Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 1/15 kur. 28-30
  • Kuwa Wenye Huruma Sana—Kama Mungu Wetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwa Wenye Huruma Sana—Kama Mungu Wetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Zinazolingana
  • Iweni Wenye “Huruma Nyororo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mwe Wenye Huruma Nyororo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Yehova—Baba Yetu Mwenye Huruma nyororo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Yehova Hutawala kwa Huruma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 1/15 kur. 28-30

Kuwa Wenye Huruma Sana​—⁠Kama Mungu Wetu

YEHOVA Mungu wetu ni mwenye huruma isiyo na kifani. Katika taabu na shida zetu zote tunaweza kuwa na hakika kwamba ataonyesha watoto wake wa kibinadamu wenye makosa huruma nyingi zitakazomfanya atayarishe njia za kuondoa huzuni na kuwapa baraka nyingi. Msingi wa tumaini hilo hakika ni kujua kwetu matendo yake ya zamani, yaliyoandikwa katika Biblia.

Wadhani ni huruma ya nani iliyoonyeshwa kwa Waisraeli waasi, wakapewa maonyo mengi sana na mfululizo wa manabii? Hata wakati watu hao walipodhoofika katika adili na dini, Yehova ndiye aliyewatolea ahadi hii: “Nitaonyesha huruma juu yao, sawa na vile mtu aonyeshavyo huruma juu ya mwana wake anayemtumikia.”​—Mal. 3:17, NW.

Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alionyesha sifa iyo hiyo ya kimungu ya kuwa na huruma nyingi, alipokuwa mwanadamu duniani. Kumbukumbu la huduma yake laonyesha alivyohurumia makundi ya watu “kwa sababu walikuwa [wamekonda] na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:35, 36) Huruma yake haikuwa ya mdomo tu. Ilikuwa huruma nyingi sana iliyomwongoza aponye wagonjwa, aponye wenye maungo mabaya, alishe wenye njaa, afungue macho ya vipofu na kuzibua masikio ya viziwi. Lakini huruma yake haikuishia hapo. Alijua sana kwamba uhitaji mkuu wa watu ulikuwa kuchungwa, kuongozwa salama, na kulindwa na maongozi maovu ya ulimwengu usiomcha Mungu. Kwa hiyo alizoeza wanafunzi wake kuwa wachungaji wenye huruma.

Ili wawe na matokeo mema wachungaji hao wanaotumikia chini ya Kristo lazima watende kama yeye alivyotenda wakiwa na makusudi yale yale. Lazima wajifunze kuwa wenye huruma nyingi, hasa kwa wale wanaojijua kuwa wana mahitaji ya kiroho. Inapaswa kuwa hivyo hata zaidi leo, kwa maana sasa tunaishi katika nyakati zenye kutaabisha zaidi sana. Umati mkubwa wa watu ni vipofu, vilema na viziwi wa kiroho, tena wana njaa na wanahitaji sana sana uchungaji mwema ambao Yesu aliwatakia. Ikiwa wewe ni mfuasi wa Kristo, je! unajiona ukifuata mfano wake katika habari hii? Je! unahangaikia pia makundi ya watu ‘waliokonda na kutawanyika’? Je! unatumia njia hiyo inayofaa uinue hali yao ya umaskini wa kiroho?

Ni kweli, huenda ukajisikia huna nafasi nyingi za kuonyesha huruma. Pengine unaweza kushiriki mwenyewe kuhubiria watu habari ya Ufalme nyumbani mwao. Si jambo jepesi sikuzote, lakini linaonyesha kwamba wewe huhurumii wenye mahitaji kwa mdomo tu. Unaweza pia kujitahidi na kusaidia umati mkubwa wa watu sehemu za mbali, ulimwenguni pote. Kwa njia gani? Kama vile Wakristo wengi wanavyofanya na ambavyo wamekuwa wakifanya makumi mengi ya miaka. Wametambua kwamba tengenezo moja la kidini kati ya matengenezo mengi yanayofanya kazi duniani kote ndilo lililo tofauti kabisa. Ni tengenezo ambalo kusudi lake la pekee ni kuendeleza utumishi wa kuchunga ambao Yesu alianzisha karne kumi na tisa zilizopita. Linatambuliwaje?

Ni jamii ya wanaume na wanawake walio katika mataifa yote ya dunia wanaofanya kazi pamoja kutumikia ufalme ‘wa Mungu, wakitukuza jina la Mungu wao, Mungu mwenye huruma, Yehova. Wameungana katika ibada yao na wanakusanya mali zao pamoja wasaidie na kuendeleza kazi ya kusaidia watu wanyenyekevu wenye mfano wa kondoo, walio na njaa na kiu ya amani na haki. Wanatumia Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, na afisi kuu yake Brooklyn, New York, na maafisi mengi ya matawi ulimwenguni kote, kama chombo chao cha kufanyia kazi hii ya lazima. Michango yao midogo inapelekewa Sosaiti hiyo kwa kujua kabisa kwamba itatumiwa kueneza ujumbe wa kweli wenye kutoa uzima kwa kugawa vitabu na kuzungumza na watu, kwamba haitatumiwa kupandisha vyeo wala kuinua mishahara ya wasimamizi walio hodari.

Jamii hiyo ya wanaume na wanawake inajua sana kwamba maafisi ya Sosaiti ulimwenguni kote, katika nchi na visiwa zaidi ya 90, yanasimamiwa na watu wenye huruma ile ile, wasiolipwa mishahara, wanaotumia wakati na nguvu zao kwa furaha waendeleze kazi hii ya uchungaji. Kwa ujumla, Wakristo hawa, wawe ndani au nje ya matawi ya Sosaiti, wanatumia mali na nguvu zao kwa ukarimu, kwa maana wote wanamwabudu Mungu yule yule mwenye huruma na wanataka kushiriki katika kazi Yake kwa kadiri wawezavyo kupelekea watu wote amani na tumaini kupitia kwa habari njema za Ufalme.

Kupitia kwa nabii wake Ezekieli, Mungu mwenye huruma alitabiri zamani za kale kazi hii kubwa ya kutafuta “kondoo” waliopotea na kuwaangalia. Alisema hivi: “Mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia.” (Eze. 34:11) Tena, kupitia kwa nabii wake Yeremia, Mungu alisema maneno haya ambayo sasa yametimizwa: “Nitakusanya mabaki ya kundi langu, katika nchi zile zote . . . Nami nitaweka juu yao Wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea hata mmoja wao.”​—Yer. 23:3, 4.

Kwa zaidi ya nusu karne sasa kumekuwa na ishara za kuonyesha kazi hiyo ya uchungaji kati ya watu wa mataifa yote inaendelea. Kwa njia hiyo makundi makubwa ya watu yameangaliwa sana na Mungu mwenye huruma. Nao pia wamejifunza kuwa ‘wenye huruma sana,’ ‘wasiangalie mambo yao wenyewe, bali waangalie mambo ya wengine.’ (Flp. 2:4; 1 Pet. 3:8) Wanaionyesha huruma hiyo kwa jitihada zao za kupelekea jirani zao ujumbe wa Ufalme, na kwa kutoa pesa ili kuendeleza utumishi uo huo katika kila bara.

Si ajabu kwamba utumishi wa kuchunga unaofanywa na watumishi wa Yehova wanapohubiri ulimwenguni pote unaendelea bila kuzuiwa na ukosefu wa pesa. Bila shaka Mungu mwenye huruma anabariki utendaji wanaofanya kwa ukarimu. Yeye anaona kwamba mioyo yao inataka kupelekea wenye shida msaada wa kiroho. Anaona vile wanavyofanya kazi kwa ushirikiano, wakitumia Watch Tower Society kama chombo chao, wafikie kila pembe ya dunia. Anajua kwamba hawatoi zawadi wala hawatumikii kwa kulazimishwa wala kwa sababu ni wajibu tu, bali wanafanya hivyo na mioyo inayoona kwamba wenye njaa na kiu ya haki wanahitaji kusaidiwa haraka.

Wale wanaotumia nguvu na mali zao kwa huruma ili kuendeleza kazi ya kuuhubiri Ufalme wanaridhika sana. Hawaridhiki kamwe wakijifikiria wenyewe tu, kwa maana thawabu yenye kuridhisha kweli kweli ni kujua kwamba wapokeaji wenye shukrani wa msaada wao wa kiroho watathamini huruma nyingi sana za Mungu wetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki