Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 10/15 kur. 473-477
  • Hukumu Inayosawazisha Haki na Rehema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hukumu Inayosawazisha Haki na Rehema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MWAMUZI” (HAKIMU) NI NANI KULINGANA NA MAANA YA BIBLIA?
  • SIKU YA HUKUMU YA WANADAMU
  • “WASIO HAKI”
  • “WENYE HAKI”
  • JE! WEWE UTAKUWAKO?
  • Ufufuo wa Uzima na Mwingine wa Hukumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Ule Ufalme na lile Tumaini la Ufufuo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Siku ya Hukumu na Baada ya Hapo
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Siku ya Hukumu Ni Nini?
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 10/15 kur. 473-477

Hukumu Inayosawazisha Haki na Rehema

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1-3. Ni picha gani inayochorwa mara nyingi juu ya Kristo kama Hakimu, nayo hii yaonyeshwaje ukutani katika Sistine Chapel katika Rumi?

WAKATI unapofikiria kwenda mbele ya hakimu, unakuwa na maoni gani?

2 Pengine unawaza juu ya mtu mkatili, mkali, asiyebadili nia anayeyasikiliza mashtaka na ushuhuda juu yako, lakini asikupe nafasi ya kueleza hali yako na sababu ya makosa yako.

3 Hii ndiyo picha ambayo mara nyingi makanisa ya Kristendomu yanachora juu ya Kristo kama hakimu. Kwa mfano, ukuta mmoja katika Sistine Chapel katika Rumi unamwonyesha Kristo akitangaza hukumu. Anatoa ishara kubwa ya mikono anapotamka laana kwa “waliolaaniwa” kwa ajili ya dhambi zao za zamani, akiwaelekeza kwenye hell ya mateso ya milele. Sura yake ni ya ukatili na ya kuogofya sana hata mama yake Mariamu, anayeonyeshwa akiwa kando yake, anajinyenyekea, kana kwamba ni mwenye haki na rehema zaidi kumpita yeye​—kwamba hukumu ya Kristo ni ya kikatili sana.

4. Je! maoni ya Kristendomu juu ya Kristo kama Hakimu ndiyo maoni ya kweli?

4 Picha hiyo ni ya uongo kabisa. Juu ya yeye aliyewekwa kama Hakimu Mkuu, mtume Yohana aliandika hivi: “Amejaa neema na kweli.” (Yohana 1:14) Na wakati wa hukumu atakuwa pamoja na watu wa kimbinguni 144,000 kama mahakimu washirika, ambao juu yao Biblia yasema: “Katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa.”​—Ufu. 14:1, 5.

5. Ukweli unatofautianaje na maoni ya Kristendomu juu ya Siku ya Hukumu?

5 Zaidi ya hayo, Siku ya Hukumu inayosimuliwa na Biblia si siku moja ya saa 24, ambayo katika hiyo mamilioni ya mamilioni ya wanadamu wamejipanga mbele ya kiti cha enzi wapate kusomewa dhambi zao za zamani na kupata hukumu ya mwisho isiyobadilika papo hapo. Siku ya hukumu ambayo Kristo na washirika wake 144,000 wanatumikia kama mahakimu ni ya miaka kamili 1,000.​—Ufu. 20:6, 12, 13.

“MWAMUZI” (HAKIMU) NI NANI KULINGANA NA MAANA YA BIBLIA?

6. Kazi ya mahakimu waliowekwa chini ya mpango wa Mungu katika Israeli ya kale ilikuwa nini?

6 Tunapoichunguza habari ya Biblia, twaona kwamba mahakimu hawakuwa watu walioketi tu wasikie na kupima uzito wa ushuhuda kisha kutangaza hukumu. Mahakimu waliwekwa kama viongozi, wasaidizi, wakombozi wa watu. (Amu. 2:18) Hawakuwahukumu wavunjaji wa sheria tu; waliwasaidia watu pia waijue na kuitumia sheria ya Mungu katika maisha zao​—walikuwa kama “baba” kwa watu.

7, 8. (a) Toa mifano miwili kuonyesha mahakimu wanaotajwa na Biblia walikuwa watu wa namna gani. (b) Matokeo ya uhakimu wao yalikuwa nini?

7 Chukua, kwa mfano, Hakimu Gideoni. Alikuwa mtu asiyejivuna, mkulima, lakini aliyeijua sana sheria. Akiwa pamoja na wanaume 300 wenye imani katika Mungu aliwakomboa Israeli mikononi mwa Wamidiani waonezi. Halafu aliliongoza taifa na kulihukumu kwa haki miaka 40, wakati huo nchi ikiwa haina msukosuko.​—Amu. sura 6-8.

8 Halafu alikuwako Yeftha, mtu maskini, aliyewakomboa Israeli na uonezi wa Waamoni. Bidii yake kwa tendo la Mungu ilikuwa nyingi sana hata akaweka nadhiri kwa kupenda kwake mwenyewe kumtoa kama dhabihu ye yote ambaye angetoka nyumbani mwake kumlaki akirudi kwa ushindi kutoka vitani. (Nadhiri hii haikuwa ya kumteketeza ye yote kwa halisi, bali kumtoa mtu huyo kwa maisha ya utumishi katika hema ya Mungu.) Ilikuwa haki yake kufanya hivi kama kichwa cha nyumba yake. Yeftha aliitimiza nadhiri yake kwa uaminifu wakati binti yake mwenyewe, mtoto wake wa pekee, alipopata kuwa mtu huyo. Baadaye “akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka sita” mpaka kufa kwake.​—Amu. sura za 11, 12.

9. Mahakimu hao “walitenda haki” kwa njia gani?

9 Mtume Petro anataja hesabu fulani ya mahakimu hawa na kusema kwamba “walitenda haki.” (Ebr. 11:33) Kwa njia gani? Walitenda kurudisha ibada safi ya Mungu; walilisafisha taifa na wakalirudisha katika hali yenye kibali na Mungu, kukawa na amani na ufanisi. (Amu. 6:28-32) Walionya na kuamuru ili watu wapatanishe maisha zao na Mungu na kwa njia hiyo wajipatie maisha ya usalama yenye ufanisi na furaha.​—Isa. 1:26.

10, 11. (a) Kazi za mahakimu kwa ujumla zilikuwa nini nyakati za Biblia? (b) Namna gani juu ya wafalme?

10 Mahakimu wengine katika Israeli ya kale walikuwa wazee pia katika mitaa yao. Walishughulika na kesi, lakini huo ulikuwa upande mmoja tu wa kazi yao. Wakati wao mwingi ulitumiwa katika kuyaongoza mambo ya mtaa, kuiangalia hali njema ya watu, kupatana na mipango aliyokuwa ameianzisha Mungu. Waliwasaidia watu wajifunze na kuishi kulingana na sheria, hivyo wakipunguza idadi ya kesi ambazo zingeweza kutokea.​—Mit. 8:15, 16.

11 Wafalme wa Israeli walikuwa mahakimu pia. Israeli waliomba “mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote.” Ajapokuwa mfalme alikuwa mwenye daraka juu ya hali njema ya idadi yote ya watu waliokuwa mikononi mwake nyakati zote, bila shaka kuamua kesi kulikuwa sehemu ya maana ya kazi yake.​—1 Sam. 8:4, 5; 2 Nya. (Sik.) 1:9-12.

SIKU YA HUKUMU YA WANADAMU

12. Twawezaje kuwa na hakika kwamba kutakuwako hukumu ya dunia “kwa haki”?

12 Mtume Paulo aliwaambia wasikilizaji katika Athene hivi: “[Mungu] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.” (Matendo 17:31) “Mtu” huyo ndiye Bwana Yesu Kristo. Ufufuo wake ni uhakikisho kamili wa kufufuliwa kwa wafu, kama vile Paulo alivyomwandikia mhudumu mwenzake Timotheo: “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake.”​—2 Tim. 4:1; 1 Kor. 15:12-19.

13. (a) Yesu Kristo ataihukumu dunia kwa haki gani? (b) Twawezaje kuwa wa hakika kwamba hukumu yake itakuwa ya haki kabisa?

13 Yesu Kristo aweza kuwahukumu wanadamu wote, kutia na wafu waliofufuliwa, kwa sababu ya kulinunua taifa la kibinadamu kwa dhabihu yake ya ukombozi. Yeye alisema hivi: “Kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao. Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka. Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na saa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai. Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo [kwa Baba ] ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.”​—Yohana 5:21-23, 27-30.

14. Ni nini maana ya kuwa kwa Kristo “Mwana wa Adamu”?

14 Kwa kuwa alikuwa mwanadamu mkamilifu duniani kama vile alivyokuwa Adamu, aliyelipotezea taifa la kibinadamu uzima, Yesu Kristo ndiye “Mwana wa Adamu.” Yumo katika hali ya jamaa wa damu na mnunuzi, kama ilivyofananishwa na Sheria. Yeye aweza kuwanunua wanadamu na kwa njia hiyo awakomboe na utumwa wa dhambi na mauti, hata na kaburi.​—Law. 25:47-49; Rum. 5:14.

15. Kwa sababu gani “ndugu” za kiroho wa Yesu hawatakuwa kati ya wale watakaohukumiwa wakati wa Siku ya Hukumu ya miaka 1,000?

15 Siku ya Hukumu ya miaka 1,000 itakuwa siku ya ufufuo kwa wote waliomo katika makaburi ya ukumbusho. Hii yamaanisha wanadamu wote waliokombolewa isipokuwa “ndugu” za kiroho wa Kristo, wafalme wake na makuhani washirika 144,000 watakaokuwa mahakimu pia wakati wa “siku” hiyo. Hii ni kwa sababu washirika hawa watapata ufufuo wa mapema, kwa maana wanashiriki katika “ufufuo wa kwanza,” ufufuo wa kwenda mbinguni.​—Ufu. 20:4-6; Flp. 3:11.

16. Huenda wengine wakasikitikia nani kwa habari ya kufufuliwa kwao na kuhukumiwa?

16 Ufufuo huu hautakuwa wa wale wanaohesabiwa kama wenye haki peke yao bali pia na wa wale waitwao “wasio haki” kwa kulinganishwa. “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia,” katangaza mtume Paulo. Hatuna haja ya kuwasikitikia “wenye haki,” lakini namna gani juu ya “wasio haki”?​—Matendo 24:15.

“WASIO HAKI”

17. Je! masikitiko haya yana msingi?

17 Hatuna haja ya kuwasikitikia na “wasio haki.” Ni juu yao kuukubali au kuukataa ukombozi wa Kristo watakapofahamishwa juu yake, wakati wa Siku ya Hukumu. Uhakika wenyewe wa kwamba miaka 1,000 imewekwa kando kwa ajili ya Siku ya Hukumu waonyesha kwamba ina mengi zaidi kuliko kutangazwa tu kwa maamuzi na hukumu. Ni mpango wenye rehema. Wote watakaofufuliwa watahitaji msaada, na mojawapo la makusudi yenyewe ya miaka 1,000 ni kuwapa msaada huo.

18. Kwa sababu gani “wasio haki” watakaofufuliwa watahitaji msaada zaidi kuliko “wenye haki”?

18 “Wasio haki” watahitaji msaada zaidi kuliko “wenye haki.” Wakati wa maisha yao hawakuusikia mpango wa Mungu, ama sivyo wao hawakuzitii habari njema walipozisikia. Hali na mazingira vilishiriki sana kuwafanya wawe na nia hizo. Wengine hata hawakujua kuna Kristo. Wengine walizuiwa sana na mikazo na masumbufu ya kilimwengu hata “mbegu” ya habari njema haikutia mizizi ya kudumu mioyoni mwao. (Mt. 13:18-22) Taratibu ya mambo iliyopo chini ya maongozi yasiyoonekana ya Shetani Ibilisi ‘imepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.’ (2 Kor. 4:4) Hii si ‘nafasi ya pili’ kwa hao waliofufuliwa. Ndiyo nafasi yao ya kwanza hasa ya kupata uzima wa milele duniani kwa kumwamini Yesu Kristo.

19. (a) Je! “wasio haki” wataweza kufanya maendeleo kuelekea ukamilifu? (b) Lazima wafanye nini ili kufikia ukamilifu?

19 “Wasio haki” watakuwa na mengi ya kufanya waweze kufikia ukamilifu. Lakini wakiwa chini ya hali bora na za rehema zaidi za Siku ya Hukumu, Shetani na mashetani zake wakiwa wameondolewa, na taratibu mbovu iliyopo ikiwa imepita, hawatazuiwa tena na vizuizi vya nje. Watazisikia habari njema wakiwa chini ya hizi hali bora nao wataweza kuzikubali au kuzikataa. Watakaozikataa watakufa; wao utakuwa ‘ufufuo unaofuatwa na mwenendo uwaleteao hukumu ya laana.’ Watakaozikubali itawapasa kuanza kugeuza nia zao. (Rum. 12:1, 2) Itawachukua muda kufanya hivi.

“WENYE HAKI”

20. Ni kwa njia gani “wenye haki” watakaofufuliwa walivyo “wenye haki”?

20 Kwa upande mwingine, “wenye haki” watakaohuishwa katika ufufuo wa kidunia watakuwa na mwanzo mzuri. Lakini itawapasa mahakimu watumie wakati wa kuwasaidia wao pia. Wote walikufa kwa sababu ya kurithi dhambi na adhabu yake mauti kutoka kwa Adamu na Hawa wasiotii. Kwa hiyo wote walikufa bila ya kuwa na haki yao wenyewe. (Rum. 5:12; 3:23) Haki yao machoni pa Mungu haikuwa kwa sababu ya ukamilifu wa adili na wa kimwili, bali kwa sababu ya uhakika wa kwamba wao walikuwa wanaume na wanawake wenye ukamilifu kwa Mungu, kama vile mzee wa ukoo Ayubu alivyokuwa.​—Ayubu 2:3, 9, 10; 27:5; Yak. 5:11.

21, 22. (a) Kwa sababu gani “wenye haki” watahitaji msaada pia watakapofufuliwa? (b) Kwa sababu gani ufufuo wakati wa Siku ya Hukumu ya miaka 1,000 unaitwa “ufufuo ulio bora”?

21 Kwa hiyo, wakati “wenye haki” watakapoirudia dunia kwa kufufuliwa, bila ya tabia zao za kipekee kubadilishwa, hata wao hawatakuwa bila kutokamilika na hali yenye dhambi. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari za wale wanaume na wanawake ambao manabii Eliya na Elisha na Bwana Yesu Kristo na mitume wake waliwafufua, wakawahuisha duniani.

22 Kwa hiyo, “wenye haki” na “wasio haki” pia watahitaji mengi zaidi kuliko kutolewa tu katika makaburi ya ukumbusho kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu. “Wenye haki” pia watahitaji kuwekwa huru na hali yenye dhambi na kutokamilika kwa kibinadamu. Kwa hiyo, Hakimu wa kimbinguni Yesu Kristo hawezi kuwatangaza kuwa wasio na hatia mara moja, kuwa wakamilifu, wasio na hali yenye dhambi ya kulaaniwa na siku ile ile ya kufufuliwa kwao akate shauri kwamba wanastahili uzima wa milele duniani. Watapewa faida za dhabihu ya Kristo ya upatanisho kwa rehema ili waweze kufikia ukamilifu wa kibinadamu, kwa kiroho na kimwili. Wakiwa watii hawatakufa tena. Ndiyo sababu ufufuo wa Siku ya Hukumu unaitwa “ufufuo ulio bora” kuliko ule wa wale waliofufuliwa nyakati za Biblia.​—Ebr. 11:35.

23. Je! “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa Har–​Magedoni utahitaji msaada pia kutoka kwa mahakimu wa kimbinguni?

23 Wale watakaouokoka uharibifu wa hii taratibu ya mambo kama “mkutano mkubwa” watakuwa katika hali ile ile. (Ufu. 7:9, 10, 13-15) Watakuwa wangali na hali yao yenye dhambi waliyoirithi, wajapokuwa wamefanya maendeleo mazuri kwa kuuvaa utu mpya. (Efe. 4:22-24) Wanaelekea kwenye uzima, na itawapasa kuendelea kufanya hivyo, wakiwa chini ya uongozi wenye rehema na uangalizi wa mahakimu wa kimbinguni, mpaka mahakimu hawa wamewakomboa kabisa na hali yenye dhambi, makosa na hali ya kufa.

JE! WEWE UTAKUWAKO?

24. Imetupasa tuifikirie Siku ya Hukumu kwa maoni gani?

24 Kwa hiyo hakuna haja ya kuiogopa Siku ya Hukumu ya miaka 1,000. Ni jambo la kutazamia kwa moyo wetu wote. Wazia kuwako kuwakaribisha tena wapendwa wako kwenye nafasi ya kuishi chini ya hali ambazo mtu angetaka kweli aendelee kuishi!

25, 26. Wale wanaozisikia habari njema za Ufalme sasa wamo katika hali gani?

25 Ulizo lililowekwa mbele ya kila mmoja wetu leo ni, Je! mimi nitakuwako kuwakaribisha tena jamaa na rafiki katika ufufuo? Kwa maana huu ndio wakati wetu wenye nafasi ya uzima. Twaijua mipango ya Mungu kupitia kwa ufalme wake chini ya Kristo, Hakimu kwa miaka 1,000. Kuifuata sana kweli, kujifunza mengi zaidi juu ya Mungu na makusudi yake mema juu yetu, na kuifanya kweli njia ya maisha yetu, kutatusaidia tuokoke.​—Sef. 2:2, 3.

26 Hata tukifa tunapomtumikia Mungu katika wakati mfupi ulioachwa na hii taratibu ya mambo, twaweza kuwa na hakika ya kupata ufufuo wa mapema. Kwa hiyo ulizo linalotokezwa ni, Je! mimi nitakuwako? Mtu mwenyewe ndiye anayeweza kulijibu hasa, kwa maana Mungu anatutolea nafasi hiyo sasa.​—Yohana 11:25, 26.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki