Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Mwanzo 9:5 ifahamikeje, ambapo Mungu alisema kwamba ‘angetaka damu’ kutoka kwa mnyama aliyeua mwanadamu?
Hasa hii ina maana ya kwamba mnyama akiua mwanadamu, lazima auawe. Lazima apoteze uhai wake mwenyewe kwa sababu ya kutoa uhai wa mwanadamu.
Baada ya Gharika, Yehova Mungu kwanza aliruhusu wanadamu kuua wanyama wawe chakula chao, ingawa hawakupaswa kula damu. (Mwa. 9:3, 4) Ndipo Mungu alipoonyesha ubora wa uhai wa mwanadamu kuliko uhai wa mnyama, kwa kuwa mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu. Yehova alisema hivi:
“Hakika damu yenu ya uhai wenu nitaitaka; na kwa mkono wa kila mnyama nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa ndugu ya mtu nitataka uhai wa mwanadamu. Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu; maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.”—Mwa. 9:5, 6.
Kwa hiyo, ingawa wanyama wangeweza kuuawa waliwe, wanadamu hawakupaswa kuuawa. Kama mtu angeua mwanadamu mwenzake, na kutoa uhai asioruhusiwa kutoa na hivyo kuwa na hatia ya damu, alipaswa apoteze uhai wake mwenyewe. Nao mpango huu ulipaswa utumiwe hata kwa wanyama wenye kuua wanadamu. Ni kweli kwamba mnyama asingejua amevunja sheria ya kimungu kwa kuua mwanadamu. Lakini bila shaka takwa hili lingekaza ubora wa uhai wa mwanadamu juu ya akili za wanadamu wenyewe, kwa maana hata mnyama asingeweza kutoa uhai wa mwanadamu akakosa kuadhibiwa.
Katika Torati yake kwa Israeli baadaye Yehova alitoa sheria iliyohusu wanyama wenye kuua wanadamu. Kulingana na Kutoka 21:28-32,ng’ombe dume aliyepiga mwanadamu kwa pembe akamwua alipaswa auawe kwa kupigwa kwa mawe. Inafahamika kila mahali kwamba sheria hiyo haikuhusu ng’ombe dume peke yao; kisa cha ng’ombe dume mwenye kupiga watu kingeweza kufahamika vizuri zaidi na watu wenye kukaa mashambani, nacho kilionyesha linalopaswa kufanywa kwa mnyama aliyeua mwanadamu. Kama alitoa uhai wa mwanadamu, kiumbe huyo mwuaji alipaswa kutolewa uhai wake mwenyewe.
Ndivyo imekuwa katika jamii nyingi za watu waliotokana na Nuhu. Kwa mfano, The International Wildlife Encyclopedia kilisema hivi: “Simba-marara akiwa mla-watu au mwua-mifugo, hata sababu yake iwe nini, mkono wa kila mtu unamwandama. Vijiji vizima vya watu vitamtafuta hata wasipumzike mpaka wamemwua, hata katika maeneo ambako simba-marara analindwa na sheria.”
Huenda watu wengine wakaiona hiyo kama njia ya kujilinda tu. Lakini maneno yaliyomo katika Mwanzo 9:5, 6 yamepaswa yakaze juu ya akili zetu ubora wa uhai wa mwanadamu. Hauwezi kutolewa na mwenye kuutoa akakosa kuadhibiwa. Hivyo imetupasa tujitahidi kutokuwa na hatia ya damu, na imetupasa tuutumie uhai bora wa kibinadamu tulio nao kumheshimu mpaji wa uhai, Yehova Mungu.—Matendo 20:26, 27; Zab. 36:7, 9.