Usijiache Uondolewe Katika Mbio ya Uzima
“Mtu hataishi kwa mkate tu, . . . Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”—Luka 4:4, 8.
1. Wakristo wanashiriki katika mbio gani ya maana, na zawadi ya wenye kumaliza vizuri ni nini?
WAKRISTO wamo katika mbio isiyo ya kawaida sana. Kushinda hakutegemei sana wepesi kama vile kunavyotegemea uvumilivu na kufuata kanuni za mbio yenyewe. Na ingawa huenda likaonekana kuwa jambo la ajabu, mbio hiyo haishindwi na mtu mmoja tu, bali na wote wanaobaki mbioni mpaka mwisho. Ni mbio inayopigwa katika njia iliyosongamana inayoingiwa kupitia mlango mwembamba, kuelekea kwenye uzima wa milele katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu. (Mt. 7:14) Zawadi ya ajabu ya uzima wa milele itapatikana na wote watakaomaliza vizuri, nayo inastahili kujizoeza sana na kujinyima unayopaswa kujinyima ndiyo ushinde.
2. Kwa sababu gani mbio hii si nyepesi, navyo viunzi vilivyo njiani vionweje?
2 Lakini hiyo si mbio nyepesi. Haimalizwi kwa siku moja. Na kuna hatari sikuzote ya kuondolewa katika njia ya uzima iliyo ngumu zaidi, uingizwe katika njia pana ambayo Yesu alieleza inaelekeza kwenye uharibifu. (Mt. 7:13) Katika mbio hii ya uzima ya kutoa jasho, udhaifu mbali-mbali wa mwili usiokamilika unaotoka ndani na mikazo na mambo yenye kuvutia katika ulimwengu ulio nje visipoonwa nyakati zote kama viunzi vya kurukwa, vitaondoa mtu mbioni. Kati ya mambo hayo makubwa yanayoweza kuondoa Mkristo, kwanza tutazungumza juu ya utafutaji wa mali za kimwili.
MAONI YANAYOFAA JUU YA MALI ZA KIMWILI
3. Kwa sababu gani maoni yanayofaa juu ya mali za kimwili ni ya maana?
3 Mwanadamu, ambaye aliumbwa na Mungu aishi duniani na kufurahia vitu vyake vingi, kwa asili anatamani vitu vyema vya maisha vilivyotolewa na Muumba wake. Kuvitamani kwenyewe si kubaya, lakini mtu anawezaje kufurahia mali zo zote za kimwili bila uhai na kadiri fulani ya afya? (Mt. 16:26) Mungu ndiye Mpaji wa Uzima, naye ana haki ya kuweka matakwa ambayo lazima yatimizwe ndiyo mtu aendelee kuwa na zawadi hiyo ya uzima. Yeye anaeleza mwanadamu waziwazi kwamba wasio na shukrani na wenye kujitafutia anasa tu hawatapata urithi wa milele duniani. Watakatiliwa mbali. Zaidi ya hayo, mtu akitafuta faida za kimwili tu na starehe sasa, bila kusitawisha kanuni za kiroho na adili zenye msingi imara katika ibada ya kweli ya Mungu, anakuwa na maisha ya bure sana na yenye kufadhaisha.
4. Yesu alionyeshaje ubora wenye kudanganya wa utajiri wa kimwili?
4 Yesu alionyesha mambo inavyofaa alipoonya hivi: “Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” Kisha akaonyesha jambo hilo kwa mfano wa tajiri aliyebomoa ghala zake apate kujenga kubwa zaidi kuwekea mazao yake yenye kuongezeka sikuzote. Akidhani wakati ujao ulikuwa salama sana kwake, akajiambia hivi: “Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi.” Walakini, Yesu aliendelea kusema hivi juu ya mtu huyo aliyekuwa ameweka tumaini lake katika mali za kimwili: “Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka [nafsi] yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?” Akionyesha maana, Yesu alimalizia kwa kusema: “Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”—Luka 12:15-21.
5. Ni nia gani zinazoweza kusitawi kwa vyepesi mtu anapofuatia mali za kimwili na starehe akijifikiria mwenyewe tu?
5 Kwa hiyo hatari ni nini hapa? Ni hatari ya kutafuta sana vitu vya kutosheleza tamaa za mwili wa mtu. Kwa njia hiyo mtu anasahau kwamba Mungu aliiumba dunia na mwanadamu na kumweka juu yake, na hivyo mtu hawezi kuwa mwenye furaha ya kweli na kutimiza kusudi la kuishi kwa kutumaini vitu awezavyo kujikusanyia karibu naye viwe usalama wa kimwili au starehe zake. Sikuzote mtu huyo anakuwa mwenye kufikiria yake mwenyewe tu. Hajali hali ya jirani yake. Anapojaribu kulinda mali zake zisichukuiiwe na wenye pupa, mara nyingi kunakuwa na jeuri na uuaji. Kujitumainia kunaelekeza kwenye kujitegemea. Mungu hata hakumbukwi, hata anasahauliwa mbali kama Mpaji halisi. Nayo ahadi ya uzima wa milele inakuwa ndoto tu. Mara nyingi mtu huyo anawaza hivi, Kuna sababu gani ya kufuatia jambo ambalo ni ndoto tu na hali inawezekana kupata starehe za kimwili sasa? Hivyo filosofia ya utafutaji wa mali za kimwili inaweza kwa vyepesi kuondoa mtu katika mbio ya uzima wa milele au kumzuia asiianze mbio hiyo.
6. (a) Sisi kama Wakristo tunawezaje kumwiga mpiga mbio katika kujitayarisha na kupiga mbio ya uzima? (b) Yesu alituwekeaje mfano bora wa kuiga?
6 Tofauti na huyo, mpiga mbio mzuri hajistareheshi bali anafuata ukawaida wa kujizoeza nyakati zote na kula chakula kinachomweka katika hali ya usawa. Katika mbio anavua vitu vyote visivyo vya lazima na kubaki na vilivyo vya lazima tu, naye anajiangalia sana asijikwae hata kuvunja kanuni asiondolewe mbioni. (1 Kor. 9:24-27; 2 Tim. 2:5) Akieleza waliyofanya wapiga mbio wa kale, Paulo alishauri Wakristo hivi: “Basi na sisi pia, . . . na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi [ukosefu wa imani] ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu.” Naam, Yesu mwenyewe alikuwa amepiga mbio hii akaonyesha namna ambavyo ingeweza kupigwa kwa matokeo mazuri. Ingawa kumaliza kwake mbio kwa ushindi kulimfisha katika mti wa mateso na kumletea aibu, baadaye Mungu alimpa zawadi ya uzima mtukufu wa kutokufa mbinguni katika mkono Wake wa kuume. Kwa sababu ya matokeo hayo mazuri, Paulo alisihi hivi: “Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”—Ebr. 12:1-3; 3:12, 13.
7. (a) Ni kanuni gani aliyoweka Yesu inayoonyesha kwamba haiwezekani mtu agawanye ushikamano wake kwa bwana wake? (b) Yehova ameahidi nini juu ya mambo yaliyo ya lazima, akituruhusu tutangulize nini?
7 Katika Mahubiri juu ya Mlima Yesu aliitaja kanuni hii: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” Halafu baada ya kueleza vile Yehova anavyoangalia mahitaji ya wanyama na mimea, na namna wanadamu ni “bora kupita hao,” akasema hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mt. 6:24-33.
8. Ni hazina gani mbili zenye kutofautiana ambazo Paulo aliandika habari zake, nayo matokeo ya kuzifuatia ni nini?
8 Mtume Paulo alionya hivi: “Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.” Badala ya kujiacha waondolewe na kuingizwa katika mwendo huu uwatosao ‘wanadamu katika uharibifu,’ Paulo alitia Wakristo moyo “wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Tim. 6:9, 10, 17-19.
9. (a) Kwa habari ya kupata mahitaji, Mkristo ana daraka gani, na hasa kichwa cha nyumba? (b) Ibilisi anawezaje kuondoa mtu kwa kutumia mali za kimwili?
9 Bila shaka tunahitaji matakwa yetu ya kila siku, na imetupasa tuyatafute kwa uaminifu na heshima tunapopiga mbio iliyowekwa mbele yetu. Kwa kweli, mwanamume asiyeruzuku jamaa yake angeondolewa mbioni, kwa maana kwa njia hiyo angekuwa ‘ameikana Imani, tena akawa mbaya kuliko mtu asiyeamini.’ (1 Tim. 5:8) Lakini hatuwezi kupiga mbio vizuri kwa kuacha tudanganywe na uzuri wa uongo wa kazi tunayofanya au kwa kuchukua mishahara tunayopata kutokana na kazi hiyo kuwa ndiyo mambo makubwa katika maisha. Ni jambo la lazima kupata mahali pa kukaa, lakini tukinunua nyumba ya pesa nyingi kuliko tunazoweza kupata na kutumia wakati wetu wote tukiinunulia vitu na kuitunza tunaweza kwa vyepesi kutoka katika mbio ya uzima. Ndivyo inavyoweza kusemwa pia juu ya gari au mashua, kutamani mavazi mapya na yenye mitindo mitindo kupita kiasi, kufunga safari za anasa zenye gharama nyingi au kujishughulisha kupita kiasi na mambo tupendayo kufanya tupishe wakati. Kumbuka, Ibilisi ana ujuzi wa miaka mingi wa namna ya kutumia mali za kimwili aunase moyo na kuondoa wasiojihadhari katika mbio ya uzima.
10. Mtu anaweza kuuliza maulizo gani aamue kufaa kwa kupata mali fulani za kimwili?
10 Unapotazama mbio iliyoko mbele, jifunze kuuliza hivi juu ya vitu vya kimwili: Je! hiki ni kitu cha lazima ili niendelee kuishi na kumtumikia Yehova? Je! hiki kitanisaidia niwe mtumishi bora wa Yehova, au kitanipunguzia mwendo? Hiki kitaniwekea wajibu na mizigo gani? Kweli nahitaji hiki ndiyo niruzuku jamaa yangu? Je! itanilazimu nifanye madeni ndiyo nikipate? Je! kitanipunguzia wakati nilio nao wa kujifunza Biblia, wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo na wa kuhubiri ujumbe wa Ufalme? Je! kwa njia yo yote kitaniondoa katika kusudi langu katika maisha?
11. Kwa sababu gani ni ubatili kufanya njia ya kujitafutia riziki katika taratibu hii ya mambo iwe ni jambo kubwa maishani?
11 Nyie wazazi, zoezeni watoto wenu wakaze fikira zao juu ya tumaini la Ufalme, ili waepuke maelekeo ya kutafuta mali za kimwili tu. Vijana leo wanatiwa moyo wajitayarishie njia za kujitafutia riziki watakazokuwa wakifuata katika ulimwengu huu wenye kutafuta mali za kimwili tu. Lakini kufanya hivyo kungekuwa kufanya alivyofanya kijana aliyekwenda kutafuta kazi baada ya miaka mingi ya masomo, kisha akaomba kazi katika iliyoelekea kuwa kampuni yenye kukua na yenye maendeleo, huku akikosa kujali ishara iliyokuwa mlangoni yenye kusema: “KAMPUNI HII INAENDELEA KUFILISIKA. JENGO HILI KUTUMIWA KWA MPANGO MPYA WA SERIKALI.” Taratibu hii ya kale pia itafilisika karibuni, ingawa sasa imejawa na shughuli za utafutaji wa mali za kimwili. Ili tuwe na wakati ujao ulio halisi, imetupasa tupange kila hatua kuhusiana na serikali mpya ya Yehova ya dunia hii kupitia kwa Mfalme wake Yesu Kristo.
12. Tunapotanguliza Ufalme na faida zake, huenda hufanya marekebisho ya kipekee kukatuwezesha kufanya nini?
12 Nguvu, mali na uwezo mbalimbali tulio nao vimepaswa vitumiwe kuendeleza faida za Ufalme, badala ya kuviacha viwe vizuizi katika mbio ya uzima. Kwa mfano, ikiwa wewe una nyumba ya ziada, je! unaweza kuiuza na kutumia pesa utakazopata uingie katika utumishi wa upainia badala ya kutia bidii utunze nyumba zote mbili? Ikiwa umejiuzulu kazi au karibuni utajiuzulu kutoka kazi ya kimwili, je! moyo wako unakuvuta utumie nafasi zaidi utakayopata ushiriki zaidi kuhubiri Ufalme? Ingawa huenda nguvu, mali na uwezo wako vikawa vichache, vinawezaje kutumiwa kwa njia nzuri zaidi katika kumtumikia Yehova?
13. Ikiwa tunapenda kweli, tutaonaje mali za kimwili?
13 Kusudi limepaswa kuwa kutumia mali za kimwili inavyohitajiwa, wala si kuwa watumwa wazo. Ikiwa tunathamini mambo ya kiroho kweli na kuweka uhusiano wetu na Yehova juu ya mambo mengine yote, yeye atatusaidia tuendelee kupiga mbio kwa uvumilivu na kupata zawadi. Ulimwengu pamoja na tamaa zake za mwili na tamaa za macho na kujionyesha kwa mtu mali yake “unapita . . . lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:15-17, NW.
KUJIEPUSHA NA UTUKUZO WA TAIFA
14. Ni vizuizi gani vinavyohusu utukuzo wa taifa vinavyokabili Wakristo wanapopiga mbio ya uzima?
14 Kizuizi kingine kinachowekwa kuondoa Wakristo katika mbio ya uzima kinahusu utukuzo wa taifa. Kizuizi hicho kinainuliwa juu zaidi na zaidi katika nchi zote tunapozidi kuingia ndani katika wakati wa mwisho. Mara nyingi mtu anapokabili kizuizi hiki, inaelekea kuwa kwamba mwendo wa hekima na unaofaa kufuatwa na mtu ni kuacha kupiga mbio na kuondoka. Kufanya hivyo kungeelekea kumwezesha mtu aepuke kulaumiwa na watu na kutofanyiwa jeuri zinazotumiwa na wakuu mara nyingi na makundi ya watu wenye ghasia wanaojaribu kulazimisha mtu afuate sheria au nia zisizopatana na Maandiko. Kwa upande mwingine, porojo za kutukuza taifa zinakusudiwa kuchochea mtu ajivunie taifa au kabila. Huo unafanywa uelekee kuwa mwendo mzuri wa kufuata. Kwa kweli, katika nchi nyingi utukuzo wa taifa umekuwa dini. Kwa sababu hiyo, kila taifa linadhani nchi yao na njia yao ya maisha ndiyo bora kupita zote kisha inakosa kuvumilia watu wengine.
15. Utukuzo wa taifa unaendeleza nia gani?
15 Mwandikaji Ivo Duchacek alisema hivi katika kitabu chake Conflict and Cooperation Among Nations: “Utukuzo wa taifa unagawanya mataifa katika mafungu mafungu ya kutovumiliana. Kwa sababu hiyo, badala ya watu kujifikiria kwanza kuwa wanadamu wanafikiria mataifa yao kwamba ni Waamerika, Warusi, Wachina, Wamisri au Waperu.” Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa U Thant alisema hivi: “Mengi ya magumu tunayokabili leo yanasababishwa na nia za uongo—nyingine zimefuatwa bila ya watu kujua. Kati ya hizo ni wazo la kutukuza taifa kwa upumbavu—kutetea ‘nchi yangu, iwe yenye haki au yenye kosa.’ “
16. Shadraka, Meshaki na Abednego walipambanaje na ulizo la utukuzo wa taifa katika Babeli?
16 Utukuzo wa taifa si jambo jipya. Ulianza katika Babeli na Nimrodi, mtu wa kwanza kujiweka kuwa mfalme kwa kumpinga Yehova. Karne nyingi baadaye Waebrania waliokuwa katika utumwa katika mji huo mwovu waliona sana ukatili na madai ya kupita kiasi ya utukuzo wa taifa. Shadraka, Meshaki na Abednego walikuwa kati ya raia za Nebukadreza waliokusanyika katika uwanda wa Dura wakaagizwa kusujudia sanamu ya kitaifa. Waabudu hao Waebrania wa Mungu wa kweli Yehova hata hivyo walikataa kuinama, ijapokuwa walitishwa kutupwa katika tanuru ya moto wakiwa hai. Walikuwa na ushujaa wa kumwambia mfalme mwenye kuwaka kwa hasira hivi: “Ee Nebukadreza, hatuna haja ya kukujibu katika neno hili. Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”—Dan. 3:16-18.
17-19. (a) Ni maulizo gani yanayofanana na hilo juu ya kutokuwamo kwa Kikristo yanayotukabili leo? (b) Yesu aliwekaje mfano alipokuwa akichunguzwa na Pilato? (c) Kuhusika katika utukuzo wa taifa kuliongoza Wayahudi waliomkataa Yesu kwenye nini?
17 Je! leo sisi tuna maoni ayo hayo ya watumishi hao waaminifu wa Mungu wa zamani? Wakati sheria ya kitaifa au watu watakapoelekea kutulazimisha tuiname mbele ya mifano ya kitaifa au kuisalimu kwa kuiabudu, watakapoelekea kutulazimisha tupigie viongozi wa kisiasa kura au kuunga mkono mipango ya kitaifa, je! tutakubali na kuondolewa katika mbio ya uzima? Au, badala yake tutafanya kama Yesu na Wakristo wa kwanza walivyofanya?
18 Yesu aliweka mfano bora alipokuwa mbele ya gavana wa Kirumi Pilato akijaribiwa. Wayahudi walidai kwa uongo kwamba Yesu alikuwa amejifanya mfalme wa kidunia. Ingalikuwa kweli, huo ungalikuwa uasi kwa serikali. Lakini Yesu alijibu ulizo la Pilato hivi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” Pilato alikuwa tayari kumfungua Yesu kwa sababu ya jibu hilo la kweli, lakini washtaki wake Wayahudi wakajibu: “Ukimfungua huyu, wewe si rafiki yake Kaisari; kila mtu ajifanyaye kuwa mfalme humfitini Kaisari.” Pilato aligombezana nao akisema: “Je! [nimtundike mtini] mfalme wenu!” Wakuu wa makuhani wakajibu: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.”—Yohana 18:33-38; 19:12-16.
19 Historia ina maandishi ya matokeo mabaya sana yaliyotokana na kuchagua kwao “Kaisari” badala ya Yesu kama Masihi, wakati Yerusalemu ulipoharibiwa miaka 37 baadaye na maisha nyingi zikapotea, na waliobaki kati ya wakaaji wake wakapelekwa utumwani kati ya mataifa. Ni nani aliyeendeleza kutokuwamo wakati huo kwa habari ya mambo ya ulimwengu huu wakati uo huo akiendelea kushikamana sana na ufalme wa Mungu? Yesu Kristo!
20. Wakristo wa kwanza walishawishwaje waondoke na utukuzo wa taifa?
20 Wakristo wa kwanza walifanya nini? Daniel P. Mannix, katika kitabu chake Those About to Die, alisema hivi: “Wakristo walikataa . . . kutolea akili nyingi za mfalme dhabihu—jambo ambalo leo kidogo linalingana na kukataa kusalimu bendera au kurudia kutaja kiapo cha uaminifu. . . . Ni Wakristo wachache sana walioacha imani zao, ingawa katika uwanja wa michezo kulikuwa na moto uliokuwa ukiwaka juu ya madhabahu waweze kuutumia. Jambo moja tu alilopaswa kufanya mfungwa ni kufukiza ubani kidogo sana katika mwali wa moto naye alipewa Hati ya Kutoa Dhabihu na kuachiliwa. Pia alielezwa kwa uangalifu kwamba kwa kufanya hivyo hakuwa akimwabudu mfalme; bali kwamba alikuwa akitambua tu sifa ya kimungu ya mfalme kama mkuu wa serikali ya Kirumi. Hata hivyo, karibu Wakristo wote walikosa kujipatia nafasi ya kufanya hivyo ndiyo waokoke.”
21. Kwa sababu gani Wakristo wanatazamia mateso kwa sababu ya kutohusika katika utukuzo wa taifa?
21 Kutoka karne ya kwanza hata leo utukuzo wa taifa umefanya Wakristo wateswe vikali. Lakini wale waliompenda Mungu na kukaza macho yao juu ya zawadi itakayopatikana mwishoni mwa mbio hawakukubaliana na watesi wao. Wao hawalioni kuwa jambo la kigeni kushindana na vipingamizi hivyo, kwa maana ilisemwa mapema kwa unabii kwamba ndivyo ingekuwa. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa.” Ingawa Mungu angeruhusu jaribu hilo liwapate watu wake ili nao watoe ushuhuda, Yesu aliongeza hivi: “Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na [nafsi]; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na [nafsi] pia katika jehanum.”—Mt. 10:16-18, 28.
22. Kwa sababu gani sasa, tukiwa ndani zaidi katika “wakati wa mwisho,” ni vigumu zaidi kujiepusha na utukuzo wa taifa?
22 Biblia inaonya kwamba hasa “wakati wa mwisho,” tengenezo la Ibilisi la kisiasa lingetumia masharti ya kiuchumi juu ya watu wenye kumcha Mungu kwa sababu wasiokubali kuabudu taratibu hii yenye mfano wa mnyama wasingeweza “kununua wala kuuza, isipokuwa [wana] chapa ile” ya mnyama huyo. (Ufu. 13:17) Ikitokea katika nchi yako hata kitambulisho cha chama cha kisiasa kitakiwe ndiyo upate kazi au mambo mengine yenye kufaa, wewe utafanya nini? Bila shaka, unahitaji kazi ndiyo uweze kuangalia jamaa yako. Ukiwa chini ya mkazo, wewe utafanya nini? Wewe utamtumaini nani akuruzuku? Je! utafadhaika usahau kwamba umekuwa ukisali hivi kwa Mungu: “Utupe leo riziki yetu”? (Mt. 6:11) Yehova anajua kwamba tunahitaji chakula, mavazi na mahali pa kukaa, lakini ni jambo la maana kukumbuka kwamba Adui, Shetani Ibilisi, anakaza ulizo la ukamilifu katika pande zote za maisha. Kama vile katika habari ya Ayubu, huenda akatokeza shtaka juu ya ye yote kati yetu kwamba atampa Mungu kisogo akinyimwa mengine ya mahitaji ya kimwili. Lakini onyo linatolewa kwamba hakuna jina linaloandikwa katika kitabu cha uzima la wale wanaoabudu taratibu yenye mfano wa mnyama. (Ufu. 13:8) Kwa kuendeleza ushikamano wetu na Yehova tukiwa chini ya jaribu, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yeye atafungua njia na kuleta faraja.
23. (a) Ni hali gani ambazo zingeweza kufanya iwe vyepesi kwa Wakristo kuhusika katika makusudi yanayohusu watu wote? (b) Kwa sababu gani haitupasi kudhani imetupasa tutumie nguvu kutengeneza mambo wakati tunapofanyiwa udhalimu wa kijamii?
23 Nyakati nyingine vizuizi vya kijamii, vya kikabila na vya kidini na chuki zisizo na sababu juu ya watu zinaletea wengi magumu na uonezi. Mara nyingi zinafanya mbio ya uzima ya Mkristo kuwa ngumu zaidi. Kunakuwa na maelekeo ya kupiga kelele, kujitetea, kutumia nguvu ili kulipia au kutengeneza mabaya, kudai haki kwa nguvu. Kwa mfano, huenda kikundi cha wachache kikatetea kwa nguvu kupata haki zaidi. Maandamano ya kuteta huenda yakatayarishwa ili kulazimisha serikali. Huenda wafanya biashara wakawekewa mkazo kwa kupangiwa kuvunjiwa uhusiano wa kibiashara. Huenda viongozi katika kikundi cha watu wakavuta watu wao wawe na kiburi, na huenda wakataka waungwe mkono na Mkristo kwa usemi au kwa nguvu. Wewe utafanya nini ukikabiliwa na hali hii au nyingine inayofanana nayo? Tena kuna uhitaji wa kuendeleza ukamilifu na kuepuka kuhusika katika mambo ya ulimwengu huu. Endelea kuwa na hakika kwamba Yehova atataka hesabu ya makosa yo yote yaliyotendwa. “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena [Yehova].”—Rum. 12:17-19.
24. Wenye kujidai kuwa Wakristo wamefuata mwendo gani, lakini wanakosa kujua nini juu ya jambo hilo?
24 Kwa hiyo, usijiache uondolewe katika mbio ya uzima na porojo au mkazo unaokusudiwa kukuachisha kutokuwamo kwako kwa Kikristo. Utalaumiwa-laumiwa kwa sababu hiyo, kwa maana maelekeo katika Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) leo ni kufanya mitaa ya wanadini na wachungaji wao wahusike katika makusudi ya kijamii. Wao wameacha kungojea ufalme wa Mungu ulete njia halisi zinazohitajiwa kuondoa magumu ya kijamii ya mwanadamu, nao wamejiunga na mambo ya ulimwengu. Lakini wanakosa kutambua kwamba hata mtu awe upande gani katika ulimwengu huu, bado yuko upande wa Ibilisi, ikiwa anaunga mkono kwa bidii wo wote wa mipango na kanuni zinazotolewa na taratibu hii ya mambo.
25. Kwa sababu gani tunaweza kumtumaini Yehova kabisa tutakapokuwa tukikabili maulizo ya wakati ujao juu ya utafutaji wa mali za kimwili na utukuzo wa taifa?
25 Kwa hiyo, wala utafutaji wa mali za kimwili wala utukuzo wa taifa usikuondoe katika mwendo wako kama Mkristo. Mtumaini Mungu kabisa na ufalme wake kupitia kwa Mwanawe, Kristo Yesu. “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?” (Ebr. 13:5, 6) Lakini viko vipingamizi vingine vinavyoweza kuondoa Mkristo katika mbio ya uzima wa milele, na katika mafunzo yanayofuata tutavizungumza.