Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 5/1 kur. 10-14
  • Fanya Mambo Yote Ukiwa na Dhamiri Njema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fanya Mambo Yote Ukiwa na Dhamiri Njema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SHERIA ‘IMEANDIKWA MIOYONI’
  • MIFANO MIWILI INAYOIWEKA KANUNI
  • KANUNI YA KUFANYIA MAAMUZI KATIKA MAMBO YASIYO HAKIKA
  • Je! Wewe Unaongozwa na Dhamiri Nyepesi ya Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kufaidika na Dhamiri Yako Uliyopewa na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kuendelea Kuwa na Dhamiri Njema
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Je, Dhamiri Yako Imezoezwa Vizuri?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 5/1 kur. 10-14

Fanya Mambo Yote Ukiwa na Dhamiri Njema

“Heri mtu yule asiyejihukumu nafsi yake katika neno lile analolikubali.”​—Rum. 14:22.

1. Kwa sababu gani inatupasa tujiangalie juu ya kuwashauri wengine kuhusu mambo ya kibinafsi?

SI JAMBO jepesi kufanya maamuzi yanayofaa juu ya matatizo yote yanayotupata maishani. Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu alikubali kwamba “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.” Hiyo ni sababu moja iliyomfanya awaambie ndugu zake ‘wasiwe waalimu wengi, wakijua ya kuwa tutapata hukumu kubwa zaidi.’ (Yak. 3:1, 2) Tukipanua shauri tunalowapa wengine, tunaongeza wajibu wetu wa kuhusika katika matokeo ya shauri lenyewe.

2. Kwa sababu gani mashauri yote wanayopewa wengine yanapasa yaitegemee sana Biblia?

2 Ikiwa shauri tunalowapa wengine linategemea dhamiri yetu au maoni yetu wenyewe tu, ni hakika kwamba tutawapoteza. Hata tukijaribu kuwashauri kulingana na Biblia peke yake, lazima tuhakikishe kwamba tuna ufahamu unaofaa, kwamba hatuwapi dhana zetu wenyewe au maoni ya kibinafsi. Mtu anapokubali na kutumia shauri linalotegemea dhamiri au maoni ya mtu mwingine, halimfaidi kitu. Hata linaweza kumletea madhara mengi. Kwa sababu gani? Kwa sababu haongozwi na dhamiri yake mwenyewe. Kwa maana, “kila tendo lisilotoka katika imani ni dhambi.”​—Rum. 14:23.

3. Mtu anatakiwa afanye nini anapojifanyia uamuzi wa kibinafsi?

3 Ili mtu awe na imani juu ya jambo, ambayo pia inatia ndani kujifanyia uamuzi wake mwenyewe, inampasa apate maarifa sahihi katika Biblia na ushuhuda imara unaotegemea mambo ya hakika. (Ebr. 11:1) “Tena si vizuri nafsi ya mtu ikose maarifa; naye afanyaye haraka kwa miguu hutenda dhambi.” (Mit. 19:2) Ikiwa hana maarifa sahihi juu ya mapenzi ya Mungu, anaweza kuingizwa moja kwa moja katika mwendo mbaya.

4. Ikiwa mtu anatatizwa kufanya uamuzi, anaweza kufanya nini apate msaada?

4 Walakini, kuna Wakristo fulani walio na udhaifu mbalimbali katika imani yao, na mara nyingi sababu ni kwamba hawana maarifa juu ya tatizo fulani la maisha. Yakobo anaeleza kwamba Mkristo anaweza kuipata hekima inayotakiwa kuondoa hali yenye kumjaribu kwa kusali Mungu ampe hekima hiyo. (Yak. 1:2, 5) Bila shaka, ili apate jibu kutoka kwa Mungu lazima aiangalie Biblia pia. Kwa sababu gani atapata msaada kwa kufanya hivyo? Ni kwa sababu Wakristo wanapatwa na matatizo yale yale ya kibinadamu yaliyowapata watumishi wa Mungu karne zote zilizopita. Tukiyategemea Maandiko tutaona jinsi watu waaminifu, kutia na mitume na wenzao, walivyoshauri watu na kutatua matatizo hayo. Bila shaka, hali zinatofautiana, lakini Biblia inaonyesha kanuni inayofaa kutumiwa kuhusu matatizo yote. Maarifa na dhamiri zinahusika katika kutumia kanuni hiyo.

SHERIA ‘IMEANDIKWA MIOYONI’

5. Kwa sababu gani mtume Paulo aliliandikia kundi la Kikristo katika Rumi habari ya dhamiri?

5 Habari hiyo inayohusu dhamiri ilizungumzwa na mtume Paulo katika Warumi, sura ya 14. Katika kundi la Rumi, washiriki wote walikubaliana juu ya mafundisho ya msingi ya Biblia, na juu ya jinsi ya kuendesha kazi ya kuzitangaza “habari njema.” (Rum. 1:8) Lakini maoni yao yalitofautiana, hasa kuhusu mambo ya watu bi nafsi. Hasa yalitofautiana kwa sababu kabla hawajaanza kushirikiana na kundi walikuwa na hali mbalimbali za maisha, tena walikuwa wamezoezwa kwa njia mbalimbali. Sababu kubwa iliyotokeza maoni yenye kutofautiana ni mtengano mkubwa uliokuwa umekuwa kati ya Wayahudi na Mataifa kabla hawajaukubali Ukristo.

6, 7. (a) Ni ‘udhaifu gani wa imani’ ambao wengine kundini walikuwa nao? (b) Kusudi kubwa la Torati lilikuwa nini, naye Masihi alileta mabadiliko gani?

6 Paulo anaandika hivi: “Yeye aliye dhaifu wa imani, mkaribisheni.” (Rum. 14:1) “Udhaifu” huo haukuhusu imani juu ya Mungu aliye Baba na Bwana Yesu Kristo, inayoletea mtu wokovu. Wote walipaswa kuwa na imani hiyo. (An American Translation inasema hivi: “Watendeeni kama ndugu watu wenye kujihadhari mno na vitu vidogo vidogo katika imani yao.”) “Udhaifu” huo ulihusu mambo ambayo Wakristo fulani hawakuwa wamefahamu vizuri, wakawa hawajui sana Mkristo alikuwa na uhuru wa kiasi gani kuyafanya mambo hayo. Kwa mfano, muda wa karne nyingi Wayahudi walikuwa wamekuwa chini ya “orodha ya sheria” ya Musa (Rum. 13:9, NW; 2 Kor. 3:6) iliyowakataza wasile vyakula fulani vilivyokuwa “najisi,” kisha ikawaamuru waadhimishe siku fulani zilizopangwa, na kadhalika. (Law. 11:46, 47; Kum. 5:12-14) Mungu aliwapa Wayahudi sheria hiyo akiwa na kusudi la kuwazuia wasichangamane na mataifa ya kipagani, wasiingilie mazoea yao ya kuabudu sanamu, mpaka wakati ambao Masihi angekuja. (Gal. 3:23-25) Hapo ndipo “sheria ‘kamilifu iliyo ya uhuru” ingechukua mahali pa sheria hiyo nyingine, iwe ‘sheria iliyo ndani yao,’ iliyoandikwa mioyoni mwao. (Yak. 1:25; Yer. 31:33) Sheria hiyo mpya imeonyeshwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

7 Masihi, Yesu Kristo, aliwakomboa Wayahudi waliomkubali kwa kutumia dhabihu ya uhai wake mwenyewe. Mataifa pia yangeweza kukombolewa katika utumwa wa kuabudu sanamu waliokuwa nao hapo kwanza. Sasa Wakristo wote​—Wayahudi na Mataifa​—walikuwa wamelingana mbele za Mungu. (Efe. 2:14-16) Hata hivyo, ilikuwa vigumu baadhi ya Wakristo Wayahudi waliokuwa wamezoea sana desturi za zamani kubadilika. Waliona mambo mengine yakipingana na dhamiri zao.

8. Wengine kundini walikuwa na maelekeo ya kuwaonaje waliokuwa na ‘udhaifu’ wa imani, lakini wangalipaswa kuwatendeaje?

8 Mtume Paulo anaonyesha maoni yanayofaa anapoendelea kuliambia kundi liwakaribishe wenye dhamiri dhaifu, kisha anawaambia ‘wasiwahukumu mawazo yao.’ (“Msichambue maoni yao,” An American Translation; “lakini si kwa ajili ya mabishano yanayohusu maoni,” Revised Standard Version.) Mtu huyo alipasa akaribishwe kwa moyo mchangamfu kama ndugu, kama mrithi mwenzao wa Kristo, ingawa maoni au dhamiri yake ilikuwa tofauti, labda hata ‘yenye kujihadhari mno na vitu vidogo vidogo.’ Wengine walikuwa na maelekeo ya kufanya ubishi juu ya maoni aliyoyatoa ndani yake, moyoni mwake. Walifanya vibaya, maana jambo hilo liliumiza wenye kuhusika na lingeweza kufanya kundi lijiunge na upande wo wote kisha liwe na mgawanyiko.

MIFANO MIWILI INAYOIWEKA KANUNI

9. Ni tatizo gani lililotokea juu ya kula nyama?

9 Paulo anatoa mfano wa kula nyama. Kwa kawaida, siku hizo wanyama waliochinjwa au nyama zilizouzwa masokoni zilikuwa zimepelekwa mbele ya sanamu kama kwamba ingezitakasa kwa ajili ya waabudu waliozila. Bila shaka nyama zenyewe hazikuharibika kwa sababu ya kufanyiwa hivyo. Sanamu ilikuwa si kitu. Lakini wale wasioyafahamu sana maoni hayo yanayofaa walikuwa na mashaka katika dhamiri zao wakati wa kula nyama hizo, kwa maana walihofu kwamba zingaliweza kuwa zimehusiana na ibada ya kipagani. (1 Kor. 8:4-7) Ndiyo sababu mtume anatoa onyo hili la upole:

“Mtu mmoja anayo imani, anakula vyote [vitu vyote ambavyo ni chakula, kutia na nyama iliyonunuliwa sokoni]; lakini yeye aliye dhaifu hula mboga [za majani, asije akala bila kujua nyama aliyoiona kuwa ‘imenajisiwa’ na mazoea ya kipagani].”​—Rum. 4:2.

10. Je! watu ambao maoni yao yanatofautiana na ya wingi wa washiriki wa kundi hawapaswi kunyoshwa ili kuwe na ‘nia moja na shauri moja’?

10 Sasa ingekuwaje? Je! mtu huyo mwenye kula mboga za majani tu hakupaswa kunyoshwa maoni yake kabla hajaweza kuheshimiwa kuwa Mkristo halisi? Huenda wengine wakaonyesha kanuni inayosema kwamba ‘wote wanene mamoja; wala pasiwe faraka kwao, bali wahitimu katika nia moja na shauri moja.’ (1 Kor. 1:10) Lakini huo haukuwa umoja wa maoni kuhusu mambo yanayopasa kuamuliwa na mtu bi nafsi au na dhamiri yake; ulikuwa umoja wa kumfuata Kristo, si wanadamu.​—1 Kor. 1:11-13.

11. Watu waliokuwa kundini walikuwa na maoni gani juu ya mtu na mwenzake kuhusu mambo ya dhamiri?

11 Wakristo fulani Wayahudi waliolielewe vizuri jambo hilo, na vilevile washiriki wengi wa kundi waliokuwa Mataifa, ambao hawakuwa wamezizoelea kamwe kanuni za Musa, walielekea kuwadharau wenye kujihadhari mno na jambo hilo, wakawaona kuwa wapumbavu na wenye kushikikilia kauli yao wenyewe, nao wenye kujihadhari mno wakawa wakiwahukumu wale wengine kwamba wanaruka mipaka ya uhuru wao na kutenda kosa machoni pa Mungu. Basi mtume aliwasahihisha wote kwa kusema:

“Yeye alaye asimdharau huyo asiyekula, wala yeye asiyekula asimhukumu huyo alaye; kwa maana Mungu amemkubali. Wewe u nani unayemhukumu mtumishi wa mwingine? Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka. Naam, atasimamishwa, kwa kuwa [Yehova] aweza kumsimamisha.”​—Rum. 14:3, 4.

12. Kwa sababu gani lazima tuwakubali kabisa Wakristo ambao huenda maoni yao juu ya mambo ya kibinafsi yakatofautiana na yetu?

12 Ikiwa Mungu amekubali mtu, akamkaribisha na kumpa roho Yake ingawa huenda bado dhamiri au maoni ya mtu huyo yakamfanya ajihadhari mno au asijihadhari sana kama wengine, sisi ni akina nani hata tumlaumu? Sisi sote tuna wajibu wa kumpa Bwana wetu jibu la mambo tunayofanya. Sisi wenyewe tuna matatizo na makosa yanayotutosha hata tusiwe na wakati wa kujiingiza katika mambo ya mtu mwingine. Haifai mtu ajiingize katika mambo ya mtumishi au mfanya kazi wa mtu mwingine kwa kuulaumu utumishi wake​—⁠kwa hiyo ni wazi zaidi kwamba haitupasi kujiingiza tulaumu mtu juu ya jinsi anavyomtumikia Mungu. Mungu ndiye Hakimu wa mtumishi huyo. Naam, “atasimamishwa” na Yehova.

13. Ni kwa njia gani Mungu atamsimamisha mtumishi wake?

13 Hapo Paulo hamaanishi kwamba Mungu atamwunga mkono mtumishi wake katika mambo yote afanyayo, maana hawezi kumwunga mkono akifanya mabaya. Lakini ingawa huenda Mkristo akawa na maoni fulani ya dhamiri yanayolaumiwa na wengine na hata kuwafanya waone kwamba hastahili kuwa Mkristo, Mungu hatamhukumu vibaya, bali atapendezwa naye kwa sababu anafuata dhamiri. Mungu akiona inafaa, katika wakati wake ataifanya dhamiri ya mtumishi wake ikomae zaidi. Lakini Mkristo ye yote asijaribu kuagiza Mkristo mwenzake afuate dhamiri yake. Akifanya hivyo, huenda akamwingiza matatani au kuiharibu imani yake. Kwa hiyo, yeye mwenyewe angestahili “hukumu kubwa zaidi,” au lawama fulani, kama Yakobo anavyosema.​—Yak. 3:1.

14-16. Eleza maana ya maneno ya Paulo katika Warumi 14:5, 6.

14 Mtume anatoa mfano mwingine:

“Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku; mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe. Yeye aadhimishaye siku, huiadhimisha kwa [Yehova]; naye alaye, hula kwa [Yehova], kwa maana amshukuru Mungu; tena asiyekula, hali kwa [Yehova], naye pia amshukuru Mungu.”​—⁠Rum. 14:5, 6.

15 Kwa mfano, Myahudi aliyemkubali Kristo lakini hapo kwanza akawa aliitii sheria ya Musa muda mrefu, angeweza kuona mashaka katika dhamiri juu ya kufanya kazi yo yote ngumu siku ya Sabato ya Kiyahudi. Kazi hiyo ingeweza kuwa upishi, useremala, au kusafiri mwendo mrefu. Hata kama ingekuwa ni kazi ya kundi, aliyotazamiwa na washiriki wale wengine wa kundi awafanyie au aifanye pamoja nao, siku hiyo labda angeweza kuzuiwa na dhamiri asiifanye. Yeye angekuwa na nia ya kuifanya siku nyingine yo yote. Lakini siku hiyo moja aliiadhimisha kama siku ya pekee ‘kwa Yehova,’ yaani, aliona kwamba alikuwa akifanya mapenzi ya Yehova kwa kuiadhimisha siku hiyo kama yenye utakatifu wa pekee. Na wakati wa kula, alimshukuru Mungu kwa kuweza kuwa safi kabisa na kujitenga na ibada ya sanamu kwa sababu Mungu alikuwa ameonyesha maoni yake waziwazi katika sheria ya Musa. (Angalia jinsi Danieli, ambaye wakati huo alikuwa chini ya Torati, alivyoona. [Dan. 1:8]) Hatua aliyochukua kwa kuongozwa na dhamiri haikuudhi mtu ye yote kundini, wala yeye hakuwa akifanya kosa kwa njia hiyo. Basi, Yehova hakumhesabu kuwa mtu mchafu. Yehova alifahamu kwamba mtu huyo alikuwa akimtii kulingana na kiasi cha maarifa aliyokuwa nayo, na vilevile kwa dhamiri safi, wala hakuwa akiikana dhabihu ya Kristo.

16 Kwa upande mwingine, kwa ujumla jamii yote ya Wakristo iliziheshimu siku zote kuwa za Mungu​—zote zikiwa takatifu​—wala hakuna siku waliyoiona kuwa takatifu kuliko nyingine. Walikula nyama wakiwa na dhamiri safi kwa kujua kwamba, ikiwa nyama hiyo ilipelekwa mbele ya sanamu, nyama yenyewe haikubadilika, kwa sababu sanamu hazikuwa na uwezo wo wote. Wao walimshukuru Mungu kwa kuweza kukila chakula alichowapa, kisha walimshukuru kwa ajili ya uhuru aliokuwa amewapa kupitia kwa Kristo.

17. Kwa sababu gani ni lazima kila mtu asadikishwe kabisa katika akili yake mwenyewe?

17 Lakini, kila mtu alipaswa kusadikishwa kabisa katika akili yake mwenyewe. Ikiwa dhamiri ya Mkristo haikuweza kuyafahamu vizuri maoni ya mwenzake, asingepata faida yo yote akitenda kinyume cha dhamiri yake kwa kufuata maoni ya mwenzake. Wala hakuna mmoja kati yao angepaswa kumlaumu mwenzake, kubishana naye, kumhukumu wala kumdharau. (Yak 4:11, 12) Hakuna ye yote kati yao aliyepaswa kujaribu kulazimisha mwenzake afuate maoni yake. Kama angefanya hivyo, angekuwa akijaribu kuitawala imani ya mwenzake.

18. Je! kuna jambo lo lote ambalo wazee au wengine wanaweza kufanya wasaidie mtu awe na maoni sahihi zaidi juu ya jambo la kibinafsi? Ikiwa kunalo, ni jambo gani?

18 Hiyo si kusema kwamba mambo yanayohusu dhamiri hayawezi kuzungumzwa na kuchunguzwa ili kupata maoni ya Biblia. Inafaa kutoa sababu za Maandiko juu ya habari inayohusika. Lakini kusiwe na mabishano makali, wala tusisisitize wenzetu wafuate maoni yetu au wafanye tunavyosema. Wazee na wengine waliokomaa wanaweza kuwasaidia walio dhaifu au wenye maoni yasiyofaa kuhusu mambo fulani. Lakini wasiruke mpaka. Baada ya kusaidia mtu, hapo itakuwa juu yake kutenda jambo ambalo dhamiri yake inamwonyesha linakubalika kwa Mungu.

KANUNI YA KUFANYIA MAAMUZI KATIKA MAMBO YASIYO HAKIKA

19. Tunawezaje kujua mambo yanayopasa na yasiyopasa kuachwa yaamuliwe na dhamiri ya mtu mwenyewe?

19 Ingawa hapo mtume anatumia mifano miwili tu, anaweka kanuni ya kuamulia mambo yote yanayohusu dhamiri. Leo kuna hali nyingi zisizo na agizo au sheria ya wazi katika Biblia. Hali hizo zinahusu kazi, matibabu (uganga), chakula, mavazi, na vitu vingine. Biblia inatoa kanuni za kutuongoza katika mambo hayo yote. Inawapasa watu wote wafuate mambo inayosema waziwazi. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba mavazi na mapambo yanapasa yawe “ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi,” yenye umalidadi na usafi. (1 Tim. 2:9; 2 Kor. 7:1) Inatupasa tuendelee kuheshimu maoni ya ndugu zetu na ya kundi, na kuangalia tusiharibu sifa nzuri ya kundi mtaani. Lakini mapendezi ya watu yanaweza kutofautiana sana katika mitindo ya mavazi, rangi na kadhalika.

20. Mtu anayepatwa na tatizo asilojua jibu lake anapaswa afanye nini?

20 Mtu anayehusika katika hali hizo zisizo na uhakika apaswa kuitegemea Biblia na vitabu vinavyoieleza Biblia. Ikiwa hajajua waziwazi uamuzi anaopaswa kufanya, anaweza kuwaendea wazee au wengine wanaoweza kumsaidia afahamu yanayosemwa na Biblia, lakini asiwaache wamfanyie uamuzi. Wao siyo “dhamiri” yake. Yeye mwenyewe afikirie mambo, kisha ajifanyie uamuzi na kuiacha dhamiri yake iufuate. Wakati upitapo huenda akapata maoni tofauti na kufanya rekebisho, lakini inampasa aepuke kufanya jambo lo lote analoonea mashaka, asije akajilaumu mwenyewe.​—Rum. 14:23.

21. Tukiwa na maoni fulani yenye kuongozwa na dhamiri, je! hiyo maana yake ni kwamba hatupaswi kamwe kubadilika, au namna gani?

21 Inawapasa Wakristo wote wajitahidi daima kufanya maendeleo ya ufahamu wao na ya kukaribia zaidi kumwiga Mungu na Kristo kwa ukamilifu. Kwa kufanya hivyo watakuwa wakifanya maendeleo nyakati zote wakawe na dhamiri iliyozoezwa kwa usahihi zaidi. Inawapasa nyakati zote wawe wakifanya mambo kwa njia yenye kudumisha dhamiri njema, tena inawapasa wawape ndugu zao Wakristo uhuru wa kufanya vivyo hivyo.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Paulo alishauri kwamba waamini wapya wakaribishwe wajapokuwa na ‘udhaifu wa imani’

[Picha katika ukurasa wa 13]

Iheshimu dhamiri ya Mkristo mpya kuhusu mwadhimisho wa Sabato au kula vyakula fulani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki