‘Uendelee Kuzishika Amri Zake’
“Na kwa hili twajua kwamba tumepata kumjua yeye, yaani, tukiendelea kuzishika amri zake.”—1 Yohana 2:3, NW.
1. Kwa sababu gani kujichunguza ni kwa lazima katika kuizoea kweli?
DUNIANI POTE leo kuna mamia ya maelfu ya mashahidi wa Yehova Mungu walio wakf na waliobatizwa ambao wanakutana pamoja na kushiriki katika kuzitangaza habari njema za Ufalme nyumba kwa nyumba na kwa njia nyingine nyingi. Watumishi hawa wa Mungu wanampenda yeye nao wanataka kufanya mapenzi yake. Hiyo ndiyo sababu wameweka maisha zao wakf watimize amri zake, wakizishika sheria zake. Walakini, nyakati nyingine huenda wakawako wengine washindwao kufahamu kabisa maana ya ‘kuendelea kuzishika amri zake [Mungu].’ Mtu asipoendelea kujichunguza mwenyewe juu ya njia yake ya maisha na nia zake, huenda akakuta kwamba mamlaka za giza katika taratibu hii zampofusha asiyaone matakwa ya Yehova. Yatupasa tuendelee kuzitimiza amri za Mungu. Mtu akiendelea kufanya jambo lile lile, baadaye yanakuwa mazoea yake, jambo analofanya kwa kawaida. Halifanyi sasa, na kulisahau baadaye. Twaweza kusema kwamba azoea “jambo fulani” kwa desturi, hata liwe nini. Kwa hiyo linakuwa njia ya maisha kwake, jambo afanyalo bila kufikiria kuliacha wakati ujao.
2. Mtu anapataje kweli kumjua Yehova?
2 Ndivyo ilivyo na wale wazishikao amri za Mungu. Wanaendelea na mwendo huu kila siku, kila mwezi, kila mwaka, wakijua kwamba hili ni takwa la Mungu. Maana ya haya yote ni kwamba njia ya pekee ya ‘kupata kumjua yeye’ kweli kweli, yaani, Yehova, ni kwa kushika sikuzote atakayo tufanye. Hii hairuhusu kumtumikia tujisikiapo tu tukitaka kufanya hivyo, kusipokatiza jambo jingine lo lote tunalofikiri ni la maana zaidi. Ukawaida huu ndio unaotiwa katika semi ‘kuizoea kweli’ na ‘kuendelea kuzishika amri zake.’
KATIKA “MAKUSANYIKO”
3. Yehova aagiza watu wake wafanye nini kwa habari ya kukutana pamoja?
3 Mtunga zaburi aliandika hivi: “Katika makusanyiko nitamhimidi [Yehova].” (Zab. 26:12) Yehova, Mungu wa nuru, ameamuru kwamba watu wake wakutane pamoja katika jina lake. Maandiko ya Kiebrania yana amri za Yehova zilizowekwa juu ya watu wake wa kale Israeli wakutane pamoja kuadhimisha matukio ya pekee wakati wa mwaka. Mara nyingi ilikuwa lazima watu wakutane hivyo. Zaidi ya hayo, ilikuwa kwa baraka na faida yao. Wajibu wa kuwa na mikutano ya ibada ulipitishwa kwa kundi la Kikristo la watu wa Mungu. Kwa msingi, Waebrania 10:24, 25 yahitaji Wakristo wakutane pamoja wala wasisahau kufanya hivyo. Ni kwa kusudi la kutiana moyo na kujenga imani yao, kuchochea kwenye upendo na kazi zifaazo.
4. (a) Ili kuizoea kweli, lazima mtu afanye nini? (b) Mtu awezaje kubisha juu ya mikutano ya kundi, lakini ni vema kukumbuka nini?
4 Kundi la Kikristo leo, katika karne yetu ya 20, lazima liwe ‘linashika amri zake’ juu ya kukutana kwa ajili ya ibada. Kila mtu mmoja mmoja katika kikundi lazima aishike amri hii ikiwa ‘kusanyiko’ litakuwako. Ili kuzoea kweli kama kikundi, lazima kila mmoja azisikilize amri za Yehova. Huenda ikabishwa kwamba katika Maandiko hamna amri ya wazi kwamba lazima tukutane pamoja saa tano kila juma, kama ilivyo desturi kati ya watu wa Yehova duniani. Hiyo ni kweli. Lakini je! haitupasi tushukuru kwamba Mungu wetu ni mkarimu, akitupa mambo mema ya kiroho kwa wingi? Twafaidiwa kiroho na kila mkutano tuhudhuriao. Imani yetu yatiwa nguvu. Tukutanapo na Wakristo wenzetu twasaidiwa kuzishika amri za Yehova, kuizoea kweli. Je! hilo silo tunalotaka kufanya?
5. Basi, ni kwa njia gani yampasa mtumishi wa Yehova aliye wakf aione mikutano ya kundi?
5 Basi, inafaa kuwaza kwamba mtumishi aliye wakf wa Yehova angefanya kila jitihada awe pamoja na ndugu na dada zake wa Kikristo’ mikutanoni. Badala ya kutafuta udhuru wa kutokuwapo, angetafuta sababu za kuwa katika kila mkutano uwezekanao wa kundi. Kwa kawaida, angetumia uamuzi mzuri kama angekuwa mgonjwa au kama hali nzito isiyotazamiwa ingetokea. Lakini, kwa ujumla, dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia itamchochea azoee kweli kwa kufuata amri ya Yehova kupitia kwa Neno lake kutoacha kukusanyika pamoja.
6. “Sababu” za kukosa mkutano zawezaje kuwa “udhuru” wa kufanya mazoea ya kuikosa?
6 Mtumishi wa Bwana asipokuwa mwangalifu, aweza kwa kawaida kuacha mambo madogo sana yamzuie asiwepo katika ushirika huu uliobarikiwa. Nyakati nyingine kutembelewa na jamaa kwaweza kuzuia mtu asihudhurie mkutano fulani, ikitegemea hali. Lakini je! mtu angeacha kila atembelewapo na jamaa na kila wakati wa namna hii umzuie asiwe pamoja na wale wanaotembea katika kweli kati ya makusanyiko? Sababu gani usikaribishe jamaa waende pamoja nawe? Vivyo hivyo, huenda mkutano wa pindi fulani ukakoswa kwa sababu ya hali mbaya ya hewa, kazi ya mtu, au magonjwa madogo madogo. Walakini, wakati “sababu” hizi zinapokuwa “udhuru” wa kuacha kuwa katika ushirika na watu wa Bwana kwa kawaida ndipo mtu anapoanza kutembea gizani, badala ya nuruni, awe kama mtu anayesema uongo badala ya mtu anayezoea kweli. Je! twadhani hata kidogo kwamba wakati wa kutoka Misri Waisraeli waaminifu waliacha jambo lo lote liwazuie wasinyunyizie sehemu fulani ya damu vizingiti vyao vya milango, wasile mwana-kondoo wao wa Kupitwa na wasiwe tayari kuondoka wakipewa taarifa ya mara hiyo? Walijua kwamba kuzishika amri za Yehova wakati huu kulimaanisha maisha zao wenyewe. Je! nyakati ni tofauti na wakati huo sasa? Je! hatuishi katika siku za hatari, zilizo ngumu kupambana nazo? Basi, imetupasa tuonyeshe nia yetu ya kutaka zaidi sana kwa kushirikiana na makusanyiko kwa kawaida kama ilivyoamriwa na Yehova.
KUIZOEA KWELI WAZIWAZI
7. Ni sifa gani iliyo nzuri sana ya Ukristo wa kwanza inayofuata kuzungumzwa katika somo letu?
7 Mojawapo ya sifa nzuri sana za wakristo wa karne ya kwanza ilikuwa kutangaza kwao waziwazi habari njema. Twasoma juu ya Yesu akienda katika Galilaya yote, akifundisha masinagogini na kuzihubiri habari njema za Ufalme. (Mt. 4:23) Alihubiri na kufundisha milimani, kati ya watu kando kando ya pwani, katika nyumba za wenye kupendezwa, po pote na kila mahali walipokuwapo watu wa kusema nao. Aliwaambia hivi wale kumi na wawili aliokuwa akiwazoeza kwa njia ya pekee: “Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Hao kumi na wawili walipopata maagizo yao, aliwatuma mijini wakafundishe na kuhubiri.—Mt. 10:5-10.
8. Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wako tofauti na idadi kubwa ya wale waliomo katika Kristendomu kwa njia gani?
8 Kwa hiyo, ni jambo la busara kwamba wakristo wa karne ya 20 wangekuwa wakifanya lili hili. Ni wazi kwamba idadi kubwa ya wale waliomo katika Kristendomu wamekuwa wasikiaji tu badala ya kuwa “watendaji wa neno,” wasifanye lo lote wenyewe kuizoea kweli kwa kulieneza Neno la kweli. Lakini kati ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova twaona “watendaji wa neno.” Wanajua kwamba ili wawe kama Yesu lazima washiriki kuwaeleza wengine habari njema za Ufalme. Ni agizo lao kama vile lilivyokuwa agizo la Yesu na wale waliokuwa wa kundi la kwanza la Kikristo. Maandishi ya Biblia yatuambia: “Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa kuenenda mwenyewe vile vile kama yeye alivyoenenda.”—Yak. 1:22; 1 Yohana 2:6.
9. Eleza kwa ufupi mengine ya magumu yaliyomo katika kuizoea kweli kwa kushiriki katika kuhubiri kwa waziwazi?
9 Kuizoea kweli hii kwa kushiriki katika kuuhubiri Ufalme si jambo jepesi sana kwa Mkristo sikuzote. Mara nyingi yampasa achukuliane na matusi kutoka kwa wapinzani. Twaweza kusema, kuna watu wachache sana waliozaliwa kwa ajili ya utendaji wa waziwazi wa kuhubiri, yaani, wenye karama (kipawa) ya kuweza kusema na watu kwa vyepesi. Kwa hiyo, lazima Mkristo mwaminifu ajitahidi kuwa hodari na mwenye uwezo. Pia lazima ajinyenyekeze atimize kazi ya waziwazi ya kuhubiri, akijua kwamba upendo wake kwa Mungu na kwa jirani yake ndio unaomchochea azishiriki habari njema na wengine. Kwa hiyo, ziko nyakati ambazo Mkristo aweza kuona ni vigumu kushiriki katika kazi hiyo, naye huenda akatoa udhuru wa kutofanya hivyo.
10. (a) Taja mengine ya mambo yawezayo kuzuia mtu asishiriki katika kazi ya kuhubiri nyakati fulani, nazo “sababu” zaweza kuwa “udhuru” wakati gani? (b) Ni vema kukumbuka nini juu ya maarifa ya Shetani, nasi twaweza kugeukia wapi kwa msaada?
10 Pindi kwa pindi huenda ikawako sababu nzuri sana ya kutoweza kushiriki katika kazi ya kuhubiri wakati fulani. Ziko nyakati ambapo nyumba anamoishi mtu inahitaji sana kufanyiwa matengenezo fulani. Gari ambalo mtu ategemea kwa kusafiri laweza kuwa lahitaji kuangaliwa kwa haraka. Huenda likawako jambo la namna ya kipekee ambalo lazima mtu alifanye ambalo lingemzuia asishiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Lakini tena ulizo ni, Ni wakati gani sababu inapokuwa udhuru? Je! mtu anaruhusu vipingamizi hivyo vimwachishe kuizoea kweli? Kila mtu ayajua yaliyomo moyoni mwake mwenyewe, na, bila shaka, Yehova ayajua. Lakini katika ulizo la uzima na mauti linalowakabili wanadamu wote sasa kwa hakika sisi kama Wakristo waaminifu twataka tuwe waangalifu tusijiache tuanze kutembea gizani. Shetani, mungu wa giza, afanya kazi juu ya udhaifu wetu mbalimbali, si juu ya nguvu zetu. Ikiwa aweza kutufanya tujisikitikie, tuwaze isivyofaa, basi atafanya hivyo hata zaidi kila mara ulizo litokeapo. Ili tupambane na kushinda nia zake kwa kufaulu, lazima tumtegemee Yehova Mungu. Twahitaji msaada wake na imetupasa tuuombe katika sala. Imetupasa tujiulize, Je! twafanya mazoea ya kutanguliza faida za Ufalme, au twafanya mazoea ya kutanguliza faida nyingine?
11. Shughuli za kimwili zawezaje kuwa kikwazo cha kuizoea kweli, nazo nguvu za kufanya yaliyo haki zatoka wapi?
11 Lazima tujihadhari tusiache cho chote kituondoe kwa upendo wa Mungu. Kumbuka, wakati wa nabii Hagai yeye aliwaambia watu wasiojali ugumu wao ulikuwa nini. Maneno yake yalikuwa haya: ‘Ninyi mnakimbilia kila mtu nyumbani kwake wakati ambapo nyumba yangu inakaa hali ya kuharibika.’ (Hag. 1:9) Je! tutaufuata mwendo ule ule na kujiondoa kwa baraka ya Yehova? Kama Yehova akiitikisa dunia, nayo milima yatetemeka kuingia moyoni mwa bahari, ni nini kitakachozipata nyumba zetu na mapambo mapya na maendeleo tuliyoyafanya? (Zab. 46:2) Basi, ni jambo la lazima namna gani kuendelea kuizoea kweli, tukishiriki kabisa katika kazi yetu ya waziwazi ya kuhubiri. Wakati unakaribia ambapo utendaji huu ambao hautarudiwa tena utakwisha. Dhiki kubwa iko mbele yetu. Kwa nguvu za Mungu wa nuru na tufanye kwa uwezo wetu lo lote mikono yetu ipatalo kulifanya. Yakumbuke maneno ya Paulo: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) “Mambo yote” hayo na yatie ndani kuhubiri kwetu waziwazi kwa sifa ya jina la Yehova.
“KUTEMBEA NURUNI” KWA KUPENDA NDUGU ZETU
12. Ni namna gani nyingine ya giza ambalo lazima tuepuke, na kwa sababu gani?
12 Sasa tukigeukia mazoea mengine ya kweli yaliyo ya maana, twasoma tena katika kitabu cha Yohana wa Kwanza: “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.” (1 Yohana 2:9-11) Kushika amri za Mungu na kuizoea kweli kunahusiana sana na kupenda ndugu ya mtu. Lingekuwa jambo la upumbavu namna gani kujiongoza wenyewe kwa unyofu katika mambo yote, tukishiriki kwa kawaida katika kukusanyika na watu wa Mungu na katika utendaji wa kuhubiri na kufundisha, na wakati ule ule tuwe hatuwajali ndugu zetu wa Kikristo nyakati nyingine, tujitenge nao, tusifikirie hali yao njema.
13. (a) Kufikia hapa mtu aweza kuuliza maulizo gani kwa busara? (b) Mifano inayohusu ndugu zetu katika Malawi na Nicaragua yaonyeshaje kwamba watumishi wa Mungu wataka kuizoea kweli kwa kuonyeshana upendo?
13 Huenda mtu akauliza, ‘Hii yaweza kuwaje?’ Mtu aweza kusema: ‘Nawapenda ndugu zangu. Ningefurahia kuwafanyia lo lote. Lakini naweza kufanya nini? Wanahitaji nini?’ Na tuone mambo namna hii: Katika miaka ya karibuni zimekuwako pindi ambapo watumishi wa Yehova wametaabika sana katika sehemu mbalimbali za dunia. Kwa mfano, katika nchi ya Malawi watu wa Yehova waliteswa sana, mwishowe ikiwalazimu walio wengi watoroke nyumbani kwao na nchini na kuanza kukaa katika nchi nyingine kwa sababu ya upinzani kwa mwenendo wao wa Kikristo. Katika nchi ya Nicaragua tetemeko la nchi liliupiga mji mkuu, Managua, na Wakristo wengi waaminifu wakapoteza mali zao zote—nyumba zao, kazi, mahali pa kukutania, kila kitu. Itikio la watumishi wa Yehova ulimwenguni pote lilikuwa nini? Hali njema ya ndugu zao hawa wa kiroho ilifikiriwa sana. Hili lilionyeshwa kwa msaada uliotumwa kwa ajili ya Wakristo hawa. Ulikuwa wonyesho mzuri sana wa kufikiria kwa Kikristo, wa uangalizi kwa ndugu za mtu.
14. Ni nani kundini tuwezao kukumbuka tuizoeapo kweli kwa kuonyesha kupendezwa kwa ndugu zetu, na ni kwa njia gani tuwezavyo kusaidia?
14 Lakini na tulete mambo kwenye kiasi kinacholingana na mahali petu. Je! twafikiria wengine hivyo na kuizoea kweli kati ya wale tukutanao kwa kawaida na wale ambao twawajua sana katika makundi yetu wenyewe? Bila shaka, wengi wanawafikiria, lakini kumbuka sasa twajichunguza wenyewe. Hizi ni nyakati ambapo watu wanaona mkazo mwingi kwa sababu ya maisha yanayozidi kuwa yenye gharama. Mkazo huo unaongezeka sana ikiwa mwenye kuruzuku jamaa anaondolewa kazini kwa muda. Vikundi vingi vya jamaa na watu mmoja mmoja wajiruzukuo kwa mapato yasiyobadilika wanapata shida kuwa na vitu vya lazima vya maisha, na miezi itakayokuja hali hiyo bila shaka itakuwa mbaya zaidi. (Hab. 3:17) Tutafanyaje mmoja mmoja tukijua kwamba mtu mwingine au kikundi cha jamaa katikati yetu, kimeingia shidani si kwa sababu ya kosa kwa upande wao wenyewe? Kama vile mwanafunzi Yakobo alivyoandika: “Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini?” (Yak. 2:15, 16) Ni jambo la kufikiriwa na wale wanaoizoea kweli.
15. Ni nani wengine wanaohitaji kufikiriwa nasi, na kwa njia gani ziwezekanazo?
15 Namna gani juu ya wengine wa ndugu na dada zetu wazee kundini? Wao wanaendeleaje? Je! tunaonyesha kwamba ‘tunatembea nuruni’ kwa kuwahurumia na kuwafikiria? Je! tunaendelea kuzishika amri za Yehova kwa habari yao? Pengine nyakati nyingine wanahitaji mtu akawachukue na kuwasaidia kufika mikutanoni au katika utumishi wa shambani. Huenda pia wakahitaji msaada kupata vitu vya kimwili vilivyo vya lazima kwa maisha au kusaidiwa watunze nyumba zao. Hizi ni njia za kuizoea kweli. Nyakati nyingine walio wakongwe wanashukuru mtu akiwapitia kuwatembelea, kuzungumza juu ya kweli ya Neno la Mungu, kupendezwa nao. Twaambiwa hivi katika Maandiko: “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” (Mit. 16:31) Bila shaka Yehova anapendezwa namna gani kuwaona watumishi wake ambao wamekuwa wakifanya mapenzi yake kwa uaminifu kwa miaka mingi sana wakiangaliwa na wengine wanaoizoea kweli, na wanaotembea nuruni!
16. Ni kwa njia gani heshima kwa wazee kundini ilivyo njia nyingine bado ya kuizoea kweli?
16 Yatupasa pia tukumbuke kwamba kuizoea kweli kwatia ndani na kuonyesha heshima kwa wazee wasimamiao kwa njia njema. Shauri la mtume Paulo ni: “Lakini, ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao. Iweni na amani ninyi kwa ninyi.” (1 The. 5:12, 13; Ebr. 13:17) Je! hivi ndivyo tuwaonavyo wanaume wazee katika makundi yetu?
17. Wazee nao wawezaje kuonyesha wanaizoea kweli?
17 Bila shaka, ni wazi pia kwamba wale wanaosimamia lazima wawe wanaizoea kweli, wakiwa na kupendezwa kwingi sana na hali ya “kondoo.” Haiwapasi wajifanye mabwana juu ya ndugu zao, kwa maana wakifanya hivyo wasingekuwa wakizionyesha njia za Yehova, Mungu wa nuru. Wako chini ya amri ya moja kwa moja ya Mungu ‘kulichunga kundi la Mungu . . . si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari . . . si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.’—1 Pet. 5:2, 3.
18. Eleza kwa ufupi hekima ya shauri lenye nguvu la Paulo kwa watu wa Mungu.
18 Mwishowe, imepaswa ikumbukwe kwamba kuizoea kweli, kutembea nuruni, kushika amri za Yehova, kujiepusha na giza la taratibu hii mbovu ya mambo, kwatuhitaji sote tulifuate shauri lenye nguvu la mtume Paulo katika maneno yake ya hekima kwa kundi la Kolosai: “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”—Kol. 3:12-14.
19, 20. Ni tukio gani katika siku za Musa litukumbushalo juu ya ulimwengu tuishimo leo, nasi twawezaje kwa kipekee kubarikiwa kwa sababu ya kuizoea kweli kwa kushika amri za Yehova?
19 Humu basi, twaona nyingine za njia tuwezavyo kuizoea kweli na kushika amri za Mungu katika siku hizi za giza tititi lililo juu ya watu kwa sababu ya kupofushwa kwa akili za watu na Shetani, ili habari njema tukufu juu ya Kristo zisiwaangazie. Giza la ulimwengu liwapo jingi zaidi, nuru ya kweli kutoka kwa Neno la Mungu yaangaza zaidi. Yatukumbusha juu ya siku za Musa Waisraeli walipokuwa Misri utumwani. Pigo la tisa juu ya Farao wa Misri mwenye moyo mgumu lilikuwa lile la giza nene juu ya nchi. Twapata habari zake katika maneno haya: “Musa akaunyosha mkono wake kuelekea mbinguni; kukawa na giza nene katika nchi yote ya Misri muda wa siku tatu; hawakupata kuonana mtu na mwenziwe, wala hakuondoka mtu mahali alipokuwa muda wa siku tatu; lakini wana wa Israeli wote walikuwa na mwanga makaoni mwao.”—Kut. 10:22, 23.
20 Tunaishi katika nyakati za maana sana, nao ulimwengu upapasapo gizani, usijue njia ya kutokea, nuru ya kweli kutoka kwa Mungu wa nuru na nuru yake ya ulimwengu, Bwana Yesu, yaangaza kwa weupe. Yafaa namna gani kwamba tufikirie kwa kawaida yanayomaanishwa kwetu sote kuizoea kweli na kuendelea kushika amri za Mungu, kutembea nuruni. Linalomaanishwa na hilo kwa siku zilizoko mbele linatajwa katika maneno haya ya mtume Yohana: “Bali tukienenda nuruni, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.” (1 Yohana 1:7) Na tuwe wenye shukrani kwa umoja wetu na Mungu wa nuru, ambaye ndani yake hamna giza lo lote.
[Picha katika ukurasa wa 133]
Katika mikutano ya kila juma ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo, mamia ya maelfu wanakusanyika kwa mazungumzo ya Biblia yenye kujenga