“Ziwa la Moto” na Kusudi Lake
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. “Ziwa la moto” linatajwa wapi katika Biblia, na ni akina nani au ni vitu gani vinavyoingia humo?
“ZIWA la moto” ni nini? Twauona usemi huu katika Biblia katika kitabu cha Ufunuo tu, na humo unatajwa katika sura ya 19 mpaka ya 21 tu. Mtajo mwingine pia unaonekana katika Mathayo 25:41.
2 Ni nani au ni nini kinachoingia katika “ziwa la moto”? Kati ya vitu vinavyotajwa yumo “mnyama” na “nabii wa uongo.” Mauti na Hades vinatiwa katika “ziwa” hili. Twasoma pia kwamba Ibilisi (pamoja na mashetani zake) anatupwa katika “ziwa” baada ya shambulio lake la mwisho juu ya enzi kuu ya Mungu.—Ufu. 19:20; 20:10, 14.
MFANO
3. Onyesha kwamba “mnyama” si mnyama-mwitu wa halisi.
3 Tunapoyachunguza maandiko haya twaona kwa vyepesi kwamba “ziwa la moto” si kiziwa cha halisi cha moto. “Mnyama” ni wa mfano, kama ilivyoonyeshwa mapema katika Ufunuo sura ya 13, “sanamu” yake ikisimuliwa katika sura ya 17, ambapo twaambiwa kwamba vichwa saba vya “mnyama” vinafananisha falme saba ‘zenye mfano wa milima.’ Hizi zinaeleweka na wafafanuzi wa Biblia kuwa mamlaka saba za ulimwengu za historia ya Biblia. Zile tano zilizokuwa ‘zimeanguka’ zilikuwa Misri, Ashuru, Babeli, Amedi-Ajemi na Ugiriki. Moja ‘iliyokuwako’ wakati mtume Yohana alipoandika ilikuwa Rumi. Kulingana na matukio ya kweli, ya saba imekuwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza na Waamerika.—Ufu. 17:9, 10; linganisha Danieli sura ya 8.
4. Onyesha kwamba “nabii wa uongo” si mtu.
4 Vivyo hivyo “nabii wa uongo” si mtu, bali ni taratibu au tengenezo. “Nabii” anajidai kuwa na habari zilizoongozwa kwa roho kuwaonyesha wengine njia ya kufuata. “Nabii wa uongo” angepotoa wengine, kuwaondoa kwa Mungu na kuwaelekeza kwenye ibada ya uongo. Huyu “nabii wa uongo” anafanya nini kutimiza kusudi hilo? Anaonyeshwa katika umbo jingine katika Ufunuo 13:11-17 kama “mnyama” mwenye pembe mbili. Akiwa hivyo anaonyeshwa akifanya mbele ya “mnyama” mwenye vichwa saba ishara ambazo kwazo anawadanganya “wale walioipokea ile chapa ya huyo mnyama, nao walioisujudia sanamu yake.”—Ufu. 19:20.
5. Kutokana na mazungumzo yaliyotangulia, twaweza kufanya mkataa gani juu ya kama “ziwa la moto” ni la halisi?
5 Kwa kuwa “mnyama” na “nabii wa uongo” ni wa mfano, kwa lazima “ziwa la moto” ni la mfano.
6, 7. Ni sababu gani nyingine zinazouunga mkono mkataa wa kwamba “ziwa la moto” si kiziwa cha halisi cha moto?
6 Unaoendelea kuuunga mkono mkataa huu ni uhakika wa kwamba jambo lisilogusika, “mauti,” linatupwa pia katika “ziwa la moto.” Mauti haiwezi kuchomwa kwa njia ya halisi.
7 Zaidi ya hayo, mashetani wanatupwa katika “ziwa” hilo. Hawa ni malaika, watu wa kiroho. Wakiwa wa kiroho, hawawezi kuumizwa na moto wa halisi, unaofanyizwa vitu vilivyochanganywa vinapowashwa. Kwa kweli, mara nyingi twasoma juu ya watu wa kiroho wenye kujionyesha kwa wanadamu katika mwali wa moto.—Kut. 3:1-5; Matendo 7:30; Amu. 13:20; Zab. 104:4; Dan. 7:9, 10.
8. (a) “Ziwa la moto” ni mfano wa nini? (b) Kwa sababu gani inaitwa “mauti ya pili”?
8 Kwa hiyo, “ziwa la moto” ni mfano wa nini? Biblia inasema kwamba linamaanisha au kufananisha, “mauti ya pili.” (Ufu. 20:14) Hii haiwezi kuwa na maana ya kwamba kila kitu kinachoingia humo kinakufa mara ya pili, kwa maana “mauti na Hades (NW)” havijapata kufa au kutoweka zamani. Usemi “mauti ya pili” unaitofautisha mauti hii, ambayo ni ya milele na isiyo na ufufuo, na mauti iliyoletwa juu ya taifa la kibinadamu na Adamu. Mauti ya Adamu ni “namna” moja ya mauti, mauti ambayo wanadamu wote wanarithi kwa kutokupenda kwao. “Mauti ya pili” ni “namna” nyingine ya mauti. Watu wanaoingia katika “mauti ya pili” wanaistahili kwa sababu ya kuchagua kwao wenyewe kwa makusudi dhambi na uadui juu ya Mungu. Hii ni wazi kwa tendo la wale ambao Biblia inawasema kama wakihukumiwa kupata “mauti ya pili.”
9. Tuna ushuhuda gani zaidi katika kitabu cha Ufunuo juu ya “ziwa la moto” lilivyo, na ni nani kati ya wanadamu wanaoingia humo?
9 Ushuhuda zaidi juu ya kinachofananishwa na “ziwa la moto” na wale ambao mwishowe wanapata hukumu ya mauti hii unaonekana katika Ufunuo 21:7, 8. Baada ya kuyasimulia matokeo mazuri yatakayoletwa duniani na Yerusalemu Mpya, unabii unayataja maneno ya Mungu, ukisema hivi: “Yeye ashindaye atayarithi haya, nami nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwanangu. Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.” Watu wote wanaochagua kuishi kwa njia hiyo kuudharau mpango wa Mungu wa dhabihu ya Kristo wa kuwaondoa katika hali hiyo ya aibu watafutiliwa mbali milele.
10. Ni nani, kati ya viumbe vyote vilivyo hai, wanaoingia katika “ziwa la moto” mwishowe?
10 Kwa hiyo hukumu ya Mungu yenye moto yawajia wale wote waliojikiri kuwa adui zake. Juu ya wale wa kundi la “Gogu na Magogu” wanaomfuata Ibilisi katika shambulio lake la pili juu ya enzi kuu ya Mungu mwishoni mwa miaka elfu, twasoma hivi: “Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala.” Wanaingia katika “mauti ya pili.” Vile vile “ziwa la moto” linateketeza wanadamu wote wasioyatii “mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu” vya maagizo wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu. Hakuna wo wote kati ya hawa wanaoona majina yao yameandikwa katika “kitabu cha uzima.” (Ufu. 20:9, 12, 15) Adhabu iyo hiyo ya “mauti ya pili” inafikilizwa juu ya Shetani na mashetani zake, wanaotupwa ndani ya “ziwa la moto.” Wote wanakufa milele.
11, 12. Twajuaje kwamba hamna dalili ya uzima katika “mauti ya pili” na kwamba ni ya daima?
11 Hamna dalili ya uzima katika “mauti ya pili,” ambayo ndiyo adhabu ya milele kwa wale wasiomtii Mungu kwa makusudi. Hakukuwa na uzima hata kidogo katika namna ya kwanza ya mauti, iliyowajia wazao wa Adamu kwa sababu ya dhambi yake ya kwanza. Namna hiyo ya mauti ingalikuwa ya daima kama isingalikuwa ni kwa ajili ya upendo na fadhili zisizostahili za Yehova Mungu katika kuitoa dhabihu ya Kristo. “Mauti ya pili” ni ya daima, kwa maana hakuna dhabihu ya kulipia dhambi kwa wale wanaoingia ndani yake. Mtume Paulo aliandika hivi:
12 “Kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; bali kuna kuitazamia hukumu kwenye kutisha, na ukali wa moto ulio tayari kuwala wao wapingao.”—Ebr. 10:26, 27.
HAKUNA KUTESEKA MTU AKIJISIKIA
13. Twajuaje kwamba hakuna kuteseka mtu akijisikia katika “ziwa la moto”?
13 Wale waliomo katika “ziwa la moto” hawana uzima. Majina yao hayaandikwi katika “kitabu cha uzima.” Nao uzima ni uzima, uwe unatumiwa katika raha au kupata maumivu. Kwa hiyo, hakuna kuona maumivu au taabu katika “ziwa la moto,” kwa maana hamna uzima hata kidogo humo. Basi, kwa sababu gani Biblia inawasema Ibilisi, “mnyama” na “nabii wa uongo” kama ‘wakiteswa mchana na usiku hata milele na milele’ katika “ziwa” hili?—Ufu. 20:10.
14, 15. Ni ‘mateso’ gani ambayo Shetani na mashetani zake watapatwa nayo katika “ziwa la moto”?
14 Ni kwa sababu wako katika mateso ya kuzuiwa. Wakati Yesu alipokuwa duniani, mashetani walimsihi asiwaagize waende zao kuingia “shimoni.” (Luka 8:31) Katika habari inayolingana juu ya kisa iki hiki, mashetani walimwuliza Yesu hivi: “Je! umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?” (Mt. 8:29) Kutiwa “shimoni” huku kutakuwa ‘mateso’ kwa maana kutakuwa ni kuzuiwa.
15 Kwa hiyo, Shetani na mashetani zake watapatwa na ‘mateso’ ya kuzuiwa kwa kutupwa “shimoni” kabla tu ya utawala wa miaka elfu wa Kristo. Watazuiwa na utendaji wote wakati wa hiyo miaka elfu. Kisha watafunguliwa baada ya miaka elfu kumalizika. (Ufu. 20:7; linganisha Ufunuo 11:7; 17:8.) Baada ya shambulio la mwisho juu ya enzi kuu ya Mungu, Ibilisi na mashetani zake wanatupwa ndani ya “ziwa la moto,” wanamopata ‘mateso’ ya kuzuiwa milele katika “mauti ya pili.” Wanaharibiwa kabisa, wasionekane tena. Zaidi ya hayo, mambo yote waliyoyatimiza, kazi zao zote, zitafutwa zitoke katika ulimwengu wote.—1 Yohana 3:8.
16, 17. Toa mifano zaidi inayoonyesha hakuna kuteseka mtu akijisikia katika ‘‘ziwa la moto,” “mauti ya pili.”
16 Ukweli wa kwamba huku kutiwa ndani ya “ziwa la moto” hakumaanishi kuteseka mtu akijisikia waonyeshwa kwa sababu “mnyama” na “nabii wa uongo,” wote wawili wakifananisha taratibu au matengenezo, wanasemekana ‘kuteswa mchana na usiku.’ Lakini taratibu au matengenezo hayawezi kuona maumivu. “Ziwa la moto” linawaharibu, linawaangamiza. Wanazuiwa wasitende, milele. Matengenezo hayo maovu hayatatokea tena kamwe kutawala au kusumbua wanadamu.
17 Pia, mauti na Hades, kaburi la kawaida la wanadamu, vinaharibiwa katika “ziwa la moto,” kwa maana mauti ya Adamu itakuwa imekwisha futiliwa mbali kabisa nayo Hades itakuwa imekwisha achwa ikiwa tupu nayo haitapokea wafu hao tena. (Ufu. 20:14) Bila shaka mambo haya mawili yasiyo na uhai hayawezi kuona mateso, bali yanaweza kuzuiwa, kuondoshwa, milele.
KUSUDI LAKE
18. (a) “Ziwa la moto” linatumikia kusudi gani? (b) Je! “ziwa la moto” litawatisha wale watakaokuwa wamelipita jaribu mwishoni mwa miaka elfu?
18 “Ziwa la moto,” linalomaanisha au kufananisha “mauti ya pili,” ‘linachomwa kwa kiberiti’ pia. (Ufu. 21:8) Kiberiti kinawaka upesi hata wakati wa baridi, kikielekea kuteketeza vitu visivyoweza kuteketea upesi kwa njia nyingine yo yote. Zamani kiberiti kilitumiwa kwa ufukizo. Hivyo “ziwa liwakalo moto na kiberiti” linaweza kufananisha uharibifu wa milele wa kila kitu na kila mtu ‘aliyeuchafua’ ulimwengu wote, akiendesha mazoea machafu, akiipinga enzi kuu ya Mungu na kuliletea jina lake aibu. Ijapokuwa Mungu anaweza sikuzote kulitumia juu ya wasiotii kwa makusudi, “ziwa la moto” au “mauti ya pili” halitawatisha wale waliohakikishwa kuwa waaminifu kupita jaribu baada ya Shetani kufunguliwa ikiisha kumalizika miaka elfu ya utawala wa Kristo. Waokokaji waaminifu wa jaribu hilo watapata uhakikisho wa Mungu wa ulinzi na kuendelezwa kwa uzima wao milele.—Rum. 8:21.
19, 20. (a) Ni kwa njia gani “ziwa la moto” si jambo linalopingana na utu wa Yehova? (b) Katika mchanganuo wa mwisho, ni nani watakaopata adhabu ya “ziwa la moto”?
19 Hivyo “ziwa la moto” ni jambo la maana katika makusudi ya Mungu. Halipingani na utu wa Yehova Mungu, asiyewazia wala kupendelea mateso ya milele ya mtu ye yote akijisikia. (Yer. 19:5; 32:35) Walakini, inapatana na utu wake wa haki na fadhili za upendo kwa Mungu kufutilia mbali wachokozi waovu milele. Kwa maana ni lazima haki ifikilizwe katika ulimwengu wote kwa ajili ya amani na utengemano wa wale wanaotaka kufanya yaliyo haki.—Zab. 145:20.
20 Yehova si mtawala atakayeachilia uvunjaji wa sheria na wavunja sheria wenyewe waenee pote, wakiiondoa amani yote na furaha ya maisha kutoka kwa watu wenye kufuata sheria. Wala Mungu si mkatili, hata kusiwe na msaada kwa wale wanaotaka kugeuza njia zao. (1 Tim. 2:3, 4) Yeye anawapa wote nafasi nzuri na ya kutosha. Wale wanaoingia katika “ziwa la moto,” ambayo ndiyo “mauti ya pili,” kwa kweli wanachagua mauti ya milele badala ya uzima, kwa kupenda kwao wenyewe, kwa maana wanazivunja sheria za Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote kwa choyo. Yeye anahitaji kwa haki heshima na ibada ya pekee. Kufutiliwa mbali huku kwa waasi hao washupavu ndiyo njia ya pekee ambavyo ulimwengu wote unaweza kupata amani. Wote wanaotaka uzima na wajifunze njia za Yehova ili majina yao yaandikwe katika “kitabu cha uzima” kwa furaha ya milele.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.