Je! Kuna Jamii Yenye Umoja ya Wakristo wa Kweli?
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1-3. Ni sifa gani ambazo lazima ziwemo katika Mkristo wa kweli?
KILA mtu, anapotafuta Mkristo wa kweli, anatazamia kuona mtu mwenye sifa bora za adili na utu mwema. Naye afanya vema. Lakini mengi zaidi yatakiwa kwa Mkristo kuliko hili.
2 Hata kati ya wale wasiojidai kuwa Wakristo, utawaona watu wenye sifa njema za adili, wakionyesha nyutu zenye kupendeka pia. Basi je, tofauti ni nini?
3 Zaidi ya mambo hayo, lazima Mkristo awe na tamaa yenye nguvu kutaka kuiendeleza ibada ya kweli ya Mungu wa Biblia, kama alivyofanya Yesu Kristo. Lazima awe mwenye bidii katika jambo hili.
4. Kwa sababu gani yaweza kutatiza kujua ni akina nani walio Wakristo wa kweli, hasa kwa kumtazama Kristendomu?
4 Hata ikiwa unalifahamu jambo hili, huenda ukaona inatatiza kujaribu kuwatambua walio Wakristo wa kweli hasa siku hizi. Kwa kweli, huenda ukakosa kujua kama kunao. Kwa maana waona watu wa kidini wa Kristendomu hawana umoja sana wa kuwaza na kutenda. Hivi ndivyo ilivyo kwa habari ya magumu ya adili na ya kijamii, na hasa ndivyo ilivyo kwa habari ya ibada ya Mungu. Hawajitahidi sana kueleza Mungu alivyo na makusudi yake na nafasi ya kupata uzima wa milele, ama mbinguni ama duniani, kwa kumpendeza Yeye katika ibada ya kweli.
WAZO NA JITIHADA YENYE UMOJA VYA LAZIMA
5, 6. Je! tutazamie kuona jamii yenye umoja ya Wakristo wa kweli duniani?
5 Je! imepaswa iweko, na je! iko, JAMII ya watu wanaojitoa kwa ibada ya Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia na wanaofanya hivyo kwa umoja na jitihada ili kuwezesha wengine wafanye hivyo?
6 Basi, imepaswa iweko, kulingana na onyo la upole la mtume Paulo kwa Wakristo katika karne ya kwanza. Aliandika mengi juu ya adili bora na nyutu za Kikristo, lakini alisema hivi pia: “Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo, ili, nikija na kuwaona ninyi, au nisipokuwapo, niyasikie mambo yenu, kama mnasimama imara katika [nafsi moja, kana kwamba wote pamoja walikuwa mtu mmoja] kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili.”—Flp. 1:27.
MFANO WA WAJIBU WA MKRISTO
7. Je! Wakristo wa kwanza walikuwa jamii yenye umoja, na ni mfano gani alioutoa Yesu kuonyesha wanafunzi wake wanavyopaswa kuwa?
7 Ni watu wachache watakaokana kwamba Yesu na mitume wake hawakuwa wenye bidii sana katika kuipanua ibada ya kweli kwenye miisho ya dunia. Walikuwa na umoja katika kusudi hili, umoja wa kufundisha na kutenda. Ili kuonyesha wanavyopaswa wanafunzi wake kuwa, Yesu alitoa mfano wa talanta. (“Talanta” ya fedha inafananisha thamani ya fedha ya mamia ya shilingi.) Mfano huu waonyesha wazi na kwa nguvu wajibu wao kuuongeza Ukristo wa kweli kwa kadiri kubwa iwezekanavyo.
8. Zilinganishe sababu kubwa zilizomfanya Yesu atoe mifano ya talanta na mina.
8 Wanafunzi wa Yesu walikuwa wamemwuliza ulizo hili: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” Katika jibu mfano wa talanta ulitiwa ndani. Kwa hiyo, mfano huu ulitolewa kuwahakikishia Wakristo wanaoishi katika “mwisho wa taratibu ya mambo” kwamba Bwana Yesu Kristo alikuwapo katika mamlaka ya Ufalme bila kuonekana. Lakini ulikuwa na utimizo huko nyuma wakati Yesu alipokuwa duniani. Twaweza kuelewa mengi juu ya maana ya mfano huo kutokana na mfano unaolingana wa mina au “pauni,” uliowaonyesha wasikilizaji wa Kristo wa karne ya kwanza kwamba ufalme wa Mungu haukupaswa ‘uonekane mara,’ kama walivyokuwa wamedhani.—Mt. 24:3; Luka 19:11-27, NW.
9, 10. Mfano wa talanta unaanza kwa kusema nini?
9 Mifano yote miwili ilihusu ufalme wa mbingu. Mfano wa talanta ulianza kwa kusema hivi:
10 “Maana [yaani, hali zinazohusiana na ufalme wa mbingu] ni mfano wa mtu atakaye kusafiri, aliwaita watumwa wake, akaweka kwao mali zake. Akampa mmoja talanta tano, na mmoja talanta mbili, na mmoja talanta moja; kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake; akasafiri.”—Mt. 25:14, 15.
11. Safari ndefu ya “mtu” iliyompasa aifunge katika mfano ilikuwa nini?
11 “Mtu” huyo ni Yesu Kristo. Alikuwa karibu ‘kusafiri,’ amrudie Baba yake mbinguni. Yesu alipaswa afanye hivi baada ya kufa kwake na kufufuliwa. Huko alipaswa aketi “mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Ebr. 10:12, 13) Ungepita muda mrefu kabla hajapata kwa Baba yake amri ya kuchukua mamlaka kamili ya ufalme, lakini wakati huo ingempasa kwanza awakague na kuwathawabisha “watumwa” wake. Angewatazamia wawe na umoja, wakifanya ‘biashara’ yake, wala si kugombana kati yao. Ukaguzi ulipomalizwa angewatupa adui zake watoke duniani, kama ionyeshwavyo katika Luka 19:15-27.—Zab. 110:1-3.
“WATUMWA” WAKABIDHIWA “MALI”
12. Onyesha kwamba “mali” za Yesu Kristo hazikuwa vitu vyenye kuonekana.
12 Sasa, “mtu” huyu alikuwa na “mali” za kuwakabidhi “watumwa” wake mpaka atakaporudi akiwa na mamlaka ya kifalme. Yesu Kristo alikuwa na mali gani za thamani kuu? Yeye hakuwa na fedha, mali nyingi za mashamba wala majengo. Wala yeye hakutambuliwa kama mwenye mamlaka na serikali za kisiasa. Aliuawa na Milki ya Kirumi Wayahudi waliposisitiza. Basi je!, yeye alikuwa na nini cha kuwakabidhi “watumwa” wake?
13-15. (a) “Mali” ambazo Kristo aliwaachia wanafunzi wake zilikuwa nini? (b) Mitume ‘wangevunaje wasiyoyataabikia’?
13 Lilikuwa fungu la vitu vyenye thamani vilivyo tofauti na namna ya mali zilizotajwa sasa hivi. Wakati wa huduma yake akiwa na mwili wenye nyama Kristo alikuwa amekuwa akiutafuta kwanza ufalme wa Baba yake wa kimbinguni. Kwa kuhubiri na kufundisha kwake alikuwa amelima shamba, alikuwa amekuza uwezo usioonekana katika shamba hili wa kutokeza wanafunzi. Hii ndiyo mali aliyowaachia wanafunzi wake. Alikuwa amekwisha waambia hivi wanafunzi wake zaidi ya miaka miwili kabla ya kufa kwake na kufufuliwa:
14 “Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao.”—Yohana 4:35-38.
15 Yesu alipanda mbegu kwa Wayahudi na waongofu wa Kiyahudi na Wasamaria waliohusiana nao peke yao. Yohana Mbatizaji pia alikuwa amepanda. Baada ya kufufuliwa kwa Yesu na kumiminwa kwa roho takatifu juu ya wanafunzi wake siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., wanafunzi hawa wangevuna sana kwanza katika shamba hili ‘lililopandwa.’ ‘Walitumwa’ wakafanye hivyo, walikuwa na wajibu wa kufanya hivyo. ‘Waliovunwa’ kwanza walikuwa wamesitawishwa na mafundisho safi ya Yesu. Kwa hiyo walipojiunga na wanafunzi waliozaliwa kwa roho walikuwa kama mtu mmoja katika kuendeleza mafundisho safi.
16. Katika utimizo ni nini kilichofananishwa na watumwa mbalimbali watatu?
16 Ni wazi kwamba Yesu alikuwa na zaidi ya “watumwa” watatu. Kwa hiyo “watumwa” wale watatu mbalimbali walioonyeshwa katika mfano wangefananisha wote wanaotazamiwa kuwa warithi pamoja na Kristo ambao kwa ajili yao amefanya agano la ufalme wa kimbinguni. Wangekuwako watu wa namna zote za maisha, wazee kwa vijana, wanaume kwa wanawake. (Linganisha Matendo 1:14; 8:12.) Lakini tofauti hizi za hali na umri hazikupaswa ziwe kizuizi cha umoja—wote wangefanya kazi ile ile moja.
17, 18. (a) Katika utimizo wa karne ya kwanza, ni nani waliokuwa jamii ya “talanta tano” nayo jamii hii iliisaidiaje jamii ya “talanta mbili”? (b) Ni kwa njia gani kazi waliyogawiwa “watumwa” ilitaka umoja kati yao?
17 Katika utimizo wa mfano Bwana alihakikisha kwamba hakuna aliyepata zaidi ya ambavyo angeweza kushughulika navyo, “kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake.” Kwa wazi jamii ya “talanta tano” ya karne hiyo ya kwanza iliwatia ndani mitume, ambao walipewa daraka lililo kuu zaidi. (Ufu. 21:14; Efe. 2:20-22) Waliwasaidia sana jamii ya “talanta mbili” kuangalia madaraka yao.
18 “Watumwa” wote, kama vile wale waliomo katika mfano wa mina, walipaswa ‘kufanya biashara mpaka atakapokuja.’ (Luka 19:11-13, NW) Ingekuwa biashara ya Yesu, biashara ya Mfalme, na kwa hiyo watumwa watiifu wangepaswa wawe na umoja na kuwaza na kutenda. Kristo hakugawanyika mwenyewe. (1 Kor. 1:10) Bila shaka “watumwa” wake wasingeiendeleza biashara yake kwa kupingana, kama vile katika Kristendomu, ambamo madhehebu moja inafundisha jambo moja na madhehebu nyingine inafundisha jingine.
19. Katika utimizo, ni nini kilichofananishwa na “uwezo” aliokuwa nao kila mtumwa?
19 Katika mfano wenyewe “uwezo” wa watumwa, msingi ambao kwao talanta ziligawanywa, ungekuwa uwezo wa kimwili au wa akili. Walakini, katika utimizo, ni uwezo wa kimwili au wa akili uliofananishwa? Bila shaka huo ungekuwa wenye thamani ukitumiwa kwa njia inayofaa. Lakini “uwezo” hapa unayafananisha madaraka ya kiroho yanayoonekana katika “mtumwa” wa Kikristo anayeutazamia ufalme wa kimbinguni. Bidii, nia, shauku aliyo nayo, vyote vyauonyesha uwezekano huu. Hii ni kupatana na kanuni ya kwamba “Mungu amevitia viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka.”—1 Kor. 12:18.
20. Lazima “watumwa” waitikieje kukabidhiwa kwao “talanta” na Kristo?
20 Bwana, Yesu Kristo, amewakabidhi “watumwa” hawa kitu fulani, bila ya kujali kama ni wa jamii ya “talanta tano” au jamii nyingine zilizotajwa katika mfano. Kwa upande wao, lazima wao pia wawe na kitu fulani au watoe kitu fulani. Wanachoweza kutoa kinakisaidia kitu chenye thamani walichokabidhiwa, nacho chaweza kulisitawisha shamba la kiroho, lililoachwa na Bwana Yesu Kristo. Kingewawezesha wao, kama jamii au kikundi chenye umoja, wavune wanafunzi wapya.
MWANZO WA UTIMIZO WA MFANO
21, 22. Yesu alitayarishaje, si “shamba” tu, bali pia na wa kwanza wa “watumwa” wake wazipokee mali zake?
21 Ni wakati gani Yesu alipoanza kuwakabidhi wanafunzi wake “mali” hizi? Je! aliwakabidhi kila mtu ajitegemee au kama kikundi chenye umoja? Habari zilizomo katika Matendo 1:1-5 zinaendeleza habari zilizoachwa na Injili ya Luka, yaani, “hata siku ile [Yesu aliyefufuliwa] alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa [roho takatifu] wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana [na jamii ya wanafunzi waaminifu] aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika [roho takatifu] baada ya siku hizi chache.”
22 Kwa hiyo si kwamba tu Yesu alikuwa ametayarisha “shamba,” akilipevusha na uwezo wa kuwa na wanafunzi wengi zaidi, bali pia alikuwa amewatayarisha wa kwanza wa jamii yake ya “watumwa” wazipokee “mali” zake.
23, 24. Mfano ulianza kutimia wakati gani? Onyesha kwa mitajo ya Maandiko.
23 Bila shaka utimizo wa mfano huu ulianza kati ya ufufuo wa Yesu kutoka kwa wafu na kupaa kwake akaonekane mbele za Baba yake wa kimbinguni. Kwa maana ni wakati gani Yesu alipowaita “watumwa” wake mara ya kwanza wakusanyike awakabidhi “mali” zake? Mtume Mathayo anatoa habari za maneno ya Yesu penye mkutano katika Galilaya baada ya kufufuliwa kwake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mt. 28:16, 19, 20, NW.
24 Lakini siku ya kupaa kwake mbinguni Yesu alionyesha wazi zaidi muda ambao kazi ya kuongeza “mali” zake ingechukua. Twasoma: “Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, [ikiisha kuwajilia juu yenu roho takatifu]; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”—Matendo 1:6-8.
ITAFUTE JAMII YENYE UMOJA INAYOFUNDISHA KWELI YA BIBLIA
25. Twajuaje kwamba walikuwako zaidi ya “watumwa” watatu walipoanza ‘kufanya biashara’ na “talanta”?
25 Baada ya ufufuo wake Yesu alijionyesha mara kwa mara kwa watu mbalimbali kati ya wanafunzi wake, wakati mmoja kwa zaidi ya watu 500. Na siku ya Pentekoste walikuwako 120 waliobatizwa kwa roho takatifu. (1 Kor. 15:6; Matendo 1:15; 2:1-4) Kwa hiyo walikuwako “watumwa” zaidi ya watatu walioanza mara hiyo ‘kufanya biashara’ na talanta, watu 3,000 wakiusikia ushuhuda juu ya makusudi ya Yehova Mungu kupitia kwa Kristo siku hiyo. Lakini wao hawakufuata kila mtu njia yake wala kugawanyika katika madhehebu mbalimbali. Wote waliungana kuiendeleza ibada ya kweli kwa nguvu na umoja.—Matendo 2:41-47.
26. Imempasa mtu akumbuke nini anapotafuta Wakristo wa kweli duniani leo?
26 Kwa hiyo, ikiwa unatatizwa kutafuta Wakristo wa kweli siku zetu, ni jambo la maana ukumbuke kutafuta JAMII yao, wote wakifundisha mambo yale yale mamoja juu ya makusudi ya Mungu. Lazima wawe wanaishi maisha safi, za adili, za unyofu. Zaidi ya hayo, lazima wawe wakisema na wengine kwa bidii juu ya Biblia, wakiiendeleza ibada ya kweli, wakiwasaidia wapya wawe wanafunzi wa Kristo. Kwa njia hiyo wanaziongeza “mali” za Mfalme. Je! wewe unaona watu wa namna hiyo katika mtaa wako?
27. Ni mambo gani zaidi juu ya mfano wa talanta yatakayoangaliwa?
27 Je! utimizo wa mfano unakamilikaje nyakati zetu? Kulipaswa kuweko ukaguzi na kuthawabishwa kwa watumwa na kabaila. Utimizo wa hili utazungumzwa katika toleo lifuatalo la Mnara wa Mlinzi.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.