‘Kula na Kunywa kwa Utukufu wa Mungu’
YEHOVA Mungu, Muumba wetu, aweza kufikiriwa na apaswa kufikiriwa katika maisha yetu ya kila siku. Onyo la upole lililoongozwa naye laambia Wakristo hivi: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Lakini mtu awezaje kumtukuza Mungu katika kawaida za maisha kama kula na kunywa?
Kwanza, Mkristo hapaswi kuumiza dhamiri za wengine wala kuwakwaza kwa kula au kunywa. Kwa mfano, katika maeneo mengine watu hudharau wale wanaokula nyama za namna fulani au wanaotumia vileo vyo vyote. Mkristo hapaswi kupuza mashaka ya dhamiri za watu wa mtaa anamoishi. Apaswa pia kufikiria sana mashaka ya dhamiri za waamini wenzake. Asingetaka kufanya iwe vigumu zaidi kwa wengine kuikubali ibada ya kweli au kudumisha uaminifu wao kwa Mungu. Ndiyo sababu mtume Paulo alipendekeza hivi: “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.”—Rum. 14:21.
Mkristo anamtukuza Mungu kwa kuepuka kufanya mambo yaliyo haki yake. Kwa njia gani? Anaonyesha anapenda sana na kufikiria sana wanadamu wenzake, akitafuta faida zao, si zake mwenyewe. (1 Kor. 10:24) Kupatana na kusudi la Mungu, yeye huonyesha kwamba maisha yake yote yanategemea kusaidia wengine wakubaliwe na Mungu. Tamaa ya kumtukuza Yehova Mungu humzuia Mkristo pia asile wala kunywa kupita kiasi. Kama angepita kiasi, angepumbaa na kuingiza akili yake usingizini, na vilevile angeacha kutaka kutimiza mambo. Kwa kunywa kupita kiasi angeweza kujidanganya kwa vyepesi. Ni kama vile mithali ya Biblia ielezavyo: “Mvinyo hudhihaki, kileo huleta ugomvi; na akosaye kwa vitu hivyo hana hekima.” (Mit. 20:1) Badala ya kumtukuza Mungu, mtu anayeongozwa na vileo huelekea kufanya kelele-kelele na kusema maneno ya kipumbavu, akitenda mambo kijinga, naye hudharauliwa. Humletea Mungu suto, Yule yule ambaye mtu huyo anadai kwamba anamwakilisha akiwa mtumishi Wake.
Walakini, kiasi katika kula na kunywa ni upande mmoja tu wa sheria ya Mungu inayoongoza mambo hayo. Pengine mtu hali sana wala hanywi sana. Lakini huenda bado akawa hamtukuzi Mungu. Hiyo ni wazi kutokana na maneno ambayo Paulo alimwambia Timotheo: “Roho [yanena] waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe [kama kwa chuma cha kuwekea alama]; . . . na kuwaamuru wajiepushe na vyakula, ambavyo Mungu aliviumba vipokewe kwa shukrani na walio na imani wenye kuijua hiyo kweli. Kwa maana kila kiumbe cha Mungu ni kizuri, wala hakuna cha kukataliwa, kama kikipokewa kwa shukrani; kwa kuwa kimetakaswa kwa neno la Mungu na kwa kuomba.”—1 Tim. 4:1-5.
Angalia kwamba sheria za kidini zinapokataza vyakula fulani, huo unakuwa ushuhuda hasa wa kuanguka kutoka Ukristo wa kweli. Hiyo yamaanisha kwamba watu wanaojidai kuwa Wakristo wakiamuru wengine kwamba wanapaswa kufuata sheria zinazokataza vyakula fulani ndiyo wakubaliwe na Mungu, wanamdharau Mungu. Iweje hivyo? Je! sheria ya Mungu kwa Israeli haikuwakataza wasile vyakula fulani?
Ni kweli kwamba Waisraeli walipewa sheria zilizowakataza kula wanyama fulani wenye kunyonyesha, ndege, wadudu na samaki. (Mambo ya Walawi, sura ya 11) Lakini sheria hizo zilikwisha wakati agano la Torati lilipobadilishwa na agano jipya mwaka 33 W.K. Baadaye, wakati mtume Petro alipokataa kula wanyama waliokuwa wachafu kulingana na sheria ya Musa, huku akiona njozi lakini macho yake yakiwa wazi, aliambiwa hivi: “Vilivyotakaswa na Mungu, usiviite wewe najisi.” (Matendo 10:15) Naam, “neno” la Mungu, ruhusa yake, ilikomesha tofauti iliyokuwako kati ya wanyama “safi” na “najisi.” Kwa hiyo, wokovu usingepatikana kwa kutii sheria ya Musa iliyokataza vyakula fulani visiliwe. Ndiyo sababu mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu aliandika hivi: “Mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.”—Kol. 2:16, 17.
Kwa hiyo, matengenezo ya dini za Jumuiya ya Wakristo yakiagiza watu wasile vyakula vyote au vingine vilivyokatazwa na sheria ya Musa, watakuwa wakikana kwamba mwili si wa Kristo. Wangekuwa wakitenda kinyume cha “neno” la Mungu ambalo limetakasa au likaonyesha kwamba, vitu vyote vinavyoweza kutumika kama chakula, vinakubaliwa. Vilevile sheria za kidini zisizo katika sheria ya Musa zingekuwa zikipinga ufunuo wa kimungu kwamba “kila kiumbe cha Mungu ni kizuri” na kinafaa kuliwa, zikikataza vyakula fulani visiliwe.
Kuanzisha sheria za kidini za kukataza vyakula visiliwe si jambo dogo. Kufanya hivyo ni kukataa imani ya Kikristo na maarifa sahihi. Ni kuonyesha kwamba “neno” la Mungu lina kasoro, kwamba halifunulii watu kwa ukamili mambo wanayopaswa kufanya ndiyo wakubaliwe na Mungu, na kwamba mawazo ya kibinadamu yanahitajiwa kwa sababu hiyo. Kufanya hivyo kunapunguza ubora wa “neno” la Mungu, na kanuni za kibinadamu zinatukuzwa. Wakati kanuni ya pekee ya kuamulia kweli inapofahamika vibaya hivyo, yaani, kanuni ya Maandiko, nafasi inatokezwa ya mafundisho mengine ya kuasi imani kuingia. Kwa hiyo, mtu akiheshimu sheria za kibinadamu zenye kukataza vyakula visiliwe, anamdharau Mungu. Lakini, Mkristo mwenye ufahamu akiepuka kuvila wakati huo ili asikwaze au asiudhi dhamiri ya mtu mwingine anayejisikia amefungwa na sheria hizo za ulaji, anakuwa mwenye huruma na anataka mtu huyo mwenye kufungwa na sheria afunguliwe na kupata wokovu.—1 Kor. 9:19.
Yehova Mungu anadharauliwa pia wakati chakula kinapoliwa bila shukrani zo zote kutolewa. Ndivyo ilivyo kwa sababu chakula kimetakaswa, si na “neno” la Mungu peke yake, bali pia na sala iliyotolewa kuhusu chakula hicho. Mwenye kusali hutambua kwamba Mungu ndiye Mpaji na hukubali chakula hicho kama zawadi iliyotoka kwake. Yeye hukubali kweli iliyoelezwa katika Zaburi 145:15, 16: “Macho ya watu wote yakuelekea Wewe, nawe huwapa chakula chao wakati wake. Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”
Nia hiyo ya kutoa shukrani ina matokeo mema juu ya Wakristo wa kweli. Inawachochea wasitumie vibaya walichopewa na Mungu, kwa kujifurisha tumbo au kwa kuharibu chakula, kupakua kingi zaidi kuliko wanachoweza kula. Halafu tena, nia hiyo inafanya mtu asiwe akichagua-chagua chakula atakachokula, bila sababu. Nia yake ya shukrani itafanya hata wale wasio na pesa nyingi wamkaribishe nyumbani kwao. Hata wakiwa na chakula kisicho cha bei, wanaweza kuondoa wasiwasi wasidhani chakula watakachompa hakiliwi na watu wa cheo chake.
Kwa kweli ziko sababu nzuri za kula na kunywa kwa utukufu wa Mungu. Mtu anayefanya hivyo huepuka kula na kunywa kupita kiasi, na huendelea kuheshimiwa na wengine. Kwa kupendeza dhamiri za wengine, yeye huepuka kuwakwaza. Juu ya yote, kwa kutenda kupatana na “neno” la Mungu na kula kwa shukrani, aweza kutosheka kweli kweli akijua kwamba mwendo huo unaongoza kwenye baraka za milele.