‘Kaeni Mkikesha na Mbaki Mkiwa na Fahamu Zenu’
“Acheni sisi tusilale kama wale wengine wote wafanyavyo, bali acheni sisi tukae tukikesha na kubaki tukiwa na fahamu zetu.”—1 Wathesalonike 5:6, NW.
1. Tunaweza kutazamia utimizo gani wa unabii wa Biblia baada ya muda mfupi?
WAKATI Yesu alipoutabiri uharibifu wa Yerusalemu katika kizazi chake, alisema: “Hizi ndizo siku za kupimia watu haki ya hukumu, ili mambo yote yale yaliyoandikwa yapate kutimizwa.” (Luka 21:22, NW) Katika mwaka wa 70 W.K., Mungu alifikiliza hukumu kwa haki juu ya wale waliokuwa wamedharau utakatifu wa jina lake, wakavunja sheria zake na kutesa watumishi wake. Vivyo hivyo, sasa karibu Mungu afikilize kwa haki hukumu juu ya taratibu hii mbovu ya mambo kwa mara nyingine aonyeshe kwamba mambo yote yaliyoandikwa katika unabii wa Biblia yanatimia bila shaka lo lote. Nayo hukumu itakuja kwa mfyatuko wenye kugutusha wale wasiokuwa tayari, kwa maana Biblia inasema: “Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.”—1 Wathesalonike 5:2, 3, NW
2. Neno la Mungu linatupa shauri gani tunaloweza kulitumia lihusu wakati ujao ulio karibu?
2 Kati ya wakati wa sasa na wakati ambao Mungu atamaliza hukumu zake, ni lazima watumishi wa Yehova waendelee kuwa macho sana na kujibidiisha kweli kweli. Mtume Paulo, ambaye ndiye aliyeandika unabii ulioongozwa na Mungu kwenye 1 Wathesalonike 5:2, 3, alisema hivi pia. “Kwa hiyo, basi, acheni sisi tusilale kama wale wengine wote wafanyavyo, bali acheni sisi tukae tukikesha na kubaki tukiwa na fahamu zetu.” (1 Wathesalonike 5:6, NW) Yesu alishauri hivi: “Endeleeni kukesha, basi, wakati wote mkifanya dua ili ninyi mpate kufaulu katika kuyakimbia mambo haya ambayo yamekusudiwa yatukie.” (Luka 21:36, NW) Naye mtume Petro aliandika ivyo hivyo: “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, nyinyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa.”—2 Petro 3:11, NW.
KUMJIA YEHOVA SASA
3. Ili mtu ye yote aokoke na kuingia katika taratibu mpya ya Mungu, lazima afanye nini?
3 Mtu ye yote anayetaka aokoke na kuingia ndani ya taratibu mpya ya Mungu yenye haki anahitajiwa haraka sana aingie katika uhusiano unaofaa pamoja na Yehova ha tengenezo Lake la kidunia sasa. “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” (Mithali 18:10) “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi.” (Isaya 2:2) Ndiyo, watu wo wote wa mataifa wanaotaka waishi katika taratibu mpya ya Mungu yenye mfano wa paradiso lazima wamiminikie mlima wa Yehova sasa, yaani, ibada safi yake, ambayo imeimarishwa sana na kuinuliwa juu ya namna nyingineyo yote ya ibada.
4. Yesu anaonyeshaje kwamba kungoja muda mrefu mno ndipo mtu aamue kumjia Yehova kungeweza kuleta msiba?
4 Kwa nini kuna haraka nyingi ya kuijia ibada ya kweli ya Yehova sasa? Je! kwani mtu mwenye moyo mnyofu hawezi kungoja mpaka aone mwanzo wa ufikilizaji wa hukumu za Yehova, na hapo ndipo aje upesi kwenye upande Wake? Ingawa huenda jambo hilo likapendeza watu wengine, je! unadhani wakati huo kungekuwa na wakati wa kutosha kukuza uhusiano unaofaa pamoja na Yehova? Ushuhuda unaotokana na Maandiko unajibu, Hapana. Yesu alionya hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima.” (Luka 21:34, 35) Ona hapo kwamba wale wasiokuwa wamekesha kiroho wananaswa bila kujua, kwa maana “siku” hiyo inawajilia ‘kwa ghafula,’ “papo kwa hapo,” sawa na vile ule ‘uharibifu wa ghafula utakavyokuja papo kwa hapo’ juu ya wale wanaosema “Amani na usalama!”
5. Ni mifano gani ya Biblia tuliyo nayo kuonyesha kwamba watu wanahitaji kujifunza habari za Yehova kabla ya uharibifu kuanza?
5 Yesu alifananisha watu wa namna hiyo na mnyama anayejiingiza mtegoni bila kujua neno. Aliwafananisha pia watu wasiojua neno kwa njia ya kiroho na wale wa siku za Noa ambao ‘hawakutambua, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.’ Je! watu hao walikuwa na wakati wo wote wa kujifunza habari za Yehova na kuja chini ya ulinzi wake baada ya Gharika kuanza? Hapana, kwa sababu Yesu anasema wazi kwamba Gharika ilipokuja ‘iliwachukua wote.’ Ilipokuja hawakuwa wamekwisha kuingia ndani ya safina ya ulinzi pamoja na Noa na jamaa yake. Pia, wakati hukumu ya Mungu ilipokuja juu ya Sodoma na Gomora, je! watu wo wote waliokoka baada ya uharibifu wa moto kuanza kuwanyea kutoka mbinguni? Hapana, kwa maana wote waliharibiwa isipokuwa Loti na binti zake, waliokuwa wamekwisha kuondoka huko. Hata mkewe Loti, ambaye alikuwa amekwisha kuanza kuondoka lakini akaanza kusita-sita, alimalizwa na zile nguvu za uharibifu. Basi Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kusema: “Mkumbukeni mkewe Lutu.”—Mathayo 24:37-39; Luka 17:32.
6. Ushuhuda mwingi ulio katika Maandiko unapinga imani gani?
6 Hata hivyo, je! huenda kukawa na kipindi fulani baada ya ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kubomokea chini, ambapo watu wataweza kupata nafasi ya kuamka kiroho na kumtafuta Yehova? Kuna ushuhuda mzito katika Maandiko wa kuonyesha sivyo. Kuongezea mifano iliyotangulia kutolewa, kuna mfano mwingine wa taifa la Kiyahudi la karne ya kwanza. Wayahudi hao wa kidini walijisikia kwamba walikuwa wakimwabudu Mungu kwa njia ya kutosha na kwamba haikuwa lazima wasikilize mahubiri ya Yesu wala ya wafuasi wake. Walakini, Yesu alikuwa amekwisha kuonya hivi: “Hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia. Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje.” (Luka 21:20-22) Lakini wakati majeshi ya Kirumi yaliyokuwa yameuzingira Yerusalemu yalipoondoka mwaka wa 66 W.K., Wayahudi wenye kujitumaini kupita kiasi ‘hawakuanza kukimbia.’ Wayahudi hawakuona uhitaji wa kukimbia kwa maana jeshi la Kirumi lilipoondoka wao walilifuata na kushambulia kikosi cha upande wa nyuma. Waliamini kwamba Mungu alikuwa pamoja nao, hata wakatengeneza sarafu ya fedha yenye maandishi ya kusema “Yerusalemu ule Mtakatifu.” Lakini unabii wa Yesu ulioongozwa na Mungu ulionyesha kwamba Yerusalemu haukuwa mtakatifu tena kwa Yehova.
7. Ni msiba gani uliowapata Wayahudi waliotenda kinyume cha shauri la Yesu?
7 Kwa kudanganywa na dini ya uongo, Wayahudi hawakuondoka Yerusalemu na Yudea walipopata nafasi ya kufanya hivyo. Kwa kweli, katika masika ya mwaka wa 70 W.K. walitenda kinyume chenyewe! Waliuingia Yerusalemu makundi makundi washerehekee sikukuu ya kidini. Lakini muda huo huo, majeshi hodari ya Kirumi yakiongozwa na Jemadari Tito yalirudi, yakauzingira Yerusalemu na kuwatega mtegoni watu hao hao, wakiwa kama wanyama walionaswa mitegoni. Baada ya mazingiwa mafupi, Yerusalemu uliharibiwa. Mtu aliyejionea mwenyewe matukio hayo, yaani, mwanahistoria Flavio Yosefo, aliandika hivi: “Sasa hesabu ya wale waliopelekwa wakiwa mateka wakati wa vita yote hiyo ilijumlishwa ikawa tisini na saba elfu; na hesabu ya wale walioangamia wakati wa mazingiwa yote ikawa milioni moja na mia moja elfu [1,100,000], na hesabu kubwa kati yao walikuwa wa taifa lile lile [pamoja na raia za Yerusalemu], lakini wasiokuwa wa mji wenyewe; kwa maana walikuwa wametoka sehemu zote za nchi waje kuhudhuria karamu ya mkate usiotiwa chachu, nao walifungiwa kwa ghafula na jeshi fulani, . . . sasa taifa zima likawa limefungiwa na msiba mbaya kama kwamba lilikuwa gerezani, nalo jeshi la Kirumi likauzunguka mji kabisa.”—Wars of the Jews, Kitabu cha 6, Sura ya 9, mafungu 3, 4, kilichotafsiriwa na William Whiston.
8. Ilikuwaje kwa Wakristo waliomsikiliza Yesu, tofauti na wale waliojaribu kukimbia dakika ya mwisho?
8 Walakini, Wakristo waliokuwa wamebaki katika kukesha na kubaki wakiwa na fahamu zao walikuwa wamekwisha kuondoka Yerusalemu na Yudea yote, wakawa wamekimbilia mahali mbalimbali pa usalama wakati nafasi ilipotokea baada ya mwaka wa 66 W.K. Kwa sababu ya kuyaamini maneno ya Yesu ya unabii na kuyafuata, waliokoka. Lakini, wakati ile “dhiki kubwa” ilipowajia Wayahudi mwaka wa 70 W.K., sasa hakukuwa tena na wakati wao wa kukimbia. Elfu kadha waliojaribu kuondoka mjini kupitia sehemu iliyozingirwa na Warumi walikamatwa na askari, hata askari hao wakafikia hatua ya kupasua wazi matumbo ya Wayahudi hao ili waitoe dhahabu ambayo wengi wao walikuwa wamemeza.
KUIOKOKA “DHIKI KUBWA” ILIYO KALI ZAIDI
9, 10. (a) “Dhiki kubwa” itakuwa kali kadiri gani? (b) Kwa nini haionekani kwamba kutakuwa na kipindi chenye utulivu baada ya uharibifu wa ‘Babeli Mkuu’?
9 Hakika hiyo ilikuwa ‘dhiki” kali iliyowajia Wayahudi, sawasawa na vile Yesu alivyokuwa ametabiri. (Luka 19:43, 44) Hata hivyo maneno ya Yesu yalionyesha kwamba “dhiki” iliyo kubwa kuliko hiyo ingekuja wakati wetu, wakati wa “siku ya kisasi” cha Yehova. Akijibu swali fulani juu ya “ishara” ya “kuwapo” kwake, Kristo alitamka hivi: “Kwa maana wakati huo kutakuwako dhiki kuu ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:3, 21, NW) Si ‘Babeli Mkuu’ peke yake atakayepatwa na “dhiki” hiyo, bali pia taratibu yote ya Shetani, kutia na mipango yayo ya kisiasa, ya kijamii na ya kiuchumi.
10 Ingawa uharibifu utaanza ‘kwa ghafula’ kwenye dini ya uongo, utasonga mbele ukiwa na ukali mwingi mpaka ukamalizike bila kukwama. (1 Wathesalonike 5:3) Unabii wa Biblia unapinga wazo la kwamba kutakuwa na kipindi cha utulivu baada ya kupinduliwa kwa ‘Babeli Mkuu’ kwa kuonyesha kwamba majeshi yenye kumpinga Mungu yatakayomharibu ‘Babeli Mkuu’ hayatapendelea hata mashahidi walio wakf wa Yehova. Badala yake, majeshi hayo yatachukia watu wa Mungu na kuwageuka wao pia ili kuwashambulia. Biblia inaonyesha kwamba yule yule ‘mnyama-mwitu mwenye pembe kumi’ aliyeharibu sehemu zote za ‘Babeli Mkuu’ ‘atapigana pia na Mwana-Kondoo,’ Yesu Kristo, kwa kuwajia wafuasi wake wanaomwakilisha yeye duniani. (Ufunuo 13:1; 17:12-14, 16;19: 19) Pasipo shaka washindi hao wenye kuwaka joto la ushindi watawachukua watumishi wa Mungu kuwa dini ya namna nyingine tu isiyokuwa tofauti na zile nyingine. Basi wataiona kuwa dini inayopasa kufagiliwa mbali kusiwe tena na kizuizi cho chote cha kuwafanya wasiitawale dunia nzima.—Ezekieli 38:14-16.
11. “Dhiki kubwa” itafikiaje upeo wayo?
11 Walakini, shambulio hilo litakalofanywa juu ya watumishi wa Mungu litakuwa sawa na kushambulia Mungu, kwa maana yeye anasema: “Yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho” langu. (Zekaria 2:8; Ezekieli 38:18, 19) Tendo hilo litamfyatusha Yehova. Litaichokoza hasira yake yenye kuleta Har–Magedoni iwajilie washambuliaji hao. (Ufunuo 16:14, 16) Yeye ndipo atakapomwamuru Mwanawe Mfalme, Kristo Yesu, na majeshi yake ya kimbinguni wasonge mbele wakashambulie! Kristo na majeshi yake ya kimbinguni atawabomoshea chini kwa nguvu nyingi wafalme wa dunia na watu wengine wote waliobaki wa taratibu hii isiyomcha Mungu, na vilevile kila mtu anayeiunga mkono. Akipiga kelele kwa sauti kubwa, malaika mmoja anawakaribisha ndege wa mbingu waje na kuwaambia: “Njooni! Kusanyikeni pamoja kwa karamu kuu ya Mungu. Njooni mkaitafune miili ya wafalme, ya majemadari, ya watu wenye nguvu, ya farasi na wapanda farasi wao; njooni mkaitafune miili ya watu wote walio huru na watumwa, wadogo na wakubwa.” (Ufunuo 19:17, 18, HNWW) Hivyo ndivyo “dhiki kubwa” itakavyofikia upeo wayo. “Siku ya kisasi” cha Mungu chenye haki ndipo itakapomalizika kwa kuijilia taratibu hii ya mambo ya Kishetani.
12. Ni wakati gani inapowapasa watu wenye mioyo minyofu ‘wamtafute Yehova’?
12 Tangu mwanzo wa ule “uharibifu wa ghafula,” unaoanza na kuharibiwa kwa sehemu zote za ‘Babeli Mkuu,’ mpaka kwenye shambulio la mataifa juu ya watumishi wa Yehova na kuendelea mpaka kwenye vita ya Mungu ya Har—Magedoni, hakuonekani kwamba “dhiki kubwa” itaacha kuwapo kwa muda fulani. Kwa hiyo hakuna sababu yo yote ya Kimaandiko ya kukata kauli kwamba kutakuwa na wakati wa kutosha watu wamgeukie Mungu baada ya dini ya uongo kuharibiwa. Badala ya hivyo, wale wanaotaka kuokoka wakiwa hai wakaingie ndani ya taratibu mpya ya Mungu wanapaswa wamgeukie Yehova sasa. “Mtafuteni [Yehova], maadamu anapatikana, mwiteni maadamu yu karibu.” (Isaya 55:6) Wakati wa sasa ndipo watu wenye mioyo minyofu wanapopaswa kukuza maisha zenye imani, ushujaa, upendo utumishi. Sasa ndipo wanapohitajiwa wajitayarishe kuivumilia mikazo itakayowajia watu wa Mungu wakati wa “dhiki kubwa” inayokaribia kasi-kasi.
13. Watumishi waaminifu wa Mungu wanafananishwa na nini, na kwa njia gani mbalimbali?
13 Neno la Mungu linafananisha watumishi wake waaminifu na askari waliozoezwa vizuri ambao wanasikiliza wanaposemeshwa, waliovaa nguo za vitani za kujikinga, na walio tayari kutii amri yo yote wanayopewa na kiongozi wao. Wao si kama askari wasiokuwa tayari wenye kulala kwenye makao yao wakati wa hatari na haraka. Paulo anasema hivi: “Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi. Maana walalao usingizi hulala usiku, pia na walewao hulewa usiku. Lakini sisi tulio wa mchana, tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani [dirii ya] imani na upendo, na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu. Kwa kuwa Mungu hakutuweka kwa hasira yake, bali tupate wokovu, kwa Bwana wetu Yesu Kristo.”—1 Wathesalonike 5:6-9.
14. Ni nini kinachoonyesha kwamba watumishi wa Mungu watakuwa wamepashwa habari ili wafanye mapenzi ya Mungu?
14 Pia, watumishi wa Mungu wanaamini kabisa kwamba yeye atazidi kulipasha tengenezo lake habari linazohitaji, ili waweze kuchukua hatua zifaazo za kuokokea. Tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hilo kwa sababu unabii ulioongozwa na Mungu ulio kwenye Ufunuo, sura ya saba, unaonyesha kwamba “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, . . . wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu” na kuokoka waingie ndani ya taratibu mpya ya Mungu. (Ufunuo 7:9, 14) Na kwa nini “mkutano mkubwa sana” unaokoka? Ni kwa sababu ‘wanamtolea Mungu utumishi mtakatifu mchana na usiku na kwa hiyo yeye ‘anatanda hema yake juu yao.’ (Ufunuo 7:15, NW) Kwa kuwa wamepashwa habari za kuwatosha, wanajua namna ya kutumikia Mungu kwa njia inayokubaliwa. Wao hawajikalii kitako tu wakingoja waone ni jambo gani litakalotukia. Wanajua kwamba yeye “afanyaye mapenzi ya Mungu” ndiye “adumu hata milele.”—1 Yohana 2:17.
UTENDAJI ULIOONGEZEKA
15. Mashahidi wa Yehova wameitii amri ya ‘kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu katika dunia yote inayokaliwa na watu’ kwa njia gani?
15 Utimizo ufuatao wa unabii wa Yesu ni sehemu ya mapenzi ya Mungu anayotaka yatendeke siku zetu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Maneno hayo ya unabii ni amri kwa Wakristo wa kweli waambie watu wale wengine habari njema za ufalme wa Mungu na taratibu mpya inayokuja. Na kwa uhakika Mashahidi wa Yehova wameitii amri hiyo katika hizi “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1; linganisha Mathayo 28:19, 20.) Wamekuwa bila uchoyo wakatumia wakati na mali zao kufundisha wengine habari za kusudi zuri sana la Mungu kwa dunia hii. Kwa sababu ya bidii nyingi hiyo, watu zaidi ya milioni tano ulimwenguni pote walionyesha wangependa kuwa katika taratibu mpya ya Mungu na kujifaidi kwa msaada wa wokovu alioutoa kupitia Yesu Kristo kwa kukutana pamoja Aprili iliyopita kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.
16, 17. (a) Ni maagizo gani liliyopewa taifa la Israeli kabla Mungu hajauharibu mji wa Yeriko? (b) Maagizo hayo yalifuatwaje?
16 Tengenezo la Yehova lenye kusonga mbele lizidipo kuikaribia miaka ya mwisho-mwisho ya utendaji walo wa kuuhubiri ulimwengu, hakuna shaka kwamba ukubwa wa kazi utaongezeka. Ebu kumbuka jambo ambalo Waisraeli waliagizwa wafanye muda mfupi tu kabla ya Mungu kuharibu mji wa Yeriko. Kwanza, waliagizwa wapige miguu kuuzunguka mji mara moja kila siku kwa muda wa siku sita. Lakini ndipo walipoambiwa: “Siku ya saba mtauzunguka mji mara saba, nao makuhani watapiga tarumbeta zao. Kisha itakuwa watakapopiga hizo pembe za kondoo waume kwa nguvu, nanyi mtakaposikia sauti ya tarumbeta, watu wote watapiga kelele [ya kivita] kwa sauti kuu; na ukuta wa mji utaanguka chini pale pale.”—Yoshua 6:2-5.
17 Siku hiyo iliyokuwa ya saba na ya mwisho, Waisraeli walipaswa kuongeza utendaji wao mara saba! Kisha walipaswa ‘kupiga kelele ya kivita kwa sauti kuu.’ Waliyafuata barabara yale waliyoagizwa. “Ikawa siku ya saba wakaondoka asubuhi na mapema wakati wa mapambazuko, wakauzunguka mji vivyo hivyo mara saba . . . Hata mara ya saba makuhani walipozipiga tarumbeta, Yoshua akawaambia watu, Pigeni kelele; kwa maana [Yehova] amewapeni mji huu. . . . Hata ikawa, hapo watu waliposikia sauti ya tarumbeta hao watu wakapiga kelele [ya kivita] kwa sauti kuu sana, na ule ukuta wa mji ukaanguka chini kabisa.”—Yoshua 6:15, 16, 20.
18. Tunatazamia nini kuhusu ukubwa na namna ya utendaji wa kuhubiri utakaofanywa kabla ya taratibu hii kufikia mwisho wayo?
18 Tunaweza kutazamia mpanuko wa namna iyo hiyo katika utendaji wetu wa kuhubiri sasa, kwenye upeo huu wa vizazi vyote. Bila shaka, kabla “dhiki kubwa” haijamalizika, tutaona ushuhuda ulio mkubwa kuliko shuhuda zote zilizopata kuwapo katika historia ya ulimwengu huu ukitolewa kuhusu jina la Mungu na ufalme wake. Na ingawa sasa ushuhuda bado unatoa ule ukaribishaji wa kulijia tengenezo la Yehova ili kupata wokovu, bila shaka wakati utafika ambapo ujumbe utakuwa wenye mambo makali zaidi, kama ‘kelele ya kivita ya sauti kuu.’ Ufunuo 16: 21 unaonyesha kwamba “mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta [kila jiwe likiwa na uzito wa karibu talanta moja, NW, karibu ratili 100], ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno.” Mawe-barafu ni maji yaliyoganda, maji ambayo yamekuwa magumu. Kwa hiyo jambo hilo linafananisha namna ujumbe wa hukumu ya Yehova itakayoletwa mwishowe juu ya wanadamu wasiotii utakavyokuwa kama mawe-barafu yenye kupiga watu kwa nguvu nyingi huku yakimiminika kweli kweli. Kwa kuwa pigo la mawe-barafu linatajwa kuwa “kubwa mno,” hiyo inaonyesha kwamba mwishoni-mwishoni kabisa “siku ya kisasi” cha Yehova itatangazwa kwa nguvu nyingi na watumishi wa Yehova.
19. Kwa sababu ya mambo yatakayotukia wakati ujao ulio karibu, ‘inatupasa tuwe watu wa namna gani?
19 Basi, inatufaa tuseme kama Petro, ya kwamba, “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa”! (2 Petro 3: 11, NW) Kwa kweli tunahitaji ‘kuendelea kufarijiana na kujengana kila mtu na mwenzake.’ Inatupasa ‘sikuzote tulifuate lililo jema kati ya sisi kwa sisi.’ (1 Wathesalonike 5:11, 15) “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Kwa kusudi hilo, usikose ‘kukaa ukiwa umekesha na kubaki ukiwa na fahamu zako.’—1 Wathesalonike 5:6, NW.—Kutoka The Watchtower, November 15 1981.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Watu wo wote wanaotaka waokoke na kuingia ndani ya taratibu mpya ya Mungu lazima waimiminikie ibada ya kweli ya Yehova sasa
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wakristo waliomtii Yesu waliukimbia Yerusalemu bila kuchelewa, wakawa hawawezi kupatwa na msiba wa mji huo mwaka wa 70 W.K.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Neno la Mungu linafananisha watumishi wake na askari waliozoezwa vizuri ambao wana silaha za kujikinga mwili na ambao wako tayari kutii
[Picha katika ukurasa wa 20, 21]
Wakati Waisraeli walipoanza ‘kupiga kelele ya kivita kwa sauti kuu,’ kuta za Yeriko zilianguka