Je! Biblia Yaweza Kukusaidia?
HUENDA maoni ya kwamba Biblia, kitabu kilichoandikwa karne nyingi zilizopita, yaweza kusaidia watu wayashinde magumu ya maisha leo yakasikika kama jambo la ajabu. Lakini imefanya hivyo. Biblia imesaidia hata watu ambao hali zao zilielekea kuwa zisizo na matumaini. Imewapa kusudi maishani na kwa hiyo sababu ya kuendelea kuishi.
Katika Netherlands mmojawapo wa mashahidi wa Yehova wa Kikristo (mwanamke) aliamka ulipokwisha kupita muda mrefu akiwa amezimia kwa kupatwa na ajali ya motokaa. Yeye aliharibika mwili na akili, akiwa na muda mfupi sana wa kuokoka na kurudiwa na fahamu. Lakini alianza kurudiwa na fahamu kidogo kidogo. Kisha akagundua kwamba ndugu yake, shemeji yake na mumewe, ambao wote vile vile walikuwa mashahidi wa Yehova, walikufa katika ajali ile ile ya motokaa iliyokuwa imemlemaza. Je! alikuwa na sababu ya kutaka aendelee kuishi?
Ndiyo, kwa maana alifahamu kwamba ahadi ya Biblia ya ufufuo inategemezwa na uhakika kamili. Yeye alisadiki kabisa kwamba angewaona jamaa zake waliokufa tena. Halafu, tena, hakuwa ameipoteza tamaa ya kusaidia wengine wafahamu kwamba, maisha yanakuwa yenye maana kweli kweli wakati mtu anapomtumikia Muumba, bila ya kujali hali. Yeye amejifunza kuandika na kusema tena. Ujapokuwa upande wake wa kulia umepooza, yeye anahangaikia utumishi wake kwa Mungu, kutia na kushiriki kweli ya Biblia na wengine. Ni kama yeye alivyosema: “Mimi namtumikia Yehova kwa kadiri niwezavyo. Ndiyo sababu nilijifunza kuandika kwa mkono wangu wa kushoto, kwa maana nataka nimtumikie Yehova. Kama nisingeendelea kumtumikia Yehova, ningemwaibisha mume wangu. Ndiyo sababu najitahidi kutoa ushuhuda nimletee Yehova heshima.”
Katika nchi ile ile mmojawapo wa mashahidi wa Yehova aliweza kusaidia mwanamume mmoja aliyekuwa karibu ya kufa apate sababu ya kuishi. Alipokuwa akitazama nje katika dirisha la nyumba yake jioni moja, Shahidi huyu aliona msukosuko wa watu upande mwingine wa barabara. Alihofu kwamba labda kulikuwa kumetokea ajali ya mtoto. Kwa hiyo alifanya haraka kuelekea mahali hapo. Hapo akaona mwanamume aliyekuwa amejinyonga naye sasa alikuwa amelala chini karibu ya kufa. Lakini uzima ulikuwamo bado katika mwanamume yule. Shahidi alimpepea upepo kwa haraka. Mwanamume yule akarudiwa na fahamu na kupelekwa hospitalini.
Mwanamume huyu alikuwa amejaribu kujiua kwa maana alikuwa amechoshwa na maisha. Hakuwa na tumaini kwa wakati ujao. Mambo yake ya kinyumbani yalikuwa katika hali ya kusikitisha naye mkewe ndiye aliyeisimamia nyumba.
Alipopona, akataka amjue Shahidi aliyekuja kumwokoa. Karibuni funzo la Biblia lilianzishwa na mwanamume huyu, mkewe na watoto wao watano. Pamoja na Biblia, kitabu “Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele” kilitumiwa kwa funzo hili. Habari iliyoangaliwa kwanza ilikuwa “Kujenga Maisha ya Furaha ya Jamaa.” Majuma machache yalipokwisha maisha ya nyumbani ya jamaa hii yaligeuka yakawa bora kwa maana wote waliiona hekima ya kutumia mashauri ya Biblia. Kwa furaha mwanamume huyu amepata maisha mapya.
Kwa kuwa Biblia imesaidia watu wakiwa katika hali mbaya sana, je! si busara kutazamia kwamba yaweza kukusaidia wewe ushinde magumu yawe ni makubwa au madogo? Je! mashauri ya Biblia juu ya yanayoweza kufanywa kuyaendeleza maisha ya jamaa na ujamaa wa mtu na wengine hayawezi labda yakawa yenye faida kwako? Mashahidi wa Yehova wangefurahia kukusaidia wewe katika funzo la Maandiko Matakatifu.