Wewe Unahusikaje kwa Kutojua “Siku Ile na Saa Ile”?
1. Sifa kuu ya Mungu inahusianaje na kutofunua kwake “siku ile na saa ile” ya kuanza kwa “dhiki kubwa”?
YEHOVA MUNGU amekuwa na kusudi kwa kutofunua “siku ile na saa ile” ya kuanza kwa “dhiki kubwa” kuvunja-vunja taratibu iliyopo ya mambo. Kusudi hilo linashikamana sana na sifa kuu ya Mungu—upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye upendo, anataka wale tu wanaompenda kweli kweli ndio wawe watumishi wake. (Zab. 119:97; 1 Yohana 5:3) Yeye hataki viumbe vyake vyenye akili vijikunje mbele zake kwa hofu, vikimtumikia kwa sababu tu anaweza kuviadhibu. Matendo yake kwa watu yamefanya wampende na wakati uo huo yakawaruhusu waonyeshe yaliyomo mioyoni mwao hasa.
2. Yehova ameonyeshaje upendo wake kwa wanadamu
2 Kwa kuonyesha fadhili kuu zisizostahilika, Yehova amewaruhusu hata wanadamu wasio na shukrani na wasiothamini mambo wafaidike kutokana na maumbile yake aliyofanyiza kuwezesha kuwe na uhai duniani. (Matendo 14:16, 17; 17:24, 25) Halafu tena, aliongoza karibu wanaume 40 kwa kipindi cha zaidi ya karne kumi na sita wafanye maandishi yanayomjulisha yeye ni Mungu wa namna gani hasa na anataka nini kwa wale anaowakubali. (2 Tim. 3:16, 17) Maandishi hayo yaliyomo katika Biblia yanatoa mambo ya kutuongoza yanayotuwezesha tupate yaliyo bora maishani hata sasa kujapokuwa kuna magumu na hali zenye kutatiza. (Zab. 19:7-11) Yanatufahamisha pia upendo mwingi sana ambao Mungu alionyesha alipomtoa Mwanawe mzaliwa wa pekee atoe uhai wake kwa ajili yetu. Hii ilitolea wanadamu nafasi ya kupata uhusiano wenye kukubaliwa na Mungu wa pekee aliye wa kweli na kuwawezesha wawe na tumaini la uzima usio na magonjwa, udhaifu wa uzee, na mauti.—Yohana 3:16; Tito 3:4-7; Ufu. 21:3, 4.
3. Kwa sababu gani kuleta kwa Yehova “dhiki kubwa” kunapatana na kuwa kwake Mungu mwenye upendo?
3 Lakini yawezekanaje kwamba Mungu wa namna hiyo ataleta pia dhiki ambayo uharibifu wake kwa wanadamu utaogofya sana? Kwa kweli, kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye upendo lazima afanye hivyo. Huenda hii ikasikika kama ajabu kwa watu wengi leo. Karibu karne 27 zilizopita, ilisikika kama ajabu pia kwa Waisraeli wengi wakati nabii Mika Mwebrania alipotangaza kwamba Yehova angeleta msiba juu ya ufalme wa Israeli wa makabila kumi na juu ya ufalme wa Yuda wa makabila mawili. Kwa kutoamini wakauliza hivi, “Roho ya [Yehova] imepunguzwa? Je! haya ni matendo yake?” Yehova alijibu hivi, “Je! maneno yangu hayamfai yeye aendaye kwa unyofu?” (Mik. 2:7) Ndiyo, kuwafaa wale wanaotembea kwa unyofu kunataka achukue hatua juu ya wote wanaokataa kwa ushupavu kujipatanisha na njia zake za haki na ambao kwa njia hiyo wanashiriki kuleta udhalimu, uonezi na uasi unaofanya maisha duniani leo yawe yenye hatari zaidi na ya kuchukiza zaidi.
4. Yehova anataka nini juu ya wanadamu wote?
4 Hata hivyo, kabla ya kuja kwa “siku ile na saa ile” yake kuchukua hatua juu ya uovu, Yehova anaomba wote kwa uchangamfu waziache njia zao mbaya. (Linganisha Isaya 55:6, 7; Yeremia 18:7-10.) Yeye ni kama baba wa kibinadamu mwenye upendo asiyefurahia kuadhibu watoto wasiotii bali afurahiaye kufanya kwao yanayofaa. Kwa habari ya vile Yehova alivyoona juu ya uharibifu wa kuogofya alioruhusu uupate Yerusalemu mwaka wa 607 B.C.E., Biblia inasema hivi: “Moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu. Wala kuwahuzunisha.” (Omb. 3:33) Yeye anapendelea watu wafuatie njia ya maisha inayofanya isiwe lazima kwake kuwachukulia hatua na inayowaletea wao wenyewe furaha na uradhi, na kuletea wanadamu wenzao usalama na furaha. Mtume Petro aliandika hivi, “Hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”—2 Pet. 3:9.
5. (a) Kutofunua kwa Yehova “siku ile na saa ile” kunafanya watu mmoja mmoja waonyeshe nini juu yao wenyewe? (b) Kutojulishwa na Mungu “siku ile na saa ile” kunasaidiaje watu wanyofu watambue Wakristo wa kweli?
5 Uhakika wa kwamba Yehova Mungu hakujulisha “siku ile na saa ile” atakapomtuma Mwanawe akafikilize hukumu juu ya taratibu mbovu ya mambo katika dunia hii bila shaka umesaidia kuonyesha wazi yaliyomo mioyoni mwa watu. Ikiwa wao hawampendi Muumba wao kweli na kuthamini ubora wa uhusiano mwema naye, watafuatia mambo ambayo mioyo yao inaelekea—wingi wa mali za kimwili, kupendwa na kujulikana sana na ulimwengu, kuwa na maisha ya kujifikiria wenyewe na kujitafutia faida zao wenyewe tu. Huenda wakaelekea kufikiri kwamba, kwa kuwa Mungu hakutuambia “siku ile na saa ile,” pengine haitatukia katika siku zetu. Wakati ule ule wale wanaotaka kufanya mapenzi ya Mungu wamefaidika kwa kutojulishwa naye “siku ile na saa ile.” Kwa njia gani? Basi, kwa kutofanya hivyo Yehova Mungu anazuia wale wanaojifanya tu kuwa watumishi wake wasijionyeshe sana kuwa wanamcha yeye kwa njia ya unafiki kabla tu ya “siku ile na saa ile” yake. Kwa hiyo watu wanyofu hawakosi kuwafahamu walio watu waaminifu wa Mungu. Wanaweza kwa wazi kuona tofauti kati ya wale wanaopuza “siku ile na saa ile” ya Mungu ya hukumu na wale wasiofanya hivyo.
KUPUZA “SIKU ILE NA SAA ILE” NI HATARI
6. Watu wengi leo wanaonyesha nia gani inayotajwa katika 2 Petro 3:3-7?
6 Wakati ushuhuda wa Maandiko juu ya kukaribia kwa “dhiki kubwa” unapokazwa katika akili za watu wengi, wao wanaupuza na kuudhihaki. Matendo yao yanapatana na masimulizi ya Biblia: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.” Kwa watu hao kufikilizwa kwa hukumu ya Mungu zamani, kama vile gharika ya siku za Nuhu, ni upuzi tu. Hawataki hata kidogo kuamini kwamba Mungu atawaharibu waovu, kama alivyofanya zamani. Hawataki kubadili njia yao ya maisha bali wanataka kuendelea kutosheleza tamaa zao wenyewe. (2 Pet. 3:3-7) Wakiendelea kuwa na nia hii kisha “siku ile na saa ile” ya Mungu iwafikilie ghafula, hawataokoka msiba hata kidogo.
7. Kukosa kuiona kwa uzito “siku ile na saa ile” inayokuja ya kufikiliza hukumu kunaweza kuhusuje hata wengine wanaoshirikiana na kundi la Kikristo?
7 Kudharau “siku ile na saa ile” inayokuja ya Yehova ya kufikiliza hukumu yake kunaweza kuambukia hata wale wanaoshirikiana na kundi la kweli la Kikristo leo. Mtu aweza kuwa anajua vile Biblia inavyosema juu ya “dhiki kubwa.” Huenda akawa amesikia habari zake kwa miaka mingi, pengine hata kwa wazazi Wakristo walio wakf. Lakini kwa kuwa haoni jambo lo lote la ajabu likitukia, huenda akaanza kuchelewesha “siku ile na saa ile” ya Mungu akidhani itakuja wakati ujao ulio mbali. Huenda akawa anafurahia ushirika wenye kufaa wa waliomo kundini, lakini yeye mwenyewe hashiriki pamoja nao kufanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ambayo Kristo aliagiza wafuasi wake waifanye. Huenda ikaelekea kwake kwamba ulimwengu unatoa faida za kimwili zenye kuvutia sana. Karibuni huenda akajikuta akifuatia faida za kimwili au huenda akaacha kufanya jitihada zaidi aache njia na tabia zinazomzuia asiwe na uhusiano wenye kukubaliwa na Yehova Mungu. Huenda hata akawaza kwamba ‘mambo yatakapoanza kuchacha kweli kweli, atafanya mabadiliko katika maisha yake. Lakini sasa hayuko tayari kufanya hivyo. Mtu wa namna hiyo hathamini haki ya matakwa ya Mungu naye yumo katika hatari kuu.
8. Kula na kunywa kupita kiasi kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya nia ya mtu kuhusu “dhiki kubwa”?
8 Wengi wanaacha mambo ya kupita kiasi yawapumbaze wasiuone uhakika wa kuja kwa “dhiki kubwa.” Yesu Kristo aliamsha wanafunzi wake waione hatari hiyo, akisema hivi: “Jiangalieni ili mioyo yenu isije ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha, na kwa ghafula siku ile iwafyatukie kama mtego.” (Luka 21:34, 35, NW) Kwa wazi, kula na kunywa kupita kiasi kunapumbaza na ‘kulemea’ moyo kwa kuufanya ujione wenye hatia. Vile vile mambo hayo ya kupita kiasi yanaondoa makusudi mema.—Mit. 20:1; linganisha Isaya 28:7.
9. Ni kwa njia gani kuhangaikia utafutaji wa riziki kunaweza kuleta hatari?
9 Vivyo hivyo, kuhangaikia isivyofaa utafutaji wa riziki kunaweza kuulemea moyo. Kama mtu angejiacha asahau uhakikisho wenye kufariji kwamba Yehova Mungu ataangalia watu wake, moyo wa mtu huyo karibuni ungemvuta afanye kila jambo awezalo ahakikishe yuko salama kwa upande wa pesa za kutumia wakati ujao. (Ebr. 13:5, 6) Baadaye utafutaji wa faida za kiroho ungesukumiwa mbali, na kumwacha mtu huyo amefilisikiwa kiroho na akiwa katika hali isiyokubaliwa na Yehova Mungu.—1 Tim. 6:9, 10.
KUISHI KUPATANA NA IMANI
10. Imetupasa tujaribu kuishije kila siku, na kwa sababu gani?
10 Ni afadhali zaidi kuishi kila siku kwa kutambua uhakika wa kwamba wakati wa Yehova wa kufikiliza hukumu unakuja. Si kwamba tu hii itamzuia mtu asinaswe katika hali isiyokubaliwa na Mungu wakati “siku ile na saa ile” yake itakapokuja, bali pia itafanya maisha yake yawe yenye kufurahisha zaidi hata sasa. (1 Tim. 4:8) Hii ndivyo ilivyo kwa sababu msingi wa amri za Mungu ni upendo nazo zinaendeleza mema. (Rum. 13:8-10) Kuzitii kunazuia mtu asifuatie mwendo wenye kudhuru akili, mwili au moyo.—Mit. 4:1-15; Mhu. 11:9, 10.
11. Ni nini kilichowezesha wanaume na wanawake wa zamani kutumia maisha yao yote kufanya mapenzi ya Mungu hata ingawa walijua mwisho wa taratibu usingekuja katika muda wa maisha yao?
11 Zamani kabla ya karne ya 20 walikuwako watu walioishi kwa njia iliyoonyesha waliamini kusudi la Mungu kukomesha uovu wote na kusimamia mambo ya dunia kwa haki. Walijua kwamba hii isingetokea katika muda wa maisha yao. Hata hivyo, tumaini la kushiriki katika alilokusudia Mungu kwao wakiisha kufufuliwa kwa wafu lilikuwa lenye nguvu sana hata wakatumia maisha yao yote kufanya mapenzi yake.—Linganisha Waebrania 11:35-40.
12. Ibrahimu na Sara walionyeshaje imani yao katika kutimizwa kwa ahadi ya Mungu?
12 Fikiria mfano wa Ibrahimu na Sara. Walikuwa wakaaji wa mji wenye maendeleo wa Uru. Lakini Ibrahimu aliondoka katika mji wa kwao kwenda nchi asiyojua lo lote juu yake, alipoombwa na Mungu afanye hivyo. (Mwa. 12:1-4) Mke wake Sara alishirikiana naye kabisa katika jambo hili. Walipoingia mwishowe katika nchi ambayo Mungu alikuwa amewaelekeza, Ibrahimu na Sara hawakujifanya wenyeji wa mji wo wote wala kukaa katika nyumba ya starehe. Wao na wazao wao waaminifu waliendelea kukaa katika hema. Kwa kuwa hakuna jambo lililowazuia wasirudie maisha yenye starehe zaidi katika Uru, sababu gani hawakufanya hivyo? Biblia inajibu hivi: “Ingawa hawakupata utimizo wa ahadi hizo, . . . waliziona kwa mbali wakazikaribisha na kutangaza waziwazi kwamba wao walikuwa wageni na wakaaji wa muda katika nchi. Kwa maana wale wanaosema mambo hayo wanatoa ushuhuda wa kwamba wanatafuta kwa bidii mahali pao wenyewe. Na hali, kama wao kweli wangaliendelea kupakumbuka mahali hapo walipotoka, wangalipata nafasi ya kurudi. Lakini sasa wanafikilia mahali bora, yaani, pa mbinguni.”—Ebr. 11:13-16, NW.
13, 14. Ni nini kinachoonyesha kwamba Ibrahimu na Sara walikuwa wenye hekima kutoacha kuhangaikia mali za kimwili isivyofaa kuongoze mwendo wao wa maisha?
13 Je! wewe unaona kwamba Ibrahimu na Sara walifanya uchaguzi wa hekima? Maisha yao yalikuwa ya kuridhisha kweli kweli. (Mwa. 25:8) Ibrahimu na Sara walipokea thawabu nyingi kwa mwendo wao wa kutenda. Yehova alizibariki jitihada za Ibrahimu kuruzuku jamaa yake, hata hakukosa cho chote bali sikuzote alikuwa na vitu tele. (Mwa. 13:2; 14:14) Ibrahimu alifurahia uhusiano wa karibu sana na Mungu, hata akapendelewa kusema na malaika na kuwapokea. (Mwa. 18:1–19:1) Yeye na mke wake pia alirudishiwa kwa mwujiza nguvu zake za uzazi, akaweza kuzaa Isaka kupitia kwa mkewe mpendwa Sara. Na kupitia kwa ukoo wake Mwana wa Mungu mwenyewe akazaliwa kama mwanadamu. (Mwa. 17:17; Ebr. 11:11, 12; Luka 3:23-34) Kwa habari ya ulinzi na uangalizi wa Mungu juu ya Ibrahimu na wazao wake waaminifu, Zaburi 105:14, 15 inasema hivi: “Hakumwacha mtu awaonee, hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, wala msiwadhuru nabii zangu.”—Mwa. 12:17; 20:3, 7.
14 Kama Ibrahimu asingaliuitikia mwito wa Mungu aondoke Uru, angalikosa nafasi za ajabu. Asingalikuwa tofauti na mkaaji mwingine ye yote wa Uru mwenye ufanisi ambaye jina lake lilisahauliwa zamani. Lakini kwa sababu aliitikia, Yehova alitimiza ahadi yake kukuza jina la Ibrahimu. (Mwa. 12:1, 2) Ni majina machache ya nyakati za kale ambayo yamekua kama la Ibrahimu, hasa ya watu wenye kuweka mfano mwema, wa imani nyingi sana. Na Ibrahimu alipata kujulikana kama ‘rafiki ya Yehova.’ (Isa. 41:8) Ibrahimu atafufuliwa kwa wafu katika wakati wake Mungu, akiwa na tumaini la kuishi milele. Waebrania 11:16 inasema hivi juu ya Ibrahimu na wazao wake waaminifu: “Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji [ufalme wa Kimasihi].”
15. Je! Wakristo wa karne ya kwanza walitazamia kwamba taratibu mpya ya Mungu yenye haki ingekuja katika muda wa maisha yao?
15 Roho njema iliyoonyeshwa na Ibrahimu na Sara ilionekana pia kati ya wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo katika karne ya kwanza C.E. Wao pia walijua kwamba taratibu mpya yenye haki ya mbingu mpya na dunia mpya isingeletwa wakati wa maisha yao. Mtume Paulo alionyesha waamini wenzake alipokuwa akiandika kwa uongozi wa Mungu kwamba ‘siku ya Yehova’ isingekuja mpaka baada ya kutokea kabisa kwa uasi wa imani ya kweli.—2 The. 2:1-8; 2 Pet. 3:13.
16. Wakristo hao wa kwanza walikuwa na nia gani juu ya mali za kimwili, na hii ilikuwaje yenye faida?
16 Kwa hiyo je! Wakristo wa karne ya kwanza waliishi kwa njia yenye kupuza kuja kwa “siku ile na saa ile” ya Yehova? Wale waliothamini uhusiano wao na Mungu wakiwa wanafunzi wa Yesu Kristo hawakufanya hivyo. Waliacha mali zao za kimwili ili wengine waweze kushiriki furaha zao za kiroho. (Luka 14:33; Flp. 3:7-9) Kwa mfano, baada ya siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., waamini wengi waliuza mali zao na kuchanga pesa za kusaidia waliozihitaji waendelee kukaa Yerusalemu ili wazidi kufaidika kutokana na fundisho la mitume.—Matendo 2:41-47; 4:34, 35.
17. Kwa sababu gani Wakristo huko nyuma katika karne ya kwanza waliona kuhubiriwa kwa “habari njema” kuwa jambo la haraka?
17 Wafuasi waaminifu wa Yesu Kristo walilichukua kwa uzito agizo lao la kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa muda unaopungua miaka 30, waliweza kutangaza “habari njema” katika sehemu zilizotawanyika sana katika Milki ya Kirumi na hata mbali ya hapo. (Kol. 1:23) Waliitambua haraka ya kufanya hivyo. Walijua kwamba watu wangeweza kufa hata kabla ya kuwa na habari za tumaini la kupata uzima usio na mwisho wakiwa watawala wenzi wa Yesu Kristo. Walifanya kazi bila kujitafutia faida zao wenyewe ili watu wengi iwezekanavyo wapate nafasi ya kushiriki katika tumaini hilo tukufu. Zaidi ya hayo, mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi ulipaswa kuja katika kizazi hicho. Kwa hiyo Wayahudi walipaswa kuelezwa unabii wa Yesu Kristo juu ya jambo hilo hata kama waliishi wapi, ili waweze kuchukua hatua na kuepuka msiba.
18. Mashahidi wa Yehova wa Kikristo kama jamii wanaonaje katika siku zetu juu ya umuhimu wa kutumia mashauri ya Biblia katika maisha zao na vile vile katika kuhubiri wengine “habari njema”?
18 Kama jamii, mashahidi wa Yehova wa Kikristo leo wanajitahidi kufanya jambo lilo hilo. Wanasadiki kwamba kutii mashauri ya Neno la Mungu ndiyo njia bora ya kuishi. Kunawezesha mtu afurahie maisha hata sasa na kumpa tumaini imara la wakati ujao. (1 Tim. 6:17-19) Wanatambua pia umuhimu wa kuamsha watu kila mahali waone uhitaji wa kuingia katika uhusiano unaokubaliwa na Muumba kabla ya “dhiki kubwa” kutokea kwa ghafula. (Linganisha Ezekieli 33:2-9; 1 Wakorintho 9:16.) Ndiyo sababu wamekuwa na nia ya kutia jitihada wasaidie wanadamu wenzao wapate maarifa ya kweli juu ya mapenzi ya Mungu.
19, 20. (a) Ni kwa kadiri gani Mashahidi wengi wamekuwa na nia ya kusaidia wengine wapate maarifa ya kusudi la Mungu? (b) Je! kuna sababu yo yote kwao kusikitika kwa sababu hawakufuatia faida nyingine?
19 Ili kusaidia wanadamu wenzetu wajifunze juu ya Yehova na kusudi lake la ajabu kwa wanadamu, watu wengi wameacha kazi zao nzuri, wakajinyima biashara zenye kuleta faida nyingi sana, wakauza mali za kimwili walizoona si za lazima, au wakarekebisha hali zao kwa njia nyingine. Kwa sababu iyo hiyo, wengi wamehamia sehemu nyingine za nchi yao wenyewe au hata nchi nyingine. Halafu wako wale waliochagua kukaa bila kuoa au kuolewa au waliooa na kuolewa lakini wakaamua kujinyima furaha ya kuwa na watoto ili wafanye utumishi ambao kama wasingalifanya hivyo ingalikuwa vigumu kuutimiza.
20 Wengine wa wanaume na wanawake hawa wamezeeka na kuwa dhaifu. Je! wamekata tamaa kwa sababu mpaka sasa hawajakombolewa kutokana na taratibu iliyopo isiyomcha Mungu? Je! wanasikitika kwa sababu hawakufuatia faida fulani ambazo hazikuwa mbaya? Je! wanaona kwamba haikuwa lazima wajinyime kama walivyofanya? Wale waliofanya uamuzi wao kwa sababu ya kumpenda Yehova Mungu sana sana na kwa sababu ya kutaka sana kusaidia wengine hawana masikitiko. Hawaonei wengine kijicho, wakidhani kwamba wangalikuwa afadhali kama wangeishi maisha tofauti. Wala hawawadharau wale waliochagua kukaa katika eneo fulani na kulelea watoto wao huko kulingana na kanuni za Biblia. Wanaridhika kwa kuwa walifanya walilojua kuwa haki nao wanafurahi kwamba waliendeleza uhusiano wa karibu na Yehova Mungu.
KUITHAMINI NJIA YA YEHOVA
21. Tuoneje “dhiki kubwa” isipokuja upesi kama sisi wenyewe tulivyotazamia?
21 Ni jambo la kawaida kwetu kutaka faraja tuondolewe upesi iwezekanavyo magumu ya ulimwengu yanayoongezeka sana, jitihada ngumu za kila siku za kutafuta riziki, magonjwa pia, uzee na kifo. Lakini namna gani faraja hiyo isipokuja upesi kama wewe mwenyewe unavyotazamia? Hiyo ingehusuje moyo wako? Je! huenda ukashawishwa kusahau umuhimu wa kuwa na uhusiano unaofaa na Yehova Mungu na kujaribu kuona unaweza bado kupata anasa gani ulimwenguni? Ikiwa unampenda Yehova kweli kweli, utumishi wako kwa Mungu hauwekewi mipaka na tarehe yo yote. Unajua kwamba jambo walilo nalo Wakristo wa kweli ni lenye thamani zaidi kuliko cho chote kinachoweza kutolewa na ulimwengu huu. Unasadiki kwamba Yehova Mungu hatakosa kuyatimiza mambo yote ambayo ameahidia watumishi wake. Kama vile barua iliyoongozwa na Mungu iliyoandikwa kwa Waebrania inavyosema: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.”—Ebr. 6:10.
22. Ikiwa kweli sisi tunayo maoni ya Yehova juu ya wanadamu, tutauonaje wakati wo wote uliobaki kabla ya “dhiki kubwa”?
22 Tusikate maneno kwamba yanayosemwa hapa yanamaanisha kwamba “dhiki kubwa” iko mbali kisha tujiachilie tuwe tukiwaza kama ulimwengu uliotenganishwa na Mungu. Maadamu watu wangali wakiitikia ombi la Mungu la uchangamfu, imetupasa tutiwe moyo na jambo hilo. Inapatana na anavyotaka Yehova kwamba ye yote asiharibiwe bali wote wafikilie toba. (2 Pet. 3:9) Tukiwa na maoni ya Mungu juu ya wanadamu tutafurahi kwa sababu njia ingali wazi kwa wengine kusimama upande wa Yehova, wakiwa na tumaini la uzima wa milele. Nasi tunapoendelea kuona utimizo wa wazi wa kusudi la Yehova kutaka watu wengi kama iwezekanavyo wawe na hali anayoikubali tunapata nguvu za kusadiki kwamba “siku ile na saa ile” yake ya kufikiliza hukumu itakuja, kwa maana hiyo pia ni sehemu ya kusudi lake lisilobadilika.
23. (a) Ni nini kinachotufanya tuwe na hakika kabisa kwamba kusudi la Mungu juu ya kuondolewa kwa taratibu iliyopo ya mambo na kuja kwa taratibu yake mpya kutatimizwa, na kwamba kutatimia katika wakati uliowekwa na Mungu? (b) Kwa sababu hiyo, imetupasa sisi mmoja mmoja tukate maneno kufanya nini?
23 Sifa ya Yehova mwenyewe, ukweli wake, unatuhakikishia kwa nguvu kwamba ahadi yake ya kumaliza udhalimu, uonezi na maumivu “inafanya haraka” ikatimie. (Zab. 117:2) Huenda watu wengine wakaona imekawia, kulingana na maoni ya kibinadamu. Hata hivyo, ni kama vile ilivyofunuliwa kwa nabii Mwebrania Habakuki: “Njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.” (Hab. 2:3) Kwa kuwa ndivyo ilivyo, je! wewe unajitahidi sasa hivi kuendeleza uhusiano wenye kukubaliwa na Yehova Mungu? Je! unakata maneno kuendelea kumtumikia hata kuwe kutatokea nini wakati ujao? Ikiwa unavutwa inavyofaa na kumpenda Mungu na wanadamu wenzako, utafanya hivyo. Nawe waweza kutazamia kwa hakika thawabu ambayo Mungu atakupa wewe na wanadamu wengine wote wanaompenda sana sana kwa moyo.
—Kutoka The Watchtower, May 1, 1975.