Je! Ukristo Unakufa?
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1-5. Mtu akiyatazama makanisa ya Kristendomu kama yanauwakilisha Ukristo wa kweli, huenda akakata shauri gani? (b) Je! makanisa ya Kristendomu yanawakilisha Ukristo wa kweli, au yamefanya hivyo wakati wo wote?
JE! Ukristo unakufa, au labda umekwisha kufa kabisa, kama wengine wamekata shauri? Tukiyatazama makanisa ya Kristendomu kama yanavyouwakilisha Ukristo wa kweli, huenda ikaelekea kuthibitisha wazo hilo. Samuel Calian, mwalimu wa mambo ya dini katika chuo kikuu cha Dubuque, Iowa, majuzi alisema hivi juu ya makasisi wa makanisa ya Kristendomu:
2 “Ni nani katika jamii yetu anayetoa maneno yenye maana na yenye unabii juu ya matukio ya nyakati zetu? . . . kwa kawaida si makasisi bila shaka. . . . Wamekuwa sauti isiyo wazi katika ulimwengu unaotafuta kusudi na tumaini kwa kusumbuliwa, kuchoka, na kutokujitayarisha vizuri.”
3 Na William L. Edelen, Jr., kasisi katika First Congregational Church Tacoma, Washington, alikubali hivi:
4 “Leo kanisa . . . karibu halitofautiani na shirika la kawaida la kibiashara au chama cha kisiasa.”
5 Lakini hili latokeza ulizo zuri sana: Je! makanisa ya Kristendomu kweli yanawakilisha Ukristo, au yanausingizia tu? Ukitazama historia ya Kristendomu, je! imeendeleza Ukristo wa kweli kati ya washiriki wake wakati wo wote?
6, 7. (a) Sababu gani twaweza kutazamia kuona Ukristo ukiwa hai leo? (b) Kwa hiyo, Yesu alitolea nini mfano?
6 Hivyo, basi, ikiwa makanisa hayawakilishi Ukristo wa kweli, labda imetupasa tuutafute mahali pengine ambapo uko hai. Hakimu ambaye mwenyewe hakuwa Mkristo aliwashauri wakati mmoja watawala wa taifa juu ya mitume wa Kristo na utendaji wao wa kuhubiri: “Shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”—Matendo 5:38, 39.
7 Mwanzishi wa Ukristo alitoa mfano wa unabii ambao katika huo alionyesha kwamba Ukristo wa kweli kutoka kwa Mungu haungetoweka, bali, ungesitawi, katika karne ya kwanza, kama ulivyositawi kweli, na tena katika wakati wa kizazi chetu, ambao Biblia inautaja kama “mwisho wa taratibu ya mambo.”—Mt. 23:3, 34; 13:40, NW.
UKRISTO WASITAWI KATIKA KARNE YA KWANZA
8, 9. Wanafunzi wa karne ya kwanza walitimizaje yale aliyosema Yesu juu ya vikundi vyenye talanta tano na vyenye talanta mbili?
8 Mfano huu ni wa “talanta,” unaopatikana katika Biblia katika Mathayo 25:14-30. Kwa namna ya mfano Yesu alijisema mwenyewe kama mtu ambaye, kabla ya kuanza safari ndefu, aliwakabidhi watumwa wake fedha yake. Juu ya utendaji wao baada ya kuondoka kwake, mfano unaendelea kusema: “Mara yule aliyepokea talanta tano [fedha nyingi] akaenda, akafanya biashara nazo, akachuma faida talanta nyingine tano. Vile vile na yule mwenye mbili, yeye naye akachuma nyingine mbili faida.”—Mist. 16, 17.
9 Hivi ndivyo walivyokuwa wanafunzi wa karne ya kwanza, mitume na washiriki wao, waliokwenda mara hiyo kufanya kazi siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., siku kumi tu baada ya kupaa kwa Kristo mbinguni. Kazi yao haikuwa ya kuchuma fedha, bali kuongeza idadi ya wanafunzi kwa kazi yenye bidii katika shamba lililolimwa alilowaachia Bwana wao, kwa njia hiyo wakiendeleza Ukristo wa kweli. Maelfu waliongezwa kwenye kundi la Kikristo katika wakati mchache sana nao ujumbe wa Kikristo ‘ulizaa matunda na kukua katika ulimwengu wote,’ nao ‘ulihubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’—Matendo 2:41; 4:4; Kol. 1:6, 23.
WATABIRIWA KUFANIKIWA KATIKA WAKATI WETU
10. Yesu alisema nini katika mfano ambayo yangetufanya tuutazamie Ukristo kufanikiwa katika wakati wetu?
10 Ule mfano ulionyeshaje kwamba Ukristo ungesitawi pia katika wakati huu, katika wakati wetu? Vema, ule mfano ulionyesha kwamba baada ya safari ndefu yule mtu angerudi na kukagua na angeona kwamba wawili wa watumwa wake watatu waliongeza “mali” alizowakabidhi mia kwa mia. Maandiko mengine ya Biblia yanaunga mkono maoni haya kwamba sehemu hii ya mfano inahusu kurudi kwa Kristo baada ya muda mrefu, ili ‘afanye hesabu’ na wale waliotiwa mafuta wamtumikie.—1 Pet. 4:17, 18; Kol. 3:24.
11. Ni ushuhuda gani wa nyakati unaotuonyesha kwamba twaweza kuutazamia Ukristo kusitawi katika wakati wetu?
11 Kuna sababu nyingine pia kutazamia Ukristo wa kweli kusitawi na kuongezeka leo. Mojawapo ya sababu hizi ni kwamba huu ndio wakati wa kuwapo kwa Kristo katika mamlaka kama Mfalme bila kuonekana. “Majira ya Mataifa,” au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zimemalizika. “Nyakati” hizi zilianza wakati ufalme wa Mungu unaowakilisha duniani ulipopinduliwa katika mwaka wa 607 B.C.E. na Wababeli. “Nyakati” hizi zilipaswa ziendelee? kwa muda gani? Zilipaswa ziwe “nyakati saba” au miaka saba ya unabii kila mwaka ukiwa na siku 360, ambao katika huo kila siku ilitakiwa ihesabiwe kuwa mwaka mmoja. Hii ingekuwa 7 x 360, au miaka 2,520. Hii inatuleta sisi kwenye mwaka wa 1914 C.E., wakati Ufalme ungerudishwa mikononi mwa “yeye ambaye ni haki yake.”—Luka 21:24; Dan. 4:17; Eze 4:6; 21:27.
12. Ni ushuhuda gani mwingine tulio nao kwamba tumo Katika “mwisho wa taratibu ya mambo”?
12 Tena, hali duniani tangu mwaka wa 1914 zinapatana na yale ambayo Yesu alitabiri kuwa yangekuwa yakitukia wakati wa kutwaa kwake mamlaka katika “mwisho wa taratibu ya mambo.”—Mathayo sura 24; Marko sura 13; Luka sura za 17, 21.
13. Sababu gani ni lazima “watumwa” wa Mungu wa Kikristo wawe wenye bidii leo, na tuna mifano gani?
13 Basi, kurudi huku kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme, katika utukufu wa kimbinguni, ni wakati wa hukumu; kwanza, ya wale waliotiwa mafuta wamwakilishe Kristo, halafu, ya ulimwengu. Kwa sababu hiyo, ni lazima ujumbe wa Ufalme, unaoeleza makusudi ya Mungu kwa wanadamu, utangazwe tena mahali pote kwa kadiri kubwa, “katika ulimwengu wote.” Sikuzote Mungu ametumia watumishi wake watoe onyo kabla ya kuchukua hatua kutekeleza hukumu juu ya watu. Kumbuka onyo la Nuhu kabla ya gharika, onyo la manabii juu ya Yerusalemu kabla haujaharibiwa katika mwaka wa 607 B.C.E. na onyo kuu lililotolewa na Yesu na wanafunzi wake kabla ya kuharibiwa kwa mji huo na majeshi ya Kirumi katika mwaka wa 70 C.E.
UKRISTO NI WENYE NGUVU LEO
14. Kristendomu alikuwa hajionyeshi namna gani kuwa “watumwa” wa Kristo katika mwaka wa 1914?
14 Hivyo, hata ingawa makanisa ya Kristendomu yanakufa, Ukristo wa kweli haufi. Walakini, ni wakati wa hatari kwa yote kwa sababu ndio mwisho wa taratibu hii ya ulimwengu. Kwa hiyo inatazamiwa kwamba Kristo angesimamisha “watumwa” zaidi na kuwakabidhi “mali zake.” Walakini, katika mwaka wa 1914, Kristo alipotwaa mamlaka ya Ufalme, vita ya ulimwengu ilikuwa ikipiganwa duniani. Vita hii ilipiganwa zaidi na majeshi ya mataifa yaitwayo ya Kristendomu.
15. Ilikuwa hali gani ya watumwa wa Kristo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza?
15 Kwa upande mwingine, wale wachache ambao wakati huo walikuwa wakijaribu kuongeza “mali” za Bwana kwa kuzoea Ukristo wa kweli waliteswa sana, kwa sababu ya maenezi ya vita na shauku ya vita. Walifungwa, wakapigwa na kufukuzwa katika miji fulani kwa sababu ya maoni yasiyo sawasawa, yenye chuki isiyo na sababu nzuri ambayo hata makasisi wa Kristendomu waliwaongoza watu wawe nayo juu ya kazi iliyotakiwa ifanywe na “watumwa” wa Yesu Kristo. Ilionekana kana kwamba kazi yao ilivunjwa.
16. Katika mwaka wa 1919, “watumwa” wa Kristo duniani walianzaje kuitimiza sehemu ya pili ya mfano wa Yesu, juu jamii yenye talanta tano na yenye talanta mbili?
16 Ingawaje, baada ya vita, mnamo mwaka wa 1919, kulikuwako bado kikundi cha uaminifu kilichoona uhitaji wa kukutangaza kuwapo kwa Bwana Yesu Kristo kwa kusudi la ukaguzi na hukumu. Hawa Bwana aliwasimamisha akawatia bidii na nguvu, wasizuiwe tena kamwe na adui zao! Mnamo mwaka wa 1922 walikuwa wamefanya matayarisho watangaze kwamba Mfalme Yesu Kristo alikuwa ametwaa mamlaka yake katika mbingu na karibuni angewakomboa wanadamu na waonezi wote. Ilipaswa iwe kazi ya ulimwenguni pote! Kwa sababu ya kuitangaza kwao kweli kwa bidii walikuwako watu 90,434 waliohudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa mauti ya Yesu Kristo katika mwaka wa 1925. Hii ilionyesha kwamba “watumwa” hao walikuwa wamefanya kweli kama ule mfano ulivyoeleza, yaani, walikuwa wamepata “talanta” zaidi faida au walikuwa wameongeza “mali” za Bwana.
17. Ni ushuhuda gani tulio nao kwamba Ukristo u hai kweli kweli leo?
17 Leo, punde ya miaka 50 baadaye, karibu kuumba kote kumepata kuhubiriwa ujumbe wa Ufalme “kuwa ushuhuda.” (Mt. 24:14) Katika nchi 208 za dunia, sasa zaidi ya milioni moja na nusu wamesikia na wameuamini ujumbe wa “watumwa” wa Kristo nao wameingia katika kazi ile ile, wakiwasaidia wengine wasikie. Kwa kuwa kuna watu 144,000 tu watakaokuwa sehemu ya mwili mzima wa “watumwa” waaminifu, ili mwishowe watawale pamoja na Kristo katika mbingu, wengi zaidi kati ya wale wanaoupokea ujumbe sasa wanalo tumaini la kuokoka uharibifu wa taratibu hii ya mambo na la kuishi duniani chini ya serikali ya Ufalme.—Ufu. 14:1, 4.
18, 19. Katika utimizo wa mfano, je! jamii yenye talanta mbili ilijitahidi kidogo kuliko jamii yenye talanta tano, na nani aliyekuwa na daraka la faida katika “talanta”?
18 Katika ule mfano tunaona kwamba kila kikundi cha watumwa waaminifu, kikundi chenye talanta tano na kikundi chenye talanta mbili, kilifanya bidii kwa kulingana, na vikundi vyote viwili vilipata ongezeko la mia kwa mia. Hivyo kila mmoja alifanya kwa kadiri alivyoweza, na hakuna aliyekuwa bora kumpita mwingine ye yote. Ndiyo, wasingeweza kujivunia maongezeko yaliyopatikana, kwa maana ni Yehova, kupitia kwa Kristo, ndiye mwenye kutenda yote, kama mtume Paulo alivyosema: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (1 Kor. 3:6, 7) “Watumwa” wa Kristo ni vyombo tu ambavyo Mungu anapendezwa kuvitumia katika kupata ongezeko. “Watumwa” hawa waaminifu wanathawabishwaje wakati wa ukaguzi na hukumu ya Bwana?
19 Katika utimizo, fahamu kwamba wale watumwa hawamfananishi mtu mmoja mmoja, bali wanafananisha jamii ya watu. Kwa hiyo, kwa kisasa hatuwezi kuelekeza kwenye watu mmoja mmoja kama wakiwa ile jamii yenye talanta tano au yenye talanta mbili. Zote zinafanya kazi kwa bidii kwa kulingana zikitimiza madaraka ziliyogawiwa bila kujali kama ni makubwa zaidi au madogo.
THAWABU YA BWANA KWA “WATUMWA” WAAMINIFU
20, 21. Mtume Paulo anasimuliaje thawabu wanayopewa “watumwa” wa Kristo wakati wa kuwapo Kwake?
20 Mtume Paulo anasema juu ya thawabu yao katika 1 Wathesalonike 4:14-17:
21 “Ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la [Yehova], kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.”
22. Mtume alionyeshaje imani ya kweli katika tumaini hili katika habari yake mwenyewe?
22 Kwamba thawabu hii ni tumaini la kweli, lililo hai mtume Paulo alionyesha wakati, upesi kabla ya kufa kwake, alipomwandikia mfanya kazi mwenzi wake Timotheo hivi: “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.”—2 Tim. 4:7, 8.
23. (a) Ni thawabu gani ambayo Bwana anawapa “watumwa” wake waliokufa kabla ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme? (b) “Watumwa” hao wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo wanathawabishwaje?
23 Wakati wa kuwapo kwa Bwana, anapokuja kukagua na kuhukumu, kwanza anawaangalia wale “watumwa” wake waliokufa tangu wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 C.E. mpaka wakati wa kufika kwake. Hawa anawafufua kwenye uzima wa kimbinguni. Wanajiunga naye kama “Bibi-arusi” wake. (Ufu. 19:7; 21:9) Ndiyo, huu ukiwa ufufuo wa kimbinguni kwenye uzima wa kiroho, hauonwi na wale waishio duniani. Wale “watumwa” wabakio duniani wakati wa kuwapo kwake, wanapokufa, ‘watanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili wamlaki Bwana hewani.’ Yaani, wakati wa kuwapo kwa Kristo bila kuonekana, kunakoonyeshwa na mawingu, wataungana na wale waliokwisha kufufuka. Tangu wakati huo na kuendelea watakuwa pamoja na Bwana sikuzote.
24. Ufunuo 14:13 unasimuliaje thawabu wanayopewa “watumwa” wale wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo?
24 Wakati wa kufa kwao, waaminifu hawa wanafufuliwa mara hiyo. Huko wanapata “kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao.” (Ufu. 14:13) Wametaabika sana na “mali” za Bwana, “talanta” walizokabidhiwa. Baada ya kufufuka kwao wanaondolewa taabu zao duniani, hata hivyo wanaendelea kufanya kazi katika cheo chao cha thawabu ya kimbinguni. Kubadilika kwao kwa mara hiyo wakati wa kufa kunasimuliwa katika 1 Wakorintho 15:50-54.
25. Ni katika thawabu au “furaha” gani wanamoingia wale “watumwa” waaminifu wabakio duniani kwa muda wakati wa kuwapo kwa Kristo?
25 Lakini namna gani “watumwa” waaminifu wakati wangali wabaki duniani kwa muda wakati wa kuwapo kwa Mfalme? Wanajifurahisha thawabu sasa kwa kuingia katika “furaha” ya Bwana wao. (Mt. 25:19-23) Ni nani aliye chanzo cha “furaha” hii? Ni Yehova Mungu, Baba ya Yesu Kristo. Yesu alivumilia mateso yake kwa sababu ya “furaha iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2) Alipoanza safari yake ndefu alikwenda kwa Baba yake, Chanzo cha “furaha” hiyo, naye alipokea kutoka kwa Baba madaraka makubwa zaidi, kutia na mamlaka ya kifalme. “Watumwa” waaminifu wanaona furaha kubwa katika kuutangaza Ufalme uliosimamishwa. Pia, kama “watu kwa ajili ya jina lake,” wanaitwa kwa jina la Yehova Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Ulimwenguni pote wanajulikana kwa jina ‘mashahidi wa Yehova.’ (Isa. 43:10-12) Na, kwa kuwa ni “watumwa” wa Kristo, wao ni mashahidi wa Yehova wa Kikristo.
UNAWEZA KUJIZOEZA UKRISTO WA KWELI
26. Ni nani zaidi ya jamii za “mtumwa” wa mfano wanaokusanywa sasa?
26 Ni kusudi la Yehova, wakati huu wa kukagua, kuwakusanyia “watumwa” waaminifu wabakio wa Kristo “mkutano mkubwa” wa watu wengine. Kwa kuwa upeo wa mwisho wa taratibu hii ya mambo u karibu sana, watu hawa watakuwa waokokaji wa uharibifu wa ulimwengu huu wawe msingi wa ‘nchi mpya, ambamo haki itakaa.’—Ufu. 7:9-17; 2 Pet. 3:13.
27. “Mkutano mkubwa” huu unasaidiaje kuthibitisha kwamba Ukristo haufi?
27 Washiriki hawa wa “mkutano mkubwa” wanashirikiana na mashahidi wa Yehova kwa haraka sana hata mamia ya mahali papya, paitwapo “Majumba ya Ufalme,” panajengwa kila mwaka. Ijapokuwa makanisa ya Kristendomu yananung’unikia upungufu wa washiriki wa kanisa na kukosa msaada, majumba ya mashahidi wa Yehova yanajaa watu. Makumi ya maelfu wanabatizwa kila mwaka. Na wapya hawa si washiriki wa kivivu, bali ni watangazaji wenye bidii wa ujumbe ule ule wa Ufalme ambao jamii ya “mtumwa” inatoa.
28. Ni nini linalopaswa lifanywe sasa na mtu anayetafuta kuuona Ukristo ukiwa hai?
28 Hivyo, Ukristo, Ukristo wa kweli, haufi, bali u hai, unasitawi, unaongezeka katika idadi na utendaji. Ikiwa wautaka unaweza kuuona sasa na kuuzoea. Lifikie shauri hili kwa akili zilizo wazi, ujionee mwenyewe anayofanya Mungu kutegemeza na kuukuza kwa nguvu Ukristo leo. Majumba ya Ufalme ya jamii hii yenye furaha yako wazi kwako na unaweza kuhudhuria bila malipo, bila kuona haya kwa kuombwa uchange fedha au kwa kupitishwa kwa sahani ya sadaka. Chunguza mambo ambayo watu hawa wanaamini na wanayofanya, ndipo ufanye unayoona ni kweli pamoja na wale unaowaona wakifanya. Hii ndiyo njia peke yake ya furaha sasa na uzima katika taratibu mpya ya mambo yenye haki iliyo karibu.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.