. Imeonekana pia kwamba kufanikiwa kwetu kama wahubiri kunategemea wingi wa upendo wetu kwa Mungu, ubora wa imani yetu, na wingi wa upendo wetu kwa wanadamu wenzetu. Tumeona pia kwamba ziko nafasi nyingi zilizo wazi za kuhubiri na kwamba haimpasi mtu avunjike moyo iwapo matokeo hayaelekei kuonekana moja kwa moja. Ustahimilivu wetu na mfano wetu mwema mtaani utachuma matunda. Matokeo ya kuhubiri kulikofanywa na mashahidi wa Yehova miaka iliyopita yamewatia moyo nayo yameliletea jina la Yehova heshima. Kwa hiyo, lo lote ufanyalo katika kuzihubiri habari njema, iendeleze kazi hii njema.
—Kutoka The Watchtower, Mar. 15, 1974.