Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 5/1 kur. 198-203
  • Wokovu na Uzima kwa Kupatana na Kusudi la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wokovu na Uzima kwa Kupatana na Kusudi la Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSUDI LA MUNGU LA KUJIPATANISHA NALO SASA
  • JAMBO LINALOSTAHILI KUOKOKEWA
  • Kusudi Lenyewe la Uhai
    Amkeni!—1992
  • Kusudi la Mungu kwa Kufanya Wengine ‘Wazaliwe Mara ya Pili’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
  • Maisha Duniani—Je! Ni Safari ya Kupitia Tukielekea Mbinguni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 5/1 kur. 198-203

Wokovu na Uzima kwa Kupatana na Kusudi la Mungu

“Alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake.”​—2 Tim. 1:9.

1. Ni nini kinachokaribisha wanadamu sasa, na kusudi limetiwaje katika maisha za wale wanaokiitikia?

KWA mara ya kwanza inaelekea kutowezekana, lakini wakati ujao ulio mzuri ajabu uliopangwa na mtu mwenye uwezo sana sasa unawaita wanadamu. Yajapokuwa makelele na ghasia za namna zote za maenezi, watu wengi wenye kutega masikio wameusikia mwito huu wakauitikia kwa kufaa. Wao ndio wanaofurahi zaidi kwa ajili yake. Sasa wanao mwito ufaao katika maisha. Ndiyo, sababu ya kweli ya kuendelea kuishi na kuokoka kuona tumaini jangavu inakuwa ya kweli. Maisha hayaelekei kuwa ya kuchosha tena, yasiyo na kusudi, yakiongoza kwenye ubatili tu. Wao wanaishi kwa ajili ya taratibu mpya yenye haki ya mambo inayokaribia.

2. Huu ni mwito wa namna gani, na kwa sababu gani kuukubali hakukatishi tamaa?

2 Watu wengi wanafikiri kwamba wanao mwito wa hili au lile. Lakini sivyo ulivyo mwito huu. Huo si nguvu tu ya kuendesha kwenye mwendo fulani wa tendo. Huo si nguvu tu ya kidini ya kuendesha inayoambatana na kusadiki kuwa na maongozi ya kimungu yaliyoshikamanishwa nayo, kama vile nguvu ya kuongoza kufanya huduma ya dini fulani. Si kichocheo cha ndani tu hata mtu asijue namna ya kusimulia na ambacho mtu mmoja anacho na wengine hawana. Badala ya kuwa usioelezeka, mara nyingi jambo la kuchukuliwa na fikira tu, mwito huu wa kisasa au mwaliko unakuja kwa maneno ya waziwazi, na mtu anajua uko wazi kwake aukubali. Si ishara ya wakati ujao unaowezekana ulio na nafasi nzuri ajabu. La, bali unatoka kwa mtu mwenye mamlaka na madaraka. Kwa hiyo analoitiwa mtu si jambo la kuwaziwa bali lililothibitishwa kabisa. Kuitikia kwetu mwito huu mzuri ajabu kwa njia ifaayo hakutafanya tukate tamaa.

3. Mwaliko kwa kawaida ni wonyesho wa nini, na kwa njia gani ndivyo ilivyo kwa yeye atoaye mwito wa kisasa?

3 Ni nini kinachoufanya mwito huu au mwaliko kuwa wa pekee sana? Basi, mara nyingi mwaliko ni tendo la ukarimu, la nia njema. Una kusudi jema. Ndivyo ilivyo kwa mwaliko ule ambao watu wengi sana wenye kuthamini mambo sana wanaukubali leo kwa shukrani. Mtu mwenye moyo mkubwa ambaye mwaliko wake wameukubali ndiye Yeye aliyepanda paradiso duniani kwa ajili ya wanadamu zamani za kale wapate kuifurahia milele. Hii ilikuwa mwanzoni mwa kuwako kwa mwanadamu duniani. Je! hilo halikuwa jambo lenye kusudi zuri kwa Huyo kufanya? Lilikuwa ndilo jambo hasa la kutazamiwa kutoka kwake Huyo, kwa maana yeye si mwingine ila Mungu, Muumba wa mbingu na dunia. Yeye Ndiye aliyemleta mwanadamu katika dunia hii, pamoja na vitu vyote vilivyohitajiwa vilivyotayarishwa bila hitilafu kwa ajili ya mwanadamu. Si kwamba tu hili lilikuwa tendo la fadhili zisizostahili kwa upande wa Mungu kwa mwanadamu, bali pia Mungu alikuwa na kusudi akilini. Lilikuwa kusudi jema.

4, 5. Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo alionyeshaje namna kusudi na fadhili zisizostahili zinaungana pamoja katika mwito wa Mungu?

4 Namna kusudi na fadhili zisizostahili zinavyoungana katika matendo ya Mungu kutokeza mwisho bora inakaziwa fikira zetu na mleta habari wa mambo mema wakati wa karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Huyu alikuwa Paulo, mwandikaji wa barua kadha kwa rafiki yake mkubwa na mfanya kazi mwenzake, Timotheo, ambazo barua hizi za Paulo tulihifadhiwa katika kurasa za mwisho za Biblia Takatifu. Barua yake ya pili iliandikwa kwa Timotheo muda mfupi baada ya Milki ya Kirumi chini ya Kaisari Nero kuanza kuwatesa Wakristo. Kwa hiyo Paulo alikuwa mfungwa Rumi kwa ajili ya Ukristo wa kweli. Lakini hakumlaumu Mungu kwa sababu ya hali hii, wala hakumlaumu Mwanzilishi wa Ukristo wa kweli, Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Bila ya kuonea haya kufungwa kwake, Paulo aliandika hivi:

5 “Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake.”​—2 Tim. 1:8, 9.

6, 7. Je! mwito wa Paulo ulikuwa wa namna ya nguvu fulani ya ndani yenye kumwendesha kwenye mwendo fulani wa tendo au kazi, au namna gani?

6 Katika maneno hayo mtume Paulo anakubali kwamba kuitwa kwake kwa mwito mtakatifu hakukuwa kwa sababu ya matendo yenye kustahili kwa upande wake, bali kwa sababu ya ‘makusudi na neema’ kwa upande wa Mungu. Ndivyo ilivyokuwa na kwa Timotheo. Kuitwa kwa Paulo na Timotheo hakukuwa kwa namna ya nguvu fulani ya ndani yenye kuwaendesha kwenye mwendo fulani wa tendo au wajibu. Paulo aliitwa moja kwa moja kupitia kwa Yesu Kristo aliyefufuliwa, aliyemtokea Paulo alipokuwa katika njia ya Dameski ya Shamu na aliyemwambia Paulo kwamba katika Dameski angearifiwa imempasa afanye nini. Baada ya Paulo kubatizwa kama Mkristo katika Dameski, alianza haraka kuyafanya mambo aliyoitiwa na kuambiwa ayafanye. (Matendo 9:1-30; 22:1-16) Kwa hiyo, alipokuwa akitoa ushahidi mbele ya Mfalme Herode Agripa katika kipindi cha baraza ya Kirumi katika Kaisaria, Paulo alisema hivi:

7 “Kwa hiyo, Ee Mfalme Agripa, sikuyaasi yale maono ya mbinguni, bali kwanza niliwahubiri wale wa Dameski na Yerusalemu, na katika nchi yote ya Uyahudi, na watu wa Mataifa, kwamba watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao.”​—Matendo 26:12-20.

8. Mtume Paulo alishirikije katika mwito wa Timotheo?

8 Kwa upande wa Timotheo, pia, wake haukuwa mwito au mwaliko wa namna ya kichocheo cha ndani chenye kuambatana na kusadiki maongozi ya kimungu. Haukuwa jambo la kuchukuliwa na fikira juu yake, bali Timotheo alimsikia mtume Paulo akilihubiri kundi katika Listra naye akakubali ujumbe wa Ufalme na kubatizwa kama Mkristo. (Matendo 14:6-23) Mtume Paulo aliuthibitisha mwito wa Kikristo wa Timotheo kwa kumwekea mikono na kumpa karama ya kiroho. Kwa hiyo, katika barua yake ya mwisho kwa Timotheo, alimwambia hivi: “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.” (2 Tim. 1:6) Kwa sababu ya kuuitikia mwito kama Mkristo aliyebatizwa, njia ilifunguliwa kwa Timotheo awe mshiriki wa karibu mwenye kutumainiwa wa mtume Paulo katika kazi yake ya umisionari. Kwa kupokea roho ya Mungu na kudhihirishwa kwake, Paulo na Timotheo pia walijua kwamba walikuwa wameitwa na Mungu kwa sababu ya kusudi la Mungu na fadhili zisizostahili.

9, 10. (a) Kujua kwa Paulo kwamba alikuwa na mwito kulitia nini katika maisha yake? (b) Kwa hiyo, Paulo aliendelea kukaza macho yake kwenye nini, kama mshindani katika michezo gani?

9 Kujua kwa mtu waziwazi kwamba anao mwito au mwaliko kunatia kusudi katika maisha yake. Paulo alikaza fikira kwenye uhakika huu, katika barua yake ya pili, wakati alipomwambia Timotheo hivi: “Wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu.” (2 Tim. 3:10) Kwa sababu Paulo alikuwa na kusudi alivumilia na kushikamana na mwendo fulani wa maisha. Aliweka jicho lake kwenye kusudi lake alilopewa na Mungu. Yeye alikuwa na “mradi wa jicho” au “lengo la jicho,” kama vile maneno ya Kijapan na Kikorea ya “kusudi” yanavyomaanisha. (Kijapan, moku teki; Kikorea, mok jok) Alijifananisha na mshindani katika shindano la kupiga mbio za miguu macho yake yakiwa yamekazwa bila kuondoka kwenye mahali ambapo mshindi angepewa zawadi. Kwa hiyo aliyaandika maneno haya juu yake mwenyewe:

10 “Nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”​—Flp. 3:12-14.

11. (a) Kwa hiyo, Paulo alipatanisha mwendo wake wa maisha na nini? (b) Paulo aliipa zawadi iliyowekwa mbele yake thamani gani?

11 Kulingana na maneno hayo ya mtume Paulo, Mungu Ndiye aliyetoa mwito kupitia kwa Kristo Yesu, nao mwito huu ulikuwa wenye kusudi. Kwa kuzithamini fadhili hizi zisizostahili kwa upande wa Mungu kwake, Paulo alipatanisha maisha yake na kusudi la Mungu. Paulo aliona waziwazi njia ya kufuata, kwa maana Mungu alikuwa ameweka mradi mbele yake. Kama angeufikia mradi huo kwa kufanikiwa, angepokea zawadi kutoka kwa Mungu. Paulo hakuidharau zawadi hiyo, kwa maana kufanya hivyo kungemaanisha kudharau fadhili zisizostahili za Mungu kwa upande wake. Ilikuwa zawadi nzuri ajabu, nayo ilifananisha ukarimu usio wa kawaida, moyo mkubwa, kwa upande wa Mungu. Kwa kweli ilikuwa ndiyo zawadi kubwa na bora zaidi kupita zote ambazo Mungu angeweza kuvipa viumbe, yaani, urithi wa ushirika pamoja na Mwana wa Mungu aliyetukuzwa, Yesu Kristo, katika ufalme wake wa kimbinguni. (Flp. 3:7-11; 2:9-11) Si ajabu kwamba Paulo alifikiria faida zote za kidunia za kichoyo kama takataka kabisa! Yeye alikaza macho yake kwenye zawadi.

KUSUDI LA MUNGU LA KUJIPATANISHA NALO SASA

12, 13. (a) Wakati wa karne kumi na tisa zilizopita, watu kama Paulo wamekuwa wakipatanisha maisha zao na nini? (b) Karibuni, mamia ya maelfu yamekuwa yakifanya nini kiwe mradi wao kulingana na kusudi la Mungu?

12 Kwa karne kumi na tisa zilizopita watu kama mtume Paulo na Timotheo wamekuwa wakipatanisha maisha zao na mwito wa Mungu kwenye tumaini la kimbinguni, wakashiriki pamoja na Yesu Kristo aliyetukuzwa sana katika ufalme wa kimbinguni utakaomimina baraka juu ya wanadamu. Wamefuata onyo na kutia moyo kwa Paulo, “ili mwenende kama ilivyo wajibu wenu kwa Mungu, mwenye kuwaita ninyi ili mwingie katika ufalme wake na utukufu wake.”​—1 The. 2:11, 12.

13 Walakini, si kwamba tu Mungu ana kusudi kwa habari ya jamii hiyo ya Ufalme bali pia ana kusudi kwa habari ya wanadamu watakaoishi katika furaha chini ya ufalme huo wa kimbinguni. Je! si vema kujua kwamba Mungu hakuwaacha wanadamu kwa ujumla nje ya makusudi yake? Kile ambacho Mungu amewekea wanadamu, na ambacho sasa anakaza kwenye fikira za pekee za wanadamu, ni kitu cha ajabu kwa wanadamu kufikia chini ya ufalme wa Mwana wa Mungu mpendwa Yesu Kristo. Kimekuwa mradi ambao sasa mamia ya maelfu ya watu wenye shukrani wanajitahidi waufikie kwa msaada wa Mungu. Kwao ni kama zawadi inayowaelekeza waendelee mbele, kitu chenye neema kinachowaalika waje na kushiriki.

14. (a) Sauti ya ukarimu ya mwaliko huu yaonyeshwaje katika Ufunuo 22:17? (b) Ni uzima wa namna gani kwa wanadamu unaotumainishwa na mwaliko huu?

14 Sauti ya ukarimu ya mwaliko inaonyeshwa katika maneno yapatikanayo katika Ufunuo 22:17: “Na [roho] na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” Uzima unaomaanishwa hapa si namna ya uzima wenye kuchukiza tunaobidishwa tuishi sasa kwa sababu ya hali za ulimwengu na urithi wetu wa asili kwa kuzaliwa. Ni uzima duniani ambao mpaka sasa hakuna serikali za kibinadamu zilizoweza kuwapa wanadamu, lakini ambao ufalme wa Mungu peke yake kupitia kwa Mwanawe Yesu Kristo itaweza kuwapa wanadamu kama raia zake. Ndio uzima ambao Mungu Muumba aliukusudia kwa wakaaji wa dunia wawe nao alipomweka mwanamume wa kwanza na mwanamke duniani katikati ya matukufu na mazuri ya paradiso hiyo iliyoitwa Bustani ya Edeni.

15, 16. (a) Kwa sababu gani Paradiso ya kidunia ikawa makao ya kitambo kwa Adamu na Hawa? (b) Alipotaja kusudi lake kwao, je! Mungu alisema lo lote juu ya kupata kwao makao ya kimbinguni, au nini?

15 Wakati Muumba mwenye upendo alipomtokeza mwanamume wa kwanza na mwanamke katika Bustani ya Edeni, yeye hakukusudia Paradiso hiyo iwe makao ya kitambo tu kwao, au “kiota cha upendo” kidogo ili wapate kuwa peke yao kwa kitambo bila ya kuwa na watoto karibu. Sababu ya Paradiso hiyo duniani kugeuka kuwa makao ya kitambo kwao ilikuwa kwamba wao waliacha kuupatanisha mwendo wao wa tendo na kusudi lenye upendo la Mungu.

16 Kusudi la Mungu halikuwa limepata kuwa la kuwapeleka mbinguni wakati wo wote baada ya kipindi cha kuwajaribu hapa duniani. Wao hawakuhitaji mbingu ili kuwa wenye furaha na kuridhika kabisa. Wala Mungu hakuwahitaji wawe pamoja naye huko mbinguni ili apate kuwa mwenye furaha na kuridhika kabisa. Kwa hiyo, wakati Mungu alipotaja kusudi lake kwao, hakusema lo lote juu ya makao ya kimbinguni bali alisema: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini; na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”​—Mwa. 1:28.

17. (a) Mungu alitoa wakati wa kadiri gani pendeleo hili la utumishi litimizwe? (b) Hali zilizoko duniani mwishoni mwa miaka elfu sita ya historia ya mwana damu zimesahahishwa na nini?

17 Kulingana na Biblia Takatifu, Mungu aliweka kipindi cha miaka elfu saba ya pendeleo hili la utumishi kutimizwa. Leo imekwisha pita karibu miaka elfu sita tu katika historia ya kibinadamu, nayo dunia hii si paradiso. Dunia sasa ina idadi ya watu ya karibu wakaaji milioni elfu nne, lakini makaburi yasiyoelezeka yanayoizunguka dunia yashuhudia kwamba wingi mkubwa wa wale waliotoka kwa Adamu na Hawa wamekufa na kwamba wanadamu wote leo wako chini ya laana ya mauti pia. Ndege wa angani, wanyama wa nchi kavu na samaki wa baharini wametiishwa na wanadamu mpaka sasa, lakini idadi zao zimeuawa sana, wengine wanakaribia kutoweka. Nchi iliyo chini ya nyayo zetu imechafuliwa, si na takataka za miji tu na mitaa yenye viwanda, bali, lililo zito kupita yote, na kumwagwa kwa damu kupitia kwa wauaji kwa njia ya siri na katika vita kubwa, za kidini, za kitaifa, za kibiashara na za kisiasa. Kwa sababu gani haya yote? Kwa wazi kwa sababu wanadamu hawakutenda kupatana na kusudi la Mungu.

18. Hali ya kusudi la Mungu la kwanza yaelekea kuwa nini, na ni ulizo gani linalotuzukia?

18 Kufanikiwa kwa kusudi la kwanza la Mungu kwa mwanadamu na makao yake ya kidunia kwaelekea kuwa kumezuiwa au, walau, kumetishwa kwa njia ya hatari sana. Kwa sababu ya kuruhusiwa kwa wakati uliobaki ulizo linatuzukia, Je! kusudi la kwanza la Mungu lenye upendo kwa wanadamu litashindwa au limeachiliwa mbali kama lisilofaa kitu?

19. Katika Isaya 55:10, 11, Mungu alisema nini juu ya kama kusudi lake lililotajwa litaachwa likose kutimia?

19 Hakuna mpango usioweza kutimia kwa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Kupita kwa vipindi virefu vya wakati hakufanyizi tofauti yo yote kwa habari ya makusudi yake. Yeye hayasahau makusudi yake yaliyotajwa. Hasemi uongo kamwe juu ya ahadi yake. Katika Bustani ya Edeni alitoa ahadi yake kwa kuvibariki viumbe vyake vikamilifu vya kibinadamu, Adamu na Hawa, na karibu miaka elfu tatu na mia tatu baadaye alisema hivi, kwa kinywa cha nabii Isaya: “Kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”​—Isa. 55:10, 11.

20, 21. (a) Ni wakati gani Yesu alipotoa tumaini la kurudishwa kwa Paradiso duniani waziwazi? (b) Baada kufufuliwa kwake, yeye alitazamia kazi gani?

20 Pia, zaidi ya karne saba baada ya tangazo hilo la kimungu, au katika siku ya Kupitwa ya mwaka wa 33 wa Wakati wetu wa Kawaida, Yesu Kristo Mwana wa Mungu alilitoa tumaini la kurudishwa kwa Paradiso kwa wanadamu. Siku hiyo, wakati ufalme wa Mungu ulipoelekea kutotoa tumaini lo lote huku Yesu akiwa amening’inia amepigiliwa misumari kwenye mti wa mateso na askari za Kirumi, mtende maovu aliyelaaniwa aliyekuwa ameangikwa kando yake alionyesha imani katika ufufuo wa wafu na katika ufalme wa Mungu wa Kimasihi.

21 Kwa kulichukua kwa uzito shtaka aliloshtakiwa Yesu la kuwa “mfalme wa Wayahudi,” huyu mtenda maovu mwenye kufa alimwambia hivi kwa heshima: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu pia alikuwa anauamini ufufuo kabisa na ufalme wa Mungu uliokuwa mbali sana wakati huo, na kwa hiyo akamjibu hivi mtenda maovu: “Kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:39-43, NW) Siku ya tatu baada ya hapo, Yesu Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu kama roho mtukufu, naye aliutazamia wakati ambao Mungu angempa mamlaka ya ufalme wa Kimasihi na wakati ambapo angeweza kurudisha Paradiso duniani kwa faida ya huyu mtenda maovu mwenye huruma na wanadamu wengine waliokombolewa.​—Ebr. 10:12, 13.

22. (a) Waebrania 13:8 yahakikishaje kutimizwa kwa kusudi la Mungu kwa wanadamu kwa njia ya kufanikiwa? (b) Utimizo huu unaunganishwa na nini sasa?

22 Hivyo Yesu Kristo analithibitisha kusudi la kwanza la Baba yake wa kimbinguni, Yehova Mungu, juu ya wanadamu na makao yao ya kidunia. Juu ya Yesu, imeandikwa hivi chini ya uongozi wa roho ya Mungu: “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.” (Ebr. 13:8) Kwa hiyo yeye hatavunja kamwe ahadi iliyotolewa, hata ingawa mwenye kuahidiwa alikuwa mtenda maovu aliyelaaniwa. Hii yahakikisha kusudi la kwanza la Mungu litatimizwa kwa kufanikiwa kuelekea wazao wa Adamu na Hawa. Lakini inaushikamanisha utimizo wa kusudi hilo la kimungu na ufalme wa Mungu wa Kimasihi mikononi mwa Mwanawe Yesu Kristo. Kwa njia hii kusudi la kwanza la Mungu juu ya wanadamu linaunganishwa na kusudi Lake juu ya ufalme wa Kimasihi.

23. Ni nani ameurithi “ulimwengu ule ujao,” naye anajiona mwenye wajibu wa kufanya nini juu ya jambo hili?

23 Yesu Kristo Mwana wa Mungu alikuwa ndiye mtu mpole zaidi kupita wote waliopata kuwa duniani, mpole hata kumpita nabii Musa. (Hes. 12:3) Katika Mahubiri yake juu ya Mlima Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.” (Mt. 5:5; Zab. 37:11) Kupatana na maneno yaliyoongozwa na Mungu, Yesu Kristo kama mtu mwenye upole kupita wote duniani aliupata urithi wa dunia. Kwa kupatana na hili, inasemwa hivi katika barua kwa Waebrania, sura ya pili, mistari ya tano mpaka tisa: “Hakuuweka chini ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, . . . ila twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu.” Kama mrithi wa dunia, Yesu Kristo aliyetukuzwa anauona wajibu wake wa kuifanya dunia yote iwe katika hali ambayo Mungu alikusudia iwe, ile ya Paradiso, Bustani ya Edeni, iwe makao ya milele yenye furaha ya wanadamu. Ataurekebisha urithi wake kabisa.

JAMBO LINALOSTAHILI KUOKOKEWA

24. Ni wokovu wa nani duniani unaotiliwa mashaka sasa, na kwa sababu gani?

24 Je! hilo si jambo ambalo wanaume na wanawake wenye shukrani wangetaka waokoke wakalipate? Leo karibu kila mtu ni mwenye shughuli nyingi za jitihada za kichoyo za kuokoka ili aendelee kuishi zaidi kidogo tu chini ya taratibu hii ya mambo isiyoridhisha. (Yak. 4:13, 14) Chini ya hali zinazozidi kuwa mbaya ulimwenguni, inakuwa vigumu zaidi na zaidi kwa wanadamu kupata wokovu. Ingawa huenda sasa hali zikawa mbaya ulimwenguni pote, watu wenye kuona mbali wanatabiri mabaya zaidi kwa wakati ujao, na lo! namna gani njaa kuu ya ulimwengu inayoanza kutokea polepole! Wokovu wa hata taifa zima la wanadamu kwa wakati usiojulikana unatiliwa mashaka sasa, kukiwa na uwezekano wa kutokea vita ya atomiki yenye maroketi ya vita kwa njia ya kutisha, pamoja na lundo la silaha zenye kuua wingi wa watu zikiwa nyingi kupita zinavyohitajiwa kufutilia mbali jamaa nzima ya wanadamu, licha ya wanyama.

25, 26. (a) Je! hali iliyopo duniani inamletea Muumba sifa yo yote, na ni jambo la busara kutazamia nini kwa upande Wake? (b) Kwa sababu gani Yeye ana haki zaidi kuchukua hatua sasa kuliko maelfu ya miaka iliyopita?

25 Bila shaka, alipokuwa akiitangaza baraka yake juu ya Adamu na Hawa katika Bustani ya Edeni mwanzoni mwa kuwako kwa wanadamu katika ukamilifu, Mungu hakukusudia wanadamu wajiingize katika hali kama hii ya mambo iliyopo leo. Dunia ikiwa katika hali hii yenye kusikitisha haimletei Yeye sifa kama Muumba. Je! asitazamiwe kuchukua hatua fulani? Je! yeye ambaye Mungu alimfanya mrithi wa dunia asitake pia kufanya jambo fulani kuirekebisha mali yake? Wakati Mungu na Yesu Kristo pia wanapolinganishwa na waliyoyafanya zamani, ni busara kwetu kuwatazamia kuchukua hatua juu ya hali yenyewe. Zamani za kale, si katika nyakati zisizojulikana zilivyokuwa bali katika nyakati za kihistoria, Mungu alichukua hatua chini ya hali inayofanana na ile ya leo lakini isiyo mbaya sana kama yetu sasa. Hali hiyo huko nyuma ilitokea miaka 1,656 tu baada ya kuumbwa kwa mwanadamu, ijapokuwa leo ni karibu miaka elfu sita tangu kuumbwa na kuanguka kwa mwanadamu.

26 Kwa sababu ya kuharibika kidogo kidogo kwa mwenendo wa mwanadamu, bila shaka hali ya wanadamu iliyopotolewa ya ufisadi ni mbaya zaidi sasa kuliko miaka elfu nne na mia tatu iliyopita. Uhakika huu unatoa sababu ya haki zaidi kwa Mungu Muumba kuchukua hatua ifaayo sasa kuliko ilivyokuwa zamani za kale. Wakati umefika kwa Yeye kufanya hivyo kwa kusudi la kujishuhudia mwenyewe.

[Picha katika ukurasa wa 201]

Kusudi la Mungu kwa mwanamume na mwanamke wa kwanza lilikuwa kwamba wazao wao wapanue bustani yao ya Kiedeni duniani pote na kufurahia Paradiso milele

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki