Sababu ya Kuchagua Kumwabudu Yehova
1, 2. (a) Watu wanatumiaje maoni ya kwamba “Kuona ni kusadiki” kwa habari ya Mungu? (b) Watu kama hao wanakumbusha mtu juu ya mwanaanga gani wa Urusi ya Ukomunisti?
“KUONA ni kusadiki!” Hilo laonyesha maoni ya watu leo kwa Mungu wanaosadiki vitu vinavyoonekana tu. Kwa sababu hawawezi kumwona kwa macho matupu ya kibinadamu au kwa msaada wa darubini yenye nguvu kuliko zote zinazotumiwa leo, hawasadiki kwamba yeye yuko; hawawezi kujisadikisha wenyewe kwamba yeye yuko.
2 Watu hao watukumbusha juu ya mwanaanga wa pili ambaye Wakomunisti wa Kirusi walipeleka juu katika chombo cha angani azunguke dunia yetu. Kulingana na taarifa ya gazeti Associated Press la Mei 6, 1962, mwanajeshi huyu Mrusi “alitangaza kutosadiki kwake juu ya kuwako kwa Mungu leo. Alisema ‘hakumwona Mungu wala malaika’ wakati wa kuzunguka kwake dunia mara kumi na saba. . . . ‘Roketi ilitengenezwa na watu wetu. Mimi sisadiki Mungu yuko. Mimi nasadiki katika mwanadamu, nguvu zake, nafasi zake na akili yake.’”—New York Times la Mei 7, 1962.
3, 4. (a) Musa alikuwaje tofauti na mwanaanga huyo Mrusi? (b) Musa alitaka kuona nini juu ya Mungu, naye akaambiwa nini?
3 Si watu wote walio hivyo. Chukua kwa mfano, mwanadamu ambaye ni mwenye kujulikana zaidi kuliko wanaanga hao wa Kikomunisti na aliyewatendea wanadamu mema zaidi. Mwanadamu huyo alikuwa Musa mwana wa Amramu Mwebrania. Inashuhudiwa juu ya Musa huyu kwamba “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.” (Ebr. 11:27) Yeye hakukata tamaa na Mungu wake huyu asiyeonekana. Yeye hakuona haya kwa sababu ya imani yake katika Mungu huyu. Musa alipokwisha kuwatoa watu wake katika utumwa katika Misri na kwa mwujiza katika Bahari ya Shamu na kuwaongoza kwenye Mlima Sinai Uarabuni, na alipokwisha kuzipokea mbao mbili za Amri Kumi katikati ya tamasha yenye kutia woga katika mlima huo, Musa hakuwa na sababu ya kutosadiki kuwako kwa Mungu huyu asiyeonekana mwenye nguvu zote. Alilotaka lilikuwa ni kumjua vizuri zaidi, kuuona utukufu wa Mungu huyu asiyeonekana.
4 “Unionyeshe utukufu wako,” ndivyo Musa alivyoomba kupitia kwa malaika wa Mungu. Kwa ombi hili jibu la kimungu lilikuwa hivi: “Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la [Yehova] mbele yako.” Lakini sababu gani atoe ufunuo huu peke yake? Yehova Mungu alimweleza Musa hivi: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.”—Kut. 33:18-20.
5. Mungu alisema nini juu yake mwenyewe alipokuwa akilitangaza jina lake mbele ya Musa?
5 Si kitu hata mwanadamu aseme nini juu ya Mungu huyu wa Musa; jambo ambalo limepaswa liwe la maana kwetu ni yeye alijitangaza mwenyewe kuwa Mungu wa namna gani. Alilosema Mungu juu yake mwenyewe tunalisoma katika masimulizi ya Musa ya pindi hiyo, katika maneno haya: “[Yehova] akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, akalitangaza jina la [Yehova]. [Yehova] akapita mbele yake, akatangaza, [Yehova, Yehova], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wao, pia, hata kizazi cha tatu na cha nne.”—Kut. 34:4-7.
6, 7. (a) Ni zipi kati ya sifa hizo za kimungu zilizotajwa ambazo twahitaji zionyeshwe kwetu tukiwa katika hali yetu? (b) Kutokosa Kwake kutoa adhabu ya makosa kunatuhakikishia nini kwa habari ya kuendelea kwa uovu?
6 Je! huyo siye Mungu ambaye tungetaka, Mungu ambaye tungechagua tuabudu? Yeye ni Mungu “mwenye huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” Bila shaka sisi tukiwa katika hali yetu mbaya ya kibinadamu leo twahitaji sifa hizo za kimungu zionyeshwe kwetu. Walakini, yeye haachilii viumbe vyake vya kibinadamu wafanye kila jambo wakati wote bila adhabu inayostahili. Yeye ni Mungu “mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi,” lakini yeye hakubali mambo hayo mabaya naye hashindwi kuleta adhabu juu ya wale wanaozoea kwa makusudi mambo hayo na kuyafurahia.
7 Kwa sababu hiyo tunaweza kuwa na hakika na jambo hili moja: Ingawa amekuwa “si mwepesi wa hasira” na ameruhusu uovu na makosa kuwamo kati ya wanadamu kwa miaka hii elfu sita iliyopita, yeye hataruhusu uovu uendelee milele duniani. Yeye ‘hataihesabia kuwa haina hatia’ milele taratibu hii mbovu ya mambo ambayo chanzo cha uovu, Shetani Ibilisi, ndiye mungu wake. Kwa furaha yetu leo, muda wake wa kuruhusu uovu umefikia mwisho wake!
8. Uwezo wa Mungu kukomesha taratibu ya mambo ya ulimwenguni pote haupaswi utiliwe mashaka kwa sababu ya tukio gani la siku za Nuhu?
8 Uwezo wake mkamilifu wa kuikomesha taratibu hii nzima ya ulimwenguni pote ya mambo katika kizazi chetu wenyewe hauna haja ya kutiliwa shaka hata kidogo. Zaidi ya karne nane kabla ya kumtangazia nabii Musa jina lake, alitupa sisi mfano wa kweli wa uwezo wake mkamilifu wa kuharibu ulimwengu mzima wa watu. Hii ilikuwa katika siku za Nuhu babu ya Musa. Mwaka wa uharibifu huo wa ulimwengu waweza kuhesabiwa kama 2370 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Ulimwengu wa wanadamu leo si mkubwa mno na si wenye kutapakaa mno asiweze kuutia katika uharibifu wake uliotabiriwa wa taratibu hii ya mambo yenye kuzunguka dunia yote. Katika siku za Nuhu maji ya gharika yaliikumba dunia nzima.
9. Kwa hiyo, ni kitu gani anachoweza kufanya Mungu kama alivyofanya huko nyuma?
9 Wakati huo dunia nzima ilikuwa kama ilivyokuwa katika mwanzo wa “siku” ya kwanza ya uumbaji wakati Muumba aliposema: “Iwe nuru.” Uso wa dunia yote ulifunikwa na maji. (Mwa. 1:1-3) Wakati maji ya gharika yalipoenea dunia yote, safina kubwa mno iliyoundwa na Nuhu na jamaa yake peke yake ndiyo iliyokuwa ikielea salama juu ya maji hayo. Uhai wote wa kibinadamu duniani ulikufa, isipokuwa jamaa ya Nuhu katika safina. Walizama, kama vile Farao na magari yake na wapanda farasi waliofuatia Waebrania walioondoka wakiongozwa na Musa walivyozama katika Bahari ya Shamu. Alilofanya Mungu Yehova Mwenye Nguvu Zote wakati wa Gharika, aweza kulifanya leo: kuharibu taratibu ya ulimwenguni pote ya mambo ‘iliyojaa dhuluma.’—Mwa. 6:11 mpaka 7:23.
MUNGU WA TARATIBU MPYA YA MAMBO
10. Kwa sababu gani uharibifu wa taratibu iliyopo ya mambo hautaacha nafasi tupu duniani, na kwa hiyo, kwa sababu gani imetupasa tumwabudu Yehova?
10 Mwisho wa kuruhusu kwa Mungu uovu na kuharibu kwake taratibu hii ya kale ya mambo katika taabu ya ulimwengu isiyo na kifani hautaacha nafasi tupu katika dunia yetu. Yeye analo jambo bora atakaloliweka badala ya mambo ya zamani. Ni taratibu mpya ya mambo, ambayo katika hiyo uovu hautaruhusiwa. Muumba wa taratibu hii mpya yenye haki ndiye atakuwa vile vile Mungu wayo. Hiyo ni sababu inayofaa kwa nini imetupasa tuchague kumwabudu Yehova Muumba kama Mungu.
11. Kwa sababu gani Shetani hatakuwa mungu katika taratibu hiyo mpya ya mambo, nalo ni nini litakalowapata waabudu wake?
11 Wakati huo mungu wa taratibu hii mbovu ya mambo, Shetani Ibilisi, atakuwa ametoweka na miungu mingine yote ya uongo ambayo wanadamu wenye kusadiki vitu vinavyoonekana tu na wasio na imani wamekuwa wakiabudu mpaka sasa. “Yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani,” hatashindana na Mungu Mwenye Nguvu Zote. Yeye ataondolewa uwezo wake kama mungu na kuvurumishwa katika shimo refu pamoja na malaika zake wote wa kishetani. (Ufu. 20:1-3) Wale wanaochagua kumwabudu kama mungu wao wataangamia pamoja na taratibu hii ya mambo yenye kutawaliwa na Ibilisi katika taabu iliyo kubwa kuliko zote ambayo sasa inaukaribia sana ulimwengu.
12. Tofauti na ile ambayo Shetani aliwapa wanadamu, ni serikali ya namna gani ya dunia nzima ambayo Yehova atawapa wanadamu, nayo itakuwa mikononi mwa nani?
12 Shetani Ibilisi, “mungu wa taratibu hii ya mambo,” aliwapa watu serikali ya siasa ya ulimwenguni pote iliyofananishwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia na “mnyama” mwenye vichwa saba na pembe kumi. Chini ya uongozi wa Kishetani alitoka katika “bahari” ya wanadamu waliotengwa na Mungu. (Ufu. 13:1-8) Tofauti na hilo, Yehova kama Mungu wa taratibu mpya ya mambo yenye haki atawapa wanadamu serikali ya dunia yote iliyo bora kuliko ile ya wanaume na wanawake wasiokamilika, wenye kuonea na wenye kujitafutia faida zao wenyewe. Itakuwa serikali ya kimbinguni, ikiwa mikononi mwa Bwana aliyefundisha wanafunzi wake kusali: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:9, 10; Luka 11:2) Mwalimu wa sala hiyo alikuwa Yesu Kristo. Yeye alikuwa Mwana wa Mungu ambaye Yehova alituma katika dunia miaka mia kumi na tisa iliyopita awe mzao wa kimwili wa Mfalme Daudi na kwa njia hiyo awe mrithi wa milele wa ufalme udumuo daima uliopaswa uendelee katika ukoo wa kifalme wa Daudi. Katika njia hii akawa Masihi aliyeahidiwa.—Yohana 1:40-49.
13. Yesu aliyetiwa mafuta alishawishwa kwa kishawishi gani aingie katika ibada mbaya na katika siasa za ulimwengu huu?
13 Kama Mrithi wa ufalme huu wa Kimasihi aliyetiwa mafuta, sababu gani Yesu Kristo ajitie mwenyewe katika siasa chafu za ulimwengu huu? Yeye hakuwa akitumaini kupata ufalme au milki ya ulimwengu kutoka kwa “mungu wa taratibu hii ya mambo.” Alipokuwa amekwisha kutiwa mafuta kwa roho ya Mungu awe Mfalme Aliyekusudiwa wa serikali ya Kimasihi, alifikiwa na “mungu wa taratibu hii ya mambo” amshawishi ili aingie katika ibada ya uongo na katika siasa za ulimwengu huu uliohukumiwa. Akitokeza kwa ushupavu ulizo la ibada, Mshawishi alimwonyesha Yesu “milki zote za ulimwengu kwa dakika moja” akasema: “Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo. Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako.” Sasa, ni nani ambaye Yesu angechagua kuabudu?
14, 15. Yesu alitiwa mafuta kama Mfalme Aliyekusudiwa kwa serikali gani, na kwa sababu gani akakataa kumwabudu Shetani ili apate milki zote za ulimwengu?
14 Yesu hakufanya kama “mnyama” mwenye vichwa saba na pembe kumi aliyetoka katika bahari, yaani, akubali uwezo wa kisiasa na kiti cha enzi kionekanacho na mamlaka kuu kutoka kwa joka jekundu, Shetani Ibilisi. (Ufu. 13:1, 2) Alikuwa amekwisha kutiwa mafuta ili atawale ufalme wa Kimasihi kwa sababu alimwabudu Yehova kama Mungu. Kama ilivyosemwa kwa kumtabiria Yesu Kristo: “Umependa haki, umechukia maasi; kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, mafuta ya shangwe kupita wenzio.” (Ebr. 1:9; Zab. 45:7) Yesu hangesujudu hata kidogo amwabudu “mungu wa taratibu hii ya mambo,” hata kwa kusudi la kupata “milki zote za ulimwengu.” Akiwa amezaliwa kama mwanadamu chini ya agano la Torati lililokuwa limepatanishwa na Musa katika Mlima Sinai, mara hiyo Yesu alitumia maneno ya Musa katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati na kusema hivi kwa Shetani Ibilisi:
15 “Imeandikwa, Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”—Luka 4:5-8; Kum. 6:13; 10:20.
16. Badala ya kugombea serikali ya kisiasa duniani, Yesu aliendelea kuhubiri ujumbe gani, na kwa sababu gani?
16 Yesu Kristo aliendelea kumkubali Mungu wa taratibu mpya ya mambo yenye haki kwa uthabiti. Huko kulimaanisha kwa Yesu kushikamana kwa uaminifu na ufalme wa Kimasihi uliotokana na mkono wa Mungu huyu, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. Kwa hiyo, yeye hakugombea ufalme wo wote wa kisiasa wa dunia inayokaliwa na watu, bali yeye aliendelea kuuhubiri ujumbe ambao mtangulizi wake, Yohana Mbatizaji, alikuwa ametangazia Israeli wote: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17) Ili awe Masihi wa kimbinguni, Yesu alipaswa atoe uhai wake kwa kujitoa kabisa kwa ufalme huo wa mbingu, ufalme wa Mungu.
17. Yesu alimtoleaje Pontio Pilato ushuhuda akiunga mkono ufalme wa Mungu?
17 Alipoulizwa na Pontio Pilato, gavana wa Kirumi wa Jimbo la Uyahudi, kama yeye alikuwa mfalme aliyetaka kuipindua milki ya Kaisari, Yesu alijibu hivi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” (Yohana 18:36) Hivyo Yesu alimtolea Pilato ushuhuda akiunga mkono ufalme wa Mungu.
HUU NDIO WAKATI WA KUCHAGUA!
18. Yesu alitimiza kazi gani katika historia ya kibinadamu, naye alihakikishaje kwamba anaamini Mungu na kumwabudu?
18 Yesu Kristo huyu ni mtu halisi. Hawezi kusukumiwa mbali na Wayahudi wasioamini na Mataifa kama mtu tu asiyekuwako au wa kuwazia tu. Kuna ushuhuda wa kuwa alikuwako hapa duniani karne kumi na tisa zilizopita unaozidi ushuhuda ulioko wa wanadamu wengine wo wote wanaotajwa katika historia. Kuja kwake kulionyesha badiliko katika historia ya kibinadamu, si katika shauri la dini tu bali pia katika shauri la serikali ya ulimwengu kwa ajili ya wanadamu, ufalme wa Mungu. Alikuja duniani katika wakati uliowekwa na Mungu, wakati ulioonyeshwa mapema katika Biblia Takatifu. Kulikuwa hakuna shaka kwa Yesu Kristo juu ya kama Mungu alikuwako au hakuwako. Yeye alitoka kwa Mungu. Alikuwa amemwona, akasema naye, akafanya kazi naye. Yeye hakuwa mwongo alipoelekeza kwenye mambo haya ya hakika ya maisha yake mbinguni kabla ya kuwa binadamu. Ijapokuwa alipokuwa duniani kama mwanadamu mwenye macho ya kibinadamu tu hakuweza kumwona Yehova Mungu, yeye aliendelea kumwamini na kumwabudu. Kazi za Yesu duniani, zilizoshuhudiwa na mashahidi wengi waaminifu, zilithibitisha kwamba yeye alimwamini Mungu na kwamba Mungu alikuwa pamoja naye.—Matendo 10:38.
19. Kwa habari ya kuamini kwamba kuna Mungu, ni ulizo gani linalotokea juu ya mtu ambaye mfano wake tutafuata?
19 Yesu alimjua Yehova Mungu Baba yake zaidi kuliko mashetani wasioonekana. Hata hivyo mashetani wanaamini kwamba kuna Mungu. Huenda wanadamu wasioamini wakadhihaki hili kulingana na hekima ya kilimwengu, lakini ndugu wa kidunia mzazi mmoja na Yesu Kristo jina lake Yakobo aliwaambia wale waliojidai kuwa wanafunzi wa Kristo hivi: “Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka.” (Yak. 2:19) Kulingana na hayo, mashetani wenye kupita uwezo wa kibinadamu wanafanya afadhali kuliko umati mkubwa wa wanaume na wanawake wasiomwamini Yehova Mungu hata kidogo. Katika jambo hili, ni mfano wa nani ambao sisi tutakuwa salama tukiufuata? Ni ule wa wanaume na wanawake wasioamini? Au ni ule wa mashetani wanaoamini lakini wasifanye zaidi kuliko kutetemeka tu? Au ni ule wa Yesu Kristo ambaye maisha yake mwenyewe duniani yanashuhudiwa na vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu?
20. Ni nani waliokuwa afadhali—wale wasiomwamini Mungu na wasiofanya kazi zinazofaa, au Yesu aliyeamini na akahakikisha imani yake? Kwa njia gani?
20 Yesu Kristo aliamini; lakini, zaidi ya hayo, alitenda mambo kuthibitisha imani yake. Je! alifanya vibaya zaidi kuliko wanaume na wanawake wasioamini au kuliko mashetani? Ni maisha ya imani na kazi za nani ambazo zimewafaidi wanadamu zaidi katika historia ya kibinadamu, hata sasa, licha ya wakati ujao? Jibu la kweli kwa maulizo hayo litapaswa limtaje Yesu Kristo kama mmoja aliyefanya vizuri zaidi na kuleta faida zaidi. Yeye yuko aliko leo kwa sababu ya maisha yenye imani na kazi alizofanya duniani mpaka kifo cha imani kwa kuunga mkono kwa uaminifu ufalme wa Mungu. Leo yeye yuna cheo cha juu zaidi katika mbingu yote na dunia isipokuwa anapitwa na cheo cha Baba yake wa kimbinguni tu, Yehova Mungu mwenyewe. (Flp. 2:5-11; 1 Pet. 3:21, 22) Na kama kusingekuwako Mungu na kama Yehova hangekuwa Mungu, Mungu awezaye kufufua wafu kwenye uzima wa kimbinguni, yeye hangekuwa katika cheo hicho kilichopandishwa sana leo.—Efe. 1:19-22.
21. Basi, wale wanaotamani sana uzima wa milele watafuata mfano wa nani?
21 Bila nafasi ya kupingana kwa kufaulu, maisha ya imani na kazi yalimtendea mema zaidi, hata kupita cho chote ambacho ye yote na viumbe vingine vyote katika ulimwengu vyaweza kutumaini kujifurahisha. Mfano wake ndio watu wote wenye akili wanaotamani sana uzima wa milele katika ukamilifu wa furaha, wanapaswa wafuate. Kufuata mfano wake kunafaa, wala si jambo la kuwazika tu. Alimfanya Yehova awe Mungu wake na akamwabudu, hata aliposhawishwa na Shetani mtawala wa mashetani.
22. Basi, Yehova ni nani, na sababu mbili za maana sana kwetu kumwabudu yeye ni nini?
22 Katika kujibu ulizo hili, “‘Yehova ni nani,’ hata wote wamwabudu yeye?” twaweza kusema kwa kweli hivi: Yehova ndiye Mungu wa Bwana Yesu Kristo, na uhakika huo peke yake ni sababu ya maana sana kwa nini wote wamepaswa wamwabudu Yehova kama Mungu. Wote wale wanaotamani uzima wa milele katika taratibu mpya ya mambo yenye haki ya Mungu itawapasa waufuate mfano wa Yesu Kristo, Yeye aliye Mkuu kuliko wote katika kuumba kote kwa Mungu. Pia, uhakika wenyewe wa kwamba Yehova ameweka ufalme wa Kimasihi mikononi mwa Yesu Kristo walifanya liwe jambo la haraka kwamba wote wamwabudu Yehova Mungu.
23. Kwa sababu gani wale wanaokana kwamba Mungu hayuko hawawezi kuepuka wasiwe na daraka kwake, nao watu hawa wasioamini wanatendaje?
23 Wanaume na wanawake leo wanadhani kwamba wanaweza kuepuka daraka kwa Yehova kwa kutoamini na kukana kwamba yeye hayuko na si Mungu. Lakini kuepuka kwao daraka kwa Yeye wasiyeweza kumwona ni kuwazia-wazia kutupu upande wao. Mfalme Daudi, babu wa kale wa Yesu Kristo, alisema, katika Zaburi kumi na nne, mstari wa kwanza na wa pili hivi: “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, hakuna atendaye mema, Toka mbinguni [Yehova] aliwachungulia wanadamu, aone kama yuko mtu mwenye akili, amtafutaye Mungu.” Hata katika wakati wake, Mfalme Daudi aliona kwamba wale waliokana kuwako kwa Yehova walitenda kwa kuharibu. Yehova Mungu katika mbingu anawachungulia. Anawacheka, akijua vema kwamba ni mateka ya sheria zake na hawawezi kuepuka kutimizwa kwa sheria hizo. Kupuza na kukana kwao sheria hizo kutawadhuru tu.
24. Kwa sababu gani ulizo lililo kubwa kuliko yote leo halihusu dini tu, na tendo la Farao kwa Musa linafananaje na lile la wanasiasa leo?
24 Ulizo lililo kubwa kuliko yote mbele ya ulimwengu wote leo si dini tu. Ni serikali vile vile. Inafaa tukumbuke kwamba alikuwa mwanasiasa mkuu wa siku hizo aliyeuliza ulizo hili mbele ya nabii Musa: “[Yehova] ni nani, hata niisikilize sauti yake?” (Kut. 5:2) Katika kuuliza ulizo hilo Farao huyo wa Misri hakuwa akimkaidi Mungu wa dini safi tu, bali vile vile Gavana, Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Vile vile, wakati huo Yehova alikuwa karibu kusimamisha ufalme wake juu ya taifa la Israeli. Ndivyo walivyo na wanasiasa wa leo na wanaowaunga mkono. Hawashughuliki na shauri la kidini tu katika kutilia shaka kuwako kwa Yehova na uwezo wake kama Mungu. Wanashughulika na serikali vile vile. Leo wanashughulika na enzi kuu ya Mungu kama inavyowakilishwa na serikali yake ya Kimasihi, ufalme wa Mungu. Ni serikali halisi na ni ya juu zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko yao wenyewe.
25. (a) Serikali hiyo ya Kimasihi imehubiriwa kwa mataifa na nani na tangu wakati gani? (b) Baada ya mataifa kupewa taarifa hiyo, serikali hiyo itaagizwa ifanye nini, na hii itakuwa na matokeo gani juu ya wanasiasa?
25 Hasa tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1918, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamekuwa wakitangaza serikali hiyo, ufalme huo wa kimbinguni wa Mungu mikononi mwa Kristo wake. Hivyo kwa hii miaka 56 iliyopita ufalme huo wa Kimasihi ndio umekuwa ukihubiriwa peke yake hasa. (Mt. 24:14; Marko 13:10) Karibuni, utaacha kuhubiriwa kwa mataifa yote ya kisiasa kuwa ushuhuda kwao. Lakini, ili kutenda kulingana na taarifa hiyo inayotangulia kutolewa kwa mataifa hayo, ufalme wa Kimasihi wa Yehova utaamriwa uchukue hatua. Hatua hiyo itahakikisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa unabii wa kweli, Mwongozi wa unabii wa Biblia ulio wa kweli na usio na makosa. Ufalme huo wa Kimasihi utatoa uhakikisho huo kwa kutimiza unabii huo. Ndipo wanasiasa hao wakaidi watakapojifunza kujua Yehova ni nani na linalowapata wale wanaokataa kwa kiburi kumwabudu Yeye. Hatua hiyo ya Ufalme haitawageuza kwenye ibada ya Yehova bali itawaharibu.—Dan. 2:44.
26. (a) Zaidi ya kuharibu waendeshaji waonekanao wa taratibu hii ya mambo, Ufalme utamfanyia nini mungu wa taratibu yenyewe? (b) Raia za kisasa za dunia za Ufalme wataingizwa katika nini, na kwa njia gani?
26 Ufalme huo wa Kimasihi utafanya zaidi kuliko kuwaharibu waendeshaji waonekanao wa hii taratibu mbovu ya mambo. Utamtia katika shimo refu mwenye kuendesha taratibu hii ya sasa ya mambo, asiyeonekana lakini aliye halisi, yaani, “mungu wa taratibu hii ya mambo,” Shetani Ibilisi, pamoja na mashetani wake. (Ufu. 20:1-3) Ufalme wa Kimasihi utahifadhi kwa usalama mabaki ya mwisho ya washiriki wa warithi wenzi wa Kristo 144,000 na vile vile “mkutano mkubwa” wa raia za kisasa za kidunia za ufalme huo wa kimbinguni katika “dhiki ile iliyo kuu” isiyo na kifani iliyoko mbele ya wanadamu sasa hivi. (2 Pet. 3:11-15; Ufu. 7:9-17) Waokokaji hawa duniani wa “dhiki ile iliyo kuu” wataingizwa na Ufalme huo katika taratibu mpya ya mambo iliyoahidiwa ambayo katika hiyo Yehova atakuwa Mungu na Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote.
27. Kulingana na Ufunuo 21:3-5, taratibu mpya pamoja na Mungu wake itawafanyia nini wakaaji wa dunia?
27 Je! hii itawafanyia tofauti wakaaji wote wa kidunia wa taratibu pamoja na Yehova kama Mungu? Hakuna jibu bora kwa ulizo hili liwezalo kupewa kuliko lile lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu katika Ufunuo 21:3-5: “[Mimi mtume Yohana] nikasikia sauti kubwa katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita. Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”
28. Kwa kujibu ulizo hili, “‘Yehova ni nani,’ hata wote wamwabudu yeye?” sisi tutasema nini?
28 Hivyo, basi, “‘Yehova ni nani,’ hata wote wamwabudu yeye?” Sikiliza, ewe Farao wa Misri ya kale! Sikiliza, ewe mtu wa leo unayesadiki vitu vinavyoonekana tu! Yehova ndiye Mungu ambaye ni wa “tangu milele hata milele” anayestahili ibada yote. (Zab. 90:2) Yeye ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Yeye ni Muumba wetu, na Chanzo cha ufalme wa Kimasihi ambao kupitia kwa huo jamaa zote za dunia, walio hai na waliokufa, watabarikiwa.—Mwa. 12:3; 22:18.
29. Ikiwa tunaamini hivyo kweli, tutaitikia kutia moyo gani kwa mtunga zaburi?
29 Je! twasadiki hayo? Je! sisi tunaojibu Ndiyo tutaonyesha imani yetu kwa kazi zinazofaa? Ikiwa ndivyo, basi kwa furaha tutaitikia kutia moyo kwa mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu hivi: “Njoni, tuabudu mbele za [Yehova] aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, na sisi tu watu wa malisho yake, na kondoo za mkono wake.”—Zab. 95:6, 7.
—Kutoka The Watchtower, Apr. 15, 1975.
[Blabu katika ukurasa wa 466]
‘Yehova, Yehova, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli . . . Je! huyo siye Mungu ambaye tungetaka kuwa naye?’
[Blabu katika ukurasa wa 470]
“Yehova ndiye Mungu wa Bwana Yesu Kristo, na uhakika huo peke yake ni sababu ya maana sana kwa nini wote wamepaswa wamwabudu Yehova kama Mungu.”
[Blabu katika ukurasa wa 471]
‘Wanapotilia mashaka kuwako kwa Yehova, wanasiasa wa leo na wanaowaunga mkono wanashughulika na ufalme wa Mungu. Ni serikali halisi na ni ya juu zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko yao wenyewe.’
[Picha katika ukurasa wa 468]
Yesu Kristo alikataa asiwe kibaraka wa Shetani Ibilisi kwa kutokuwa sehemu ya taratibu ya kisiasa ya ulimwengu