Je! Uwepo Mtengano wa Wazazi na Watoto Katika Nyumba ya Kikristo?
“Mwache Kufanyizwa Kulingana na Mtindo wa Taratibu hii ya Mambo.”—Rum. 12:2, NW.
1. Habari mbalimbali zinasema nini juu ya mtengano wa wazazi na watoto ulioenea sana?
MWANAHISTORIA Arnold Toynbee alisema, “Jambo lililonishangaza mimi ni mtengano unaozidi kupanuka kati ya watoto na wazazi wao.” Mtajo huo juu ya mtengano wa wazazi na watoto ni jambo linalosikika sana katika habari leo. Mtengano wa wazazi na watoto si jambo la kuwazia tu. Ni uhakika wenye kutatiza wa hii taratibu ya mambo. Unapatikana katika sehemu nyingi za ulimwengu, kama vile Ulaya na Asia, si katika Amerika ya Kaskazini tu. New York Times lilisema, “Mtengano wa Wazazi na Watoto katika Japan Unaelekea Kuwa Mkubwa Sana.” Na makala ndefu katika gazeti la Urusi Pravda ilisema kwamba mtengano wa wazazi na watoto ni tatizo kubwa la jamii ya Urusi. Mwanasayansi anayeshughulika na mambo ya kijamii Margaret Mead anazungumza juu ya “mtengano mwingi wa wazazi na watoto usiopata kuonekana hapo kwanza ulimwenguni pote.”
2, 3. (a) Mtengano wa wazazi na watoto ni nini? (b) Je! uwepo mtengano wa wazazi na watoto katika nyumba ya Kikristo? Kwa sababu gani?
2 Mtengano huu ni nini hasa? Ni mtengano au kuharibika kwa kupashana habari na kuelewana kati ya vijana na watu wazima. Vijana wengi wanaona kwamba watu wazima wamefanya ulimwengu wenye msiba na kwamba lazima iwepo njia bora na kwamba lazima waitafute. Mara nyingi vijana hawa wanaasi lo lote ambalo wazee wanalipenda au kuliunga mkono. Kwa upande mwingine, wazee wanaelekea kuona kwamba vijana wengi wanafuata yao wenyewe, wameharibika, ni wachoyo na wasio na shukrani. Hivyo mtengano unaleta tofauti kubwa ya kuwaza kati ya wazazi na watoto.
3 Bila ya kujali mtengano huu umeenea ulimwenguni pote kwa kadiri gani, namna gani juu ya nyumba za Kikristo? Je! uwepo mtengano uu huu katika nyumba ya Kikristo ati kwa sababu tu hii taratibu ya mambo inao mtengano wenye kufadhaisha? Basi, je! Wakristo wa kweli ni sehemu ya ulimwengu? Yesu Kristo alionyesha wazi sana kwamba imewapasa Wakristo wawe “si wa ulimwengu.” (Yohana 15:19) Kwa hiyo ikiwa wewe u Mkristo wa kweli, uwe kijana au mzee, hutaki uushiriki mtengano huu nyumbani mwako, sivyo?
4, 5. (a) Kuna hatari gani kwa Wakristo vijana, na kwa hiyo imewapasa watii shauri gani? (b) Ni ulizo gani la maana linalotokea sasa?
4 Lakini ni lazima tukubali kwamba vijana wa Kikristo, na watu wazima vile vile, wanaweza kuvutwa na watu wa kilimwengu walio karibu yao. Kuwaza kwa kilimwengu kwaweza kuingizwa, na, mtu asipojihadhari, aweza kufanyizwa kulingana na mtindo wa hii taratibu ya mambo. Kuna hatari kwa Wakristo, na yaweza kuhitaji jitihada nyingi. Haipaswi kudharauliwa. Ni kushindana na maoni ya kilimwengu, miradi na tamaa za makuu na kuiga watu wa kilimwengu, wawe ni vijana au wazee. Hasa imewapasa Wakristo vijana wayatii maneno ya mtume wa Kikristo Paulo, aliyeonya hivi: “Msiige njia ya ulimwengu huu.”—Rum. 12:2, tafsiri ya Lamsa.
5 Sasa, ninyi vijana wa Kikristo mwawezaje kusaidiwa katika kushindana huku msije mkafanyizwa kulingana na mtindo wa dunia na kuja kutengana na wazazi? Katika kutafuta jibu kwa ulizo hilo, ni vema kuzichunguza sababu za mtengano huu.
MABADILIKO MAKUBWA NI SABABU
6, 7. Ni mabadiliko gani yaliyoshiriki kuleta mtengano wa wazazi na watoto?
6 Mabadiliko makubwa na matukio ya miaka 50 au 60 iliyopita ni sababu kubwa ya mtengano kati ya wazazi na watoto. Vijana hawakupata kuona mabadiliko ya haraka haraka hivyo hapo kwanza. Nusu karne iliyopita kulikuwa kungali na farasi wengi na magari yao wakitumiwa, na maisha hayakuwa ya msukosuko. Maendeleo ya ndege za abiria yameifanya dunia kuwa ndogo hata safari ya kutoka bara moja mpaka nyingine inachukua saa chache tu. Maendeleo mengine ya ufundi yanawezesha wanadamu watembee mwezini, na kusema nasi wakati wanapofanya hivyo.
7 Na yamekuwako mabadiliko makubwa ajabu katika mawasiliano na pia katika mambo ya kujifurahisha. Radio na televisheni zimetokea katika kipindi iki hiki. Vyote viwili ni vifaa vyenye nguvu vya waeneza propaganda na wataalamu wa akili ya wanadamu. Asema hivi Hakimu wa muda mrefu wa Mahakma ya Vijana P. Gilliam wa Portland, Oregon: “Kumalizika kwa kupashana habari ndiyo sababu kubwa ya uasi. Katika kila . . . nyumba mna televisheni—jeuri ya ghafula mahali pote.” Uvunjaji wa sheria haukuwa ndilo tatizo kubwa miaka 50 iliyopita kama ulivyo leo. Ufisadi haukuwa umeenea sana.
8. Muziki upendwao na wengi wauonyeshaje mtengano wa wazazi na watoto, na ni nini maoni ya Maandiko juu ya mwingi wa muziki huo?
8 Fikiria, pia, mabadiliko katika muziki upendwao na wengi. The National Observer kilisema, “Pengine hakuna kitu kinachoonyesha mtengano kati ya wazazi na watoto kwa njia ya kushangaza zaidi kuliko muziki mpya.” “Unaonyesha uasi mwingine wote wa vijana juu ya utaratibu uliowekwa—“hippie movement,” matumizi ya dawa za kulevya, mateto ya kijamii . . . kukataa dini kulikoenea sana na desturi za adili, kuchukia vichana vya nywele sikuzote, vinyozi na maduka ya mapambo.” Si kwamba tu kuna mdundo wa sauti ya juu, bali maneno ya nyimbo nyingi za rock ‘n’ roll yanamkufuru Muumba, yanadharau wazazi sana, yanafundisha uasi, yanatia moyo ufisadi na matumizi ya dawa za kulevya zilizo hatari. Kama vile usemavyo wimbo mmoja: “Kuishi kwa ajili ya leo maana huenda kesho isiwepo.” Hivyo wengi wa mabingwa wa muziki wa, rock ‘n’ roll na wale wawapendao wanashiriki kule ambako mwandikaji mmoja alikuita “kutoujali wakati ujao kwa uwazimu.” Bila shaka, hii ndiyo “hekima” ya hii taratibu ya kale, inayosimuliwa na Biblia katika Yakobo 3:15 kama “ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani.”
9. Ni nini lisilofichika kwa vijana, na vijana wengi wanatendaje kwa sababu ya hali za sasa zisizopendeza?
9 Kwa hiyo mabadiliko haya yote na matukio yamewageuza vijana sana. Vita vya ulimwengu viwili vimekipata kizazi hiki, nao uhakika huu haufichiki kwa vijana. “Tumekuwa na vita vya ulimwengu viwili—makosa mawili yenye maangamizi—nao vijana wanajua hivyo,” alisema waziri wa mashauri ya nchi za kigeni, Carlos P. Romulo. “Wanataka kufanyiza ulimwengu wao wenyewe kulingana na matumaini yao wenyewe. Vijana wa leo wanaishi katika kiitwacho “kizazi cha jeuri” isiyopata kuonekana hapo kwanza, nayo jeuri hii yaendelea kuongezeka. Ili kuondosha machukio ya ulimwengu, vijana wengi wanafanya machezo ya mapenzi au wanatafuta kuepuka matatizo maishani kwa kutumia dawa za kulevya. Wanadharau Ujamii kwa kufuata inayoitwa “adili mpya,” ambayo si adili hata kidogo. Vijana wengi wa ulimwengu wanataka kuasi “kanuni” za zamani za mwenendo wa kijamii.
KUSHINDWA KWA WATU WAZIMA NI SABABU
10, 11, (a) Ni nini sababu kubwa ya mtengano wa wazazi na watoto, kama vile vijana wenyewe waionavyo? (b) Ni maoni gani ya watu wazima ambayo yameshiriki kuleta mtengano wa wazazi na watoto?
10 Ni wazi kwa vijana kwamba watu wazima kwa ujumla wameshindwa kuwekea vijana mfano bora. “Twauona ulimwengu kama mngurumo mkubwa unapopita kasi ukiwa na vita, umaskini, chuki isiyo na sababu, na kukosa kuelewana kati ya watu na mataifa,” kaandika mvulana wa Texas wa miaka kumi na mitano. Katika insha hii mvulana huyu anaendelea kusema hivi, “Twawaona watu wenye kubishana wakipiga mbio sana wakijaribu kumfukuza mwenzao. Haya yote yanaongezeka, yakileta msukosuko kati ya mataifa na nyumbani.” Hivyo kushindwa kwa watu wazima ni sababu kubwa ya mtengano wa wazazi na watoto.
11 Kwa mfano, watu wazima wengi wajapokuwa wanajidai kuwa Wakristo, wameiacha Biblia; ikiwa wanaisoma wanaisoma mara chache sana nao hawazifuati kanuni zake. Kwa hiyo ni sababu gani ya kuichunguza Biblia wanayowapa watoto wao wazazi kama hao? Zaidi ya hayo, vijana wanasikia viongozi wa kidini wa namna zote za madhehebu za kidini wakiirahisisha Biblia, kuizungumza kama “hadithi ya uongo,” na kadhalika. Mwanahistoria Arnold Toynbee alisema: “Zamani, tuliambiwa kweli. ‘Hii ndiyo Biblia, hii ndiyo kweli juu ya Mungu na ulimwengu.’ Sasa, hatuijui kweli juu ya mambo ya maana zaidi. Watoto watatilia mambo mashaka kwa maana wazazi wao wanatilia mambo mashaka.”—Look, Machi 18, 1969.
12. Mwanafunzi mwenye umri wa miaka kumi na saba alisema nini juu ya kizazi kilichopo cha watu wazima na dini yake ya kilimwengu, nayo hii yahusianaje na mtengano wa wazazi na watoto?
12 Unafiki wa watu wazima wengi ndio unaotatiza vijana wengi. Mwanafunzi wa miaka kumi na saba wa shule ya masomo ya juu alitoa maelezo juu ya jamii hii ya kilimwengu. Akiandika katika Chicago Tribune la Aprili 26, 1970, kijana huyu alisema hivi, chini ya kichwa “Sauti ya Vijana”:
“Vijana wanazigundua kwa vyepesi kanuni za udanganyifu za wazee wao. Siku sita kwa juma wanawaona wakitamani waziwazi au kwa njia isiyo ya wazi, wakisema uongo, wakiiba, na kuabudu mungu wa uongo, dola yenye nguvu zote (sarafu ya Amerika). Halafu, Jumapili au Jumamosi inafika, watu awa hawa wanakuwa waangalifu kwa saa moja hivi wanapohudhuria katika ibada. Wakati uliobakia wa siku wanaendeleza njia za kinafiki. . . . Nyakati nyingine wazazi hata hawafichi kwamba wao ni wa dini fulani kwa sababu tu wanataka waheshimiwe na watu au waepuke kulaumiwa na wenzao. Mashaka ya vijana juu ya dini yanatokana pia na mambo wanayoyaona kwa ujumla. Matengenezo mengi mbalimbali ya kidini yenye maoni yenye kupingana, kila moja likijidai kuwa ndilo kanisa lililochaguliwa, yanamfanya hata kijana mwenye malezi ya kidini atilie mashaka ubora wa kufuata maisha ya kidini.”
Hivyo unafiki na mapingano ya dini ya kilimwengu hayakosi kuonekana na vijana, nako kushindwa huku kwa dini na watu wazima kunaupanua mtengano wa wazee na vijana. Wanapoyaona mambo haya, vijana wanafuata njia nyingine, wakitafuta njia bora ya maisha.
DARAKA LA VIJANA
13. (a) Kijana aliye bingwa kama mwanasinema anausimuliaje mtengano uliopo wa wazazi na watoto, na kwa hiyo ni furaha gani inayokosekana? (b) Kwa kufuata njia yao wenyewe, je! vijana wameipata furaha wanayoitafuta, na namna gani juu ya tumaini wakati ujao?
13 Lakini wanapofuata njia yao wenyewe na kutafuta jambo tofauti, je! vijana wameiona furaha wanayoitafuta? Sivyo kabisa, na katika mtengano unaopanuka wa wazazi na watoto wao wanaikosa furaha ya kupashana habari na wazazi wao. Mtengano kati ya wazazi na vijana umepanuka sana hata inaelekea kutowezekana kupata njia ya kupashana habari kwa wazazi na watoto katika jamaa nyingi. Kama vile mwanasinema aliye bingwa wa Hollywood wa miaka 22 alivyosema: “Hakuna matumaini sasa kati ya wazazi wangu na mimi. . . . Tungali twapashana habari, lakini tunalaumiana. . . . Kuna mtengano mkubwa ajabu, nao wanadhani kizazi changu kina wazimu.” Lakini twauliza: Bingwa huyu wa kike na wengine walio kama yeye wanafaidi nini kutokana na “mapenzi ya hiari” yao na maoni yaliyo tofauti juu ya mambo? Je! wana amani ya akili pamoja na uradhi? Je! wana tumaini la wakati ujao? Msichana uyu huyu alisema hivi: “Leo nina hofu ya kuwa mwenye umri wa miaka 30. Wazo la uzee, na zaidi wazo la kufa, linanivunja moyo. Na kwa kuwa mimi si mwanadini, sina tumaini nitakapokufa.” Je! hii yasikika kama njia ya kupata furaha?
14, 15. (a) Vijana wa Kikristo wana maoni gani tofauti juu ya wakati ujao, na ni kauli gani tofauti wanazokata? (b) Ili wawe na wakati ujao ulio mzuri ajabu, imewapasa vijana wa Kikristo waepuke nini, hii ikihitaji jitihada gani?
14 Ni tofauti namna gani na kijana wa Kikristo, kwa maana yeye analo tumaini la kuishi milele katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki! (2 Pet. 3:13; Ufu. 21:3-5) Yeye hana hofu ya kuwa mwenye umri wa miaka 30! Sababu gani awe na hofu? Yeye analo tumaini la umilele wa wakati mbele yake, ikiwa atamtii Muumba wake sasa na kuendelea kufanya hivyo. (Mhu. 12:1, 13; Tito 1:2) Zaidi ya hayo, anaweza kuuona unafiki wa njia ya maisha ya kufuatia vitu vya kimwili ambayo watu wa ulimwengu huu wamejifanyizia. Lakini inampasa Mkristo akate kauli tofauti na za vijana wa ulimwengu. Yeye anajua kwamba “shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha” na kwamba watu wengi ‘wamejichoma kwa maumivu mengi’ kwa kupenda fedha na vitu itakavyovinunua. (1 Tim. 6:10) Pia anakirihi chuki na jeuri, naye anaonyesha hivyo kwa kuwatendea wengine mema, hata kuwapenda adui zake, wala si kwa ajili ya kupata raha ya kichoyo ya tamaa zake mwenyewe.—Gal. 6:10; Mt. 5:44; Kol. 3:5.
15 Kwa hiyo wakati ujao wa vijana wa Kikristo utakuwa mzuri ajabu ikiwa wataiepuka “roho ya dunia” na mtengano wake kati ya wazazi na watoto! (1 Kor. 2:12) Walakini, hii yamaanisha jitihada nyingi kwa vijana. Inawapasa wajitahidi sana kushindana na maelekeo, majaribu, vishawishi, mivuto na mikazo ambayo huenda wazazi wao hawakupatwa nayo walipokuwa vijana. Ni lazima sasa ‘kuishindania imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu’ kuliko wakati mwingine wo wote.—Yuda 3.
16, 17. (a) Daraka kubwa la kuepukia mtengano wa wazazi na watoto linamkalia nani? (b) Imewapasa vijana wa Kikristo waoneje mambo wapate kuepuka mtengano na wazazi wao na matokeo yake yenye msiba?
16 Kwa kweli daraka kubwa la kuepukia mtengano wa wazazi na watoto nyumbani linawakalia vijana. Basi, je! ninyi mlio vijana wa Kikristo mtalichukuaje daraka hili? Kwanza, mfanye vile mtume Paulo asemavyo katika Warumi 12:2, NW: “Mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo, bali mgeuzwe kwa kubadili akili zenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Hii inahusu namna unavyoona mambo. Nia yako ni nini juu ya kufuatia vitu vya kimwili? Wayaonaje matumizi ya dawa za kulevya kwa sababu ya kupata raha tu au kama njia ya kuyaepukia matatizo ya ulimwengu? Wauonaje ufisadi na fujo za jamii ya kisasa? Wauonaje muziki na kujifurahisha kunakotafutwa na vijana wa ulimwengu?
17 Haikupasi na huwezi kuyaona mambo haya kama vile watu wazima na vijana wa hii taratibu mbovu ya mambo wanavyoyaona mambo. “Mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo [katika kuwaza kwenu].” Kuzuie kuwaza kwa kilimwengu na mikazo yake: “Msiuache ulimwengu uwazungukao uwafinyange katika umbo lake.” (Rum. 12:2, tafsiri ya J. B. Phillip) Kufanyiza kuwaza kwako kulingana na Neno la Mungu ndiyo hatua ya maana zaidi ikiwa wataka kudumu katika “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu” na kuepuka mtengano kati yako na wazazi wako.—1 Pet. 1:14-16; Efe. 4:22-24.
18. Imewapasa vijana wafuate shauri gani jema ikiwa wanataka wafanikiwe?
18 Enyi vijana mtakao kufanya mapenzi ya Mungu imewapasa msitawishe upendo wa Neno la Mungu Biblia. Mjifunze, myatafakari lisemayo, mweke hazina ya kweli zake, mzitii amri zake na kuishi kulingana na kanuni zake za haki. Mfanye kama vile Mithali 3:5-7 isemavyo: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; mche [Yehova], ukajiepushe na uovu.” Maana yake nini ‘kumkiri Yehova’ katika njia zako zote? Maana yake ni kumkubali Yehova, hasa kwa kufanya ayasemayo tufanye, kuzifuata njia zake. Ukifanya hivyo, atayaongoza mapito yako nawe utafanikiwa na kufurahia kibali ya kimungu.
19. Nia ya vijana wa Kikristo imepaswa kuwa nini juu ya maovu ya hii taratibu ya kilimwengu?
19 Ukilifuata shauri hilo, hutakuwa mwasi kwa sababu ya maovu mengi ya hii taratibu ya mambo. Wajua vema kwamba hii taratibu mbovu ya mambo haiwezi kugeuzwa, kwa hiyo hakuna haja ya kuwaka kwa hasira na kujitia katika mateto ya jeuri. Bali, lisikilize na kulifuata shauri lenye hekima la Zaburi 37:8, 9: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya. Maana watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao [Yehova] ndio watakaoirithi nchi.”
JIFAIDI KUTOKANA NA WAZEE KATIKA TENGENEZO LA MUNGU
20. Imepaswa nia ya vijana wa Kikristo iwe nini juu ya wazazi wao “katika Bwana” na wazee katika tengenezo la Mungu?
20 Je! nyie vijana mumo kati ya “wamngojao [Yehova],” ambao karibuni ndio “watakaoirithi nchi”? Ikiwa ndivyo, kuna amri nyingine ya Biblia isiyowapasa kusahau. Katika Waefeso 6:2, 3 vijana wa Kikristo wanaambiwa: “Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia.” Hili ni la maana hasa ikiwa baba yako na mama yako ni wafuasi wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, walio wakf na waliobatizwa kwa maana wao ni sehemu ya jamii ya watu wazima ya tengenezo la Mungu ambao 1 Petro 5:5 inawataja inaposema: “Ninyi vijana, watiini wazee.” Kanuni hii inatajwa pia katika Mambo ya Walawi 19:32: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee.”
21. Ni kwa njia gani na kwa sababu gani vijana wa Kikristo wanaweza kufaidika kutokana na wazee katika tengenezo la Mungu?
21 Hapa, basi, upo uhakika unaowahusu ninyi vijana nanyi wazee pia ikiwa mwaiamini Biblia. Hakupaswi kuwepo mtengano kati yenu, kama kulivyo nao katika ulimwengu. Imewapasa ninyi vijana mwatumaini hawa watu wazima kabisa katika kundi la Kikristo, hasa wazee. Wao pia ni watumishi walio wakf wa Mungu Aliye Juu Zaidi, kama wengi wenu walivyo. Tofauti iliyo kubwa ni kwamba wao wana miaka mingi zaidi ya ujuzi—ujuzi ambao waweza kufaidika kutokana nao, ikiwa tu utawaomba mawaidha na mashauri. Ikiwa hujapata kutengeneza motokaa bila shaka waweza kujifunza mengi kwa mzee ambaye muda mrefu wa maisha yake amekuwa fundi wa magari. Ikiwa hujapata kushona vazi, waweza kuepuka makosa mengi na kujifunza njia nyepesi za kufanikiwa kama mshoni kutoka kwa mama ambaye ameshona mavazi ya jamaa kwa miaka mingi. Jifaidi kutokana na ujuzi wa wazee, walio na maoni yenye kusawazika zaidi juu ya maisha. Waliyoyaona yamebadili maoni yao juu ya ubora wa mambo. Wazee walikuwa vijana wakati mmoja; wao wanajua namna kuwa vijana kulivyo. Lakini ninyi vijana hamjapata kuwa wazee na kwa hiyo hamjui lo lote juu ya maoni ya maisha yanayofuatana na miaka ya uzee. Kwa hiyo mwithamini faida inayotokana na walio wazee zaidi.
22. Ni nia gani ya kilimwengu inayofanya vijana wengi watengane na wazazi, na kwa hiyo vijana wa Kikristo wanawezaje kuepuka msiba?
22 Vijana fulani wa kilimwengu leo wanasema ni wenye nia ya kuzungumza na watu wa umri wa zaidi ya miaka 30, lakini ikiwa tu wazee watajizuia wasitoe mashauri. Roho hii ndiyo inayofanya vijana wengi watengane na wazazi wao. Lakini ninyi vijana wa Kikristo, msiwe hivyo. Msichukie mashauri yenye kufaa, kwa sababu tu hamkuyaomba! Nyakati nyingine hatujui kwamba twahitaji mashauri. Wakati kama huo inasaidia sana mtu fulani aliyekomaa anaposema kwa upole na kuyatoa kwetu. Tukisikiliza mashauri twaweza kuepuka maumivu ya moyoni. Mara nyingi msiba waweza kuepukwa.—Mit. 10:17; 12:1; 13:18; 15:31-33.
23. Ni kosa gani wanalolifanya vijana wengi linapokuwa shauri la kutafuta mawaidha, na ni mfano gani wa Biblia unaoonyesha upumbavu wa mwendo huu?
23 Mara nyingi vijana wanawaendea vijana wenzao kutafuta mawaidha na mashauri yao, wakiyapuza wayasemayo wazazi wao na wazee walio Wakristo. Vijana hao wanamkumbusha mtu juu ya Mfalme Rehoboamu kijana. Waweza kusoma juu yake katika Wafalme wa kwanza, sura ya kumi na mbili. Baada ya kifo cha baba yake Sulemani, Rehoboamu aliomba mawaidha ya wazee waliokuwa wamekuwa washauri wa baba yake, kisha akayapuza. Rehoboamu aliwaendea vijana ambao walikua pamoja naye akawaomba mashauri na mawaidha yao. Walimtolea mawaidha mabaya na kumtia moyo afuate mwendo mkatili na wa uadui. Matokeo yalikuwa nini? Kwa kuyafuata mawaidha ya vijana badala ya yale ya wazee, Mfalme Rehoboamu alipoteza sehemu tano kwa sita za ufalme wake, naye hakupata lo lote ila huzuni na taabu maisha yake yote.
24, 25. (a) Ni kijana gani wa Kikristo wa karne ya kwanza aliyekubali mashauri mema kwa furaha kutoka kwa mzee? (b) Kwa sababu gani imewapasa vijana wa Kikristo wajitahidi waepuke mtengano wao na wazazi?
24 Kwa upande mwingine, alikuwako mzee, mtume Paulo, asiyesita-sita kumpa kijana Timotheo mashauri mema, aliyoyakubali kwa furaha na kufaidika sana kutokana nayo. Ni wangapi kati yenu ninyi vijana wa Kikristo mlio kama Timotheo moyoni?—1 Tim. 4:12-16.
25 Kwa hiyo, ninyi vijana nyote, mfaidike kutokana na mashauri mema ya waliokomaa walio mashahidi wa Yehova. Jitahidini msitengane na wazazi na kupatwa na matokeo yake. Kupatwa nayo kwamaanisha kukata tumaini na kufa tu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—1 Yohana 2:15-17.
26, 27. Ni nini thawabu za kuuepuka mtengano wa wazazi na watoto, na sasa ni ulizo gani linalohitaji kufikiriwa?
26 Je! wewe wataka udumu hata milele? Bila shaka wataka! Basi uyafanye mapenzi ya Mungu. Ushikamane sana na Neno lake na tengenezo lake la watu walio wakf na kubatizwa. Na uzifikirie thawabu uwezazo kuzipata ukiepuka kutengana na wazazi! Hata sasa waweza kufurahia mengi ikiwa tu utafikia na kuyashika mapendeleo ya kitheokrasi yanayotolewa kwa vijana wa Kikristo. Na wakati ujao? Basi, Mithali 3:1, 2 inasema hivi: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani.”
27 Walakini, wazazi wanaweza kusaidia sana kuzuia mtengano usitokee kati yao na watoto. Makala ifuatayo itawasaidia kutimiza daraka lao juu ya watoto.
[Picha katika ukurasa wa 484]
Mavutano kama haya—yote yakiwa matokeo ya miaka ya majuzi—ni sababu kubwa ya mtengano wa wazazi na watoto
[Picha katika ukurasa wa 485]
Vijana wanauona unafiki wa wale wanaojifanya kuwa wanadini siku moja ya juma na wanaopiga porojo na kudanganya nyakati nyingine