Kimbilio Letu Chini ya “Ufalme wa Mbinguni” Usioharibika
1. Nyingine za sababu za kujiona na wasiwasi wa kukosa usalama ni nini, na hiyo inafanya watu wazidi kuliaje?
JE! WEWE umepata kuona uhitaji mkubwa sana wa kutafuta kimbilio, kupata mahali pa kinga na ulinzi wa hatari au dhiki? Pengine unakumbuka sana kwamba ulipata kimbilio usiku mmoja baada ya mwingine ukijikinga usishambuliwe na ndege za vita, hiyo ikakufanya ujisikie umelindwa, umepata faraja ya kadiri fulani. Lakini namna gani hatari na mikazo ya hali za kisasa? Wewe kama mwanamume, je! unajiona salama katika kazi yako? Wewe kama mwanamke, je! unajiona salama katika maisha yako ya nyumbani na katika uhusiano wa kipekee? Je! ni salama kwako wewe au kwa watoto kutembea peke yenu usiku, au pengine hata wakati wa mchana? Tungeweza kutaja sababu nyingi zaidi za kuona wasiwasi wa kukosa usalama, kutia na mambo kama vile kupunguka kwa thamani ya pesa, kuharibu mali za watu bila sababu, dawa za kulevya, uchafuzi wa hewa, maji na chakula na kadhalika. Hali za ulimwengu hazikuwa zenye kuhuzunisha kama zilivyo leo. Dhiki ya ulimwengu inaongezeka. Mwanadamu anakuwa hoi zaidi na zaidi. Kwa wazi faraja haiwezi kuletwa na wanadamu. Watu wanazidi kulia kwa moyo wakiuliza, Ni wapi tunakoweza kupata mahali hapo pa kimbilio salama?
2. (a) Ni kwa njia gani mwaka wa 1914 W. K. mambo yalibadilika sana? (b) Tangu wakati huo, kumekuwa na ongezeko la mambo gani?
2 Kabla ya kujibu ulizo hilo, acheni tuangalie sababu hasa ya mambo haya. Ni wakati gani na jinsi gani yote yalivyoanza? Tukitazama nyuma, tunaweza kuona kwamba mwaka wa 1914 W.K. ndio uliobadili mambo sana. Kufikia wakati wa kiangazi cha mwaka huo kulikuwa na matumaini mazuri. Ilikuwako Baraza ya Kudumu ya Utatuzi wa Mizozo katika Ulaya ya kutatulia mizozo kati ya mataifa. Maisha yalikuwa ya uchangamfu na yenye matumaini mazuri kwa watu wengi. Ndipo Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipofyatuka, ikianzishwa na mfyatuo wa risasi uliofanya makombora yaanze kumiminwa angani. Ilitumainiwa kuwa ndiyo vita ambayo ingekomesha vita vyote. Badala yake Vita ya Ulimwengu ya Pili ikatokea. Na sasa, kulundikwa kwa silaha za atomiki za kurusha angani kunatisha kuwako kwetu. Ongezeko linaonekana katika mambo mengine pia. Idadi ya ulimwengu inaongezeka kweli kweli. Kwa sababu ya ongezeko hili la watu wanaohitaji kulishwa, inasemekana kwamba kutakuwa na njaa kali ya ulimwengu wakati ujao ulio karibu. Na namna gani juu ya kuenea sana kwa magonjwa mabaya sana? “Flu ya Kispania” ya mwaka wa 1918 iliua watu milioni 20, lakini pia magonjwa ya kisonono na kaswende yenye kutapisha yameenea sana, kwa sababu jamii yetu inaendekeza watu. Uvunjaji wa sheria, jeuri na uasi ni mambo ya kawaida. Kwa kuwa kunazidi kuwa na uhitaji wa mtu kujilinda mwenyewe, nao ugomvi ni mwingi, pupa ni nyingi, wizi, kutumia watu wengine kwa faida ya mtu mwenyewe, bila shaka choyo alichozaliwa nacho mwanadamu kitaongezeka. Na kwa kuwa mwanadamu ameacha kupenda mwenzake, kumpenda Mungu kumepoa. Si kwamba kumepoa tu, bali pia ni jambo la kawaida sana leo kusema kwamba Mungu amekufa! Bila shaka, kwa urahisi tunakubali kwamba, bado wako watu wengi mmoja mmoja wenye mioyo myema na wanaoishi maisha za adabu, lakini lazima pia ikubaliwe kwamba wanaona ni vigumu zaidi kufanya hivyo.
3. (a) Tunaongozwaje kuona maana halisi ya hali za kisasa? (b) Ni ulizo gani la maana sana lililofanya Yesu Kristo atoe unabii wake mkuu?
3 Haya basi, tumeona maelekeo ya mambo kwa ujumla tangu mwaka wa 1914, lakini je! tumeiona sababu yenyewe hasa? Na, lililo la maana zaidi, dawa ya mambo haya ni nini? Je! iko? Twawezaje kupata majibu yenye kutosheleza ya maulizo haya? Twaweza kumwendea nani? Naam, linalofurahisha ni kwamba yuko mtu anayeweza kutoa majibu yenye kutosheleza kabisa ya maulizo haya yote. Tunawakumbusheni kwamba huko nyuma mwaka wa 876 Mwanafunzi wa Biblia ambaye akawa msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society aliandika akasema kwamba “majira ya Mataifa” yanayotajwa na Biblia yangekwisha katika vuli ya mwaka wa 1914 na kuleta taabu isiyo na kifani kwa ulimwengu mzima. Alipata wapi habari zake? Katika Neno la Mungu, Biblia Takatifu, na hasa katika Danieli 4:16, 23, 25, 32 na unabii mkuu uliotolewa na Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, aliyeongozwa na roho takatifu ya Mungu. Unabii huu ni sehemu kamili ya Neno la Mungu nao umeandikwa katika Mathayo 24:4-51, pia katika Marko 13:5-37 na Luka 21:8-36. Unabii huo ulitolewa kwa kujibu ulizo linalostahili kuangaliwa lililoulizwa na wanafunzi wa Yesu: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW) Naam, Yesu alitabiri mwisho wa taratibu ya mambo, si ya siku zake tu, bali pia yenye ulinganifu kwa siku zetu. Alitambulisha pia kimbilio linalohitajiwa sana tunalopendezwa sana nalo.
4. Ni nini uliokuwa utimizo wa siku za Yesu wa unabii wake, na hiyo ilionyesha kungekuwa na ulinganifu gani katika siku zetu?
4 Tukiangalia kwa ufupi utimizo wa unabii wa Yesu uliotukia siku zake yeye na wanafunzi wake, twajua kwamba mambo yaliyotabiriwa yaliyofikia upeo hekalu lilipoharibiwa, “patakatifu,” na “mji mtakatifu,” Yerusalemu, vilevile jimbo la Uyahudi mwaka wa 70 W.K., yalionyesha mwisho wenye msiba wa taratibu hiyo ya mambo. Namna gani juu ya siku zetu? Je! tunayaona yale mambo mengi aliyoyatabiri Yesu yanayofanyiza “ishara” kamili yakionyesha kuwapo kwake na mwisho wa taratibu ya mambo? Tumekwisha taja baadhi yake, na hata mbali na hesabu ya tarehe zinazohusu “majira ya Mataifa,” twaweza kusema kwa hakika kwamba mwaka wa 1914 ndio uliokuwa mwanzo wa “siku za mwisho” za taratibu hii ya mambo ambapo kama alivyosema Paulo, “kutakuwako nyakati za hatari.”—2 Tim. 3:1.
DAWA NA KIMBILIO
5. Katika Luka 21:28-31, Yesu alielezaje kimbilio la pekee tunalopaswa kukimbilia?
5 Halafu tunauliza hivi, Kunayo dawa? Hakuna dawa kwa taratibu iliyopo ya mambo. Kulingana na Neno la Mungu, kwa kustahili imehukumiwa maangamizi. Lakini je! hakuna cho chote ambacho watu mmoja mmoja wanaweza kuelekea kitakachoondoa maovu ya kisasa? Bila shaka kunacho, na ndiko fikira zetu zinakovutwa tukapate kimbilio lililo la maana zaidi kupita yote ambalo imetupasa tulikimbilie bila kukawia. Angalia maneno ya Yesu aliposema hivi:
“Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia. Akawaambia mfano; Utazameni mtini na miti mingine yote. Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:28-31.
6. (a) Yesu alimtambulishaje mfalme wa ufalme wa Mungu’ (b) Ni utambulisho gani zaidi unaoonekana katika Maandiko ya Kiebrania?
6 Hicho ndicho kitu chenyewe! Huo “ufalme wa Mungu” unastahili tuukazie fikira zetu zote. Ni nani mfalme wa ufalme huo? Kabla tu ya kusema maneno yaliyotajwa, Yesu alisema hivi juu yake mwenyewe: “Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika wingu pamoja na nguvu na utukufu mwingi.” Na baada ya unabii wake akatoa mifano mitatu, akamalizia na ule unaohusu kondoo na mbuzi, ambao unaanza kwa kusema hivi: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake.” (Luka 21:27; Mt. 25:31) Hakuna shaka juu ya aliye Mfalme mtiwa-mafuta wa ufalme wa Mungu. Na hakuna shaka juu ya kustahili kwake! Kwanza, yeye alijiondolea kwa kupenda utukufu wa kimbinguni aliokuwa nao kisha, “alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam mauti ya [mti wa mateso]. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina.” (Flp. 2:5-11) Yeye ni mtu aliye hai leo—naam, naye apendezwa sana na kutimizwa kwa unabii wake mwenyewe ulioongozwa na Mungu! Maisha yake duniani yalikuwa ya maana sana nayo yalikuwa yametabiriwa juu ya mambo yake ya maana sana katika Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na Mungu, ili kujulisha waziwazi Masihi ni nani. Mojawapo la maandiko hayo linatabiri siku zetu ambapo “wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi wake”; kisha Yehova anaambia adui hawa kwa kicheko cha dhihaka na hasira kwamba wamechelewa mno. Anawaambia: “Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” Akiendelea kumtambulisha, Yehova anamwambia mfalme wake mtiwa-mafuta hivi: “Ndiwe mwanangu.” Mataifa wapinzani wanapewa kwake ‘awaponde.’ Lakini zaburi inafikia mwisho mzuri: “Heri wote wanaomkimbilia.” (Zab. 2:1-12) Zaburi nyingine nyingi, kama vile Zaburi 91:1, 2, zinamsema Yehova kuwa kimbilio letu, au “kimbilio langu,” lakini njia ambayo ametumia kutoa kimbilio siku hizi ni ufalme wake ulio mikononi mwa Mwanawe mtiwa-mafuta anayetawala, Kristo Yesu.—Tazama Zaburi 110:1-4.
7. Kusudi la Mungu ni nini juu ya kushiriki kwa wengine pamoja na Kristo Yesu, na sababu gani jambo hilo linashangaza sana?
7 Mara nyingi Yesu alizungumza juu ya “ufalme wa Mungu,” au “ufalme wa mbinguni.” Alisema pia wengine wangeshiriki pamoja naye, kushiriki hasa pamoja naye wakiwa wafalme wenzake. Nani amepata kusikia mpango wa namna hiyo? Je! kumepata kuwako taifa au milki yenye wafalme 144,000 na mmoja wakitawala wakati ule ule mmoja? Hakujapata kuwa hivyo wakati wo wote. Hata leo, idadi ya watu ulimwenguni ikiwa imezidi milioni elfu nne, hakuna wafalme wala watawala wengi hivyo, hata wote wakiwekwa pamoja. Wazo hili lilianzwa na nani? Bila shaka si na mwanadamu! Ni wazo la Mungu. Ndilo kusudi la Muumba wa mbingu na dunia. Huenda serikali hiyo ya kimbinguni yenye wafalme wengi hivyo wenye kufanyiza serikali ya ulimwengu ikaelekea kuwa ya ajabu sana kwa watu wenye mawazo ya kisiasa. Lakini hiyo ni kwa sababu Muumba wa kimbinguni, Mungu, ana njia ya kuwaza iliyo juu kuliko njia ya kuwaza ya mwanadamu wa kidunia, sawa na vile mbingu halisi zilivyo juu kuliko dunia. Ni kama vile Mungu alivyowaambia watu wake wa kale, Israeli: “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema [Yehova]. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”—Isa. 55:8, 9.
8, 9. (a) Ni maelezo gani zaidi yanayotolewa katika Ufunuo 1:5, 6 juu ya jambo hili? (b) Ni habari gani zinazotolewa juu ya Jambo hili katika kitabu cha Ufunuo?
8 Kwa hiyo tusishangazwe na jambo lo lote alilokusudia ati kwa sababu ni kubwa sana kuliko lile ambalo lingeweza kuwaziwa na mwanadamu wa kawaida. Karne nyingi baadaye, Mungu alifunua mambo zaidi juu ya serikali hii ya ulimwengu katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo. Kinampa Mwana wa Mungu pia sifa kamili kwa sababu ya kufuatia mwendo wa kujitoa awe dhabihu kama mwanadamu mkamilifu duniani. Angalia vile mtume Yohana alivyolitaja jambo hili alipokuwa akiandika kwa kuongozwa na Mungu: “Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina.”—Ufu. 1:5, 6.
9 Kama Yesu Kristo asingalimwaga damu yake yenye uhai kwa kujitoa kama dhabihu kwa Mungu, wafuasi wa nyayo zake wasingaliweza kamwe kufanywa wafalme na makuhani wa Mungu Baba yake mbinguni. Hivyo Yesu Kristo alifanya jambo la maana sana kwa kuwezesha wafalme wenzake hawa washiriki pamoja naye katika ufalme wa kimbinguni. Ni kama vile yeye alivyosema: “Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.” (Ufu. 3:21) Kupatana na hili, wale wazee 24 wanasemekana kuwa wakimwambia Yesu Kristo hivi: “Ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao [watamiliki] juu ya nchi.”—Ufu. 5:9, 10.
10. Ni akina nani wanaoonekana wakiwa pamoja na Mwana-Kondoo juu ya Mlima Sayuni, nao wanasimuliwaje?
10 Hatuachwi tukiwa na mashaka juu ya hesabu ya wafalme na makuhani hawa wenzi wa Kristo Yesu. Akisimulia wale watakaotawala pamoja na Kristo Yesu katika Mlima Sayuni wa kimbinguni na kueleza sifa zao njema, Yohana anaandika hivi: “Tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao. . . . Na kuimba wimbo mpya mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele ya wale wenye uhai wanne, na wale wazee; wala hapana mtu aliyeweza kujifunza wimbo ule, ila wale mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi. Hawa ndio wasiotiwa unajisi pamoja na wanawake, kwa maana ni bikira. Hawa ndio wamfuatao Mwana-Kondoo kila aendako. Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Na katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa.”—Ufu. 14:1-5.
11, 12. (a) Hawa wanatofautishwaje na wanadamu kwa ujumla? (b) Ni wakati gani makuhani-wafalme hawa wanapotawala na Kristo Yesu, nao wanaingiaje katika ufalme wa kimbinguni?
11 Wafuasi hawa wa Mwana-Kondoo wanatofautishwa waziwazi na wanadamu kwa ujumla wakati Ufunuo 7:4-8 unapowazungumza kuwa Waisraeli wa kiroho. Wakiwa hivyo, wametiwa muhuri “ya Mungu aliye hai” katika vipaji vya nyuso zao. Mtume Yohana anapanga makabila kumi na mawili yao pamoja na majina ya Kiisraeli ya mababa za ukoo. Anasema kwamba 12,000 walitiwa muhuri kutoka kila mojawapo la makabila haya kumi na mawili, hii ikileta jumla ya Waisraeli wa kiroho 144,000. Mwana-Kondoo mwenyewe, Yesu Kristo, anasemekana kuwa “Simba aliye wa kabila ya Yuda.” (Ufu. 5:5) Hivyo, mwishowe wote pamoja wanakuwa 144,000.
12 Sura ya 20 ya Ufunuo inafunua kwamba hawa makuhani-wafalme 144,000 wanaingia katika utawala wa miaka elfu pamoja na Mwana-Kondoo Yesu Kristo mara tu baada ya Shetani Ibilisi na mashetani wake kufungwa minyororo na kuvurumishwa ndani ya shimo kubwa, ambamo majeshi haya ya viumbe vibaya vya kiroho hayawezi kuongoza mataifa ya dunia vibaya wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo akiwa pamoja na wale aliowanunua kwa damu yake ya dhabihu. Wanaingia katika ufalme wa kimbinguni pamoja na Kristo kwa kufufuliwa kwenye uzima wa kiroho, unaosemwa kuwa “ufufuo wa kwanza.” Hivyo, Ufunuo 20:6 unasema hivi: “Heri, na mtakatifu, ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hao mauti ya pili haina nguvu [kwa sababu wamefanywa kuwa wasioweza kufa]; bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.”
KIMBILIO LISILOHARIBIKA
13. Kutokana na ushuhuda wote uliotangulia, tunakata maneno namna gani?
13 Tukiwa na ushuhuda wote huo ulioongozwa na Mungu, hatuna sababu za kutia shaka kwamba Yehova Mungu hakukusudia kuwe na serikali halisi ya wafalme mia na arobaini na nne elfu na mmoja watawale dunia nzima wakati wa miaka elfu iliyoamriwa, wakati ambapo Shetani na mashetani wake watakuwa wamefungwa katika “shimo kubwa.” Mpaka sasa, dunia yetu haijapata kubarikiwa na serikali ya namna hiyo, ikiwa na maafisa wa serikali wenye sifa hizo za Kimungu. Serikali hiyo ya kimbinguni ya ulimwengu imekaribia sana. Ndiyo ufalme ambao watu wote wamepaswa watafute kama kimbilio ambalo halitakosa kuwakinga.
14. (a) Ni kwa njia gani mbili watawala wa kisasa wanaweza kuharibika? (b) Ni nini linaloweza kusemwa juu ya washiriki wote wa serikali ya Mungu ya kimbinguni?
14 Falme zote au serikali za kibinadamu zinazowakilishwa na watawala wazo bila shaka zitaharibika, hata ziwe zinajulikana kwa jina gani. Zinaweza kuharibika kwa sababu watawala wote wanakuwa wagonjwa na kufa kwa sababu ya dhambi na kutokamilika, lakini pia wanaharibika kwa adili. Hakuna haja ya kutoa uhakikisho wa jambo hili. Tunajua sana mambo yalivyo. Lakini sivyo ilivyo kwa serikali inayofanyiza “ufalme wa mbinguni,” ingawa ina watu wengi sana. Kila mmoja wao atakuwa asiyeharibika umbo na adili. Hakuna shaka juu ya aliye juu zaidi ya wote, Kristo Yesu, ambaye katika Waebrania 7:26 anasimuliwa kuwa “mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu.” Lakini namna gani juu ya wenzake, waliochaguliwa kati ya wanadamu wenye dhambi? Baada ya wao kutubu na kugeuka kwa unyofu, kumgeukia Mungu kwa kujiweka wakf kwa nafsi yote na kuonyesha imani katika ustahili wa dhabihu ya ukombozi ya Kristo, wanakubaliwa na Mungu na kuharakishwa na roho yake wawe na tumaini jipya, la kimbinguni. Kama vile mtume Petro alivyosema: “[Mungu] alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; mpate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu.” Halafu akiisha kusema, “Mkiisha kujitakasa [nafsi] zenu kwa kutii kweli,” anaendelea kusema: “Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele.”—1 Pet–1:3, 4, 22, 23; tazama pia Matendo 26:20.
15, 16. Tunapata habari gani zaidi juu ya jambo hili, kutia na maandiko yaliyo katika 2 Petro 1:4 na 1 Wakorintho 15:53?
15 Kwa habari ya kutimizwa kwa tumaini lao la kimbinguni, Petro anasema hivi: “[Mungu] ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa.” Na hili linahakikishwa na maneno ya Paulo juu ya hali na umbo lao alipoandika hivi: “Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa.”—2 Pet. 1:4; 1 Kor. 15:53.
16 Kwa habari ya wale wasio wa jamii ya “ufalme wa mbinguni,” lakini wanaotafuta na kupata kimbilio chini ya Ufalme huo, wao pia lazima wajihakikishe kuwa wasioharibika kwa adili, lakini jambo hili litazungumzwa baadaye.
KIMBILIO LA UONGO LA KISERIKALI
17. Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ni jinsi gani na wa sababu gani watu wameendelea kugeukia serikali ya binadamu, nao wamefanya hivyo ijapokuwa kumekuwa kukihubiriwaje?
17 Kwa sasa na tuangalie kimbilio la uongo la kiserikali ambalo limeletwa kwa hila juu ya wanadamu hata likawa kubwa siku zetu, ili tupate ufahamu zaidi kwa kuona tofauti kubwa ya makimbilio haya mawili. Tangu kuzuka kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mwaka wa 1914 imekuwa wazi zaidi na zaidi kwamba serikali za kibinadamu haziwezi kutawala wanadamu kwa matokeo mazuri. Na hali watu wanazidi kugeukia serikali ya kibinadamu, nazo serikali za kitaifa zinazidi kuanzishwa tangu mwaka wa 1919 kuliko ilivyokuwa katika kipindi kingine cho chote kilichotangulia. Ushirika wa Mataifa uliokwisha wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, ulikuwa na mataifa mashirika yanayopungua 60. Lakini Umoja wa Mataifa wa leo una mataifa mashirika 138. Kanuni yenye kuongoza imekuwa utawala wa kienyeji, si serikali za kikoloni. Serikali za kibinadamu zimezidi kuongezeka ijapokuwa mashahidi wa Yehova wamezidi kuhubiri sana kwamba ufalme wa Mungu wa Kimasihi ndilo tumaini la pekee la wanadamu linaloweza kupatikana. Wakati wa miaka 61 iliyopita mamia ya maelfu wameuitikia ujumbe huu wa Ufalme, lakini mawakili hawa milioni mbili wa ufalme wa Mungu wanapitwa kwa mbali na wingi mkubwa mno wa wakaaji wa dunia milioni elfu nne. Uhakika wa kwamba sehemu iliyo kubwa ya wanadamu kwa wazi hawakimbilii ufalme wa Mungu kama tumaini lao la pekee hauwezi kukanwa.
18. (a) Ni mfano gani wa Yesu uliotabiri jamii mbili zenye kutofautiana, na jinsi gani? (b) Ni mambo gani aliyoendelea kusema Yesu yaliyotia maana halisi kwa mingi ya mifano yake?
18 Je! tushangae kwamba sehemu kubwa zaidi ya wanadamu wamefunga mioyo na akili zao wasisikie injili ya Ufalme na kupendelea serikali za kisiasa za kibinadamu kama kimbilio lao katika nyakati hizi zenye matata? Sivyo, ikiwa tunayafahamu sana maandiko yenye kutoa unabii ya Biblia Takatifu ya Mungu. Mwanawe, Mwana-Kondoo Yesu Kristo, alitabiri kwamba ndivyo ingekuwa. Alisema hivi katika mmojawapo wa mifano yake: “Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake.” Akaendelea kusema kwamba kutenganisha magugu na ngano kusingefanywa mpaka wakati wa mavuno ufike. Baadaye, alipokuwa akiueleza mfano huu, akasema hivi: “Zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu,” kisha akaongezea kwamba “mavuno ni mwisho wa dunia.” (Mt. 13:24-30, 36-43) Kumbuka pia jibu ambalo Yesu alitoa wanafunzi wake walipomwuliza hivi: “Kwa nini wasema nao kwa mifano?” Sasa angalia jibu lake: “Ninyi [wanafunzi] mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa . . . kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya [katika sura 6:9,10] linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya.” (Mt. 13:10-15) Mfano huu unatia nguvu mifano mingi ya Yesu. Je! “magugu” katika “mavuno” haya, “mwisho wa dunia,” hayako sawasawa na ilivyotabiriwa? Mioyo yao na akili zao zimefungwa.
19. (a) Ni onyo gani kama hilo ambalo Paulo alitoa katika Matendo 20:27-30? (b) “Mtu wa kuasi” alisitawije, mwishowe akawa kimbilio gani la uongo la kiserikali?
19 Tukiendelea na habari ii hii, tunalikumbuka onyo ambalo mtume Paulo aliwapa wazee wa kundi katika Efeso aliposema hivi: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:27-30) Waalimu hawa wa uongo wangekuwa wapotovu sana na, kama vile Paulo alivyotabiri, kidogo kidogo wangefanyiza jamii ya “mtu wa kuasi.” (2 The. 2:3-12) Ilikuwa imekwisha anza kufanya kazi katika siku za mitume, lakini haikuonekana wazi mpaka karne ya nne wakati Mfalme Konstantino Mkuu alipowalazimisha waitwao “maaskofu,” waalimu wa uongo wa siku zake, wakubaliane naye. Kwa hiyo Ukristo uliochafuliwa uliosimamiwa na “maaskofu” hawa ukachanganywa na dini ya kipagani ya Kirumi. Dini hii ya mchanganyiko ikawa ndiyo dini ya Serikali, na kwa njia hii Jumuiya ya Wakristo (yaani, Kristendomu) ikaanzishwa. Ni jumuiya kubwa ya kidini leo nayo imetiwa chachu ya upagani kweli kweli, imetiwa mambo ya ulimwengu, ubaya, mapokeo ya wanadamu, unafiki, mafundisho ya mashetani. Jumuiya ya Wakristo hii ikajifanya sehemu ya Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, nayo ndiyo sehemu kuu ya milki ya kidini.—Ufu. 17:3-6; Gal. 5:9, 19-21.