Tegemezo la Kimungu Laondoa Woga
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. (a) Kila mtu anayetumikia Mungu huenda akapaswa kufanya uamuzi gani juu ya kuendelea kufanya kazi iliyoamriwa naye? (b) Wakristo wa kweli wamepatwaje na ugumu huu?
WEWE ungeonaje kama ungeagizwa na Mungu Mwenye nguvu zote ufanye kazi fulani, halafu ukatazwe kufanya hivyo na amri fulani rasmi ya kibinadamu? Na namna gani kama amri hiyo ingetolewa na Mamlaka ya Ulimwengu ya siku zako? Je! wewe ungetetema kwa woga, hasa kama kazi hiyo ingepaswa ifanywe waziwazi, ambapo watu wote wangeweza kuiona? Je! ungeacha kazi yako, au ungeendelea kuifanya kijasiri?
2 Wakristo wenye kuzitangaza habari njema za ufalme wa Mungu wamepatwa na hali hiyo mara nyingi na mahali pengi. Wanajua kwamba wamepewa agizo la kuhubiri na Mungu. Kiongozi wao Yesu Kristo, aliyezungumza mambo aliyoyasikia kwa Mungu, alisema hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Pia: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha.” (Mt. 24:14; 28:19, 20, NW; Yohana 8:28, 29) Lakini watawala katika nchi fulani wametoa amri ya kuacha kuhubiri, na sheria zimetungwa hata na mamlaka kuu za ulimwengu kupiga kazi hii marufuku. Hata hivyo, Wakristo wa kweli wameendelea bila woga ujapokuwapo upinzani huo. Wamewezaje kufanya hivyo wakiwa na ujasiri halisi?
MFANO WA UNABII
3. Wayahudi waliokuwa wamerudi Yerusalemu kutoka Babeli walikabiliwaje na ulizo la watakayetii?
3 Karne nyingi zilizopita hii ilionyeshwa kwa unabii. Huo ulikuwa wakati utawala wa Uajemi ulipokuwa Mamlaka ya Nne ya Ulimwengu ya historia ya Biblia. Kupitia kwa Koreshi, mfalme wa Uajemi, Mungu alikuwa amevunja uwezo wa Babeli akakomboa Israeli katika utumwa wake. Wote waliotaka kurudi Yerusalemu wakajenge upya hekalu la Yehova na kurudisha ibada ya kweli waliruhusiwa kufanya hivyo. Wakiongozwa na gavana aliyewekwa, Zerubabeli, kundi la karibu watu 50,000 lilionyesha imani na bidii yao kufunga safari hiyo ndefu. Walipofika, wakasimamisha madhabahu na baadaye wakaweka msingi wa hekalu. Lakini upinzani wa mataifa jirani ulikuwa mkali. Mtawala mpya alipata mamlaka katika Uajemi, nao maadui hawa wakaweza kupata amri ya kifalme kuhakikisha kwamba ujenzi wa hekalu umekomeshwa mara moja.—Ezra 3:8-10; 4:17-22.
4. Mara ya kwanza mabaki hayo yaliyorudi walitendaje walipopingwa wasijenge hekalu, na kwa hiyo kukatokea ulizo gani?
4 Wenye kujenga hekalu wakaacha kwa sababu ya woga. Kwa karibu miaka kumi na sita hakuna kazi iliyofanywa. Lakini amri ya kujenga ilikuwa imetolewa na Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, Yehova Mungu mwenyewe, si na mamlaka dhaifu tu ya kidunia. Je! yeye angeacha woga wa watumishi wake ubatilishe amri yake? Au angewatia nguvu na kuwategemeza kwa uwezo wa kimungu?
5. Ijapokuwa Wayahudi waliacha kufanya kazi, Mungu alifanya nini, naye Gavana wa Wayahudi Zerubabeli aliitikiaje?
5 Mungu aliwasubiri watu wake, kwa maana alijua walikabiliwa na upinzani mkali. Walakini, hawakupaswa kuogopeshwa waachilie mbali agizo walilopewa na Mungu. Ili kutimiza kusudi lake mwenyewe na kwa sababu ya kuwarehemu, alituma manabii wake Hagai na Zekaria kuwasahihisha, kuwatia moyo na kuwachochea waingie katika utendaji. Gavana Zerubabeli akaitikia, akachukua hatua kwa ujasiri, kwa wazi ili aikaidi Milki ya Uajemi yenye nguvu. Hatua hii ya kumtii Yehova Mungu ilikuwa nzuri na yenye kufaa. Kupitia kwa Hagai, Yehova alimhakikishia Zerubabeli hivi kwa kumfariji:
6, 7. Maneno ya Yehova kupitia kwa Hagai, ambayo yanapatikana katika Hagai 2:21, 22, yalimtiaje Zerubabeli moyo?
6 “Nitazitikisa mbingu na dunia; nami nitakipindua kiti cha enzi cha falme, nami nitaziharibu nguvu za falme za mataifa; nami nitayapindua magari, na hao wapandao ndani yake; farasi na hao wawapandao wataanguka chini; kila mtu kwa upanga wa ndugu yake.”—Hag. 2:21, 22.
7 Kupitia kwa tendo lake la utii Zerubabeli alikuwa amehakikishiwa kwamba uwezo wa Yehova wa majeshi ulikuwa ukimwunga mkono. Kwa hiyo kukataa kwa wanadamu kulikuwa kazi bure tu. Mungu huyu akiwa ndiye Mtawala mtukufu alipaswa atiiwe kuliko watawala wa kibinadamu. Ala! yeye angeweza kutikisa mbingu na dunia pia! Sasa basi, ni nini ambacho mtu angeweza kufanya aharibu au apinge makusudi yake aliyoyatangaza? Hakuna!
8, 9. Zerubabeli alikuwaje “kama pete yenye muhuri,” nayo hii ilimpa uhakikisho gani?
8 Tena, Yehova alimwambia Zerubabeli hivi: “Nitakutwaa wewe, Ee Zerubabeli, mtumishi wangu, mwana wa Shealtieli, . . . nami nitakufanya kuwa kama pete yenye muhuri; kwa kuwa nimekuchagua.”—Hag. 2:23.
9 Zerubabeli akawa mwenye thamani kuu kwa Yehova, kama pete yenye muhuri katika mkono wa kuume wa Yehova wa majeshi. Kwa sababu ya kutii amri za Yehova na kuonyesha uaminifu wenye ushujaa kwa ajili ya ibada safi ya Yehova katika hekalu lake, alikuwa kama pete yenye muhuri, yenye kumtumikia Yehova wa majeshi kwa njia rasmi, kwa ajili ya utukufu na sifa ya jina Lake takatifu. Haikumpasa Zerubabeli aogope kwamba atashushwa na mfalme wa Uajemi. Bila shaka Mungu asingemtikisa Zerubabeli amwondoe katika cheo cha heshima cha kumtumikia Yeye, hata Milki ya Uajemi yote ikitikiswa ipoteze imara yake, kama ilivyotukia hasa miaka mingi baadaye. Zerubabeli angepata tegemezo kamili la kimungu. Ndivyo ilivyokuwa. Karibu miaka mitano baadaye mwishowe hekalu lilimalizwa kukawa na shangwe nyingi.—Ezra 6:14, 15, 22.
TEGEMEZO LA KIMUNGU LEO
10, 11. (a) Cheo na utendaji wa Zerubabeli vilifananisha nini? (b) Kazi anayofanya Yesu Kristo inafananaje na ile ya Zerubabeli, kama inavyoelezwa katika Isaya 2:2, 3?
10 Cheo cha Zerubabeli juu ya watu wa Mungu huko nyuma, na kazi aliyofanya, vilifananisha utendaji wa Yesu Kristo akiwa Gavana wa kimbinguni wa Israeli wa la kiroho. Yeye ndiye Mwendelezaji mkuu wa kazi inayohusiana na hekalu kuu la kiroho la Yehova. Ijapokuwa alipingwa na ulimwengu huu, Yesu alipokuwa duniani alizihubiri habari njema za Ufalme bila woga. Sasa anayo roho ile ile, akiwa ametukuzwa mbinguni kuwa Gavana wa Israeli wa kiroho leo. Yeye anaongoza na kuamuru Wakristo wa kweli, akiwawezesha kuhubiri na kukusanya pamoja watu kwenye ibada safi ya Mungu, katika hekalu la kiroho la Yehova, kama ilivyosemwa kwa unabii katika Isaya 2:2, 3:
11 “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”
12. (a) Hapo kale pete yenye muhuri ilitumiwaje? (b) Yesu Kristo ni kama pete yenye muhuri katika mkono wa Yehova kwa njia gani?
12 Gavana huyu wa kimbinguni ni mwenye thamani kuu kwa Yehova Mungu kama Zerubabeli, kama pete yenye muhuri katika mkono wake wa kuume, pete yenye jina lake la kimungu. Pete ya kale yenye muhuri ilitumiwa kutia jina la mwenyewe katika hati, kwa njia hiyo kuhakikisha kwamba hati hiyo kweli imetoka kwake na kwamba inaonyesha mapenzi yake, makusudi na maagizo yake. Vivyo hivyo, Yesu Kristo anatumiwa kutimiza unabii mbali-mbali na ahadi za kimungu na kwa njia hiyo kuhakikisha kwamba matangazo hayo yaliyoandikwa yalitokana kweli na Chanzo cha kimungu kisichokosea na kwamba yana ukweli wa kimungu.
13. Kwa kuwa Yesu ni kama pete yenye muhuri katika mkono wa Yehova, twawezaje kuwa na hakika tutapata tegemezo la kimungu?
13 Mkuu alikuwa akitegemeza mambo yaliyoandikwa katika hati yenye muhuri yake. Vivyo hivyo, Yehova wa majeshi anamtegemeza Yesu Kristo. Kupitia kwa Yesu, jina la Mungu na makusudi yake yanashuhudiwa, nasi tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba tutapata tegemezo la kimungu tukifuata amri na mfano wa Yesu Kristo. Yeye ndiye kweli, yaani, Yeye ndiye ambaye ndani yake makusudi yote ya Mungu juu ya watu wake yanatimizwa. (Yohana 14:6) Mtume Paulo alisema hivi juu yake: “Maana ahadi zote za Mungu zilizopo katika yeye ni Ndiyo; tena kwa hiyo katika yeye ni Amin; Mungu apate kutukuzwa kwa sisi [wanafunzi wa Kikristo].”—2 Kor. 1:20.
14. Tuna uhakikisho wa kupata nini tukifa tunapomtumikia Mungu?
14 Kwa hiyo Kristo ndiye mkuu ambaye ndani yake makusudi ya Yehova yanatimizwa. Tunaposali kwa Mungu kwa jina la Yesu, tunaweza kusema “Amina,” tukiwa na hakika kwamba tutapata tegemezo la kimungu kwa kujibiwa mambo tuliyoomba kulingana na mapenzi ya Mungu. (Ufu. 3:14) Hata tukipatwa na upinzani mkali sana, tunaweza kuwa na hakika, kwa maana hata tukifa tunalo tumaini hakika la kufufuliwa kwa wafu. Hii ni kwa sababu Mungu “amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua [Kristo] katika wafu.” (Matendo 17:31) Ni kana kwamba Mungu ametupa hati ya kufanyiwa hivyo, yenye muhuri yake. Kwa kweli, Biblia ndiyo hati hiyo. “Kumtolea Yesu ushuhuda ndiko kunakovuvia unabii,” kwa maana Yesu ndiye kweli.—Ufu. 19:10, NW.
15. Kama vile Zerubabeli wa kale, ni kwa njia gani Yesu haogopeshwi na kutikiswa kwa mataifa, na hii itakuwa na maana gani kwetu?
15 Tangu kumalizika kwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 C.E., mataifa ya ulimwengu wa wanadamu yanatikisika kwa maana Yehova ametetea enzi kuu yake kupitia kwa Ufalme wake wa Kimasihi na kujulisha mataifa hivyo kwa kuhubiriwa kwa ujumbe wa Ufalme. Kwa hiyo, Yehova wa majeshi ndiye mwenye kutikisa, sawa na alivyomwambia Gavana Zerubabeli wa kale. Mtikiso usioweza kuzuiwa na wanadamu utafikia upeo wake katika “dhiki kubwa” ambayo sasa inaonekana iko karibu sana. (Mt. 24:21, 22) Lakini Zerubabeli Mkuu, Yesu Kristo, haogopeshwi na mtikiso. Cheo chake cha kimbinguni cha ugavana kimeimarishwa kisiweze kutikisika. Ufalme wake ni “ufalme usioweza kutetemeshwa.” (Ebr. 12:28) Hautasogezwa. Utakapokwisha kuondoa dini yote ya uongo na mamlaka za ulimwengu za leo, utawabariki waabudu wote wa Yehova Mungu watakaookoka wakiwa katika hekalu lake la kiroho kwa kuwapa utawala mzuri milele.
16. Kwa sababu gani tegemezo walilo nalo Wakristo linawafanya wasiwe na woga mwingi sana juu ya upinzani unaoweza kuletwa na wanadamu?
16 Kwa hiyo, ingawa ni jambo la kawaida kuogopa uwezo ulio mkuu kuliko wetu wenyewe, Wakristo wa kweli wanalo tegemezo la Chanzo chenye uwezo wote katika ulimwengu wote. Yeye ndiye Muumba wa vitu vya kimbinguni, vingine vikiwa na ukubwa unaozidi jua letu mara milioni, naye ndiye Amiri wa majeshi yenye nguvu yasiyoonekana ya kimbinguni, ambaye mbele zake falme za ulimwengu si kitu. Haiwapasi Wakristo kuwa na woga mwingi sana hata walegee au waache kutii amri za Mungu kwa sababu ya mambo wanayoweza kutendwa na wanadamu. (Mit. 29:25) Kwa sababu ya kuwa na tegemezo hilo wao wako salama salimini wanapofuatisha kila hatua ya maisha zao kulingana na amri zake.
17. Ni hali gani ambazo zimewapata Wakristo wa kisasa kuthibitisha ahadi ya Mungu ya kuwapa watumishi wake tegemezo la kimungu?
17 Wakiwa na tegemezo hilo, wanao uhakika mwingi nao hawawezi kuzuiwa na mamlaka yo yote wanapoendelea kuuhubiri Ufalme. Tegemezo la Yehova limeonyeshwa kwa kuwakomboa wanapopingwa na kuchukiwa katika mataifa yote, kama Yesu alivyosema kwa unabii. (Mt. 24:9) Zaidi ya hayo, Yehova hasa ameyapa majeshi ya malaika kazi ya kuongoza utangazaji wa Ufalme na kukusanywa kwa watu wanyofu kwenye hekalu Lake la kiroho. (Ufu. 14:6) Wakiwa wanajua mambo haya, na wakiwa wameyaona na kupatwa nayo, Wakristo wa kweli watathubutuje kuogofywa walegee au waache kufanya kazi yao ya kuokoa uhai yenye tegemezo la kimungu?
—Kutoka Kitabu Paradise Restored to Mankind—by Theocracy!