Sababu Twauhitaji Ufalme wa Yesu Kristo
1. Yesu alizaliwa kama mwana wa “mungu” gani, na sababu gani hakuzaliwa vivi hivi tu bila kukusudiwa?
TWAONA jambo moja la maana juu ya Mwana wa Mungu aliyekuwa duniani kama mwanadamu wakati wa karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Yeye hakuzaliwa katika jamaa fulani ya Kibanyani katika India. Yeye hakuzaliwa katika jamaa fulani ya Buddha katika Tibet, wala katika jamaa ya kifalme ya China ya kale, wala katika jamaa ya Kaisari wa Milki ya Rumi. (Esta 1:1; Luka 2:1, 2) Badala yake, alizaliwa “katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili.” (Rum. 1:3) Hili halikutukia bila kukusudiwa. Kulikuwako na uhitaji wa kuzaliwa kwa Mwana huyu wa Mungu kama “ukoo wa Daudi.” Hii ilikuwa ndiyo sababu Mungu alimchagua msichana bikira wa Kiyahudi aliyekuwa wa ukoo wa Daudi wa Bethlehemu awe mama wa Yesu Kristo. (Luka 1:26-32) Mariamu huyu alikuwa mwabudu wa Mungu aliyemwezesha awe na mimba kwa mwujiza, na hivyo mtoto wake wa kiume hakuzaliwa kama mwana wa mungu fulani wa Kibanyani au mungu fulani wa Kibuddha au wa Jupiter wa Kirumi au wa Zeu wa Kigiriki.—Luka 1:34-55; Matendo 14:12, 13.
2. Kwa sababu gani haikuwa lazima Yesu azaliwe akiwa wa kabila la Lawi na wa jamaa ya Haruni ndiyo awe Mwana-Kondoo wa dhabihu, naye alikufa siku gani?
2 Katika Israeli wa kale, kabila la Mfalme Daudi lilikuwa lile la Yuda, kabila ambalo katika hilo makuhani hawakutwaliwa watoe dhabihu. Hata hivyo, Yesu Kristo aliweza kuzaliwa kama “ukoo wa Daudi” wa kabila la Yuda na bado akawa Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Haikuwa lazima awe wa kabila la Lawi na wa jamaa ya ukuhani wa Haruni, jamaa ambayo katika hiyo makuhani wa Israeli walitwaliwa. Aliweza kuzaliwa katika kabila la Daudi wa Yuda bado akawa mwanadamu mkamilifu, asiye na dhambi anayefaa dhabihu yenye kukubalika kwa Mungu kwa sababu ya kuwa mkamilifu na asiyetiwa mawaa na dhambi. Kukamilika na kutokuwa na dhambi alikokuwa amedumisha kama Mwana wa Mungu mbinguni kuliendelea naye alipotumwa duniani awe mwanadamu anayelingana kabisa na Adamu mkamilifu, asiye na dhambi wakati alipoumbwa katika Bustani ya Edeni. Ilikuwa lazima Yesu Kristo awe hivyo ili ‘ajitoe mwenyewe kama ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.’ (1 Tim. 2:5, 6, NW; Mt. 20:28) Alimwaga damu yake kama dhabihu yenye kupatanisha dhambi wakati wa Siku ya Kupitwa wa mwaka wa 33 W.K., siku wakati Wayahudi walipomtoa dhabihu mwana-kondoo wa Kupitwa wakala nyama yake ya kuokwa kwa kuadhimisha kukombolewa kwa taifa lao kutoka Misri ya kale.
3. Mambo ya Walawi 17:11, 12 ilisema nini juu ya damu, na kwa hiyo tunapata faida gani kutokana na damu ya Yesu, na kwa njia gani?
3 Katika kuagana na Israeli wa kale alisema maneno yafuatayo, kama yanavyopatikana katika Mambo ya Walawi 17:11, 12: “Uhai [au, nafsi] wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi [uhai]. . . . Hapana mtu miongoni mwenu aliye na ruhusa kula damu, wala mgeni aketiye kati yenu asile damu.” Hivyo, katika kuimwaga damu yake katika kumtolea Mungu dhabihu, Yesu Kristo alikuwa akimwaga uhai wake kama dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya sisi sote wazao wa Adamu mwenye dhambi. Alitoa damu yenye uhai ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu kwa Mungu mbinguni, na hivyo hatuwezi kula wala kunywa damu ya Yesu ili tupate faida yake. Yatupasa tuiamini kama yenye kupatanisha kabisa dhambi zetu zenye kufisha ili tufaidike na damu yenye uhai ya Yesu.—Ebr. 9:11-14, 24.
4. Maneno ya Simoni Petro juu ya damu ya Kristo yafanyaje Ufunuo ufae kumfananisha na Mwana-Kondoo?
4 Mmojawapo wa Wayahudi wa karne ya kwanza aliyeamini ubora wenye kupatanisha wa damu ya Yesu alikuwa Simoni Petro, ambaye wakati mmoja alikuwa mvuvi wa samaki katika Bahari ya Galilaya. Alipokuwa akiwaandikia waamini wenzake, Simoni Petro alisema hivi: “Mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo.” (1 Pet. 1:18, 19) Hivyo, sasa, twaweza kufahamu kufaa kwa kitabu cha Ufunuo kwa kuendelea kumtaja Yesu Kristo kama “Mwana-Kondoo,” ‘aliyechinjwa.’ (Ufu. 5:6) Bila shaka sote tulio wa wanadamu twamhitaji Mwana-Kondoo huyo wa upatanisho ambaye, kwa damu yake, aweza kutusafisha na dhambi zetu na kutuondolea laana ya mauti. Bila uzima kupitia kwa dhabihu ya Mwana-Kondoo huyu hakuna wo wote kati yetu wanaoweza kufurahia jambo lo lote wakati ujao kwa dhamiri safi mbele za Mungu. Basi, kwa kweli hatuwezi kuishi bila Mwana-Kondoo huyu!
5. Alipojitoa kama dhabihu, Yesu Kristo alikuwa akifananishwa na nani katika Siku ya Upatanisho ya Israeli?
5 Katika kujitoa mwenyewe kama Mwana-Kondoo wa dhabihu, Yesu Kristo alitumika kama Kuhani Mkuu wa Mungu aliyefananishwa na kuhani mkuu wa kwanza wa Israeli, yaani, Haruni wa kabila la Lawi. Makuhani wakuu wengine wa dhabihu wa Israeli wa kale walitokana na Haruni huyu ndugu ya Musa. Hiyo ni sababu nyingine wanadamu wote wamhitaji Yesu Kristo, atumikie kama mfano wa makuhani wakuu wa Israeli katika kuipeleka damu ya dhabihu katika Patakatifu Zaidi pa hekalu Siku ya Upatanisho ya kila mwaka, Yom Kippur.
6. Wayahudi waliogeuzwa kuwa Wakristo waliambiwa watumainie nani kwa upatanisho wa dhambi, na sababu gani?
6 Yesu Kristo aliyefufuliwa alitimiza mfano huu wa Siku ya Upatanisho alipopaa mbinguni kutoka duniani, akaonekane mbele za Mungu na kutoa kufaa au thamani ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu kwa upatanisho wa dhambi za wanadamu wote. Ndiyo sababu Wayahudi wa Kikristo waliambiwa wasiwatumainie tena makuhani wakuu wa Kiharuni bali wautumainie mfano wake, katika maneno haya yaliyoandikwa katika Waebrania 3:1, 2: “Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki mwito wa mbinguni, mtafakarini sana Mtume na Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu, aliyekuwa mwaminifu kwake yeye aliyemweka, kama Musa naye alivyokuwa, katika nyumba ya Mungu.”
JAMBO ZAIDI YA KUHANI MKUU LAHITAJIWA
7. Ni kwa njia gani Yesu Kristo ni kuhani mkuu anayetufaa, na Ufunuo sura ya kwanza yamwonyesha akitumikia wapi kama kuhani mkuu?
7 Katika kuwaeleza zaidi Wayahudi wa Kikristo jinsi Yesu Kristo kama Kuhani Mkuu anavyotumikia kwa kufaa zaidi kuliko Haruni na wafuasi wake, kitabu cha Waebrania chaendelea kusema, katika sura ya saba, mstari wa 26: “Kuhani mkuu wa namna hii [alitufaa sisi] aliye mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu.” Kitabu cha Ufunuo, sura ya kwanza, mistari 11-18, humfananisha Yesu Kristo aliyetukuzwa akitumikia makundi ya Kikristo kama Kuhani Mkuu. Walakini, sura ya tano yamfananisha akiwa na zaidi ya cheo cha Kuhani Mkuu wa Mungu. Hili laeleza uhakika wa kwamba sote twamhitaji Yesu Kristo kwa sababu nyingine zaidi ya kuwa Mwana-Kondoo wa dhabihu na Kuhani Mkuu wetu.
8. Mwana-Kondoo apewa majina gani katika Ufunuo 5:9, 10, nayo yote yamaanisha nini zaidi ya ukuhani?
8 Ufunuo 5:5, 6 wamtambulisha Mwana-Kondoo aliyechinjwa akiwa “Simba aliye wa kabila ya Yuda, Shina la Daudi.” Majina haya ya cheo yaonyesha jambo fulani juu ya Mwana-Kondoo Yesu Kristo. Mistari ya tisa na kumi yakazia hili zaidi. Katika mistari hiyo Mwana-Kondoo aambiwa hivi: “Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao [watamiliki] juu ya nchi.” Basi, zaidi ya ukuhani, yote hayo yamaanisha nini? Bila shaka, yamaanisha serikali, ufalme. Ahaa, ndiyo, sote twahitaji serikali kamilifu, yenye haki juu ya dunia yote.
9. Kulingana na Mwanzo 49:9 10, ‘Simba wa kabila ya Yuda’ angekuwa na nini, na, katika habari hii, ni kitu gani kilichofanya iwe lazima Yesu awe “Shina la Daudi”?
9 Kulingana na unabii katika Mwanzo 49:9, 10, yule Simba aliye wa kabila la Yuda alipaswa awe na fimbo ya kifalme na gongo la kiongozi, na mataifa yote yalipaswa wamtii kwa kufaa. Hilo lilimaanisha Simba wa kabila la Yuda angekuwa na serikali. Daudi alikuwa wa kabila la Yuda, naye alitawala kama mfalme juu ya Waisraeli kwa miaka 40. Yesu Kristo alipaswa awe “ukoo wa Daudi,” kwa maana Mungu alikuwa amemwahidi Mfalme Daudi wa Yerusalemu nasaba ya wafuasi katika ukoo wake ambao ungekuwa na ufalme milele.
10. Kulingana na maneno ambayo Gabrieli alimwambia Mariamu, mwana wake alipaswa kukalia kiti cha enzi cha nani na kwa muda gani?
10 Yaani, kama thawabu kwa Mfalme Daudi kwa sababu ya kumwabudu Yehova peke yake kwa uaminifu kama Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, Yehova alifanya agano na Daudi la ufalme wa milele katika ukoo wake. (2 Sam. 7:1-17) Ndiyo sababu malaika Gabrieli, alipokuwa akimtangazia Mariamu aliyekuwa wa kabila la Yuda kuzaliwa kwa Yesu baadaye, alisema hivi: “Yehova Mungu atampa yeye kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala kama mfalme juu ya nyumba ya Yakobo [Israeli] milele, na hakutakuwako na mwisho wa ufalme wake.”—Luka 1:26-33, NW.
11. Tunaposali maneno yaliyomo katika Mathayo 6:9, 10, tunakubali kwa Mungu kwamba twahitaji nini?
11 Namna gani, basi, tukisali kwa Yehova Mungu kama Yesu alivyoagiza wanafunzi wake wasali: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatukie, kama mbinguni, pia duniani”? Basi, kwa hivyo tunakiri kwa Mungu ya kwamba twauhitaji ufalme wa Mwana wake Yesu Kristo.—Mt. 6:9, 10, NW.
12. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kufanya nini, kwa hiyo ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo utafanya nini kwa falme za ulimwengu huu?
12 Jumuiya ya Wakristo haijapata kamwe kuwa ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa katika kujitahidi kwake katika kuzigeuza serikali za ulimwengu ziwe serikali kweli kweli za Kristo. Basi, ni katika njia gani tutakuwa na ufalme wa Kristo ukitawala juu ya dunia hali serikali hizi zote za kisiasa zipo na zinaongoza mambo ya dunia? Hatuwezi kuwa nao chini ya hali hizo. Ndiyo sababu twahitaji serikali hizi zisizokamilika na zenye makosa za wanadamu ziondolewe mbali na dunia. Hili haliwezi kufanywa kwa uwezo wa kibinadamu. Kwa sababu hiyo twauhitaji ufalme wa Yesu Kristo utimize hili. Utatimiza hili, kulingana na unabii wa Mungu katika Danieli 2:44, unaosema: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”
13. Ni wakati gani na wapi serikali hizo za kilimwengu zitaondolewa kwa mshindo, lakini waokokaji wa kidunia watapaswa kuwa na nini zaidi?
13 Kuondolewa huku kwa serikali za kisiasa za leo katika njia yenye kuharibu kutatimizwa wakati wa upeo wa “dhiki kubwa” inayokuja katika lile linaloitwa na Ufunuo 16:14, 16, Har–Magedoni. Watakuwako waokokaji wa kibinadamu wa hiyo “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. Hawa watahitaji kuwa na zaidi ya dunia yenye kuondolewa serikali chafu, zisizofaa kitu za wanadamu wenye dhambi, wenye kufa. Ni nini zaidi ya hilo watakalohitaji? Ni kuondolewa kwa watu wabaya wote wasioonekana na wenye uwezo usio wa kibinadamu ambao wamekuwa wakiziongoza serikali hizi za kisiasa. Lakini ni watu gani hao wasioonekana wenye uwezo usio wa kibinadamu? Tukijibu ni Shetani Ibilisi na malaika zake wa kishetani, sayansi ya kisasa haitasadiki. Lakini acha Yesu Kristo mwenyewe apatikane wa kweli, si sayansi ya kisasa. Yeye alisema kwamba Shetani Ibilisi ndiye “mtawala wa ulimwengu huu.” Bila shaka Yesu Kristo, ambaye Mungu alituma kutoka mbinguni, apaswa ajue.—Yohana 12:31; 14:30, NW.
14. Ni serikali gani itakayokuwa na uwezo wa kutosha kuondoa Shetani na mashetani wake katika cheo chao cha kutawala wakaaji wa dunia, na kwa njia gani?
14 Pia, katika njozi ambayo Yesu Kristo aliyetukuzwa alimpelekea mtume Yohana alieleza kwamba Shetani Ibilisi ndiye “audanganyaye ulimwengu wote.” (Ufu. 12:9) Basi itataka serikali ya kiroho ya kimbinguni kumwondoa Shetani na malaika zake wa kishetani katika cheo chao cha kutawala juu ya wakaaji wote wa dunia. Ufalme wa Yesu Kristo ndiyo serikali hiyo ya kimbinguni yenye nguvu ya kuweza kuletea wanadamu faraja hii. Hii, pia, ni sababu kwa nini twahitaji ufalme huo. Baada ya ushindi wake katika vita ya Har–Magedoni, utamfunga Shetani Ibilisi na malaika zake wote wa kishetani katika shimo refu mbali na ujirani wa dunia yetu. Kufungwa kwao kutakuwa kwa muda wa miaka elfu ya ufalme wa Kristo.—Ufu. 19:11 mpaka 20:3.
15. Ufunuo waonyeshaje faida zenye kutoa uzima zitakazokuwa tele kwa wote watakaokuwa duniani chini ya ufalme wa Kristo?
15 Wakati wa utawala huu wa miaka elfu wa Yesu Kristo, faida zenye kutoa uzima zitatiririka kama mto kwa wale wote watakaoishi duniani ambao alitolea uhai wake kama Mwana-Kondoo wa dhabihu. Hili lafananishwa vizuri katika sura ya mwisho ya Ufunuo. Ndani yake mtume Yohana huonyesha kilicho chanzo cha mipango ya uzima wa milele wa jamaa ya kibinadamu. Yohana asema hivi: “Kisha [malaika wa Mungu] akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo, katikati ya njia kuu [ya mji]. Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi.”
16. Chanzo cha faida zote hizo zenye kutoa uzima ni nini, nao Ufalme utahakikishaje kwamba wanadamu hawana laana tena?
16 Ndipo, ili kuonyesha kwamba baraka hizo zatokana na kiti cha kifalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo Yesu Kristo, mtume Yohana anaongeza maneno haya: “Wala hapatakuwa na laana yo yote tena. Na kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwamo ndani yake. Na watumwa wake watamtumikia.” (Ufu. 22:1-3) Ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo wahitajiwa ili kubariki wanadamu, si kuwalaani. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, atahakikisha kwamba mambo duniani yataendeshwa katika haki ili yatokeze baraka.
WANADAMU WALIOKUFA WAHITAJI UFALME
17. Ni nani watakaokuwa wa kwanza kushiriki mipango hiyo yenye kutoa uzima, lakini kwa sababu gani kutakuwa na washiriki wengine?
17 Watakaokuwa wa kwanza kushiriki mipango hiyo yenye kutoa uzima kutoka katika kiti cha enzi cha Mungu kupitia kwa Kristo ni “mkutano mkubwa” wa waabudu watakaookoka “dhiki ile iliyo kuu” ambayo katika hiyo falme za ulimwengu huu zitavunjwa vipande vipande. (Ufu. 7:9-14; Dan. 2:44; Mt. 24:21, 22) Hivyo, basi, je! watakuwako washiriki wengine wa mto wa mfano wa maji ya uzima na miti ya uzima ya mfano? Ndiyo, kwa sababu Yesu Kristo kama “Mwana-kondoo wa Mungu” alifia wanadamu zaidi, si hao watakaookoka dhiki tu. Na tukumbuke yale ambayo Yesu alisema karibu na kaburi la kuzikia katika Bethania karibu na Yerusalemu katika mwaka wa 33 W.K. Wakati huo alisema hivi: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa hata milele. Je! unayasadiki hayo?” Martha, dada yake Lazaro aliyekufa, akajibu: “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.” (Yohana 11:25-27) Basi namna gani sisi leo? Je! sisi wenyewe twaweza kutoa jibu lile lile la imani kwa ulizo hilo?
18. Kwa sababu gani tuna sababu thabiti kujibu Ndiyo kwa ulizo la Yesu, kama alivyofanya Martha, na kwa sababu gani Yesu aweza bado kusema: “Mimi ndimi huo ufufuo na uzima”?
18 Tuna sababu thabiti kujibu Ndiyo, kwa kuwa kisha Yesu alithibitisha maneno yake yenye maana kwa kumfufua rafiki yake Lazaro ijapokuwa ilikuwa siku ya nne tangu huyo alipokufa. (Yohana 11:28-45) Punde baada ya hapo, wakati ulimfikia Yesu mwenyewe afufuliwe kutoka kwa wafu. Alikufa Siku ya Kupitwa. Siku ya tatu tokea wakati huo alifufuliwa kutoka kwa wafu kwa nguvu za uweza wa Baba yake wa kimbinguni. Siku ya 40 tokea hapo, alipaa mbinguni kutoka mahali karibu na Bethania juu ya Mlima wa Mizeituni. (Luka 24:50-53; Matendo 1:1-12) Huko mbinguni Yesu Kristo aliyetukuzwa bado aweza kusema hivi: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima.” Kuonyesha kwamba amepewa mamlaka na Mungu Baba yake kufufua wafu, anatuhakikishia kwa maneno yake katika njozi ya Ufunuo kwa Yohana: “Nami nilikuwa nimekufa, na tazama, mimi ni hai hata milele na milele. Nami nina fungulo za mauti, na za Hadeze.”—Ufu. 1:18, SCB.
19. Alipofufuliwa, Yesu Kristo alikuwaje “mzaliwa wa kwanza katika wafu,” na kwa sababu gani Lazaro rafiki yake na wengine waliofufuliwa na Yesu hawakuwa hivyo?
19 Yesu Kristo alikuwa ndiye wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu aishi milele kama mtu aliyefufuliwa. Hivyo anaitwa kwa usahihi “mzaliwa wa kwanza katika wafu” na “limbuko lao waliolala” katika mauti. (Kol. 1:18; 1 Kor. 15:20) Hata Lazaro rafiki yake na wengine ambao yeye na mitume wake walifufua kutoka kwa wafu mwishowe walikufa wakazikwa katika kaburi la kawaida la wanadamu, yaani, katika Hadeze. Kufunguliwa kwao mapema katika mauti na Hadeze kulikuwa kumekuwa kwa muda tu. Hivyo, “milango ya Hadeze” yapaswa iendelee kuwa imefungia watu hao na wanadamu wengine wote waliokufa na kukombolewa mpaka kusimamishwa kwa ufalme wa Kristo katika mbingu katika wakati wa Mungu uliowekwa.—Mt. 16:18; Isa. 38:10, 18, SCB.
20, 21. Ni wakati gani na wapi ufalme wa Kristo ulisimamishwa, naye akiwa Mfalme mwenye Kutawala angefufua nani kwanza?
20 Historia ya ulimwengu katika karne yetu ya 20 yatupatia utimizo wa unabii wa Biblia na yaonyesha kwamba ufalme wa Kristo ulianza kutawala katika mbingu mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 W.K. (Luka 21:24; Eze. 21:25-27) Akiwa katika mamlaka ya kimbinguni ya Ufalme Yesu Kristo angeelekeza uangalifu wake kwanza kwenye wanafunzi wake waaminifu waliokufa, kama vile mitume wake na wanafunzi wengine walioitwa kwenye ufalme wa kimbinguni pamoja naye. Angewafufua hawa kwenye uzima usioweza kufa wa kimbinguni, ili wawe “ufalme na makuhani kwa Mungu wetu,” kama inavyoelezwa katika Ufunuo 5:10. Kwa njia hiyo yangetimizwa yale ambayo mtume Yohana hutuambia katika Ufunuo 20:4-6, NW:
21 “Nami nikaviona viti vya enzi, nao walikuwako wale walioketi juu yake, na uwezo wa kuhukumu ulipewa kwao. Naam, nikaziona nafsi za wale waliokatwa kwa shoka kwa sababu ya ushuhuda waliomtolea Yesu na kwa kusema juu ya Mungu, . . . Nao wakawa hai wakatawala kama wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu. . . . Huu ndio ufufuo wa kwanza. Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa mauti ya pili haina mamlaka, lakini watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala kama wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.”
22. Wakati wa utawala wake wa mileani, Yesu atazitumiaje “fungulo za mauti, na za Hadeze, nao “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa dhiki wataonaje kitu kisichopata kushuhudiwa duniani?
22 Wakati wa utawala wake wa miaka elfu Yesu Kristo kama Kuhani Mkuu na pia kama Mfalme atazitumia “fungulo za mauti, na za Hadeze” kwa ajili ya wanadamu wengine waliokufa. Wafu hawa watasikia sauti yake na watatoka, kama mwenyewe alivyotabiri katika maneno yake yaliyoandikwa katika Yohana 5:28, 29. Ndipo “mkutano mkubwa” watakaookoka ‘dhiki ile iliyo kuu’ na kufungwa na kutupwa kwa Shetani na mashetani zake katika shimo refu watakapoona mwujiza usio na mfano wo wote. Wataona ufufuo wa duniani wa wanadamu wote waliokufa ambao Kuhani Mkuu Yesu alitolea uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kama “Mwana-kondoo wa Mungu.” (Yohana 1:29; 1 Tim. 2:5, 6; Ebr. 2:9) Mwishowe wale watakaofufuliwa watakuwa mamilioni na mamilioni idadi yao, wote hawa wakiwa wazao wa Adamu mkosaji ambaye kutoka kwake walirithi kutokamilika, udhambi na laana ya mauti. Hakutakuwako wakati wo wote kamwe ambapo lo lote mfano wa hili litakuwa limetukia katika dunia hii. Mtume Yohana alipewa njozi fupi ya mwujiza huu wa ajabu wa Mungu kupitia kwa Kristo, naye Yohana aisimulia katika Ufunuo 20:11-14.
23. Kwa sababu gani Yohana hakushangazwa na njozi ya Ufufuo, na wakaaji wa dunia wataona wakati gani 1 Wakorintho 15:26 ikitimizwa?
23 Je! Yohana alishangazwa na maono haya? Je! aliiona dunia imejaa mno watu? Hata kidogo! Yehova Mungu aliifanya dunia ijae wanaume na wanawake kwa kufaa, bila laana ya mauti kuwakalia bali wapewe haki ya uzima wa milele kama zawadi ya kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova Mungu. Wote wataishi katika paradiso yenye kuenea dunia yote! (Mwa. 1:26-28) Hivyo, wakati yule wa mwisho wa wanadamu wafu waliokombolewa atakapoitwa atoke kupitia kwa “milango ya Hadeze,” lile kaburi la kawaida la wanadamu halitakuwapo tena. Hadeze itakuwa imetupwa katika “ziwa la moto,” iharibiwe milele. Na wale watakaokuwa wakiishi duniani chini ya ufalme wa Kristo wa miaka elfu watakapokuwa wameitikia mafundisho yake na kukombolewa na udhambi wote na kuponywa kutokamilika kote kwa kibinadamu, ndipo kweli watakapokuwa hai kabisa. Ndipo “mauti,” ile mauti ambayo wanadamu walirithi kutoka kwa Adamu, itakapoungana na Hadeze katika “ziwa la moto.” (Ufu. 20:14) Katika tendo hilo tukufu wanadamu wataona utimizo maneno ya 1 Wakorintho 15:26, SCB: “Adui ya mwisho ya kuondoshwa ni mauti.” Wo wote watakaoharibiwa baada ya hapo pamoja na Shetani na mashetani zake kwa uasi wa kukusudia watapatwa na “mauti ya pili,” isiyo na ufufuo kutoka kwayo.
24. Kwa sababu gani hatuna haja kamwe ya kuona haya kumtolea Yesu ushuhuda, nasi twaongozwa kumtolea ushuhuda pamoja na nani?
24 Hatungekuwa na wakati wa kutosha kutoa ushuhuda juu ya Yesu Kristo na kusimulia yote yanayoonyesha jinsi alivyo na maana kwetu kama washiriki wa jamaa yenye dhambi ya kibinadamu. Hatutakata tumaini kamwe ndani yake. “Kwa maana lile Andiko lasema: ‘Hakuna anayemwamini atakayekata tumaini.’” (Rum. 10:11; Isa. 28:16, NW) Hakuna lazima kwetu kuona haya ya kumtolea Yesu Kristo ushuhuda kwa neno la kinywa au kwa vitabu. Kuthamini kunakoongezeka kwa namna tunavyomhitaji sana kwatuongoza tuungane na malaika katika kumtolea ushuhuda kwa utukufu wa Yehova Mungu na kwa ajili ya wanadamu walio katika hali yao mbaya sasa.
25. Kwa sababu gani sisi Mashahidi hatupaswi kusifiwa kwa asili ya ushuhuda tunaotoa, na ni nani aliyeongoza unabii mbalimbali juu ya Yesu, na kwa kusudi gani?
25 Na tukumbuke aliyosema malaika wakati mtume Yohana kwa kushukuru alipoangukia miguu yake amwabudu: “Mimi ni mutumishi mwenzako na wa ndugu zako walio na ushuhuda wa Yesu. Abudu Mungu kwa maana ushuhuda wa Yesu [ndio unaoongoza kutoa] unabii.” (Ufu. 19:10, SCB) Hivyo sifa isitujie sisi wanadamu kana kwamba asili ya ushuhuda wa Yesu Kristo yatokana nasi. Ni Yehova Mungu aliyeona haja yetu kubwa na ukosefu wetu wa msaada na aliyemtoa Mwanawe wa kimbinguni kwa upendo awe mwanadamu Yesu Kristo kwa ajili yetu sote. Tena, kwa roho yake ya utendaji Mungu aliongoza unabii wote wa Biblia juu ya Yesu Kristo ili tupate kuongozwa nao kwa “Mwana-kondoo wa Mungu,” kwa Kuhani Mkuu huyu wa Mungu, kwa Mfalme huyu wa Kimasihi ambaye mwishowe atawapa wanadamu ambao wametawalwa vibaya kwa muda mrefu serikali kamilifu, yenye haki.
26. Tumeongozwa kwenye jibu gani na uchunguzi wetu wa ulizo, Yesu Kristo ni nani, hata sote tumhitaji?
26 Basi, Yesu Kristo ni nani, hata sote tumhitaji? Uchunguzi wetu wa uhakika wa ulizo hili linalotaka kujibiwa umetuongoza kwenye jibu lenye kufaa. Yeye ndiye Mhitajiwa ambaye Muumba vitu vyote hutoa na humtumia aturudishe sisi kwenye jamaa yenye furaha, yenye baraka ya Baba yetu wa kimbinguni. Ndani ya jamaa hiyo ya ulimwengu wote tutajifurahisha uzima milele katika furaha nyingi, tukizidi katika upendo wake na utunzaji wake na kumwabudu na kumtumikia kwa upendo kwa vizazi vyote.—1 Kor. 15:28; Yohana 14:6; Matendo 4:12.
—Kutoka The Watchtower, April 15, 1976.
[Picha ya ukurasa nzima katika ukurasa wa 471]