Yesu Kristo Ni Nani, Hata Sote Tumhitaji?
“Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”—Matendo 4:12.
1. Kwa sababu gani sote kwa ujumla twahitaji mwokozi wa ulimwengu?
MWOKOZI WA ULIMWENGU—ndiye ulimwengu wa wanadamu wahitaji kwa haraka sana. Mwokozi wa jamaa nzima ya kibinadamu! Sote ni wa mwili na damu ile ile, wenye mwanzo mmoja. Sote tumo katika meli moja ya angani—dunia hii ya sayari, Kama meli hii ingezama, sote tungezama nayo katika bahari isiyo na mwisho yenye nafasi isiyopimika. Je! hili litatupata sisi? Kwa jinsi mambo yanavyotendeka katika meli yetu ya angani, yaonekana kama uharibifu huu mkubwa wa dunia yote u karibu zaidi sana kuliko wanasayansi wa kisasa wanavyokadiri. Je! jambo hilo lenye kuogofya sana litatukia? Ni nani na yuko wapi mwokozi wa ulimwengu awezaye kulizuia? Watu zaidi na zaidi wangependa kujua.
2. Mwokozi wa ulimwengu hawezi kupatikana katika miji gani mashuhuri leo, na ni nini kinachoonyesha hivyo?
2 Mwokozi huyo wa ulimwengu hayuko mjini New York leo—wenye jengo kubwa mno la Umoja wa Mataifa. Mataifa 144 yaliyo wanachama wa tengenezo hilo la amani na usalama wa ulimwengu wanapata taabu yakujisalimisha wenyewe mmoja mmoja. Mwokozi huyo wa ulimwengu hayuko Moscow, Urusi, ambako mfufulizo wa watawala wenye kujinyakulia mamlaka kwa nguvu umetawala kwa kuonea na kwa matumaini ya kuona ulimwengu ukigeuka kuwa wa Kikomunisti. Mwokozi huyo wa ulimwengu hayuko Yerusalemu, Israeli, ambako dini kubwa tatu za ulimwengu zina shughuli zile zile za muda mrefu, lakini zenye kupingana. Wala mwokozi wa ulimwengu hawezi kupatikana katika mji mwingine wo wote wenye maana ya ulimwengu ya zamani au ya kisasa. Huzuni kuu ya mataifa inayoendelea na kuugua kwa watu kunakoongezeka huonyesha uhakika huu.
3. Watu wa kilimwengu wanakataa kweli gani, lakini jambo la akili kwetu kutafuta wapi mwokozi wa ulimwengu?
3 Huenda hali ya ulimwengu ikawa isiyo na tumaini kabisa katika maana yake ya vivi hivi. Hata hivyo watu wanaofuata fikira za kisasa hawaikubali kweli. Kweli gani? Kwamba italazimu msaada unaohitajiwa wa ulimwengu uje kutokana na chanzo cha juu zaidi ya wanadamu. Wanakataa kuacha kuwatumaini wanadamu, wasaidizi wenye nguvu, wenye akili peke yao ambao wanaweza kufahamu katika akili zao zinazotegemea vitu vinavyoonekana tu. Tukifuata fikira zao, twaachwa bila uongozi. Twapotea. Lakini bila kujali cheo cha watu hao wenye nia ya kilimwengu, sisi wenyewe twajua kwamba sisi sio waumba wala hatukujiumba wenyewe. Tumebuniwa na kufanywa na kupewa akili kwa ajabu mno hata haiwezekani kuwa tuliumbwa vivi hivi na mwanadamu. Mbuni na Muumba wetu, aliyetuweka katika meli hii ya angani, ni mwenye uwezo kushinda mwanadamu bila shaka. Yeye yu juu juu yetu kama vile mbingu zilivyo juu zaidi ya meli yetu ya kidunia. Kwa kuwa tu maajabu ya ufundi Wake yampasa apendezwe nasi. Huenda isipatane na fikira za kimamboleo, lakini inafaa na ni jambo lenye akili kumtumaini Yeye kama mwenye uwezo wa kututokezea mwokozi wa ulimwengu.
4. Ni nani aliyetia katika wanadamu tumaini la kupata mwokozi wa ulimwengu, naye alituambia zamani za kale tugeukie nani tupate wokovu?
4 Hivyo, basi, je! yaelekea Muumba wetu huyu ndiye Yule aliyetia katika wanadamu tumaini la kuokolewa kwa wanadamu wote? Na mwokozi fulani wa ulimwengu? Ndiyo! Wazo hilo bora na lenye ujasiri lingeweza kutoka wapi kwingineko? Wakati wa karne saba kabla ya Wakati wetu wa Kawaida, ndiyo, zaidi ya karne moja kabla ya Wakati wa Buddha, Huyo aliandikisha maneno haya: “Niangalieni mimi, mkaokolewe, enyi ncha zote za dunia; maana mimi ni Mungu; hapana mwingine. Kwa nafsi yangu nimeapa, neno hili limetoka kinywani mwangu katika haki, wala halitarudi, ya kwamba mbele zangu kila goti litapigwa, kila ulimi utaapa. Mmoja ataniambia, Kwa [Yehova], peke yake, iko haki na nguvu; naam, watu watamwendea yeye, na wote waliomkasirikia watatahayarika.”—Isa. 45:22-24.
5. Jambo gani lisitufanye tuone haya kumgeukia Yehova tupate wokovu, na sababu gani?
5 Wokovu unaotolewa na Yehova waweza kufika kwenye miisho ya mbali ya dunia na kuenea ulimwengu wote wa wanadamu. Ndiye wa kugeukia katika tumaini la wokovu wa milele na kumwomba wokovu huo kwa hakika. Chuki ya ulimwengu juu ya jina Yehova isitutahayarishe na kutupotoa kwake. Wote wale wanaomkasirikia ndio watakaokuja moja kwa moja kwake Yeye na kutahayarika. Watashindwa kuupata wokovu ambao ni akiba ya wale wanaomtumaini bila kulazimishwa, wapate wokovu.
6. Kitabu cha mwisho cha Biblia chaonyeshaje kwamba mwito wa Yehova wa zamani za kale. kumgeukia yeye ungeitikiwa ulimwenguni pote?
6 Mwito wa Yehova kugeukia kwake kama Mungu peke yake wa wokovu uliandikwa katika kitabu cha ishirini na tatu cha Biblia Takatifu. Kitabu hicho kina unabii ulioongozwa na Mungu wa mtu wa Mashariki ya Kati aitwaye Isaya mwana wa Amozi, mkazi wa Yerusalemu wa kale. Kuonyesha kwamba mwito wa kimungu ungeitikiwa ulimwenguni pote imetabiriwa katika kitabu cha sitini na sita ambacho ndicho cha mwisho cha Biblia Takatifu kiitwacho Ufunuo na kilichoandikwa katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Katika sura ya saba, mstari wa tisa na kumi, Yohana mwana wa Zebedayo, mwandikaji aliyeongozwa na Mungu anasimulia njozi ya unabii aliyoona. Akionyesha kwamba, katika wakati wetu wenyewe, mkutano usiohesabika wa watu ungegeukia kwa Yehova ili kupata wokovu, Yohana huandika hivi: “Tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”
MWOKOZI WA ULIMWENGU ATAMBULISHWA
7, 8. (a) Neno “Mwana-Kondoo” lapaswa kufahamikaje? (b) Ni wapi ambapo Ufunuo waanza kutumia neno hilo, kuonyesha nini?
7 Ni kwa sababu gani mkutano huu wenye watu wa makabila yote, mataifa na rangi zote haukiri kwamba wokovu wao watoka kwa Mungu tu, bali pia na kwa “Mwana-Kondoo”? Je! twaweza kumtambua kwa usahihi huyu anayeitwa kwa mfano “Mwana-Kondoo”? Ndiyo!
8 Bila shaka lazima tumtambue. Kwanza, mtajo huu “Mwana-Kondoo” hautumiwi kama neno la mapendezi. Badala yake, mtajo huu waelekeza kwenye dhabihu, kwenye dhabihu ya lazima sana kwa ajili yetu sote. Katika kitabu cha Ufunuo mtajo huu “Mwana-Kondoo” watumiwa mara ishirini na saba kwa huyu anayehitajiwa. Mitajo hii ya “Mwana-Kondoo” inaanza katika sura ya tano, ambamo Yohana aliambiwa hivi: “Usilie; tazama, Simba aliye wa kabila ya Yuda, Shina la Daudi, yeye ameshinda apate kukifungua kile kitabu, na zile muhuri zake saba.” (Ufu. 5:5) Yohana alipoacha kulia, aliona nini? Anasema hivi: “Nikaona katikati ya kile kiti cha enzi . . . Mwana-Kondoo amesimama, alikuwa kana kwamba amechinjwa.”—Ufu. 5:6.
9. Huyu ‘Simba wa kabila ya Yuda’ ni nani, nacho cheo hicho chaonyesha nini juu yake?
9 Basi, ni nani Mwana-Kondoo huyu ambaye Biblia Takatifu hutambulisha kama “Simba aliye wa kabila ya Yuda” na kama “Shina” lenye kutoa uzima kwa mfalme wa kwanza wa Kiyahudi wa Yerusalemu, aitwaye Daudi? Ni Yesu Kristo, mzao wa kimwili wa mzee Ibrahimu na wa Mfalme Daudi wa kabila la Yuda. (Mwa. 49:9, 10; Mt. 1:1-6) Kuitwa kwake “Simba aliye wa kabila ya Yuda” humaanisha kwamba alikuwa ndiye “Shilo” aliyekuwa akitazamiwa kuja na “ambaye mataifa watamtii.” Hili lilimaanisha kwamba alipaswa awe Mfalme (kama baba yake Daudi alivyokuwa) wa serikali halisi ambayo mataifa yote ya dunia wangepaswa kutii kwa faida yao wenyewe. Kama Daudi alivyokuwa ametiwa mafuta kama mfalme na kwa hiyo alikuwa mtiwa mafuta, vivyo hivyo Mzao wake wa kifalme angekuwa mtiwa mafuta, ambaye Waebrania waliita “Masihi” lakini ambaye Wayahudi wasemao Kigiriki waliita “Kristo.” Ndiyo sababu tunao usemi huu “Yesu Kristo” (Yesu Mtiwa Mafuta) au “Kristo Yesu” (Mtiwa Mafuta Yesu). Lakini ikiwa anafananishwa na simba wa Yuda aliye mfano wa mfalme, sababu gani anafananishwa pia na “mwana-kondoo”?
10. Kulingana na aliyoona Yohana, Mwana-Kondoo huyu alikuwa amepatwa na nini, naye akanunua nini?
10 Mwandikaji Yohana anaeleza sababu, wakati anapotuambia aliyoona tena na kusikia, akisema: “Hata alipokitwaa kile kitabu, . . . [wakaimba] wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao [watamiliki] juu ya nchi.”—Ufu. 5:8-10.
11. Ni kwa kusudi gani huyu mwenye mfano wa mwana-kondoo alichinjwa, nayo Isaya, sura ya 53, ilikuwa imetabirije hilo?
11 Hivyo huyu “Simba aliye wa kabila ya Yuda” mfanya-ufalme aliuawa kama dhabihu, kama vile Torati ya Mungu iliyotolewa kwa taifa la Israeli kupitia kwa Musa ilivyokuwa na mpango wa kutolewa dhabihu kwa mwana-kondoo asiye na waa kwa ajili ya dhambi. Yeye alikuwa ndiye yule “mtumishi” wa Yehova, ambaye Isaya nabii aliyeongozwa na Mungu alitabiri yafuatayo juu yake: “Alionewa, lakini alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; naam, hakufunua kinywa chake. . . . alimwaga nafsi yake hata kufa, akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, na kuwaombea wakosaji.”—Isa. 53:7, 12; Matendo 8:30-35.
12. Kwa sababu gani hatuwezi kukataa kwamba hatuhitaji dhabihu ya Mwana-kondoo kwa sababu tu wenye dhambi na wakosaji?
12 Hili lafunua sababu yenye nguvu kwa nini twamhitaji Yesu Kristo. Twamhitaji kama Mwana-Kondoo wa dhabihu aliyetolewa kwa Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu. Unabii wa Isaya uliotumiwa sasa hivi husema juu ya wenye dhambi na wakosaji. Kwa jumla watu hawataki waitwe wenye dhambi na wakosaji. Vivyo hivyo, hakuna watu kati yetu wawezao kukana kwamba sote hatuna hitilafu na maelekeo ya kutenda mabaya. Tulipata mambo haya mahali fulani. Sote twaweza kulaumu wazazi wetu. Lakini nao, walipata kutokamilika na maelekeo mabaya kutoka kwa wazazi wao. Na hivyo twaweza kurudi moja kwa moja mpaka kwa mume na mke, watu wa kwanza wawili, ambao Biblia Takatifu huwaita Adamu na Hawa. Kushtakiwa kwa wazazi kuwapa watoto wao kutokamilika na maelekeo yenye makosa kwaishia na Adamu na Hawa. Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu Adamu na Hawa hawakupata kutokamilika na udhambi wao kutoka kwa Mungu, Muumba na Baba yao wa kimbinguni. “Kazi yake ni kamilifu,” naye akaumba Adamu na Hawa wakamilifu, kwa vile walivyoumbwa kwa mfano wake mwenyewe’.—Kum. 32:4; Luka 3:38; Mwa. 1:26-28.
13. Ni ulizo gani linalotokea juu ya mahali pa kuzaliwa kwetu, na ni nini kilichotuzuia sote tusizaliwe wakamilifu?
13 Hakuna wo wote kati yetu waliozaliwa katika Paradiso, yaani katika Bustani ya Edeni, kwa miaka elfu sita iliyopita. Lakini Adamu na Hawa waliumbwa wakawekwa humo. (Mwa. 2:7-25) Bila shaka, paradiso hiyo ya kidunia ya kwanza haingeweza kututosha sote leo; ingalipanuliwa ienee dunia yote. Hata hivyo, ni kwa sababu gani hatukuzaliwa sote katika paradiso ya kidunia ya kuenea dunia yote? Ndiyo, na ni kwa sababu gani sote tukazaliwa wasiokamilika, wenye maelekeo mabaya, wanyonge-wanyonge na wenye kufa? Maelezo yenye akili peke yake yangeweza kuwa kwamba wale wanadamu wawili wa kwanza, ambao sote tulitokana nao, walikosa. Basi, habari ya kweli katika Biblia Takatifu yapatana na maelezo hayo yenye akili. Adamu na Hawa walikosa kabla ya kuzaa watoto. Hii lamaanisha kwamba hawakufanya waliloambiwa na Mungu wafanye. Walimwasi, Baba yao wa kimbinguni. Walifanya dhambi au wakakosa shabaha ya kukamilika kwa kibinadamu.
14. Kwa sababu gani Mungu alikuwa na haki ya kuwafukuza Adamu na Hawa katika paradiso, na ni rehema gani upande Wake imetufanya tuwe hai leo?
14 Je! twaweza kumlaumu Mungu kwa adhabu ya hakika aliyosema ingetolewa juu ya tendo dogo zaidi sana la kumwasi kama Mpaji-sheria na Hakimu Mkuu kuliko wote? Tusingeweza kufanya hivyo kwa kufaa. Lakini twaweza kumlaumu Mungu kwa kuwafukuza katika paradiso yao? Hata! Kama Muumba wa Bustani ya Edeni anazo haki za uenyeji wa mali. Ana haki kabisa kuamua nani wamepaswa kuwa wapangaji katika mali yake. Ebu tazama namna watu wachoyo, wasiofikiri wanavyoharibu makao mazuri wakiyafanya kuwa makao machafu sana. Ebu tazama jinsi jamii yote ya kibinadamu inavyoiharibu dunia nzima, kutaka kuiharibu kwa vita ya atomiki, pamoja na hasara na uchafuzi ambao tendo hili lingefanyia uso wa dunia. Tunapolifikiria, inapendeza sana kujua kwamba Mungu aliruhusu Adamu na Hawa wenye dhambi waishi nje ya paradiso ya Edeni, ili waijaze dunia watu kwa kadiri ilivyo leo. Bila shaka lilikuwa tendo lenye rehema upande wa Mungu kuruhusu Adamu na Hawa waendelee kuishi wapate kuzaa watoto, hata twajikuta sasa twaishi duniani miaka elfu sita baadaye.—Mwa. 3:1 mpaka 4:2.
15. Adamu aliamua kuwa baba wa namna gani kwa wazao wake, nasi sote tukawaje wenye dhambi kwa sababu yake?
15 Aliposhawishwa atende dhambi pamoja na mke wake Hawa, ilimpasa Adamu aamue angekuwa baba wa namna gani kwa watoto wake, kama ni baba mwenye kumwogopa Mungu, mwenye kumtii sana Baba yake wa kimbinguni na kuwa katika uhusiano usiovunjika pamoja na Yeye, ama kama baba mwenye kumwasi Mpaji-Uzima wake na kuhukumiwa kufa, adhabu ya dhambi. (Mwa. 2:15-17) Adamu alichagua kuwa baba huyo wa pili kwetu. Hivyo hatuwezi kumshtakia Mungu Muumba wa wanadamu kutokamilika na udhambi wetu. Ni kama mwandikaji wa Biblia wa karne ya kwanza, mtume wa Kikristo Paulo, alivyoandika, akisema: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Rum. 5:12) Kwa kuwa Mungu alitia uzazi katika mtu wa kwanza, sisi sote wazao wake tulikuwa viunoni mwake Adamu alipofanya dhambi. Kwa njia hiyo sote tulifanya dhambi ndani yake na, kwa sababu hiyo, sote tumezaliwa wenye dhambi, chini ya laana ya mauti.
16. Tusisahau kusawazika gani kwa haki ya kimungu na 1 Wakorintho 15:21, 22 yatuhakikishiaje hilo?
16 Tusikose hapa kuangalia jambo moja lenye maana linalofundishwa katika Biblia Takatifu ya Mungu. Jambo gani hilo? Hili: Kama vile Mungu anavyomwona mtu huyo mmoja Adamu kuwa mwenye kuhusika na dhambi yote na adhabu yake mauti katika ulimwengu leo, ndivyo awezavyo kumwona mtu mmoja mwingine, anayelingana na Adamu, kuwa mwenye uwezo wa kufuta dhambi ya ulimwengu na kuuondolea ulimwengu wa wanadamu waliozaliwa katika dhambi adhabu ya dhambi. Kwa kuwa na mpango huo wenye hekima na wenye rehema, haki ya kimungu inasawazika sana. Hili ni jambo tulilohitaji sote, na hili ndilo tunalohakikishiwa katika Biblia Takatifu ya Mungu, katika 1 Wakorintho 15:21, 22, SCB, katika maneno haya: “Maana kwa kuwa kufa kuliletwa na mutu, hivyo ufufuko wa wafu uliletwa na mutu. Kwa sababu kama katika Adamu wote wanakufa, hivyo wote katika Kristo watapatizwa uhai.”
17. Mtu wa kulingana na Adamu angeweza kutokezwa duniani kwa njia gani peke yake, na ni nani aliyetangaziwa kwa kufaa kuzaliwa kwa mtu huyo?
17 Lo! jinsi huu ulivyo mpango wa ajabu na usio wa gharama, na rahisi sana! Tuliyehitaji ni mtu mmoja tu, anayelingana na Adamu alipokuwa katika ukamilifu wa kibinadamu na bila dhambi. Kwa kuwa hakuna mmoja wetu sisi wazao wa wanadamu wa kwanza wawili aliyezaliwa kama anayelingana na Adamu katika hali yake isiyo na hatia katika Edeni, mtu huyo angewezaje kutokezwa duniani? Mtu anayehitajiwa angeweza kutolewa kwa mwujiza wa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Mwujiza huu ulitukia kuelekea mwisho wa karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Ulitokeza kuonekana kwa yeye ambaye mara nyingi Ufunuo unamwita “Simba.” Ijapokuwa ni kama mwana-kondoo, huyu alionekana kuwa “Simba aliye wa kabila ya Yuda” na “Shina la Daudi.” Ushuhuda wote wa Biblia Takatifu ya Mungu unaelekeza kwa huyu kama akiwa Yesu Kristo, aliyezaliwa katika mji wa Daudi wa Bethlehemu mwanzoni mwa Oktoba wa mwaka wa 2 K.W.K. Kwa kupatana sana na kugeuka kwake awe mwana-kondoo wa dhabihu, kuzaliwa kwake kulitangazwa na malaika wa Mungu kwa mashahidi wa Mungu waliochaguliwa, kwa wachungaji waliokuwa wakilinda makundi yao ya kondoo usiku.—Luka 2:4-18; Mt. 2:1-18.
18. Mwana huyu wa “ukoo wa Daudi” aliyeitwa kwa kufufuliwa kwa wafu ni wa nani?
18 Kama mtume wa Kikristo Paulo anavyoiita, yote haya yalikuwa “Injili ya Mungu; ambayo Mungu amekwisha kuiahidi kwa kinywa cha manabii wake katika maandiko matakatifu; yaani, habari za Mwanawe, aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili, na kudhihirishwa kwa uweza kuwa mwana wa Mungu, kwa jinsi ya roho ya utakatifu, kwa ufufuo wa wafu, Yesu Kristo Bwana wetu.”— Rum. 1:1-4.
19. Ni katika hali gani Yesu alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu kwa kufufuliwa, lakini hapo kwanza alikuwa amekuwa nini alipokuwa duniani?
19 Basi kwa habari ya mtu kuwa mwana wa Mungu katika maana ya kweli, mtu wa kwanza Adamu alikuwa “mwana wa Mungu,” kulingana na habari ya ukoo wa kimwili wa Yesu Kristo kama inavyotolewa katika Luka 3:23-38, NW. Lakini Adamu alikosa kumtii Baba yake wa kimbinguni akafa akatuletea sote dhambi na mauti. Angali amekufa; hajafufuliwa kutoka kwa wafu. Alipoteza hali yake ya kuwa mwana wa Mungu. Lakini Yesu Kristo amefufuliwa katika hali ya kiroho na kwa njia hiyo ametangazwa upya kuwa Mwana wa Mungu akiwa na nguvu kubwa zaidi kuliko alizokuwa nazo duniani. Lakini hata alipokuwa duniani, na ijapokuwa alizaliwa kama mwanadamu mwenye mwili kupitia kwa bikira wa Kiyahudi aitwaye Mariamu, Yesu alikuwa Mwana wa Mungu. Hatuna sababu ya kutilia uhakika huo shaka. Kwa sababu gani sivyo?
20. Ni kwa sababu gani Yohana Mbatizaji hakutoa wazo lake mwenyewe aliposhuhudia kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?
20 Wakati huo mahitaji ya hali yalimtaka “mwana wa Mungu” apatikane duniani. Yesu Kristo alionekana kuwa ndiye Mwana wa Mungu aliyehitajiwa. Alipokuwa mtu mzima mwenye umri wa miaka thelathini, alibatizwa katika maji na Yohana Mbatizaji, mwana wa kuhani wa Kiyahudi aitwaye Zekaria. Yohana alimtangaza wazi Yesu Kristo kuwa nani? Yohana Mbatizaji aliwaambia wanafunzi wake kwamba Yesu Kristo alikuwa Mwana wa Mungu. Yohana alijua hili, si kutokana na kuwazia kwake mambo. Sababu gani hivyo? Kwa sababu mara alipombatiza Yesu, Yohana alisikia sauti ya Mungu ikisema kutoka mbinguni hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mt. 3:13-17; Marko 1:9-11; Luka 3:21, 22) Hivyo, Yohana alisema hivi hadharani: “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu.”—Yohana 1:34.
21. Kwa sababu gani Yesu asingeweza kuwa alikuwa na baba wa kibinadamu, wa kimwili, lakini ni nani aliyekiri kuwa ndiye baba yake?
21 Walakini, kuwa kwa Yesu mwana wa Mungu hakukuanza na kuzaliwa kwake kwa kibinadamu kupitia kwa Mariamu, bikira wa Kiyahudi. Kwa kuwa Yesu alizaliwa na bikira aliyekuwa hajapata kufanya ngono yo yote na mwanamume mzao wa Adamu, Yeye asingaliweza kuwa na baba wa kibinadamu, wa kimwili. Hakuna malaika aliyekuwa baba yake, kwa maana Mariamu hakufanya ngono na malaika mwenye kuvaa mwili kama akina mama wa Wanefili wabaya sana katika siku za Nuhu mwunda-safina. (Mwa. 6:1-4) Malaika Gabrieli, aliyemtokea Mariamu akamweleza jinsi angekuwa mama wa Yesu kwa njia ya mwujiza, hakuwa baba ya mwana mzaliwa wa kwanza wa Mariamu. (Luka 1:26-38; Mt. 1:18-25) Sayansi ya kisasa leo huenda ikapinga kuzaliwa kwa Yesu na bikira kwa dai la kwamba haiwezekani, lakini malaika Gabrieli aliondoa shaka lo lote katika akili ya Mariamu kwa kusema: “Hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.” (Luka 1:37) Kwa hiyo Mungu alikiri mbele ya ulimwengu wote kuwa ndiye Baba ya mtoto Yesu katika ukoo wa Daudi.
22. Maneno ya Yohana na ya Yesu katika sala kwa Mungu yaonyeshaje kwamba Yesu alikuwa amekuwa Mwana wa Mungu mbinguni?
22 Yote hayo ni kweli, lakini je! kuzaliwa kwa Yesu katika Bethlehemu-Uyahudi ulikuwa ndio mwanzo wa kuwako kwake kama Mwana wa Mungu? La! Yohana Mbatizaji, aliyezaliwa karibu miezi sita kabla ya kuzaliwa Yesu, alisema waziwazi juu ya Yesu ambaye alikuwa amebatiza hivi: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu.” (Yohana 1:29, 30) Basi, kwa kuwa Yesu hakuwako duniani kama mwanadamu kabla ya Yohana Mbatizaji, alikuwa amekuwako wapi kabla ya Yohana? Alikuwa juu mbinguni. Huko ndiko alikokuwa amekuwako kama Mwana wa Mungu. Huko ndiko alikokuwa ameonana uso kwa uso na kushirikiana na Baba yake wa kimbinguni. Hii ndiyo sababu usiku kabla ya kufa kama mfia imani nje ya kuta za Yerusalemu, alimwambia Baba yake wa kimbinguni katika sala hivi: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”—Yohana 17:4, 5.
23. Mwana wa Mungu alikuwa wapi alipotumwa Nayo ulimwenguni, na kwa njia gani?
23 Hivyo, yeye ambaye akawa Yesu Kristo, “Mwana-kondoo wa Mungu,” alikuwa amekuwako kama Mwana wa Mungu pamoja na Baba yake wa kimbinguni katika makao ya kiroho yasiyoonekana. Hivyo, ili awe Mwana wa Mungu wa kibinadamu kwa jina la Yesu Kristo, ilimpasa Mungu Mwenye Nguvu Zote ahamishe uhai wake kutoka mbinguni kuutia katika tumbo la uzazi la kibinadamu mwilini mwa bikira wa Kiyahudi. Katika njia hii Mungu aliendelea kuwa Baba yake wakati wa kuzaliwa kwake katika Bethlehemu. Ni kutoka mbinguni peke yake ndiko Mungu alikouhamisha uhai wa Mwana wake kwa mwujiza na kwa njia hiyo ‘akamtuma’ Mwana wake, kama Yesu Kristo alivyomwambia mtawala wa Kiyahudi Nikodemo: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.”—Yohana 3:16, 17.
24. Kwa sababu gani twamhitaji Mwana wa Mungu kama “Mwana-kondoo”?
24 Katika njia hii twaona jinsi Mungu alivyomtoa mtu mmoja ambaye tulimhitaji ili tupate wokovu wa milele, mtu mmoja aliyelingana na Adamu wakati alipokuwa mkamilifu na katika hali isiyo na dhambi katika Bustani ya Edeni. Mtu huyu peke yake ndiye aliyeweza kujitoa kwa Mungu atolewe dhabihu kama “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Kwa sababu dhambi yetu yahusika, twamhitaji.