Maoni Yanayofaa Ni Ulinzi
1. (a) Ni wakati gani Petro alipoandika akiwasihi Wakristo ‘wakumbuke kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova’? (b) Tokea hapo, ungekuwa muda gani mbele ya kuja kwa “siku ya Yehova”?
WAPATA mwaka wa 64 C.E. mtume Petro aliliandikia kundi la Kikristo akiwasihi wakumbuke kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova. Wakati Wakristo waliposoma maneno hayo kwa mara ya kwanza ilikuwa inabakia kama miaka sita mbele ya kuharibiwa kwa Yerusalemu na Warumi, wakati “siku” ya Mungu yenye hukumu juu ya mji huo ilipokuwa haijaja. (Matendo 2:14-21) Ilikuwa bado kuna zaidi ya miaka 1,900 mbele ya kuwapo kwa “siku” ya hukumu ya Yehova juu ya Kristendomu na taratibu ya sasa ya mambo. Lakini maneno ya Petro yaliwapasa Wakristo waliokuwa wakiishi wakati huo.
2, 3. Ni kwa sababu gani ilikuwa lazima kwa Wakristo waliotiwa mafuta katika karne kumi na tisa zilizopita ‘wakumbuke kukaribia kwa siku ya Yehova’?
2 Sababu gani ingekuwa lazima kwa Wakristo wanaoishi mbali sana na “siku” ya Mungu ya hukumu ya mwisho waone hivi? Kwa sababu maoni mengine yo yote yangewaongoza katika mtego wa kujitia katika ulimwengu na katika kuweka tumaini lao katika mambo ya kilimwengu. Iliwapasa wakumbuke kwamba mambo yaliyokuwa karibu yao yaliandikiwa kuharibiwa. Zaidi ya hayo, ingewapasa waonyeshe ukamilifu wao kwa Mungu kwa ‘kutokuupenda ulimwengu au mambo yaliyomo katika ulimwengu,’ kwa maana mwisho wangekufa, na wakati huo hali yao kama waliozaliwa kwa roho, Wakristo waliotiwa mafuta, ndugu za Yesu Kristo ingekuwaje?—1 Yohana 2:15.
3 Ulizo ambalo limewatokea Wakristo waliotiwa mafuta katika karne zote kumi na tisa zilizopita limekuwa, Hali yangu na Yehova Mungu ni nini sasa? Je! mimi ninahakikisha kuchaguliwa na kuitwa kwangu na Mungu, ili nistahili kuwa mmoja wa “ukuhani wa kifalme” wake, nikiwa na matumaini ya kutawala pamoja na Kristo? (2 Pet. 2:9; 2 Pet. 1:10; Ufu. 20:4, 6) Ili wahukumiwe na Yehova kama wanastahili au kama hawastahili cheo hicho cha kimbinguni walichoitiwa haikuwa lazima wawe wakiishi katika “siku ya Yehova.”—Ebr. 3:1.
4. Sababu gani ni lazima sisi leo na kila siku tufikirie sana tunavyotumia maisha zetu?
4 Namna gani sisi leo? Je! ni tofauti kwa sababu sisi tu karibu sana na mwisho wa taratibu hii ya mambo? Hapana, si shauri la kungojea mpaka “dhiki kubwa” itufikie. Kwa maana twajuaje kama tutakuwa tungali hai wakati huo? Katika Yakobo 4:14, Biblia inatukumbusha hivi: “Hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka.” Tukiyaona mambo kwa mchezo, hatujui wakati moyo wetu usiotumainika utakapotupotoa. (Yer. 17:9) Tena, hatujui wakati ambapo huenda hali zikatokea ambazo zingeweza kutufikia kwa ghafula, tukapatwa na msiba, hata mbele ya kuja kwa “dhiki kubwa.” Hilo lingewezaje kuwa? Ebu tuone.
KINACHOMAANISHWA NA KUVUMILIA MPAKA MWISHO
5. (a) Ni nini maana ya maneno ya Yesu, “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka”? (b) Sulemani anatukumbusha uhakika gani juu ya “mwisho” unaoelekea kuyapata maisha ya mtu ya sasa?
5 Wakati Yesu aliposema juu ya wakati ambao katika huo mitume waliishi na uliofananisha wakati ambao katika huo tunaishi, alisema hivi: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mt. 24:13) Alikuwa akisema juu ya kuvumilia mateso, kuongezeka kwa maasi na chuki ya ulimwengu. Alisema kwamba wengine kati ya wanafunzi wake wangeuawa wakati wa mateso. Lakini ikiwa Mkristo angevumilia yote haya mpaka kufa au mpaka mwisho wa hali hii ya uadui wa kilimwengu, angeokolewa kwa sababu ya ukamilifu wake. (Mt. 24:9-12) Huenda asiishi mpaka mwisho wa taratibu ya mambo, lakini yeye angehukumiwa juu ya kama alikuwa upande wa ulimwengu huu au sivyo, bila kujali “mwisho” wake ulikuwa wakati gani. (1 Yohana 2:15; Yak. 4:4) Mtu ye yote kati yetu, kwamba ni wa wale waliozaliwa kwa roho, ndugu za Yesu Kristo waliotiwa mafuta, ama wa wale wa “kondoo wengine,” wenye matumaini ya kidunia, kijana ama mzee, anaweza kufa upesi sana, leo au kesho, kwa sababu ya hali zisizotazamiwa. Sulemani Mfalme mwenye hekima alisema juu ya hali inayowapata wanadamu wote aliposema hivi: “Wakati na bahati huwapata wote. Maana mwanadamu naye hajui wakati wake; kama samaki wanaokamatwa katika nyavu mbaya, na mfano wa ndege wanaonaswa mtegoni, kadhalika wanadamu hunaswa katika wakati mbaya, unapowaangukia kwa ghafula.”—Mhu. 9:11, 12.
6. Ni jambo gani lisilotazamiwa ambalo majuzi lilimpata mmoja wa washiriki wa jamii ya makao makuu ya Sosaiti, lakini mpaka wakati huo yeye alikuwa akifanya nini?
6 Ili kutia mkazo maana ya kuwa katika hali nzuri mbele za Mungu na kibali chake nyakati zote, tunayo mifano inayoonyesha namna mwisho wetu mmoja mmoja unavyoweza kuja. Haujapita muda mrefu sana wakati mmoja wa washiriki wa jamii ya makao makuu ya Watchtower Society alipokuwa akifanya kazi pamoja na ndugu mwingine katika Jumba la Ufalme mjini New York. Alifikiwa na kijana aliyeingia katika jumba akauliza habari fulani, ambazo Shahidi huyo alimpatia vizuri. Kwa ghafula, kwa chuki ya kidini, kijana huyo alichomoa kisu akamchoma Shahidi mpaka akafa. Ni vyema kujua kwamba alikuwa akitumikia kwa uaminifu mpaka wakati huo!
7, 8. Imetupasa tujifunze nini kutokana na yaliyowapata ndugu zetu katika Malawi?
7 Tena, tunazo habari za mambo yaliyowapata ndugu katika Malawi. Hii ilikuwa nchi ambayo watu walikuwa wameitikia sana ujumbe wa Ufalme. Katika mwaka wa 1972 kulikuwako kadiri ya mmoja wa mashahidi wa Yehova kwa kila watu 194 ya watu wa nchi hiyo. Wakati wa mwaka huo wapya 1,617 walibatizwa. Twaweza kusema kwamba makundi 447 ya mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo yalipata “ufanisi” kweli kweli, na zaidi ya Mashahidi 22,000 walioshirikiana kwa bidii na makundi haya. Kweli yalikuwa yametokea mateso huko katika mwaka wa 1967. Lakini pengine katika mwaka wa 1972 mtu angaliwaza hivi, ‘Kwa kuwa tunao ufanisi huo wa kiroho bila shaka hatutapatwa na mabaya.’ Ingawa hivyo, ni nini lililowapata Mashahidi katika Malawi karibu katika usiku mmoja? Kwa sababu walijiepusha kabisa na siasa za ulimwengu huu nyumba zao zilichomwa moto, wengine kati ya wake zao walinajisiwa, wakashambuliwa na watu wenye ghasia, wengine waliteswa au wakauawa, na karibu wote walifukuzwa wakaenda kwenye nchi zilizo jirani ili waepushe maisha zao.
8 Je! twajifunza nini kutokana na hili? Imempasa Mkristo aishi kila siku kana kwamba huenda ukawa ndio mwisho wa maisha yake ya sasa ya kidunia. Inampasa aufanye Ukristo wa kweli uwe njia ya maisha, akifungamana sana na ndugu zake katika makundi, akimtumikia Yehova kwa bidii na kwa nguvu zake zote. Kwa maana ikiwa Mashahidi hao wa Malawi wangalikuwa wasiojali hali yao ya kiroho, ingalikuwaje kwao? Wale wenye nguvu za kiroho peke yao ndio wangeweza kusimama imara wakati jaribu lingekuja, na kwa sifa ya Mashahidi wa Malawi, wingi wao walifanya hivyo.
9. Ni jambo gani linaloamua kwamba tutapatikana tukimpendeza Yehova ama sivyo wakati “dhiki kubwa” itakapofika?
9 Mungu anatufunulia sisi tunayohitaji kujua ili tuweze kuchukua mwendo wenye hekima na kuwasaidia wengine kwa kuwaonya juu ya hatari na kukaribia kwa “siku” ya Yehova. Lakini yeye hakutuambia mwaka au siku, hata saa barabara atakapoanza “dhiki kubwa” juu ya ulimwengu huu. (Mt. 24:36) Si kujua wakati barabara “dhiki kubwa” itakapoanza ndiko kunakoamua kama tutakuwa wenye bidii katika utumishi wake ama sivyo, ama kama tutakuwa tukiishi katika njia inayompendeza ama sivyo. Ili tumpendeze Mungu, inatupasa tumtumikie nyakati zote, tukifanya hivyo si kwa sababu ya kukaribia kwa mwisho, bali kwa sababu twampenda yeye kama Baba yetu wa kimbinguni ambaye ni mwema sana.
SABABU WAKATI WA MUNGU NI WA KWELI
10-12. (a) Ni katika maana gani “siku ya Yehova” inakuja kama “mtego”? (b) Wale wanaopoteza imani kwa sababu mambo hayatukii kwa wakati ambao wanayatazamia yatukie wanaonyeshaje kwamba wanashindwa kuufahamu ukubwa wa cheo cha Yehova?
10 Tumefahamu kwamba “dhiki kubwa” inakuja kwa ghafula. Yesu alisema kwamba inakuja kama “mtego.” (Luka 21:34-36) Mnyama aliye karibu kunaswa mtegoni huenda asijue kwamba yeye hata yu karibu na hatari, anaponaswa kwa ghafula na bila tumaini. Biblia haituonyi juu ya hali isiyo ya kweli. Ni kweli, na itatukia kwa wakati barabara na inapotakiwa kutukia. Mungu ameweka wakati wa kuiharibu taratibu hii ya mambo. Lakini wengine wanachoka kuvumilia na wanapoteza imani kwa sababu wanaona mambo hayatukii kama wanavyoyatazamia kutukia na tendo la Mungu linaonekana kwao kama linakawia. Hii ni kwa sababu ya ufupi wa maisha ya wanadamu na haraka yao ya kutaka mambo yafanyike katika muda wao mfupi. Kwa sababu ya ujuzi wao mdogo, wanadamu wanaweza kuelekea kumlaumu Mungu.—Hab. 2:3.
11 Kwa upande mwingine, Yehova anaishi milele. Si lazima yeye awe na haraka. Yeye anaweza kuichunguza hali na kujua barabara wakati matendo yake yatakapomtimizia kila mtu faida, na vile vile yatimize kabisa kusudi lake.—Mit. 15:3.
12 Petro anasema wazo hili katika njia hii: “Wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa [Yehova] siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja. [Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”—2 Pet. 3:8, 9.
13. (a) Ni nani wanaofaidika kwa vile Yehova bado hajafikiliza hukumu juu ya taratibu hii ya mambo? (b) Ni kweli namna gani kwamba “kwa Yehova siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja”?
13 Basi kukawia ko kote upande wa Yehova ni kwa sababu ya faida yake mwenyewe, wala si kwa sababu anatenda polepole. Ni kwa faida yetu sisi wanadamu. Yehova angeweza kuuharibu ulimwengu huu upesi! Kama Petro anavyosema, yeye aweza kufanya hivyo katika siku moja kuliko ambavyo wanadamu wangeweza kufanya katika muda wa miaka elfu. Yesu alipokuwa duniani, aliponya mikono iliyopooza, macho yaliyopofuka, hata akamfufua mtu ambaye nusu alikuwa ameoza. Alitimiza matendo haya yenye nguvu mara hiyo. Ebu fikiria namna ambavyo ingalichukua muda mrefu chini ya hali za kawaida ili mkono mwingine wa mtu upate kukua, au mtu ambaye amefufuka apate viungo vingine vya mwili pahali pa vile vilivyooza kwa ukuzi wa kawaida. Halafu, kuyatazama mambo katika njia nyingine, Yehova anayeishi milele na anayetangulia kuyakusudia mambo, kwake yeye, kupita kwa miaka elfu ni “kama kesha la usiku.” (Zab. 90:4) Yeye hana mpaka wa wakati, kama sisi. Hivyo ikiwa yeye anatenda katika njia inayoonekana kwetu kama kukawia, inatupasa tukumbuke kwamba anatufikiria sisi, na ndiyo njia bora sana kwa wote wanaopaswa.
14. Sababu gani si lazima tujue wakati barabara “siku ya Yehova” itakapofika, lakini imetupasa tuwe tukifanya nini?
14 Mtu anayefahamu hali yake mbele za Mungu, mwenye imani katika Mungu, hana lazima ya kuwa mwenye mashaka. Mtume anawahakikishia Wakristo hivi: “Taabu yenu siyo bure katika Bwana.” (1 Kor. 15:58) Tukijua kusudi lake, mapenzi yake yalivyo kwetu sasa, na tumaini la mbele, si lazima tujue wakati barabara wa matukio. Bila kujali wakati “siku ya Yehova” itakapofika, tutakuwa wenye bidii katika kuyafanya mapenzi ya kimungu. Je! hivyo ndivyo umeamua kufanya?
JE WEWE UNAYO “ALAMA”?
15. (a) Ni “alama” gani ambayo inawapasa wawe nayo wale wote watakaookolewa wapate uzima duniani katika taratibu mpya ya Mungu? (b) Ni maulizo gani juu ya maoni ya mtu juu ya hali mbaya zilizomo katika ulimwengu yatakayomsaidia achanganue kama kweli anayo maoni ambayo Mungu anataka?
15 Wakati Yerusalemu wa kale ulipokuwa haujaharibiwa na Wababeli, Yehova alimpa Ezekieli njozi ambayo katika hiyo alimwona mtu wa mfano akipita katika Yerusalemu, akitia alama juu ya vipaji vya nyuso vya wote waliokuwa ‘wakiugua na kulia kwa sababu ya machukizo yote’ yaliyokuwa yakifanyika katika Yerusalemu. (Eze. 9:4) Huo ulikuwa unabii wenye kuonyesha kazi inayofanywa leo. Kila mtu anayejidai kuwa mmoja wa wale “kondoo wengine,” walio na tumaini la kuishi apa hapa duniani katika taratibu mpya ya Mungu, amepaswa ajiulize mwenyewe hivi: ‘Je! kweli mimi ninayo ile alama? Je! maisha yangu yanatoa ushahidi, waziwazi kama alama juu ya kipaji changu cha uso, kwamba ninao utu ambao ni wa Kikristo kweli kweli? Je! kweli mimi nayachukia mambo mabaya ninayoona yakifanyika, zaidi katika Kristendomu? Je! ninayachukia kwa sababu mambo haya yananiletea mimi hatari na masumbuo tu, au ninasikitika kwa sababu ninaona jina la Mungu likisutwa?’
16. (a) Ijapokuwa huenda sikuzote mtu amekuwa safi kwa adili, ni kwa sababu gani hiyo peke yake haimaanishi kwamba anayo ile “alama”? (b) Hata hivyo ni kwa sababu gani ni jambo la lazima kuepuka uasherati?
16 Wale wanaoonyesha kweli kweli ile “alama” ya utu wa Kikristo wanaangalia sana isije ile siku ya Yehova ikawakuta wakizoea mambo ambayo yangewatia katika jamii ya watu wanaoupenda ulimwengu. Je! wewe ndivyo ulivyo? Kwa mfano, wewe waonaje mambo kama mwenendo mpotovu, uasherati na uzinzi? Bila kujali namna maisha yako yamekuwa zamani, je! wewe unakubaliana kabisa na hukumu ya Yehova juu ya wale wanaozoea mambo hayo? (1 Kor. 6:9-11; Ebr. 13:4) Kwa kweli, watu wengine hawajafanya jambo kama hilo hata kidogo. Hata hivyo hilo peke yake halimaanishi kwamba ‘wametiwa alama’ ya wokovu. Wale walio na ile “alama” si watu wanaoepuka mwenendo huo kwa sababu unaweza kuongoza kwenye matokeo mabaya tu. Wanachukia mabaya kwa sababu yanahalifu vile vile njia za haki za Yehova. Kama Yusufu mwaminifu, wanafahamu kwamba uasherati au uzinzi hautii unajisi tu, bali hakika ni ‘ubaya mkubwa’ na ni ‘kumkosea Mungu.’ (Mwa. 39:9) Ni maoni ya Yehova ndiyo ya maana sana kwao. Kwa kujua kwamba uasherati ndio mmojawapo wa mitego mikubwa sana ya Shetani, ni lazima kuziepuka hali ambazo huenda zikamshawishi mtu afanye dhambi hii na kushindwa na kumbe sisi tuko karibu sana na kuingia katika Taratibu Mpya. Ukumbuke mfano ule wa Israeli katika Moabu mipakani mwa Nchi ya Ahadi. Watu 24,000 walipoteza maisha zao katika mtego wa uasherati.—Hes. 25:1-9.
17. Ikiwa kweli tunayo ile “alama,” maoni yetu yatakuwa nini juu ya kusema kweli, na kwa sababu gani?
17 Namna gani juu ya kusema kweli? Je! sisi tunaiheshimu kweli, au tunapenda kuipotoa kweli kidogo, ili tutoke katika hali yenye kusumbua, au ili tujipatie tunachotaka? Kusema uongo ndiyo kawaida katika biashara leo. Lakini kusema uongo kulitoka wapi? Yesu alisema kwamba Ibilisi “ni mwongo, na baba wa huo” uongo. (Yohana 8:44) Kwa hiyo, kweli mwongo anamtumikia Ibilisi. Lakini ikiwa sikuzote tunasema kweli tunaonyesha kwamba tumeuvaa utu mpya, kwamba kweli tunayo ile “alama.” Neno la Mungu lasema: “Sasa kwa kuwa mmeuacha uongo, semeni kweli kila mmoja wa ninyi na jirani yake.” (Efe. 4:25, NW) Je! wewe, unapokuwa katika shida, unajiona kushawishwa kusema uongo kama ndiyo njia nyepesi ya kutoka katika shida? Au wewe ni kama mwandikaji wa Mithali aliyesema hivi: “Uniondolee ubatili na uongo”?—Mit. 30:8.
18, 19. Sababu gani kunatakiwa zaidi ya kuhudhuria mikutano na kushirikiana tu na mashahidi wa Yehova, ikiwa twataka tuwe na dhamiri njema mbele za Mungu?
18 Watu wengi ambao ni wapya wanaingia katika njia ya kweli wakati huu ulio karibu na “siku ya Yehova.” Zamani walikuwa wakifanya mazoea yaliyokuwa yenye hatari kwa akili na miili yao wenyewe. Lakini wanabatizwa, wakimwomba Mungu dhamiri njema. (1 Pet. 3:21) Ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaofikiria kuchukua hatua hiyo ya ubatizo, au ikiwa ulichukua hatua hiyo zamani, je! waweza kupata au kupokea dhamiri njema, iliyo safi kutoka kwa Mungu ikiwa unaendelea kufanya mazoea ambayo unajua yana matokeo yenye hatari katika akili na mwili? Je! waweza kuipata dhamiri safi kwa kushirikiana tu na mashahidi wa Yehova, wanaojaribu kuifuata kanuni bora ya Biblia ya usafi, ikiwa wakati uo huo unaendeleza mazoea ambayo wanakataa? Je! unaweza kusema kweli kwamba wewe ni mmoja wao? Je! wataka uwe mmoja wao?
19 Ikiwa watazamia kupokea kibali na uzima kutoka kwa Mungu ni lazima uwe na dhamiri safi. Kwa hiyo, katika mambo yote tunayoyafanya jambo la kwanza kufikiriwa na sisi limepaswa liwe: Mambo haya, yanaleta matokeo gani juu ya jina la Mungu? Na pili: Mambo haya yanaleta matokeo gani juu ya kundi lake la Kikristo linalowakilisha jina na ufalme wake? Kufanya hivi kutatusaidia tuendeleze dhamiri njema katika mwendo tunaochagua. Ni lazima tukumbuke ya kwamba Mungu amelifanya kundi la Kikristo kuwa “nguzo na msingi wa kweli” katika dunia. (1 Tim 3:15) Imetupasa tuishi kupatana na mambo ambayo kundi hilo linafundisha. Kukumbuka kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova kutatulinda sisi tusikifuate kitu fulani ambacho, kikilinganishwa na hazina yenye utukufu ya kibali cha Yehova, ni “kama mavi.” (Flp. 3:8) Kutamfanya mtu ajitahidi kuendeleza dhamiri njema. Yeye atauzuia mwili wake, isiwe, akiisha kuwahubiri wengine, yeye mwenyewe awe mtu wa kukataliwa na Mungu.—1 Kor. 9:27.
YESU ALIWAONYA WANAFUNZI WAKE JUU YA NINI?
20-23. (a) Yesu alionya juu ya mambo gani ambayo yangeweza kuifanya imani yetu iwe dhaifu, kama inavyoonyeshwa katika Luka 21:34-36? (b) Eleza namna masumbufu haya ya kila siku ya maisha yangeweza kuwa na matokeo hayo yenye kuharibu imani. (c) Ikiwa twataka kweli roho ya Mungu ituongoze, imetupasa tuwe wapi?
20 Walakini, si lazima yawe mambo makubwa yanayoweza kuiharibu imani ya mtu. Akikazia shauri la kuishi kwa imani kila siku, Bwana Yesu Kristo alionya hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:34-36.
21 Hapa Yesu alikuwa akionya juu ya mambo ya namna gani? Alikuwa hasemi juu ya dhambi zile kama uasherati, uzinzi na wivi. Bila shaka, mambo hayo yangemzuia mtu asiingie katika ufalme wa Mungu. Lakini Yesu alikuwa akiwaonya juu ya mambo ya kawaida ambayo kwa vyepesi yanaweza kumpata ye yote wa sisi, yakitia ulaji, unywaji na masumbufu ya kila siku ya maisha. Lakini ni vyepesi kujitia ndani ya haya yote kwa kadiri ya kufanya dhambi. Katika mambo hayo mna werevu na hatari. Mtu anaweza kudanganywa kwa vyepesi afikiri kwamba anachukua mwendo ulio salama, halafu anaswe pasipo kujua. Mtu aweza kujitia na kunaswa na mambo ya ulimwengu huu na masumbufu yanayoletwa nayo, apate kujiumiza kwa kiroho. Anaweza kusumbukia mno kujipatia mambo ya maisha haya ambayo anafikiri anayahitaji. Huenda akaanza kufikiri kwamba inampasa awe na vitu vyote vya anasa na vya starehe vilivyo bora sana ambavyo ulimwengu wote unavyo. Huenda akaona kwamba inampa haki ya kufanya kazi kwa wakati wa ziada ili apate vitu hivi.
22 Kwa sababu hiyo, yeye anasahau maisha yake ya kiroho; hatumii wakati ili ajifunze; anashindwa kuipa jamaa yake msaada unaohitajiwa ili waendelee kuwa wenye afya kwa kiroho; anakosa ushirika pamoja na ndugu. Kwa hiyo anakuwa na bidii kidogo ya kushiriki katika utumishi wa shambani. Hata analofanya ni mradi lifanywe, bila bidii ya kujitoa kuwasaidia wengine wawe wanafunzi. Kwa kweli anaonyesha kwamba haamini kwamba Kristo anatawala na kwamba ile siku ya Yehova imekaribia.
23 Kwa upande mwingine, ikiwa kweli mtu anafanya maombi kwa Mungu, anatamani roho ya Mungu iwe juu yake, imwongoze. Atajiweka mwenyewe mahali roho ya Mungu inapotenda kazi, akishirikiana na kuwa rafiki wa kweli na mfanya kazi mwenzi wa wale walio na roho ya Mungu.
KUSUDI LINALOFAA KWA KAZI YA KUHUBIRI
24. Ni nini kilichomwongoza Yesu katika kuhubiri kwake kwa “habari njema”?
24 Ni jambo gani lililomwongoza Yesu Kristo, Mhubiri mkubwa kuliko wote duniani? Upendo wake kwa Yehova na kwa “kondoo” za Yehova. “Alipowaona makutano,” Mathayo anaripoti katika sura ya 9, mstari wa 36, “aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” Je! Yesu aliwachukia, au alisema tu kwa wanafunzi wake juu ya hali yao yenye kusikitikiwa? Hapana. Aliwapenda watu kwa moyo wake, na ilimwongoza ajitahidi kuwasaidia. Maneno yanayofuata ya masimulizi ya Mathayo (mist. 37, 38) yanasomwa hivi: “Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” Na Yesu na wanafunzi wake walivuna mavuno mengi. Katika Matendo 4:4 tunaona kwamba hesabu ya watu walioamini wakati huo ilikuwa 5,000, halafu, katika Matendo 6:7, tunasoma hivi: “Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”
25, 26. (a) Kwa vile watu wanahitaji wajifunze kweli, ni maulizo gani yanayomwelekea kila mmoja wetu? (b) Kama inavyoonyeshwa na yaliyompata mume na mke katika Ireland, ni nini kinachopaswa kituongoze tuendelee kuhubiri?
25 Vivyo hivyo leo, uhitaji ni mkubwa sana. Watu katika ulimwengu wote hawakuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa kweli zamani kama leo. Hivyo, kila mmoja wa sisi anakutana na ulizo hili, Je! mimi nazipenda “kondoo” za Yehova zilizotawanyika? Kuliko kulaumu tu hali mbaya, je! mimi nina nia ya kufanya jambo litakalowasaidia sana watu hawa? Je! nampenda sana Yehova hata naweza kuuonyesha upendo wangu katika njia hiyo?
26 Ndugu ambaye, pamoja na mkewe, alikuwa ametumikia kwa muda wa miaka kumi na minne kama painia katika Ireland alisema hivi: ‘Kila siku tulikwenda nyumba kwa nyumba mchana kutwa na mtu asiitikie. Nikiisha kurudi nyumbani nilikuwa nikijiuliza mwenyewe hivi, Sababu gani ninafanya hivi? Na sikuzote jibu lilikuwa, Kwa sababu nampenda Yehova.’
27. Ikiwa twaona watu hawapendezwi au wanapinga katika huduma yetu, ni shauri gani la Maandiko tuwezalo kulikumbuka kwa kufaidika?
27 Namna gani wewe mwenyewe? Je! katika eneo lako unaona watu hawapendezwi au wanapinga? Ikiwa ndivyo, yakumbuke maneno ya mtume Paulo katika Waebrania 10:35-39: “Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi. Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, yeye ajaye atakuja, wala hatakawia. Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye. Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu.”
28. Basi imetupasa tuoneje juu ya pendeleo la kuwa mashahidi wa Yehova?
28 Basi, kulingana na mambo haya yote, inatufaa sote tujichunguze wenyewe ili tuhakikishe roho tuliyo nayo. Ikiwa tumekuwa mashahidi wa Yehova waliobatizwa, bila shaka hatutaki tusitawishe maoni yenye kupatilia shaka mahali penye utukufu tunaposimama. Kibali hiki chenye maana sana kimepaswa kitufanye tupendezwe kwa shauku na kutamani sana kuwasaidia wengine. Kimepaswa kituongoze ‘tulifanye kwa nguvu zetu lile ambalo mikono yetu itakalolipata kulifanya’ kwa wakati wake unaofaa, tukimtumikia Yehova kwa nafsi yote. (Mhu. 9:10) Tukiwa na hazina ya kweli, na kupendelewa na huduma ya Kikristo hatuwezi sasa kuliepuka daraka letu kwa namna ya kuwaza kwa bila kutenda au udhuru.
29. Ni nini kitakachotuwezesha sisi tuitazamie “siku ya Yehova” tukiwa na uhakika wenye furaha?
29 Kupitia kwa nabii Isaya, Yehova anatutia moyo akisema: “Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye [hatashikwa na woga].” (Isa. 28:16) Katika wakati wa Isaya watu walitumainia amani na usalama wa uongo. Lakini leo, tunajua ya kwamba Mfalme Yesu Kristo anatawala na kwamba taratibu mpya tukufu yenye amani na usalama wa kweli iko karibu. Tukiwa na imani tutakuwa imara, hatutatikiswa na mashaka. Hakuna shaka juu ya yanayotakiwa kwetu ili tuishi katika taratibu hiyo mpya. Imani iliyo imara pamoja na “matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya kumwabudu Mungu” vitatuhakikishia wokovu. Kwa njia hii tutasimama hali tumekubaliwa mbele za Mwana wa Adamu wakati ile “siku” yenye moto ya Yehova itakapofika.
—Kutoka The Watchtower, Jan. 15, 1974.