Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 5/15 kur. 232-238
  • Uamuzi wa Hakika Unatakiwa kwa Wale Wanaopata Kimbilio

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uamuzi wa Hakika Unatakiwa kwa Wale Wanaopata Kimbilio
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MKIMBIE BABELI MKUU UJE ALIKO MWANAMKE WA KWELI WA MUNGU
  • UKARIBISHAJI KUJA KWENYE PARADISO YA KIROHO
  • Ahadi ya Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Tutakuwa Upande wa Nani Taabu ya Ulimwengu Ifikiapo Upeo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kimbilio Letu Chini ya “Ufalme wa Mbinguni” Usioharibika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 5/15 kur. 232-238

Uamuzi wa Hakika Unatakiwa kwa Wale Wanaopata Kimbilio

1. Ni wanawake gani wawili wa mfano wanaotajwa katika kitabu cha Ufunuo, nao wanatambulishwaje?

TUNAPOTAZAMA katika kitabu cha mwisho cha Biblia, tunaona wanawake wawili wa mfano wanaotofautiana sana. Mmoja ndiye ‘Babeli Mkuu,’ na yule mwingine ndiye “mke” wa Mwana-Kondoo wa Mungu. Yule wa kwanza amepewa jina “kahaba.” Yule wa pili, “bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo,” ni bikira. Wote wawili ni matengenezo ya kidini, moja ni chafu, lile jingine safi. “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo,” ndilo kundi la wafuasi waaminifu 144,000 wenye mfano wa bikira wa Mwana-Kondoo Yesu Kristo, wote wakiwa Waisraeli wa kiroho. Babeli Mkuu ndiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo iliyotolewa katika Babeli ya kale. Hivyo, imefanyizwa na wote wale wanaozoea dini kwa kupinga Ukristo wa kweli. Ndiyo sababu mtume Yohana ‘alimwona yule mwanamke amelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu.’ (Ufu. 17:6) Kwa hiyo, dini ya washiriki wa Babeli Mkuu si ya Kikristo, bali ni ya Kibabeli, na kwa hiyo ni ya uongo.

2. Kuna uhusiano gani kati ya Jumuiya ya Wakristo na Babeli Mkuu, na hii inaonyeshwaje wazi?

2 Kwa sababu ya kuwa tengenezo kuu la kidini la Mamlaka ya Ulimwengu ya Kirumi, Jumuiya ya Wakristo (yaani, Kristendomu) ikawa binti ya Babeli Mkuu, anayesemwa kuwa hivi: “Na katika kipaji cha uso wake alikuwa na jina limeandikwa, la siri, BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI.” (Ufu. 17:5) Kwa hiyo, si ajabu kwamba Jumuiya ya Wakristo inamwiga mama yake wa kidini, ambaye juu yake yasemwa hivi: “Wafalme wa nchi wamezini naye, nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo ya uasherati wake.” (Ufu. 17:1, 2) Jumuiya ya Wakristo inafurahia urafiki mkubwa na ulimwengu. Hii inatukumbusha juu ya andiko lililomo katika Yakobo 4:4: “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” Miungano mingi ya Kanisa na Serikali katika Jumuiya ya Wakristo haiiletei sifa. Inaitia alama kuwa mwasherati-mke wa kiroho, mwenye kujitia katika siasa za ulimwengu. Analaaniwa kama kimbilio la uongo na chafu la wanadamu.

3. Litakalompata Babeli Mkuu, kutia na Jumuiya ya Wakristo, linaonyeshwaje waziwazi?

3 Limpatalo Babeli Mkuu laipata Jumuiya ya Wakristo pia. Hakuna tofauti. Ufunuo sura ya 17 yaonyesha jambo hili wazi kabisa, ingawa imeandikwa kwa usemi wa mfano. Tunapofikia upeo wa mfano huu unaoonyeshwa katika sura hiyo, twasoma hivi: “Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama [ambaye Babeli Mkuu alikuwa amekuwa akimpanda kama bibi-mkuu], hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.” Hiyo si hali nzuri hata!​—Ufu. 17:16.

MKIMBIE BABELI MKUU UJE ALIKO MWANAMKE WA KWELI WA MUNGU

4. (a) Yohana alisikia kelele gani yenye kulazimisha iliyo katika Ufunuo 18:4-8, na kwa sababu gani ilikuwa ya haraka? (b) Huenda wengine wakaitikiaje kelele hiyo, lakini lazima sote tukabili ulizo gani leo?

4 Si ajabu kwamba, mapema katika Ufunuo, sura ya 18, tunaisikia kelele ya haraka na yenye kulazimisha ikisema: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. . . . Mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti, na huzuni, na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana Bwana Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu.” (Ufu. 18:4-8) Je! wewe umeisikia na kuitii kelele hiyo? Pengine wasema umeona unafiki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ukayaacha, ikiwa kweli ulikuwa ukijihesabu kuwa mshiriki katika mojawapo. Wako watu wengi katika kizazi chetu ambao hawakulelewa wakiwa na dini, lakini wanaosema kwa mdomo tu kwamba wanaamini bila shaka Mungu yuko. Je! wewe unajiona kutosheka kuwa mkosa dini tu? Huwezi kujidai kuwamo katika mahali penye usalama pa kimbilio wala huwezi kujidai unapatafuta ikiwa unashikilia maoni hayo yasiyofaa ya kutoonyesha upande ulioko. Kwa sababu ya ushuhuda wote uliopo wa mwisho unaokaribia wa taratibu iliyopo ya mambo, kutia na Jumuiya ya Wakristo, lazima tuelekeane na ulizo hili: Sisi tuko upande gani katika siku hii ya tukio kubwa sana linalokaribia?

5. Baada ya kuona njozi ya 144,000, ni kundi gani la watu aliloliona Yohana, akatoa maelezo gani?

5 Pengine wasema wewe si mmoja wa jamii ya “ufalme wa mbinguni” yenye wale wanaojua kwamba wana tumaini la kimbinguni, kama ilivyozungumzwa mapema. Lakini hii haikuondoi katika kibali ya Mungu usipate kimbilio chini ya mabawa yake. (Zab. 91:4) Baada ya masimulizi ya Waisraeli wa kiroho 144,000 katika Ufunuo 7:4-8, twasoma hivi: “Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Halafu, ili kuendelea kuwatambua zaidi, twasoma hivi: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake . . . [na] huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.” Lo! hiyo ni hali yenye kuvutia namna gani!​—Ufu. 7:9-17.

6. (a) Yesu alisema nini juu ya watu hao? (b) Ni kwa njia gani alifanya hilo liwe jambo la kipekee sana, na hiyo ikahakikisha nini?

6 Ili kuendelea kuonyesha ni akina nani waliomo katika huu “mkutano mkubwa,” na kukukaribisha uwe mmoja wao, tunataka kukukumbusha aliyoyasema Yesu juu ya wafuasi wake, ambao aliwafananisha na kondoo. Kwa habari ya wale watakaoshiriki pamoja naye katika kiti chake cha enzi, alisema hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32) Naam, “kundi dogo.” Lakini wakati mwingine, alipokuwa akitoa habari nyingi zaidi juu ya “kondoo” zake na yeye mwenyewe kama “mchungaji mwema” ‘atoaye nafsi yake kwa ajili ya kondoo,’ alisema hivi: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” Alifanya hili kuwa jambo la kipekee sana pia. Mapema kidogo alisema hivi: .“[Mchungaji] huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje.” Hii maana yake ni kwamba ukiwa mmoja wa kondoo zake kwa kujikana mwenyewe na kuendelea kumfuata, basi yeye anakujua wewe kwa kipekee. Na ebu angalia anavyokujua kwa kipekee katika maneno yake yanayofuata: “Kondoo wangu waisikia sauti yangu [si ya mtu mwingine ye yote]; nami nawajua [mmoja mmoja], nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.” Lo! huo ni uhakikisho wa kimbilio salama!​—Yohana 10:3, 16, 27-29; tazama pia Mathayo 16:24.

7. Ni onyo gani alilotoa Petro juu ya ‘’waalimu wa uongo”?

7 Tukirudia lile ulizo tuko upande wa mtu gani, inatufaa tufikirie yale ambayo mtume Petro aliongozwa na Mungu kusema juu ya jambo hili. Karibu na mwisho wa barua yake ya pili kwanza alionya juu ya kutokea kwa ‘waalimu wa uongo kwenu, watakaoingiza kwa werevu uzushi wa kupoteza, wakimkana hata Bwana aliyewanunua, wakijiletea uharibufu usiokawia.’ Akiwafikiria Wakristo hawa wa kusingizia, baadaye aliandika hivi: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.” Je! hayo si maoni yale yale yanayofuatwa kwa ujumla na viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo na wafuasi wao? Twatumaini kwamba hayo siyo maoni yako.​—2 Pet. 2:1, 2; 3:3, 4.

8. Petro aliendeleaje kutoa onyo linalohusu hasa siku zetu?.

8 Bali, twatumaini kwamba maoni yetu sote manyofu yanapatana na maonyo anayoendelea kutoa mtume. Baada ya kueleza kwamba “kwa neno la Mungu” taratibu ya zamani ya mambo, mbingu na dunia ya zamani, “iligharikishwa na maji, ikaangamia,” ndipo alipoendelea kusema kwamba “mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo [la Mungu], zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.” Halafu akaonya juu ya kutokuwa na subira, kama vile wengi walivyo siku hizi, kwa sababu Mungu anaelekea kuwa amekawia, akisema: “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, [sasa iangalie sababu] bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” Alionya tena kwamba ‘siku ya Yehova itakuja kama mwivi’ ambamo mbingu na dunia ya sasa ya mfano, zikiwa chini ya uongozi usioonekana wa Shetani, zitaharibiwa.​—2 Pet. 3:5-10.

9. Kwa sababu gani ni jambo la maana kuwa na maoni yanayofaa juu ya subira ya Mungu?

9 Halafu linakuja onyo: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa nyinyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza.” (2 Pet. 3:11, 12) Wadhihaki wa leo hawatumii vizuri subira ya Mungu. Walakini, ingawa hawaithamini, Mungu amewatendea kwa fadhili sana akitazamia watubu. Kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Au waudharau wingi wa wema wake na ustahimili wake na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu?” (Rum. 2:4) Ole wetu tukizidharau fadhili za Mungu!

10. Ni kwa msingi gani na kwa njia gani tunavyoweza kuitikia ombi katika 2 Petro 3:14?

10 Lakini, kwa upande unaofaa, imetupasa tulijibuje ulizo hili: Imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani? Nasi twawezaje kuonyesha kwamba ‘tunaitazamia ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza?’ Kwanza, lazima sote tuitikie ombi la Petro, tumaini letu la uzima liwe ni la kimbinguni au la kidunia: “Fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.” (2 Pet. 3:12, 14) Naam, lazima tujitahidi sikuzote tuwe wasioharibika kwa adili. Lazima tuendeleze ukamilifu wetu, tukiwa “wenye moyo safi” katika kujitoa kwa nafsi yote kwa Yehova. (Mt. 5:8) Ni kweli, sote hatujakamilika nasi twapungukiwa kila siku, lakini kama inavyotajwa katika barua ile ile inayofuata katika Biblia, katika 1 Yohana 1:7: “Tukienenda nuruni, kama yeye [Mungu] alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.” Naam, Yesu Kristo “ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu [kundi la Kikristo, “kundi dogo”]; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” Hivyo, hata wawe ni watu wangapi watakaoingia katika “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine,” wanaweza na lazima ‘wafue mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’​—1 Yohana 2:2; Ufu. 7:14.

11. Zaidi ya kuacha dini ya uongo, ni uamuzi gani wa wazi unaoonyeshwa ufanywe katika Ufunuo 18:4?

11 Lakini si hayo tu. Je! wakumbuka tuliwataja wale wanawake wawili wa mfano wanaotofautishwa sana? Mmoja ni kahaba, Babeli Mkuu, kutia na Jumuiya ya Wakristo, yule mwingine ni bikira, mke wa Mwana-Kondoo, kundi la Kikristo. Haitoshi kutoka katika Babeli Mkuu, kuacha dini yote ya uongo. Ni akina nani walioambiwa ‘watoke kwake’ katika Ufunuo 18:4? Walikuwa: “Watu wangu.” Hii yamaanisha kwamba lazima ujitambulishe waziwazi kuwa mmoja wa watu wa Mungu, kuwa mmoja wa watumishi au watumwa wake waliojitoa, kuwa mfuasi wa mchungaji mwema, Kristo Yesu, mmoja wa “kondoo” zake. Ili tupate habari zaidi juu ya jambo hili, lazima tuyarudie maandiko ya Kiebrania na unabii wake wenye kuweka msingi, si wa amri iliyomo katika Ufunuo 18:4 tu, bali pia wa mengi ya mambo yaliyomo katika kitabu hicho cha mwisho cha Biblia.

12. (a) Unabii wa Isaya ulisemaje juu ya tengenezo la Yehova la kimbinguni? (b) Kristo Yesu alikuwa na shirika gani katika tengenezo hilo?

12 Kulingana na unabii wa Isaya, Mtumishi wa Kimasihi wa Yehova, Kristo Yesu, alikuwa mshiriki wa tengenezo la kimbinguni la Yehova la “wana wa Mungu” waaminifu. (Ayubu 1:6; 2:1; 38:7) Tengenezo hilo la kiroho la kimbinguni ni “mke” wa Yehova Muumba, kama vile taifa la kale la Israeli lilivyokuwa kana kwamba limeolewa na Yehova na kufananishwa na mke wake wa kidunia, lilipoingizwa katika agano la Torati. (Isa. 54:1, 5-8) Yehova alimchagua mwana wake mkuu wa kimbinguni atumikie kama Mtumishi wa Kimasihi duniani. Kwa hiyo tengenezo la Yehova mbinguni lililo kama mama lilimtoa huyo awe mshuhudiaji mkuu wa enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mume wake. Mtumishi huyu alipokwisha kutimiza mwendo wake duniani kwa uaminifu na kufufuliwa kwa wafu, tengenezo lenye mfano wa mama mbinguni lilimpokea tena kama “mzaliwa wa kwanza wa waliokufa.” (Kol. 1:18; Ufu. 1:5, 17, 18) Furaha yake ilikuwa imetabiriwa! Ebu sikiliza: “Imba,” yasema Isaya 54:1, “wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema [Yehova].”

13. (a) Paulo alitumiaje Isaya 54:1, na aliitumia kwa nani? (b) Kupatana na hilo, Yesu alitumiaje Isaya 54:13?

13 Andiko hili linatumiwa na mtume Paulo kwa tengenezo la Yehova lililo kama mke kwake mbinguni, si kwa taifa la Kiyahudi baada ya uhamisho wake katika Babeli. Katika Wagalatia 4:22 mpaka 5:1, Paulo analitofautisha taifa la Kiyahudi na mji Wake mkuu katika Yerusalemu, taifa ambalo lilimkataa Yesu Kristo, na tengenezo la kimbinguni la Mungu lililo kama mke kwake, na kusema kwamba “Yerusalemu wa juu ni mwungwana, naye ndiye mama yetu sisi.” Kulingana na unabii wa Isaya, tengenezo la Mungu la kimbinguni lilipaswa liwe na watoto zaidi kuliko Masihi Yesu tu, ambaye lilikuwa limengojea kwa muda mrefu kana kwamba likiwa tasa. Lilipaswa liwe mama ya kiroho wa washirika 144,000 wa Masihi Yesu. Hii inaonyeshwa waziwazi katika Isaya 54:13, iliyoandikwa kwa “Yerusalemu wa juu,” ‘Yerusalemu wa kimbinguni’ au “Mlima Sayuni,” inayosema hivi: “Na watoto wako watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” Huo ndio ufahamu sahihi unaoshuhudiwa na uhakika wa kwamba Yesu Kristo alilitumia andiko hilo kwa wanafunzi wake mwenyewe, katika Yohana 6:45.​—Ebr. 12:22.

14. Tengenezo la Mungu linawakilishwaje duniani, na hiyo inahitaji uamuzi gani wa hakika ufanywe?

14 Hivyo tunaweza kusema kwamba tengenezo la Mungu la kimbinguni lililo kama mke kwake linawakilishwa duniani na washirika waliofunzwa vizuri na kuzoezwa vizuri wa Kristo Yesu. Kwa hiyo, si kwamba tu lazima tumkimbie yule kahaba mchafu, Babeli Mkuu, bali pia lazima tupate kimbilio kwa kushirikiana sana na mwanamke wa kweli wa Mungu, ‘Yerusalemu wa kimbinguni,’ anayewakilishwa na wafuasi walio kama mabikira wa Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, walio duniani. Hii inaonekana wazi katika hali iliyo nayo leo jamii hiyo ya Wakristo wanaojulikana kama mashahidi wa Yehova. Wako mabaki ya wale waliotiwa mafuta na roho ya Mungu wawe na tumaini la kimbinguni kati yao ambao ndicho kiini chao. “Mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wenye kuongezeka sikuzote na unaofanyiza “kundi moja [chini ya] mchungaji mmoja” umekusanyika karibu kuzunguka kiini hicho.​—Yohana 10:16.

15. Ni kwa njia gani mashahidi wa Yehova wanaonyesha kwamba ‘wanatazamia na kuhimiza’ siku ya Yehova?

15 Hilo si dai lisilo na msingi. Wanaonyesha kwamba ‘wanatazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza.’ Ijapokuwa mikazo yote inayoongezeka, wao wanashikamana na “dini iliyo safi, isiyo na taka” kwa kutokuwa na doa la ulimwengu mchafu. Wanakataa kumwabudu “mnyama” wa kisiasa na “sanamu” yake ya kuundwa na wanadamu, Umoja wa Mataifa. Wanajiepusha wasitiwe madoa ya hatia ya damu, wakiendelea kutokuwamo kabisa na kutoshiriki katika vita vya umwagaji wa damu vya mataifa na vyama vya kisiasa vya ulimwengu huu. Wao wanamwiga Yesu Kristo kiongozi wao kwa kutokuwa sehemu ya ulimwengu huu.​—Yak. 1:27; Ufu. 13:1-15; 15:2-4; Yohana 15:19; 17:14,16.

16. Wao wanatimizaje amri mbili zilizo katika Mathayo 24:14 na Mathayo 28:18-20, na kuna ushuhuda gani kwamba Yehova anawabariki?

16 Kwa kuendelea kukaa upande unaofaa, wanahakikisha kwamba ‘wanautafuta ufalme [wa Baba yao wa kimbinguni] kwanza na haki yake’ kwa kuendelea kutangaza wanachojua kuwa ndilo tumaini na kimbilio la pekee la mwanadamu, kama vile Yesu alivyotabiri: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Maadamu kuna wakati, wao wanaendelea pia kutimiza amri ya Yesu Kristo aliyefufuliwa kwenda kufanya watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi, kuwabatiza katika maji na kuwafundisha kuyashika mambo yote aliyowaamuru. (Mt. 6:33; 24:14, NW; 28:18-20) Inaonekana kwamba haya yote yamebarikiwa na Yehova, si katika ongezeko kubwa sana la wale wenye kusongamana kwenye tengenezo la Yehova tu, bali pia katika hali ya amani, furaha, usalama na usafi iliyo kati ya watu walio wakf wa Yehova duniani pote. Kwa kweli ni kama paradiso ya kiroho. Basi sikiliza na kuutii ukaribishaji huu wa Maandiko, uje na kupata kimbilio katika hii paradiso ya kiroho.

UKARIBISHAJI KUJA KWENYE PARADISO YA KIROHO

17. Ni ahadi na ukaribishaji gani uliotolewa katika Isaya 54:17 na Isaya 55:1, 2, na kumekuwa na utimizo gani mdogo?

17 Mwishoni mwa Isaya, sura ya 54, kuna ahadi ya ajabu kwa wana wa kiroho wa “Yerusalemu wa juu”: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa, na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa.” (Isa. 54:17) Ndipo unapokuja ukaribishaji wenye kusisimua: “Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; naam, njoni, nunueni divai na maziwa, bila fedha na bila thamani. . . . Nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono.” (Isa. 55:1, 2) Dokezo la hali yenyewe laonekana tunapokumbuka kwamba Isaya alitabiri kuharibiwa kwa Yerusalemu na Uyahudi na kuhamishwa kwa Wayahudi kupelekwa Babeli kwa miaka 70. Alitabiri pia kukombolewa kwao kupitia kwa Koreshi Mwajemi, aliyetumiwa kama mfano wa unabii wa Mtumishi wa Kimasihi wa Mungu, Kristo Yesu, ambaye angepindua na kuharibu Babeli Mkuu. (Isa. 44:28-45:6) Lakini namna gani leo?

18. Yaliyowapata mashahidi wa Yehova tangu mwaka wa 1914 mpaka 1919 yaliongozaje kwenye utimizo mkubwa wa maandiko yaliyo juu?

18 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Babeli Mkuu aliteka mashahidi wa Yehova kweli kweli kwa kutumia hawara zake wa kilimwengu, wakuu wa kisiasa, wa kijeshi na wa mahakma. Mateso na marufuku yalienea pote, upeo ukafika wakati washiriki wa baraza inayoongoza ya mashahidi wa Yehova walipofungwa. Hakukuwa na matumaini yo yote. Halafu kwa ghafula na bila kutazamiwa kipindi kilichofuata vita kikawa wazi mbele yao. Ujumbe wa ukombozi ukatoka kwa Yehova, ujumbe wa Maandiko wa kukombolewa kutoka kwa Babeli Mkuu kupitia kwa ufalme uliosimamishwa wa Kimasihi. Uhakikisho kamili wa jambo hili ulionekana wakati washiriki waliotajwa walipofunguliwa wakaondolewa kabisa mashtaka yote ya uongo. Karibuni baada ya mwaka uo huo wa 1919, makala ya kwanza ilitokea katika The Watch Tower yenye kichwa “Waliobarikiwa Ni Wasioogopa,” na hicho ndicho kilichokuwa kichwa cha Kusanyiko Kuu katika Cedar Point, Ohio, Septemba 1-8, 1919. Katika kusanyiko hilo lilitangazwa gazeti jipya lenye kuchapwa kila juma mbili lililoitwa The Golden Age, kama ishara ya kwamba kulikuwa na chakula zaidi cha kiroho na kazi kubwa zaidi huko mbele. Kama unavyoweza kuwazia, haya yote yalikuwa kama maji yenye kuburudisha, mkate wenye kutia nguvu, divai yenye kufurahisha na maziwa yenye kunenepesha watumishi wa kweli wa Mungu.

19. Ni hatua gani ambazo zimechukuliwa baada ya hapo kurudisha paradiso ya kiroho?

19 Huo ulikuwa ndio mwanzo tu, hatua ya kwanza, ya kurudishwa kwa paradiso ya kiroho kwa ajili ya watu wa Mungu. Hatua kubwa sana zimechukuliwa tangu wakati huo, kama vile inavyoonyesha historia ya kisasa ya mashahidi wa Yehova, nayo maandishi yake yanapatikana ili wote wajionee na kujichunguzia wenyewe. Tena, kila hatua moja zaidi yaweza kuonekana kuwa inaongozwa na Mbuni wa Biblia, aliyesema hivi: “Neno langu, . . . halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma. Maana mtatoka kwa furaha, mtaongozwa kwa amani . . . miti yote ya kondeni itapiga makofi. Badala ya michongoma utamea msunobari, na badala ya mibigili, mhadesi; jambo hili litakuwa la kumpatia [Yehova] jina, litakuwa ishara ya milele isiyokatiliwa mbali.”​—Isa. 55:10-13.

20. Ukaribishaji wa kushiriki katika paradiso hii unatolewaje katika Zaburi 1:1-3?

20 Lo! jinsi yalivyo masimulizi yenye kuvutia ya paradiso ya kiroho! Nawe unakaribishwa ushiriki bi nafsi katika paradiso hiyo ukishikamana sana na Neno la Mungu. Kama vile inavyosemwa katika Zaburi 1:1-3: “Heri mtu yule . . . [ambaye] sheria ya [Yehova] ndiyo impendezayo, na sheria yake hutafakari mchana na usiku.” Ni nini kinachotokea kwa mtu huyo? “Atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki [linaendelea kuzaa na kuwa bichi]; na kila alitendalo litafanikiwa.”

21, 22. (a) Maandiko katika Mathayo 25:34 na Ufunuo 22:17-20 yanaendeleaje kutoa ukaribishaji huu? (b) Tunaweza kufanya uamuzi gani wa kipekee na wa hakika kwa kuitikia ukaribishaji huo?

21 Njia ya kuingia katika paradiso ya kiroho ingali wazi! Ukaribishaji wa kuiingia na kuifurahia ungali unatangazwa ulimwenguni pote! Kama vile mfalme alivyosema katika mfano wa Yesu: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.” (Mt. 25:34) Kwa kweli, Maandiko Matakatifu, Neno la Mungu, linamalizia kwa ukaribishaji huu: “Na [roho] na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” Kristo Yesu anapomalizia, Yohana katika njozi anamsikia akisema hivi: “Yeye mwenye kuyashuhudia haya asema, Naam; naja upesi.” Halafu Yohana anaitikia kwa shauku: “Amina; na uje, Bwana Yesu.”​—Ufu. 22:17-20.

22 Sababu gani usifanye uamuzi wa hakika kupata kimbilio chini ya “ufalme wa mbinguni” usioharibika? Ukaribishaji huo ukiwa unarudiwa-rudiwa na kusihi-sihi hivyo, je! wewe hutaitikia kwa shauku? Je! wewe hutakuja?

​—Kutoka The Watchtower, November 15, 1975.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki