Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 2/15 kur. 90-95
  • Usiache Imani Yako Iangamizwe na Kuvunjika Moyo Wala Nyutu za Watu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usiache Imani Yako Iangamizwe na Kuvunjika Moyo Wala Nyutu za Watu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUACHA KUVUNJIKA MOYO
  • NYUTU ZA WATU ZINAWEZA KUANGAMIZA IMANI YA MTU
  • KUCHUKULIANA KWA UPENDO
  • EPUKA KUKWAZA WENGINE
  • Tunaweza Kufanya Nini Tunapovunjika Moyo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Tianeni Moyo Kwa Kadiri Siku Ile Inavyokaribia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Nanga Yao Ni Tumaini, Nao Huchochewa na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Jinsi Unavyoweza Kushinda Hisia za Kuvunjika Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 2/15 kur. 90-95

Usiache Imani Yako Iangamizwe na Kuvunjika Moyo Wala Nyutu za Watu

“Uvipige vile vita vizuri; uwe mwenye imani na dhamiri njema, ambayo wengine wameisukumia mbali, wakaangamia kwa habari ya Imani.”​—1 Tim. 1:18, 19.

1. Wakristo wakoje kama meli baharini?

WAKRISTO katika ulimwengu huu usio haki wa wanadamu ni kama meli zilizo katika bahari pana. Wote wanakabiliwa na hatari sikuzote. Dhoruba zinazochafua bahari zinaweza kuvunja meli vipande vipande. Magenge na vilima vya barafu vinavyoelea baharini vinaweza kuatua mashimo ndani yake, na kuididimiza meli upesi katika bahari kuu. Kutoweza kuona vizuri kwa sababu ya hali ya anga au kupoteza nguvu za umeme au kutofanya kazi kwa usukani kunaweza kufanya meli igongane na nyingine au ikwame katika mchanga wa bahari. Vivyo hivyo, Wakristo wanaweza kupata maangamizi ya imani yao wasipokuwa macho sikuzote kuziona hatari za ulimwengu huu. Mamilioni ya watu katika ulimwengu huu wasiomjua Mungu ni kama bahari yenye msukosuko, na Wakristo wako kana kwamba wanaelea katika bahari hii ya wanadamu. (Isa. 57:20, 21) Yesu alijua kwamba ingekuwa lazima wanafunzi wake waendelee kuwamo katika ulimwengu huu kwa kitambo, lakini hawakupaswa kuwa sehemu yake. (Yohana 17:11, 14-16) Kama meli, wao wanaweza kuwa baharini, lakini maji ya bahari yaanzapo kuingia melini, hilo ni jambo la kupigia kamsa mara moja.

2. Ingawa kwa njia hiyo Wakristo wanaweza kuwa katika bahari ya wanadamu, ni hatari gani iliyoko juu ya nia na mazoea ya ulimwengu huu?

2 Hivyo lazima Wakristo wajihadhari mazoea na nia zinazoonekana sana katika taratibu hii zisipenye kidogo kidogo katika kundi la Kikristo au kuangamiza imani zao mmoja mmoja. Nia mbili na mazoea yanayoonekana sana ambayo ni hatari yanahusu kuvunjika moyo na kuacha nyutu za watu ziondoe mtu au kumkengeusha, nasi tutayazungumza mambo hayo katika makala hii.

KUACHA KUVUNJIKA MOYO

3, 4. (a) Shetani ametumiaje hali zenye kuvunja aweke wanadamu chini ya utumwa wake? (b) Ni mambo gani yanayovunja moyo mara nyingi?

3 Matokeo ya kuvunjika moyo yanaweza kuonekana waziwazi sana katika nyuso zenye huzuni za umati wa wanadamu. Kwa karne nyingi Shetani ametumia hali zenye kuvunja moyo kuingiza watu katika utumwa wake mwenyewe na wa taratibu yake, naye hasa anafurahi kuona Wakristo wakipunguza mwendo au kuacha azimio lao la kumtumikia Yehova, kwa sababu ya kuvunjika moyo. Hivyo imewapasa Wakristo wawe macho sikuzote wasije wakalemewa na kuvunjika moyo.

4 Mambo mengi yanavunja moyo. Sababu ya kawaida sana inahusu afya. Mtu anapoumwa, na hasa kuumwa kwa muda mrefu, maelekeo ya kawaida ni kujitenga na kujisikitikia. Kufanya hivyo hakutii mtu nguvu wala kumchochea afanye anayopenda kufanya. Au, huenda mtu akawa anajitahidi kumaliza udhaifu fulani au kutokamilika kwa mwili kunakomsumbua. Ugonjwa uliosedeka wa mshiriki wa jamaa au kifo katika jamaa kinaleta huzuni na majonzi. Ikiwa si wote katika jamaa walio Wakristo, huenda mtu akapingwa vikali na mwenzi wake mwenyewe wa ndoa na hata kudhihakiwa na watoto. Hali za maisha ya chini sana ziko katika sehemu nyingi zaidi za ulimwengu, na umaskini, uvunjaji wa sheria na hofu yanavunja moyo sana.

5. Ni jambo gani la maana zaidi ili kuacha kuvunjika moyo?

5 Ili kuacha kuvunjika moyo, ni lazima sana Wakristo wakaze akili zao juu ya uhusiano wao na Yehova na kuwa na hakika kabisa kwamba yeye hatakosa kuwapa watu wake faraja na msaada katika kila wakati wa shida. Ingawa anaruhusu ukamilifu wa watumishi wake ujaribiwe na majaribu makali nyakati nyingine, yeye atasaidia waaminifu wake wastahimili, naye atawafariji na kuwakomboa katika wakati wake. (Yak. 1:5-8) Daudi, ambaye alikabiliwa na hali nyingi zenye kujaribu, aliandika hivi kwa uongozi wa Mungu ili atutie moyo: “Iweni hodari, mpige moyo konde, ninyi nyote mnaomngoja [Yehova].”​—Zab. 31:24.

6. Kwa sababu gani Wakristo wanaweza kupambana na ugonjwa na mauti bila kuacha walemewe na kuvunjika moyo?

6 Tumaini hakika la ufufuo linaondoa maumivu ya ugonjwa na hofu ya mauti. Tukiendelea kuburudisha akili zetu na ahadi za Yehova za ajabu, tunasisimka na kuwa na furaha na faraja ambayo Yehova peke yake ndiye awezaye kutoa. “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”​—2 Kor. 4:16-18.

7. Ni nini inayokuwa kama nanga kwa kuleta imara sasa na katika nyakati zenye msukosuko zilizoko mbele?

7 Alipokuwa akizungumza juu ya ahadi za hakika za Mungu, Paulo aliandika hivi kwa Wakristo Waebrania: “Matumaini yale yawekwayo mbele yetu; tuliyo nayo kama nanga ya [nafsi], yenye salama, yenye nguvu, yaingiayo hata mle mlimo ndani ya pazia [yaani, mbinguni mwenyewe], alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu.” (Ebr. 6:18-20) Hivyo, tumaini lenye msingi imara na lenye mfano wa nanga katika Yehova na katika baraka zake zilizohakikishwa kabisa za taratibu yake mpya linawapa Wakristo imara na faraja ijapokuwa wana dhiki katika mwili na wanapatwa na hali zenye msukosuko zinazowazunguka katika ulimwengu huu. “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”​—Zab. 46:1-3.

8. Kwa sababu gani mtu asivunjike moyo asipoweza kufanya mengi kama ambavyo angependa kufanya katika utumishi wa Yehova kwa sababu ya afya mbaya?

8 Ikiwa ugonjwa au hali nyingine zinakuzuia usifanye yote ambayo ungependa kufanya katika utumishi wa Yehova, bado unaweza kufurahia yale unayoweza kufanya, ukikumbuka maneno ya Paulo yenye kutia moyo na kufariji: “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.” (Ebr. 6:10) Nawe usisahau kwamba kuweka mfano mwema wa ukamilifu na uvumilivu kunatia wengine moyo, hata ikiwa udhaifu fulani wa mwili umekupunguzia mwendo kidogo.​—Linganisha 2 Wakorintho 12:7-10.

9. Kwa sababu gani sala na kushirikiana na Wakristo wenzetu ni kwa maana tunapojizuia tusivunjike moyo?

9 Ili waendeleze imani yao kuwa yenye nguvu na kuzuia wasijione kukata tamaa na kuwa na hangaiko, Wakristo wanaujua ubora wa kupatanisha mwendo wao na Neno la Mungu na kuchunguza hali yao sikuzote waone sehemu zinazohitaji mabadiliko. Imewapasa wapashane habari mara nyingi na Baba yao wa kimbinguni. “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Kushirikiana na Wakristo wenzetu ni kwa maana pia. Paulo aliandika hivi kwa Wakristo katika Rumi: “Kwa maana ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu.”​—Rum. 1:11, 12.

10. Ukijisikia unakosa ushirika wa Kikristo, unaweza kufanya nini?

10 Ikiwa unataka sana kushirikiana na bado unajiona kuwa peke yako, kujionyesha kuwa mwenye urafiki zaidi huenda kukakusaidia upate ushirika zaidi wa kirafiki, usitawishe uhusiano wenye kuendelea pamoja na wengine. Ingawa Wakristo wana wajibu wa kuwa wenye urafiki kwa watu wote, na hasa kutenda mema kwa “jamaa ya waaminio,” wengine wanaona ni vyepesi zaidi kushirikiana nasi tukiwa wenye kufurahisha, wenye kujenga na wenye kuelekea kuwa na maoni yanayofaa juu ya mambo. (Gal. 6:10) Huenda mtu akahurumiwa kwa sababu ya kusema maneno ya kujisikitikia lakini huenda sikuzote asipate heshima ya kweli kwa kufanya hivyo.

11. Ni kwa njia gani tunavyofaidiana tunapojaribu kutafuta nafasi za kusaidia wengine?

11 Jiulize pia unavyoweza kufanya usaidie wengine badala ya kukaza fikira zote juu yako mwenyewe. Katika Matendo 20:35 Paulo anaelekeza fikira kwenye kanuni iliyowekwa na Yesu: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” Furaha inaongezeka kweli kweli tunapojitoa tutumikie wengine. “Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.” (1 Kor. 15:58) Petro anashauri hivi: “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali na Mungu.” (1 Pet. 4:8-10) Hivyo furaha yetu wenyewe inaongezeka tunapotumia nafasi zetu tutie wengine moyo.​—Luka 6:38.

12. Maono ya ndugu na dada zetu yanawezaje kutusaidia tuache kuvunjika moyo?

12 Ufanisi wa kiroho wa tengenezo la Yehova unawatia Wakristo moyo. Tunaposoma au kusikia habari za maono ya ndugu zetu ulimwenguni pote, twaona namna Yehova anavyoongeza baraka yake anapotia watu wake nguvu washinde mateso na magumu na kuacha kuvunjika moyo. “Heri taifa ambalo [Yehova] ni Mungu wao, watu aliowachagua kuwa urithi wake.” (Zab. 33:12) Katika safari zao Paulo na Barnaba walieleza wengine “habari za kuongoka kwao Mataifa.” Nayo matokeo yalikuwa nini? “Wakawafurahisha ndugu [wote] sana.” (Matendo 15:3) Usikose kueleza wengine mambo unayoona katika utumishi wa Yehova ili uwatie moyo, nawe waombe wengine wakueleze mambo waliyoona au uyasome yale yaliyoandikwa.​—Zab. 122:1-9.

13. Yehova amefanya mipango gani kuendelea kutia watu wake moyo ijapokuwa wamezungukwa na hali zenye kuvunja moyo?

13 Kwa hiyo, ili tuepuke kuangamiziwa imani yetu na kuvunjika moyo, kuna uhitaji wa kutiwa moyo na kutiana moyo pia. “Basi, farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile kama mnavyofanya. . . . ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote.” (1 The. 5:11, 14) Ingawa kuna msukosuko kila mahali karibu yetu na hali zinaelekea kuangamiza imani yetu, tunaweza kumtegemea Yehova kwa matumaini atusaidie tusalimike katika hali hizo na kuepuka kuvunjika moyo. “Akawaponya na shida zao. Huituliza dhoruba, ikawa shwari, mawimbi yake yakanyamaza. Ndipo walipofurahi kuwa yametulia; naye huwaleta mpaka bandari waliyoitamani. Na wamshukuru [Yehova] kwa fadhili zake, na maajabu yake kwa wanadamu.”​—Zab. 107:28-31.

NYUTU ZA WATU ZINAWEZA KUANGAMIZA IMANI YA MTU

14. Nyutu za watu zinawezaje kuangamiza imani ya mtu?

14 Wakristo wanakabili pia hatari ya kupigana dafurao na Wakristo wenzao hata kufikia hatua ya kuangamiza imani yao au ya wengine. Zaidi ya hayo, Maandiko yanaonya kwamba wachache katikati ya kundi la Kikristo wangeondoka katika imani na kujaribu kuvuta wengine wawafuate. Kwa upande mwingine, Wakristo wanatumaini na kuheshimu ndugu na dada zao walio thabiti na waaminifu nao wanathamini uongozi na mfano wa wachungaji wao waaminifu, lakini haiwapasi kuacha yanayofanywa na viumbe vingine vya kibinadamu yafanye ‘waangamie kwa habari ya Imani yao.’ Kwa hiyo, imewapasa watumishi wa Mungu wasiache nyutu za watu ziwaudhi isivyofaa wanapopanga mwendo wao utakavyokuwa.​—1 Tim. 1:18, 19.

15. Yuda anaelezaje habari za wengine ambao angeweza kuwa hatari kundini kabla ya kufukuzwa?

15 Yuda anataja wengine waliopenya katika kundi la Kikristo wakajaribu ‘kubadili neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi,’ naye anawaeleza kuwa “miamba [“iliyofichwa chini ya maji,” NW] yenye hatari katika karamu zenu za upendo.” “Watu hawa ni wenye kunung’unika, wenye kulalamika, waendao kwa tamaa zao, na vinywa vyao vyanena maneno makuu mno ya kiburi, wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida.” (Yuda 3, 4, 12, 16; linganisha 2 Petro, sura ya 2.) Wakigunduliwa, watu wa namna hiyo wanafukuzwa au kutengwa na ushirika kama wasiostahili kuwamo kundini. Lakini mtu akikataa kweli ya Neno la Mungu, akiwa mwenye kunung’unika-nung’unika hata kufanya hayo kuwa mazoea yake huku akijaribu kuficha uasi wake juu ya imani na kupotoa wengine kwa kutumia nyutu zake zenye kuvutia, je! tuambatane na huyo tutoke katika kweli na kuingia uharibifuni? Ungekuwa upumbavu weee! Jiangalie imani yako isiangamizwe kwa kugonga mmoja wa hiyo “miamba iliyofichwa chini ya maji”!

16. (a) Mzee anapotusaidia tulitumie Neno la Mungu, nia yetu imepaswa kuwaje? (b) Ni nia gani zenye kutofautiana zilizoonyeshwa na wengine wa wanafunzi wa Yesu?

16 Tofauti na hilo, wakati wachungaji na waalimu katika kundi wanapojaribu kutusaidia tufanye maendeleo katika kweli ya Neno la Mungu, je! tunakwazwa na nyutu? Wengi ambao wakawa wanafunzi wa Yesu walipenda mengine ya mafundisho yake, nao walifurahi kupokea chakula na mapozo ya mwujiza, lakini walipoambiwa kwamba lazima ‘wale mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake,’ jambo hilo liliwashtua hata “wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena.” Hawakukaa muda mrefu vya kutosha wapate ufahamu juu ya fundisho hilo la maana.​—Yohana 6:48-69.

17, 18. (a) Mitume walionyeshaje nia inayofaa kwa habari ya fundisho lililokuwa gumu kukubaliwa? (b) Kwa sababu gani kutoaminika kwa Yuda Iskariote hakukutikisa imani ya mitume wale wengine? Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

17 Wakati tengenezo la Yehova la “mtumwa mwaminifu mwenye akili” linapotoa ufahamu mpya wenye msingi wa Neno la Mungu, nyakati nyingine huenda tukaona ugumu fulani kufahamu kabisa yaliyoandikwa. Lakini tufanye nini? Tuwe wenye kulaumu-laumu na pengine tuazimie kwamba hayo ni maoni ya watu wachache tu walio katika makao makuu? Au, tutaonyesha nia ile ile ya mitume walipoulizwa ulizo na Yesu wakati uo huo ambapo wanafunzi wengi waliondoka: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”

18 Kwa kulinganisha mafundisho ya Yesu na mwendo wake wa maisha pamoja na Maandiko ya Kiebrania mitume walisadiki kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi wa kweli, nao wasingeacha kumfuata ati kwa sababu alileta fundisho jipya lililokuwa gumu kukubaliwa wakati huo. Ni kweli kwamba mmoja aliondoka baadaye, yaani Yuda Iskariote. Pupa ilibadili nia na moyo wake. Lakini je! kutoaminika kwa mmoja wa mitume waliochaguliwa kuliharibu imani ya wale wengine kumi na mmoja? Sivyo, ingawa imani yao ilitikisika kidogo Yesu alipokamatwa na kufa juu ya mti wa mateso. Walipona kiroho, naye Yehova aliwatia nguvu kwa roho yake takatifu kuanzia na Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea.

19. (a) Kwa habari ya uongozi ndani ya kundi la Kikristo, imetupasa tukumbuke jambo gani nyakati zote? (b) Wazee wana daraka gani, nasi tusiruhusu nini linalohusu nyutu za watu litokee?

19 Usisahau kwamba sisi, kama mitume, tunamfuata Yesu Kristo wala si mwanadamu fulani wala kikundi cha wanadamu walio viongozi duniani. Naam, wanadamu wasiokamilika wanatumiwa kutusaidia, tangu baraza inayoongoza mpaka kwenye wazee katika makundi yetu, lakini hawa wana daraka zito la kufundisha sawasawa kabisa na Neno la Mungu. Imewapasa wamwige mtume Paulo, aliyewaambia wazee katika Efeso hivi: “Sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa, bali naliwafundisha waziwazi na nyumba kwa nyumba.” (Matendo 20:20) Alimwomba Timotheo kwa uzito kama mzee ‘alihubiri neno’ la Mungu kwa kujenga imani ya kundi na kulitayarisha kwa ajili ya kipindi ambacho wengine ‘wangeyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe wangejipatia waalimu makundi makundi, wapate kutekenywa masikio yao.’ (2 Tim. 4:1-4) Sisi tunataka nini? Tunataka mtu fulani wa kututekenya masikio na kutuambia kwamba kila jambo ni sawa, hata lisipokuwa sawa, au tunataka mtu atakayetuambia kweli lakini kwa upole, na kutusaidia tutembee katika njia itakayompendeza Mungu? (Efe. 4:11-15) Usiache nyutu za watu ziwe kizuizi kati yako na Baba yako wa kimbinguni, Yehova, na Kichwa cha kundi la Kikristo, Kristo Yesu!

KUCHUKULIANA KWA UPENDO

20, 21. (a) Ni mambo gani yanayofanya iwe lazima tutumie saburi na uvumilivu tunaposhughulikiana? (b) Paulo anatoa shauri gani la kuendeleza amani na kifungo cha upendo katika kundi, katika Wakolosai 3:13, 14.

20 Kwa kuwa sote tumezaliwa katika dhambi, kuna uhitaji wa kuondoa tabia za utu wa zamani na kujitahidi kuvaa utu mpya. (Efe. 4:23, 24) Yehova ataendelea kutugeuza maadamu tunanyenyekea kufanya mapenzi yake. Hata hivyo, tabia za utu usiofaa zina maelekeo ya kuzidi kuwapo hata tunapojitahidi kuziondoa, na huenda tukajikuta bado tukijaribu kuondoa mojawapo ya tabia hizo miaka mingi baada ya kuonyesha wakf wetu kufanya mapenzi ya Yehova. Hivyo imetupasa tuvumiliane. Zaidi ya hayo, si kila mara tabia za utu zenye kutofautiana zinapoonyesha udhaifu, bali nyakati nyingine zinaonyesha namna za nyutu mbalimbali alizopanga Yehova ziwe katika viumbe vya kibinadamu.

21 Upendo na kuvumiliana utatusaidia kutokuwa wepesi wa kuchukizwa na mambo. Kwa sababu ya magumu yenye kumkaza, huenda ndugu akapita karibu nasi bila kutusemeza au huenda akasema kwa hasira wakati fulani. Au huenda tabia au desturi ya mwingine ikaelekea kutuudhi. Hata hali yenyewe iweje, Biblia inashauri hivi: “[Endeleeni kuwa] mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”​—Kol. 3:13, 14.

22. (a) Kukasirikia makosa ya ndugu kwaweza kufanyiza mtu nini? (b) Ili tusamehewe makosa yetu na Mungu, lazima tufanye nini kwanza?

22 Kwa hiyo, usiache kutofautiana kwa nyutu kukuangamizie imani. Jiongoze kwa njia ya kutogongana dafurao na ndugu yako. Ibilisi akiweza kukukasirisha sana kwa sababu ya makosa ya ndugu yako hata usihudhurie mikutano mingine au uache kuzihubiri habari njema za Ufalme, atafurahi sana. Je! unataka kumpendeza Adui kwa sababu ya udhia fulani au roho ya kiburi? Je! uhusiano wako na Yehova haufai kitu ndiyo uache kumtumikia au kupunguza mwendo kwa sababu ya ndugu fulani kufanya kosa? Kumbuka, kama Yehova angehitaji ndugu yako awe mkamilifu sasa, angekuhitaji wewe pia uwe mkamilifu. Ikiwa unataka Mungu akusamehe makosa yako, lazima uwe na nia ya kusamehe ndugu yako kwa makosa yake. Yesu alisema kusamehewa dhambi zetu kunategemea kuwa kwetu na nia ya kusamehe wengine.​—Mt. 6:12, 14, 15.

EPUKA KUKWAZA WENGINE

23, 24. (a) Ni kwa njia gani ulimi unavyofananishwa na usukani wa meli kwa kufaa? (b) Biblia inatoa shauri gani juu ya kusema kweli na mambo yenye kujenga?

23 Ulimi unaweza kudhuru sana usipoangaliwa vizuri. Yakobo anaufananisha hivi: “Angalieni merikebu; ingawa ni kubwa kama nini, na kuchukuliwa na pepo kali, zageuzwa na usukani mdogo sana, ko kote anakoazimia kwenda nahodha. Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu.” Sababu gani tukose kuzuia ndimi zetu hata zitamke-tamke mambo kama usukani ulioongozwa vibaya na kutufanya tukosane na msifaji wa Yehova mwenzetu? “Katika kinywa kile kile hutoka baraka na laana. Ndugu zangu, haifai mambo hayo kuwa hivyo. Je! chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu?”​—Yak. 3:4, 5, 10, 11.

24 Kunapokuwa na maelekeo ya kusema neno kwa hasira, au kupiga-piga domo juu ya wengine kwa njia yenye kudhuru au kuchongea, kumbuka kwamba nahodha wa meli ndiye anayeongoza mwendo wa chombo kwa kutumia usukani. Ikiwa hatufikirii ndugu zetu mabaya moyoni, hatutaongozwa kusema mambo yenye kudhuru kwa ulimi. “Basi [kwa kuwa mmevua uongo], mkaseme kweli kila mtu na jirani yake.” “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.”​—Efe. 4:25, 26.

25. Ni shauri gani linalotolewa juu ya kumaliza matata ya kipekee?

25 Malizeni matata upesi. Mara nyingi mambo madogo yanaweza kusahauliwa mbali bila kuleta matata kwa sababu yake. Ugumu ukiendelea kuwapo, mwendee ndugu aliyekukosea mzungumze jambo lenyewe kwa faragha na kwa upole na wema. Na ndugu akikufikia mzungumze jambo analolalamikia, jiweze na kusikiliza kwanza anayosema upate kufahamu mambo yalivyo wala usikimbilie kujitetea au kupinga shtaka lake kwa kumshtakia jambo jingine na wewe pia.​—Efe. 4:26, 32.

26. Tunahakikishiwaje katika Neno la Mungu kwamba tunaweza kumaliza mwendo wetu kupita nyakati zenye msukosuko zilizoko mbele na kuingia katika taratibu mpya ya mambo ya Yehova?

26 Shetani Ibilisi, adui ya Mungu, anasukasukisha bahari za wanadamu zaidi kila siku, akijua wakati wake ni mfupi. (Dan. 7:2, 3; Ufu. 13:1) Mpinzani mkuu huyo wa Mungu angependa kuiangamiza imani yetu kwa kutuvunja moyo kabisa na kwa kutukosanisha na wengine. Lakini kwa kuimarisha imani yetu na kuhakikisha tunajiongoza kulingana na Neno la Mungu lililo hakika, kwa msaada wa Yehova usioshindwa tutamaliza mwendo wetu kupitia katika nyakati hizi zenye msukosuko, tuendelee moja kwa moja kupita “dhiki kubwa” na kuingia katika taratibu mpya ya mambo ya Yehova, ambamo ‘hamna bahari tena.’ (Ufu. 21:1) Jamani! tutamshukuruje Yehova wakati huo, kwamba hatukuacha lo lote la mambo yenye kuvutia au magumu tuliyopatwa nayo yaangamize imani yetu na kutupotezea baraka za ajabu zitakazofurahiwa milele na wenye kumpenda Mungu kabisa! “Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu.”​—Ebr. 10:39.

​—Kutoka The Watchtower, Aug. 15, 1975.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki