Kumwamini Mwana wa Mungu Kukuhusuje Wewe?
“Mwenendo wenu uwe kama inavyopasa habari njema ya Kristo . . . [Mukisimama] imara katika roho moja, kwa moyo mumoja Mukishindana kwa imani ya habari njema.”—Flp. 1:27, ZSB.
1. (a) Ni kazi gani inayokaribia upeo wake sasa? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba kwa kweli imani inapatikana duniani leo?
UNABII uliotimizwa unaonyesha kwamba tumekwisha kuingia sana katika wakati wa “mwisho wa taratibu ya mambo.”. (Mt. 28:20, NW) Sasa miaka 64 tangu “Mwana wa Adamu,” Yesu Kristo, alipofika pamoja na malaika zake wote ‘kuketi katika kiti chake cha mbinguni cha utukufu wake.’ Kuhukumu na kutenganisha Watu walio “kondoo” wenye kujaa imani na “mbuzi” wasio na imani kunakaribia upeo wake. (Mt. 25:31-33) Kwa hiyo twauliza, Je! kweli “Mwana wa Adamu” amekuta imani ishindayo duniani? Mkusanyiko wa kundi la mataifa yote la Mashahidi wa Yehova—hesabu yao ikiwa zaidi ya milioni 2—washuhudia waziwazi kwamba amekuta.
2. Kwa sababu gani makusanyiko ya watu wa Mungu yameelezwa kwa kufaa kuwa ‘kitu kisichoonekana katika ulimwengu huu’?
2 Magazeti na njia nyinginezo za kutangazia habari yameyaeleza makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova kuwa ‘kitu kisichoonekana hata kidogo katika ulimwengu huu.’ Nayo yapasa kuwa kitu cha pekee kabisa! Kwa maana watu wa Mungu wanajitahidi wakijaribu kuwa bora kabisa. Kwa kweli, kundi hilo kubwa sana liko katika safari ya kuuacha ulimwengu wa sasa usio mkamilifu kuelekea kwenye “taratibu mpya” ambako hakutakuwa tena na magonjwa, kifo wala huzuni. Neno ya Yehova linatuhakikishia hilo! (Ufu. 21:1-4) Ili tufikie mradi huo tunahitaji kushikamana sana na ushindi wetu wa kutumia imani. Tutafanya hivyo?
HUKUMU YA ULIMWENGU YAANZA
3. Ni mabadiliko gani yaliyotukia katika mwaka 1914, yakionyesha nini?
3 Wakati “mwisho wa taratibu ya mambo” ulipoanza mwaka 1914, mabadiliko makubwa sana yalianza kutukia juu ya dunia hii. Ilikuwa sawa na vile Yesu mwenyewe alivyokuwa ametabiri—vita vya ulimwengu, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, njaa kuu, kuongezeka kwa ukosefu wa kutojali sheria na kupotea kwa upendo. (Mt. 24:3-12, NW; Luka 21:10, 11, NW) Wakati wa hukumu ya ulimwengu ulikuwa umeanza.
4, 5. (a) Dini za Jumuiya ya Wakristo zimeonyeshaje ukosefu wa imani? (b) Dini hizi zimetofautianaje na Mashahidi wa Yehova kwa habari ya uhusiano na ulimwengu huu? (c) Imani yetu isiyoshindika inaonyeshwaje?
4 Dini za Jumuiya ya Wakristo zingeionaje hali hiyo? Je! zingeonyesha “Imani duniani”? (Luka 18:8) Hata kidogo! Badala ya kuikubali “ishara” kwamba ufalme wa Mungu umekaribia, viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo waliunga mkono “taratibu ya mambo” yenye kufa. Vita ya ulimwengu ilipoipata Ulaya yote, makanisa ya pande zote mbili yalihimiza Wakristo wachinje Wakristo wenzao, kwa njia hiyo yakawa na hatia kubwa ya damu. Nayo vita ilipoamalizika, dini za Jumuiya ya Wakristo hazikumchagua mfalme anayetawala sasa, Yesu Kristo, bali baraza ya kisiasa ya kibinadamu walioibandika kwa makufuru jina “wonyesho wa Ufalme wa Mungu duniani.” Baraza hiyo ilikuwa ni Ushirikia wa Mataifa, iliyotokezwa mwaka 1919 kwa kusudi lililotangazwa la “kuufanya ulimwengu salama kwa ajili ya demokrasi.” Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinaueleza kuwa “mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru.”—Ufu. 17:3.
5 Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yameonyesha wazi msimamo wao, kwamba ni sehemu ya ulimwengu huu, kwa kuunga mkono vita vya jumla, halafu yakaunga mkono chombo hicho cha kibinadamu. Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova wameonyesha kwa njia isiyoleta shaka lo lote kwamba wao si “sehemu ya ulimwengu,” kwa kuchukua msimamo wa kutokuwamo katika jeuri kati ya mataifa na siasa. (Yohana 15:19 NW) Imani yetu haitegemei kinga za kimwili wala silaha za vita za wanadamu wenye kufa. Bali imani yetu isiyoshindika inamkubali “Mungu [kama mtawala] kuliko wanadamu.” Na kwa sababu sisi ‘tunamtii Mungu kama mtawala’ kwa kutoa ushuhuda kuhusu makusudi yake ya ufalme, tunaonyesha kwamba tuna roho ya Mungu. (Matendo 5:29-32; 1 Kor. 12:3) Hivyo tumetiwa nguvu tuzifanye kazi alizozitaja Yesu: “Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya”—katika kuuhubiri duniani pote ufalme uliosimamishwa.—Yohana 14:12.
6. Ushuhuda wa kuwako kwa roho takatifu umekuwa ukionekanaje tangu 1919?
6 Roho takatifu hiyo ya Yehova ilionekana sana kuwapo kwenye makusanyiko ya mataifa yote ya Mashahidi wa Yehova yaliyofanywa Cedar Point, Ohio, U.S.A., miaka 1919 na 1922. Iliitia nguvu imani ya mabaki machache ya Wakristo watiwa mafuta na kuwapa nguvu za kuujibu mwito huu: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Kwa jitihada wakaendelea kuzihubiri “habari njema” kote kote. Wakati wa kutokea vita ya ulimwengu ya pili yenye ukali mwingi, hesabu yao ilikuwa imeongezeka kutoka maelfu fulani kufikia zaidi ya 67,000, wenye kuhubiri katika nchi mbalimbali za dunia.
IMANI YASHINDA MATESO
7. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba imani Inashinda mateso?
7 Mpanuko huo haukufanywa bila ya kutokea mateso makali. Kwa mfano, sababu mashahidi wa Yehova wenye kushika ukamilifu walikataa kuiabudu serikali ya Nazi, waliwindwa na kusukumiwa kwa wingi katika kambi chafu-chafu za mateso, ambako zaidi ya 600 walikufa kwa ukosefu wa chakula kinachofaa au kwa kutendwa ukatili uliokuwamo. Lakini imani yao haikuweza kuvunjwa. Mtazamaji mmoja alieleza habari za Shahidi mmoja akasema alikuwa “ngome iwezayo kuharibiwa lakini isiyoweza kutekwa hata kidogo.” Ni kama vile mtu aliyejionea mwenyewe alivyoeleza kuhusu ndugu yake mwenyewe aliyepigwa risasi bila huruma na walinzi Wa SS wa Nazi akiuawa mbele ya watu: “Kila mtu alishangazwa na utulivu na unyamavu wake, akiwa kama mtu aliyekuwa ameshinda tayari.”
8. (a) Katika wakati wa miaka yenye kujaribu ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, imani ya Kikristo ilifanikiwaje? (b) Lakini viongozi wa dini walibariki na kutukuza kitu gani?
8 Kama ilivyokwisha kusemwa, Mashahidi wa Yehova waliianza miaka yenye magumu ya vita ya ulimwengu ya pili hesabu yao ikiwa yapata 67,000, lakini walitokea katika pigano hilo wakiwa 141,000. Marufuku, vifungo na majaribu mengine ya ukamilifu hayakuwafanya waiache imani yao kwa woga. Walakini, dini za Jumuiya ya Wakristo ziliyabariki mateso na machinjo waliyotendwa. Na ingawa yule “mnyama mwekundu sana” aliye Ushirika wa Mataifa alishindwa kuwasaidia viongozi wa dini, wao walifanya haraka’ wakamshangilia tena alipotokea akiwa Umoja wa Mataifa. Walifanya werevu waweze kumpanda waendeshwe naye. Wakati wa ziara yake kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa katika New York mwaka 1965, Papa Paulo wa Sita aliitukuza baraza hiyo kuwa “lile tengenezo lililo kubwa ,kuliko matengenezo yote ya mataifa” na “tumaini la mwisho la mapatano na amani.”
USHINDI UNAOENDELEA KWA KUTUMIA IMANI
9. (a) Ni habari gani ya wakati uliofaa iliyotolewa na Mashahidi wa Yehova katika mwaka 1942? (b) Basi, watu wa Mungu waliendeleaje kusonga mbele katika ushindi wao?
9 Mwaka 1942 wakati mataifa yenye mwungano yalipopendekeza mara ya kwanza Umoja wa Mataifa uanzwe, Mashahidi wa Yehova walitangaza kwenye kusanyiko lao la mataifa yote mwaka huo kwamba kufanya hivyo kungekuwa ni kuutengeneza Ushirikia upya kwa kuutia viraka. Walionyesha katika Neno la Mungu kwamba lazima mwishowe Umoja wa Mataifa umalizikie mbali kwa kuharibiwa, pamoja na matengenezo mengine yote ya kisiasa, katika pigano la mwisho kwenye Har–Magedoni. Kwa kuzungukwa na ushuhuda mwingi wenye kuonyesha wanaishi katika “wakati wa mwisho,” (Dan. 11:35) watu wa Yehova walisonga mbele katika ushindi wao wa kutumia imani. Shule ya Gileadi ilitayarishwa, wamisionari wakatumwa kwenda kwenye miisho yenyewe ya dunia. Matokeo yakawaje? Ijapokuwa mwaka 1945 walikuwako wahubiri wa Ufalme 141,606 wenye bidii katika nchi 66, mwaka 1978 walikuwako 2,182,341 wenye kuripoti utumishi katika nchi 205. Ushindi wa kutumia imani umekuwa wazi sana, na sana sana katika zile nchi 46 ambako Mashahidi wa Yehova wanatumikia sasa wakiwa chini ya marufuku au vizuizi vingine.
10. Ubora uliojaribiwa wa imani umeonyeshawaje katika Malawi na katika nchi nyingine chini ya vizuizi?
10 Nchi mojawapo ambako jaribu la imani limekuwa gumu sana ni lile taifa dogo la Afrika la Malawi. Kufikia mwaka 1962, Mashahidi wa Yehova walifurahia ongezeko la haraka katika nchi hiyo. Lakini mwaka 1964 kukatokea mateso makali sana. Kwa sababu Mashahidi wa Yehova walikataa kukiabudu kisehemu cha Malawi cha yule ‘mnyama aliyetoka baharini’ (Ufu. 13:1, 4) kwa kununua vipande vya ushirika wa chama cha kisiasa, walikwenda kuwindwa nyumbani kwao, wengi wakalalwa kwa nguvu na kuuawa. Mwishowe wengi wao walifukuzwa waiache nchi ya kwao. Lakini sifa iliyojaribiwa ya imani yao, iliyojaribiwa kana kwamba kwa moto, imewaletea furaha, si wao wenyewe tu bali pia na ndugu zao Wakristo katika dunia yote. (1 Pet. 1:7, NW) Katika nchi zote ambako Mashahidi wa Yehova wanalazimika kutumikia kwa siri, sifa iyo hiyo halisi ya imani inaonekana. Mashahidi hao wote, ambao ni zaidi ya 200,000 katika nchi hizo, wanafaulu sana katika ushindi wao wa kutumia imani.
11. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba lazima tuvumilie katika ushindi wetu wa kutumia imani?
11 Walakini, namna gani Mashahidi wa Yehova katika nchi ambako mambo si magumu sana, ambako hatulazimiki kuishi daima tukiwa katika hatari ya kukamatwa, kufungwa au kuuawa? Linalohuzunisha ni kwamba, baadhi ya sehemu hizo zimekuwa haziendelei vizuri sana. Hizo ni pamoja na nchi nyingi zenye ufanisi, ambako kuna anasa na ufisadi tele. Lakini hakuna sehemu yo yote inayopasa kusahau jambo hili: Lazima tuvumilie katika ushindi wetu wa kutumia imani mpaka tutakapoachishwa na taratibu hii mbovu ya mambo, iwe ni kupitia kwa kifo au kwa kuiokoka “dhiki kubwa.”
12. Ni maneno gani ya unabii wa Yesu tunayopaswa kuangalia sana leo, na kwa sababu gani?
12 Ni jambo la haraka sana wote wawe na ufahamu huo ulio wazi! Ushuhuda u wazi kila upande kwamba ulimwengu unajikokota kwenye ukingo wa uharibifu. “Siku za mwisho” ni kama zimefikia kikomo. Kwa hiyo maneno ya kumalizia unabii wa Yesu juu ya mwisho wa taratibu ya mambo yanapasa yasikike wazi na kuwashtua watu wote wa Yehova leo: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajilia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.” —Luka 21:34-36.
“WAKATI ULIOAMRIWA” WAKARIBIA
13. Sababu gani ni jambo la muhimu tuendelee kuitazamia siku ya hukumu ya Yehova?
13 Ingawa labda “dhiki kubwa” haikuja upesi kama wengi wetu tulivyokuwa tumetazamia, hiyo si sababu ya kutuvunja moyo. Mungu hageuki. (Mal. 3:6) Wala makusudi yake matukufu hayajageuka. Yehova anasema hivi kuhusu “habari njema” tunazozihubiri: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isa. 55:11) Wakati wa Mungu kuleta hukumu haujasongea mbele. Unakaribia zaidi kila siku ipitapo. Kwa hiyo acheni tuyakumbuke maneno ya Isaya 30:18: “[Yehova] ni Mungu wa hukumu; heri wote wamngojao.”
14. (a) Ni kushikilia uhakika gani kutatuwezesha sisi mwishowe tuyafanye maneno ya Yoshua yawe yetu sisi wenyewe? (b) Ni kitia-moyo gani tunachoweza kupata katika unabii wa Habakuki?
14 Linalotuwezesha kupata ushindi wa imani si kutegemea kipindi fulani cha wakati, bali ni kumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote kama Mungu “asiyeweza kusema uongo.”(Tito 1:2) Matumaini hayo mwishowe yatatufikisha mahali ambapo, kama Yoshua wa kale, tutaweza kuwaambia wenzi wetu katika huu ushindi wa kutumia imani hivi: “Nyote mnajua mioyoni mwenu, na [nafsini] mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” (Yos. 23:14; 21:45) Tunaweza kuyatumaini kabisa maneno ya Habakuki kwamba “njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake.” Na tuendelee kufanya haraka pamoja na njozi hiyo mpaka ushindi wetu utakapokamilika! Unabii unatuhakikishia hivi: “Haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia [“haitachelewa,NW].”—Hab. 2:3.
‘YEHOVA SI MKAWIVU’
15. (a) Ni kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba ‘Yehova si mkawivu’? (b) Mwishowe siku yake yajaje?
15 Miaka mia kumi na tisa imepita tangu siku za mitume. Lakini machoni pa Mungu muda huo ni mchache kuliko siku mbili. Ni kama vile mtume Petro alivyosema: “Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa [Yehova] siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja. [Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba. Lakini siku ya [Yehova] itakuja kama mwivi”—2 Pet. 3:8-10.
16. Ni kwa sababu gani siku ya Yehova bado haijaja, na kwa sababu hiyo twapaswa kuionaje hali hiyo?
16 Kwa hiyo, namna gani ikiwa katika saa ya Yehova siku yake imepangwa ije baada ya nukta chache kupita? Je! hatufurahi kwamba hiyo imewezesha mamia ya maelfu ya “kondoo” zake zaidi wakusanywe? Wakati saa hiyo inapoendelea kupiga-piga nukta zake, makumi ya maelfu ya watu waliokuwa Wakatoliki katika nchi za kusini za Ulaya wanaumiminikia Ufalme, mamia katika visiwa vya bahari vilivyo peke yake wanaiacha ibada ya sanamu, nayo maelfu ya Waasia wanajitenga na mambo yao ya ushirikina wa Mashariki wazikubali kwa moyo “habari njema.” Sababu ambayo imefanya siku ya Yehova ya kimwizi isifike bado ni kwamba yeye angali ana kazi ya kutupa tuifanye kwa kuyakusanya mavuno. Yehova si mkawivu. Sisi tusiwe wakawivu katika kuishika kila nafasi tushiriki kwa ukamili katika kazi Yake.
17. (a) Ni shauri gani la wakati wake analotoa Petro kwa siku hizi? (b) Ni kitu gani kinachowatambulisha watu wa Yehova, nao wanaionyeshaje imani yao?
17 Mtume Petro anashauri hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote Iweni na juhudi nyingi katika kupendana.” (1 Pet. 4:7, 8) Wakati hii “taratibu ya mambo” iliyo mbovu inapojikakamua ijitahidi mara ya mwisho kuwaangamiza watu wa Mungu, hakika tunahitaji kubaki bila kutiwa msukosuko, tukeshe na kuwa watu wa sala, tukiwa na matumaini hakika katika ushindi wetu wa kutumia imani. Tunahitaji kuwa na umoja katika huo upendo wa juhudi nyingi, ambao ni alama yenye kuwatambulisha watu wa Yehova mwenyewe katika dunia yote. Ni wapi, katika historia yote ya kibinadamu, kumekuwa na watu kama Mashahidi wa Yehova leo? Huu ndio udugu wa pekee ambao umepenya katika pembe za mbali za dunia inayokaliwa na watu. Ni nguvu gani nyingine, isipokuwa roho ya Yehova, ingaliweza kuunganisha watu milioni mbili “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” wawe katika umoja mzuri hivyo wa imani, kusudi na utendaji? Sote pamoja tumeupata ushindi kwa kutumia imani, na sote pamoja tunaonyesha wazi imani hiyo kwa kuutolea ushuhuda ufalme wa Yehova upitiao kwa Mwanawe.—Ufu. 7:9.
18, 19. (a) Katika siku za mitume, matukio yaliendeleaje katika utimizo wa unabii wa Biblia? (b) Huenda wengine wakawa walifanya kosa gani lenye kuhuzunisha?
18 Watu wa Yehova leo ni kama wale Wakristo waaminifu waliongojea kwa bidii utimizo wa kwanza wa ile “ishara” huko nyuma katika Yerusalemu wa siku za mitume. Walikutazamia kuja kwa “chukizo” ambalo lingesimama katika “patakatifu.” Mwishowe, likatukia! Jeshi la Kirumi lilishambulia na kupenya kwenye ukuta wa magharibi wa eneo la hekalu. Sasa Wakristo wafanyeje? Yesu alikuwa amesema: ‘Anzeni kukimbilia milimani.’ Wakati jeshi hilo lilipoondoka isivyotazamiwa, Wakristo hao waliishika nafasi hiyo. Acha wakimbie! Walikwenda kwenye milima ya Perea. Lakini sasa walikuwa wameokoka? Je! ushindi wao wa kutumia imani ulikuwa kamili? Hapana, bado!—Mt. 24:15, 16.
19 Kwa hamu nyingi Wakristo hao walilingojea tukio lile jingine—kuleta kwa Yehova hukumu juu ya Yerusalemu. Walingoja mwaka mmoja. Hakuna lililotokea. Miaka miwili, tena hakuna lililotokea. Miaka mitatu, na bado hakuna lililotokea. Labda baadhi ya Wakristo hao walichoka kungojea. Labda walisema, Na turudie mji tukaingilie biashara na raha ya maisha. Hilo lingalikuwa kosa lenye kusikitisha wee!
20. Wakati huo imani ililetaje wokovu?
20 Kwa maana kwa ghafula, katika mwawa nne, majeshi ya Kirumi yalirudi. Mji na hekalu lake uliharibiwa kiukamili, pasibaki hata jiwe moja juu ya jingine. Ilikuwa sawasawa na vile Yesu alivyokuwa ametabiri. (Luka 19:41-44; 21:20-24) Lakini watu wa Mungu nje ya Yudea walikuwa wameendelea kuwa wenye bidii na kukesha. Walikuwa wamemngojea Yehova. Imani yao ilikuwa imewaletea wokovu.
21. Ni unabii gani wa Biblia wenye kutokeza ulioanza kutimizwa mwaka 1945?
21 Leo, sisi tumo katika hali kama iyo hiyo. Jumuiya ya Wakristo ndiyo ulinganifu wa kisiku-hizi wa mji wa kale wa Yerusalemu usio mwaminifu. “Chukizo” la unabii wa Yesu linatambulishwa wazi na Andiko kuwa ndilo tengenezo la Umoja wa Mataifa leo. Ni kitu kimoja na yule “mnyama mwekundu sana” wa Ufunuo sura ya 17. “Mnyama” huyo alipotoka shimoni mwaka 1945, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, yaani, ‘Babeli Mkuu,’ ambayo Jumuiya ya Wakristo ndiyo sehemu yake kubwa, iliweza kumpanda na kutumia mamlaka fulani.
22. Ni hali gani iliyobadilika inayoweza kuonekana katika Umoja wa Mataifa, ikionyesha nini?
22 Walakini, leo mambo ni tofauti. Mataifa yanayochukua dini kuwa ndiyo “kasumba ya watu” yanazidi kupata uwezo mwingi katika Umoja wa Mataifa. Yako kama tisho kubwa sana kwa makao ya utendaji wa dini za Jumuiya ya Wakristo, ndiyo, la dini zote. Karibuni sana tunaweza kutazamia kuona zile “pembe kumi” za “mnyama” zikizigeukia dini za ulimwengu, na kuyaacha ukiwa hata makao ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo. Hapo ile “dhiki kubwa” itakuwa imekwisha kuanza, nayo itasonga haraka ifikie upeo kwenye Har–Magedoni.
23. (a) Kwa sababu ya hali yenye hatari iliyopo duniani, lazima sisi tufanye nini sasa? (b) Wewe unawezaje kuwa mshindi wa ulimwengu kwa kutumia imani?
23 Kwa kuiona hali hiyo yenye hatari duniani, Mashahidi wa Yehova wafanyeje? Lazima tuhakikishe kwamba tumekamilisha kimbilio letu kwenye “mlima” wa ulinzi ambao ni ufalme wa Mungu. Lazima tuwe watu wasioyumbayumba katika kuufuatia ushindi wa kutumia imani yetu. Lazima tujikaze tuwe washindi kupitia kwa Mungu wetu atupendaye. Maadamu kuna wakati wa kufanya hivyo, lazima tuendelee kushiriki kwa juhudi katika kuzihubiri habari njema hizi za Ufalme katika dunia yote na kufanya wanafunzi. Je! ninyi, pamoja na Mashahidi wa Yehova wote ulimwenguni pote, mtaendelea ‘kusimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili’? (Flp. 1:27) Je! kwa njia hiyo ninyi mtaliadhimisha jina la Yehova na ufalme wa Mwanawe, Yesu Kristo? Mkifanya hivyo, ninyi pia mwaweza kufaulu kwa njia yenye utukufu mkiwa washindi wa ulimwengu kwa kutumia imani. —Kutoka The Watchtower Feb. 15, 1979.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Angalia moyo wako usipate kamwe kulemewa na ulafi na ulevi