Karibu Kwenye “Ujitoaji Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya
NI KICHWA kizuri kama nini tulicho nacho kwa mkusanyiko wa wilaya wa mwaka huu: “Ujitoaji Kimungu”! Na ni kielelezo kizuri kama nini cha ujitoaji kimungu ambacho Yesu Kristo alituwekea! Si ajabu kwamba mtume Paulo alivuviwa kuandika hivi kuhusu yeye: “Kweli kweli, siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu inakiriwa wazi kuwa kubwa: ‘Yeye alidhihirishwa katika mnofu, alitangazwa mwadilifu katika roho, aliwatokea malaika, alihubiriwa miongoni mwa mataifa, aliaminiwa katika ulimwengu, alipokewa juu katika utukufu.’”—1 Timotheo 3:16, NW.
Mkusanyiko wetu wa wilaya utatuimarisha tuwe watu wenye ujitoaji kimungu kweli kweli, kama alivyokuwa Yesu. Basi, kwanza kabisa, tunataka kuhakikisha kwamba haturuhusu kitu chochote kile kivuruge utwaaji wetu wa karamu hii ya kiroho. Kwa hiyo, acheni tuwe katika viti vyetu asubuhi ya Ijumaa saa 4:20 ili kufurahia mtokezo wa muziki na hivyo tuwe na hali inayofaa akilini ili kunufaika kikamili na programu itakayofuata. Kichwa kilichochaguliwa kwa siku ya kwanza ni “Kutumikia Mungu Anayesisitizia Ujitoaji Usiotia Ndani Wengine,” msingi wacho ukiwa ni Kutoka 20:5, NW. Hotuba ya mwenyekiti inafaa sana: “Karibuni, Nyinyi Watu Wenye Ujitoaji Kimungu!” Siku ya kwanza, tutajengwa kielimu pia na hotuba zinazoonyesha kwa nini Yehova husisitiza juu ya ujitoaji kimungu na kwa nini tunahitaji kujifunza siri ya ujitoaji kimungu. Kutakuwa pia na habari za kusisimua juu ya utambulishi wa Mungu wa kweli na ukweli wa Neno lake.
Kichwa cha Jumamosi ni “Ujitoaji Kimungu Humaanisha Pato Kubwa,” msingi wacho ukiwa ni 1 Timotheo 6:6, NW. Asubuhi, tutapokea maagizo juu ya mambo ambayo hasa huhitajiwa ili kufuatia ujitoaji kimungu. Na, bila shaka, kutakuwa na hotuba juu ya ubatizo kwa wale walio tayari kuingia mwendo wa maisha ya ujitoaji kimungu. Alasiri ya Jumamosi tutakaziwa uhitaji wa kuwa na ushikamanifu kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” halafu tutajifunza jinsi tunavyoweza kudhihirisha matendo ya ujitoaji kimungu katika mzingo wa jamaa. Kwa sababu ya matatizo ambayo vijana wetu wanakabili, kutakuwa na ujumbe wa pekee kwao.
“Kataa Katakata Kutoamini Mungu Uishi na Ujitoaji Kimungu,” kilichotolewa katika Tito 2:12, NW, ndicho kichwa cha Jumapili. Asubuhi, tutapokea maagizo fulani ya wakati unaofaa yakituonya dhidi ya “mtu wa kuasi” na dhidi ya kukengeuka katika mambo ya chakula na kinywaji, kujipamba, na tafrija. (2 Wathesalonike 2:3) Hiyo itafuatwa na drama ya ki-siku-hizi ikikazia umaana wa kujitiisha wenyewe kwa Mungu. Hotuba ya watu wote alasiri itatokeza habari njema kwamba ukombozi u karibu kwa watu wenye ujitoaji kimungu. Karamu yetu ya kiroho itamalizika kwa zungumzio linaloonyesha kwamba “Mazoezi Yetu Kuendelea Pamoja na Ujitoaji Kimungu Ni Yenye Manufaa.”
Kwa hiyo uje ukiwa tayari kuyafuata katika Biblia yako marejezo ya wanenaji na kuandika mawazo ya hotuba yaliyo ya kutokeza zaidi katika kitabu cha kuandikia habari. Kuandika habari ni msaada mkubwa wa kukaza fikira na kunufaika kikamili na yale ambayo mtu anasikia. Na tusisahau kamwe uhakika wa kwamba kazi nyingi inatakiwa kufanywa ili mkusanyiko uendelee vizuri na kwa ulaini na kwamba mikono mingi hurahisisha kazi. Kwa kujitolea kusaidia, tutapata ile furaha kubwa zaidi ya kutoa.—Matendo 20:35, NW.
Kwa hiyo ujitoaji kimungu wetu na utushurutishe tuje kwenye mkusanyiko huu na kutusukuma tufaidike kabisa nao. Na tuondoke hapo tukiwa tumeimarishwa na kuazimia kuendesha maisha za ujitoaji kimungu kwa ukamili kuliko wakati mwingine wowote.