Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/15 kur. 125-127
  • Je! Wewe Ni Mbaya Mno Kiasi cha Kutosamehewa na Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Ni Mbaya Mno Kiasi cha Kutosamehewa na Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! MTU AWEZA KUSAMEHEWA DHAMBI ZOTE?
  • MIFANO YA KISASA
  • Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Kwa Sababu Gani Watu Hawawezi Kusamehewa Dhambi Nyingine?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Yehova—Mfano Bora wa Kusamehe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/15 kur. 125-127

Je! Wewe Ni Mbaya Mno Kiasi cha Kutosamehewa na Mungu?

MAMILIONI ya watu ulimwenguni mwote, watu wa namna zote za maisha, wanazisikia habari njema juu ya ufalme wa Mungu. Wanajifunza juu ya baraka zitakazoletwa na ufalme huo: Kuondoa kifo, huzuni na maumivu; na kila mtu atakaa chini ya mzabibu na mtini wake mwenyewe, bila ya mtu wa kumwogopesha. Ahadi zote hizo zimetolewa kwa wale wanaomtafuta Yehova na haki yake kwa unyenyekevu.​—Isa. 2:4; Sef. 2:3; Ufu. 21:4.

Pengine unaona kwamba ahadi hizo hazikuhusu wewe kwa sababu ya maisha yako ya zamani, ingawa umezisikia pia habari njema hizo. Kama ungalijua mapema zaidi habari za Mungu na baraka za ufalme wake, pengine maisha yako yangalikuwa tofauti. Pengine wewe ulidhani ulikuwa na haki ya kujiamulia mambo kwa kutumia nguvu, udhalimu hata jeuri, kwa sababu ya kuona hali zisizo haki. Halafu tena, pengine wewe ulilelewa katika mazingira mabaya kama watu wengine wengi, ukaingia katika namna mbalimbali za mwenendo usiofaa, na pengine hata ulifuata mwenendo huo miaka mingi. Ni kama vile Biblia isemavyo: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”​—1 Kor. 15:33, NW.

Unapokumbuka yaliyopita, huenda ukajisikia umejifanyia kumbukumbu baya. Pengine unajisikia kwamba ungependa kubadilika, lakini labda unaona ni kazi bure, kwamba Mungu hawezi kusamehe mtu wa namna yako. Walakini, Biblia yaonyesha kwamba, ingawa Yehova hakubali makosa na wenye kuyafanya, yeye si Mungu mwenye kutaka kujilipiza tu, mwenye kupasisha watu adhabu kwa makosa yote waliyofanya maishani mwao.

Sivyo Mungu alivyo. Ni kama vile mtunga zaburi alivyoeleza zamani: “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Badala ya kufanya hivyo, yeye anatuhakikishia kwamba, tukiacha kabisa njia zetu mbaya zenye madhara na kumgeukia, ‘atatusamehe kabisa.’​—Zab. 130:3; Isa. 55:7.

Unaweza kuwa na hakika kwa sababu Biblia inatupa mifano mizuri sana ya watenda dhambi wabaya sana waliosamehewa na Mungu kwa sababu walitubu kweli-kweli. Mmoja alikuwa Mfalme Manase wa Yuda. Yeye alikuwa mmoja wa wafalme waovu zaidi waliopata kutawala katika Yerusalemu. Kwa sababu ya uovu wake mwingi sana, Mungu alimwacha akachukuliwa mateka Ashuru. Lakini Manase alipotubu, akanyenyekea na kumwomba sana Mungu, Yehova alisikia sala zake akamkubali tena na kumrudishia ufalme wake.​—Fal. 21:2-16; 2 Nya. 33:2-13.

Tena mfano na mafundisho ya Yesu na mitume wake yanakutia moyo kwa njia iyo hiyo. Yesu alitolea hata malaya na watoza kodi (waliofikiriwa kuwa kati ya watenda dhambi wabaya zaidi siku zake) tumaini la kusamehewa, kwa sababu walifahamu kwamba walimhitaji na wakatubia mwenendo wao wa zamani. Ni kama vile alivyowaambia wenye kumlaumu: “Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. . . . Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.” Na wakati mwingine alisema hivi: “Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu.”​—Mt. 9:11-13; Luka 15:7.

Hasa mfano mzuri sana wa Yesu juu ya mwana mpotevu wapaswa kukufariji. Walikuwako wana wawili, na aliye mdogo alimwomba baba yake ampe sehemu ya urithi iliyokuwa haki yake kisha akaenda nchi ya mbali “akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati.” Baadaye, aliporudiwa na fikira, alitubu akarudia baba yake kwa unyenyekevu, naye baba yake hakumkataa bali alimkaribisha kwa mikono mikunjufu.​—Luka 15:11-32.

Maneno ya Paulo yanayopatikana katika 1 Wakorintho 6:9-11 yanafariji na kutia tumaini pia. Humo, baada ya kuonya Wakristo juu ya dhambi zilizo mbaya sana zinazoweza kuwazuia wasiurithi ufalme wa Yehova Mungu, anaendelea kusema hivi: “Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa.”

JE! MTU AWEZA KUSAMEHEWA DHAMBI ZOTE?

Je! hiyo maana yake ni kwamba mtu aweza kusamehewa bila kujali anafanya dhambi za namna gani? Sivyo. Yesu alieleza hilo wazi alipokuwa akisema na wapinzani wake wanafiki: “Nawaambia, Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa [kuikufuru roho] hawatasamehewa. Naye mtu ye yote atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali yeye atakayenena neno juu ya [roho takatifu] hatasamehewa katika ulimwengu wa sasa, wala katika ule ujao.”​—Mt. 12:31, 32.

Ni nini kilichomfanya Yesu aseme hivyo? Maneno yanayozunguka habari hizo yaonyesha kwamba wanafiki hao wa kidini walimwona Yesu, Mwana wa Mungu, akifanya miujiza ya namna zote, hata kutoa mashetani ndani ya watu, kwa kutumia uwezo wa roho takatifu ya Mungu, lakini wao wakasema kwa makusudi na chuki kwamba uwezo wa Shetani Ibilisi ndio uliofanya hivyo.

Wengine wasioweza kusamehewa dhambi zao ni wale waliopata maarifa ya kweli juu ya Yehova Mungu wakati mmoja, wakaiamini damu ya Kristo iliyomwagwa kisha wakaikana au wakageukia mazoea maovu. Lakini namna gani ukijisikia kwamba pengine umefanya dhambi ya namna hiyo​—je! hiyo yaonyesha bila shaka umeifanya? Sivyo ikiwa unataka kutubu kwa unyofu na kufanya yaliyo haki, kwa maana hiyo yaonyesha labda hukupita kiasi, kama inavyoonyeshwa na mfano wa Mfalme Manase.​—Ebr. 6:4-6; 10:26, 27.

Mambo mawili yenye kufariji yanatuhakikishia kwamba mtu aweza kusamehewa matendo yake ya zamani. Jambo moja ni rehema ya Mungu. Yeye hufurahia kuwa mkarimu, kusamehe, kama vile Neno lake linavyotuhakikishia: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu . . . Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.”​—Mik. 7:18, 19.

Jambo lile jingine ni kwamba, hali zinapunguza uzito wa kosa. Ingawa Mfalme Daudi alitenda dhambi nzito juu ya Yehova katika habari iliyohusu Bathsheba, mke wa Uria, alisamehewa lakini akaadhibiwa vikali. Kwa sababu gani? Kwa sababu alizaliwa katika dhambi. Vilevile, alikubali kosa lake mara moja na akatubu kwa unyofu, kama tusomavyo katika Zaburi 51. (2 Sam. 12:1-23) Ndivyo ilivyokuwa juu ya mtume Paulo. Wakati mmoja alitesa Wakristo hata akawaua, na kwa sababu hiyo anajitaja kuwa mtenda dhambi “wa kwanza” (‘apitaye wote,’ NW). Lakini, kama asemavyo mwenyewe, “Hata hivyo, nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikuwa mjinga na nilitenda kwa kukosa imani.” Naam, yeye alipinga Wakristo kwa uaminifu na moyo mnyofu, ingawa alikosea sana. Kama anavyoendelea kusema, sababu nyingine pia ya kuonyeshwa rehema ilikuwa, “ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”​—1 Tim. 1:13-16; Matendo 26:9-18.

MIFANO YA KISASA

Leo, kama katika nyakati za Biblia, watu ambao wamekuwa watenda dhambi wabaya sana wanaweza kutubu na kupata msamaha. Mambo ya hakika yaonyesha hivyo. Kulikuwa na mwanamume mmoja aliyehukumiwa kifungo chenye ulinzi mkali sana New York State kwa sababu alikuwa mvunja sheria mbaya sana. Shahidi wa Yehova, aliyekuwa mmoja wa waalimu wa gereza, alimhubiri mtu huyo hata dhamiri yake ikaanza kumsumbua. Alisumbukia sana maisha yake ya zamani. Alikosa kujua kama Mungu angeweza kumsamehe makosa mengi na uvunjaji wa sheria mwingi sana aliokuwa amefanya. Lakini alihakikishiwa kwamba angeweza kusamehewa akitubu kwa unyofu. Alitubu. Alibadili kabisa mwenendo wake mbaya, akaweka maisha yake wakf kwa Yehova Mungu na kubatizwa. Sasa yeye ni Mkristo mwenye furaha sana na ana dhamiri safi.

Fikiria, pia, kisa cha mwanamume aliyekuwa mshiriki hatari sana, sana, wa chama cha maharamia waitwao Mafia wa kisiwa cha Sicily (Italia). Alikamatwa akahukumiwa kifungo cha maisha. Huko gerezani alikutana na mmoja wa mashahidi wa Yehova akamweleza habari za Mungu wa kweli mmoja, juu ya ibada safi na baraka za ajabu ambazo Mungu amewekea wanadamu akibani. Alipokuwa mwana-chama wa Mafia alikuwa Mkatoliki “thabiti” ati, lakini hakuona ubaya wa kufanya kazi mbili hizo. Lakini sasa, aliposadiki kwamba ujumbe aliokuwa akiletewa na Shahidi ulikuwa wa kweli, alitubu kwa unyofu, akageuka na kujiweka wakf afanye mapenzi ya Yehova Mungu. Alibadili sana maisha yake hata akahojiwa katika kimojawapo cha vituo vya televisheni vya Italia.

Naam, liko tumaini kwamba unaweza kusamehewa, uwe na dhamiri safi na kukubaliwa na Mungu ingawa umefanya makosa mazito nyakati zilizopita. Lakini kusema tu unasikitikia mwenendo wako wa zamani hakutoshi. Lazima utwae maarifa juu ya Yehova Mungu, ujifunze matakwa yake yenye haki. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova walio katika ujirani wako wako tayari kukusaidia kwa kujifunza nawe Biblia nyumbani mwako na kuhudhuria pamoja nawe mikutano yao inayofanywa katika Jumba la Ufalme.

Ujifunzapo nao utaweza kujihakikishia Mungu angependa kwa haki na utakatifu ufanye nini. (Rum. 12:2) Utasaidiwa uzidi kuchukia mabaya, na uzidi kupenda kweli kweli mapenzi ya Mungu yenye haki. (Zab. 97:10) Hutajifunza kuepuka mabaya tu, bali pia utasaidiwa ujue jinsi ya kufanya yaliyo haki machoni pa Mungu. Nawe utaweza kufanya mambo hayo ukiwa na dhamiri safi, kwa kuamini ubora wenye kulipia dhambi wa dhabihu ya Kristo, kwa maana “damu yake Yesu, Mwana wake [Mungu], yatusafisha dhambi yote.”​—1 Yohana 1:7.

Ni kweli kwamba uanzapo kubadili maisha yako yapatane na matakwa ya Mungu yenye haki, inawezekana sana kwamba utateleza-teleza na kuiacha njia mara kwa mara. Lakini usivunjike moyo, kwa maana mtunga zaburi Daudi aliandika faraja hii: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo [Mungu] alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:12, 14) Uhakikisho huo na ukutie nguvu udumu katika njia inayofaa.

Neno la Mungu limejawa kweli kweli na mahakikisho yenye kufariji wale wanaotaka kufanya yaliyo haki kwa unyofu wa moyo, si kitu mwenendo wao umekuwaje wakati uliopita!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki