Msingi Imara wa Kuwa na Tumaini Hakika
1. Ni hali gani ya watu wa Yehova kuhusiana na ulimwengu huu?
WALE ambao wamejiweka wakf, wakawa watumishi waliobatizwa wa Mungu walikabidhi nafsi zao kwake. Kila walicho nacho, kila walicho au watakachokuwa, kimo mikononi mwa Mungu—wakati wao uliopo, wakati wao ujao, maisha zao zote na tumaini la kuishi katika taratibu mpya ya Mungu ya mambo itakayokuja. Wao wameyasahau mambo yao ya nyuma, wakaacha kutumaini mambo ya sasa ya taratibu hii ya ulimwengu au yanayoweza kutokea siku zijazo.
2. Ijapokuwa alidhihakiwa na ulimwengu na pia na wengine waliojidai kuwa “ndugu,” Paulo alionaje?
2 Juu ya jambo hili, mtume wa Bwana Yesu Kristo alisema yafuatayo, ijapokuwa alitiwa gerezani, na dhihaka na upinzani ukafanya waitwao “ndugu” zake wa Kikristo wamwache: “wa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile.”—2 Tim. 1:12.
3. Ni tumaini gani hakika wanaloweza kuwa nalo Wakristo juu ya kuja kwa “siku” ya Yehova na kuingia kwao katika mapumziko ya Mungu?
3 “Siku ile” ndiyo siku ambayo Wakristo ulimwenguni mwote wametazamia, wakati Mungu atakaposafisha dunia na kutimiza mapenzi yake “hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:10) Tuna ahadi ya Mungu kwamba hilo litafanyika. Bila shaka wakati huo utakuwa wa faraja na mapumziko, kwa wanadamu. Twaweza kuwa na matumaini gani hakika kwamba tutafurahia? Tuna matumaini hakika kabisa, kwa maana Biblia yatuambia kwamba “siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe,” naye aahidi walio watii kwamba wanaweza kuingia katika mapumziko yake. (Mwa. 2:2; Ebr. 4:1, 4, 9) Je! twaamini kweli ahadi hiyo?
4. Waisraeli waliwekewa nafasi gani walipotoka misri, lakini walilionaje neno la Mungu kwa habari hiyo?
4 Waisraeli, walipokombolewa utumwani Misri, walipewa ahadi ya kuingia katika mapumziko ya Mungu, na ya kuwa na mapumziko ya kutokuwa katika utumwa na uonezi wakati wa maisha yao katika Nchi ya Ahadi. Wangefurahia maisha katika sehemu ya dunia ambayo Mungu alikuwa amehifadhi kama bustani ya kiparadiso. (Kum. 11:11, 12; Mwa. 13:10) Lakini walio wengi walionyesha ukosefu wa imani katika ahadi aliyowafanyia Mungu. Walionyesha kutoamini huko kwa kiasi cha kutaka kurudi Misri. Waliona kwamba ahadi hiyo ya Mungu haikuwa hai tena, ilikuwa ahadi iliyokufa, iliyodhoofika, isiweze kutimizwa.
UHAKIKA WA NENO LA MUNGU
5, 6. (a) Jambo gani laonyesha kwamba neno la Mungu kwa Israeli halikuwa lisilo na nguvu? (b) Sababu gani twaweza kuwa na tumaini hakika sana katika neno la Mungu leo, juu ya kuingia katika mapumziko (“raha”) yake?
5 Ni katika habari hiyo mtume Paulo aliandika maneno kama hayo katika Waebrania 4:12: “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”
6 Neno hilo au ahadi hiyo iliyofanywa kwa Israeli haikuwa imekufa wala kudhoofika. Kwa kweli, wachache walioonyesha imani waliingia katika “raha” (mapumziko) ya kidunia katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 14:5-9, 30; Yos. 14:6-10) Vivyo hivyo leo, tuna ahadi ya Mungu yenye thamani juu ya maisha katika taratibu mpya yenye haki. Tumesikia “neno” lake kwamba kizazi kinachoishi katika huu “wakati wa mwisho” ndicho kizazi kitakachopatwa na “dhiki kubwa.” (Mt. 24:34) Tumesikia neno lake la ahadi kwamba tunaweza kuingia katika “raha” yake sasa, kwa imani, na kwamba mkutano mkubwa wa watumishi wake utaokoka dhiki hiyo uingie katika taratibu mpya itakayofuata. (Ufu. 7:9-14) “Neno” hilo li hai tena lina nguvu za kutimiza kila jambo ambalo Yehova amekusudia; halitashindwa. (Isa. 55:10, 11) Sababu gani sivyo? Mungu aliyetoa neno hilo, yu hai na sikuzote yeye hufanya mambo yanayotimiza neno lake. Yeye hakulala wala si msahaulifu wa sehemu yo yote ya “neno” hilo, kama wanadamu wasahaulifu. (Hes. 23:19) Hilo lawezaje kusemwa kwa matumaini kamili?
7, 8. (a) Taja mambo fulani yanayotutumainisha zaidi juu ya uhakika wa neno la Mungu. (b) Petro alisema nini juu ya uhakika wa neno la Mungu katika wakati wake?
7 Kwani hatuna ushuhuda wa hakika? Twaweza kutoa mamia ya mahakikisho. Maandiko na historia vilevile yamejawa na mifano ambamo Neno la Mungu lilitimizwa.a Na je! kuamini na kutumia neno hilo katika maisha zetu, kutegemeza tumaini letu katika mipango ya Mungu na imani yetu katika ahadi yake, hakukuwa na matokeo mema katika maisha zetu, kukatufanya wenye furaha? Tungekuwa na tumaini gani wakati ujao tukiliacha neno hilo na kufuatana na ulimwengu?—Mt. 16:25, 26.
8 Kama uhakikisho wa kutegemeka kwa neno la Mungu, jambo lili hili tunalozungumza—kwamba Wakristo wengine wa kujidai wangekosa imani—lilitabiriwa na Yesu, Paulo na Petro. Twauona uasi huu wa imani ya kweli wazi katika taratibu za kidini za Jumuiya ya Wakristo. (Mt. 13:38, 39; Matendo 20:29, 30; 2 The. 2:3; 2 Pet. 2:1-3) Petro alionyesha pia Wakristo wa siku zake kwamba yeye na wafanya kazi wenzake hawakuwa wakifuata hadithi zilizotungwa kwa ujanja, bali walikuwa wakifuata masimulizi ya mambo yaliyoshuhudiwa na watu kwa macho yao wenyewe, na kwamba hata wakati huo wao, Wakristo wa karne ya kwanza, hawakuwa na unabii peke yake. Walikuwa na ‘lile neno la unabii lililofanywa imara zaidi’ mbele ya macho yao wenyewe kwa kushuhudia utimizo wenyewe.—2 Pet. 1:16-19.
9. Kwa sababu gani ni jambo la maana kwetu kuliangalia sana neno la Mungu la unabii kama lilivyokuwa kwa mitume?
9 Lo! tuna ushuhuda mwingi zaidi namna gani leo, karne kumi na tisa baadaye! Petro alimalizia hivi: “Mkiliangalia [neno la unabii], kama taa ing’aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu.” (2 Pet. 1:19) Neno la Mungu lastahili tulikazie fikira zetu za moyoni sasa kuliko wakati mwingine wo wote. Kwani hatuoni magumu yanayopatikana sasa na ulimwengu, sawa na vile Mungu alivyotangaza katika neno lake la unabii? Na je! hatuoni mpanuko wa habari njema duniani mwote, mamilioni ya watu wakikusanyika pamoja kufanyiza ule “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa “dhiki kubwa”?
UWE MWANGALIFU UWE NA MAONI YA KIASI
10. (a) Neno la Mungu linafunua nini juu yetu? (b) Twaweza kujiuliza maulizo gani katika habari hii?
10 Neno au ujumbe wa Yehova ni wa kweli unapoeleza habari za kuingia kwetu katika raha (mapumziko) ya Mungu sasa na kukaa humo hata kupita “dhiki kubwa,” ambayo baada yake utawala wa Kristo wa miaka elfu utageuza dunia iwe bustani ya paradiso. Neno la Mungu ni ‘kali kweli kweli kama upanga ukatao kuwili.’ Litaonyesha vile tulivyo hasa kufunua mawazo na makusudi ya mioyo yetu ni nini. Je! tunamtumikia Yehova Mungu kwa sababu twampenda, twamtumaini na kusadiki kabisa anayosema? Au ‘tunachoka katika kutenda mema,’ tukitafuta tarehe fulani hasa tujiletee faraja sisi wenyewe, bila kufikiria maisha za watu wengine? (Gal. 6:9) Je! tunayathamini mambo mema ambayo tumepata kwa Yehova na kwa kushirikiana na watu wake? Je! mambo ambayo tumejifunza hayakutusaidia katika maisha zetu za jamaa? Je! hatuwapendi rafiki wengi wa kweli ambao tumepata sasa kwa sababu ya kuijua kweli?—Marko 10:29, 30.
11. Huenda ikawa kwamba wengine wamefanya kosa gani juu ya mwendo wao wa Kikristo?
11 Huenda ikawa kwamba wengine ambao wamekuwa wakimtumikia Mungu walipanga maisha zao kulingana na maoni yenye makosa juu ya jambo ambalo lingetukia tarehe fulani au mwaka fulani. Kwa sababu hiyo, huenda wakawa waliahirisha au wakakosa kujali mambo ambayo kama wangalijua wangaliyafanya. Lakini wamekosa kuelewa maana ya maonyo ya Biblia juu ya mwisho wa taratibu hii ya mambo, wakidhani kwamba tarehe za Biblia hufunua tarehe yenyewe.
12, 13. Ni jambo gani ambalo Yesu hakumaanisha kwa maneno yake katika Luka 21:34-36?
12 Maneno ya Yesu mwenyewe yaonyeshaje juu ya nia inayofaa kwa habari ya mwisho—je! yaonyesha ni kutafuta tarehe, au namna gani? Yeye alisema: “Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:34-36.
13 Je! Yesu alimaanisha kwamba yatupasa turekebishe mambo yetu ya pesa na ya kimwili ili mali zetu zitufikishe kwenye tarehe fulani tunayodhani ndipo mwisho utakuja? Ikiwa nyumba yetu imeanza kubomoka, je! tuiachilie tu, tukidhani kwamba twaihitaji miezi michache tu inayokuja? Au, ikiwa mtu fulani katika jamaa apaswa kutibiwa na madaktari, je! tuseme, ‘Ah, tutaahirisha kufanya hivyo kwa sababu wakati u karibu sana wa kuondoka kwa taratibu hii ya mambo’? Yesu hakushauri tuwe tukiwaza hivyo.
14. (a) Yesu na mitume wake waliposema juu ya wakati wa mwisho, walikuwa wakipendekeza tuwe na maoni gani? (b) Je! yamaanisha inawapasa Wakristo wafanye mabadiliko makubwa katika maisha yao, au nini, kwa vile mwisho ni karibu?
14 Basi Yesu na mitume wake walimaanisha nini waliposema juu ya kuwa macho kuona ishara za mwisho, au ‘kutazamia hata ije siku ile ya Yehova, na kuihimiza’? Walimaanisha tuwe na hakika kabisa kwamba siku hiyo haitachelewa dakika moja kuliko wakati anaokusudia Yehova. Petro alisema hilo lapaswa kutuharakisha tuwe na ‘mwenendo mtakatifu na utawa,’ tukiwa macho kuona tunaishi kulingana na kanuni za Biblia na kwamba tu wenye kujibidiisha tukiutangaza ujumbe wa Ufalme na kusadikisha watu kwamba ni wakati wa haraka kumgeukia Mungu. (2 Pet. 3:11, 12) Sote twaweza kufanya maendeleo katika ibada yetu kwa Mungu, tukiimarisha uhusiano wa karibu naye. Pengine kufika hapo tumefanya yote tuwezayo, na tumefanya maendeleo tulipokuwa tukisonga mbele. Je! basi uhakika wa kwamba mwisho unakaribia sana wamaanisha kwamba yatupasa tufanye mabadiliko makubwa katika njia yetu ya maisha na katika kumtumikia Mungu? Si lazima. Walakini, huenda tukawa tunahitaji kufanya maendeleo makubwa kulingana na Maandiko. Pia, ikiwa ziko sehemu za maisha zetu ambamo twaweza ‘kukomboa’ wakati kutoka shughuli za bure katika taratibu hii yatupasa kufanya hivyo. Kwa njia hiyo, wengi wameendelea kupata furaha ya utumishi wa wakati wote wa “upainia” miaka iliyopita. Sote twaweza kuchunguza tuone tunaloweza kufanya.—Efe. 5:15, 16.
15. Ikiwa mtu amerekebisha maisha yake kwa kutazamia kwamba mwisho ungekuja tarehe fulani, sasa yampasa afanye nini?
15 Lakini si hekima kwetu kukaza macho yetu kwenye tarehe fulani, tukikosa kuangalia mambo ya kila siku ambayo kwa kawaida sisi huangalia kama Wakristo, kama mambo ambayo sisi na jamaa zetu twayahitaji kweli. Huenda tukawa tunasahau kwamba, wakati “siku” hiyo itakapokuja, haitabadili kanuni ya kwamba lazima Wakristo waangalie madaraka yao yote nyakati zote. Ikiwa mtu fulani amekata tamaa kwa sababu ya kutowaza hivyo, sasa yampasa ajitahidi kurekebisha maoni yake, baada ya kuona kwamba si neno la Mungu lililomkatisha tamaa wala kumdanganya, bali kwamba ufahamu wake mwenyewe ulitegemea maoni mabaya.
16. Kama umetegemea sana tarehe fulani kwa unyofu wote wa moyo, ni faraja gani unayoweza kuona katika hali hii?
16 Walakini, tuseme kwamba wewe ulitegemea sana tarehe kwa njia ya kusifika, ukakaza fikira zako zaidi juu ya haraka ya nyakati na uhitaji wa watu kusikia. Na tuseme sasa kwa muda unajiona kukata tamaa; je! umepata hasara kweli? Je! umeudhika kweli? Twaamini waweza kusema umepata faida kwa kufuata mwendo huo wa uaminifu. Pia, umewezeshwa kupata maoni ya kukomaa kweli kweli, ya kiasi zaidi.—Efe. 5:1-17.
17. Twajuaje kwamba hatutaambiwa tarehe mapema ya “kuja” kwa Kristo kuhukumu?
17 Maandiko yanaeleza mara nyingi kwamba mwisho utakuja juu ya ulimwengu kwa ghafula kabisa. Mtume alitaja hilo, akisema: “Ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya [Yehova ya hukumu] yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.” (1 The. 5:2) Ili Wakristo wa kweli ‘wasipatikane kama kwamba na wevi,’ Yesu alisema hata kwa wanafunzi wake nyuma huko, na kwetu leo hivi: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.” Baada ya hapo alisema: “Jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.” (Mt. 24:42-44) Maneno hayo ya Yesu yaliyo wazi yaonyesha kwamba watumishi wa Mungu hawatapewa wakati wo wote tarehe ya “kuja” kwa Kristo kuhukumu mpaka itakapofika yenyewe. Kwa kweli, itafika wakati ambao watadhani ‘haielekei’ kufika.—Luka 12:39, 40.
USIDANGANYWE NA ‘KUOKOKA’ KWA MATAIFA KATIKA HATARI NYINGI
18. Kwa sababu gani tusidhani kwamba mataifa yote, kila mahali, yatakaribia hali ya kufa njaa kabla ya kutokea “dhiki kubwa”?
18 Hata hivyo, angalia lile ambalo hasa Yesu alionya. Maneno yake hayaonyeshi kwamba, “dhiki kubwa” ikaribiapo, hali ya ulimwengu itakuwa mbaya sana hata kila mtu, kila mahali, akaribie kufa njaa. Kama ingekuwa hivyo, kungewezaje kuwa na hatari kwa wanafunzi wa Yesu ya ‘kulemewa na ulafi na ulevi’ wakati huo? Kumbuka, pia, kwamba Yesu alitumia hali za siku za Nuhu kabla ya gharika na siku za Lutu kabla ya kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora kama mifano. Alionyesha kwamba wakati huo maisha ya watu yalikuwa ya kikawaida tu. Walikuwa ‘wakila, wakinywa, wakioa na kuolewa, wakioza, wakinunua, wakiuza, wakipanda mimea na kujenga,’ mpaka siku ile ile uharibifu wa ghafula ulipowafyatukia.—Luka 17:26-30.
19. Ijapokuwa huenda mataifa wakaweza kutengeneza hali ya mambo na kuyaendesha mambo, tutakumbuka nini?
19 Kwa hiyo hatutatazamia taratibu hizi za ulimwengu zikaribie kukoma au kufikia hali ya kuharibika kabisa ndiyo tujue lazima sasa “dhiki kubwa” ije. Hatutadanganyika taratibu hizi zikielekea ‘kufufuka’ kutoka hatari kubwa sana, kama kwamba hiyo itaahirisha kufika kwa siku ya Mungu ya hukumu. Hatutaanza ‘kujenga upya’ na ulimwengu, kama kwamba taratibu hii itaendelea kwa wakati usiojulikana. Maneno yaliyoongozwa na Mungu ya mtume Paulo yaliyo katika 1 Wathesalonike 5:3 yaonyesha kwamba watu wa ulimwengu huu hakika watakuwa wakitangaza, “Kuna amani na salama’.” kabla tu ‘uharibifu wa ghafula haujawajia, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba,’ wasiweze kabisa kuokoka.
20, 21. (a) Tunataka tuepuke nini katika kula na kunywa, kujenga, na mengine kama hayo, kama ilivyokuwa Kabla ya Gharika? (b) Maneno ya mtume Paulo katika 1 Wathesalonike 5:4-6 yatuonyaje juu ya kuokoka hatari inayokaribia sana ya “siku” hiyo? (c) Paulo anaonyeshaje maana ya kukesha katika Warumi 13:11-14?
20 Hakuna ubaya kula wala kunywa, wala kuoa wala kuolewa wala kukuza jamaa, wala kununua, wala kuuza, wala kupanda wala kujenga. Lililo baya ni kufanya kama watu wa siku za Nuhu na Lutu—kuacha mambo hayo yatushughulishe sana hata tukose kuona makusudi ya Mungu na kanuni zake zenye haki kisha kutanguliza mambo ya kimwili katika maisha zetu. Kufanya hivyo ni kulala kiroho. Tofauti na mwendo huo, mtume Paulo asema: “Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza. Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe.”—1 The. 5:4-6.
21 Akionyesha maana ya kukesha na kuthibitisha kwamba sisi ni “wana wa mchana” badala ya wana wa giza, Paulo katika Warumi 13:11-14 anasema hivi: “Tukijua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini. Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia; basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake.”
22. Je! kutojua wakati ile “siku” itakapokuja kutulegeze tusiwe macho?
22 Kwa wazi, basi, uhakika wa kwamba hatujui wakati hasa “dhiki kubwa” itakapoanza wala wakati utawala wa miaka elfu wa Mwana wa Mungu utakapoanza haupunguzi lazima ya kukesha leo. Unaongeza na kuikuza sana lazima ya kuwa macho, kukesha, kuwa tayari. Kama tungejua wakati barabara tungeweza kustarehe halafu wakati huo ukaribiapo tungeweza kuanza kujitayarisha. Lakini kutojua kwetu kwatutaka tuwe tayari wakati wote. Maana yote ya Neno la Mungu, na hasa shauri la Mwana wake, laonyesha hivyo.
23. Ni mwendo gani ambao Paulo anatuambia tufuate huku tukingojea “siku” hiyo?
23 Kwa hiyo shauri la mtume latuhusu sisi kwa nguvu sana, anaposema hivi: “Basi, farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile kama mnavyofanya.” (1 The. 5:11) Tutatumia kila nafasi kusaidia, si ndugu zetu tu, bali pia wale walio nje ya kundi wachukue mwendo utakaowawezesha ‘kuokoka mambo haya yote yanayotazamiwa kutokea.’ Sisi wazazi, tutajitahidi kuwekea watoto wetu mfano mzuri wa kuthamini na kukesha kwa kiroho ili nao pia wapate kuwa macho na kuendelea kukesha pamoja nasi.
KUSONGA MBELE KWA TUMAINI HAKIKA LENYE KUONGEZEKA
24. Kwa habari ya kukaribia kwa mwisho, orodha ya tarehe ina faida gani kwetu?
24 Ile orodha ya tarehe inayopatikana katika Biblia haimo humo bila kusudi jema. Orodha hiyo ya tarehe yaonyesha kwamba tumo mwishoni mwa miaka elfu sita ya historia ya kibinadamu. Ijapokuwa haufunui wakati siku ya Mungu ya hukumu kali juu ya taratibu hii mbovu ya mambo itakapoanza, uhakika huu wa orodha ya tarehe unaongeza sababu moja zaidi kwa sababu nyingine nyingi tulizo nazo za kuwa na tumaini hakika kwamba wakati ubakio ni mfupi sana. Unatoa uthibitisho zaidi kwa sababu hizi kama msingi wa kuwa na tumaini hakika na lenye nguvu katika neno la Mungu, kwamba li hai na lenye nguvu na litatuingiza katika taratibu mpya yenye haki.
25. Kwa hiyo, tutakuwa na maoni gani tukiwa na msingi imara wa tumaini hakika?
25 Hivyo, basi, kwa kumpenda Mungu, kwa kumpenda Mwana wake, kwa kuipenda kweli na haki, kwa kupenda jamaa yako, jirani zako, ndiyo, kwa kuupenda uzima wenyewe—na tukeshe, tujionyeshe kuwa hai na watendaji kiroho, leo na kila siku, nasi tutafaulu kuokoka mambo haya yote yanayotazamiwa kutokea. Yehova Mungu, Mungu wa kweli, ametupa “neno” lake zito, na “kila amwaminiye hatatahayarika.” (Rum. 10:11) Yeye na Mwana wake na wakubariki sana uendelee kutumikia kwa uaminifu, sasa na kwa wakati wote utakaokuja.—Kutoka The Watchtower, July 1, 1976.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama kitabu “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial,” kurasa 343-346, kilichochapwa na Watchtower Bible and Tract Society, Brooklyn, N.Y. (1963) Hapa pamepangwa utimizo wa kihistoria wa unabii wa Mungu.