Unavyofaidika Kutokana na Kufuatia Utawa
‘Walakini utawa pamoja na kuridhika ni faida kubwa.’—1 Tim. 6:6.
1. Ni akina nani peke yao wanaofuatia utawa, nao wanapata nini?
WANAOMJUA Mungu kwa usahihi na kutenda kupatana na wanayojua ndio watu wa pekee walio katika hali ya kumwabudu yeye kwa njia inayofaa. Wao peke yao wanaweza kusemekana wanafuata mwendo wa ‘utawa’ au uchaji. Kufuatia mwendo huu kunaleta faida ya milele. “Walakini,” kaandika mtume Paulo kwa mwangalizi kijana wa Kikristo Timotheo, ‘utawa pamoja na kuridhika ni faida kubwa.’ (1 Tim. 6:6) ‘Utawa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.’ (1 Tim. 4:8) Angalia kwamba Paulo anasema utawa unaleta “faida kubwa” sasa, si thawabu ya wakati ujao peke yake.
2. 1 Timotheo 3:16 inakaza nini kwenye fikira zetu juu ya utawa?
2 ‘Utawa’ au uchaji maana yake ni nini hasa? Hakuwezi kuwa na jibu bora kuliko mfano wa mtu aliyeendeleza utawa kwa njia inayofaa kabisa. Biblia inamwonyesha mtu mmoja kuwa mfano huo. Katika 1 Timotheo 3:16 tunasoma hivi: ‘Bila shaka siri ya utawa [kwa halisi, uchaji mwingi], ni kuu. Mungu alidhihirishwa katika mwili, akajulika kuwa na haki katika roho, akaonekana na malaika, akahubiriwa katika mataifa, akaaminiwa katika ulimwengu, akachukuliwa juu katika utukufu.’ Huyu alikuwa nani, nayo siri hii takatifu ilitimizwaje katika habari yake?
3. (a) Ni ulizo gani lililotokea juu ya utawa karibu miaka elfu sita iliyopita, na kwa sababu gani? (b) Ni katika maana gani jibu la ulizo hilo lilikuwa “siri” takatifu?
3 Karibu miaka elfu sita iliyopita ulizo lilitokea, Ni mwanadamu gani anayeweza kuendeleza utawa kwa njia inayofaa kabisa? Tendo la kumdharau Mungu lililotendwa na mwanadamu wa kwanza Adamu ndilo lililotokeza ulizo hili. Ingawa Adamu mkamilifu alikuwa na deni ya Muumba ya kila kitu, yeye alivunja sheria ya Mungu, kwa njia hiyo akakosa kumpenda Baba yake wa kimbinguni, kumheshimu na kumwabudu alivyostahili kufanyiwa. Baada ya kupoteza ukamilifu kwa kutokutii, Adamu angeweza kuzaa watoto wenye dhambi tu ambao wasingeweza kuendeleza utawa kwa njia inayofaa kabisa. Hata hivyo, Yehova Mungu alijua kwamba angeweza kuweka mwanadamu mkamilifu duniani ambaye angeweza kufanya hivyo. Kabla mwanadamu huyo hajatokea duniani, jibu la nani angeweza kuendeleza utawa kwa njia inayofaa kabisa liliendelea kuwa siri takatifu, yaani, siri iliyojulikana na Mungu peke yake. Kama vile maandiko mengine yanavyoonyesha waziwazi, yeye ambaye siri hii ilitegemea ni Mwana wa Mungu ambaye “alifanyika mwili” akiwa mwanadamu Yesu. (Yohana 1:14; 1 Yohana 4:2, 3) Kwa hiyo, mwendo wote wa maisha ya Yesu Kristo akiwa mwanadamu wa kushikamana na Mungu na Baba yake kwa uaminifu ni wonyesho wa wazi wa utawa au uchaji. Tukiangalia sana masomo yanayohusika katika “siri” hii takatifu tunaweza kupata faida za ajabu sasa na wakati ujao.
4. Mwendo wa Adamu unafunua nini juu ya matokeo ya kukosa kuendeleza utawa?
4 Tunapoangalia yaliyompata Adamu, tunaweza kuona waziwazi kwamba kuacha mwendo wa utawa hakuleti faida yo yote. Kwa sababu ya kutomcha Mungu na Baba yake, Adamu alipoteza uzima mkamilifu wa kibinadamu pamoja na haki zake zote na matumaini. Uhusiano wa karibu karibu aliokuwa amefurahia wakati mmoja na Baba yake wa kimbinguni ulitoweka. Yeye hakuongozwa na Mungu tena. Dhamiri yake ilichafuka. Urithi wa pekee ambao angeweza kupitishia watoto wake ulikuwa kutokamilika na kifo. Baada ya kufukuzwa kwa nguvu alizuiwa asiingie tena ndani ya paradiso nzuri iliyokuwa imekuwa makao yake akiwa mkamilifu.—Mwa. 3:8, 17-19, 24.
5. Yesu Kristo alipata faida kwa kuendeleza utawa?
5 Lakini namna gani juu ya Yesu Kristo? Je! alipata hasara kwa kuendeleza utawa? Ni kweli, haukuwa mwendo mwepesi kwake kufuata. Ulimwengu ulimchukia kwa sababu hiyo. Alitukanwa, akatendewa vibaya kimwili na mwishowe akapigiliwa misumari kwenye mti wa kufishia kama mvunja sheria wa kupindukia. (Yohana 15:18; 1 Pet. 2:23, 24) Hata hivyo, mwendo wake bado ulikuwa wenye faida kubwa. Aliendeleza dhamiri safi akaendelea kufaidika kutokana na msaada, uongozi na mahakikisho ya Baba yake. Yesu Kristo alisikia sauti ya Baba yake mara tatu ikiukubali mwendo wake. (Mt. 3:17; 17:5; Yohana 12:28, 29) Alitegemezwa na Baba yake, akapewa uwezo wa kufanya miujiza, ishara na maajabu. (Matendo 2:22) Yesu Kristo aliposhinda vishawishi vya Ibilisi, “wakaja malaika wakamtumikia.” (Mt. 4:11) Pia, usiku wa mwisho kabla ya kufa kwake, malaika “akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Kwa sababu ya uaminifu wa Mwanawe mpaka kufa, Yehova Mungu alimfufua, akampa zawadi kubwa ya uzima wa kutokufa wa kimbinguni. Mtume Paulo aliandika hivi kwa kuongozwa na Mungu: “Mungu vilevile alimutukuza sana, na kumupa jina lililo yulu ya kila jina; hata kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni na vya duniani, na chini ya dunia [katika makaburi lakini vikingoja kufufuliwa], na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:9-11, Swahili Congo Bible.
6. Eleza maana ya neno “faida” lililotumiwa na Paulo katika 1 Timotheo 6:6.
6 Kwa kuendelea kumwabudu Mungu peke yake kama Yesu Kristo alivyofanya, tunaweza kuwa kati ya wale wanaopata faida kubwa sasa walio na tumaini la kupata baraka kubwa hata zaidi wakati ujao. Hii si kusema kwamba sababu ya pekee ya kumtumikia Mungu na kufuatia mwendo kama wa Kristo ni kupata faida za kipekee. Kufahamu neno “faida” (Kiingereza, “gain”) la lugha ya kwanza kama linavyopatikana katika 1 Timotheo 6:6 kunasaidia mtu apate maoni yaliyosawazika ya shauri hili. Neno hilo lilitumiwa mara mbili tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yaani, katika 1 Timotheo 6:5, 6. Neno hili la Kigiriki (po·ri·smosʹ, si poʹri·sma) linatoka kwa kiarifa (verb) cha Kigiriki chenye maana ya “kuruzuku; kupatia” halafu “njia ya kupatia faida; njia ya kupatia riziki.” Tafsiri ya Moffatt inalitafsiri “jambo la kuhangaikiwa lenye manufaa” na “faida nyingi.” The New English Bible inalitafsiri “magawio ya faida.”
FAIDA YA KUSAMEHEWA DHAMBI
7. Biblia inafunua nini juu ya uhitaji wetu wa kusamehewa dhambi, naye Mungu anautoa juu ya msingi gani?
7 Faida moja kubwa sana inayotokana na kufuata mwendo wa utawa ni kusamehewa dhambi zetu. Kwa mara ya kwanza, hii ilitukia kwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo alipotubu, akageuka mwendo wake wa zamani, akamwomba Mungu amsamehe kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, kisha akajitoa abatizwe, akajiweka wakf kwa Baba (Yehova Mungu) kupitia kwa Mwana (Yesu Kristo) katika jina la Baba, Mwana na roho takatifu. Hata hivyo yeye angali anatenda dhambi baada ya hapo kwa kuwa si mkamilifu na kwa hiyo anaendelea kuhitaji msamaha wa Mungu. Mtume Yohana alisema hivi: “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.” (1 Yohana 1:8) Walakini, mwanafunzi mwaminifu wa Yesu Kristo hataki afanye dhambi moyoni. Anajisikia kama mtume Paulo alivyojisikia alipoandika hivi: “Naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani.” Kwa kuwa ndivyo ilivyo, anasikitikia sana dhambi yo yote ambayo huenda akafanya na kumwomba Mungu amsamehe kwa unyenyekevu. Kwa sababu ya nia yake ya kutubu na kuamini faida za kuondolea dhambi zinatokana na dhabihu ya Yesu, anapata msamaha huo.—Rum. 7:22-25; 1 Yohana 2:1, 2.
8. Kwa sababu ya kusamehewa dhambi zetu, tunaweza kujisikiaje juu ya kumfikia Mungu katika sala, nasi tunaweza kuwa na hakika gani kwamba atatujibu?
8 Kwa sababu ya kusamehewa dhambi zao, wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo wanaendelea kufurahia kuwa na dhamiri safi. Wao wana hakika kwamba Yehova Mungu anapendezwa na jitihada zao za unyofu wa moyo kuishi maisha yanayopatana na maongozi ya roho yake. (Gal. 5:16-18) Kwa hiyo wana uhuru kamili wa kusema wanapomfikia Mungu wakiwa na jambo lo lote, wakiwa na hakika kwamba yeye atawaongoza na kuwasaidia kupitia kwa roho yake washindane na majaribu au watatue magumu ambayo huenda yanawakabili. (Luka 11:11-13) Ni kama mtume Yohana alivyosema: “Lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.”—1 Yohana 3:22.
9, 10. Kama inavyoonyeshwa katika Warumi 8:26, 27, Mungu anatusaidiaje hata wakati ambapo huenda tusijue la kuomba?
9 Walakini, huenda nyakati nyingine Mkristo wa kweli hata akakosa kujua ataomba nini kwa sababu ya mambo yanayomkabili. Huenda kukawa mateso ya mfululizo. Huenda akajisikia mwenye kulemewa na madaraka mengi mazito. Pengine kuna ugumu wa kipekee unaomlemea. Huenda hata akakosa kufahamu ugumu wenyewe ni nini hasa. Hata hivyo, yeye haachwi bila msaada kwa sababu ana hali safi mbele za Mungu. Kama inavyoonyeshwa katika Warumi 8:26, 27, NW, roho ya Mungu itamsaidia. Tunasoma hivi: “Kwa njia iyo hiyo roho pia hujiunga itusaidie udhaifu wetu; kwa maana tatizo la tunayopaswa kuomba hatulijui, lakini roho yenyewe inatuombea kwa mauguzi yasiyotamkwa. Lakini yeye achunguzaye mioyo ajua maana ya roho ni nini, kwa sababu inaomba kupatana na Mungu kwa ajili ya watakatifu.”
10 Kama ilivyotajwa hapa, ni kwa njia gani roho ya Mungu “hujiunga” na “mauguzi yasiyotamkwa” ya Mkristo kumsaidia? Basi, Yehova Mungu aliongoza watu kwa roho yake waandike Biblia, kutia na sala zenye kuonyesha mapenzi na nia yake juu ya mambo. Yeye anajua “maana ya roho,” ya mambo ambayo alifanya roho takatifu yake iseme kupitia kwa waandikaji wa Biblia. Anajua pia mawazo ya ndani na mahitaji ya watu wake. Kwa hiyo, anazikubali sala zilizoongozwa kwa roho Yake kuwa ndizo watu wake wangekuwa wakitoa kama tu wangalijua jambo la kuomba, naye anawajibu. Kwa njia hiyo anasaidia watu wake kufanya mambo maishani mwao kwa njia inayopatana na Neno lake, hata ingawa huenda wakakosa kujua mapema mwendo watakaofuata. Haachi waaminifu wake ‘wajaribiwe kupita wawezavyo,’ wala hawaachi bila kuwasaidia wakati wanapohitaji msaada hasa kwa sababu ya magumu.—1 Kor. 10:13; 2 Kor. 4:8, 9.
KULINDWA NA MAGONJWA YA ULIMWENGU
11, 12. Kufuatia utawa kunamlindaje Mkristo na magonjwa kama ya kisonono na kaswende?
11 Zaidi ya kutuwezesha tuendeleze dhamiri safi na kuendelea kupata msamaha na msaada wa Mungu, kufuatia utawa kunatulinda na magonjwa ya ulimwengu. Kwa mfano, leo magonjwa ya kisonono na kaswende yameenea pote ulimwenguni. Yanapatikana hata katika mahali pa mbali duniani. Tatizo la magonjwa ya kisonono na kaswende ni kubwa sana hata Dr. Marcolino G. Candau wa United Nations’ World Health Organization alionya hivi (katika kipupwe cha mwaka wa 1973): “Hatua ya haraka ni ya lazima kabla magonjwa yenye kuambukiza kwa kufanya ngono hayajawa yasiyoweza kabisa kuzuiwa . . . ulimwengu umeshikwa sana na ugonjwa wa kuambukia watu wengi sana lakini haikubaliwi waziwazi.”
12 Walakini, hakuna ‘ugonjwa wa kuambukia watu wengi sana usiokubaliwa waziwazi’ unaopatikana kati ya wale wanaofuatia utawa. Wao wanafahamu kwamba magonjwa ya kisonono na kaswende si tatizo linalohusu utabibu;. ni la adili hasa. Wanaheshimu sana maneno ya Yesu Kristo: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mt. 5:27, 28) Wakitii amri hii, Wakristo wa kweli wanajilinda wasiingie katika hali ambazo zingeweza kutokeza vishawishi. Kushindana kwao na nyege kumesaidia kuwaepusha na kaswende na kisonono na matokeo yazo mabaya sana—upofu, kumalizika kwa nguvu za uzazi, wazimu na kifo cha mapema. Bila shaka utawa wao umewalinda.
13. Ni faida gani zinazowajia wale wanaotii onyo la upole wajitakase nafsi zao na uchafu wote wa mwili na roho’?
13 Vivyo hivyo, wakithamini onyo la upole la Biblia ‘wajitakase nafsi zao na uchafu wote wa mwili na roho,’ watumishi wa Yehova wanaepuka matumizi ya tumbako, popoo na dawa nyingine zenye kuzoeleza zenye kudhuru. (2 Kor. 7:1) Kushikamana kwao na Neno la Mungu kumewakinga pia na matokeo yenye kuharibu ya kutumia vileo mno kama mazoea. (1 Kor. 6:9-11) Mali zilizokuwa zikipondwa hapo kwanza kwa mazoea yenye kudhuru zimetumiwa upya kufanya watu mmoja mmoja na jamaa zao wawe washiriki wenye matokeo mazuri wa mtaa na kumpa Mungu na watu wake sifa. Mwendo wa utawa umewaletea hili kama “gawio la faida.”
14. Tunapotazama matokeo ya walimwengu, kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba kufuatia utawa kunaleta faida yenye kuonekana? Toa mfano.
14 Faida yenye kuonekana inayofuatana na utawa inaonekana waziwazi inapolinganishwa na hasara kubwa sana inayotokana na kufuata njia za ulimwengu. Chukua mfano wa msichana ambaye amepata namna fulani ya ugonjwa kama kisonono au kaswende au ambaye maisha yake yameharibiwa na dawa za kulevya. Je! hakupata hasara kubwa? Namna gani wazazi wake? Unadhani watalipa pesa ngapi ili wamrudishe binti yao katika hali aliyokuwa nayo wakati mmoja? Pengine hakuna kiasi cho chote kikubwa ambacho wasingelipa wakiwa nacho au wakikipata. Namna gani juu ya mume mzoevu wa vileo? Je! asingeona ni faida kubwa sana kupata tena afya, heshima na cheo ambacho huenda alipoteza kwa kutumia vileo isivyofaa? Je! mke wake asingekuwa na nia ya kutoa pesa nyingi sana ili mumewe awe kichwa kizuri cha jamaa, akiangalia vema madaraka yake? Ndiyo, walimwengu wangetoa vitu vingi wajipatie wenyewe au wapendwa wao faida ambayo utawa unaleta hata sasa.
UTAWA UNALETA RAFIKI
15. Kufuatia utawa kunatupaje rafiki za kweli?
15 Zaidi ya hayo, kufuatia mwendo wa utawa kunatuletea rafiki za kweli. Kama Wakristo wa kweli, rafiki zetu wakubwa zaidi ni Yehova Mungu na Mwanawe Yesu Kristo. Kama vile Yesu alivyowaambia mitume wake kumi na mmoja waaminifu: “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:15) Sisi ni rafiki mtu na mwenzake pia. Kama rafiki, wale wanaomjua Mungu na Kristo wanafaa masimulizi ya Mithali 17:17: “Rafiki [wa kweli] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Ni kati ya wale wanaofuatia utawa katika kundi la Kikristo peke yao unapoweza kupata rafiki hao. Hamna vizuizi vya kikabila, vya kijamii wala vya kiuchumi kundini; wote waliomo ni “ndugu” na “dada.” (Mt. 23:8) Ko kote uendako katika dunia hii, utapata rafiki za kweli kati ya wale wanaozoea utawa. Rafiki hawa ni watu unaoweza kuwaamini ukiwaachia mali zako na ambao hutawaonea mashaka. Wana nia ya kutumia wakati wao, nguvu na mali zao wakusaidie na kukutia moyo. Tena, wako wanaume wenye kustahili katika kila kundi la watu wa Yehova wanaohangaikia kikweli afya ya washirika wenzao, zaidi kwa upande wa kiroho, nao wanaitikia watosheleze mahitaji yao kwa nia na shauku.
“PAMOJA NA KURIDHIKA”
16. Kama inavyoonyeshwa katika 1 Timotheo 6:6, ni nini kinachohitajiwa kulinda faida inayotokana na kufuatia utawa?
16 Kwa kweli, tunapata faida nyingi kutokana na kufuatia mwendo wa utawa. Hata sasa faida hii ni kitu chenye thamani mno hata hakistahili kupotezwa. Kwa hiyo na tuhangaikie kukilinda. Njia bora tunavyoweza kufanya hivi ni kwa kuendelea kuwa wenye kuridhika, kuthamini kweli kweli faida nyingi sana tunazopata. Inastahili kuangaliwa kwamba mtume Paulo aliunganisha utawa na kuridhika, akisema hivi: ‘Walakini utawa pamoja na kuridhika ni faida kubwa.’—1 Tim. 6:6.
17. Kukosa kuridhika na vitu vya kimwili tulivyo navyo kunawezaje kudhuru kwa kiroho?
17 Wakati wo wote tukikosa kuridhika, tukiacha kuthamini baraka ambazo tumezipata kutokana na kufuatia utawa, tunaweza kufikiri kwamba faida kubwa zaidi inaweza kupatikana kwingineko. Kwa mfano, huenda mtu akaacha kuwa na nia inayosemwa katika 1 Timotheo 6:8: “Tukiwa na chakula na nguo [na mahali pa kukaa] tutaridhika na vitu hivyo.” Huenda akaanza kuonea mali za wengine kijicho na kujitia kabisa katika utafutaji wa vitu vya kimwili. Kwa upande wa kiroho, huenda hii ikaharibu, pengine mwishowe iongoze kwenye kupoteza uhusiano unaokubaliwa na Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi akionyesha hatari hii: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”—1 Tim. 6:9, 10; tazama pia Waebrania 13:5.
18. (a) Hatupaswi kuruhusu nini kiharibu kuridhika kwetu? (b) Kama ilivyoonyeshwa na mtume Paulo, sababu ya kuridhika kwa Mkristo imepaswa kuwa nini?
18 Halafu, tena, lazima tujihadhari hali zisije zikatuharibia sana kuridhika kwetu. Mtume Paulo aliweka mfano bora katika habari hii: “Nimejifunza kuwa radhi [au, kuridhika] na hali yo yote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa.” (Flp. 4:11-13) Angalia kwamba Paulo alikuwa akiridhika wakati wote. Yeye hakuwaza hivi, ‘Mimi nitaridhika nikipata utajiri, cheo au ukubwa au mambo kama hayo.’ Kuridhika kwake kulitegemea uhusiano wake na Yehova Mungu na Yesu Kristo, akawajua na kujulikana nao. Huu ndio msingi wa pekee wenye kutegemeka wa kuridhika.
19. Kwa sababu gani ni hatari kuacha vitu vya kimwili au uhusiano wa kidunia uharibu sana kuridhika kwetu?
19 Katika ulimwengu huu, hakuna kingine cho chote chenye imara yo yote. Kifo kinaweza kutuondolea watu wa ukoo wetu tuwapendao sana na rafiki zetu. Matukio yasiyotazamiwa au magonjwa huenda yakatuacha sisi au wapendwa wetu wakiwa hoi na wenye kulemaa. Mali zinaweza kuibwa au kuharibiwa. Hivyo, kufanya vitu vya kimwili, cheo au uhusiano wo wote wa kidunia uwe msingi halisi wa kuridhika kunaweza kutukatisha tumaini kwa njia yenye kusikitisha sana. Huenda kukatishwa tumaini huko kukamfanya mtu hata amlaumu Mungu na kuanza kuwaza kama Asafu: “Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa.” (Zab. 73:13) Kusipoangaliwa, kuwaza huko kunaweza kumfanya mtu aache kufuatia utawa.
20. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuridhika sikuzote?
20 Imetupasa nyakati zote tuendelee kujihadhari ulimwengu huu na nia zake, maoni yake ya kufuatia mali za kimwili na njia zake zisiharibu kuridhika kwetu. Ndiyo sababu ni vema kutumia wakati tukifikiria kwa kuthamini faida kubwa ambayo tumeipata tangu tulipoanza kufuatia utawa. Na tujisikie kama mtunga zaburi alivyojisikia kwa kupata uhusiano wenye kukubaliwa na Mungu: “Heri mtu yule umchaguaye, na kumkaribisha akae nyuani mwako. Na tushibe wema wa nyumba yako, patakatifu pa hekalu lako.” (Zab. 65:4) Ingekuwa ujinga kama nini kuacha mambo haya kwa sababu huenda jambo fulani likakosa kufanyika tunavyotaka sisi!
21, 22. (a) Ni faida gani za wakati ujao watakazozipata wale wanaofuatia utawa? (b) Tunaweza kufanya nini tusije tukapoteza faida hizi?
21 Kumbuka, pia, kwamba kufuatia utawa ‘kunayo ahadi ya uzima utakaokuwapo baadaye.’ (1 Tim. 4:8) Ndugu za Kristo waliotiwa mafuta ambao wangali duniani ‘hawamtumaini Kristo katika maisha haya tu.’ Thawabu nzuri sana ya kutawala pamoja naye katika mbingu kwa miaka elfu iko mbele yao. (1 Kor. 15:19, 50-54; Ufu. 20:6) “Mkutano mkubwa” unaoongezeka sikuzote wa watu wanaoshirikiana na watiwa mafuta hawa wanalo pia tumaini zuri sana. Wanatazamia “dhiki kubwa” inayokaribia, itakayoondoa wote wanaokataa ‘kumjua Mungu’ wakiwa watumishi wake waliokubaliwa katika dunia hii. Wale wanaotumikia Mungu kwa uaminifu pamoja na ndugu za kiroho wa Kristo wanaendelea kusisimkia tumaini la kuishi milele katika dunia iliyosafishwa, isiyo na maumivu, magonjwa wala uzee, ama kwa kufufuliwa kwa wafu ama kwa kuiokoka dhiki hiyo. Wakati huo “dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari,” si kumjua kwa akili tu, bali kumjua ili kutimiza mapenzi ya kimungu.—Isa. 11:9; 2 The. 1:6-10; Ufu. 7:9-17; 21:3-5.
22 Lo! ni baraka kubwa kama nini zilizomo akibani kwa wale wanaoendelea kufuatia utawa! Sisi tunaofuatia utawa na tusiruhusu cho chote kipunguze thamani isiyokadirika ya kujulikana kwetu na Mungu na Kristo kama watumishi wao waliokubaliwa. Na tuendelee kujihadhari na cho chote ambacho huenda kikatuondolea kuridhika. Sikuzote na tuweke mbele yetu mfano mwema sana Yesu Kristo. “Na tupige mbio kwa uvumilivu katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukitazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiliza imani yetu, ndiye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake alivumilia [mti wa mateso], na kuzarau haya, naye ameketi kwa mukono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu. Maana kumbukeni sana yeye aliyevumilia mabishano makubwa namuna hii ya wenye zambi yulu yake, kusudi musipate kuchoka wala kulegela katika nafsi zenu.”—Ebr. 12:1-3, Swahili Congo Bible.