Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 6/1 kur. 243-250
  • Usalama wa Kiroho Wapewa Kwetu na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usalama wa Kiroho Wapewa Kwetu na Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MAHALI PA SIRI PAKE ALIYE JUU”
  • “UVULI WAKE MWENYEZI”
  • Yehova Ni Kimbilio Letu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Faida na Thawabu Kutokana na Kuwa Salama Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Uhuru wa Kutokuwa na Woga wa Hatari za Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Mwe na Imani Kama ya Abrahamu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 6/1 kur. 243-250

Usalama wa Kiroho Wapewa Kwetu na Mungu

“Nitasema, [Yehova] ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini.”​—Zab. 91:2.

1, 2. (a) Kama isemekanavyo, Bonaparte alisema nini juu ya upanga na roho? (b) Hitler alijifunza kweli ya maneno hayo kwa habari ya Wakristo gani?

YASEMEKANA kwamba Napoleon Bonaparte mwenye kutumia upanga alisema hivi: “Ziko nguvu mbili ulimwenguni​—upanga na roho. Lakini mwishowe, roho ndiyo yashinda sikuzote.”

2 Kwa wazi mtawala mwenye kutumia nguvu Adolf Hitler hakuyaamini maoni hayo yaliyotolewa na shujaa mshupavu. Kwa nguvu za “upanga” wa vita ya umwagaji wa damu, yeye aliondoka akaushinde ulimwengu. Hitler alijaribu kuivunja roho ya wale walioshikamana na kutokuwamo kwa Kikristo juu ya mapigano ya kilimwengu, katika eneo alilolitwaa kwa jeuri. Katika mwaka wa 1945 nguvu za “upanga” wake zilimwishia na, akikiri kushindwa, akajipiga risasi na mzoga wake ukateketezwa kwa moto. Lakini mashahidi wa Kikristo wa Yehova walioteswa walitokea wakiwa washindi na wenye roho isiyovunjwa nao wakarudia kazi yao ya kutangaza ufalme wa Mungu katika nchi zilizoshambuliwa na Hitler, ingawa idadi zao zilipunguzwa kwa maelfu kadha. Roho ya Mungu iliyokuwa ndani yao ilishinda baada ya miaka kumi na miwili ya kutawala kwa Hitler.

3. (a) Mashujaa hao walitumainia usalama wa namna gani, na kwa matokeo gani? (b) Mashahidi wa Yehova walitumainia usalama wa namna gani, na kwa sababu gani?

3 Bonaparte na Hitler pia walijitafutia usalama katika tengenezo lenye nguvu la kijeshi, pamoja na uwezo mkuu wa kisiasa na maongozi ya mtu mmoja mwenye kutawala kwa nguvu zake peke yake. Namna hiyo ya usalama wa kilimwengu ilionekana kukatisha tamaa, yenye kudanganya. Mashahidi wa Yehova walioelekea kutokuwa salama na kutolindwa walipendezwa na namna tofauti ya usalama. Ulikuwa usalama wa kiroho, kwa maana usalama wa namna hiyo ndio utakaohifadhi mtu katika hali ambapo astahili uzima wa milele katika amani na furaha katika taratibu mpya ya mambo inayokuja kwa ajili ya wanadamu. Mpaka leo hii mashahidi wa Yehova ambao wangali hai katika Ulaya wanajaribu kukaa ndani ya usalama huu wa kiroho, kwa maana njia za kutungwa na mwanadamu za usalama wa vitu vya kimwili, wa fedha na wa kijeshi hazitahifadhia mtu uhai katika taratibu mpya ya Mungu. “Hazina za uovu hazifaidii kitu; bali haki huokoa na mauti.”​—Mit. 10:2.

4. Kwa sababu gani usalama wa kiroho upendelewe kuliko wa kimwili, na ni zaburi gani ya Biblia iusimuliayo?

4 Usalama wa kiroho wamaanisha kuwa na ulinzi wa Mungu wa maisha yetu ya kiroho kupatana na matakwa yake Yeye ya uzima wa milele. Wale walio na usalama wa kiroho ndio Mungu akubali, hata ingawa huenda akaruhusu wapatwe na mauti kwa ajili ya uaminifu wao kwake Yeye mikononi mwa adui. Yeye atathawabisha hali yao ya kiroho itakayoendelezwa mpaka kufa na ufufuo kwenye baraka na nafasi za uzima katika taratibu yake mpya yenye haki. Usalama wa kiroho umepaswa upendelewe kuliko usalama wa kimwili ambao watu wenye kuamini vitu vionekanavyo tu wajaribu kutoa. Usalama wa kiroho ndiyo namna ya lazima tutamaniyo. Huu ndio usalama inayotusimulia Zaburi nzuri ya Biblia ya 91.

5. Kusemwe nini juu ya mtungaji wa Zaburi 91, nayo yakaza fikira zetu kwenye nani?

5 Mtungaji aliyeongozwa na Mungu wa Zaburi 91 yaelekea alikuwa mtu yule yule aliyeandika Zaburi 90, ambayo mstari wake wa mwisho wafuatwa na Zaburi 91 bila kukatizwa na maandishi juu ya sura yenye kumtangaza mtungaji. Ikiwa hivyo nabii Musa ndiye aliyeitunga, ambaye jina lake limepewa katika maandishi yaliyo juu ya Zaburi 90 (NW). Lakini ingawa hali zaelekea kuonyesha hivi, hakuna uhakika juu yake. Hata hivyo, ni mojawapo la maandishi yaliyoongozwa na Mungu ya Neno Lake Takatifu, nalo hili ndilo jambo la maana, ndilo jambo liifanyayo ya kweli na ya kutegemeka. Ikiwa iliandikwa walau miaka 460 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida, haimtaji wazi Masihi aliyeahidiwa kwa muda mrefu, Mtiwa Mafuta wa Mungu, au Kristo. Yakaza fikira zetu juu ya Yeye aliyekuwa Chanzo cha Kimungu cha usalama wa kiroho wa hata Masihi, Kristo.

6, 7. Shetani alitumiaje Zaburi 91:11, 12 alipokuwa akijaribu kumshawishi Yesu Kristo, na kwa sababu gani hakufanikiwa?

6 Kwa mfano, katika mwaka wa 29 wa Wakati wetu wa Kawaida, Adui ya Mungu aliye mkuu alitumia mstari wa kumi na mmoja na wa kumi na mbili kwa mtu fulani katika Mashariki ya Kati. Shetani Ibilisi, Mshawishi, alikuwa ameondoka akaharibu hali ya kiroho ya mtu huyu, akifanya hivyo kwa hila kwa kutumia vibaya Neno lililoongozwa na Mungu mwenyewe. Mshawishi aliingiza wazo la usalama wa kiroho katika mistari hiyo ya Zaburi 91. Alitoa sababu kwamba hasa “Mwana wa Mungu” angepata ulinzi huo wa kimwili wa kipekee. Kwa kumhakikishia Ibilisi hivi na Wayahudi, mtu huyo amepaswa ajitupe chini kutoka kinara cha hekalu katika Yerusalemu na kuacha malaika wamchukue polepole mpaka kwenye sakafu ya mawe ya hekalu kinyume cha sheria za uvutano. Hii ingekuwa kama “ishara itokayo mbinguni.”

7 Kati ya watu wote, Zaburi hii ya 91 imepaswa imfae mtu huyu aliyekuwa ametiwa mafuta kwa roho ya Mungu majuzi apate kuwa Masihi, Kristo. Kwa hiyo Ibilisi alipanga alichodhani kilikuwa kishawishi halisi kwa mtu huyu aliyetiwa mafuta na Mungu. Lakini mtu huyo, Yesu Kristo, aliiona hila hii, akaona namna Zaburi 91:11, 12 ilivyotumiwa vibaya. Akakataa kuuacha usalama wake wa kiroho.

8. Yesu alipingaje kishawishi cha Shetani, na kwa faida gani kwake mwenyewe?

8 Alifanya hivyo kwa kutaja amri iliyoongozwa na Mungu iliyopewa kupitia kwa nabii Musa. Maandishi ya Biblia yatuambia hivi: “Yesu akamwambia [yaani, Ibilisi], Tena imeandikwa, Usimjaribu [Yehova] Mungu wako.” (Mt. 4:7; Kum. 6:16) Ni kweli Yesu aliamini malaika watakatifu wako, lakini yeye hakuamini kwamba malaika hao wangemlinda asijidhuru akijaribu isivyofaa kudharau sheria ya Mungu ijulikanayo ya uvutano ili ajionyeshe na kujihatirisha kipumbavu mbele ya Wayahudi hekaluni. Kwa hekima, katika habari hii, kukaa kwa Yesu katika mahali pake pa usalama wa kiroho kulitokeza usalama wake wa kimwili. Yeye hakufa kifo cha kabla ya wakati wake kwa njia isiyotimiza Andiko. Aliendelea kuishi, katika “mahali pa siri pake Aliye juu.”​—Zab. 91:1.

“MAHALI PA SIRI PAKE ALIYE JUU”

9, 10. (a) Je! Yesu alikuwa akikataa kwamba Zaburi 91 haikutumika kwake mwenyewe kama mtu mmoja? (b) Zaburi hii yatumika kwa nani pia, na kwa njia gani?

9 Zaburi 91 yatumika kwa wakati wenye hatari nyingi kama zitajwazo na mtunga zaburi, ili kutoa faraja, matumaini na uhakikisho kwa wale wanaopitia katika wakati huo wa hatari. Alipokuwa duniani kama mwanadamu, Yesu Kristo angeweza kuifikiria zaburi hii nzuri sana, kwa maana hakuwezi kuwa na shaka kwamba haikutumika kwake kama mtu mmoja. Alipoukataa mpango wa Ibilisi, uliokuwa na msingi wa mstari wa kumi na mmoja na wa kumi na mbili kwa uongo, yeye hakuwa akikataa zaburi hiyo haikutumika kwake kwa njia yenye kufaa. Yesu Kristo ndiye aliyempenda Yehova Mungu kwa utimizo wa mstari wa kumi na nne.

10 Kwa busara ingetumika kwa wanafunzi wake wote waliobatizwa wafuatao nyayo zake kwa uaminifu na kuuiga mfano wake. Si kwamba kila mmoja wa hawa aweza kusema, ‘Zaburi hii yatumika kwangu kama mtu mmoja sawa na ilivyotumika kwa Yesu Kristo.’ Sivyo, bali yatumika kwa wanafunzi hawa wa kweli kama jamii, na ye yote ajikutaye katika jamii hiyo aweza kupata nguvu za kiroho kutokana nayo. Zaburi hiyo haikumsema ye yote hasa wa wanafunzi wa kweli na waaminifu wa Kristo kwa unabii.

11-13. (a) Ni wapi Ufunuo uyatajapo mabaki ya ndugu za kiroho wa Yesu Kristo, na kwa sababu gani lazima wawe katika mahali pa usalama upewao na Mungu? (b) Toleo la Watch Tower la Agosti 1, 1927 lilionyeshaje aliyekuwa katika “mahali pa siri pa usalama”?

11 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo, sura ya kumi na mbili, mstari wa kumi na saba, chataja “mabaki” ya ndugu za kiroho wa Yesu Kristo kama wakiwa juu ya dunia yenye kupigwa na ole baada ya kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi katika mbingu mwaka wa 1914 C.E.

12 Kwa habari ya waliosalia wa “uzao” wa mama wa kimbinguni wa ufalme huo, Ufunuo 12:17 wasema: “Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” Kwa kuwa mabaki haya ya uzao wa mwanamke walioko duniani wafanyiwa vita na Shetani Ibilisi na malaika zake wa kishetani, bila shaka mabaki wamepaswa wawe katika mahali pa usalama wa kiroho upewao na Mungu ambaye amri zake mabaki washika. Kupatana na uhakika huu, katika makala “Mahali pa Usalama,” iliyochapwa katika toleo la Watch Tower la Agosti 1, 1927, fungu la kwanza katika ukurasa 227 lilitaja Ufunuo 12:17 halafu likasema:

13 “Wale walio wa ‘mabaki’ bila shaka watajaribu kwa bidii kupajua mahali pa siri pa usalama nao watakuwa wenye tamaa nyingi ya kukaa humo wakiingizwa ndani.”

14, 15. (a) Kwa ufahamu huo, ni mfululizo gani wa matoleo ulioanzwa huko nyuma mwaka wa 1927? (b) Hii ilikuwa miaka minane kabla ya kundi gani la kisasa la watu kuzungumzwa katika The Watchtower?

14 Kwa hiyo, kwa ufahamu huo wa wale waliokuwa wakikaa wakati huo katika “mahali pa siri pake Aliye juu,” mfululizo wa makala tatu zenye kufuatana zenye kuzungumza juu ya Zaburi 91 ulianzwa, zenye vichwa “Mahali pa Usalama,” “Kwa Nini katika Usalama,” na “Ulinzi na Usalama,” zilizochapwa katika matoleo ya Watch Tower ya Agosti 1 na 15 na Septemba 1, 1927.a Kama ilivyokuwa, maelezo hayo juu ya Zaburi 91 yalichapwa miaka minane kabla ya “umati mkubwa” usimuliwao katika Ufunuo 7:9-17 (AV) kuanza kutokea, au tangu mwaka 1935 na kuendelea. (Tazama makala yenye sehemu mbili iitwayo “The Great Multitude,” iliyochapwa katika matoleo ya Watchtower ya Agosti 1 na 15, 1935.) Katika kuusimulia “umati mkubwa” huu, mtume Yohana aliyeongozwa na Mungu asema hivi, katika Ufunuo 7:14, 15, (AV):

15 “Hawa ndio wao waliotoka katika dhiki kubwa, na wamefua kanzu zao, na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo ndio wao walio mbele za kiti cha enzi cha Mungu, na wamtumikia yeye mchana na usiku katika hekalu lake: naye aketiye juu ya kiti cha enzi atakaa miongoni mwao [au, atatanda hema yake juu yao, Union Version].”

16. (a) “Kundi kubwa” pia limepaswa liwe katika mahali gani pa usalama, na kwa sababu gani? (b) Mbali na Yesu Kristo, ni nani aliyesemwa kwa unabii katika Zaburi 91, na ni tangu lini ndio wakati wa uhitaji wa pekee Zaburi 91 itumike?

16 Kulingana na masimulizi hayo ya unabii, washiriki waaminifu wa “umati mkubwa” au “kundi kubwa” (NW) wamepaswa wawe wakishiriki usalama wa kiroho na “mabaki” ya uzao wa mwanamke leo katika “mahali pa siri pake Aliye juu.” Ama sivyo, Mungu Aliye Juu Zaidi hatawahifadhi wakati wa “dhiki kubwa” wapate kutoka katika hiyo wakiwa hai duniani na kuingia katika taratibu mpya ya Mungu. Katika taratibu mpya hiyo yenye haki wale wa “kundi kubwa” wataendelea kumtolea Mungu utumishi mtakatifu mchana na usiku katika nyua za hekalu lake la kiroho. Hivyo yaweza kuonekana kwamba, mbali na Yesu Kristo mwenyewe, Zaburi 91 haikumsema mwanafunzi ye yote mmoja wa Kristo kwa unabii, bali ilimaanisha wanafunzi wake waliobatizwa kama jamii au kundi, mpaka leo hii. Wakati wa uhitaji wa pekee wa matumizi yake ni tangu mwaka wa 1919 na kuendelea, baada ya kutupwa kwa Shetani na malaika zake wa kishetani, ambako kutupwa huko kulitokea baada ya kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi katika mbingu mwaka wa 1914 C.E.​—Ufu. 12:1-13.

17. Tunapochunguza Zaburi 91 sasa, twaweza kujiuliza ulizo gani la kipekee?

17 Sasa tunapochunguza Zaburi 91, twaweza kujiuliza kwa kipekee, Je! mimi ni mmoja wa jamii iliyopendelewa itajwayo na kusemezwa katika zaburi hii yenye kutia imani nguvu? Ikiwa twaweza kusema Ndiyo, basi twaweza kuwa na uhakika wa kwamba tutaupata usalama wa kiroho usimuliwao katika zaburi hiyo. Kwa kusimulia, zaburi hiyo yaanza, ikisema hivi: “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu atakaa katika uvuli wake Mwenyezi.”​—Zab. 91:1.

18. Hapo “mahali pa siri pake Aliye juu” ni nini, na kwa sababu gani walimwengu hawawezi kupaona wala kupafahamu?

18 “Mahali pa siri pake Aliye juu” sipo mahali ambapo yeye mwenyewe akaa katika mbingu zisizoonekana kwa macho ya kibinadamu, au hata akiwa amejitenga na majeshi ya kimbinguni. Sipo mahali pa kimbinguni palipofananishwa na Patakatifu Zaidi, chumba cha ndani zaidi cha hema ya ibada iliyojengwa na nabii Musa katika jangwa la Mlima Sinai mwaka wa 1513 B.C.E. Humo kuwapo kwa kimungu kulifananishwa na nuru ya mwujiza Shekina iliyokaa juu ya kiti cha rehema cha Sanduku la Agano la dhahabu. Aliye juu hahitaji mahali pa siri pake mwenyewe, ili kujikinga na matisho na hatari zisimuliwazo katika Zaburi 91. Bali, “mahali pa siri” ndipo mahali palipofichwa, maficho, ambapo amewatolea wale watimizao matakwa yaliyoandikwa katika Zaburi 91. Ni mahali pa kimbilio kwao, mahali pa ulinzi kwao. Kwa kuwa ni mahali pa usalama wa kiroho, walimwengu hawawezi kupaona kwa macho yao ya asili, nao hawawezi kuona kwamba wakaaji wake wamo katika “mahali pa siri” hapo, kwa maana hawana ufahamu wa kiroho.

19. (a) Wale waliomo katika “mahali pa siri” walilindwa juu ya ulizo gani, kama ilivyoonyeshwa katika cheo gani? (b) Ni wakati gani ulizo hili lilipotangazwa kwa ulimwengu?

19 Walakini, usalama wa kiroho ufurahiwao na wakaao humo kwa uaminifu washuhudia kwamba kweli wao wamo humo. Mambo ya hakika yaonyesha kwamba wanalindwa kiroho juu ya ulizo kuu ambalo sasa liko mbele ya mbingu yote na dunia. Ndilo ulizo lionyeshwalo na cheo cha Yeye anayetoa “mahali pa siri,” yaani, “Aliye juu.” Ah ndiyo, ndilo ulizo la Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Lilikazwa kwenye fikira za ulimwengu wa wanadamu katikati ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, ambamo mataifa yalikuwa yakipigania ulizo la nani ataitawala dunia, na miezi kadha kabla United States ya Amerika haijajitia katika mpambano huo wa ulimwengu. Katika kusanyiko la mataifa yote la mashahidi wa Yehova wa Kikristo katika St. Louis, Missouri, U.S.A., katika kiangazi cha mwaka wa 1941, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society wakati huo alitoa hotuba juu ya habari “Ukamilifu.” Katika hotuba hiyo kwa makorija ya maelfu ya wakusanyikaji, alisema na akaeleza wazi kwamba ulizo lililo mbele ya uumbaji wote lilikuwa Utawala wa Ulimwengu Wote.​—Tazama makala ya kwanza “Integrity,” iliyochapwa katika toleo la Watchtower la Agosti 15, 1941, ukurasa 245, fungu la 19.

20. Ni wakati gani wa kulitatua ulizo kuu hili, na ni akina nani walionao na kusimama upande wa ulizo hilo wa kumpendelea yeye atakayeshuhudiwa nalo?

20 Maulizo ya utawala wa dunia na enzi za kitaifa za watu yanashindaniwa vikali kwa sasa. Hali ya ulimwengu na orodha ya tarehe za Biblia pia yakionyesha hiki kuwa ndicho kizazi ambamo Aliye juu lazima aamue kwa umilele wote ulizo la muda mrefu sana la Utawala wa Ulimwengu Wote. Wanaokaa katika “mahali pa siri pake Aliye juu” ndio walionao ulizo nao bila shaka wametokea wakiipendelea enzi kuu Yake ya ulimwengu wote na kwa hiyo wanaendeleza kutokuwamo kwa Kikristo juu ya mapigano ya mataifa ya kilimwengu kwa ajili ya enzi ya kitaifa na utawala wa dunia. Wakaaji wasio wa kisiasa wa “mahali pa siri pake Aliye juu” hawakuweza kuingia humo na kubaki humo bila kuitambua na kushikamana na enzi kuu Yake ya ulimwengu wote. Wanatazamia kwa shauku kushuhudia Kwake enzi kuu yake ya ulimwengu wote katika kizazi hiki, katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika mahali pa mfano paitwapo Har–​Magedoni.​—Ufu. 16:13-16.

21. Katika karne ya 20 B.C.E., ni mfalme gani aliyekuwa upande ufaao wa ulizo la enzi kuu ya ulimwengu wote, naye alibariki mzee gani wa ukoo na kwa maneno gani?

21 Katika maandishi ya Biblia Melkizedeki, mfalme wa Salemu katika Mashariki ya Kati, alikuwa katika upande ufaao wa ulizo la enzi kuu ya ulimwengu wote katika kame ya 20 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Masimulizi mafupi yaliyoandikwa juu yake na nabii Musa yahakikisha hilo. Mfalme huyu wa kale alimhesabia Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote ushindi alioupata Abramu (au Ibrahimu) juu ya wafalme washambuliaji wanne waliotoka katika nchi ya Mesopotamia. Kwa habari hii, Mwanzo 14:18-20 watuambia: “Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana. Akambariki, akasema, Abramu na abarikiwe na Mungu aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi. Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. Abramu akampa fungu la kumi la vitu vyote.”

22, 23. (a) Mara baada ya hapo, Abramu alitoaje ushuhuda kwa watu wote juu ya kusimama kwake upande wa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote? (b) Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote alitendaje kulingana na haki yake, kama ilivyoandikwa katika Kumbukumbu la Torati 32:8?

22 Kwa kumpa Melkizedeki kama kuhani wa Mfanyi wa mbingu na dunia fungu la kumi la mateka yote ya ushindi juu ya wafalme washambuliaji wanne, Abramu alisimama pamoja na mfalme-kuhani Melkizedeki katika upande wa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Akishuhudia kwa wote jambo hili Abramu aliapa kwa jina la Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Alifanya hivi alipokuwa akimrudishia mfalme wa Sodoma mali ambazo yeye, Abramu, alikuwa amemtekulia. Mwanzo 14:21-23 watuarifu hivi: “Mfalme wa Sodoma akamwambia Abramu, Nipe mimi hao watu [waliookolewa], na hizo mali uchukue wewe. Abramu akamwambia mfalme wa Sodoma, Nimeinua mkono wangu kwa [Yehova], Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi, ya kuwa sitatwaa uzi wala gidamu ya kiatu wala cho chote kilicho chako, usije ukasema, Nimemtajirisha Abramu.” Yeye ambaye Abramu aliapa kwa jina lake alitenda kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote alipowekea wazao wa Abramu, Waisraeli, nchi katika Mashariki ya Kati aliyokuwa amemwahidia Ibrahimu. Musa asema hivi juu ya jambo hili:

23 “Yeye Aliye Juu alipowapa mataifa urithi wao, alipowabagua wanadamu, aliweka mipaka ya watu kwa kadiri ya hesabu ya wana wa Israeli.”​—Kum. 32:8.

24. Ni kwa njia gani ilivyoonyeshwa katika tangazo kwa Mariamu kwamba malaika waaminifu wamtambua Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, na Yesu Kristo alionyeshaje utambuzi huo katika maneno yake kwa wanafunzi wake yaliyokuwa juu ya kukopesha?

24 Hata malaika waaminifu wa kimbinguni waitambua enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mfanyi mwenye kuumba wa mbingu na dunia. Kwa hiyo, wakati malaika Gabrieli alipomweleza bikira wa Kiyahudi, Mariamu, namna ambavyo angekuwa mama ya mwana wake mzaliwa wa kwanza kwa mwujiza, ambaye angeitwa Yesu, alimwambia hivi: “Roho [takatifu itakujilia] juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Na baadaye Mwana huyo aliyepata kuwa mtu mzima alionyesha kwamba yeye pia alitambua aliyekuwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu.”​—Luka 6:35.

25. Ni sala gani juu ya ulizo la ubora mwingi itajibiwa katika kizazi chetu, nao usalama wetu wategemea nini kwa sababu hiyo?

25 Wakati umekaribia ambapo sala iliyoongozwa na Mungu itajibiwa kwa kuwapinga wapingao enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mfanyi wa mbingu na dunia: “Waaibike, wafadhaike milele, naam, watahayarike na kupotea. Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, Ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zab. 83:17, 18) Kwa hiyo, katika kizazi hiki ambapo ulizo kuu la enzi kuu ya ulimwengu wote litaamuliwa milele, usalama wetu wategemea kukaa katika “mahali pa siri pake Aliye juu,” tukiunga mkono upande Wake wa ulizo bila kuyumbayumba. Kukaa kwetu humo kutakuwa ulinzi tusiongozwe na kupotolewa kwa njia yenye msiba na maenezi yote ya kisiasa yenye kuleta mabishano ambayo yameenea duniani pote sasa.​—Zab. 27:5.

“UVULI WAKE MWENYEZI”

26, 27. (a) Ni akina nani wanaoingizwa kama wageni katika “mahali pa siri pa Aliye juu”? (b) Kwa sababu gani Huyu aweza kufikiliza enzi kuu yake, na kwa hiyo ni jambo gani la busara kwetu kufanya?

26 “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu” atajipatia nini? Mstari kamili wa kwanza wa Zaburi 91 wajibu: “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu atakaa katika uvuli wake Mwenyezi.” Katika habari hii, kujipatia makao kwamaanisha kwamba mtu atatendewa kama mgeni wa Mwenyezi. Mwenyezi huyu ndiye yule yule Aliye juu. Mungu yule yule mmoja ana sifa zote mbili za ukuu upitao wote na uenyezi.

27 Kwa sababu yeye ndiye mwenye uwezo wote, aweza kuendeleza ukuu wake uzidio wa mtu ye yote, enzi yake kuu ya ulimwengu wote. Aweza kufikiliza enzi yake kuu katika sehemu zote za uumbaji, kupinga viumbe vyo vyote vyenye akili na vilivyo hai ambavyo huenda vikamwasi. Ni kazi bure kwa kiumbe cho chote kuipinga au kuipuza enzi kuu ya Aliye juu, kwa maana Yeye ndiye Mwenyezi. Jambo la busara kufanya ni kuitambua enzi kuu Yake ya haki na kuitii, kuwa waaminifu kwayo, sikuzote tukimtambua yeye kama Mwenye Enzi Kuu wa uzima wa mtu. Wafanyao hivyo ndio waingizwao katika “mahali pa siri pake Aliye juu,” kama wageni wa Mwenyezi.

28. Ni wakati gani Aliye juu alipokazia fikira za Ibrahimu ukuu wake upitao wa mtu mwingine ye yote, na Yeye alihakikishaje hivyo?

28 Ni vigumu kwa mamia ya mamilioni ya watu leo wasiofahamiana na Biblia Takatifu kuelewa wazo la Mungu mwenyezi, asiye na kifani katika makao yote ya vilivyo hai. Lakini zamani katika karne ya 20 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida, Aliye juu, Mfanyi wa mbingu na dunia, alikazia uhakika huo fikira za rafiki yake wa kidunia, mzee wa ukoo Abramu. Katika mwaka uliotangulia kuzaliwa kwa mwana wa Abramu Isaka, Aliye juu alijisema kuwa mwenye uwezo wote kupitia kwa malaika Wake. Mwanzo 17:1, 2 watuambia hivi: “Abramu alipokuwa mtu wa miaka tisini na kenda, [Yehova] akamtokea Abramu, akamwambia, Mimi ni Mungu Mwenyezi, uende mbele yangu, ukawe mkamilifu. Nami nitafanya agano langu kati ya mimi na wewe, nami nitakuzidisha sana sana.” Alihakikisha kwamba hakuna lisilowezekana kwake kwa kumpa Abramu na mkewe mzee mwana wao Isaka kwa mwujiza, wakati ambao wote wawili walikuwa wamekufa kwa kadiri kuzaa watoto kulivyohusika. Abramu alikuwa mwenye umri wa miaka 100 na mkewe 90 wakati wa kuzaliwa kwa Isaka. (Mwa. 17:17; 21:1-5; Rum. 4:19-21) Mwenyezi huyu angali yuko.

29. Leo twaweza kuingia katika “mahali pa siri pake Aliye juu” kupitia kwa nani peke yake, na kwa sababu gani?

29 Mwenyezi alikuwa Mungu msiri sana kwa mjukuu wa Ibrahimu Yakobo. (Mwa. 35:11; 43:14; 48:3; 49:25; Kut. 6:3) Aweza kuwa msiri sana kwetu pia, hata ingawa tu viumbe dhaifu sana tukilinganishwa naye. Ebu fikiria kuwa mgeni Wake katika “mahali pa siri pake Aliye juu”! Lakini lazima tukumbuke leo twaruhusiwa tuingie katika usiri huu kupitia kwa kazi nzuri tu za Mwanawe wa kimbinguni aliye msiri zaidi sana, Yesu Kristo. Wakati wa usiku uliotangulia kutoa kwake uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kama dhabihu kwa Mungu kwa ajili ya dhambi zetu, Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Kwa hiyo twamfikia Aliye Juu Zaidi Sana kuliko vyote vilivyo hai kupitia kwake na kumtambua Yeye kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, Mwenye Enzi Kuu wetu ambaye maisha zetu na uaminifu wenye upendo na ibada ni vyake. Kwa njia hii twajipatia ‘makao katika uvuli wake Mwenyezi.’

30, 31. Kwa wazi ni mfano gani aliokuwa akiufikiria mtunga zaburi alipokuwa akisema juu ya kuwa “katika uvuli wake Mwenyezi”?

30 Lo! ni jambo zuri namna gani kwetu kuwekewa uvuli na Mwenyezi! Hii yamaanisha apendezwa nasi, atuhangaikia na kutuangalia. Mfano hapa si ule wa mtu mdogo zaidi akiwa katika uvuli wa mtu mkubwa zaidi wala ule wa kuwa katika uvuli wa kitu kisicho na uhai, “kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isa. 32:2) Mfano ufaao anaowazia mtunga zaburi ndio ule unaoshauriwa katika Zaburi 17:8, ambapo Daudi asali kwa Aliye juu: “Unilinde kama mboni ya jicho, unifiche chini ya uvuli wa mbawa zako.”

31 Ndiyo, mfano unaotumiwa ni ule wa ndege-mzazi mwenye kukaa juu ya makinda yake na kutupa kivuli juu yao. Wakati makinda yaliyo chini yanaona yako katika kivuli cha mzazi wao aliye juu, yanajua yanaangaliwa naye na kulindwa nayo hayawezi kuliwa na ndege walao wengine. Yasemwayo katika Isaya 31:4, 5 yahakikisha kwamba kuruka juu huko kwa ndege kwamaanisha uangalizi na ulinzi: “Ndivyo [Yehova] wa majeshi atakavyoshuka ili kufanya vita juu ya mlima Sayuni, na juu ya kilima chake. Kama ndege warukao, [Yehova] wa majeshi ataulinda Yerusalemu; ataulinda na kuuokoa, atapita juu yake na kuuhifadhi.”

32. (a) Hivyo Mwenyezi na sisi tuliomo katika “uvuli” Wake twafananishwa na nini? (b) Kuwa kwake Aliye juu pia kwamwezesha Yeye afanye nini kama Mkaribishaji mwaminifu?

32 Hivyo Mwenyezi afananishwa na ndege hodari, na wale waliomo katika “mahali pa siri” pa usalama wa kiroho wafananishwa na makinda ya ndege-mzazi. Kuwa kwao “katika uvuli wake Mwenyezi” kwapafanya “mahali pa siri” pawe pasalama zaidi kwao. Kwa kuwa yeye ndiye Aliye juu, kitu kingine cho chote ki chini yake, na hakuna cho chote kilicho chini asichokiona kwa nguvu zake za uenyezi. Aweza kuona mara moja mwendo wo wote kwa upande wa cho chote au ye yote aliye chini akielekea kwenye wale walio chini ya “uvuli” wake. Mara moja aweza kuja kuwalinda na kuwahifadhi waliowekewa uvuli ambao wanakaa naye kama wageni wa kiroho. Yeye kama Mkaribishaji aendeleza heshima yake kwa habari ya daraka lake kwa wale akaribishao kama wageni wake. Wazo hili lafariji namna gani! Ni kupi kwingineko tuwezako kupata usalama wa kiroho?

[Maelezo ya Chini]

a Miaka mingi mapema, kitabu chenye kichwa “The Battle of Armageddon,” kilichochapwa mwaka wa 1897, kilisema hivi katika ukurasa wa 592, fungu la 1: “Zaburi yenye kueleza kipindi hiki yatangaza:​—‘Elfu wataanguka upande wako, na elfu kumi mkono wako wa kuume; lakini haitakukaribia [watakatifu waaminifu, washiriki wa mwili wa Kristo, ambao washiriki wake waliochaguliwa karibuni watakwisha.]’​—Zaburi 91:7.”

Hivyo tayari nyuma huko mwaka wa 1897 mtu aliyesemezwa katika Zaburi 91 alionwa kama mtu mwenye watu wengi ndani yake, jamii ya wanafunzi wa Yesu Kristo.

[Picha katika ukurasa wa 243]

Alipokuwa akimsihi Yesu ajitupe kutoka kinara cha hekalu, Ibilisi alitaja Zaburi kwa udanganyifu kana kwamba ilikuwa uhakikisho kamili wa usalama wa kimwili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki