Uhuru wa Kutokuwa na Woga wa Hatari za Kiroho
1. Ili ajipatie uhuru huo wa kutokuwa na woga, lazima mtu afuate mwendo gani?
ILI kupata uhuru wa kutokuwa na woga wa hatari za kiroho zisimuliwazo katika Zaburi 91, lazima tufuate mwendo iagizao. Kwa habari ya sehemu ya mwendo huu, mtunga zaburi aendelea kusema: “Nitasema, [Yehova] ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini.”—Zab. 91:2.
2. Ni nani atambuliwaye hivyo na jina hilo la pekee, kupatana na Kutoka 6:2, 3?
2 Sote na tuangalie kwamba ni Yehova ambaye mtunga zaburi (au yeye awakilishwaye naye) amwambia hivi: ‘Wewe ndiwe kimbilio langu na ngome yangu.’ Kwa njia hii amtambua Aliye juu na Mwenyezi kama Yeye aliye na jina la pekee Yehova. Hii yapatana na Aliye juu alivyomwambia Musa baada ya kurudi kwake Misri: “Mimi ni YEHOVA; nami nilimtokea Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao.”—Kut. 6:2, 3.
3. Alipokuwa akitoa maelezo zaidi juu ya ubora wa jina lake, Mwenyezi alitumia usemi gani wa Kiebrania, nao ulimaanisha nini kama ulivyotafsiriwa na tafsiri fulani za Kiingereza?
3 Alipokuwa akitoa maelezo zaidi juu ya ubora wa jina Lake, Mwenyezi alimwambia Musa: Eh·yehʹ a·sherʹ eh·yehʹ.” Usemi huo, upatikanao katika andiko la Kiebrania la Kutoka 3:14, wamaanisha: “NITAKUWA KILE NITAKACHOKUWA” (tafsiri ya Rabbi Leeser); au, “Mimi Nitakuwa cho chote kile nitakacho” (tafsiri ya Rotherham); au, “NITAJITHIBITISHA KUWA NITAKACHOJITHIBITISHA KUWA.” (New World Translation) Hii ilimaanisha kwamba Mwenyezi huyu angeweza kujigeuza kulingana na hali za watu wake, na kwamba, cho chote alichohitaji kuwa au kujithibitisha kuwa kwa ajili ya watu wake na kupatana na kusudi lake, angeweza kuwa na angekuwa au kujithibitisha kuwa hicho. Angeweza na angepambana na hali yo yote kwa matokeo mazuri. Kwa hiyo, kwa usemi huu wa Kiebrania, Yeye hakuwa akizungumza juu ya kuwako kwake mwenyewe, kuwa kwake wa milele.
4. (a) Kulingana na asili yake ya Kiebrania, jina Yehova lina maana gani, na likimaanisha nani au nini? (b) Namna gani juu ya matumizi ya jina hili kwa Kristo, Mwana wa Mungu?
4 Jina la kimungu lahusiana na usemi huo. Jina Yehova lilifanywa jina lake la “kumbukumbu,” “kumbukumbu langu hata vizazi vyote.” (Kut. 3:15) Kulingana na asili ya jina Yehova katika Kiebrania, laelekea kumaanisha “Yeye Afanya Iwe (au, Kujithibitisha Kuwa),” yaani, kwa habari Yake mwenyewe na kwa habari ya atakachokuwa Yeye au kujithibitisha kuwa, na si kwa habari ya kuumba vitu. Ni nani mwingine katika makao yote ya viumbe vyenye akili angeweza kujipa kwa haki jina kama hilo, isipokuwa Aliye juu na Mwenyezi? Hata Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, hakujipatia jina kama hilo. Angeweza kupewa jina lililounganisha jina la Mungu nalo, kama vile Yeshua au Yesu, limaanishalo “Yehova Ni Wokovu,” lakini si jina Yehova likiwa peke yake kamwe.—Yer. 23:6; 33:16.
5. Kwa sababu gani yafaa kumwambia Yehova kwamba Yeye ni “kimbilio” la mtu na “ngome” yake, na Mithali 18:10 yasema nini kwa hekima?
5 Basi, kwa usahihi wale wafananishwao na mtunga zaburi anayesema katika Zaburi 91:2 waweza kumwambia Yehova: ‘Wewe ndiwe kimbilio langu na ngome yangu.’ Hasa tangu mwaka uliofuata vita wa 1919 C.E., yeye amekuwa vitu hivyo kwao, bila shaka kwa maana ya kiroho. Kwa kuwa Yehova haonekani, yahitaji imani yenye nguvu kwa mtu kumwambia hilo Yeye, na kumaanisha hilo hasa na kutenda kupatana nalo. Walakini, kuna nani mwingine wa kukimbilia kwa ajili ya usalama isipokuwa Yehova Aliye juu? Ni ngome gani ingeweza kuwa imara zaidi au ngumu zaidi kushambuliwa na kushindwa kuliko Mwenyezi mwenyewe? Mfalme wa kale Sulemani aliandika hivi akiwa na hekima iliyoongozwa na Mungu kweli kweli: “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”—Mit. 18:10.
6. Ingawa Kristo sasa ahusika, ni jina la nani linaloitiwa kwa wokovu, na ni nani aliye “kimbilio” na “ngome” kwa Wakristo?
6 Mwishowe viumbe vya kibinadamu visivyokamilika na vyenye dhambi lazima viliitie jina la Yehova kwa wokovu wa milele, hata ingawa sasa jambo hili lafanywa kupitia kwa Yesu Mwana wa Mungu. Si nabii Yoeli aliyekuwako kabla ya wakati wa Ukristo aliyesema hivyo peke yake. (Yoeli 2:32) Mtume Petro pia alisema hivyo siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., wakati kundi la Kikristo lilipoanzishwa. (Matendo 2:21) Miaka mingi baadaye, mtume Paulo pia aliandika hivyo, katika Warumi 10:13. Ingawa ruhusa ya kufika kwa Aliye juu na Mwenyezi sasa yapatikana kupitia kwa Mpatanishi wake tu Yesu Kristo, Yehova angali ndiye ambaye lazima tutafute kimbilio letu katika yeye na ambaye ndiye ngome yetu isiyoshindika.—Sef. 3:12.
MUNGU WA KUTUMAINI
7-9. (a) Kwa sababu gani matumizi ya usemi “Mungu wangu” katika Zaburi 91 hayaizuii isitumiwe kwa Yesu Kristo? (b) Mshangao wa Tomaso mwenye kutia shaka ulikuwa nini mbele ya Yesu aliyefufuliwa, na Yohana alihakikisha nini kwa kutia kisa hicho katika Injili yake?
7 Yehova huyu alimaanisha mengi zaidi kwa mtunga zaburi kuliko kuwa kimbilio na ngome. Maneno yake kamili kwa Yehova ni: “Wewe ndiwe kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtumaini.”—Zab. 91:2, NW.
8 Kumwita kwa mtunga zaburi “Mungu wangu” kulimaanisha kwamba Yehova Ndiye ambaye mtunga zaburi alipaswa amwabudu kama Mungu. Huu ungekuwa usemi ufaao Yesu Kristo mwenyewe autumie kwa Yehova, na matumizi ya usemi “Mungu wangu” hayazuii Zaburi 91 isitumike kwa Yesu Kristo. Alipokuwa karibu ya kufa juu ya mti wa kufishia nje ya Yerusalemu, yeye aliitaja Zaburi 22:1 na kumlilia Baba yake wa kimbinguni kwa nguvu: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” (Mt. 27:46; Marko 15:34) Ni kweli, baada ya ufufuo wake kutoka kwa wafu, Yesu alimruhusu mtume Tomaso achunguze alama za misumari mikononi na miguuni mwake, naye Tomaso akasema kwa mshangao: “Bwana wangu na Mungu wangu!” Lakini Yesu aliuelewa mshangao wa Tomaso ifaavyo, ndivyo na mtume Yohana. Katika kuliaandika hili katika masimulizi yake ya Injili, Yohana hakuwa akijaribu kutoa wazo la kwamba Yesu alikuwa ndiye Yehova Mungu au kwamba Yesu alikuwa “Mungu Mwana” wa utatu; lakini Yohana alisema kusudi la kuandika mshangao wa Tomaso kwa kusema hivi mara tu baada ya itikio la Yesu kwa Tomaso:
9 “Kuna ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake, zisizoandikwa katika kitabu hiki. Lakini hizi zimeandikwa; ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu [si, Mungu Mwana].”—Yohana 20:26-31; Mt. 16:16.
10. (a) Kulingana na ujumbe wake kwa ndugu zake kupitia kwa Mariamu Magdalene, Yesu aliyefufuliwa alikuwa anapaa kwenda kwa nani? (b) Kwa kumwabudu Yehova kama Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, twalindwa na mafundisho gani?
10 Juma moja kabla ya kisa hiki na Tomaso, Yesu aliyefufuliwa alimwambia Mariamu Magdalene hivi, karibu na kaburi ambapo maiti yake ilikuwa imezikwa: “Enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Baba wa kimbinguni alikuwa Mungu kwa Yesu sawa na Yeye alivyokuwa kwa wanafunzi wa Yesu. Mara nyingi Maandiko yaliyoongozwa na Mungu yamsema Yesu Kristo kama “Mwana wa Mungu,” lakini si kama “Mungu Mwana” kamwe. (Mt. 14:33; 27:40, 43, 54; Marko 1:11; 5:7; 15:39; Luka 1:35; Yohana 1:34, 49; 5:25; 10:36; 11:4, 27; Matendo 9:20; Ufu. 2:18; n.k.) Hivyo kwa kumwabudu Aliye juu na Mwenyezi, Yehova, kama Mungu mmoja aishiye na wa kweli (Yohana 17:3) tunalindwa na ibada ya uongo ya utatu na namna nyingine za ibada ya kipagani. Yehova ndiye Mungu tupaswaye kumtumaini.
11. Paulo, Yesu, mtunga zaburi na mtunga mithali walimtumaini nani?
11 Mtume Paulo alisema hivi: “Ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu, aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa.” (2 Kor. 1:9, 10) Pia, Waebrania 2:13 yamtaja Yesu Kristo akiyasema maneno ya Isaya 8:17, 18, nayo yasema: “Na tena, Nitakuwa nimemtumaini yeye. Na tena, Tazama, mimi nipo hapa na watoto niliopewa na Mungu.” Tusijaribu kujitumaini wenyewe au wanadamu wengine wenye kufa: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. . . . Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, na tumaini lake ni kwa [Yehova], Mungu wake.” (Zab. 146:3-5) Mtu mwenye hekima Sulemani aliitaja kanuni ile ile salama ya mwenendo, akisema: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.”—Mit. 3:5.
12. Kumtumaini Yehova kama Mungu kwamaanisha nini kwetu kwa habari ya Neno lake, amri zake na ibada yake?
12 Kwa hiyo, kutumaini kwetu Mungu huyu ambaye jina lake ni Yehova kwamaanisha kushikamana na ibada yake bila kutengeka, bila kuridhiana na Babeli Mkuu, ambayo ndiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Ufu. 17:1 mpaka 18:24) ‘Kumtumaini Yehova kama Mungu’ kwamaanisha kuyaamini kabisa Maandiko Matakatifu ambayo Yeye ameongoza kwa roho takatifu yake na kushika amri zake, kama Mwanawe Yesu Kristo alivyofanya. Yamaanisha kulinda ibada ya Yehova Mungu kwa uaminifu kabisa, kuiweka safi bila mapokeo ya kibinadamu na mazoea ya kilimwengu.
13. (a) Katika mistari hiyo ya mwanzo ya Zaburi 91, twaona mambo gani manne yenye kufanya kazi pamoja kwa ajili ya usalama wetu? (b) Ni wakati gani hasa sifa nne hizo zimefanya kazi kwa ajili yetu, nasi twapata mifano wapi ya hatari tulindwazo nazo?
13 Hapa na tutue na kuangalia kwamba, katika mistari hiyo miwili tu ya mwanzo ya Zaburi 91, tuna majina manne ya maana ya Yeye tuabuduye, pia mambo manne ya lazima yashikamanayo na majina hayo. Angalia haya: (1) Aliye juu pamoja na “mahali pa siri” pake pa kukaa; (2) Mwenyezi pamoja na “uvuli” wake wa kukaa chini yake; (3) Yehova pamoja na kimbilio lake na ngome yake; na (4) Mungu pamoja na kutumainika kwake. Kwa kweli huu ni mwungano usioshindika wa mambo yanayofanya kazi pamoja kwa ajili ya usalama na kuhifadhiwa kwa waabudu wa kweli watimizao matakwa ya kufurahia faida hizo! Mwungano huu usiolinganika wa sifa za kimungu sasa umekuwa ukifanya kazi makumi yote haya ya miaka iliyopita ya “wakati wa mwisho” huu wa taratibu hii ya mambo, ambao kwa sababu yake tumefurahia usalama mzuri sana wa kiroho mpaka sasa. Namna ambavyo jambo hili limetuletea usalama wa kiroho hasa mtunga zaburi sasa aendelea kuonyesha, akitujulisha zaidi na kutufahamisha hatari ambazo tumelindwa nazo.
“MTEGO” WENYE KUTISHA WA “MWINDAJI”
14, 15. (a) Twaona usemi wa namna gani katika Zaburi 91:3, na kwa sababu gani? (b) Ni mfano gani ufananao na huo atoao Daudi katika Zaburi 124, nao watumika kwa nani?
14 “Maana,” asema mtunga zaburi anapotoa habari za namna mambo yaliyotajwa katika mistari miwili ya kwanza yalivyo kweli na hakika, “Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, na katika tauni iharibuyo.”—Zab. 91:3.
15 Usemi hapa ni wa mfano kwa maana sisi si ndege halisi waliomo katika hatari ya mtego wa “mwindaji” halisi. Lakini kufananishwa kwetu na ndege “katika uvuli wake Mwenyezi” kwaendelezwa hapa. Mtunga zaburi Daudi ajifananisha yeye mwenyewe na wenzi wake na ndege ambao kweli wamenaswa mtegoni, lakini ambao wamekombolewa nao. Katika Zaburi 124:1-8 yeye asema hivi: “Israeli na aseme sasa, Kama si [Yehova] aliyekuwa pamoja nasi, wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, . . . Na ahimidiwe [Yehova]; asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege katika mtego wa wawindaji, mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la [Yehova], aliyezifanya mbingu na nchi.” Katika habari hii “wawindaji” hawakuwa wawinda ndege halisi, na “ndege” aliyeponyoka katika mtego wao uliovunjika hakuwa ndege halisi, bali amaanisha “nafsi yetu,” nafsi au uhai wa taifa la Israeli.
16. Kulikuwaje na utimizo wa kisasa wa Zaburi 124, na Je! kuna hatari ya “mtego” mwingine?
16 Katika utimizo wa zaburi hiyo ya unabii, Yehova Mungu aliuvunja mtego ambamo mabaki waliotiwa mafuta wa Israeli wa kiroho walinaswa. Ulikuwa mtego uliofyatuliwa na Babeli Mkuu na wenzi wake wa kisiasa, wa mahakma na wa kijeshi. Katika masika ya mwaka uliofuata vita wa 1919 Yehova uliuvunja mtego huo kwa ajili ya mabaki yake wenye kutubu naye hakuwaacha “wawindaji,” wawinda ndege wa mfano, wadidimishe meno yao ndani ya nyama ya “ndege” aliyenaswa mtegoni. Baada ya hapo mabaki yenye kuokoka ya Israeli wa kiroho waliingizwa katika “mahali pa siri pake Aliye juu,” na “katika uvuli wake Mwenyezi.” Lakini “mtego” ungali umetegwa kwao na “mwindaji,” na Yehova lazima awakomboe wasinaswe ndani yake.
17. Ni nani “mwinda ndege” wa mfano kama ilivyoonyeshwa katika matoleo ya Watch Tower ya mwaka wa 1904 na 1927?
17 Ni nani basi “mwindaji” huyo, nao “mtego” wake ni nini? Imefahamika na kukubaliwa kwa muda mrefu kwamba “mwindaji” wa mfano ni Shetani Ibilisi. Huko nyuma katika toleo la Machi 1, 1904, la Watch Tower, makala yenye kichwa “Chini ya Mbawa Zake!” ilitoa maelezo juu ya Zaburi 91:3 na kusema juu ya “mtego wa mwinda ndege,” kwamba huyu alikuwa “madanganyo ya Shetani, ambamo wote wale wasiolindwa watajikwaa.” (Ukurasa 74, safu 2) Toleo la baadaye zaidi la The Watch Tower lilikubaliana na hilo na kusema hivi: “Yaelekea kuwa hakika kwamba ‘mwinda ndege’ atajwaye hapa na nabii ndiye Ibilisi, na kwamba mtego wake una njia zake atumiazo kupitia kwa tengenezo lake, akifanya kazi kwa njia nyingi mbalimbali za madanganyo ili awanase wale wajidaio kuwa watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi.” (Ukurasa 231, fungu 37, la toleo la Watch Tower la Agosti 1, 1927, lenye kutoa makala ya kwanza ya mfululizo wa makala tatu juu ya Zaburi 91, Authorized Version) Kati ya “wawinda ndege” wote watajwao katika Biblia, Shetani Ibilisi ndiye mkubwa zaidi.
18. Ni nani wafananishwao na wawinda ndege na Yeremia na Hosea, na njia zao ni nini?
18 Akisimulia njia itumiwayo na mwinda ndege wa mfano, Yeremia 5:26 asema hivi: “Maana katika watu wangu wameonekana watu waovu; huotea kama vile watu wategao mitego; hutega mtego, na kunasa watu.” Juu ya namna manabii wa uongo walivyotenda kama wawinda ndege katika taifa la Efraimu lenye kukana imani yake (ufalme wa Israeli wenye makabila kumi), Hosea 9:8 alisema hivi: “Na huyo nabii, mtego wa mwinda ndege u katika njia zake zote.” “Mwinda ndege” mkuu, Shetani Ibilisi, ana kusudi la kunasa watu, wale wanaokaa “katika uvuli wake Mwenyezi.”
19. “Mtego” wa mfano wa “mwinda ndege” mkuu ni nini?
19 “Mtego” wake wa mfano ambao Yehova Mungu awakomboa na kuwasalimisha nao wale wanaoendelea kukaa “mahali pa siri pake Aliye juu” ni nini? “Mtego” wa mfano ambao Shetani Ibilisi ameutega kwa wale wamtumainio Yehova Mungu kama “kimbilio” na “ngome” yao ndio tengenezo la kidunia lipingalo tengenezo la Mungu, yaani, tengenezo la Shetani lionekanalo. Katika hilo Adui mkuu wa Mungu ajaribu kunasa waabudu wa Yehova na kuwashikilia kama mateka, wapatwe na uharibifu wa kiroho kabisa.
20. (a) Ni tangu wakati gani na kuendelea inafaa kuangaliwa kwamba ilionyeshwa Mungu ana tengenezo na kwamba, mtu asipokuwa walo, yeye ni wa nani? (b) Kulingana na maneno ya wazi, Yesu na wanafunzi wake walikuwa wa tengenezo gani?
20 Linalofaa kuangaliwa ni kwamba tangu mwaka wa 1922 na kuendelea ilionyeshwa kutoka Maandiko yaliyoongozwa na Mungu kwamba Yehova Mungu ana tengenezo, kutia na “mabaki” yake waliotengenezwa duniani, na kwamba kuna tengenezo adui, tengenezo la Shetani, lenye sehemu isiyoonekana ya kishetani na sehemu ionekanayo ya kidunia. Ilionyeshwa wazi kwamba, ikiwa mtu si wa tengenezo la Yehova lionekanalo, basi ni wa tengenezo la Adui. Yesu Kristo, ambaye Zaburi 91 yatumika kwake kwanza, alikuwa wa tengenezo la Yehova Mungu. Wanafunzi wake waaminifu pia walikuwa wa tengenezo lilo hilo la kimungu. Ndiyo sababu, alipokuwa akiongoza mitume wake waaminifu kumi na mmoja katika sala, alimwambia Mungu hivi: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14, 16) Alisema ndiyo sababu ulimwengu uliwachukia.—Yohana 15:18-20.
21, 22. (a) Kwa ujumla ni nini kitumiwacho kama chambo kuvuta kitu kwenye mtego, na chambo kitumiwacho na Mwinda ndege aliye Mkuu ni nini? (b) Mungu alimwongoza Yohana aandike nini kwa kupinga chambo yenye kudanganya?
21 Kwa kawaida mtu au kiumbe chatembea kuingia mtegoni bila kujua. Kwa ujumla, mtegaji aweka chambo cha kuvuta kiumbe asiye na habari afikie mahali pa mtego na kuufyatusha mtego kwa kutafuna-tafuna chambo. “Mwinda ndege” Shetani Ibilisi ndiye Mweka Chambo mkuu. Yeye atumia chambo gani kuvuta watu katika tengenezo lake lionekanalo la kilimwengu, wapate kutekwa ndani yake kama vile mtegoni? Chambo ndiyo mambo yenye kuvutia ya ulimwengu huu, nafasi zake zielekeazo kuwa zenye matokeo mazuri za kupatia utajiri kwa choyo, sifa, cheo na uwezo. Akionya juu ya chambo hiyo yenye kudanganya, Yehova Mungu alimwongoza mtume Yohana wa Kikristo awaandikie hivi wale wanaokaa “katika uvuli wake Mwenyezi”:
22 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—1 Yohana 2:15-17.
23. (a) Kwa sababu gani hatutaki kuwa kama Dema, atajwaye akishirikiana na Paulo? (b) Kutii Ufunuo 18:4 kumetutoa katika “mtego” gani, kukatuingiza wapi?
23 Sasa, miaka mia kumi na tisa baada ya maneno hayo kuandikwa na Yohana, tengenezo la Shetani Ibilisi lenye mfano wa mtego lakaribia sana kupita milele. Wale kati yetu ambao tumetoka katika tengenezo la Shetani lionekanalo kuingia “mahali pa siri pake Aliye juu,” sababu gani tutake tuvutwe tena kuingizwa katika tengenezo hilo lililohukumiwa maangamizi? Hatutaki tuwe kama Dema aliyekuwa Mkristo wakati mmoja, ambaye mtume Paulo alisema hivi katika barua ya mwisho kabla ya kufa kwake: “Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike.” (2Tim. 4:10) Babeli Mkuu wa kidini, kutia na Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu), amenaswa naye ashikiliwa sana katika mtego wa tengenezo la Shetani lionekanalo na atapatwa na uharibifu wa mapema pamoja nalo. Kwa kutii amri ya Mungu iliyomo katika Ufunuo 18:4 sisi tumetoka katika Babeli Mkuu na katika mtego wa Shetani ambamo huyo amenaswa. Kwa kutomrudia, twaweza kuendelea kuzifurahia faida za kukombolewa kwetu na “mtego wa mwindaji.” Sisi tuna usalama wa kiroho chini ya “uvuli wake Mwenyezi.”
“TAUNI IHARIBUYO”
24, 25. (a) Mtunga zaburi ashirikisha nini na mtego wa mwinda ndege, katika mstari uo huo? (b) Hii yafananisha nini, na sababu gani kwa kufaa hivyo?
24 Katika mstari uo huo, mtunga zaburi ataja tisho jingine la usalama wa kiroho liwezalo kutokea pamoja na “mtego wa mwindaji,” yaani, ugonjwa wenye kufisha wa kipuku wenye kuenea na kuambukia. Asema hivi: “Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, na katika tauni iharibuyo.”—Zab. 91:3.
25 Kama vile “mtego” wa mwinda ndege, “tauni” hii iharibuyo ni ya mfano. Maana kwa uongozi wa Mungu mtunga zaburi ashirikisha mambo mawili haya pamoja, tauni ya mfano ya leo ni jambo liambatanalo na mtego wa mwinda ndege, yaani, pamoja na tengenezo la Shetani lionekanalo, tengenezo la kidunia. “Tauni” hii ya mfano kwa kweli yazalishwa na kulelewa ndani ya tengenezo hilo la kichoyo la kilimwengu. “Tauni” hii yenye kuambukia ieneayo sana kama tufani duniani mwote ni utukuzo wa taifa.
26. Ni tangu wakati gani utukuzo wa taifa umeshika mataifa, na mwanahistoria Toynbee alisema nini majuzi juu ya utukuzo wa taifa?
26 Wanahistoria wa ulimwengu wameuona uhakika wa kwamba, tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914-1918 C.E., roho ya utukuzo wa taifa imeyashika mataifa ya ulimwengu. Kwa vyepesi hivyo kwa maana vita hiyo ilipigwa na Washirika “kwa ajili ya hiari ya mataifa.” Kasema mwanahistoria Mwingereza Arnold Toynbee majuzi Novemba 21, 1972:
“Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili utukuzo wa taifa umekuwa mara mbili zaidi ya jamii zilizo huru za enzi ya nchini nao umekuwa nusu ya ukubwa wazo wa wastani. . . . Magumu ya wanadamu ya mambo ya afya yasiyotatulika yako katika dunia nzima nayo ni yenye kulemea; hayawezi kutatuliwa na serikali za jamii za nchini. Yahitaji serikali yenye mamlaka ya dunia nzima yenye uwezo mwingi mno wa kutatua magumu. Wokovu wa wanadamu wahitaji umoja wa kisiasa, lakini hali ya wanadamu ya sasa yazidi kuwa yenye migawanyiko. Je! tumepatwa na wazimu?”
27. Utukuzo wa taifa umekuwaje kama “tauni iharibuyo”?
27 Shetani Ibilisi, aliyeitwa na Yesu Kristo “mkuu wa ulimwengu huu,” ndiye wa kulaumiwa kwa sababu ya ongezeko hili la utukuzo wa taifa ambao kwao ametumaini kuharibu wale ambao wamemwambia Yehova: “Wewe ndiwe kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtumaini.” (Zab. 91:2, NW) “Tauni” hii ya kisiasa ya utukuzo wa taifa imesababisha ‘uharibifu’ mwingi. Kujapokuwa kusimamishwa kwa Ushirika wa Mataifa mwaka wa 1920, watawala wenye kutumia nguvu waliojawa sana na utukuzo wa taifa wametokea, kama vile Mussolini wa Italia, Stalin wa Urusi, Hitler wa Ujeremani, chama cha kisiasa chenye kujitakia milki cha Japan, na kadhalika. Kwa hiyo ilichochea Vita ya Ulimwengu ya Pili. Imeongeza sana uzalendo wa ushupavu, imefanya dini zikubali ishara na mifano ya kitaifa, imefanya majeshi yajitayarishe na watu wakatozwa kodi mno fedha ikusanywe, imeleta mashindano ya mataifa yote, ikafanya wasisitizie enzi ya kitaifa badala ya kutii enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote na ufalme wake wa Kimasihi.
28. “Tauni” hii imeleta magumu ya pekee kwa nani, lakini hawa hawakuridhiana na mashirika hayo juu ya ulizo gani?
28 Mbali na misiba iliyoletwa kwa taifa la kibinadamu kwa ujumla, hii imesababisha magumu ya pekee kwa mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Lakini Mwenyezi hakuacha waambukiwe na “tauni” ya utukuzo wa taifa wala kuwa mateka kwa matokeo yake yenye kuharibu sana hali ya kiroho ya Kikristo. Wao hawakuvutwa kwa udanganyifu wala kulemewa wamwabudu “mnyama” wa kisiasa mwenye hesabu 666, wala “mfano” wake wa kisiasa, Umoja wa Mataifa, mrithi wa Ushirika wa Mataifa. (Ufunuo, sura 13; 15:2-4; 20:4) Wao hawakuridhiana na mashirika hayo juu ya kumtolea Mungu ibada ya pekee na kuitegemeza enzi yake kuu ya ulimwengu wote.
29. Ijapokuwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, hawa walitokea wakipendelea nini mwaka wa 1939, na kwa matokeo gani juu ya hali yao ya kiroho?
29 Mwaka wa 1939, ijapokuwa Vita ya Ulimwengu ya Pili yenye kuvuma sana, wao walitokea ulimwenguni pote wakipendelea kutokuwamo kamili kwa Kikristo juu ya mapigano ya kilimwengu ya kisiasa na ya kijeshi. (Tazama makala “Neutrality” katika toleo la Watchtower la Novemba 1, 1939.) Ingawa wametaabika, wengine mpaka kufa, kwa ajili ya uaminifu wao, Yehova Mungu amewasalimisha kiroho katika “mahali pa siri pake Aliye juu” na “katika uvuli wake Mwenyezi.”
—Kutoka The Watchtower, Dec. 1, 1974.
(Itaendelezwa)