Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Neno la Mungu linaonyesha imewapasa Wakristo wawe na maoni gani juu ya kujiua kwa mtu mwenyewe?
Yehova akiwa ndiye chanzo cha uzima ameamuru kwamba uhai wa kibinadamu ni wenye thamani nyingi, ni mtakatifu. (Mwa. 9:5; Zab. 36:9) Hivyo, kujiua kwa mtu mwenyewe kunakatazwa na Biblia.. (Kut. 20:13; 1 Yohana 3:15) Watu wachache wanaotajwa katika Biblia kama waliojiua wenyewe walikuwa wasioaminika kwa Yehova nao walikosa kuangalia kwamba maisha zao kwa kweli zilikuwa za Mungu.—1 Sam. 31:4; 2 Sam. 17:5-14, 23; 1 Fal. 16:18; Mt. 27:5.
Mtu anayejiua anafanya hivyo kwa kudharau kabisa utakatifu wa uhai; anakuwa mwenye hatia ya damu. Mtu anapojiua akiwa na akili timamu, hiyo inaonyesha hana adili, hana imani, hamwogopi Mungu. Ni tendo la unyonge, ambapo mtu anakataa kupambana na magumu na madaraka ya maisha. Ikiwa mtu huyo alikuwa akijidai kuwa Mkristo wa kweli, tendo hilo lingevunja kabisa uhusiano wake na Yehova. Kujiua kwaweza kuwa ni kushindwa na mikazo ya mashetani wanaotia mtu moyo ajiharibu. (Mt. 17:14-18) Tendo hilo la mtu kujifikiria yeye peke yake kwa kujiua halionyeshi upendo kwa washiriki wa jamaa ya mtu wanaobaki, wala halionyeshi upendo wo wote kwa kundi na rafiki za mtu, wala hata halionyeshi upendo kwa watu wa mtaa walio karibu, kwa maana linaleta aibu na kutaabisha akili za washirika wote.—Marko 12:31.
Katika nchi nyingi afisa wa serikali ndiye anayetoa sababu ya kufa kwa mtu kwa njia rasmi. Ingawa ripoti ya kujiua kwa mtu inaweza kutolewa na afisa huyo, huenda isiwe inapatana na mambo ya hakika. Kwa mfano, katika ripoti ya namna hiyo ya mtu kujiua mwenyewe, baada ya juma tatu ushuhuda wa wazi ulitokea ukaonyesha kwamba kifo kilisababishwa na jambo lisilo la kawaida. Kwa hiyo, lazima sikuzote hali zifikiriwe. Je! alikuwa na ugonjwa wa akili? Je! mtu huyo alikuwa timamu katika akili? Je! alistahili laumu? Katika visa vingi ni vigumu kujua mambo yote ya hakika.
Basi nia ya washiriki wa kundi la Kikristo imepaswa iwe nini juu ya kuhudhuria mazishi ya watu waliojiua ambao pengine walikuwa wakishirikiana na kundi? Namna gani juu ya mzee ambaye ameombwa akaongoze mazishi hayo? Wakati kifo kinaelekea kuwa kilitokea bila kutazamiwa, ingawa imeripotiwa kuwa mtu mwenyewe amejiua au kifo kimesababishwa na ugonjwa wa akili, huenda dhamiri za Washiriki fulani wa kundi zikawaruhusu wahudhurie mazishi ili kufariji waliofiwa. Vile vile, ni juu ya uamuzi wa mzee mwenyewe kama ataongoza mazishi hayo akiombwa au kama hatafanya hivyo. Walakini, huenda kundi likapendelea kutosimamia mazishi hayo hadharani au kutoyafanyia katika Jumba la Ufalme kwa sababu ya matokeo yanayoweza kuwa nayo juu ya watu wa mtaa wasiojua habari zote.
Kwa upande mwingine, ikiwa imehakikishwa kwamba mtu alijiua mwenyewe, washiriki wa kundi na wazee wanaweza kutaka wasijitie katika mazishi. Ikiwa hivyo jamaa yenyewe itaachiwa mipango ya mazishi ya faragha ambapo mshiriki fulani wa jamaa hiyo aweza kusema machache kwa ajili ya watu wa ukoo. Zaidi ya hayo, huenda wengine wasitake kuhudhuria mazishi ya mtu anayeaminiwa alijiua mwenyewe ikiwa mazishi yanaongozwa na mtu asiye mshiriki wa kundi au ikiwa yanaongozwa na msimamizi wa mambo ya mazishi aliyeombwa kufanya hivyo na jamaa.
Tukiwa wapenda haki tunaliacha jambo hili mikononi mwa Mungu mwenye rehema na hekima yote tuone kama waliokazwa wakajiua wenyewe watafufuliwa wakati ujao. Sisi tupendao uzima, tunaoona kila siku ya kuishi kuwa takatifu, tunajaribu kuongoza mambo yetu ya kila siku na mashirika yetu kwa njia itakayostahili kibali ya Yeye aliyewapa wanadamu uhai.