Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 11/15 kur. 516-522
  • Kujizoeza Kanuni za Biblia Nyumbani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujizoeza Kanuni za Biblia Nyumbani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTEGEMEANA
  • KUONYESHA UZURI WA “UTU MPYA”
  • UPENDO WA KWELI NA UNYENYEKEVU
  • ‘Tiini’ kwa Sababu Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Faida za Kujitiisha Katika Mpango wa Kitheokrasi
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Ujitiisho Katika Ndoa Humaanisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kile Ambacho Ujitiisho wa Kimungu Wataka Kwetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 11/15 kur. 516-522

Kujizoeza Kanuni za Biblia Nyumbani

1. Tofauti za utu zaweza kufanya kazi kwa njia gani mbili, ikiongoza kwenye ulizo gani?

SISI sote tu watu walio tofauti. Kwa njia fulani hivyo ni vema. Inafanya maisha yenye kupendeza zaidi na yenye namna nyingi. Yaweza kusaidia kutatua magumu. Hali nyingine zinatatuliwa kwa njia bora zaidi wakati wale wenye uwezo mbalimbali wanaposhirikiana. Ndivyo ilivyo na nyumbani. Walakini, kwa sababu ya kutokamilika matokeo yaliyo tofauti yanapatikana nyakati nyingine. Kuwa na nyutu mbalimbali kunatokeza magumu, kufanya iwe vigumu kushirikiana. Bila shaka, magumu yaweza kutokana na mambo mengine yasiyo tofauti za nyutu, lakini ulizo hapa ni, Mkristo akate kauli kwamba ugumu fulani unaohusu watu hautatuliki hata kidogo, au kwamba nyutu fulani haziwezi kupatanishwa?

2. Tukipatwa na magumu, twatiwaje moyo badala ya kupewa sheria?

2 Kusudi letu si kutoa sheria nyingi sana. Bali, tunataka kuwatieni moyo mwone uwezekano wa utatuzi wa magumu mahali ambapo pengine mlidhani hauwezi kupatikana. Au pengine unauona uwezekano, lakini hujui kuutumia. Watu wahusikapo, usisahau kamwe kwamba hali zaweza kubadilika. Ndivyo na watu wanaohusika. Ndivyo na wewe. Kwa kweli, Mkristo wa kweli ana nafasi bora na sababu ya kugeuza au kurekebisha utu wake kuliko mtu mwingine ye yote. Yeye yuna wajibu wa kufanya hivyo. Namna gani hivyo?

3. Paulo anatiaje moyo nguvu za kubadili utu?

3 Biblia inazungumza waziwazi sana juu ya mabadiliko yanayopaswa kufanywa katika utu. Inatia moyo na nguvu kwa kueleza ni kwa sababu gani na ni kwa njia gani yanavyoweza kufanywa. Alipokuwa akiwaandikia Wakristo katika Efeso, Paulo alisema hivi: “Mpate kuuvua utu wa kale unaofanana na namna ya mwenendo wenu wa zamani na unaoharibika kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali mpate kufanywa wapya katika nguvu yenye kuendesha akili zenu, na kuuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki ya kweli na uaminifu.” Hii yaonyesha wazi sababu ya utu mpya. Kwa kweli imetupasa kila mmoja tukubali kwamba utu wetu wa kale uliongozwa sana na ‘tamaa za udanganyifu,’ kwa sababu ya kuwamo “gizani kwa akili, na kutenganishwa na uzima ulio wa Mungu.” Walakini, tulipoikubali kweli, “kama vile kweli ilivyo katika Yesu,” tulianza kujifunza namna ya kuushika sana uzima ulio kweli kweli.’ Tulikuza tamaa mpya ya moyoni, iliyoonyeshwa na wakf wetu kwa Mungu kufanya mapenzi yake katika uaminifu ulio thabiti.​—Efe. 4:17-24; 1 Tim. 6:19, NW.

4. Tutafute msaada kutoka chanzo gani, nayo hii yasaidiaje?

4 Ijapokuwa unakubaliana na hili, huenda ukashangaa namna inavyowezekana kulitimiza kwa kushughulika na magumu yanayokutatiza sana katika maisha ya nyumbani. Huenda ukajisikia kwamba ‘nguvu yenye kuendesha akili yako’ (kwa halisi, ‘roho ya akili yako’) si yenye nguvu vya kutosha. Kweli, huenda usiwe na nguvu za kutosha ndani yako mwenyewe. Lakini kwa wakf wako umejiweka mkononi mwa Yehova, naye ni mwenye nguvu vya kutosha. Anaweza na ni mwenye nia ya kukuongoza na kukutia nguvu utimize wajibu wako. “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.” (Flp. 2:13) Haikupasi kuitegemea nguvu au roho ya akili yako mwenyewe. Bali, unajifunza namna ya kushirikiana na roho ya Mungu. Hakuna ugumu ulio mkubwa mno kwake, hata ule wa Kristo aliyekufa. Asema Paulo: “Ikiwa [roho yake] yeye aliyemfufua Yesu katika wafu [inakaa] ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa roho yake [inayokaa] ndani yenu.”​—Rum. 8:11; tazama pia Waefeso 1:19, 20.

5. Yajapokuwa magumu ya maisha yaendelee kuwapo, ni faraja gani tuwezayo kupata?

5 Hii haina maana ya kwamba wewe unaweza kutatua magumu yako yote kwa kuyaondoa akilini tu. Maana yake ni kwamba unaweza kupata faraja ya kujua kwamba nia yako na tendo ndiyo ya haki na inayolingana na Maandiko. Kutokana na maoni ya Yehova, kumbukumbu lako na dhamiri ni safi. Ni kusudi lake kwamba “maagizo ya torati [kanuni zake za msingi] yatimizwe ndani yetu sisi, tusioenenda kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya roho.” Ni kweli, ungali mtu asiyekamilika, lakini mpango umefanywa kwa huruma ambapo dhambi zako waweza kusamehewa kwa sababu hiyo.​—Rum. 8:4.

6. Katika habari hii, twaweza kujifunza nini kutokana na yaliyoandikwa katika Waebrania, sura ya 11?

6 Ijapokuwa ni kweli kwamba maandiko yaliyotangulia kutajwa yanatumika hasa kwa wale waliomo katika kundi la Kikristo wenye tumaini la kimbinguni, kwa kanuni yanatumika pia kwa “mkutano mkubwa” wa mashahidi wa Kikristo wanaotajwa katika Ufunuo 7:9 wanaofurahia tumaini la kidunia. Hii inategemezwa na ushuhuda usioweza kukanwa wa kibali ya Yehova na baraka juu ya wale wote walio mashahidi waliotangulia Ukristo wanaosimuliwa katika Waebrania, sura ya 11. Kwa roho yake waliwezeshwa kuyatatua magumu yao mengi, kutia na ya kinyumbani, uasi twakutia moyo ufanye vivyo hivyo. Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu tulipewa maandishi ya “wingu kubwa la mashahidi.” (Ebr. 12:1) Tukilikumbuka hili, na tuendelee kuliangalia shauri la Paulo lililoongozwa kwa roho walilopewa Wakristo katika Efeso.

7. Baada ya ombi lake katika Waefeso 4:22-24, Paulo anatoa shauri linalohusu nini?

7 Paulo anaendelea kutoa shauri lifaalo, msingi wake ukiwa ombi la kuvaa utu mpya. Lijapokuwa limetolewa kwa kufikiria mwenendo ndani ya kundi, linatumika kwa maisha ya nyumbani pia, na sehemu yake kwa uhusiano wa jamaa kwa njia ya moja kwa moja. Badala ya kuweka sheria, yeye anazungumza kanuni, akionyesha ni kwa njia gani na sababu gani zimepaswa zishikwe. Anaandika hivi: “Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake.”​—Efe. 4:25.

KUTEGEMEANA

8. (a) Kuwa “kila mmoja kiungo cha wenzake” kunatumikaje kwa uhusiano wa kimwili na kiroho pia? (b) Hii yaonyeshwaje kwa njia nzuri?

8 Kwa wakf wako umekuwa mshiriki wa jamaa ya Mungu, nawe waweza kumwita “Baba yetu” kwa kweli. (Mt. 6:9) Huu ni uhusiano wa kiroho, nao ni wa maana zaidi kuliko mambo yote maishani mwako. Walakini, haufuti uhusiano wa kimwili na wajibu wake. Mungu alikuanzisha kuumba kwa jamaa ya kibinadamu katika ukamilifu, akiwaambia waongezeke, wakiwa na tumaini la kuwa jamaa nyingi zenye wazazi na watoto. (Mwa. 1:28) Wakati Paulo aliposema “tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake,” alikuwa akitaja kanuni ya msingi, yenye kutumika kwa uhusiano wa namna mbili uliotangulia kutajwa. Akihakikisha hili, mahali pengine anautumia mwili wa kibinadamu na viungo vyake kama mfano mwepesi wa kutegemeana.​—Tazama 1 Wakorintho 12:12-27; Waefeso 4:4, 15, 16.

9. (a) Kanuni iliyotangulia inatumikaje kwa kundi la Kikristo kwa njia yenye kufaidi? (b) Ni wapi leo ambapo kanuni hii haionekani, ikiongoza kwenye ugumu gani?

9 Kuithamini kanuni hii kutakusaidia sana. Je! unaelewa? Hata katika kundi la Kikristo washiriki si mali ya Mungu tu na Kichwa chao, Kristo Yesu, bali pia ni mali ya mtu na mwenzake. Wao si mali yao wenyewe. Hiyo inauendeleza umoja wa kweli unaouona kati ya mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Walakini, kwa sababu ya mikazo mingi ya hizi “nyakati za hatari,” inasikitisha kwamba umoja huo hauonekani mara nyingi katika maisha ya jamaa. Kama ilivyotabiriwa, roho iliyopo katika hizi “siku za mwisho” ni ya choyo, kutokushukuru na kutokuaminika. (2 Tim. 3:1-5) Katika jamaa nyingi, kila mshiriki anafuata njia yake mwenyewe, hata kutia na watoto wenye umri mdogo sana. Huenda ukajiona kutaka kuwa namna ile ile, ukidhani kwamba una wajibu wa kufanya hivyo, ikiwa wewe ndiwe wa pekee nyumbani unayependezwa na ibada ya kweli. Mapendezi na utendaji wako ni tofauti sana, nawe ‘unaacha kushirikiana na matendo yasiyozaa ya giza.’ (Efe. 5:11) Hata hivyo. unapoishi katika nyumba hiyo u sehemu ya jamaa, na kwa hiyo una wajibu fulani juu ya washiriki wengine.

10. Ni kwa njia gani tuwezavyo kufanya jitihada za kuendeleza amani na umoja wa jamaa?

10 Imekupasa ufuate nia na mwendo gani? Ijapokuwa huenda jitihada zako zisithaminiwe, tafuta nafasi, hata katika mambo madogo, kuendeleza amani ya jamaa na umoja. Ikiwa wengine wanapinga, usionyeshe ubaridi na ukatili ule ule walio nao. Usitokeze ushindani juu ya mambo isipokuwa kanuni ya Biblia ikihusika. Hata wakati huo, huwezi kusisitiza kwamba wengine washike kanuni za haki, isipokuwa kama wewe ni mzazi unayesisitiza kwa watoto wako. Unapokuwa na wengine kila siku, kumbuka kwamba mambo unayoyatenda yanakutetea zaidi kuliko unayoyasema, isipokuwa ukifanyiwa shtaka au ukiulizwa ulizo fulani. Jaribu kuwa mfano wa maisha mema ya Kikristo. Jaribu kuonyesha kweli inamaanisha nini kwako, katika kukupa wewe furaha ya kweli na uradhi na tumaini jangavu juu ya wakati ujao, wakati ule ule ukiwahurumia wale waliotaabishwa sana na hali zilizopo.

KUONYESHA UZURI WA “UTU MPYA”

11. Shauri la Paulo latumikaje kwa habari ya (a) kusema uongo, (b) hasira, na (c) kuiba?

11 Mengi ya mashauri yaliyotolewa hapa yanatumika kwa maisha ya nyumbani, bila ya kujali hali ya jamaa ilivyo. Ni vyepesi sana kusema uongo mdogo, ukijidhania kwamba sikuzote hakuna faida ya kusema kweli. Je! unapendezwa ukiona washiriki wengine wa jamaa wakifuata mashauri hayo? Je! haiharibu matumaini na kufanyiza shuku? Bila shaka haikuzi maoni ya ‘kila mtu kuwa wa mwenzake? Paulo asema hivi: “Uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake.” Tena, ni vyepesi kuendeleza uchungu kwa sababu ya kuchokozwa daima. Bila ya kutaka kukubali hivi, huenda ukasema uongo kwa kukana hivyo. Hata wakati hasira yako inapokuwa ya haki, jihadhari; ‘jua lisichwe na uchungu wako bado haujakutoka.’ Huenda sababu ya kukasirika ikawapo bado, lakini jaribu kupata maoni ya Yehova juu ya ugumu wenyewe, na kuomba msaada wake. “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza.” (Efe. 4:25, 26; Zab. 55:22) Ukifanya hivyo ‘hutampa Ibilisi nafasi.’ Halafu, yaelezwa: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi . . . apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” Inaweza kushawishi namna gani kuiba kidogo​—kuiba kidonge kidogo tu cha chakula ukipendacho kabla hakijaletwa mezani. Hakuna mtu atakayeona kwamba kimekosekana, isipokuwa ukisahau kupangusa mdomo wako! Hili ni jambo la kawaida kwa watoto wadogo, ijapokuwa huo ndio wakati wa kufundisha kanuni zifaazo, kwa upole lakini bila kukoma. Kila mshiriki wa jamaa ana haki pia ya kuwa na siri kwa kadiri fulani, ikitegemea umri na hali. Usijiingize katika hali hiyo ya siri. Hiyo pia ni namna ya kuiba.​—Efe. 4:27, 28.

12. (a) Shauri juu ya usemi linatumikaje hasa kwa maisha ya nyumbani? (b) Twawezaje kuyabadili yaliyo mabaya na yaliyo mema, kupatana na shauri lililomo katika Warumi 12:14?

12 Halafu, shauri jema linatolewa juu ya usemi, kutia na sababu ya usemi wenyewe. “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji . . . Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya,” kutia na “usemi wa kipumbavu” na “mizaha ya matusi.” (Efe. 4:29-31; 5:4, NW) Mara nyingi nyumbani ndipo mahali unapojiona mwenye uhuru wa kusema utakavyo, hata zaidi kuliko kundini, ambapo kanuni za haki zinafuatwa zaidi. Kwa hiyo, ni jambo la lazima sana kuiona haja ya kujiweza, hasa ikiwa hali ya watu wote inakuwa ya uzembe, bila ya kujizuia katika kusimulia hadithi za kuchekesha na mizaha, wala kujihadhari na maneno ya kutumia mtu akichokozwa. Si lazima ‘neno lililo ovu’ liwe la matusi. Huenda kukawa ni kutumia maneno kwa njia ya ujanja, jambo fulani lenye maana mbili, kama vile tunda linaloonekana safi sana nje, lakini lililooza ndani kabisa. Ndiyo, inategemea moyo wako ulivyo. (Mt. 12:34) Mambo hayo ni ya utu wa kale. Lazima mahali pake pachukuliwe na yale ya utu mpya, na ‘yenye kufaa,’ na “kutoa shukrani.” Badala ya kuwa wenye uchungu na hasira, pamoja na matusi lazima tuwe ‘wafadhili sisi kwa sisi, wenye huruma, tukasameheane.’ Hizi ndizo kanuni za Biblia zinazopaswa kuzoewa nyumbani.​—Efe. 4:32; Kol. 3:8-10.

13. (a) Kuna uhakika gani juu ya nyutu zote? (b) Haitupasi kudharau nini, nao unyenyekevu unashirikije sehemu ya maana?

13 Hatuonyeshi hata kidogo kwamba ni vyepesi kufanya mambo haya. Si vyepesi kuyafanya kama ilivyo vyepesi kuyasoma. Hushughuliki na vitu visivyokuwapo, wala na mambo ya kusahaulika kwa kuwazia tu. Unashughulika na nyutu, utu wako na nyutu za wengine. Kwa habari ya nyutu hizo, kutia na wako mwenyewe, yaweza yakawamo mambo ya ndani akilini na moyoni, yafaayo au yasiyofaa. Utu bora sana wa Yehova umepaswa pia ukumbukwe. Usikudharau kamwe kupendezwa kwake na kuendeleza kwako uhusiano ulio wakf kwake. Usiidharau kamwe mipango mingi isiyoshindwa aliyoifanya kupitia kwa Neno lake na tengenezo, kwa roho yake na kupitia kwa sala, kukuwezesha wewe uvae utu kama wa Kristo. (Efe. 3:20) Kwa kawaida maendeleo ya hali ya kiroho ni ya taratibu kuliko utazamiavyo. Kanuni bora zaweza kuwaziwa, lakini huenda zikawa ngumu kufikiwa, kama vilele vipya vinavyoonekana ukizunguka pembe ya kitu fulani. Jambo kubwa ni hali yako ya akili​—kama wewe u mnyenyekevu wa akili na u mwenye nia ya kukubali makosa yako, na kama sikuzote u mwenye nia ya kufanya jitihada zaidi, kujaribu mara nyingine. Yehova anaibariki nia hiyo bila shaka, na ndugu na dada zako katika jamaa ya Mungu watakupendea hilo, nao watajitahidi sana wakusaidie.

14. (a) Tujaribuje kushinda chuki isiyo na sababu tunayoonyeshwa? (b) Yesu alituwekea mfano gani katika habari hii?

14 Hata uwe mnyofu na mnyenyekevu wa akili namna gani, huenda hii isithaminiwe na washiriki wengine wa jamaa yako ya kimwili wenye chuki isiyo na sababu, hata ukatili. Huenda wakasema kwamba unajaribu kujionyesha ubora wako. Si vigumu kuelewa sababu ya kuambiwa hivyo. Huenda kanuni zako kama Mkristo wa kweli zikawa bora kuliko zao, lakini hiyo haikufanyi bora, sivyo? Wewe uko kama ulivyo kwa fadhili za Yehova zisizostahili. Wewe unajua hivyo, lakini wao hawajui. Bila ya kuridhiana nao au kuvunja kanuni yo yote ya Biblia, imekupasa ujitahidi kufuata desturi. Kwa kadiri hiyo, onyesha kwamba unahusika. Usikasirikie wengine au kukasirishwa nao. Yesu alivumilia hili mara nyingi alipokuwa pamoja na watu waliokuwa na chuki isiyo na sababu na ukatili. Yeye hakuacha kuongea na kujificha. Ni kama vile Petro alivyosema juu yake: “Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake. . . . Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.”​—1 Pet. 2:21-23.

UPENDO WA KWELI NA UNYENYEKEVU

15. Anaposhauri washiriki wa jamaa, kichwa cha Paulo hasa ni nini, lakini kanuni hii ilipotoshwaje mapema?

15 Paulo anaendelea kutoa shauri lake lenye maelezo mengi kwanza kwa wake, kisha kwa waume na watoto, kwa kuwasihi wote hivi: “Hali mnanyenyekeana katika kicho cha Kristo.” (Efe. 5:21) Hiki ndicho kichwa cha Paulo hasa anaposhauri waume na wake. Kwa tendo lake la haraka haraka mwanamke wa kwanza, Hawa, alionyesha hakuwa mnyenyekevu, si kwa Mungu tu, bali pia kwa mumewe. Kweli, Adamu alionyesha unyenyekevu kadiri fulani kwa Hawa kwa kufuata mfano wake, lakini haukufaa hata kidogo. Alikuwa akikosa kumnyenyekea Mungu. Hivyo unyenyekevu ukapotoshwa mara tu baada ya dhambi kuingia katika jamaa ya kibinadamu.

16. Unyenyekevu ni wonyesho wa upendo wa kweli kwa njia gani, nao umepaswa uonyeshweje wazi?

16 Unyenyekevu ufaao ni wonyesho wa upendo wa kweli. Wakati ulipochukua hatua ya wakf kama Mkristo wa kweli, ulikuwa ushuhuda wa upendo wako kwa Yehova, na wa unyenyekevu wako kamili na wa hiari kwake, kuyafanya mapenzi yake. Katika kundi la Kikristo, imepaswa iwepo roho ya kufikiriana pia na ‘kunyenyekeana katika kicho cha Kristo.’ Imewapasa wazee waongoze katika jambo hili, “si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.” Roho iyo hiyo ionyeshwe nyumbani. Hii inaonyeshwa vizuri na mwili wa kibinadamu, ambamo viungo vyote lazima ‘viungamanishwe na kufanywa vishirikiane’ ili mambo yafanywe. Hata kichwa, kilicho juu, hakiwezi kuiambia miguu: “Sina haja na ninyi.” ​—1 Pet. 5:3; Efe. 4:16; 1 Kor. 12:21.

17. Mara nyingi kutopatana kunasababishwa na nini, lakini dawa yaweza kuwa nini mara nyingi?

17 Nia hii ya ushirikiano ikionyeshwa, magumu ya ndoa na ya jamaa yasiyotatulika ni machache, kwa vyepesi. Yaani, kutokuwapo kwa nia hii mara nyingi ndilo shina la ugumu. Hata wakati mwenzi mmoja tu ndiye Mkristo aliye wakf anayeionyesha nia hii, inaweza kusaidia sana kuzuia magumu yasilete ugomvi na faraka. Paulo alisihi “mwenende kama unavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo.”​—Efe. 4:1, 2.

18. (a) Twaweza kujifunza nini kutokana na shauri la Paulo katika Wafilipi 2:2-4? (b) Yawezekanaje kwamba ‘wenzio ni bora kuliko nafsi yako’?

18 Alisema hivi kwa nguvu zaidi kwa Wafilipi, akisema: “Ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja, . . . msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.” (Flp. 2:2-4) Je! wewe ni mnyenyekevu wa akili hivyo, au wewe u mtu wa kujifikiria mwenyewe tu na mwenye majivuno, ukisisitiza kwamba sikuzote u mwenye haki katika maoni yako juu ya mambo na watu? Kama mume au mzee, je! mke wako au wengine kundini wanaona kwamba u mnyenyekevu wa akili? Je! wote wanaona waziwazi kwamba unawaona wengine kama bora kuliko wewe mwenyewe? Bila shaka ndivyo walivyo katika sifa fulani na uwezo. Huenda ukaleta vifaa vyote vya nyumbani, lakini je! unaweza kuvipanga kwa njia ya malidadi kama mkeo? Je! watoto wako si wenye nia zaidi kuonyesha furaha na shauku?

19. Ni kwa kadiri gani mke atamnyenyekea mumewe, na kwa sababu gani?

19 Paulo anaendelea kuonyesha uhusiano mwema kati ya kanuni za Biblia za upendo, unyenyekevu na ukichwa. Kwa kuwa “mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa,” mke yuna wajibu wa kumnyenyekea. Kwa kadiri gani? “Kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.” Huenda mumewe asiwe Mkristo aliye wakf, na huenda hata akawa anapinga kwa sababu hii, lakini hiyo haivunji wala kurahisisha kanuni ya ukichwa. Haimpasi mke kunyenyekea ukichwa wa mume kwa kunung’unika, na imempasa akose kunyenyekea wakati tu unyenyekevu ungemfanya avunje kanuni nyingine ya Biblia.​—Efe. 5:22-24.

20. Ni kwa kadiri gani ambavyo imempasa mume ampende mkewe, na kwa sababu gani?

20 Kutumia kanuni ya upendo wa kweli wa agape ndilo daraka la kwanza la mume wa Kikristo. Kwa kadiri gani? “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase . . . [na baadaye] apate kujiletea Kanisa tukufu, . . . takatifu lisilo na mawaa,” kama bibi arusi mtukufu. Kwa kweli hii inaonyesha heshima nyingi kwa upande wa mume kwa mkewe, hali “mke asikose kumstahi mumewe.”​—Efe. 5:25-27, 33.

21. Ni kwa njia gani na kwa sababu gani upendo na unyenyekevu unahusu watoto?

21 Kwa watoto, utii ufaao na unyenyekevu unatiliwa mkazo. Wakiwa chini ya mafundisho ya Maandiko yafaayo na ya upendo ya ‘wazazi wao katika Bwana,’ imewapasa watii “katika kila jambo,” wakiwa na ahadi ya ‘kupata heri, ukae siku nyingi katika dunia.’​—Efe. 6:1-4; Kol. 3:20.

22. Petro anauthibitishaje uhitaji wa wote kuwa wanyenyekevu wa akili?

22 Mwishowe, inatia moyo na nguvu kuona namna Petro anavyozithibitisha kwa njia yake mwenyewe kanuni izi hizi za Biblia alizozisisitizia Paulo. Vile vile Petro anatilia mkazo uhitaji kwa upande wa kila mmoja kuwa mnyenyekevu wa akili. Anaandika hivi: “Basi, ninyi nyote iweni na nia iyo hiyo, mkihurumiana, mkiwa na upendano wa kidugu, mkisikitikiana, mkiwa wanyenyekevu wa akili.” Na tena: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.” (1 Pet. 3:8, NW; 5:5) Hii ilionyeshwa vizuri kwa ambavyo Yesu aliiosha miguu ya wanafunzi wake kama mfano unaostahili kufuatwa. Ni wakati gani ilipokuwa mara yako ya mwisho kuosha miguu ya mtu kwa njia ya mfano, kwa kutoa utumishi mdogo kwa mshiriki wa jamaa au kwa mtu fulani kundini? Hii pia ni kanuni ya upendo ya Biblia inayofaa tuizoee mara nyingi zaidi.​—Yohana 13:4-9.

​—Kutoka The Watchtower, May 15, 1974.

[Picha katika ukurasa wa 518]

“Tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki