Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 10/1 kur. 438-443
  • Je! Wewe Ni Mtu wa Kiroho Kweli Kweli?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Ni Mtu wa Kiroho Kweli Kweli?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WEWE PIA WAWEZA KUWA MTU WA KIROHO
  • UJIFUNZE UPATE KUWA MTU WA KIROHO
  • SALA INASAIDIA KULETA UTU MZIMA WA KIROHO
  • DARAKA LA KUNDI KATIKA KUKUFANYA WEWE MTU WA KIROHO
  • Kikubali Cheo Kikuu Cha Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Inamaanisha Nini Kuwa Mtu wa Kiroho?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Kukomaa kwa Kikristo Ni kwa Lazima Ili Kupata Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Songa Mbele Ukiwa Mtu wa Kiroho!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 10/1 kur. 438-443

Je! Wewe Ni Mtu wa Kiroho Kweli Kweli?

“Sikuweza kusema nanyi kana kwamba kwa watu wa kiroho, bali kana kwamba kwa watu wa kimwili, kana kwamba kwa vitoto vichanga katika Kristo.”​—1 Kor. 3:1, NW.

1, 2. Kwa sababu gani tunapendezwa kujifunza namna ya kuwa mtu wa kiroho?

BIBLIA Takatifu inazungumza kwa kuwapendelea sana wale wanaoitwa watu “wa kiroho.” Kwa upande mwingine, haiwasifu wale wanaosimuliwa kama “wa kimwili.” Kwa hiyo, kwa wazi mtu mwenye kumcha Mungu anataka awe mtu wa kiroho, sivyo?​—Rum. 8:5-8; Gal. 5:16-18

2 Walakini, watu wengi wanaopaswa kuwa wa kiroho kwa kweli mara nyingi wanakuwa kinyume chake. Kwa sababu hii, Paulo mwandikaji wa Biblia wa karne ya kwanza, akilihutubia kundi la Kikristo katika Korintho, Ugiriki, alisema hivi: “Sikuweza kusema nanyi kana kwamba kwa watu wa kiroho, bali kana kwamba kwa watu wa kimwili, kana kwamba kwa vitoto vichanga katika Kristo.” (1 Kor. 3:1, NW) Kwa hiyo, je! twataka kweli kuwa wanaume na wanawake wa kiroho?

3. Maana yake nini kuwa mtu “wa kimwili”?

3 Ili kufahamu maana ya kuwa mtu “wa kiroho,” itasaidia kuyaelewa maneno yale mengine, “wa kimwili,” kama yalivyotumiwa na mwandikaji Paulo. Huku kuwa “wa kimwili” kuna maana gani? Maana yake ni kutawaliwa na mwili, yaani, kuwa na maoni ya kidunia, ya kilimwengu. Kuwaza huko ni kule kwa watu wasiokamilika, wenye dhambi; huku ndiko kumeijaa hii taratibu nzima. Watu wa kimwili wanaamua “kulingana na kanuni za kibinadamu.”​—1 Kor. 9:8, NW.

4. Maana yake nini kuwa mtu “wa kiroho”?

4 Lakini, kwa maana zaidi, maana yake nini kuwa “watu wa kiroho”? Maana yake ni kuwaza kama Mungu, ambaye mawazo yake yameinuliwa juu kupita yale ya mwanadamu. (Isa. 55:8, 9; Rum. 11:33) Uwezo huu wa kuwaza unawajia wale wanaowasikiliza wanenaji wa Mungu, hasa Yesu Kristo, ‘yeye aliyemfunua Yehova.’ (Yohana 1:18) Mitume wa Yesu Kristo ni mfano bora unaoonyesha namna ambavyo mtu aweza kuwa wa kiroho kweli kweli. Na tuchunguze polepole maendeleo yao ya kiroho.

5, 6. (a) Mitume walipataje kuwa watu wa kiroho? (b) Mazoezi ya Yesu yaliwapa mitume nini?

5 Kwanza, wale ambao Mungu alimpa Yesu kama mitume wote walikuwa watu wanyenyekevu, wenye bidii na waaminifu. Sifa hizi ziliwafanya wakuitikie kufundisha kwa Yesu. Walipokwisha kuchaguliwa wengine walifuatana naye daima kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili. Waliiona miujiza yake, wakasikia hotuba zake, wakapata nguvu zake, wakatazama njia yake ya kushughulika na rafiki na adui, na kuona kushikamana kwake na kanuni za haki. Kama vile Petro alivyosema miaka fulani baadaye: “Nasi tu mashahidi wa mambo yote aliyoyatenda.” (Matendo 10:39; Marko 3:14) Vile vile, aliwafundisha kwamba imewapasa wawaeleze wengine imani yao.

6 Mazoezi haya ya ajabu ndiyo yaliyowasaidia mitume kuwa watu wa kiroho. Yaliwapa “nia ya Kristo,” mawazo ya ndani, moyo na maoni ya Kristo, hivi kwamba wangeweza kuamua mambo kwa njia yake, ambayo pia ndiyo njia ya Yehova. Watu wa kiroho wanaona mambo kulingana na “maoni ya Mungu wetu.”​—1 Kor. 2:16; 1 Pet. 4:6; Yak. 1:27, NW.

WEWE PIA WAWEZA KUWA MTU WA KIROHO

7, 8. (a) Ili tuwe watu wa kiroho, lazima tusitawishe nini ndani yetu? (b) Je! ni akili tu ya mtu inayopaswa kubadilika?

7 Ili mtu aweze kuwa wa kiroho leo inahitaji mazoezi ya namna iyo hiyo kusitawisha ndani ya mtu mwenyewe “nia ya Kristo.” Hii inakuja kwa ‘kufanywa mpya katika nguvu yenye kuendesha akili ya mtu.’ (Efe. 4:23, 24, NW) Katika kawaida ya kila siku ya maisha, jambo ‘la asili’ kwa watu wasio na hali ya kiroho ni kushindwa na kuwaza kwa kimwili. “Nguvu” yenye kuendesha akili zao inawavuta kwenye upande unaofuatana na hii taratibu ya mambo ya kale. “Nguvu” au nia kuu ya akili ya Mkristo, hata hivyo, inapaswa ibadilishwe iwe kitu ‘kipya,’ hata mtu awaze kupatana na njia ya Mungu, hivyo akipata kuwa mtu wa kiroho.

8 Kuwaza kwa mtu kunapobadilika, kila upande wa maisha yake umepaswa pia ‘ufanywe mpya’; “utu mpya” unapaswa usitawishwe. Hata kama mtu amekuwa shahidi wa Kikristo wa Yehova kwa miaka mingi usitawi huu unapaswa uendelee na kujaa kila sehemu ya maisha ya mtu. Namna ambavyo Mkristo anajiongoza kazini au shuleni, usemi wake na tabia zake nyingine, vyote vimepaswa vionyeshe kuwaza kwa kiroho, “nia ya Kristo.” Lakini jambo gani linalotukia wakati mtu anapoacha kuwaza kwa kimwili kuyageuze maisha yake?

9, 10. Ni nini linaloweza kutokea wakati watu wanapojiacha wavutwe na kuwaza kwa kimwili, kama inavyoonyeshwa katika kundi la Korintho

9 Biblia inatoa mfano wa hili uliokuwa katika kundi katika Korintho, Ugiriki, karne ya kwanza. Wakorintho hawa walikuwa wamekwisha kuwa Wakristo. (1 Kor. 1:2) Lakini wengi walijiacha wavutwe mno na ulimwengu wa Kigiriki uliowazunguka. Ni kwa njia gani hasa ambavyo watu hao katika kundi walipata kuwa “wa kimwili”?

10 Wengine wao waliokuwa waalimu wenye kiburi na mitume wa uongo waliingiza kanuni za ulimwengu kundini. Mchafuko, ubaya na uovu vilipaswa vifuate bila shaka, vikiwafanya wengi wawe kama ulimwengu huo, wa kimwili. Pasipo shaka ulimwengu wa kale wa Kigiriki haukuwa wenye mfano wa Kristo. Kila jambo lililohusiana na utamaduni wake​—ufundi wake, sayansi, dini, michezo, filosofia​—lilikuwa la kidunia, la kimwili, la kibinadamu.

11, 12. Eleza namna kuwaza kwa kimwili kulivyozigeuza maisha za washiriki wengi wa kundi la Korintho.

11 Matokeo yalikuwa nini walipojaribu kuzipenyeza kanuni hizo kundini kidogo kidogo? Maoni yao ya kimwili yalionyeshwa na mambo mengi waliyoyafanya na kuyaamini. Isingefichika. Ilikuwa wazi kwa namna ambavyo waliwaona wengine kundini, wakimpa mmoja ukubwa kupita mwingine. Hii ilileta migawanyiko, roho ya madhehebu na baadaye mashindano. (1 Kor. sura 1-4; linganisha Yakobo 3:13-18.) Uasherati uliachiliwa. (1 Kor. sura ya 5) Walipelekana kortini. (Sura ya 6) Wakisisitiza haki zao wenyewe, walikaribia sana kukwaza wengine katika shauri la ibada ya sanamu. (Sura za 8-10) Kulikosekana ufahamu wa ukichwa ufaao katika kundi na pia ulafi ulikuwako kuhusiana na Chakula cha Bwana cha Jioni. (Sura ya 11) Ilimpasa Paulo awaambie kwamba hata wale washiriki ambao huenda ‘wakadhaniwa kuwa wanyonge zaidi walihitajiwa zaidi’ kundini.​—Sura ya 12, mstari 22.

12 Wajapokuwa waandikaji wa Kigiriki wa kilimwengu, wenye hekima ya kilimwengu na wa kimwili walisisitizia sifa “za kiume,” kama vile kiburi na majisifu, Mungu hafanyi hivyo. Iliwapasa Wakorintho kusitawisha upendo, upendo wa kimungu. (Sura ya 13) Hata maoni ya Wakorintho juu ya mafundisho ya Kikristo yalivutwa sana na kuwaza kwa kimwili. Kama vile Wagiriki katika Athene, wengine waliona ni vigumu kulikubali fundisho la ufufuo. ‘Wapumbavu’ hao walihitaji akili ya kiroho. (1 Kor. 15:12-57; Matendo 17:32) Je! hii haionyeshi kwamba kujaribu kuchanganya kuwaza kwa kilimwengu na mafundisho ya Kristo kunatokeza matokeo mabaya kwa vyo vyote? Imetupasa tuukubali ukweli huu katika maisha zetu wenyewe. Lakini awezaje mtu kusitawisha “nia ya Kristo” na kupata kuwa mtu wa kiroho kweli kweli?

UJIFUNZE UPATE KUWA MTU WA KIROHO

13. Kwa sababu gani kujifunza na kutafakari ni kwa lazima ili kuwa mtu wa kiroho?

13 Funzo la kawaida la Neno la Mungu ni la lazima, na pamoja na kujifunza kutafakari kunahitajiwa. Usikosee ufikiri kutafakari ni utaratibu usio na matendo. Kunahitaji jitihada ya hakika, yenye kusudi. Kusoma Biblia yenyewe kila siku kumepaswa kufanywe sehemu ya maisha yetu, kwa maana kwa kusoma huko twajifunza juu ya maisha ya Yesu na juu ya watu wengine wa kiroho waliokuwa na kibali ya Mungu. Lakini wakati unapaswa utumiwe kufikiria namna ambavyo shauri hili latumika kwa mtu mwenyewe, namna linavyomtenga mtu na ulimwengu. Kwa njia hii kuwaza kwa Mungu kunazidi kutiwa akilini mwetu, kukiachwa kugeuze au kuvute njia zetu zote za kuwaza kwenye upande ufaao. Baada ya kusoma sehemu ya Andiko, mtu aweza kujiuliza: “Nawezaje kutumia hili nisije nikarudia makosa ya zamani? Linaongezaje ufahamu wangu juu ya wema wa Yehova na kuzidisha ndani yangu tamaa ya kuwa kama yeye?”

14. Eleza maana ya Mithali 28:14.

14 Kwa njia hii twaona namna ya kumwiga Mungu wala si ulimwengu wa kimwili. Tunapovumilia kwa njia ya Kikristo tunapata kuufahamu ubora mwingi wa kuwaza kwa Mungu, nalo funzo la Neno lake linakuwa na maana nyingi zaidi kwetu. Tunajulishwa zaidi juu ya haja ya kumtumikia yeye kwa uangalifu. Kama vile Mithali 28:14 isemavyo: “Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote; bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara.” Tunasitawisha uchaji ufaao juu ya Mungu na kwa njia hiyo kuogopa kwa uaminifu mambo ya kilimwengu anayoyachukia Mungu. Tunapopata kuuona ukosefu wetu wa uwezo, twamtegemea Yehova zaidi. Kujifunza kwa uangalifu kunatufanya tuwe macho juu ya matatizo na mabadiliko yanayokuja ili yajapo yasitushangaze. Namna hii ya kujifunza inaelekeza akili zetu kwenye mambo yaliyo ya kiroho nasi tunakuwa “heri.”

15. Ikiwa tutakuwa watu wa kiroho, ni maelekeo gani yanayopaswa kuepukwa katika kujifunza?

15 Walakini, kujifunza kwa uangalifu kwapaswa kuwe juu ya mambo yaliyo ya kiroho kweli kweli. Watu wengine wanaojidai kuwa Wakristo wanajivunia elimu ya kibinadamu. Huenda roho ya kilimwengu ikapenya katika mafundisho yao ya Kikristo; ilifanya hivyo katika Korintho. Yesu aliwaambia hivi wale waliojaribu kuyafasiri maneno yake kwa njia ya kibinadamu: “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu.” Ujuzi na hekima yote ya kibinadamu, maandishi yake yote, filosofia na mafundisho, haviwezi kutegemewa kwa uzima. ‘Havifai kitu’ kama njia ya kupatia uzima wa milele. (Yohana 6:63) Kwa hiyo, sababu gani kutumia saa nyingi kuchungua maandishi hayo, yanayompa mtu maoni, si ya kimungu, bali ya kibinadamu, ya kimwili tu na kumfuatisha mtu na ulimwengu? Mtume Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Andiko lote liliongozwa na roho ya Mungu . . . Nakuagiza kwa uzito . . . lihubiri neno.”​—2 Tim. 3:16-4:2, NW; linganisha 1 Wakorintho 2:1-5, 13.

SALA INASAIDIA KULETA UTU MZIMA WA KIROHO

16. Kwa sababu gani sala ni ya maana sana kwa mtu anayetaka kuwa wa kiroho?

16 Sala pia ni msaada usiokadirika wa kuelekeza mawazo yetu kwenye mawazo ya Mungu. Mtu mnyenyekevu, anapozungumza na Yehova katika sala, anakumbushwa namna alivyo mbali na ukamilifu wa Mungu na haja yake ya kuondosha kuwaza kwake katika ulimwengu na kukuinua kuwe kama kwa Yehova. Kwa hiyo, “ombeni bila kukoma” ni shauri zuri. (1 The. 5:17) Yaani, zaidi ya kusali kwa kawaida nyakati zilizowekwa kando kwa sababu hiyo kundini au katika jamaa yako, sitawisha maelekeo ya kusali, wepesi wa kutafuta sikuzote uongozi wa Yehova mchana na usiku. (Linganisha Zaburi 119:62.) Je! wajua kwamba yale unayosali juu yake​—au unayokosa kusali juu yake​—yaweza kuonyesha kama una hali ya kimwili ya akili? Kwamba yaonyesha hivyo yaweza kuelezwa kwa mfano.

17. Namna gani na sababu gani huenda sala za mume zikazuiliwa akimdharau au akimtendea mkewe vibaya?

17 Mtume Petro aliyeoa anasema kwamba imempasa mwanamume ‘ampe mke wake heshima, kama chombo kisicho na nguvu,’ akishughulika naye kwa “akili.” Kwa sababu gani? Ili sala zake zisizuiliwe. (1 Pet. 3:7) Mkristo anayeshindwa kumhurumia mkewe kwa makusudi au kumpa uongozi unaohitajiwa hawezi kusema na Mungu kwa hiari akiwa na dhamiri safi. Bali, anajiona kulaaniwa, kukataliwa, akijua kwamba hatii amri ya Mungu. Anasita-sita kusema na Mungu waziwazi, na kwa sababu ya mwenendo wake usio wa Kikristo hawezi kutazamia kwamba Mungu atamkubali au kumtia nguvu katika mwendo wa kichoyo anaoufuata. Hii ingeweza kuleta msiba kwa kiroho. Ingeweza kumaanisha kukosa kupata roho takatifu, ambayo ni ya lazima ili kudumisha uaminifu. Halafu, kwa sababu ya hali yake iliyodhoofishwa, anaweza kufanya kosa zito, likihitaji kuchukuliwa hatua na kundi. Ndiyo, maisha yake mwenyewe yakiongozwa na kuwaza kwa ulimwengu, si kwa Mungu, yameigeuza sala yake kwa Yehova na hali yake katika kundi la Kikristo. Kuujua uvutano huu mwingi kati ya maisha yake ya faragha na uhusiano wake na Mungu katika sala kunamharakisha Mkristo mwenye ufahamu aelekee kwenye kuwaza na matendo ya kimungu nyakati zote.​—Luka 11:9-13; linganisha Yakobo 1:5-8; 1 Yohana 4:17.

DARAKA LA KUNDI KATIKA KUKUFANYA WEWE MTU WA KIROHO

18, 19. (a) Wazee katika kundi wanawezaje kutusaidia tuisitawishe “nia ya Kristo”? (b) Ni kwa njia gani mtu wa kiroho alivyo bora kuliko wa kimwili?

18 Ili awe mtu wa kiroho, na hivyo, awe tofauti na ulimwengu, mtu anahitaji ushirika wa kawaida pia na kundi la kisasa la mashahidi wa Yehova. Wazee wa kiroho, waliowekwa na tengenezo la Mungu la kitheokrasi, wanaweza kumsaidia mtu kwa kipekee. (Efe. 4:11-16) Iwapo maishani mwako mna dalili inayoonyesha kuwaza kubaya, baadaye kutaonekana waziwazi, kwa maana kosa lo lote lina njia ya kujidhihirisha kwa watazamaji mwishowe. (Gal. 6:7; 1 Tim. 5:24, 25) Wazee katika makundi ya mashahidi wa Yehova ni wanaume wenye ufahamu nao mara nyingi wanaona dalili za kuwaza kwa kimwili katika wengine. Wameagizwa ‘waangalie sana’ mtu ye yote ‘asiyethamini mambo matakatifu [“mwenye kuwaza ya kilimwengu,” New English Bible]’ asije akawa na matokeo mabaya juu ya kundi. (Ebr. 12:15-17, NW) Kwa sababu fulani​—mashirika mabaya, kazi ya kilimwengu au hali ya maisha​—huenda wewe mwenyewe ukose kuona mambo vizuri; huenda kuwaza kwako kukawa kwa kimwili kidogo.

19 Mtume Paulo alisema hivi: “Mtu wa kimwili hayapokei mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake; naye hawezi kuyajua, kwa maana yanachunguzwa kwa njia ya kiroho. Walakini, mtu wa kiroho anayachunguza hasa mambo yote, lakini yeye mwenyewe hachunguzwi na mtu ye yote.” (1 Kor. 2:14, 15, NW) Mtu anayesisitizia kuwa na maoni ya kimwili juu ya mambo hawezi kuuona ubaya wa hali yake mbele za Mungu. Lakini mtu wa kiroho, akiwa anapatana na kuwaza kwa Kristo, si kwamba tu anafahamu kusudi la Mungu lililofunuliwa kwa njia ya roho Yake, bali pia anauona mwendo wenye makosa wa mtu wa kimwili. Kwa hiyo, basi, tutasaidiwa tuepuke maelekeo ya kimwili tukiukubali msaada wa wazee katika kundi la Kikristo.

20. Je! ni wazee peke yao wanaotusaidia tuwe watu wa kiroho? Eleza.

20 Lakini kwa njia nyingi twasaidiwa kuwa wanaume na wanawake wa kiroho na mashahidi wa Yehova wote, si wazee peke yao. Tukichangamana nao, twaona kwamba sifa nzuri tunazozisoma katika Biblia, na zinazowatenga Wakristo na ulimwengu, ni sehemu ya utu wa watu wa Mungu leo. Zaidi ya hayo, wengi kundini wana tabia au uwezo wao wenyewe wenye kutokeza. Mmoja ni mkarimu, mwingine mwenye maarifa, na hata mwingine ni mwenye kufahamu sana hali za watu pasipo kuambiwa. Halafu, wako wale ambao huenda wakaelekea kuwa watu “wa kawaida tu.” Lakini tunapopata kuwajua, na jitihada iliyowapasa kutia wadumishe imani yao, je! hatuvutwi karibu nao? Huenda hata tukaona kwamba watu hawa “wa kawaida tu” wamekwisha shinda matatizo yale yale yanayotukabili. Ushirika huu wa karibu unapaswa usitawishe ndani yetu sifa kama uchangamfu, upole na unyenyekevu. Sifa hizi njema zinasitawishwa zaidi mtu anaposhiriki na kundi katika kufundisha watu wengine “habari njema hizi za ufalme” katika huduma ya shambani.​—Mt. 24:14, NW.

21. (a) Ni hatari gani inayopaswa kuepukwa inayoonyesha hali ya kimwili ya moyoni? (b) Zitaje sifa moja moja za utu wa kweli wa Kikristo.

21 Bila shaka, mtu anapojitahidi asitawishe utu mpya inampasa ahakikishe kwamba tabia anazozichukua ni za kiroho kweli kweli. Kwa mfano, mtu anayedhani ni “wa kiroho” ati kwa sababu anaonyesha kwa uso wake kwamba ni mchaji wa Mungu, au anayejinyima mengi sana ili aonekane kuwa “mwenye haki” mbele ya wengine, ni mnafiki hasa. (Mt. 6:5-8) Paulo anaonyesha katika Wakolosai 2:16-23, NW, kwamba wale wanaopendezwa na “namna ya ibada ya kujitungia wenyewe na unyenyekevu wa uongo, [au] kuutesa mwili,” kwa kweli wana “hali ya kimwili ya moyoni.” Tamaa ya kiburi ya kusifiwa ndiyo inayoongoza kuwaza kwao, si unyenyekevu wa kweli wa moyoni. Utu wa kweli wa Kikristo unaelezwa kwa urefu baada ya hapo na mtume Paulo katika Wakolosai 3:5-15:

“Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu: kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu. Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba. . . . Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu. Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani.”

22, 23. Maisha ya Petro yanaonyeshaje kwamba kuwa mtu wa kiroho hakuhitaji kwamba mtu awe mkamilifu?

22 Kuwa mtu wa kiroho kweli kweli kunahitaji jitihada. Usife moyo unapojitahidi kusitawisha “nia ya Kristo.” Kumbuka, sababu tu ya kuwa mtu ni wa kiroho haimaanishi kwamba yeye hafanyi kosa katika jambo lo lote na kwamba matatizo yake yote na maelekeo yanatoweka. Matukio machache maishani mwa Petro yaonyesha hivi, Wakati mmoja Petro alijibu ulizo la Yesu kwa usawa, “Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?” Maoni yake ya kiroho yalisifiwa, Yesu akisema, “Mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni.” Lakini, angalia kwamba baada ya hapo Petro alipojaribu kumwonyesha Yesu fadhili isiyofaa, aliambiwa hivi: “Huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.” Kuwaza kwa kimwili kungali kulipaswa kupambanwa nako!​—Mt. 16:15-23.

23 Muda unaopungua mwaka mmoja baadaye, Petro alihuzunika alipomkana Yesu mara tatu kwa sababu ya kumwogopa mwanadamu. Alitubu. Lakini je! haya maelekeo ya kugeuka-geuka kwa kukazwa na kundi la watu yalitoweka? Sivyo. Miaka mingi baadaye ilikuwa lazima Petro aonyeshwe kosa tena, wakati huu na Paulo, kwa sababu ya udhaifu ule ule. (Luka 22:34, 54-62; Gal. 2:11-14) Yaelekea kwamba ilimlazimu Petro, mtume, mtu wa kiroho, ajitahidi maisha yake yote akijaribu kuuondoa udhaifu huo. Paulo, pia, anatuambia kwamba ilimpasa ajiadibishe mwenyewe adumishe matendo yake kuwa yanayofaa. (1 Kor. 9:24-27) Kwa hiyo, leo, huenda mtu wa kiroho akawa na udhaifu wake, lakini kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii sana na kulitumia katika maisha yake na kuitegemea roho ya Mungu yenye kutia nguvu aweza kusaidiwa aushinde.

24. Kuna jambo gani zaidi juu ya kuwa mtu wa kiroho tutakalolizungumza?

24 Lakini kuna jambo kubwa la kufikiria kwa habari ya kujionyesha kuwa mtu wa kiroho kweli kweli. Hilo ndilo nini? Nia ya kuukubali upinzani wote unaoletwa juu ya wafuasi wa nyayo za Kristo Yesu na ulimwengu wa kimwili. Wajua, ulimwengu hauwapendi wale wanaoidhihirisha “nia ya Kristo.” Lakini wewe waweza kuivumilia chuki yake kwa furaha kuu na uradhi ukitaka. Jifunze ni kwa njia gani katika makala ifuatayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki