Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 2/15 kur. 84-89
  • Usijiache Unaswe na Mitindo na Tafrija

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usijiache Unaswe na Mitindo na Tafrija
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MITINDO YA AFYA INAWEZA KUWA MTEGO
  • KUTOACHA TAFRIJA ZITUTEGE
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani Inayofaa
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Vitumbuizo vya Kijamii —Furahia Manufaa, Epuka Mitego
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Waweza Kupata Vitumbuizo Vifaavyo
    Amkeni!—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 2/15 kur. 84-89

Usijiache Unaswe na Mitindo na Tafrija

“[Waonye] kwa upole wao washindanao . . . ili ikiwezekana, Mungu awape kutubu na kuijua kweli; wapate tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata kuyafanya mapenzi yake.”​—2 Tim. 2:25, 26.

1. Njia za Shetani za kunasa mapendezi ya viumbe vya kibinadamu zinafananishwaje na mitego?

WAINDAJI wanajua uhitaji wa kuficha mitego yao wanase wanyama wasiojua neno. Kabla ya mateka kujua lo lote, mtego unawafyatukia au wananaswa barabara na mtego. Mitego mingine inawekewa chambo, na wanyama wengi wamenaswa kwa sababu ya kuondolewa kwa uangalifu wao na tonge la mlo lenye kushawishi lililo katikati ya meno ya chuma ya mtego. Adui ya Mungu, Shetani Ibilisi, ametengeneza taratibu inayoongozwa na tamaa ya kichoyo, nayo taratibu hii imejawa na mitego na mambo ya kunasa ambamo Mkristo anaweza kunaswa kwa vyepesi na kwa njia yenye msiba asipoendelea kuwa macho.​—Zab. 119:110.

2. Kwa sababu gani imewapasa Wakristo wawe macho zaidi leo?

2 Na kwa kuwa tunaishi ndani zaidi katika “wakati wa mwisho,” iko hatari zaidi kwa wengine ya kunaswa si katika mitego yenye kushawishi ya ulimwengu huu tu, bali pia ya kuacha siku kuu ya Yehova iwafyatukie kama mtego. Wakiwa wanajishughulisha sana na mambo ya kilimwengu, wakati wa Yehova wa kuharibu waovu utawajia kama mtego uliofichwa ambao umefyatuliwa kwa ghafula nao wataharibiwa. (Luka 21:34, 35) “Miiba na mitego huwa katika njia ya mshupavu; yeye aitunzaye nafsi yake atakuwa mbali nayo.”​—Mit. 22:5.

3. Mtindo unafafanuliwaje, na kuna hatari gani ya kufuatia mitindo?

3 Mitindo na tafrija inakaziwa fikira zetu katika funzo hili kwa maana inaweza kuwa ndiyo mitego ya Ibilisi iliyowekwa kwa hila zaidi ikiwa na chambo ili kushawishi Wakristo. Mtindo unafafanuliwa kuwa desturi au njia ya kujifurahisha inayofuatwa kwa muda kwa juhudi ya kupita kiasi. Ni mapendezi mengi mno au wazo la jambo linalokaa kwa muda tu. Iko mitindo mingi, lakini pengine mitindo inayoonekana sana ni ile inayohusu kuvalia na kujipamba, na maakuli. Ingawa mitindo ni mambo yanayofuatiwa kwa muda tu, inaweza kunasa mapendezi na wakati wa Mkristo hata mambo ya maana yanayohusu ibada ya kweli na kutimiza takwa la Mungu la uzima yakawa hayana ubora mwingi.

4. Ni mitindo gani ya kupita kiasi ya kuvalia imetokea miaka ya karibuni?

4 Katika maeneo fulani ya ulimwengu mitindo ya mavazi ya wanaume na wanawake haibadiliki sana kila mwaka, lakini katika nchi nyingi, kwa miaka kadha kumekuwa na maelekeo zaidi juu ya mitindo ya kupita kiasi isiyo ya adabu, hata wengine wakawa na maoni ya kwamba “cho chote chafaa.” Kuwa kwao na mawazo ya ufisadi, ya kiburi au ya uasi hakuwatoshi. Kunakuwa na lazima ya kusonga mbele na kutangaza na hata kutembeza mno nia hizo mbele ya wengine kwa mitindo yao ya kujipamba na kuvalia. Katika nchi za Uzunguni twaona wanaume wakizidi kuvalia kama wanawake, na wanawake wakizidi kuvalia kama wanaume. Mitindo mingi inayopendwa sana sasa na watu ilikuwa ikionwa kuwa ya kimashamba miaka michache iliyopita.

5. Mitindo ya Kuvalia na kujipamba inawezaje kuwa mtego wa Ibilisi?

5 Kwa sababu ya hali hizi, wanaume na wanawake wa Kikristo wanawezaje kuamua mavazi ya kuvaa au yasiyo ya kuvaa? Kwa asili, hawataki kuwa tofauti kama washamba au watu wa kikale, lakini kupita kiasi kwa upande mwingine na kuacha ulimwengu wa zamani uweke fikira za mtu juu ya mitindo ya kuvalia na kujipamba tu kungekuwa kuanguka mle mle ndani ya mitego hii ya Ibilisi yenye kushawishi. Yeye anajua sana kwamba mtu akiweza kushawishwa achukue hatua ya kwanza ya kujitambulisha waziwazi na mitindo ya ulimwengu huu anaousimamia, si vigumu sana kumshawishi achukue hatua zaidi za kuingia katika shughuli za kilimwengu.

6. Ni nini kitakachomwongoza Mkristo anapochagua mtindo wa kuvalia na kujipamba?

6 Katika 1 Timotheo 2:9, 10, wanawake wa Kikristo wanasihiwa wawe na mavazi ya kiasi, wajipambe kwa adabu. Bila shaka, kanuni hiyo inahusu wanaume pia kundini. Tunapoamua kama tutavaa mtindo fulani, tunaweza kujiuliza kama kuvalia au kujipamba kwenyewe kunaonyesha adabu, au kama si kwa adabu na kunaudhi wengine. Suruali za kubana zinaelekea kutokuwa za adabu kwa mwanamume, sawa na vile mavazi mafupi au yenye kufunua uchi yanavyoweza kutokuwa ya adabu kwa mwanamke. Wakati dada anapoinama au kujaribu kuketi kwa adabu jukwaani, je! anapata ugumu kwa sababu ya vazi lake fupi? Je! inawezekana tunapotoa wengine wadhani sisi ni wafisadi au wenye nia ya kiburi, ya kutaka vita, kwa vile tunavyovalia au kujipamba?

7. Ni uhakika gani wa maana utakaosaidia mashahidi wa Yehova wa Kikristo wavalie inavyofaa, hata wawe wapi duniani?

7 Mashahidi wa Yehova wa Kikristo ni watumishi wa Yehova, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, na kutambua hivyo bila shaka kumepaswa kuamue namna tunavyovalia. Watu katika eneo fulani wanatazamia nini kwa watumishi wa Mungu? Mitindo inatofautiana ulimwenguni pote na kwa hiyo si juu ya baraza inayoongoza ya mashahidi wa Yehova kuamua mitindo halisi inayofaa au iliyo ya adabu kwa kila nchi au mtaa. Ikiwa kuna mashaka sana juu ya mtindo fulani, ingekuwa afadhali kutouvaa. Afadhali kuonekana wa kimashamba kidogo kuliko kuonekana kuwa wasio na adabu au wenye kiburi au walio ovyo ovyo.

8. Dada anawezaje kujua kama itafaa avalie suruali katika mtaa wake?

8 Ikiwa suruali za wanawake zinakunjiwa nyuso na wengi mtaani, inaelekea mtindo fulani tofauti wa kuvalia hadharani ungemfaa dada wa Kikristo. Nyakati za baridi anaweza kupanga muda kwa muda asivae mavazi mazito, au mara kwa mara anaweza kujipasha moto. Lakini nyakati za baridi nyingi sana, ambapo kila mtu mtaani anavalia mavazi yanayofaa hali ya hewa, kama vile suruali za kike, bila shaka inafaa wanawake wa Kikristo nao wafanye vivyo hivyo. Sehemu nyingine, mapainia wamesaidiwa kwa njia hiyo wawe wenye afya kuweza kukaa saa nyingi katika utumishi. Ikiwa dada wa Kikristo ana mashaka juu ya mtindo fulani, anaweza kuzungumza jambo hilo na mumewe au na mzee katika kundi la Kikristo. Wazee wasijaribu kutwika wengine mapendezi yao wenyewe, lakini inaelekea wanaweza kutoa mashauri juu ya yanayoweza kukubalika katika mitaa yao. Imewapasa watoto wawe watii kwa wazazi wao katika mambo yanayohusu kuvalia na kujipamba.

9. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha uhitaji wa kufanya mabadiliko katika sura ya mtu inapofaa, ili kuepuka kuwekea wengine kizuizi wasijifunze njia ya uzima?

9 Mitindo ya nywele ya kupita kiasi inaweza kwa vyepesi kuongoza mtu kwenye mtego wa Ibilisi pia, na kukwaza wengine. Kwa mfano, kijana mmoja katika United States alikuwa akifanya maendeleo mazuri katika kujifunza Biblia, naye akataka kushiriki na Shahidi mwenye ujuzi kuhubiri wengine juu ya mambo mema aliyokuwa akijifunza katika Biblia. Tangu ujana wake alikuwa ameacha ndevu zake zikue, na kwa kuwa wengine wa wafanya biashara walikuwa na ndevu, yeye alidhani kuwa na ndevu anapohubiri wengine kungekubaliwa na watu wengi. Lakini alipokuwa akizungumza na mama mmoja hakuweza kusema mengi kabla ya kuambiwa hivi naye: “Pole, kijana, mimi sitaki kuingia katika uasi wa wanafunzi.” Hata maelezo mengi namna gani hayakutosha kuondoa maoni mabaya aliyoleta baada ya hapo. Mazungumzo yalipokwisha mlango ulipofungwa, kijana huyo akamwuliza Shahidi yule mwenye ujuzi sababu ya mambo kuwa hivyo. Aliombwa afikirie sura yake kuhusiana na alivyojidai kuwa, mtumishi wa Mungu. Kwa sababu hakutaka kuwa na lawama la hata kukwazika kwa mtu mmoja tu hata akose njia ya uzima wa milele, mhubiri huyu mpya wa Ufalme alinyoa ndevu zake. Je! wewe ungekuwa na nia ya kufanya mabadiliko kama hayo sura yako ikitoa maoni mabaya katika mtaa fulani?

10. Mtu anawezaje kuharibu kusudi la kwenda mtaani akahubiri habari njema za Ufalme kwa mitindo ya kuvalia au kujipamba?

10 Lazima tujue kwamba watu wa Yehova wanachunguzwa sana sana na ulimwengu. Ujumbe wa Ufalme wanaopelekea watu unaamuliwa ulivyo na sura ya wale wenye kuupeleka. Inawezekana ndugu au dada wa Kikristo aliyevalia mtindo fulani akavuta akili za mtu mlangoni hata mtu huyo akakosa kusikiliza anayosema Mkristo, au akaazimu kwamba sisi si tofauti na walimwengu katika adili au kanuni. Ikiwa ndivyo, mwenye kupeleka ujumbe anaharibu kabisa kusudi lake la kufanya utumishi wa shambani. Nyakati nyingine tunatakiwa tujinyime mambo fulani yanayotufaa kwa njia kubwa au ndogo, kulingana na uhitaji, ili kuepuka kukwaza wengine. Hii ndiyo iliyokuwa nia ya mtume Paulo: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu.”​—2 Kor. 6:3, 4.

MITINDO YA AFYA INAWEZA KUWA MTEGO

11. Mitindo ya afya inawezaje kuwa mtego kwa Mkristo?

11 Kumetokea mitindo mingi kuhusiana na kula na kuangalia mwili. Lakini mitindo ya afya pia inaweza kututega. Kuna hatari ya kushughulika sana na maakuli na magonjwa hata mambo hayo yanakuwa ya maana zaidi kuliko kuhubiri ufalme wa Mungu na kutazamia taratibu mpya ambapo mwili utaponywa kabisa. Bila shaka, imetupasa tutumie hekima inayofaa sasa tujiangalie, na maakuli fulani au dawa huenda zikafaa hali zetu wenyewe, lakini hayo yamepaswa kuwa mambo ya kipekee yaliyo madogo yakilinganishwa na utumishi wetu kwa Yehova. Paulo alishauri kwa imara tusitokeze matata juu ya vyakula. (Rum. 14:1-23) “Basi, mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Kwa hiyo, usiache mitindo ya chakula wala ya afya iwe mtego kwako au kikwazo kwa wengine.

12. Kuchunguza mitindo inavyofaa kwa msaada wa Biblia kutatuonyesha nini?

12 Imetupasa tujue kwamba mitindo, iwe inahusiana na mavazi, kujipamba au chakula, au mambo mengine, inaweza kutuzuia tusifanye mapenzi ya Mungu na kutegwa na mambo ya ulimwengu. Mara nyingi mitindo inahusu gharama zaidi, na ili kuweza kulipia gharama hizo inataka kufanya kazi zaidi ya kimwili. Basi, mitindo ni mitego ya hila ya Adui mkuu, Shetani Ibilisi. “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.”​—Efe. 5:15-17.

KUTOACHA TAFRIJA ZITUTEGE

13. (a) Ibilisi ametumiaje tamaa ya mwanadamu ya kuwa na tafrija na kumdhuru? (b) Kukipangwa kuwe na tafrija, imepawa itimize nini?

13 Baba yetu wa kimbinguni alitupa uwezo wa kufurahia anasa za namna mbali-mbali kwa kumwumba mwanadamu, kutia na uwezo na njia za kujifurahisha sisi wenyewe na wengine. Lakini mara nyingi Ibilisi anatumia nafasi ya kufurahia mema na kuipotoa hata inakuwa mbaya, yenye kuleta aibu au kudhuru mwanadamu. Ndivyo hasa imekuwa kwa habari ya tafrija (au kujifurahisha). Wakristo wanajua kwamba tafrija zinazofaa zinatimiza uhitaji fulani. Zinaleta badiliko lenye kufurahisha katika mwendo na utendaji wa maisha, hata miili na akili zetu zinapata pumziko na burudisho linalohitajiwa. Walakini, ili tafrija zifaidi, zimepaswa kuwa zenye kujenga na kutia moyo, si zenye kudhuru kimwili wala kiroho.

14. Ni maulizo gani yatakayosaidia kuchagua tafrija yenye kujenga na kutia moyo?

14 Hivyo, wakati wa kuchagua tafrija, imetupasa tujizoeze kuuliza hivi: Je! zinapatana na kanuni za Kikristo? Zitahusuje mioyo na akili zetu? Zitahusuje wengine? Kuwa macho hivyo kutazuia tafrija zisiwe mtego unasao mapendezi yetu kabisa hata tuondolewe katika imani au kunaswa katika mwenendo usio wa Kikristo.

15, 16. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wanapendezwa sana na michezo kama namna ya tafrija? (b) Ni maoni gani ya kiasi imewapasa Wakristo wawe nayo juu ya michezo?

15 Mojawapo ya njia kuu za kujifurahisha katika ulimwengu ni kutazama au kushiriki michezoni. Tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili watu wamekuwa wakipenda sana michezo mbalimbali. Viwanja vya michezo vinajaa pomoni. Wapenda michezo wanajikaza wavumilie hali mbaya ya hewa, wanasafiri sana, na kulipa pesa nyingi sana waone michezo. Wengine wanaweza kueleza mambo mengi sana juu ya wachezaji na michezo, kuonyesha kadiri ambavyo mambo hayo yanachukua wakati na fikira zao.

16 Alipokuwa akimpa mwangalizi kijana Timotheo maagizo, mtume Paulo alisema hivi: “Nawe ujizoeze kupata utauwa. Kwa maana kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:7, 8) Hivyo mtume Paulo alijua kwamba kujizoeza kupata nguvu za mwili kunaweza kuufaa mwili, lakini lazima kufanywe kidogo kukilinganishwa na lengo kubwa la utawa. Michezo inaweza kuleta ushirika unaofaa, inaweza kufurahisha na kutoa mazoezi yanayofaa mwili na akili pia ikifanywa kwa kiasi, lakini kujitia kupita kiasi katika anasa hiyo kunaweza kumkosesha mtu usingizi au pumziko lililo la lazima. Hilo lisingekuwa jambo la hekima. Huenda tukaanza kuona michezo kama ya maana sana na kuishiriki kwa bidii ya kupita kiasi. Madhara makubwa yanaweza kutokea. Michezo inaweza kukuza roho ya kushindana. Walakini, Mkristo mwenye kiasi anaepuka roho ya kushindana inayofanya mtu ajivune kwa sababu ya kushinda wengine michezoni. (Gal. 5:26) Kiasi ni cha lazima ili kuhifadhi nguvu na wakati pia wa mambo ya maana zaidi yanayohusu utawa. Biblia inashauri hivi: “Kiasi chenu na kijulikane na watu wote.” (Flp. 4:5, NW) Yesu alionya tujihadhari na “anasa za maisha haya” zisilisonge “neno la Mungu” lililopandwa moyoni.​—Luka 8:11, 14.

17. Kwa sababu gani imewapasa Wakristo vijana wajiangalie shuleni wasije wakanaswa na michezo?

17 Wakristo vijana hasa wanapaswa wajiangalie shuleni wasiache michezo iwe ndilo jambo la maana zaidi maishani mwao. Kushiriki katika michezo kupita kiasi kunaweza kufanya mtu aachilie mbali kujifunza Biblia na utendaji wa Ufalme. Uzuri wa kudanganya wa kuwa katika kikoa (timu), msisimko wa kushinda michezo, ni mitego ya hila inayoweza kunasa Mkristo bila ya yeye kujua. Kutojiangalia kiroho, huku mtu akivutwa na mashirika mabaya, roho ya kushindana na tamaa ya kujulikana na watu wengi, yote hayo yanaweza kuleta mauti. “Sheria ya mwenye akili ni chemchemi ya uzima, ili kuepukana na tanzi za mauti.”​—Mit. 13:14.

18. Mtu akitazama sinema, televisheni au michezo ya jukwaani apate kujifurahisha, kwa sababu gani imempasa achague kwa uangalifu mambo ya kutazama?

18 Je! mtu aweza kutazama sinema, televisheni, au michezo ya jukwaani apate kujiburudisha? Bila shaka hilo ni jambo la kuamuliwa na mtu mwenyewe. Lakini Biblia inaonya hivi: “Mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo, bali mgeuzwe kwa kubadili akili zenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Rum. 12:2, NW) Lazima Wakristo wakubali kwamba Shetani ndiye “mungu wa taratibu hii ya mambo,” na wingi wa wanadamu wanaoishi leo wamekuja chini ya maongozi yake maovu. “Ulimwengu mzima uko katika nguvu ya yule mwovu.” (2 Kor. 4:4; 1 Yohana 5:19, NW) Hiyo ni wazi tunapoangalia mengi ya mambo yanayoonyeshwa katika sinema na televisheni na katika michezo ya jukwaani leo. Wenye kutayarisha mambo ya kuonyesha wanafanya biashara, na wengi wao wanakueleza waziwazi kwamba kinachowapatia pesa leo ni maonyesho ya ngono na jeuri. Kwa hiyo, washiriki wa jamaa ya Kikristo wakitazama sinema mara kwa mara au michezo ya jukwaani wapate kujifurahisha, wana daraka la kuchagua kwa uangalifu mambo watakayotazama.

19. Kwa sababu gani hatuwezi kukosa kujihadhari na tafrija isiyofaa?

19 Lakini ijapokuwa ujitahidi kuchagua yanayofaa, huenda wakati fulani ukajikuta ukitazama televisheni au ukiwa katika jumba la sinema ambamo mambo yanayoonyeshwa yamekuwa si yenye kufundisha tena, si yenye kufurahisha wala kuburudisha tena. Yanachafua. Je! utakuwa na ushujaa wa kusimama na kufunga televisheni au kuondoka katika jumba la sinema? Lazima sikuzote tuwe macho kuangalia mambo yanayoingia katika akili na mioyo yetu, si kudhani kwamba lazima tupate kujua habari za ubaya ndiyo tusadiki ni mbaya. Hakuna nafasi ya kutafakari juu ya mambo ya ufisadi au ya jeuri au mapotovu ikiwa tunaendelea ‘kuyatafakari’ mambo “yaliyo ya staha, . . . ya haki, . . . yaliyo safi, . . . yenye kupendeza, . . . yenye sifa njema, ikiwapo sifa nzuri yo yote.”​—Flp. 4:8.

20, 21. (a) Kwa sababu gani imewapasa wazazi wa Kikristo wachunguze sana mambo ambayo watoto wao wanatazama katika televisheni? (b) Badala ya kuacha kipindi cha mambo yasiyofaa sana kiharibu wakati wa mtu, ni nini linalopendekezwa?

20 Wachunguzi wanasema kwamba mtoto wa kawaida katika United States anatumia saa 500 kufikia 1,000 kwa mwaka akitazama televisheni. Wazazi wengine wanaweka watoto wao mbele ya televisheni kuwatuliza, kwa sababu hawataki kusumbuliwa nao. Lakini kufanya hivyo kunatendeaje watoto, ambao akili zao zinavutwa sana na mambo? Daktari wa kuchunguza akili za watoto Dr. Arthur R. Timme alionya kwamba njia hiyo ya kutulizia watoto “inadhuru sana akili ya watoto wenye kukua. . . . Wao wanakua wakiwa na maoni yaliyopotoka kabisa juu ya mambo yaliyo haki na mabaya katika tabia ya kibinadamu.” Vyanzo vya habari kila siku vinatoa habari za watoto wanaohusika katika uvunjaji wa sheria wa kutumia nguvu na upotovu, na inajulikana wazi juu ya mahali walipotoa mawazo mengi ya kufanya mambo hayo ya kustaajabisha. Nyie wazazi, je! mnachunguza sana mambo ambayo watoto wenu wanatazama katika televisheni?

21 Imeonekana pia kwamba watu wazima wengine wanafungua televisheni na kutazama lo lote linaloonyeshwa, badala ya kusoma, kuwaza, au kuendesha utendaji mwingine wenye kujenga. Mara nyingi chumba kinakuwa kimejawa na kelele, na kukitulia kidogo, fujo zinatokea. Lakini watumishi wa kweli wa Mungu hawawezi kujiacha wawe sehemu ya hiki “Kizazi cha Tafrija.” Wakati ni wenye thamani mno kutoweza kupotezwa. Nyakati hizo, ingeburudisha namna gani kufunga televisheni na kusoma kwa utulivu kisehemu cha Neno la Mungu! Hiyo inahitaji mtu ajiadibishe, lakini inathawabisha sana.

22. Mkristo akichagua kucheza dansi kama namna ya tafrija, ni maulizo na kanuni gani zinazoweza Kumwongoza?

22 Kucheza dansi ni namna nyingine ya tafrija (au kujifurahisha). Ilitumiwa katika nyakati za Biblia kama namna ya kuonyesha furaha na kumsifu Mungu. (Zab. 149:3;150:4) Je! Mkristo anaweza kushiriki katika dansi za kisasa? Kila mtu atajiamulia la kufanya. Yako mambo ya kuamulia yanayopaswa kufikiriwa. Je! Mkristo atacheza dansi na nani? Yeye atakuwa akishirikiana na nani? Dansi yenyewe itachezewa wapi? Chanzo cha dansi hiyo ni nini? Ni miendo gani ya kujipindua-pindua inayohusika? Je! ina maelekeo ya kuleta mawazo machafu akilini, au ni ya kuzoeza mwili tu na kuleta furaha inayofaa? Wakristo waliooa au kuolewa wakicheza dansi, inafaa wafanye hivyo na wenzi wao wenyewe. Wakristo wasiooa au kuolewa wakicheza dansi mvulana kwa msichana, wafanye hivyo kwa adabu wala si kwa njia ya kuchocheana nyege. Kucheza dansi katika majumba ya kilimwengu ya dansi kunaweza kuwa hatari, si kwa sababu tu ya hali iliyoko, kwa kawaida ya kuwa mbali na Wakristo wenzako, bali pia kwa sababu ya mashirika mabaya. Hata wakati Wakristo wanapokutana wacheze dansi, ni vizuri zaidi kutokuwa na watu wengi katika kikundi hicho, kwa maana kwa vyepesi mambo yanaweza kukosa kuzuilika na wengine wakaruka mipaka ya hekima. Tunataka kutenda kwa njia ya kujilinda wenyewe, na pia kuepuka kukwaza wengine. (1 Kor. 8:9; Rum. 13:14) Ikiwa tunafurahia kucheza dansi, na tuchague zinazofaa, za adabu na kiasi, tukifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.​—1 Kor. 10:31; 1 Pet. 1:15, 16.

23. Ni kwa njia gani mtu anayetaka kumpendeza Yehova anavyoweza kuepuka muziki usiwe mtego kwake?

23 Muziki unaweza kuwa namna nzuri ya tafrija, lakini unaweza kuwa mtego pia tukiuruhusu uwe hivyo. Mwingi wa muziki unaotungwa na kupigwa leo unakusudiwa kuchochea tamaa za mtu za kichoyo. Kwa hiyo, imempasa Mkristo ajiulize hivi juu ya namna yo yote ya muziki: Chanzo chake ni nini? Kusudi lake ni nini? Matokeo yake yatakuwa nini juu yangu? Je! muziki wangu unasumbua wengine? Muziki fulani, kama vile “rock ‘n’ roll,” wa karibuni, unaonyesha roho ya uasi na mara nyingi unakuwa na maneno yenye kutia watu moyo wafanye jeuri. Inafaa Mkristo achague muziki utakaofurahisha, kuburudisha na kumwacha akiwa na dhamiri njema.

24. (a) Kusudi la Ibilisi la kuweka mitego inayohusiana na mitindo na tafrija ni nini? (b) Tunapojiepusha na mitego hiyo ya mauti, imetupasa tujione kuwa na wajibu gani juu ya wanyofu wanaotaka kutoka mtegoni?

24 Ulimwengu huu unapozidi kutopea-topea katika upotovu wake wenyewe na kukaribia kuharibiwa, Wakristo wanaujua ubora wa kutonaswa na roho ya ulimwengu huu. Wao wanajua kwamba mitindo na tafrija za ulimwengu huu ni kama vishawishi vya kuvuta wanadamu waingie ndani ya “mtego wa Ibilisi.” (2 Tim. 2:25, 26; Zab. 140:4, 5) Tayari amekwisha nasa wengi wa wanadamu, lakini angependa kushawishi watumishi wa Mungu waingie mtegoni pia, huku akijaribu kudumisha wanyofu wanaotaka kutoroka mtegoni. Karibuni sana yeye mwenyewe atatiwa mnyororo na kufungwa shimoni, lakini kwa sasa katika wakati mfupi unaobaki, tunaweza kujiepusha na mitego yake ya mauti tukiangalia sana tunavyotembea mbele za Yehova, tukiangaza Neno lake la kweli sikuzote katika njia yetu. (Ufu. 20:1-3; Zab. 119:105) Nasi tuna pendeleo la kusaidia wale wanaojaribu kutoka mtegoni kwa kuwatangazia kweli inayoweka wanadamu huru na kwa kuonyesha kwamba sisi kweli ni wapenda Mungu wala si wapenda anasa tu.​—2 Tim. 3:4, 5; Yohana 8:32.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki