Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/15 kur. 569-575
  • Tumikia kwa Tumaini la Umilele

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tumikia kwa Tumaini la Umilele
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UMILELE NI WA ASILI KATIKA IBADA YETU
  • WATAWALA WA MILELE KATIKA UFALME
  • NI ZAIDI KULIKO TUMAINI TU LA UZIMA WA MILELE
  • SI KUTUMIKIA MPAKA TAREHE FULANI TU
  • ONYESHA IBADA YA MILELE KATIKA MWENENDO WAKO NA MAAMUZI YAKO
  • Kutembea Pamoja na Mungu—Tukifikiria Umilele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Tunaweza Kuishi Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Msifuni Mfalme wa Umilele!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kuishi Milele Si Ndoto Tu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/15 kur. 569-575

Tumikia kwa Tumaini la Umilele

1, 2. (a) Watu mmoja mmoja na mataifa wana maoni gani juu ya wakati ujao? (b) Kwa sababu gani wengine hata hawaelekei kuufikiria wakati wao ujao?

JE! SI jambo la kawaida leo kukutana na watu ambao maoni yao makuu ya maisha, kama yanavyoonyeshwa na wanayoyasema au kuyafanya, ni: “Jifurahishe maadamu unaweza; nani ajuaye kesho itakavyokuwa?” Hata mataifa mengi yanaelekea kufuata maoni hayo. Mmojawapo wa wasimamizi mashuhuri wanaoshughulika na upunguzaji wa gharama wa Ulaya aliilaumu serikali yake juu ya kufuata shauri la kupanga na kutumia fedha ikitumainia leo tu, si wakati ujao.

2 Na watu wengi wamefumbuliwa macho sana na miradi na mambo yaliyotimizwa na “serikali” hata hawapendezwi na wakati ujao wenye mambo yale yale. Katika mwaka wa 1972 mtaalamu mmoja wa chuo kikuu aliona kwamba “vijana hawaelekei kupendezwa sana na wakati wao wenyewe ujao.” Akaongezea: “Vijana wanakosa kinachoitwa na wanasayansi wanaoshughulika na mambo ya kijamii ‘kusawazisha mradi,’ nao wanaelekea kupoteza wakati wao ovyo ovyo kwa kutumia dawa za kulevya na kupinga njia mbalimbali za maisha na miradi au anasa zisizo na maana.” Halafu wako watu wengine wanaoona ni afadhali wasiufikirie wakati ujao kwa sababu ya maonyo yanayozidi kuogofya juu ya uchafu, uvunjaji wa sheria, njaa na vita.

3. Ni uhakika gani unaofanya watu wengi waishi kwa ajili ya sasa tu?

3 Hata kama mataifa makubwa yakitatua magumu katika uhusiano wa mataifa yote, hata tangazo lenye maana lililotabiriwa la “amani na salama” litimie, watu wengi hata hivyo ‘wangeishi kwa ajili ya kitambo hicho tu.’ (1 The. 5:3) Wanaamini kwamba wanaweza pia kujifaidi wawezavyo kutokana na maisha maadamu wanaweza kufanya hivyo, kwa maana sayansi (waliyoitumainia) haiwezi kuzuia kifo. Kwa mfano, akitoa maelezo juu ya uvumbuzi wa sayansi, mwandishi mmoja wa habari alikubali kwamba mtaalamu wa Tübingen Friedhelm Shneider amethibitisha kwamba “hakuna kinachotegemeza [maoni ya] kwamba kifo kimefungamana na wazo la maisha kuwa ni cha lazima.” Mwandishi huyu alikubali kwamba “majimaji ya chembe yanayoingia damuni yakichanganywa ifaavyo na kila chembe moja mtu hawezi kufa tena.” Hata hivyo ilimlazimu aongezee, “Isipokuwa: Kwa sasa hakuna uwezekano wa kufanyiza mchanganyiko huu ufaao!” Kwa hiyo, shauri la watu wengi ni ‘Ishi kwa ajili ya leo!’ kwa maana kifo chaelekea kuwa kisichoepukika.

4. (a) Je! haya ndiyo maoni ya mashahidi wa Yehova? (b) Lakini imempasa kila mmoja wetu afikirie nini?

4 Ingawa hivyo, ni maoni yaliyo tofauti namna gani yanayoonekana kati ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova! Maoni yao si ya “tule, na tunywe, maana kesho tutakufa” kwa sababu ya kutegemea bahati mbaya. (1 Kor. 15:32) Bali, wao wanapendezwa sana sana na wakati ujao, wakiutazamia. Kwa kweli, maisha yao yote na kuwaza kunategemea umilele, si kuwako kwa kitambo kwenye mipaka. Lakini, je! ndivyo ilivyo kwako wewe kama mtu mmoja? Ili tuone namna iwezavyo kuwa hivyo, na tuufikirie “umilele” kwa habari ya Mungu na makusudi yake.

UMILELE NI WA ASILI KATIKA IBADA YETU

5. Kwa sababu gani ibada yetu inategemea umilele?

5 Yaweza kusemwa kwa kufaa kwamba ibada ya Kikristo inategemea umilele, kwa maana Mungu mwenyewe ni wa milele. Huenda hiyo ikawa vigumu kwa wanadamu kufahamu​—kutokuwa na mwanzo kwa Mungu. Lakini ebu ifikirie milima, dunia nzima, ndiyo, na ulimwengu wote. Je! hivi ni vitu vipya, vya majuzi? Wanasayansi wanasema ulimwengu wote ni wa maelfu ya mamilioni ya miaka iliyopita. Kwa hiyo je! Muumba wao asiwe ni wa zamani hata kupita wakati huo? Kwa ufahamu, mtume Paulo aliandika kwamba ‘uweza wa milele na Uungu’ wa Yehova unaonekana wazi kutokana na alivyoviumba Yeye.​—Rum. 1:20.

6. Biblia inaonyesha nini juu ya wakati ujao wa Mungu?

6 Umilele wa Mungu ni wa wakati ujao pia. Waandikaji wa Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia walijua Mungu hatakufa kamwe, na hivyo, kwamba Yehova atatawala kwa umilele wote ujao. Mtunga zaburi alitangaza hivi: “Yehova ni Mfalme kwa wakati usiojulikana [Kieb., ‘ohlam], hata milele [Kieb., ‘adh] (Zab. 10:16; Kut. 15:18, NW) Na katika kitabu cha mwisho cha Biblia mtume Yohana alitaja sauti kutoka mbinguni zilizosema hivi juu ya Bwana Yehova: “Atamiliki hata milele na milele.” Hapa mwandikaji Yohana alitumia wingi wa fungu la maneno ya Kigiriki, yanayomaanisha kwa halisi “hata vizazi vya vizazi.” (Ufu. 11:15; 1 Tim. 1:17) Kwa hiyo, kwa habari ya wakati ujao Yohana alijua bila shaka kwamba Muumba wetu atatawala “hata vizazi vya vizazi.” (Kingdom Interlinear Translation) Hii yaweza kuwa na maana gani kwako sasa na wakati ujao?

7. Je! kuwako milele kunahusiana na viumbe vyote vya Mungu vilivyo hai duniani? Na namna gani juu ya mwanadamu?

7 Si viumbe vyote vya Mungu vilivyo hai vilivyo vya milele. Twajua kwamba mimea, hata miti inayoishi muda mrefu sana, mwishowe inakufa. (1 Pet. 1:24) Na hakuna ushuhuda wa Biblia wa kwamba Mungu alikusudia wanyama mmoja mmoja waishi milele. Lakini ilikuwa tofauti kwa habari ya wanadamu. Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza tumaini la kutokufa kamwe. Kwa kutii wangaliweza kutumainia kuishi milele. (Mwa. 2:17) Kusudi la Mungu kwa habari hii halikukatizwa na kuanguka kwa mwanadamu kwenye dhambi. Lakini Biblia yaonyesha kwamba kusudi lake Yeye la kuwafanya wanadamu watiifu waishi milele duniani litatimizwa pasipo shaka. Hilo litatimizwa kwa njia ya ufalme wa Mungu, ambao, kama unavyosimuliwa katika Ufunuo 12:1-5, ulizaliwa mbinguni katika mwaka wa 1914 C.E. Ndiyo, tangu wakati huo imefaa kusema hivi: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu.”​—Ufu. 11:15.

WATAWALA WA MILELE KATIKA UFALME

8. Kwa sababu gani ufalme wa Mungu unakaziwa katika Biblia?

8 Ufalme huu, ambao kwao uzima wa milele wawezekana kwetu, ni serikali ya kimbinguni. Yesu mwenyewe ndiye Mtawala mkuu, naye atakuwa na watawala wenzake 144,000 ambao wamechaguliwa kati ya wanadamu na kuitwa na Mungu kwenye uzima wa kimbinguni. (Rum. 8:16, 17; Luka 22:29; Ufu. 5:9, 10; 14:1) Maana kuu ya ufalme huu yaonekana katika mkazo ambao Mungu aliutilia katika Biblia. Ndiyo iliyokuwa habari kuu ya kuhubiri kwa Yesu. (Mt. 4:23) Pia, mengi ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaelekezwa kwa Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho, kutia na ahadi za uzima wa milele.

9. Twawezaje kuelewa alivyomaanisha Yohana kwa “uzima wa milele” katika 1 Yohana 2:25?

9 Kwa mfano, mtume Yohana aliandika hivi katika 1 Yohana 2:25: “Hii ndiyo ahadi aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele.” Je! alimaanisha uzima wa milele duniani, au uzima usiokoma mbinguni? Yohana alijua kwamba kusudi la Mungu tangu wakati wa Adamu lilikuwa kujazwa kwa dunia na waabudu wa kweli ambao wangepokea uzima wa milele. Lakini katika maneno haya Yohana alikuwa akisema na Wakristo waliokuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu na kuitwa kwenye uzima wa kimbinguni. (1 Yohana 2:20) Hivyo, aliendelea kusema hivi: “Haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa [Mungu] atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo.”​—1 Yohana 3:2.

10. Kwa kuahidi kwamba wanafunzi wake ‘wasingeona mauti milele,’ Yesu alikuwa na maana gani?

10 Ahadi kama hii ya uzima wa milele yaonekana katika maneno ya Yesu: “Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele.” (Yohana 8:51; 6:51, 58; 11:25, 26; 12:25) Kwa wazi Kristo hakumaanisha kwamba mitume waaminifu na wengine ambao karibuni wangetiwa mafuta kwa roho takatifu wasingezeeka wala kufa. Yeye alijua kwamba lazima wafe ili wapokee uzima wa kimbinguni. Miezi fulani mapema Yesu alikuwa amewaambia kwamba yeye mwenyewe angekufa kisha afufuliwe. (Mt. 16:21; 17:22, 23; Yohana 2:19-22) Wafuasi wake wote waliotiwa mafuta iliwapasa kufa pia wakawe watawala wasioweza kufa katika ufalme wake. (1 Kor. 15:42-44, 49, 53, 2 Tim. 4:18) Basi ni kwa njia gani ambavyo hao ‘wasingeona mauti milele’? Kwa sababu kwa kuwa waaminifu hata kufa wasingedhuriwa hata kidogo na mauti ya pili, kama inavyoonyeshwa wazi na Ufunuo 2:10, 11. Hivyo, baada ya kufufuliwa, watakuwa wafalme milele mbinguni, kwa faida ya watumishi wote wa Mungu duniani. (Ufu. 22:5) Lo! baraka namna gani!

11. Twawezaje kuwa na hakika kwamba uzima wa milele duniani wawezekana kwa watu walio hai wakati huu?

11 Walakini, tumaini hili la uzima wa milele si la wale walio sehemu ya ufalme wa kimbinguni peke yao. Hasha. Alipokuwa akisema juu ya wakati huu au kizazi ambacho kingeona kusimamishwa kwa Ufalme, Yesu bila shaka aliahidi uzima wa milele wa kidunia. Huu ndio wakati wa kutenganisha “kondoo” na “mbuzi.” (Mt. 25:31-33) Nayo ni thawabu gani ambayo Yesu aliahidi kwa “kondoo” wanaosaidia na kutumikia pamoja na “ndugu” zake waliotiwa mafuta lakini ambao wenyewe si “ndugu” hao wa Kristo wenye tumaini la uzima wa kimbinguni? Yeye aliahidi kwamba wenye haki hawa wataingia katika “uzima wa milele,” ndiyo, uzima wa papa hapa duniani. (Mt. 25:46) Lo! ni tumaini lenye kusisimua namna gani, kuishi milele katika dunia, ambayo Mungu amekusudia iwe paradiso! Lakini hiyo hasa ina maana gani kwako? Je! waonyesha kwamba unaamini hivyo? Je! inaongoza maamuzi yako ya kila siku? nia yako juu ya kazi yako? masomo unayoyachagua shuleni? kama utaoa au kuolewa karibuni? Ndiyo, je! wewe unaishi kwa kuutumainia umilele?

NI ZAIDI KULIKO TUMAINI TU LA UZIMA WA MILELE

12. Ni katika maana gani tulivyo na pendeleo hasa?

12 Uwezekano wa kuhesabiwa kati ya “kondoo” watakaoingia katika uzima wa milele duniani bila kufa wapaswa uusisimue uaminifu wako kwa Mungu. Wewe umo katika hali ya kuyaona mambo ambayo watumishi wengi waaminifu wa Mungu karne zilizopita waliweza kuyatumainia tu. Angalia namna hili lilivyokuwa kwa habari ya Mfalme Daudi.

13. Kwa wazi Daudi alikuwa na maana gani kwa aliyoyaandika katika Zaburi 37:11, 29?

13 Katika Zaburi 37:11, 29 Daudi aliandika hivi: “Wenye upole watairithi nchi, . . . Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Kwa kusema hivi kwa wazi alimaanisha namna Nchi ya Ahadi ilivyopaswa kuwa siku zake na katika vizazi vitakavyofuata. Kulingana na agano la Mungu kwa Ibrahimu, wapagani waovu waliokuwa wameishi nchini walipaswa waondolewe kabisa. (Mwa. 15:18-21; 17:8; Kum. 7:22; Yos. 21:43-45) Hivyo kila kizazi cha waabudu wenye haki kilichofuata chenye kufanyiza taifa la Israeli kingaliweza kukaa nchini, sehemu ya dunia aliyowapa Mungu. (Kum. 30:20) Walakini, twajua kwamba Waisraeli walio wengi walionekana kutoaminika, na kwa hiyo hawakulitimiza kusudi la Mungu katika habari hii. Kwa kweli, mwishowe Mungu aliwaacha Waashuru na Wababeli waishinde nchi na kuiacha bila wakaaji kwa kitambo.

14. Yesu alionyesha kwamba Zaburi 37:11, 29 ilikuwa na maana gani kubwa zaidi?

14 Hata hivyo, aliyoyaandika Daudi katika Zaburi 37 yalikuwa mwangaza mdogo tu wa tumaini ambalo Wakristo leo wanaweza kuwa nalo. Kwamba maneno ya Daudi yalikuwa na matumizi makubwa zaidi ya utawala wa Ufalme juu ya dunia nzima yaonyeshwa na uhakika wa kwamba Yesu aliitaja Zaburi ya 37 katika Mathayo 5:5. Je! Kristo alisema kwamba ilitimia kabisa wakati uliopita? Sivyo, kwa maana aliielekeza kwenye wakati ujao, akisema kwamba ‘wenye upole watairithi nchi.’ Ndiyo, wapole hao watakaokuwa pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni watatawala dunia hii. (Ufu. 5:9, 10) Yesu alijua kwamba Ufalme ungeitawala dunia kwa haki milele. Kwa hiyo, dunia yenyewe itajazwa na “wenye haki” ambao “watakaa humo milele.” Hivyo, kwa uongozi wa roho, Daudi alikuwa amekwisha simulia mwisho utakavyokuwa wakati Yehova atakapolitimiza kusudi lake kwa dunia yetu. Wakristo wanaweza kufurahi kwamba mambo ambayo Daudi aliyaona kwa mbali, na ambayo angeweza kuyashiriki kwa kufufuliwa tu wakati ujao, wanaweza kuyaona. Wale ambao Bwana anawaweka mkono wake wa kulia kama “kondoo” wana nafasi ya ‘kukaa milele’ katika dunia ya paradiso itakayotawaliwa milele kutoka mbinguni.

15. Maoni ya Mika yalikuwa nini kwa habari ya kumwabudu Yehova, nayo hii yamaanisha nini kwetu?

15 Basi, inafaa namna gani tukaze fikira zetu, mipango na matumaini juu ya kumtumikia Yehova tukiutumainia umilele! Fikiria namna ambavyo Daudi, Ibrahimu na manabii kama vile Isaya na Mika wangalisisimka kuwa hai sasa wakiwa na pendeleo hilo. Alipokuwa akisimulia kwa unabii kurudishwa kwa ibada safi kati ya Wayahudi baada ya kurudi kwao kutoka utumwani mwaka wa 537 B.C.E., Mika aliionyesha nia ambayo yeye na waabudu wengine wa kweli walikuwa nayo: “Kwa maana mataifa yote, kwa upande wao, watatembea kila moja katika jina la mungu wake; lakini sisi, kwa upande wetu, tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu kwa wakati usiojulikana, hata milele.” (Mik. 4:1-5, NW; Isa. 65:18) Yeye alikuwa ameamua kabisa kumwabudu Mungu milele. Wakati huo Mika hakuwa na uzima wa milele. Mpaka wakati huo kifo kilikuwa hakiepukiki kwa wanadamu wenye kufa. Lakini Mika angemtumikia Mungu mpaka siku ya kufa kwake, na akifufuliwa katika Taratibu Mpya angeuendeleza utumishi wake kana kwamba haukukatizwa. Lo! Mika alikuwa na maoni mema namna gani! Lakini je!, sisi, ambao wengi wetu wana tumaini la kutembea hasa katika jina la Mungu milele, bila ya kukatizwa, tusiwe na maoni yale yale?

SI KUTUMIKIA MPAKA TAREHE FULANI TU

16. Wale waliopata kuwa Wakristo katika karne ya kwanza C.E. waliuonaje utumishi wao?

16 Kama sisi wenyewe tuna tumaini la uzima mbinguni pamoja na Yesu au katika paradiso ya kidunia, ni lazima kukumbuka kwamba mradi wetu si tarehe yo yote iliyowekwa, bali ni umilele. Katika habari hii, twaweza kuwaiga wale waliokuwa Wakristo kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 C.E. Kwa kufaa waliutazamia mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi ambao ungetukia karibuni, wakati wa “dhiki kubwa” ambayo Yesu alisema ingekuja katika kizazi hicho. (Mt. 24:3, 21, 22, 34) Lakini je! wao walikuwa wameamua kutumikia mpaka tarehe au tukio fulani tu, wakati walipotubu wakawa Wakristo? Hasha. Waliyokuwa wamejifunza na kuyakubali, kama yale ambayo Petro alimhubiri Kornelio na nyumba yake, hayakuwa kwamba walipaswa wawe Wakristo mpaka tarehe fulani tu iliyokuwa ikikaribia ifike. Bali, Mungu ‘aliwajalia hata mataifa nao toba liletalo uzima,’ uzima usiokoma kama Wakristo.​—Matendo 10:34-43; 11:18.

17. Yuda alionyeshaje wazi maoni haya?

17 Hivyo, wakati ndugu wa mama-mzazi mmoja na Yesu Yuda alipoiandika barua yake iliyoongozwa kwa roho karibu mwaka wa 65 C.E., karibu mwaka mmoja kabla Warumi hawajaushambulia Yerusalemu kwa mara ya kwanza, yeye hakutaja tarehe fulani ya mwisho. Bali, aliandika hivi: “Dumuni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kuutumainia uzima wa milele.” (Yuda 20, 21, NW) Alijua kwamba mradi ulikuwa kumtumikia Mungu milele. Hata kama “dhiki” juu ya taratibu ya Kiyahudi ingekuja baada ya miaka miwili, au mitatu, au baada ya hapo, hiyo isingeubadili uhakika wa kwamba wao wangeendelea tu kumtumikia Mungu.

18. (a) Tuko wapi katika kipindi cha wakati? (b) Orodha ya tarehe za Biblia yaonyesha nini, bila ya kuweka tarehe?

18 Na ndivyo ilivyo leo kati ya Wakristo wa kweli wanaojua kutokana na unabii wa Biblia kwamba mwisho wa hii taratibu nzima ya mambo iliyo mbovu unakaribia sana. Kweli, orodha ya tarehe za Biblia iliyo sahihi kupita zote iwezayo kupatikana yaonyesha kwamba miaka 6,000 ya kuwako kwa mwanadamu itamalizika mwaka wa 1975.a Kwa hiyo Wakristo hawa wanapendezwa sana sana kuona kama hiyo italingana na kutokea kwa “dhiki kubwa” ya siku zetu itakayowaondoa waovu wote duniani. Inaweza. Lakini wao hata hawajaribu kutabiri wakati barabara ambapo uharibifu wa taratibu mbovu ya mambo ya Shetani utakapotokea. Wao wanaridhika wangoje na kuona, wakijua kwamba hakuna mwanadamu duniani aijuaye tarehe.​—Mt. 24:36.

19. Hii inaongoza kwenye matumaini gani kati ya watumishi wa Mungu leo?

19 Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanasadiki kwamba Mungu atauleta mwisho wa hii taratibu isiyomcha Yeye katika wakati wake YEYE. “Dhiki kubwa” itakapoanza, tutaweza kuitambua. Kwa hiyo badala ya kufikiri-fikiri juu ya tarehe fulani, kana kwamba mradi wetu ni tarehe hiyo, twaweza kuifikiria kazi ya maana zaidi ya kuhubiri aliyosema Yesu wanafunzi wake wangeifanya katika kipindi hiki. (Marko 13:10) Hivyo, wakati wo wote “dhiki” itakapotokea, tutapatikana wenye shughuli na wenye bidii kuutimiza mgawo tulio nao. Nayo matumaini yetu ya wakati ujao hayatategemea tarehe fulani, bali tutakuwa tukitumikia kwa kutumainia umilele, kama vile Yuda alivyowasihi Wakristo wafanye.

ONYESHA IBADA YA MILELE KATIKA MWENENDO WAKO NA MAAMUZI YAKO

20, 21. (a) Maisha ya mtu yanaweza kuonyesha nini juu ya maoni yake ya wakati ujao? (b) Je! haya ndiyo maoni ya hekima kuwa nayo?

20 Imani yetu imara kwamba twaweza kumtumikia Mungu milele yapaswa pia iwe wazi katika mambo mengine zaidi ya kuhubiri kwetu. Imepaswa iongoze mawazo yetu ya kila siku na matendo. Hii inatajwa kwa sababu huenda mtu akasema kwamba anakubaliana na yote tuliyoyaangalia kufikia hapo lakini aonyeshe wazi kwa maisha yake ya kila siku kwamba yangali hayabadili mawazo yake na matendo. Huenda akaonyesha kwamba kwa kweli anaishi kwa ajili ya SASA tu. Lo! namna hilo lingekuwa jambo la kusikitisha!

21 Uhakika wenyewe wa kwamba waabudu wa kweli wanaweza kuwa na mahali katika kusudi la milele la Yehova wahakikisha namna sasa ilivyo muda mfupi. Inalinganika na nusu inchi katika kijiti cha kupimia cha maelfu ya maili, ikiwa waweza kukiwazia. Je! lingekuwa jambo la busara kuongoza maisha yote ya mtu kwa nusu inchi hiyo, kana kwamba hilo ndilo jambo kubwa? Namna alivyosawazika na alivyo mwenye hekima mtu aishiye sasa kwa kusudi la kuishi milele, na anayekadiri mambo kwa kufikiria namna yatakavyoihusu hali yake ya milele!

22, 23. (a) Maandiko yanawasaidia Wakristo waelewe nini juu ya ndoa? (b) Kwa kutofautiana na ulimwengu, vijana wa Kikristo watumikiao kwa kuutumainia umilele wana nia gani juu ya ndoa?

22 Mfano mmoja wa kuonyesha kuishi kwa kuutumainia umilele wahusu ndoa. Maelekeo ya vijana wa kiume na wa kike juu ya ndoa yanajulikana. Ndoa ni mpango ambao Mungu alitoa nao una baraka nyingi. Lakini kati ya wanadamu wasiokamilika una magumu yake pia na upungufu. (1 Kor. 7:28) Mtume Paulo alijua hivi, naye alipendekeza kutooa au kutoolewa kwa Wakristo ambao wangeweza kuiendeleza hali hiyo bila ya kusumbuliwa-sumbuliwa na nyege. Vijana hao wangeweza “kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine” yanayohusiana na maisha ya ndoa. Naye Paulo alisema kwamba faida hii ya kutooa au kutoolewa ilikuwa ya thamani sana kwa maana “muda ubakio si mwingi.”​—1 Kor. 7:29-38.

23 Kwa vijana wengi wasiouamini uwezekano wa kumtumikia Mungu milele, nia ni, ‘Kwani tuhangaike na kujiweza. Tukitaka kufurahia ngono au kuoa na kuolewa, na tufanye hivyo. Nani ajuaye ya wakati ujao?’ Lakini Mkristo kijana anayetumikia kweli kwa kuutumainia umilele hafanyi haraka haraka hivyo. Yeye ana nia ya kungojea mpaka “amepita uzuri wa ujana wake” aamue kama ingekuwa afadhali kwake aoe au kuolewa au sivyo. Kwa sasa anaweza kuiona faida ya kutooa au kutoolewa: “kujitoa kusikogawanyika kwa Bwana.” (1 Kor. 7:35, Revised Standard Version) Ikiwa baadaye anaamua kuoa au kuolewa, wakati huo atakuwa tayari zaidi kuyachukua madaraka yanayohusika. Kutumikia kwake akiutumainia umilele kunamsaidia aepuke kuishi kwa ajili ya “sasa” tu. Na angalia kwamba, hii yaonyeshwa katika maamuzi yake ya kila siku.

24. “Umilele” unayahusuje maoni ya mtu juu ya mali za kimwili?

24 Imani ya mtu ya kutumikia milele imepaswa pia ihusu maoni ya mtu juu ya fedha na mali. Watu wengi ulimwenguni wana nia ya ‘kipate maadamu unaweza’ kwa habari ya vitu hivi. Nayo matangazo yanakazia kununua vitu vipya sasa. Lakini wewe waitikiaje? Maoni yako ni nini? Unaposhawishwa katika mambo ya kutafuta vitu vya kimwili, je! unaufikiria umilele? Imekupasa ufanye hivyo, kwa maana baada ya kuzionyesha hatari za kupenda fedha na mali za kimwili, Biblia inapendekeza kuufikiria uzima wa milele. (1 Tim. 6:6-12) Kwa hiyo unapokazwa moja kwa moja au kwa werevu upate fedha au mali zaidi, jiulize hivi: ‘Miaka elfu tangu sasa, nitasikitika kwamba niliamua nisipate kazi ya ziada ambayo ingaliniwezesha kununua gari au mashua mpya?’ Au ujiulize, ‘Miaka milioni moja katika Taratibu Mpya, je! nitatazama nyuma na kuona nilifanya uamuzi mbaya kwa kukataa kazi ya ziada nisiikose mikutano yangu ya Kikristo?’ Ndiyo, umilele umepaswa uongoze maisha zetu za kila siku na kuwaza.

25. Maoni yafaayo juu ya umilele yana thamani gani wakati wa kuvumilia majaribu mbalimbali?

25 Maoni aya haya​—kutumikia kwa kuutumainia umilele​—yatawasaidia Wakristo wavumilie kwa furaha. Ingawa upinzani, magonjwa na uzee yanaweza kuwa majaribu magumu kuvumilia, ukilinganishwa na umilele, uvumilivu huu ni wa kitambo tu. Twaweza kuwa na umilele mbele yetu, kama vile mtume alivyosema: “Ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”​—2 Kor. 4:16-18; Mt. 19:29.

26. Basi, imempasa Mkristo awe na maoni gani juu ya wakati ujao?

26 Basi, kama Wakristo na tujitahidi kila siku tukumbuke kwamba Mungu wetu ni wa milele na kwamba imetupasa tumtumikie tukiutumainia umilele. Naye atatusaidia kwa kuuongeza ujuzi wetu wa kweli yake ya milele na kutupa roho takatifu yake, inayoahidiwa kwa watumishi wake kama msaidizi milele. (2 Yohana 2; Yohana 14:16, 17) Hivyo utumishi wetu kwake hautakuwa wa sasa tu, wala wa kipindi kidogo cha maisha. Bali, tutamtumikia yeye milele, kwa maana kwake yeye na uwepo “utukufu . . . hata vizazi vyote vya kizazi cha vizazi.”​—Efe. 3:20, 21, Kingdom Interlinear Translation.

​—Kutoka The Watchtower, June 15, 1974.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama Aid to Bible Understanding, kurasa 322-348.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki